Thursday, January 26, 2023

WAZIRI SIMBACHAWENE: IMARISHENI MIFUMO WA USHUGHULIKIAJI WA MATUKIO YA UKATILI DHIDI YA WANAWAKE NA WATOTO.

Serikali yahimiza jamii  kuanzia ngazi ya familia kuimarisha mfumo wa ushughulikiaji wa matukio ya ukatili dhidi ya watoto ndani na nje ya shule unaowajumuisha wasimamizi wa shule, wazazi, walezi na jamii kwa lengo kuendelea kutokomeza matukio ya ukatili nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulika na Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene katika Mkutano wa Kitaifa wa tafakuri ya Utekelezaji wa Mpango Kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto (MTAKUWWA) uliofanyika katika Ukumbi wa Saint Gaspar Jijini Dodoma.

Waziri ameeleza kwamba Mfumo wa Ushughulikiwaji wa matukio ya ukatili utasaidia Taifa kupunguza kwa kiasi kubwa changamoto iliyopo katika jamii ya ukatili wa kijinsia na unyanyasaji wa Watoto.

“tuendelee kuunga mkono juhudi za Serikali kwa hali na mali ili kuhakikisha makundi yote ndani ya jamii yanalindwa dhidi ya ukatili wa kijinsia na unyanyasaji wa watoto alisema,” alisema Waziri Simbachawene.

Akieleza kuhusu Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Mtoto wa mwaka 1989, wa Sera ya Maendeleo ya Mtoto 2008 na Sheria ya Mtoto Na. 21, 2009, ambao unaoelezea masuala ya ukatili kwa watoto ni kinyume cha haki zao za msingi za kuishi, kuendelezwa, kulindwa na kutokubaguliwa.

Aidha umeeleza kuwa,vitendo vya ukatili vinarudisha nyuma jitihada za Serikali katika kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu ya mwaka 2030 na Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Mtoto wa mwaka 1989 ambayo nchi imeridhia kutekeleza.

Waziri amehimiza kuendeleza juhudi za kukabiliana na ukatili huo katika zama za utandawazi kuwa na msukumo mpya na wa pamoja ili kuwalinda watoto dhidi ya ukatili.

Amesema kuwa, athari za utandawazi zimedhoofisha mifumo ya ulinzi na usalama wa watoto hivyo kufanya kundi hilo kutokuwa salama kwani tatizo la ukatili bado ni changamoto katika ngazi zote.

Kwa upande wake, Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake  na Makundi Maalum  Mhe. Dorothy Gwajima amesema wizara ya Maendeleo ya jamii imekuwa ikiratibu utekelezaji wa MTAKUWWA toka kuzinduliwa kwake mwaka 2016, na baada ya kukamilika kwake Wizara pamoja na Wadau wa maendeleo walifanya tathimini ya utekelezaji wake kuanzia 2017/2018 hadi 2021/2022 kupitia Mtaalam mwelekezi Chuo Kikuu cha Dodoma.

Waziri amesema taarifa ya tathimini imekamilika na imebainisha utekelezaji wa MTAKUWWA kwenye maeneo yote nane yalliyopo kwenye mpango huu, na imebainishwa maeneo muhimu yatakayoenda kutekelezwa kwenye mpango kazi ujao.

“Niwaombea wadau tuwe na subira tukiwa tunaendelea mapitio ya pamoja mpaka itakapotangazwa kwamba serikali pamoja na wadau,”aliomba Waziri Gwajima

Naye Mkurugenzi wa Shirika la ICS Tanzania Bwn.  Kudely Sokoine  Joram amesema wataendelea kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuhakikisha mapambano haya yanatokomezwa huku akiipongeza Serikali kwa hatua inazochukua katika kukabiliana na changamoto ya ukatili wa makundi haya muhimu huku akitaja maeneo muhimu ikiwemo la kuimarisha mifumo ya ulinzi wa Wanawake na Watoto, kujenga uwezo wa Kamati za ulinzi wa Wanawake na watoto pamoja na kusaidia uratibu wa Masuala yote.

Read More

Thursday, January 19, 2023

"TATUENI CHANGAMOTO ZA WANANCHI," WAZIRI SIMBACHAWENE.

Waziri wa Nchi Ofisi ya waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene amewataka watendaji wa Serikali kuendelea kutatua changamoto za wananchi zinazowakabili ili kuchochea kasi ya maendeleo nchini.

Waziri ametoa kauli hiyo wakati akifungua mafunzo ya siku mbili ya kujenga uwezo kwa Menejimenti ya Ofisi ya Waziri Mkuu yaliyolenga kuwajengea uelewa kuhusu Idara ya  Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji wa Shughuli za Serikalini yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi uliopo Njedengwa Jijini Dodoma Januari 19, 2023.

Waziri alihimiza kila mtendaji wa Serikali kuhakikisha anatekeleza majukumu yake kwa ufanisi huku akitatua changamoto za wananchi katika eneo lake la kazi.

Aliongezea kuwa ni muhimu kwa watendaji kuwajibika kwa kuyafikia malengo ya Serikali ya Awamu ya Sita huku wakileta matokeo chanya yatokanayo na utendaji mzuri wa kazi zao za umma.

"Hakikisheni mnakuwa watu wa  msaada kwa wengine katika kuyatekeleza majukumu yenu, muwe watengeneza furaha na hii iwe kipimo kwa kila mwenye kukufikia huku ukizingatia taratibu za utumishi wa umma na sheria zilizopo,"alisema Waziri Simbachawene

Aidha aliwaasa waendelee kutumia taaluma zao kuleta matokeo chanya kwa Serikali na jamii huku wakijitathimini utendaji wa kila siku.

 “Ni sahihi kujitathimini kila iitwapo leo ili kuona namna unavyoleta matokeo chanya kwenye utendaji wako wa kila siku, matokeo utayoyapata  yatatusaidia kuongeza tija ,” alisisitiza Waziri Simbachawene.

Akieleza umuhimu wa mafunzo hayo aliwataka kuhakikisha mafunzo  yanawafikia watendaji katika ngazi zote ili kuendelea kuongeza uelewa kwa watumishi wa umma.

" Mafunzo haya yawafikie watumishi wote katika Idara na vitengo vyetu bila kumuacha nyuma mtu yeyote ili kuleta chachu katika utendaji na  kuondokana na tabia ya mazoea," alisema.

Aliongezea kuwa matokeo ya Mafunzo haya yatumike kuboresha mifumo ya uratibu, usimamizi na ufuatiliaji wa shughuli za Serikali ili kuwa na uwezo wa kupima utendaji wa Wizara na Taasisi mbalimbali za Serikali kisayansi.

Aidha uwekwe utaratibu ambao utawezesha uchambuzi wa Taarifa za kisekta na kutoa mrejesho wa maeneo yanayohitaji kuboreshwa au kupewa msukumo zaidi.

 "Ili kuendelea kuboresha shughuli za uratibu naamini uwepo Idara mpya ya Ufuatiliaji na Tathmini itasimamia hili na kuhakikisha kunakuwa na mrejesho kwa Wizara na Taasisi zote ili kuimarisha uwajibikaji," alihimiza.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Dkt. John Jingu  amesema mafunzo haya yanalenga watendaji wa serikali kufanya kazi kwa ufanisi kwa weledi na kwa namna ambayo itakidhi mahitaji pia yatajikita katika majukumu ya Ofisi ya Waziri Mkuu  katika eneo la uratibu wa shughuli za serikali, na jukumu la kufanya kazi ya ufuatiliaji na tathmini ya utendaji wa  shughuli za Serikali.

 

Read More

Tuesday, January 17, 2023

WAZIRI SIMBACHAWENE, ARIDHISHWA NA HATUA ZA UJENZI KIWANDA KIPYA CHA MPIGA CHAPA MKUU WA SERIKALI

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu  ameridhishwa na kasi ya ujenzi wa kiwanda  cha kupiga chapa cha serikali ambacho mpaka sasa msingi wa jengo na ujenzi wa boma la jengo; kuta, kupiga plasta na kupauwa vimeshafanyika.

“Hiki kiwanda tunatarajia kukifunga mitambo na mashine za kisasa ili kiweze kufanya jukumu la kuchapa nyaraka za Serikali na  shughuli za Mpiga Chapa ziweze kufanyika kwa ufanisi.”

Kauli hiyo ameitoa alipotembelea na kujionea maendeleo ya ujenzi wa kiwanda hicho cha Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali kilichopo Kisasa katika Jiji la Dodoma.

Ofisi hii ni muhimu sana kwa nchi, ni lazima iwe Ofisi bora kwa sababu nyaraka nyingi za siri za serikali zinapaswa kuchapwa na Ofisi ya Mpiga Chapa wa Serikali,

Waziri Simbachawene amempongeza Rais Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa kiwanda hicho cha mpiga chapa wa serikali kwa kiasi cha billioni 1.88

“Serikali imetoa pia kiasi cha million kiasi cha millioni 350 ambazo zitatumika kufanyia ukarabati kiwanda na Mashine za Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali Jijini Dar es Salaam ikiwa ni pamoja na kiasi kingine cha shilingi billioni 1.4 kwa ajili ya kununua malighafi kwa viwanda vinavyondelea na uzalishaji, cha Dodoma na Dar es salaam.”

Amefafanua kiwanda kipya cha Dodoma cha Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali imetoa kiasi cha shilingi billioni 3.9 ambayo itasaidia kununua mitambo mipya na ya kisasa ili kuhakikisha nyaraka zote muhimu za serikali zinachapishwa katika kiwanda hicho.

“Nembo ya Taifa, Bendera ya Taifa na Mhuri ni vitu ambavyo vimewekwa katika uangalizi wa Ofisi ya Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali.”

Naye Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali Bwn. George Lugome ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kutoa fedha kwa ajili ya kuboresha idara ya Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali  kwa kuiwekea majengo yenye uwezo wa kuwa na miundo mbinu mizuri na mashine za kisasa ambazo zitasaidia kuchapa nyaraka zenye alama ya siri.

“Sheria ya alama za Taifa ya mwaka 1971 inatamka wazi kabisa kwa yoyote anayekiuka au anaibadili nembo ya Taifa au alama za Taifa anastahili kupewa adhabu ya kifungo cha miaka miwili jela,” amesema Bwn, Lugome.

Ametoa wito kwa taasisi binafsi zinazotaka kujihusisha na uchapaji wa nyaraka  kuhakikisha wanathibitishwa na Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Usalama ya Serikali ili waweze kupata kibali.

 



Read More

JAMII YA WATANZANIA IPEWE ELIMU YA KUTOSHA JUU YA URAHIBU WA DAWA ZA KULEVYA.

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe.  George Simbachawene ametoa wito kwa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Nchini kuongeza nguvu katika kutoa elimu kwa umma juu ya athari za dawa za kulevya kwa vijana na wanachi wote kwa ujumla.

Hayo ameyasema alipotembelea na kujionea eneo la Hekta saba ambalo linatarajiwa kujengwa jengo la Makao Makuu ya Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Kanda ya Kati, katika eneo la Itega Jijijni Dodoma.

 “lazima tuvunje ukimya na tuongeze udhibiti wa matumizi ya bangi, hatuwezi kudhibiti matumizi ya bangi kwa kutegemea mamlaka pekee yake lazima tuweke mfumo na uratibu kwa kuanza kudhibiti kuanzia ngazi ya kijiji, Kata na Wilaya.” Amesema Simbachawene.

 Tufike mahali tuone tunauwa Taifa; Vitu vingi vinavyotokea kwenye familia, na matokeo ya ajabu ya unyanyasaji msukumo wake ni matumizi ya madawa ya kulevya na ukipata urahibu unashindwa kuisadia jamii, unashindwa kuwajibika kwenye familia unashindwa kufanya shughuli za uzalishaji mali.

Waziri Simbachawene, ameongeza kuwa aina mpya ya Urahibu wa kucheza Kamari (Kubeti) ambayo inawakumba watu wote, na ina madhara kama urahibu wa madawa ya kulevya, lazima tujipange.

Kila mmoja ni shahidi watu wanapokuwa wanafanya Kamari ya kubahatisha, kwenye michezo ya mpira, hata kufanya kazi hawawezi, muda wote ni kuangalia mkeka tuu(kubeti)

Aidha kuna umuhimu wa kuziunganisha kwa kuziimarisha Taasisi zetu hizi za Hospitali ya Taifa ya Afya ya Akili Mirembe na Mamlaka wa Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya kisera na kisheria ili ziweze kushirikiana vizuri katika utendaji wa kazi.

Naye Kamishna wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya  Jenerali Gerald Kusaya amesema  katika Mwaka huu wa fedha serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu imeweza kupeleka Vyuo vya Ufundi warahibu  walioachana na matumizi ya  dawa za kulevya wapatao 245 wanaolipiwa ada zote na Ofisi ya Waziri Mkuu na kila mmoja amechagua kitu anachotaka kusoma ili watakapomaliza warudi mtaani na waweze kuanza kujitegemea na kujenga uchumi wa nchi.

Katika kuhitimisha ziara hiyo kamishna Jenerali Kusaya ameomba serikali kuwasaidia  warahibu wanaohitimu mafunzo ya Ufundi stadi na stadi za kazi kupewa vitendea kazi vitakavyowasaidia pindi watakaporudi kwenye jamii yao

Jumla ya warahibu wapatao 12,800 wanatarajia kuhitimu mafunzo kutoka kwenye vyuo vya ufundi wakiwa na ujuzi wa stadi mbalimbali za kazi na kuweza kujitegemea na kujenga uchumi.

 

 

Read More

Monday, January 16, 2023

TAASISI ZINAZOENDELEA NA UJENZI WA OFISI ZATAKIWA KUKAMILISHA MAJENGO YAO KWA WAKATI JIJINI DODOMA


Serikali imeziagiza Taasisi zote zinazoendelea na ujenzi wa majengo ya Ofisi zao Jijini Dodoma kuhakikisha ujenzi huo unakamilika kwa kuzingatia taratibu zote za ujenzi ikiwemo ubora, muda, bajeti iliyotengwa na thamani ya fedha ili kuleta tija inayotarajiwa.

Maagizo hayo yametolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George simbachawene wakati wa hafla ya kukabidhi Vibali vya Ujenzi wa Ofisi za Taasisi za Serikali Dodoma iliyofanyika katika Ukumbi wa Hazina mapema.

 

Waziri Simbachawene amesema, kila Taasisi ya Serikali ihakikishe inajenga majengo ya Ofisi zake ili kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali za kuhamishia Makao makuu yake Dodoma na kuifanya Dodoma kuwa eneo lenye ufanisi.

 

“Taasisi zote zilizoelekezwa kuhamia Dodoma kwa mujibu wa ratiba niliyoitoa leo zihakikishe zinatekeleza maagizo hayo na Makatibu Wakuu wa Wizara husika wahakikishe wanasimamia mpango kazi wa utekelezaji wake,”alisema Mhe.Simbachawene.

 

Aliongezea kuwa, Mpango huu ni utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2015 kama ilivyoainishwa katika Ibara ya 151 chini ya kifungu (a), (b) na (c) vinavyoielekeza Serikali kutunga Sheria ya kuitambua Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi na kuhakikisha kwamba majengo ya Wizara na Taasisi yanajengwa Dodoma badala ya Dar es Salaam.

Aidha Waziri ameagiza Ofisi ya Katibu Mkuu – Sera, Bunge na Uratibu kwa kushirikiana na Mamlaka husika kuendelea kuratibu Mpango wa Serikali na taasisi zake kuhamia Dodoma pamoja na ujenzi wa miundombinu ya kiuchumi na uboreshaji wa huduma mbalimbali za kijamii Dodoma.

Sambamba na hilo, Serikali imekamilisha ratiba na mwongozo utakaowezesha Taasisi za Serikali ambazo bado zinaendelea kutekeleza majukumu yake Dar es Salaam kuweza kuhamishia shughuli zao Jijini Dodoma kwa awamu.

“Katika utekelezaji wa suala hili, Mheshimiwa Waziri Mkuu ametoa maelekezo kwamba Taasisi 42 zihamie Dodoma ndani ya mwaka huu wa fedha wa 2022/23; Taasisi 36 zitahamia Dodoma katika mwaka ujao wa fedha wa 2023/24 na Taasisi 19 zitahamia katika mwaka 2024/25 wakati Taasisi 27 zimeelekezwa, kwa kuzingatia aina ya majukumu zilizonazo, kuendelea kutekeleza majukumu yake Mkoani Dar es Salaam.” Alieleza.

Alisisitiza kuwa, hatua hii itakamilisha sehemu kubwa ya Mpango wa Serikali wa kuhamia Dodoma ambapo hadi sasa tayari Taasisi 65 zilishahamia Dodoma tangu mwaka 2016 hadi 2022.

Waziri ameziagiza Taasisi nyingine ambazo bado hazijaanza maandalizi ya ujenzi wa Ofisi za serikali Dodoma ziwasilishe Ofisi ya Waziri Mkuu Mahitaji ya Viwanja vya ujenzi wa Ofisi za taasisi Dodoma kwa ajili ya uratibu wa pamojal.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule, ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi wa miundo mbinu ya kuwezesha taasisi kuwepo.

 

“Tunaishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kazi kubwa mnayoifanya kwa kupanga makao makuu ya serikali yetu yanakuwa ni mji wa kisasa na mji uliopangwa.”alisema Mhe. Rosemary

 

Awali Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Dkt, John Jingu akitoa taarifa ya utekelezajia amesema Ofisi ya waziri Mkuu imeidhinisha vibali 55 kwa nyakati tofauti kuanzia mwaka 2018 kati ya hizo taasisi 20 zimekamilisha ujenzi, taasisi 16 zinaendelea na ujenzi na taasisi 19 zimeanza maandalizi ya ujenzi.

“Majengo haya yanajengwa katika maeneo mbalimbali, na ujenzi huu unazingatia mpango kabambe wa Jiji la Dodoma.”

Read More

Wednesday, January 11, 2023

SERIKALI YATOA MSAADA KWA WAATHIRIKA WA MAFURIKO YA MAJI MKOANI MBEYA

Serikali Kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu imetoa msaada kwa wananchi walioathirika na Maafa ya Mafuriko ya Maji Mkoani Mbeya, yaliyosabisha nyumba kubomoka, kuharibika kwa vifaa, vyakula, uharibifu wa mifugo na mazao yaliyoko mashambani.

“Msaada huo unajumuisha Magodoro 300 kwa kuanzia, mablanketi 1200 ya wakubwa na wadogo, mikeka 600, madumu ya maji, sufuria bakuli sahani pamoja na vijiko kwa kila familia ambayo imeathirika.”

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene alipotembelea maeneo yaliyoathirika wa mafuriko ya mvua katika kata saba Mkoani Mbeya kutokana na Mvua zilizonyesha  terehe 07/01/2023.

“Kwa mujibu wa sheria no. 6 ya Maafa ya Mwaka 2022 sisi kama Ofisi ya Waziri Mkuu tunayo dhamana ya kuwaunganisha wadau ili kuwasaidia watu walioathirika na tutafanya hivyo kwa kutumia Ofisi zetu za Mkoa na wilaya, naomba wadau wote wa ndani na nje ya Mkoa wa Mbeya kutusaidia ili kuhakikisha watu hawa wanarudi katika hali yao.”

Natoa pole kwa wote walioathirika, TARURA kwa kushirikiana TANROAD Halmashauri ya jiji  la Mbeya na Halmashauri ya Mbeya vijijini wahakikishe wanaenda kuona kwenye vyanzo kuangalia ni eneo gani maji yametoka kwenye mkondo wake wa asili.

Akimkaribisha Waziri wa Nchi, Mbunge wa jimbo la Mbeya Mjini na Spika wa Bunge la jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Tulia Ackson ameishukuru serikali kwa mchango iliyoutoa kwa  waathirika wa mafuriko ya Mvua Mkoani Mbeya .

“Naomba sisi kama Halmashauri tusitoe vibali vya ujenzi kwenye  maeneo ambayo ni mikondo ya maji, kwa sababu athari za mafuriko zinarudisha nyuma  maendeleo ya uchumi kwa wananchi”

Naye Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe. Juma Homera katika taarifa yake amesema watu waliopata athari za mafuriko ya maji, kaya 281 zenye watu idadi ya watu 1405 ambao wanahitaji chakula takribani tani 50 kwa miezi mitatu ili ziweze kuwasaidia.

 

Read More

Friday, January 6, 2023

WAZIRI SIMBACHWENE AHIMIZA MAPAMBANO DHIDI YA UDHALILISHAJI WANAWAKE NA WATOTO


 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene ametoa wito kwa Walezi na jamii kwa ujumla kupiga vita dhidi ya udhalilishaji kwa Wanawake na Watoto mambo ambayo yanapoteza heshima na haiba kwa nchi yetu.

 “tushirikiane katika kutokomeza udhalilishaji kupinga, kuwafichua na kuwafikisha katika vyombo vya Sheria wale wote wanaofanya unyama huu kwa wanawake na Watoto, lakini pia hatunabudi kurejesha utamaduni wetu wa malezi ya pamoja ili kulidhibiti janga hili kwa jamii na Taifa kwa ujumla.”

wito huo ameutoa wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi ujenzi wa kituo cha afya Shehia ya Uzi Mkoa wa Kusini Unguja katika sherehe ya kuadhimisha miaka 59 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.

Katika shughuli yetu kuu ya uwekaji wa jiwe la msingi la mradi   wetu huu, ambayo tayari tumeshaifanya kwa ukamilifu wake, hivyo iliyobaki kwetu ni kuhakikisha mradi huu   unakamilika kwa hatua zilizobakia ili kukidhi  malengo tuliyoyakusudia. 

tunaendelea kushuhudia mapinduzi makubwa ya kiuchumi yanayoendelea kufanyika nchi nzima na hii inathibitisha kauli ya mwaka huu isemayo “Mapinduzi yetu ndio Amani yetu tuyalinde kwa Maendeleo yetu”.

Aidha  serikali zetu zote mbili ya SMT na SMZ zimeendelea kusogeza huduma mbalimbali kwa wananchi wake na tunashuhudia ujenzi wa Miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo huu wa ujenzi wa Kituo cha Afya katika Shehia zetu za Uzi na Ng’ambwa. Mradi ambao unafadhiliwa na Serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii -TASAF ambao ni miongoni mwa matunda ya Mapinduzi yetu yaliyofanyika Januari 12 mwaka 1964.

“ujenzi huu wa Kituo cha Afya umekuja baada ya kuona upo uhitaji mkubwa wa jengo hili kwa wanajamii wa Shehia zetu za Uzi na Ng’ambwa, hali ambayo itarahisisha upatikanaji wa huduma bora ya afya kwa wananchi hususani mama na watoto,”alisema Waziri.

Waziri amesisitiza ushirikiano wa hali na mali katika ufuatiliaji, usimamizi na utekelezaji wa mradi ili uweze kukamilika kwa wakati na kwa ubora wa hali ya juu. Pia, amewaomba viongozi  wa  Mkoa, Wilaya, Baraza la Mji Kati na Shehia zote kuwa karibu katika kusimamia utekelezaji wa  mradi huo muhimu kwa jamii na Taifa kwa ujumla na kuendelea  kutoa msaada pale unapohitajika  ili kufanikisha ukamilishaji wa  mradi kwa wakati.

Akimkaribisha Mgeni Rasmi Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja Mhe Rashid Hadid Rashid amewapongeza TASAF kwa jinsi wanavyoshirikiana na serikali katika kutekeleza Miradi ya maendeleo.

“Katika kipindi kifupi cha miaka miwili wameweza kujenga ukumbi wa mitihani, Kizimkazi Dimbani na katika Maswala ya Kilimo cha Mwani, wazee wetu wanashughulika na kilimo hicho na walikuwa wanapata tabu kuchukua Mwani baharini kuja juu TASAF imewajengea ngazi  ili iwe rahisi kufika juu.”

Naye Mkurugenzi Mtendaji - Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Tanzania (TASAF) Bwn. Ladisius Joseph Mwamanga amesema TASAF inajenga uwezo wananchi kwa kukuza rasilimali watu  katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

“Napenda kuwapongeza wananchi kwa ushirikiano mkubwa ambao wameuonesha katika ujenzi wa kituo cha afya uzi, mradi umesimamiwa kwa ukaribu na wananchi wenyewe wa Shehia ya Uzi na Ng’ambwa.”

Awali katika risala ya wananchi iliyosomwa Bi. Lemi Khalifa amesema utekelezaji wa mradi ulianza mwezi wa nane 2022 kwa kusimamiwa na kamati kuu mbili; kamati ya Shehia na kamati ya usimamizi ngazi ya jamii CMC.

“Mradi ulitengewa kiasi cha million 184,8 21,428 kati ya hizo shilingi million 134,270.261 zimetumika na ujenzi unaendelea.”

Read More

Wednesday, December 21, 2022

MAWAZIRI WAKUTANA KUIMARISHA MIKAKATI YA KUPAMBANA NA UKATILI WA KIJINSIA KWA WATOTO


 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene ahimiza ushirikishwaji wa wadau wote katika kuunganisha nguvu ili kupambana na ukatili wa kijinsia kwa watoto.

Kauli hiyo ameitoa wakati akiongoza kikao kilichowakutanisha Mawaziri wa kisekta kilichofanyika leo jijini Dar es salaam, kilicholenga kuimarisha mikakati ya kupambana dhidi ya ukatili wa kijinsia kwa watoto.

“Waziri Simbachawene, amemuelekeza Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera Bunge na Uratibu kwa kushirikiana na wataalamu waandae miongozo yote izungumze kwa pamoja kuhusu ukatili wa kijinsia na baada ya kikao cha Mawaziri ushauri upelekwe kwa Waziri Mkuu ili aridhie.”

Ili hatua za muda mfupi hatua za muda wa kati na hatua za muda mrefu ziweze kuchukuliwa katika kupambana na vita hii, binadamu wamekuwa waajabu kuliko wanyama matukio mengi ya ukatili wa kijinsia yanafanywa na ndugu wa karibu.

Katika kikao hicho amesema Mwaka 2021 viliripotiwa vitendo vya unyanyasaji wa watoto 110499 ni asilimia chache yawalioripoti.

“Uliongoza ni ukatili wa ubakaji 5899 na waliolawitiwa 1114 na waliopata mimba za utotoni ni 1677 na utafiti ukaonesha namba hizi uzigawe kwa 60, utaona asilimia 60 inafanyika nyumbani walipo baba na mama ndugu jamaa na marafiki na asilimia 40 ni nje ya nyumbani, wakiwa shuleni au wanapoenda shuleni.”

Lazima tuimarishe mifumo izungumze na uwajibikaji, sheria tunazo tayari tuna miongozo mbalimbali sasa tunahitaji mawasiliano yaanzie kwa Mawaziri yashuke kwa Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, ishuke kwenye kata zetu, ishuke kwenye mitaa na vijiji.

“Mfumo wa mawasiliano uende kwenye kamati za mabaraza ya madiwani kwenye Halmashauri zetu, lakini kwenye vikao vya maendeleo vya kata ili viwe na nguvu ya kukabiliana na vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia kwa watoto ili hata marekebisho ya sheria ndogo ndogo yaanzie kule chini,” alisema Waziri Gwajima.

 

Read More

Friday, December 9, 2022

MIAKA 61 YA UHURU

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene  amesema nchi imepiga hatua kubwa katika ujenzi wa maendeleo ambayo ni shirikishi na yamelenga watu.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu katika kilele cha maadhimisho ya siku ya uhuru wa Tanzania Bara kilichofanyika Kibakwe Katika Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa.

“Katika ujenzi wa maendeleo ukisema ujenzi wa sekondari za kata, ujenzi wa vituo vya afya ujenzi wa barabara vyote vimetekelezwa kwa kushirikisha wananchi.”

Kauli mbiu ya miaka 61 ya uhuru ambayo inasema, Amani na Umoja ni nguvu ya maendeleo yetu.” Imetusaidia kutimiza shabaha zetu.

“Mabadiliko ya kisiasa, mabadiliko ya kiuchumi, Mhe. Rais amepeleka maendeleo hayo kwa watu na maendeleo ya watu yanahitaji rasilimali fedha,” alisema waziri .

Sisi watanzania tuna misingi yetu kila awamu inayoingia  inategemea misingi ya awamu iliyopita ndio maana tumefika hapa tulipofika.

 “Watanzania wanapenda furaha watanzania hawapendi hofu watanzania ni watii kwa mamlaka, tuendelee kuheshimiana na kuipenda nchi yetu.”

Hata wenye mawazo mbadala Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amefungua mipaka ndio maana anazungumzia R-nne watu wawe na utaratibu wa maridhiano; maelewano, kujenga upya, na kuendelea mbele.

“Tunaiona Tanzania iliyobadilika sana kimaendeleo, lakini imebakia na misingi ile ile iliyoachwa na waasisi wa Taifa letu katika mioyo ya watu.”

Tulivyopata uhuru falsafa ya Baba wa Taifa alisema, Uhuru ni kazi ndio maana wananchi wamejikita katika kufanya kazi.

Awali Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Mpwapwa Mhe. George Fuime amesema nchi imepiga hatua kwenye miundo mbinu ya Mawasiliano.

“Ujenzi wa miundo mbinu ya afya, ujenzi wa miundo mbinu ya elimu, mabadiliko haya yameasisiwa na viongozi wetu kutokana  na Amani na utulivu uliojengwa na wazee wetu.”

Naye muwasilishaji mada Mwl Charles Malugu amesema serikali ya awamu ya sita imefanya ujenzi wa sekondari vyumba 20000, na ujenzi wa vyumba 3000 kwa shule shikizi  ambao utasaidia wanafunzi wa kidato cha kwanza na wanafunzi wa darasa la kwanza kuanza masomo bila kuwa na kikwazo cha aina yoyote.

“Serikali ya awamu ya sita imeruhusu wanafunzi walikatisha masomo kutokana na ujauzito, kuendelea na masomo ili wasikatize ndoto zao.”

 

Read More

Thursday, December 8, 2022

RAIS WA JAMHURI YA WATU WA SAHRAWI ATEMBELEA MJI WA SERIKALI MTUMBA

 

Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Sahrawi, Mhe. Brahim Ghali leo amefanya ziara ndogo katika mji wa Serikali  Mtumba ambapo alitembelea jengo la Ofisi ya Rais Menejiment na Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Katika ziara hiyo ndogo Mhe. Rais Brahim Ghali alikaribishwa na kuoneshwa Mji wa Serikali na Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge na Uratibu ambaye ni Mkurugenzi Msaidizi wa Uratibu Bwn. Omar S Ilyas, pamoja na Mratibu wa Mradi wa Ujenzi wa Mji wa Serikali Bwn.  Meshack Bandawe, ambapo walipata nafasi ya kuonyeshwa kiwanja cha Ubalozi wa Taifa la watu wa Sahrawi.

Read More

Tuesday, December 6, 2022

DKT. GWAJIMA: ELIMU YA LISHE IPEWE KIPAUMBELE

Serikali imesisitiza utoaji wa elimu kwa jamii namna ya kuzingatia masuala ya lishe nchini ili kuwa na Taifa lenye afya bora na kujiletea maendeleo yake.

 

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt.Doroth Gwajima wakati akimwakilisha  Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Kassim Majaliwa  wakati wa Mkutano wa Nane wa Mwaka wa Wadau wa Lishe nchini uliofanyika uwanja wa shule ya Msingi Mukendo  Wilaya ya Musoma Mkoani Mara.

 

Akizugumza kuhusu Mkutano huo alisema, umewezesha washiriki kupata maelezo kuhusu utekelezaji wa afua za lishe kwa kipindi cha mwaka wa kwanza (2021/2022) wa utekelezaji wa Mpango Jumuishi wa Pili wa Kitaifa wa Lishe (2021/22 - 2025/26) na kusema kuwa tathmini hizo ni za muhimu kwani ndio kipimo cha kujua hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa Mpango.

 

Kaulimbiu ya mkutano wa mwaka huu ni“KUONGEZA KASI KATIKA KUBORESHA HALI YA LISHE KWA MAENDELEO YA RASILIMALI WATU NA UCHUMI” .

 

Waziri alisema katika kutekeleza mpango Juishi wa Lishe suala la elimu lina umuhimu wa kipekee kwa kila mmoja ili kufikia malengo.

 

Alifafanua kuwa Serikali itaendelea kutoa kipaumbele juu ya jamii kupewa elimu ya namna ya kuzingatia lishe bora ili kuweza kuepukana na udumavu kwa watoto na kuwa na afya bora.

 

“Ili kupata matokeo chanya katika kuboresha hali ya lishe nchini ni muhimu kuendelea kuhamasisha jamii kuhusu masuala ya lishe. Pamoja na uhamasishaji kufanyika kabla ya mkutano na wakati wa  mkutano huu, natoa rai kwa Taasisi ya Chakula na Lishe na wadau wengine kuhakikisha tunabuni mikakati zaidi ya kufikisha elimu sahihi ya lishe kwa umma ili kusaidia jamii kuelewa changamoto,”Alisisitiza Dkt.  Gwajima

 

Aliekeza  kuwa,  upo  umuhimu  wa  kuwa  na  jitihada za makusudi ili kuhakikisha wadau wa sekta binafsi wanashirikishwa na kuwa na utaratibu mzuri wa kuchangia utekelezaji wa afua za lishe.

 

Aidha, Serikali chini ya uongozi wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea kulipa umuhimu wa kipekee suala la lishe nchini ili kuifanya nchi yetu kuwa na uchumi imara kupitia maendeleo ya viwanda ambapo alieleza kuwa Maendeleo haya hayawezi kupatikana iwapo hatutaimarisha kasi ya kujenga na kulinda kizazi chenye nguvu, afya njema na uwezo wa kufikiri.

 

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Kilimo Mhe. Anthony Mavunde aliasema Wizara yake itaendelea kutoa kipaumbele katika kutenga fedha nyingi kwenye masuala ya lishe na kuimarisha kilimo cha umwagiliaji ili kuchagiza ongezeko la upatikanaji wa chakula nchini.

 

"Uwekezaji katika kilimo utaleta matokeo chanya katika lishe, lazima tuwekeze katika uzalishaji wa mbegu, huduma za ugani, umwagiliaji na miundombinu ya uhifadhi wa mazao ili kufikia malengo kama yalivyotarajiwa," alisema Mhe. Mavunde

Naye, Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega alisema kumekuwa na  chagamoto ya ulaji kwa kutozingatia  kauni za lishe bora inayosababisha changamoto za kifya kwa wengi.

“Takwimu zinaonesha kuwa kiwango cha ulaji wa nyama kwa wastani wa mtu mmoja kwa mwaka ni kilo 15 wakati kiwango kinachopendekezwa na FAO kwa mtu mmoja kwa mwaka ni wastani wa kilo 50, upande wa ulaji wa samaki wastani wa kilo nane na nusu kwa mtu mmoja kwa mwaka, kiwango hichi kipo chini kulinganisha kiwango kinachopendekezwa cha kilo 23 kwa mtu mmoja kwa mwaka, aidha ulaji wa mayai na kuku bado si wa kuridhisha," alisisitiza Ulega.

Aidha  wizara imeendelea kutekeleza afua mbalimbali za kuhamasisha hali ya ulaji nchini ambapo wanahamasisha ulaji na utumiaji mazao ya mifugo kwa kushirikina na wadau mbalimbali sambamba na kuongeza uzalishaji nchini.

 

Read More

Monday, December 5, 2022

FEDHA ZA MAADHIMISHO YA UHURU KUJENGA MABWENI YA SHULE NANE

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene amesema fedha zilizokuwa zimetengwa na Wizara na Taasisi kwa ajili ya Maadhimisho ya Sherehe za Uhuru mwaka huu zitapelekwe Ofisi ya Rais – TAMISEMI nakutumika kujenga mabweni katika shule nane za Msingi za wanafunzi wenye mahitaji maalum hapa nchini.

Taarifa hiyo na Waziri wa Nchi Ofisi ya waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene katika mkutano wake na waandishi wa habari Mjini Dodoma.

“Shilingi Milioni 960,000,000/- (Tshs Milioni Mia Tisa Sitini)  zitatumika kujenga shule ya msingi Buhangija Shinyanga, Goweko Tabora, Darajani Singida, Mtanga Lindi, Songambele Lindi, Msanzi Rukwa,  Idofi Njombe, na Longido Arusha.”

Ni dhamira ya dhati ya Mheshimiwa Rais wetu ya kuwajali na kuwajengea mazingira rafiki watu wenye mahitaji maalum hapa nchini. Hili ni jambo kubwa la kishujaa na la kupongezwa sana na Wananchi wote wa Tanzania.

Aidha Maadhimisho ya Sherehe za Miaka 61 ya Uhuru wa Tanzania Bara mwaka huu 2022 yatafanyika kwa Midahalo na Makongamano mbalimbali yatakayofanyika katika Wilaya zote hapa nchini kujadili, kutafakari kwa pamoja na kukumbuka tulikotoka, tulipo na tunakoelekea kuhusu Maendeleo Endelevu ambayo Nchi yetu adhimu Tanzania imeyafikia. Hivyo hakutakuwa na Gwaride na shughuli nyingine za Kitaifa.

 

Waziri amesema, Maadhimisho ya MIAKA 61 YA UHURU yataadhimishwa kwa Kauli mbiu inayosema  “AMANI NA UMOJA NI NGUZO YA MAENDELEO YETU”.

“Makongamano hayo yatatanguliwa na ratiba mbalimbali kwa Viongozi wa Mikoa na Wilaya kufanya shughuli za Kijamii kama vile kufanya usafi katika maeneo ya Hospitali, shule, nyumba za Wazee na makundi yenye mahitaji maalum”

Waziri ameelekeza Ofisi zote za Serikali hapa nchini kupambwa kwa mapambo ya rangi za Bendera ya Taifa pamoja na picha ya Mheshimiwa Rais.

Read More

MKUU WA WILAYA YA MUSOMA DKT. HAULE AHIMIZA UPANDAJI WA MITI

MKUU wa Wilaya ya Musoma Dkt. Khalifan Haule amehimiza wananchi kuendelea kuwa mstari wa mbele katika upandaji wa miti ya matunda ili kupata matunda na vivuli katika maeneo yao.

 

Ametoa kauli hiyo  wakati wa zoezi la upandaji miti ya matunda katika shule ya Msingi ya Mwisenge iliyopo mkoani Mara.Zoezi hili ni moja ya shughuli zinazoambatana na Mkutano Mkuu wa Nane wa mwaka wa Wadau wa Lishe.

 

Aidha jumla ya miti 300 imetolewa na kugawa katika shule sita ikiwemo; Mwisenge, Mtakuja, Nyarigamba A, Nyarigamba B, Nyabisare na Nyarugusu ambapo kila shule itapewa miti 50.

 

“Leo tunazindua upandaji wa miti hii kwenye shule ya Kihistoria aliyosoma Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyeyere ikiwa ni ishara ya kuunga mkono jitihada za kuhamasisha ulaji wa matunda kwa lengo la kuimarisha masuala ya lishe nchini,”aslisema Dkt. Haule

 

Aidha lengo la zoezi hilo ni kuimarisha utekelezaji wa masuala ya  lishe nchini kwa kuhamasisha ulaji wa matunda na mbogamboga katika jamii zetu.

 

Akizungumza wakati wa zoezi hilo Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Chakula na Lishe nchini Dkt.Germana Leyna amesema taasisi yake imejithatiti kuhakikisha elimu ya masuala ya chakula na lishe bora inatolewa kwa makundi yote ikiwemo watoto waliopo mashuleni.

 

Aliongezea kuwa watu wengi wanakula kwa mazoea na si kula lishe bora hivyo jamii haina budi kubadilisha mitazamo juu ya masuala ya lishe na kuyapa kipaumbele.

 

"Hakuna mtu anayeweza kufanikiwa ikiwa anachamoto za kiafya zinazochangiwa na lishe duni, hivyo kila mmoja anajukumu la kuzingatia lishe bora kwa afya bora,"alisisitiza Dkt. Germana

 

Alitoa neno la Shukrani Mstahiki Meya wa Manispaa la Musoma Kapteni Mstaafu Patrick Gumbo alipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Taasisi ya Chakula na Lishe pamoja na Mkoa kwa kuratibu zoezi hilo huku akitoa rai kwa kila shule kuhakikisha wanatunza miti hiyo ili kutimiza malengo yaliyokusudiwa.

 

"Ni jambo jema limefanyika leo, jukumu lililopo mbele yetu ni kuhakikisha miti inatunzwa na inaleta manufaa kama ilivyokusudiwa," alisema Patrick

 

Naye Mkuu wa Shule hiyo Mwalimu Sigawa Mwita alitoa shukrani kwa kuitumia shule hiyo yenye historia kubwa nchini kwa kuzingatia Rais wa Awamu ya Kwanza Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alisoma hapo na kueleza zoezi hilo ni sehemu ya kumuenzi mwalimu kwa kuzingatia alikuwa kinara wa masuala ya upandaji wa miti.

 

"Shule yetu inajumuisha na wanafunzi wenye mahitaji maalum na imendelea kuwa na ufaulu mzuri sana hii imetupa hamasa na kuonesha mnajali na mnatambua mchango wa shule hii," alisema Mwalimu Mwita

 

Read More

Saturday, December 3, 2022

SERIKALI KUJA NA MAELEKEZO KUIMARISHA UTENDAJI KAZI OFISI ZA KONGA

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene amesema serikali itatoa maelekezo kwa Halmashauri kuweka mipango maalumu ya kuziwezesha ofisi za vikundi vya watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI (Konga) katika maeneo ya usimamizi, ruzuku na mikopo. Ili kuwa imara na endelevu na kuwa na mchango mkubwa katika kufikia malengo ya kitaifa na dunia kuhusu UKIMWI.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene wakati wa uzinduzi wa magari nane ya mradi wa HEBU TUYAJENGE uliofanyika katika Ofisi za NACOPHA Mbezi Beach Dar es salaam.

“Serikali inatambua umuhimu wa mifumo ya kijamii kwa sababu ina mchango mkubwa katika maendeleo ya Taifa. Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Tume ya Kudhibiti UKIMWI itaendelea kuhakikisha Uratibu wa Sera na miongozo unatoa fursa ya kuziwezesha Konga za WAVIU”

Aidha, katika hotuba yake, Mheshimiwa Rais alitoa maelekezo mahususi kwa Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia TACAID, Wizara ya Afya na wadau wengine kuweka jitihada na mikakati madhubuti katika kuzuia maambukizi mapya ili tuweze kufikia hatua ya kutokomeza kabisa.

 Ikiwa ni pamoja na Kuimarisha huduma za upimaji wa VVU na matumizi ya ARV ili kutokomeza vifo vitokanavyo na UKIMWI, kuweka mikakati ya kutokomeza ubaguzi na unyanyapaa kwa WAVIU.

“Ofisi ya Waziri Mkuu chini ya Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb.), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itayatekeleza maelekezo ya Mheshimiwa Rais kwa haraka ikiwa ni pamoja na kuziratibu Wizara husika na Wadau katika kuhakikisha maelekezo haya yanatekelezwa kwa wakati, alisema Waziri.”

Naye Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Bwn. Kaspar Mmuya amewapongeza NACOPHA kwa kazi nzuri ya kupambana na maambukizi ya virusi vya UKIMWI.

“Kuhamasisha watu kujitokeza na kupima afya zao ni njia mojawapo ya kukabiliana na maambukizi mapya ya virusi vya UKIMWI.”

Akitoa taarifa Mwenyekiti wa Baraza la Watu Wanaoishi na Virusi vya UKIMWI (NACOPHA) Bi, Leticia Mourice Kapela, amesema baraza limeneemeka kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu kwa upande wa vijana, wanawake na WAVIU kwa ujumla.

“Uwezeshi huu katika fursa za mafunzo, mitaji ya kifedha, vifaa vya kuanzia shughuli za ujasiriamali, umesaidia vijana WAVIU kupata ujasiri wa kukabiliana na kuziepuka changamoto mbalimbali zinazowaweka katika hatari ya kupata maambukizi, ikiwemo kuanza ngono katika umri mdogo, kuwa na mahusiano na watu wenye umri mkubwa  na ulevi wa kupindukia”

Naye Mkurugenzi TACAIDS Bi. Audrey Njelekela, amesema Konga ziko kwenye Halmashauri 184 na Afua zote zinatekelezwa kwa kushirikiana na Halmashauri.

“Kupata magari kutasaidia kuongeza kasi na ufanisi katika kuhakikisha muitikio wa kitaifa unatekelezwa”

Read More