Friday, June 19, 2026

WITO WATOLEWA WANANCHI KUTEMBELEA BANDA LA OWM MAONESHO YA WIKI YA UTUMISHI


Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu kupitia Wakala wa Serikali wa Uchapaji Tanzania inawaalika wananchi kutembelea Banda la Ofisi hiyo kwenye Maonesho ya Wiki ya Utumishi ili kupata elimu kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa ikiwemo uchapishaji wa  Sheria, Kanuni, Katiba ya Tanzania, machapisho mbalimbali ya vitambulisho vitambulisho, vyeti na nyaraka zote za kiserikali.

Wito huo umetolewa leo katika viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma na Afisa Biashara Bi. Witness  Njunde kutoka Wakala wa Serikali wa Uchapaji Tanzania wakati akizungumzia kuhusu huduma zinazotolewa na Wakala huyo wa Serikali.

Bi. Njunde amesema “Moja ya kazi tunazofanya ni kuchapisha  gazeti la Serikali, Gazeti hili la Serikali limebeba maudhui ambayo ni ya kiserikali na kibinafsi. Katika maudhui ya kibinafsi huwa linatangaza mabadiliko ya majina, mirathi, kupotea kwa leseni za makazi, kufungwa kwa makampuni hali kadhalika pindi mtu anapopotelewa na vyeti vyake vya shule, passport, leseni zote hizo tunatangaza katika gazeti la serikali”.

Aidha, ameongeza kuwa, Gazeti hilo la Serikali huwa linatangazwa mara moja kwa wiki kila ijumaa  na nakala laini ya gazeti hilo huwekwa katika tovuti ya Ofisi ya Waziri Mkuu au Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora.

Read More

Thursday, June 18, 2026

OWM YATHIBITISHA NYENZO MUHIMU ZA KUIMARISHA USIMAMIZI WA MAAFA NCHINI

 

SERIKALI imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini ili kuongeza uwezo wa kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali baada ya maafa, kufuatia kuongezeka kwa matukio yanayochochewa na mabadiliko ya tabianchi pamoja na vihatarishi vingine vya asili na kijamii.

Hayo yameelezwa  jijini Dodoma na Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, wakati akifungua Kikao cha Jukwaa la Taifa la Wadau wa Usimamizi wa Maafa kilicholenga kupitia na kuthibitisha Mwongozo wa Urejeshaji Hali Baada ya Maafa, Mwongozo wa Uendeshaji na Uratibu wa Uhawilishaji Fedha kwa Walioathirika wa Maafa, pamoja na Mfumo wa Usimamizi wa Taarifa za Maafa (DMIS).

Brigedia Jenerali Ndagala amesema kuwa katika miaka ya hivi karibuni Tanzania imekumbwa na matukio mbalimbali ya maafa yakiwemo mafuriko, ukame, maporomoko ya ardhi, upepo mkali, magonjwa ya mlipuko na ajali mbalimbali, hali ambayo imeathiri maisha ya wananchi, miundombinu, mazingira na shughuli za kiuchumi.

“Kwa kuzingatia hali hiyo, Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu imeendelea kuimarisha sera, mifumo, mikakati, mipango na nyenzo mbalimbali za usimamizi wa maafa ili kuhakikisha hatua zote za kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali baada ya maafa zinafanyika kwa ufanisi na kwa kuzingatia matakwa ya Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 6 ya Mwaka 2022,” amesema.

Amesema kikao hicho ni hatua muhimu katika kuimarisha uratibu wa kitaifa wa usimamizi wa maafa kwa kuwa kinahusisha uthibitishaji wa nyenzo tatu muhimu zitakazochangia uwazi, uwajibikaji na ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi wakati wa maafa na baada ya maafa.

Kwa mujibu wa Brigedia Jenerali Ndagala, Mwongozo wa Urejeshaji Hali Baada ya Maafa utaweka mfumo wa pamoja wa kitaifa wa kupanga na kuratibu shughuli za urejeshaji baada ya maafa, huku Mwongozo wa Uhawilishaji Fedha kwa Walioathirika wa Maafa ukiboresha utaratibu wa utoaji wa misaada ya fedha kwa waathirika. Aidha, Mfumo wa Usimamizi wa Taarifa za Maafa (DMIS) utaimarisha ukusanyaji, uchambuzi, uhifadhi na matumizi ya taarifa za maafa kwa ajili ya kufanya maamuzi sahihi na kwa wakati.

“Nyenzo hizi zina mchango mkubwa katika utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 6 ya Mwaka 2022 kwa kuimarisha usimamizi wa taarifa, uratibu wa wadau, utoaji wa misaada na shughuli za urejeshaji hali baada ya maafa. Vilevile, zinachangia utekelezaji wa Mfumo wa Sendai wa Kupunguza Hatari za Maafa kwa kuimarisha uelewa wa hatari za maafa, usimamizi wa vihatarishi, uwekezaji katika ustahimilivu na kuimarisha hatua za kujiandaa na kujenga upya kwa ubora zaidi baada ya maafa,” amesisitiza.

Ameeleza kuwa mafanikio yanayoendelea kupatikana katika sekta ya usimamizi wa maafa nchini yanatokana na ushirikiano madhubuti kati ya Serikali na wadau wa maendeleo, mashirika ya Umoja wa Mataifa, sekta binafsi na asasi za kiraia.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF), Bi. Judith Bihondwa, amesema shirika hilo litaendelea kushirikiana na Serikali katika kuimarisha uwezo wa jamii kukabiliana na maafa pamoja na kujenga ustahimilivu dhidi ya majanga mbalimbali.

Amesema ushirikiano huo utaendelea kulenga kuimarisha mifumo ya maandalizi, mwitikio na urejeshaji hali baada ya maafa kwa kuzingatia makundi yote ya jamii, hususan watoto na watu walio katika mazingira hatarishi.

Kikao hicho kimewakutanisha wadau mbalimbali wa usimamizi wa maafa kutoka taasisi za Serikali, mashirika ya Umoja wa Mataifa, asasi za kiraia na wadau wa maendeleo kwa lengo la kujadili na kuthibitisha nyenzo zitakazochangia kuimarisha usimamizi wa maafa na kuongeza ustahimilivu wa jamii nchini.

 

Read More

Wednesday, June 17, 2026

OWM YASHIRIKI MAONESHO YA WIKI YA UTUMISHI WA UMMA 2026


 Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Stella Mwaiswaga pamoja na Watumishi wengine kutoka Ofisi hiyo wameshiriki ufunguzi wa Maonesho ya Wiki ya Utumishi tarehe 17 Juni, 2026 katika viwanja vya Chinangali Park Jijini Dodoma.

Maonesho ya Wiki ya Utumishi ni moja ya matukio katika kalenda ya Umoja wa Afrika (AU) ambapo nchi wanachama huadhimisha kwa kaulimbiu moja na kufanya maonesho ya kazi mbalimbali kuhusu masuala ya Utumishi wa Umma ambapo hufanyika kila mwaka kuanzia tarehe 16 hadi 23 Juni.

Kwa mwaka huu Maadhimisho hayo yamebeba kaulimbiu isemayo; “Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi wa Huduma Endelevu”.

Sambamba na hilo Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu inashiriki maonesho hayo huku ikitoa elimu mbalimbali kwa umma kuhusiana na shughuli za Wakala Serikali wa uchapishaji Tanzania, elimu kuhusu masuala ya Menejimenti ya Maafa, Watu wenye Ulemavu, Ufuatiliaji na Tathimini pamoja na Masuala ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi.

Read More

Saturday, June 13, 2026

MGONGANO WA MASLAHI WATAJWA KURUDISHA NYUMA MAENDELEO


Mgongano wa maslahi kwa watumishi wa umma umetajwa kuathiri ufanisi kwenye utendaji na majukumu ya Serikali kutokana na matokeo hasi ya vitendo hivyo vinavyopelekea kuchochea mazingira ya rushwa na kujinufaisha binafsi badala ya ofisi na kukwamisha utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

Hayo yameelezwa mapema mwishoni mwa wiki Jijini Arusha na Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Stella Mwaiswaga wakati akifunga mafunzo kwa wajumbe wa Kamati Maalum ya Menejimenti ya ofisi hiyo yaliyolenga kuwajengea uwezo wajumbe hao katika kusimamia masuala ya uadilifu sehemu za kazi .

Aliongezea kuwa ni muhimu kuendelea kuzingatia taratibu, kanuni na sheria za utumishi wa umma ili kuepuka vitendo vinavyoathiri utendaji wa watumishi hasa katika kujali maslahi binafsi yanayochochea kukosekana kwa huduma bora kwa wananchi.

Alisema kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu imeendelea kuwa Ofisi ya mfano katika masuala ya Uratibu wa Shughuli za Serikali hivyo ni wajibu wa kila mtumishi kuendelea kuzingatia masuala ya uadilifu ikiwemo la kujilinda na vitendo vyote vinavyoweza kuharibu taswira ya ofisi hiyo.

Akiwasilisha mada kuhusu masuala ya dhana ya Mgongano wa Maslahi, Katibu Msaidizi Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Kaskazini Bw. Gerald Mwaitebele amesema ni vyema kuzingatia na kuepuka masuala ya mgongano wa maslahi katika maeneo ya kazi kwani yameendelea kuwa chachu ya kuondoa ufanisi na uwazi wa ofisi zetu.

Aliongezea kuwa,kiongozi anayetekeleza majukumu kwa kujali maslahi binafsi humpelekea kutokuwa na maamuzi sahihi na kusababisha kuharibu utendaji wa taasisi na ofisi anayoihudumia hivyo kuondoa uaminifu kwa jamii, hadi ngazi ya Taifa.

"Mgongano wa maslahi hutokea pale ambapo maslahi yako binafsi (kifedha, kijamii au kindugu) yanapokinzana na majukumu yako ya kikazi. Hali hii inapaswa kuepukwa kwani inaharibu uadilifu, inasababisha upendeleo, na inaweza kuondoa uaminifu wa umma au wa taasisi tunazofanyia kazi," alisisitiza Mwaitebele.

Akitoa neno la shukran kwa niaba ya wajumbe wa kamati hiyo, Bi.Ngole Keya, Naibu Katibu wa Mheshimiwa Waziri Mkuu ameshukuru mafunzo hayo yenye lengo la kuwajengea uelewa na kuendelea kuwakumbusha masuala ya msingi katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku.

“Kipekee tunawapongeza watoa mada wametujenga na kutupa maarifa zaidi katika kuendelea kuboresha utendaji wetu ili kuendelea kutoa huduma bora na kuhakikisha tunaendelea vyema na majukumu yetu ikiwemo la kuratibu shughuli za Serikali kwa kuzingatia misingi na kanuni za kiutumishi zinavyoelekeza,” alisema Bi.Ngole.

 

Read More

Friday, June 12, 2026

SERIKALI YASISITIZA UMUHIMU WA UADILIFU KATIKA UTUMISHI WA UMMA


 SERIKALI imeendelea kusisitiza umuhimu wa kuzingatia misingi ya uadilifu katika utumishi wa umma ili kuhakikisha utekelezaji wa majukumu na mipango ya maendeleo unafanyika kwa ufanisi na kwa kuzingatia maadili ya kazi.

Hayo yamesemwa hii leo  na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, wakati akifungua Mafunzo ya Kamati ya Uadilifu yaliyolenga kuwajengea uwezo wajumbe wa Kamati Maalum ya Menejimenti katika kusimamia masuala ya uadilifu katika ofisi hiyo.

“Uadilifu ni nguzo muhimu katika ufanikishaji wa majukumu na utekelezaji wa mipango ya maendeleo katika sehemu za kazi,” amesema Dkt. Yonazi.

Dkt. Yonazi amesema kuwa ni wajibu wa kila mtumishi wa umma kuhakikisha anazingatia maadili ya kazi na kulinda misingi ya uadilifu ili kuimarisha utendaji na kuongeza imani ya wananchi kwa Serikali.

Aidha, Dkt. Yonazi amesema mafunzo hayo yanalenga kuwawezesha wajumbe kusimamia utekelezaji wa Mkakati wa Uadilifu kwa kuhakikisha unaingizwa katika mipango kazi na bajeti za mwaka za taasisi.

Vilevile, amebainisha kuwa Kamati za Uadilifu zina jukumu la kusimamia utekelezaji wa sera dhidi ya rushwa na kuhakikisha watumishi wanazingatia sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma.

“Kuna umuhimu wa kuimarisha uwazi na uwajibikaji pamoja na kuanzisha mifumo madhubuti ya kupokea na kushughulikia malalamiko ya wananchi kwa kuzingatia usiri.

Akiwasilisha mada ya masuala ya Mkakati wa Taifa Dhidi ya Rushwa na Mpango wa Utekelezaji (NACSAP IV) 2023-2030 Mkurugenzi kutoka Ofisi ya Rais Ikulu Bw. Andrew Massawe amesema, ni wajibu wa watumishi kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu na kupinga vitendo vyote vinavyoashiria mazingira ya rushwa ili kuendelea kuhudumia wananchi, na Taifa kwa ujumla katika misingi sahihi ya utumishi wa umma.

“Tufanye kazi kwa uadilifu na kuzingatia masuala ya huduma bora kwa wateja, tusihudumie watu kama favor bali tutoe huduma kwa viwango bora vinavyotakiwa,”alisema Bw. Massawe

 

Read More

Thursday, June 11, 2026

TANZANIA YAELEZA MAFANIKIO YA UJUMUISHWAJI WA WATU WENYE ULEMAVU, YAAHIDI KUIMARISHA UPATIKANAJI WA TEKNOLOJIA SAIDIZI.


Serikali ya Tanzania imeeleza mafanikio makubwa iliyoyapata katika kuimarisha ustawi na ujumuishwaji wa watu wenye ulemavu, huku ikisisitiza umuhimu wa kuongeza upatikanaji wa vifaa na teknolojia saidizi ili kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii na kiuchumi.

 Akihitimisha ushiriki wa Tanzania katika Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19-CRPD) uliofanyika New York, Marekani, Juni 11, 2026, Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, amesema teknolojia na vifaa saidizi vina mchango mkubwa katika kuwawezesha watu wenye ulemavu kuishi kwa kujitegemea na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya jamii.

“Ni muhimu kuendelea kuongeza upatikanaji na matumizi ya vifaa na teknolojia saidizi kwa watu wenye ulemavu ili kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii na kiuchumi kwa usawa pia Serikali inaendelea kutekeleza kwa vitendo dhana ya ujumuishwaji kwa kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata fursa na haki kwa usawa katika sekta mbalimbali za kijamii na kiuchumi,” alisema  Mhe. Mahundi.

 Akizungumza kwa niaba ya Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Naibu Katibu Mkuu, Dkt. James Kilabuko, amesema ushiriki wa Tanzania katika mkutano huo umeiwezesha nchi kujifunza uzoefu na mbinu mbalimbali za kukabiliana na changamoto zinazowakabili watu wenye ulemavu.

“Tanzania imepiga hatua kubwa katika uwezeshaji na ushirikishwaji wa watu wenye ulemavu hivyo Kupitia mkutano huu, tumejifunza mbinu na uzoefu kutoka mataifa mbalimbali ambazo zitatusaidia kuimarisha zaidi juhudi zetu, lakini pia Serikali itaandaa mpango kazi mahususi kwa kushirikiana na wizara, taasisi na wadau mbalimbali ili kuendeleza utekelezaji wa masuala ya watu wenye ulemavu na kushughulikia changamoto zilizobainishwa wakati wa mkutano huu.,” alisema Dkt. Kilabuko.

 Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Grace Maghembe, amesema Tanzania imeendelea kuboresha huduma za afya za msingi kwa watu wenye ulemavu kwa kusogeza huduma karibu na wananchi kuanzia ngazi ya jamii, sambamba na kuboresha miundombinu ya afya na kuwajengea uwezo watumishi wa sekta hiyo katika utoaji wa huduma jumuishi.

Aidha, ameshauri Shirika la Afya Duniani (WHO) kuangalia uwezekano wa kutumia mifumo inayotumika katika upatikanaji wa chanjo na dawa muhimu duniani ili kuboresha upatikanaji wa vifaa saidizi kwa watu wenye ulemavu, hususan katika nchi zinazoendelea.

Mkutano wa COSP19 umezikutanisha nchi wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu kujadili mafanikio, changamoto na mikakati ya kuimarisha haki, ushiriki na ustawi wa watu wenye ulemavu duniani.

 

 

 

 

 

 

Read More

OWM YATOA MAFUNZO KWA VITENDO KWA WANAFUNZI WA SHAHADA YA USIMAMIZI WA HATARI ZA MAAFA KUTOKA UDOM

KATIKA kuendelea kuimarika kwa sekta ya usimamizi wa maafa nchini na kuongezeka kwa hamasa ya kujifunza mifumo ya usimamizi wa maafa, tahadhari ya mapema na uratibu wa dharura, wanafunzi wa Shahada ya Usimamizi wa Hatari za Maafa kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) wamefanya ziara ya mafunzo kupitia Idara ya Usimamizi wa Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu).

Ziara hiyo imefanyika tarehe 10 na 11 Juni, 2026 iliyolenga kuwajengea uelewa kwa vitendo kuhusu mifumo ya usimamizi wa maafa, ufuatiliaji wa vihatarishi mbalimbali, utoaji wa taarifa za tahadhari ya mapema pamoja na uratibu wa operesheni za dharura nchini.

Katika ziara hiyo, wanafunzi walitembelea Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura kilichopo Ngome, Chumba cha Ufuatiliaji wa Mienendo ya Majanga na Tahadhari za Mapema kilichopo Mtumba pamoja na eneo la ujenzi wa Kituo Kikuu cha Taifa cha Usimamizi wa Maafa na Maghala ya Kuhifadhi Vifaa vya Dharura kilichopo Nzughuni, jijini Dodoma.

Akizungumza na wanafunzi hao, Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo Dkt. Jim Yonazi, aliwapongeza kwa uamuzi wao wa kujifunza kwa vitendo kuhusu masuala ya usimamizi wa maafa na kuonesha dhamira ya kuchangia maendeleo ya sekta hiyo nchini.

Dkt. Yonazi aliwahimiza wanafunzi kuendelea kujiongezea maarifa kupitia tafiti, ubunifu na uandishi wa machapisho mbalimbali kuhusu usimamizi wa hatari za maafa ili kuchangia katika kuimarisha uwezo wa Taifa wa kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali baada ya maafa.

Aidha, aliwahakikishia kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za elimu ya juu katika kukuza taaluma ya usimamizi wa maafa na kuahidi kutembelea Chuo Kikuu cha Dodoma siku zijazo kwa ajili ya kutoa mihadhara na kushiriki katika mijadala ya kitaaluma.

“Ziara yenu ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za elimu ya juu na Serikali katika kujenga kizazi cha wataalamu wenye uelewa wa kina kuhusu usimamizi wa hatari za maafa, tahadhari ya mapema na uratibu wa dharura. Aidha, inaonesha mafanikio ya uwekezaji uliofanywa na Serikali katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa, jambo ambalo limeendelea kuvutia wadau mbalimbali, watafiti na wanafunzi kutoka ndani na nje ya nchi kujifunza na kubadilishana uzoefu,”alisema Dkt. Yonazi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Maafa, Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, aliwaeleza wanafunzi hao kuwa wamefanya jambo la msingi kwa kutenga muda wa kujifunza na kushuhudia kwa vitendo namna Serikali inavyotekeleza majukumu yake ya usimamizi wa maafa nchini.

Alisema kuwa mifumo iliyowekwa na Serikali katika ufuatiliaji wa vihatarishi, utoaji wa tahadhari za mapema na uratibu wa operesheni za dharura ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha usalama wa wananchi na mali zao dhidi ya madhara yatokanayo na maafa mbalimbali.

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, Bi. Jane Alfred Kikunya, ambaye aliongoza mafunzo hayo, alisema ameridhishwa na hamasa na ari kubwa iliyooneshwa na wanafunzi katika kujifunza masuala ya usimamizi wa maafa na tahadhari ya mapema.

Bi. Jane alieleza kuwa ujio wa wanafunzi hao unaonesha namna sekta ya usimamizi wa maafa inavyoendelea kupata umuhimu katika jamii na taasisi za elimu ya juu. Aliongeza kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu itaendelea kufungua milango kwa wanafunzi, watafiti na wadau mbalimbali wanaotaka kujifunza kuhusu mifumo ya ufuatiliaji wa majanga, uchambuzi wa vihatarishi, tahadhari za mapema na uratibu wa operesheni za dharura kutembelea ofisi hiyo.

Kwa upande wake, Dkt. Japhet Ringo kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma ambaye aliambatana na wanafunzi hao, aliishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuwapatia wanafunzi fursa ya kujifunza kwa vitendo kuhusu mifumo ya usimamizi wa maafa nchini.

Dkt. Ringo alisema kuwa ziara hiyo imekuwa darasa muhimu lililowawezesha wanafunzi kuunganisha maarifa ya kinadharia wanayojifunza darasani na utekelezaji halisi wa shughuli za usimamizi wa maafa katika ngazi ya Taifa.

Aliongeza kuwa Chuo Kikuu cha Dodoma kitaendelea kushirikiana na Serikali katika kukuza tafiti, ubunifu na maendeleo ya taaluma ya usimamizi wa hatari za maafa ili kusaidia juhudi za Taifa za kujenga ustahimilivu dhidi ya majanga mbalimbali.

 

 

Read More

Wednesday, June 10, 2026

OWM YATOA MAFUNZO KWA VITENDO KWA WANAFUNZI WA SHAHADA YA USIMAMIZI WA HATARI ZA MAAFA KUTOKA UDOM


 KATIKA kuendelea kuimarika kwa sekta ya usimamizi wa maafa nchini na kuongezeka kwa hamasa ya kujifunza mifumo ya usimamizi wa maafa, tahadhari ya mapema na uratibu wa dharura, wanafunzi wa Shahada ya Usimamizi wa Hatari za Maafa kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) wamefanya ziara ya mafunzo kupitia Idara ya Usimamizi wa Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu).

Ziara hiyo imefanyika tarehe 10 na 11 Juni, 2026 iliyolenga kuwajengea uelewa kwa vitendo kuhusu mifumo ya usimamizi wa maafa, ufuatiliaji wa vihatarishi mbalimbali, utoaji wa taarifa za tahadhari ya mapema pamoja na uratibu wa operesheni za dharura nchini.

Katika ziara hiyo, wanafunzi walitembelea Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura kilichopo Ngome, Chumba cha Ufuatiliaji wa Mienendo ya Majanga na Tahadhari za Mapema kilichopo Mtumba pamoja na eneo la ujenzi wa Kituo Kikuu cha Taifa cha Usimamizi wa Maafa na Maghala ya Kuhifadhi Vifaa vya Dharura kilichopo Nzughuni, jijini Dodoma.

Akizungumza na wanafunzi hao, Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo Dkt. Jim Yonazi, aliwapongeza kwa uamuzi wao wa kujifunza kwa vitendo kuhusu masuala ya usimamizi wa maafa na kuonesha dhamira ya kuchangia maendeleo ya sekta hiyo nchini.

Dkt. Yonazi aliwahimiza wanafunzi kuendelea kujiongezea maarifa kupitia tafiti, ubunifu na uandishi wa machapisho mbalimbali kuhusu usimamizi wa hatari za maafa ili kuchangia katika kuimarisha uwezo wa Taifa wa kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali baada ya maafa.

Aidha, aliwahakikishia kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za elimu ya juu katika kukuza taaluma ya usimamizi wa maafa na kuahidi kutembelea Chuo Kikuu cha Dodoma siku zijazo kwa ajili ya kutoa mihadhara na kushiriki katika mijadala ya kitaaluma.

“Ziara yenu ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za elimu ya juu na Serikali katika kujenga kizazi cha wataalamu wenye uelewa wa kina kuhusu usimamizi wa hatari za maafa, tahadhari ya mapema na uratibu wa dharura. Aidha, inaonesha mafanikio ya uwekezaji uliofanywa na Serikali katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa, jambo ambalo limeendelea kuvutia wadau mbalimbali, watafiti na wanafunzi kutoka ndani na nje ya nchi kujifunza na kubadilishana uzoefu,”alisema Dkt. Yonazi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Maafa, Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, aliwaeleza wanafunzi hao kuwa wamefanya jambo la msingi kwa kutenga muda wa kujifunza na kushuhudia kwa vitendo namna Serikali inavyotekeleza majukumu yake ya usimamizi wa maafa nchini.

Alisema kuwa mifumo iliyowekwa na Serikali katika ufuatiliaji wa vihatarishi, utoaji wa tahadhari za mapema na uratibu wa operesheni za dharura ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha usalama wa wananchi na mali zao dhidi ya madhara yatokanayo na maafa mbalimbali.

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, Bi. Jane Alfred Kikunya, ambaye aliongoza mafunzo hayo, alisema ameridhishwa na hamasa na ari kubwa iliyooneshwa na wanafunzi katika kujifunza masuala ya usimamizi wa maafa na tahadhari ya mapema.

Bi. Jane alieleza kuwa ujio wa wanafunzi hao unaonesha namna sekta ya usimamizi wa maafa inavyoendelea kupata umuhimu katika jamii na taasisi za elimu ya juu. Aliongeza kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu itaendelea kufungua milango kwa wanafunzi, watafiti na wadau mbalimbali wanaotaka kujifunza kuhusu mifumo ya ufuatiliaji wa majanga, uchambuzi wa vihatarishi, tahadhari za mapema na uratibu wa operesheni za dharura kutembelea ofisi hiyo.

Kwa upande wake, Dkt. Japhet Ringo kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma ambaye aliambatana na wanafunzi hao, aliishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuwapatia wanafunzi fursa ya kujifunza kwa vitendo kuhusu mifumo ya usimamizi wa maafa nchini.

Dkt. Ringo alisema kuwa ziara hiyo imekuwa darasa muhimu lililowawezesha wanafunzi kuunganisha maarifa ya kinadharia wanayojifunza darasani na utekelezaji halisi wa shughuli za usimamizi wa maafa katika ngazi ya Taifa.

Aliongeza kuwa Chuo Kikuu cha Dodoma kitaendelea kushirikiana na Serikali katika kukuza tafiti, ubunifu na maendeleo ya taaluma ya usimamizi wa hatari za maafa ili kusaidia juhudi za Taifa za kujenga ustahimilivu dhidi ya majanga mbalimbali.

 

 

Read More

TANZANIA YAONGOZA MJADALA WA KIMATAIFA KUHUSU UIMARISHAJI WA HUDUMA NA MSAADA KWA WATU WENYE ULEMAVU


 Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Mhe. Balozi Togolani Mavura, ameongoza mjadala wa ngazi ya juu katika Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19), uliojikita katika mada ndogo ya “Jamii Imara: Kuimarisha Mifumo ya Huduma na Msaada ili Kuhakikisha Uwezeshaji, Uhuru na Kujitegemea kwa Watu Wote Wenye Ulemavu.”

 Akifungua mjadala huo, Mhe. Balozi Togolani  amesema huduma na mifumo ya msaada ni msingi muhimu wa ustawi wa watu binafsi, jamii na uchumi kwa ujumla, huku akisisitiza kuwa utekelezaji wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu umeleta mafanikio makubwa duniani katika kipindi cha miaka 20 tangu kupitishwa kwake.

 "licha ya hatua zilizofikiwa, bado watu wengi wenye ulemavu wanakabiliwa na changamoto za kupata huduma na msaada unaokidhi mahitaji yao, hali iliyodhihirika zaidi wakati wa janga la UVIKO-19 ambapo mifumo mingi ya huduma ilionekana kutokuwa imara na jumuishi vya kutosha hivyo ni muhimu  kuimarisha huduma za usaidizi binafsi, huduma za urekebishaji na uendelezaji uwezo, vifaa saidizi, mifumo ya hifadhi ya jamii pamoja na huduma za kijamii zinazotolewa katika ngazi ya jamii katika kuwawezesha watu wenye ulemavu kufanya maamuzi yao wenyewe, kuishi kwa kujitegemea na kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii, kiuchumi na kisiasa."Alisema Mhe. Balozi Togolani.

 Aidha, amesema kuwa uwekezaji katika mifumo ya huduma na msaada si suala la maendeleo pekee bali ni wajibu wa kuheshimu haki za binadamu, huku akizitaka serikali, mashirika ya maendeleo, asasi za kiraia, mashirika ya watu wenye ulemavu na wadau wengine kushirikiana kwa karibu ili kuziba mapengo yaliyopo na kuharakisha utekelezaji wa sera na programu zinazolenga kujenga jamii jumuishi na himilivu.

 Kwa upande wake Afisa  Sheria kutoka kitengo cha  Watu Wenye Ulemavu,Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Bw. Jacob C. Mwinula, akiwasilisha uzoefu wa Tanzania katika kuimarisha mifumo ya huduma na msaada kwa watu wenye ulemavu wakati wa mjadala (Roundtable Discussion) ameeleza hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kuimarisha ujumuishaji, kujitegemea na ushiriki wa watu wenye ulemavu kupitia sera, sheria, mifumo ya hifadhi ya jamii, huduma za afya, elimu jumuishi na uwezeshaji wa kiuchumi.

 


Read More

TANZANIA NA KANADA ZAIMARISHA USHIRIKIANO KATIKA KUENDELEZA HAKI ZA WATU WENYE ULEMAVU


 Tanzania na Kanada zimejadili fursa za kuimarisha ushirikiano katika kukuza haki, ujumuishwaji na ustawi wa watu wenye ulemavu katika kikao cha pande mbili kilichofanyika leo Juni 10, 2026 katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa New York, Marekani, pembezoni mwa Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19).

 Kikao hicho kiliwakutanisha Naibu Waziri wa Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kutoka Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi na Katibu wa Bunge anayeshughulikia Masuala ya watu wenye Ulemavu Mhe. Leslie Church kutoka Kanada pamoja na viongozi na wataalamu mbalimbali wa masuala ya watu wenye ulemavu kutoka pande zote mbili.

 Akizungumza katika kikao hicho,Mhe. Mahundi ameeleza kuwa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 imeweka kipaumbele katika kujenga taifa jumuishi ambapo watu wenye ulemavu wanatambuliwa kama wadau muhimu wa maendeleo na wanapewa fursa sawa katika elimu, afya, ajira na kinga ya jamii.

 Pia, Pande hizo mbili zilijadiliana kuhusu namna ya kuimarisha ajira kwa watu wenye ulemavu, ambapo Tanzania ilieleza utekelezaji wa Sheria ya Watu Wenye Ulemavu ya mwaka 2010 inayotaka waajiri wenye wafanyakazi 20 au zaidi kuhakikisha angalau asilimia tatu ya watumishi wao ni watu wenye ulemavu na wenye sifa stahiki.

 Kwa Upande wake, Mhe.Leslie Church ameishauri Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania juu ya Uimarishwaji wa mifumo ya kinga ya jamii, uwezeshaji wa kiuchumi kwa watu wenye ulemavu na utoaji wa elimu kwa umma juu ya aina zote za ulemavu na uwezo wa kundi hili, hali itakayosaidia kuepuka unyanyapaa kwa watu wenye ulemavu ili kuimarisha maisha huru na kuongeza fursa za kiuchumi kupitia mafunzo ya ujuzi, mikopo na programu za kinga ya jamii.

 Katika majadiliano hayo, Tanzania na Kanada zilionesha nia ya kuendelea kushirikiana katika maeneo ya uboreshaji wa sheria na viwango vya upatikanaji wa huduma kwa watu wenye ulemavu, ukusanyaji wa takwimu, utekelezaji wa sera na sheria za watu wenye ulemavu pamoja na programu za ajira jumuishi.

 Kikao hicho kilihitimishwa kwa pande zote mbili kueleza utayari wa kuimarisha ushirikiano na kubadilishana uzoefu ili kuhakikisha haki za watu wenye ulemavu zinatambuliwa, kulindwa na kutekelezwa kikamilifu kwa manufaa ya jamii jumuishi na endelevu

 


Read More

Tuesday, June 9, 2026

TANZANIA YAIELEZEA DUNIA HATUA ZILIZOPIGWA KATIKA KULINDA HAKI ZA WATU WENYE ULEMAVU.

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, ameieleza Jumuiya ya Kimataifa hatua kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kulinda na kuendeleza haki za watu wenye ulemavu, wakati aliposhiriki Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani.

 Mhe. Mahundi, ambaye amemuwakilisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge na Uratibu  na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Palamagamba John Kabudi, amesema Tanzania imeendelea kuimarisha mifumo ya kisheria, kisera na kiutendaji ili kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata haki, fursa na huduma stahiki kama wananchi wengine.

 Akiwasilisha taarifa ya nchi, Mhe. Mahundi amesema Tanzania imepiga hatua kubwa kupitia Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na. 9 ya mwaka 2010 kwa Tanzania Bara pamoja na Sheria Na. 8 ya mwaka 2022 ya Zanzibar, ambazo zimeweka msingi imara wa kulinda haki na ustawi wa watu wenye ulemavu.

 “Masuala ya ulemavu yamejumuishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na mipango mbalimbali ya maendeleo ili kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma katika safari ya maendeleo ya taifa na kusema kuwa Serikali imeendelea kupanua upatikanaji wa elimu jumuishi, huduma za afya, huduma za urekebishaji na tiba, teknolojia saidizi, programu za uwezeshaji kiuchumi pamoja na huduma za hifadhi ya jamii kwa watu wenye ulemavu” amesema Mhe. Mahundi

 Aidha  Mhe. Mahundi amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi wake madhubuti na dhamira ya dhati ya kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata huduma bora na fursa zinazowawezesha kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi.

 “Serikali ya Tanzania itaendelea kushirikiana na nchi wanachama, Umoja wa Mataifa, asasi za kiraia na watu wenye ulemavu wenyewe katika kuharakisha utekelezaji wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu na kujenga jamii jumuishi inayoheshimu usawa, utu na haki za kila mtu,” amesema Mhe. Mahundi

 Mkutano huo wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu umebeba kaulimbiu inayosema “CRPD at 20: Celebrating and Consolidating Achievements and Shaping the Next Phase of Implementation in a Changing World,” ukilenga kutathmini mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 20 tangu kuanzishwa kwa mkataba huo na kuweka mikakati ya kuendeleza utekelezaji wake duniani.

 

 

 

Read More

Monday, June 8, 2026

OWM, DIT YAINGIA MAKUBALIANO KUIMARISHA USIMAMIZI WA MAAFA NCHINI

 SERIKALI kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) imeingia Makubaliano ya Ushirikiano (MoU) na Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam (DIT) yenye lengo la kuimarisha usimamizi wa maafa nchini kwa kutumia sayansi, teknolojia na ubunifu.

Akizungumza mapema hii leo  katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo Katibu Mkuu wa ofisi hiyo, Dkt. Jim Yonazi, amesema hatua hiyo ni utekelezaji wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa  Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kujenga mifumo madhubuti ya kiutendaji inayoongozwa na maarifa, sayansi na teknolojia ikiwemo matumizi ya Akili Unde (AI) katika kukabiliana na maafa.

Amesema makubaliano hayo yanatekeleza pia mapendekezo ya Mkutano wa Nane wa Umoja wa Mataifa wa Jukwaa la Dunia la Upunguzaji wa Vihatarishi vya Maafa uliofanyika Geneva, Uswisi, mwezi Juni 2025, na yanaashiria mabadiliko ya kimkakati katika namna Serikali inavyoshughulikia changamoto za maafa kutoka mfumo wa kusubiri majanga hadi mfumo wa kujikita katika kinga, maandalizi na tahadhari.

“Vyuo vikuu na taasisi za utafiti, ikiwemo Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam, zina jukumu muhimu la kuzalisha maarifa na suluhisho za kisayansi zitakazosaidia kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini,”amesema.

Ameongeza kuwa ili kuhakikisha utekelezaji madhubuti wa makubaliano hayo, Serikali itaandaa Mpango Kazi wa utekelezaji pamoja na Agenda ya Kitaifa ya Utafiti wa Usimamizi wa Maafa itakayobainisha maeneo ya kipaumbele yanayohitaji ufumbuzi wa kisayansi na kiteknolojia.

Dkt. Yonazi amesisitiza kuwa mafanikio ya makubaliano hayo yatapimwa kwa matokeo halisi yatakayochangia kuongeza usalama wa wananchi, kulinda rasilimali za taifa na kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya maafa.

Ushirikiano huo unaendana na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayoweka msisitizo katika matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu kama nguzo kuu ya maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii.

Kwa upande wake Mkuu wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam Prof.Preksedis Marco Ndomba amesema kuwa taasisi imeandika historia kwa kusaini hati ya ushirikiano na Ofisi ya Waziri Mkuu ambapo ameeleza kuwa mchakato huu ulianza muda mrefu na matunda yake yameanza kuonekana jambo ambalo ni mafanikio makubwa.

Read More

DKT. YONAZI AONGOZA KIKAO CHA MAKATIBU MAKUU CHA MAANDALIZI YA AFCON 2027


 Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Dkt.Jim Yonazi ameongoza Kikao cha Makatibu Wakuu cha Maandalizi ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) kwa ajili ya kupitia hatua mbalimbali zilizofikiwa katika maandalizi ya michuano hiyo mikubwa itakayofanyika mwaka 2027 katika nchi za Tanzania, Uganda na Kenya.

Dkt. Yonazi ameongoza kikao hicho leo katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ndogo ya Waziri Mkuu Magogoni jijini Dar es Salaam.

Ametumia nafasi hiyo kuwasihi wajumbe wa kikao hicho kuendelea kufanya maandalizi kwa weledi huku wakishirikisha sekta zote muhimu katika kufanikisha michuano hiyo na kufikia malengo yanayotarajiwa ili kuipa nchi heshima inayostahili.

“Kila sekta iendelee kutekeleza jukumu lake kwa ufanisi ili kuleta matokeo chanya, “ alisema Dkt. Yonazi

Aidha, Dkt. Yonazi amewashukuru wajumbe wote na kusema kuwa Ofisi yake itaendelea kuratibu shughuli hizo kwa ushirikiano wa pamoja.

Read More