Kamati ya Uongozi wa Mradi wa Bwawa la Julius Nyerere (JNHPP), tarehe 26 Februari 2026, imekagua maendeleo ya uzalishaji wa umeme katika mradi huo na kueleza kuridhishwa na usimamizi pamoja na utekelezaji wake, uliokidhi viwango vya ubora vinavyoendana na thamani ya fedha iliyowekezwa na Serikali.
Mwenyekiti
wa Kamati hiyo, ambaye pia ni Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,
Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, amesema kamati imefurahishwa na
namna bwawa hilo linavyochochea ukuaji wa uchumi kwa kuongeza uzalishaji wa
umeme unaosambazwa katika maeneo mbalimbali nchini, hatua inayochangia
kuimarika kwa upatikanaji wa nishati ya umeme.
“Tumeridhishwa
na jinsi mradi huu ulivyosimamiwa na kutekelezwa kwa ufanisi mkubwa.
Ukilinganisha na miradi mingine barani Afrika, mradi huu umejengwa kwa ubora wa
hali ya juu na umeleta unafuu katika huduma ya umeme nchini. Haya ni mafanikio
makubwa kwa Taifa,” alieleza Dkt. Yonazi.
Akizungumza
kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mkurugenzi wa Sera na Mipango,
Bw. Petro Lyatuu, amesema mradi huo umekamilika kwa asilimia 100 na
mchango wake tayari umeanza kuonekana.
Amefafanua
kuwa mwaka 2021, gridi ya taifa ilikuwa na jumla ya megawati 1,600, lakini kwa
sasa uwezo wa uzalishaji umefikia zaidi ya megawati 4,000, zaidi ya mara mbili
ya kiwango cha awali.
“Kwa
sasa bwawa linazalisha umeme na tija yake imeonekana wazi. Kuongezeka kwa
uzalishaji kumeimarisha gridi ya taifa na tunaendelea kuongeza nguvu katika
sekta ya nishati kwa ajili ya maendeleo ya nchi na ustawi wa wananchi,”
alisisitiza Bw. Lyatuu.
Aidha
kwa hatua nyingine Kamati hiyo ilitembelea kituo cha kupokea na kupoza umeme
cha Chalinze, kinachopokea umeme kutoka Bwawa la Julius Nyerere na kusambaza
katika maeneo mbalimbali ya nchi.
Akizungumza
kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Naibu
Mkurugenzi Mtendaji Uzalishaji, Mhandisi Antony Mbushi, amesema kituo hicho
kimekamilika na tayari kinafanya kazi.
Ameongeza
kuwa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme kutoka Chalinze hadi Dodoma umefikia
asilimia 71.58, huku mradi wa kusafirisha umeme kutoka Chalinze kupitia
Kinyerezi hadi Mkuranga umefikia asilimia 59.76.




.jpeg)
.jpeg)













.jpg)








.jpeg)



.jpeg)


