Thursday, June 25, 2026

SERIKALI YAZITAKA TAASISI ZOTE KUJIANDAA KUKABILIANA NA ATHARI ZA EL NIÑO


SERIKALI imesema itaendelea kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini ili kupunguza madhara yanayosababishwa na majanga mbalimbali ambayo yamekuwa yakigharimu maisha ya watu, kuharibu mali na kurudisha nyuma maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Kauli hiyo imetolewa hii leo na Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. James Kilabuko, wakati akifunga Jukwaa la Wadau wa Usimamizi wa Maafa lililojadili Rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kuzuia na Kukabiliana na Madhara ya El Niño Jijini Dodoma.

Amesema Tanzania imeendelea kukabiliwa na matukio ya maafa yanayosababisha athari kubwa kwa wananchi na uchumi wa Taifa, hali inayolazimu kuwepo kwa maandalizi madhubuti ya kukabiliana na changamoto hizo kabla hazijatokea.

“Nchi yetu imekuwa ikishuhudia matukio ya majanga ambayo yamekuwa yakisababisha maafa na kuathiri mfumo wa kawaida wa maisha ya jamii. Majanga hayo yamesababisha vifo, ulemavu wa kudumu, upotevu wa mali na uharibifu wa miundombinu,” amesema Dkt. Kilabuko.

Amesema kufuatia taarifa ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ya Aprili 28, 2026 kuhusu uwezekano wa kujitokeza kwa hali ya El Niño, Ofisi ya Waziri Mkuu imeandaa Rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura kwa ajili ya kuzuia na kukabiliana na madhara yanayoweza kutokea kuanzia Agosti 2026 hadi Juni 2027.

Kwa mujibu wa Dkt. Kilabuko, rasimu hiyo imejadiliwa na wadau mbalimbali ili kuiboresha kwa kuzingatia uzoefu uliopatikana wakati wa matukio ya El Niño yaliyowahi kutokea nchini, hususan ya mwaka 2023/2024.

Amesema ushirikishwaji wa wadau ni hatua muhimu itakayoiwezesha Serikali kuwa na mpango shirikishi na unaotekelezeka katika kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali endapo maafa yatatokea.

“Ni vema kushiriki kikamilifu na kutoa maoni yetu huku tukijielekeza kwenye athari tarajiwa na hatua za kuchukua ili kuwa na mpango thabiti utakaoiwezesha Serikali na wadau kuchukua hatua stahiki za kuzuia au kupunguza madhara,” amesema.

  

Read More

Wednesday, June 24, 2026

SERIKALI YAJIPANGA KUKABILIANA NA ATHARI ZA EL NIÑO

SERIKALI imesema imejipanga kikamilifu kukabiliana na madhara yanayoweza kusababishwa na hali ya El Niño kufuatia tahadhari iliyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA).

Akizungumza hii leo wakati wa ufunguzi wa kikao cha wadau wa usimamizi wa maafa, Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Operesheni na Uratibu kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Kanali Selestine Masalamado, amesema kuwa tayari Serikali imeandaa Rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura ili kuimarisha maandalizi na hatua za kukabiliana na hali hiyo.

Amesema mpango huo unalenga kuhakikisha kunakuwa na uratibu madhubuti, utekelezaji wa hatua za mapema pamoja na kupunguza athari zinazoweza kujitokeza kwa wananchi, mali zao na miundombinu.

“Kikao hiki kinatoa fursa kwa wizara, taasisi, mikoa na wadau wengine kupitia rasimu hii kwa kina na kutoa maoni yatakayosaidia kupatikana kwa mpango shirikishi na unaotekelezeka,” amesema Kanali Masalamado

Ameongeza kuwa Serikali inathamini mchango wa wadau wote katika kuboresha mpango huo ili uwe mwongozo thabiti wa kuzuia, kujiandaa na kukabiliana na madhara ya El Niño.

Aidha, amewataka washiriki kushiriki kikamilifu katika majadiliano na kutoa mapendekezo yenye kujenga yatakayosaidia kulinda maisha ya wananchi na kuhakikisha huduma muhimu zinaendelea kutolewa hata wakati wa majanga.

Katika hatua za maandalizi, amesisitiza umuhimu wa kutoa elimu kwa umma kuhusu tahadhari za kuchukua, ikiwemo kuhama katika maeneo hatarishi na kuendelea na shughuli za kiuchumi katika maeneo salama.

Read More

Sunday, June 21, 2026

RAIS WA NAMIBIA ATEMBELEA KIWANJA CHA UBALOZI WA NAMIBIA MJI WA SERIKALI MTUMBA

 

Rais wa Jamhuri ya Namibia,  Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah leo, ametembelea kiwanja cha Ubalozi wa Namibia kilichopo katika Mji wa Serikali Mtumba, Jijini Dodoma.

Akiwasili katika Mji huo, Mhe. Rais Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah alipokelewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi.

Wakati wa ziara hiyo Katika Mji wa Serikali, Rais Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah alipata maelezo kuhusu mpango kabambe wa Mji wa Serikali pamoja na historia fupi ya maendeleo ya mji huo, ambayo yalitolewa na viongozi na wataalamu wanaosimamia utekelezaji wa mradi huo.

Katika kuendeleza ushirikiano na kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Namibia, Rais Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah amepanda mti katika kiwanja cha Ubalozi wa Namibia na kuupa jina la "UMOJA TREE", ikiwa ni ishara ya urafiki, mshikamano na ushirikiano endelevu kati ya mataifa hayo mawili.

Read More

Friday, June 19, 2026

WAKANDARASI WATAKIWA KUKAMILISHA MIRADI KWA WAKATI KATIKA MJI WA SERIKALI, MTUMBA



Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Prof. Palamagamba Kabudi, amesema Serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kuwekeza katika maendeleo ya Mji wa Serikali, Mtumba, ili kuimarisha utoaji wa huduma za Serikali na kuongeza ufanisi wa utendaji wa taasisi za umma. Amesisitiza kuwa utekelezaji wa azma hiyo unategemea pia wakandarasi kukamilisha miradi wanayopewa kwa wakati na kwa kuzingatia viwango vya ubora vinavyotakiwa.

Prof. Kabudi amesema hayo  alipokagua maendeleo ya ujenzi wa Mji wa Serikali, Mtumba, jijini Dodoma. Alieleza kuridhishwa na hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa miradi mbalimbali pamoja na uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali katika ujenzi wa majengo ya Wizara, taasisi na miundombinu muhimu.

Amesema uwekezaji mkubwa uliofanyika jijini Dodoma, hususan katika Mji wa Serikali, unaakisi dhamira ya Serikali ya kuimarisha makao makuu ya nchi kwa viwango vya kimataifa. Kutokana na mafanikio hayo, Prof. Kabudi amesema kuna kila sababu ya kumpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maono yake na uamuzi wa kuendelea kuwekeza katika maendeleo ya Mji wa Serikali.

Katika ziara hiyo, Waziri Kabudi alikagua maendeleo ya ujenzi wa jengo la Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), ambapo aliwataka wakandarasi wa Suma JKT kwa kushirikiana na vikosi vyote vya ujenzi kuongeza kasi, ubora na ufanisi ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati uliopangwa.

Aidha, alikagua mradi wa majisafi na mfumo wa ukusanyaji na uondoshaji wa majitaka katika Mji wa Serikali unaotekelezwa na Kampuni ya China Harbour Engineering Company Limited (CHEC) chini ya usimamizi wa NORPLAN. Akiwa katika eneo la mradi, alimtaka mkandarasi kuzingatia viwango vya ubora na kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati ili kuwezesha majengo ya Serikali kutoa huduma kwa ufanisi.

Katika hatua nyingine, Prof. Kabudi, akiwa ameambatana na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT), Emmanuel Tutuba, pamoja na wajumbe wa Bodi ya Benki hiyo, walikagua kiwanja cha Benki Kuu ya Tanzania kilichopo katika Mji wa Serikali. Ziara hiyo ilikuwa sehemu ya maandalizi ya utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa Ofisi za Benki Kuu katika eneo hilo.

Ziara ya Prof. Kabudi ni sehemu ya utaratibu wa Serikali, chini ya uratibu wa Ofisi ya Waziri Mkuu,  kufuatilia utekelezaji wa miradi ya kimkakati ili kuhakikisha inakamilika kwa wakati, kwa ubora unaokusudiwa na kuendelea kuboresha mazingira ya utoaji wa huduma kwa wananchi.



 


Read More

WITO WATOLEWA WANANCHI KUTEMBELEA BANDA LA OWM MAONESHO YA WIKI YA UTUMISHI


Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu kupitia Wakala wa Serikali wa Uchapaji Tanzania inawaalika wananchi kutembelea Banda la Ofisi hiyo kwenye Maonesho ya Wiki ya Utumishi ili kupata elimu kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa ikiwemo uchapishaji wa  Sheria, Kanuni, Katiba ya Tanzania, machapisho mbalimbali ya vitambulisho vitambulisho, vyeti na nyaraka zote za kiserikali.

Wito huo umetolewa leo katika viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma na Afisa Biashara Bi. Witness  Njunde kutoka Wakala wa Serikali wa Uchapaji Tanzania wakati akizungumzia kuhusu huduma zinazotolewa na Wakala huyo wa Serikali.

Bi. Njunde amesema “Moja ya kazi tunazofanya ni kuchapisha  gazeti la Serikali, Gazeti hili la Serikali limebeba maudhui ambayo ni ya kiserikali na kibinafsi. Katika maudhui ya kibinafsi huwa linatangaza mabadiliko ya majina, mirathi, kupotea kwa leseni za makazi, kufungwa kwa makampuni hali kadhalika pindi mtu anapopotelewa na vyeti vyake vya shule, passport, leseni zote hizo tunatangaza katika gazeti la serikali”.

Aidha, ameongeza kuwa, Gazeti hilo la Serikali huwa linatangazwa mara moja kwa wiki kila ijumaa  na nakala laini ya gazeti hilo huwekwa katika tovuti ya Ofisi ya Waziri Mkuu au Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora.

Read More

Thursday, June 18, 2026

OWM YATHIBITISHA NYENZO MUHIMU ZA KUIMARISHA USIMAMIZI WA MAAFA NCHINI

 

SERIKALI imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini ili kuongeza uwezo wa kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali baada ya maafa, kufuatia kuongezeka kwa matukio yanayochochewa na mabadiliko ya tabianchi pamoja na vihatarishi vingine vya asili na kijamii.

Hayo yameelezwa  jijini Dodoma na Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, wakati akifungua Kikao cha Jukwaa la Taifa la Wadau wa Usimamizi wa Maafa kilicholenga kupitia na kuthibitisha Mwongozo wa Urejeshaji Hali Baada ya Maafa, Mwongozo wa Uendeshaji na Uratibu wa Uhawilishaji Fedha kwa Walioathirika wa Maafa, pamoja na Mfumo wa Usimamizi wa Taarifa za Maafa (DMIS).

Brigedia Jenerali Ndagala amesema kuwa katika miaka ya hivi karibuni Tanzania imekumbwa na matukio mbalimbali ya maafa yakiwemo mafuriko, ukame, maporomoko ya ardhi, upepo mkali, magonjwa ya mlipuko na ajali mbalimbali, hali ambayo imeathiri maisha ya wananchi, miundombinu, mazingira na shughuli za kiuchumi.

“Kwa kuzingatia hali hiyo, Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu imeendelea kuimarisha sera, mifumo, mikakati, mipango na nyenzo mbalimbali za usimamizi wa maafa ili kuhakikisha hatua zote za kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali baada ya maafa zinafanyika kwa ufanisi na kwa kuzingatia matakwa ya Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 6 ya Mwaka 2022,” amesema.

Amesema kikao hicho ni hatua muhimu katika kuimarisha uratibu wa kitaifa wa usimamizi wa maafa kwa kuwa kinahusisha uthibitishaji wa nyenzo tatu muhimu zitakazochangia uwazi, uwajibikaji na ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi wakati wa maafa na baada ya maafa.

Kwa mujibu wa Brigedia Jenerali Ndagala, Mwongozo wa Urejeshaji Hali Baada ya Maafa utaweka mfumo wa pamoja wa kitaifa wa kupanga na kuratibu shughuli za urejeshaji baada ya maafa, huku Mwongozo wa Uhawilishaji Fedha kwa Walioathirika wa Maafa ukiboresha utaratibu wa utoaji wa misaada ya fedha kwa waathirika. Aidha, Mfumo wa Usimamizi wa Taarifa za Maafa (DMIS) utaimarisha ukusanyaji, uchambuzi, uhifadhi na matumizi ya taarifa za maafa kwa ajili ya kufanya maamuzi sahihi na kwa wakati.

“Nyenzo hizi zina mchango mkubwa katika utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 6 ya Mwaka 2022 kwa kuimarisha usimamizi wa taarifa, uratibu wa wadau, utoaji wa misaada na shughuli za urejeshaji hali baada ya maafa. Vilevile, zinachangia utekelezaji wa Mfumo wa Sendai wa Kupunguza Hatari za Maafa kwa kuimarisha uelewa wa hatari za maafa, usimamizi wa vihatarishi, uwekezaji katika ustahimilivu na kuimarisha hatua za kujiandaa na kujenga upya kwa ubora zaidi baada ya maafa,” amesisitiza.

Ameeleza kuwa mafanikio yanayoendelea kupatikana katika sekta ya usimamizi wa maafa nchini yanatokana na ushirikiano madhubuti kati ya Serikali na wadau wa maendeleo, mashirika ya Umoja wa Mataifa, sekta binafsi na asasi za kiraia.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF), Bi. Judith Bihondwa, amesema shirika hilo litaendelea kushirikiana na Serikali katika kuimarisha uwezo wa jamii kukabiliana na maafa pamoja na kujenga ustahimilivu dhidi ya majanga mbalimbali.

Amesema ushirikiano huo utaendelea kulenga kuimarisha mifumo ya maandalizi, mwitikio na urejeshaji hali baada ya maafa kwa kuzingatia makundi yote ya jamii, hususan watoto na watu walio katika mazingira hatarishi.

Kikao hicho kimewakutanisha wadau mbalimbali wa usimamizi wa maafa kutoka taasisi za Serikali, mashirika ya Umoja wa Mataifa, asasi za kiraia na wadau wa maendeleo kwa lengo la kujadili na kuthibitisha nyenzo zitakazochangia kuimarisha usimamizi wa maafa na kuongeza ustahimilivu wa jamii nchini.

 

Read More

Wednesday, June 17, 2026

OWM YASHIRIKI MAONESHO YA WIKI YA UTUMISHI WA UMMA 2026


 Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Stella Mwaiswaga pamoja na Watumishi wengine kutoka Ofisi hiyo wameshiriki ufunguzi wa Maonesho ya Wiki ya Utumishi tarehe 17 Juni, 2026 katika viwanja vya Chinangali Park Jijini Dodoma.

Maonesho ya Wiki ya Utumishi ni moja ya matukio katika kalenda ya Umoja wa Afrika (AU) ambapo nchi wanachama huadhimisha kwa kaulimbiu moja na kufanya maonesho ya kazi mbalimbali kuhusu masuala ya Utumishi wa Umma ambapo hufanyika kila mwaka kuanzia tarehe 16 hadi 23 Juni.

Kwa mwaka huu Maadhimisho hayo yamebeba kaulimbiu isemayo; “Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi wa Huduma Endelevu”.

Sambamba na hilo Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu inashiriki maonesho hayo huku ikitoa elimu mbalimbali kwa umma kuhusiana na shughuli za Wakala Serikali wa uchapishaji Tanzania, elimu kuhusu masuala ya Menejimenti ya Maafa, Watu wenye Ulemavu, Ufuatiliaji na Tathimini pamoja na Masuala ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi.

Read More

Saturday, June 13, 2026

MGONGANO WA MASLAHI WATAJWA KURUDISHA NYUMA MAENDELEO


Mgongano wa maslahi kwa watumishi wa umma umetajwa kuathiri ufanisi kwenye utendaji na majukumu ya Serikali kutokana na matokeo hasi ya vitendo hivyo vinavyopelekea kuchochea mazingira ya rushwa na kujinufaisha binafsi badala ya ofisi na kukwamisha utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

Hayo yameelezwa mapema mwishoni mwa wiki Jijini Arusha na Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Stella Mwaiswaga wakati akifunga mafunzo kwa wajumbe wa Kamati Maalum ya Menejimenti ya ofisi hiyo yaliyolenga kuwajengea uwezo wajumbe hao katika kusimamia masuala ya uadilifu sehemu za kazi .

Aliongezea kuwa ni muhimu kuendelea kuzingatia taratibu, kanuni na sheria za utumishi wa umma ili kuepuka vitendo vinavyoathiri utendaji wa watumishi hasa katika kujali maslahi binafsi yanayochochea kukosekana kwa huduma bora kwa wananchi.

Alisema kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu imeendelea kuwa Ofisi ya mfano katika masuala ya Uratibu wa Shughuli za Serikali hivyo ni wajibu wa kila mtumishi kuendelea kuzingatia masuala ya uadilifu ikiwemo la kujilinda na vitendo vyote vinavyoweza kuharibu taswira ya ofisi hiyo.

Akiwasilisha mada kuhusu masuala ya dhana ya Mgongano wa Maslahi, Katibu Msaidizi Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Kaskazini Bw. Gerald Mwaitebele amesema ni vyema kuzingatia na kuepuka masuala ya mgongano wa maslahi katika maeneo ya kazi kwani yameendelea kuwa chachu ya kuondoa ufanisi na uwazi wa ofisi zetu.

Aliongezea kuwa,kiongozi anayetekeleza majukumu kwa kujali maslahi binafsi humpelekea kutokuwa na maamuzi sahihi na kusababisha kuharibu utendaji wa taasisi na ofisi anayoihudumia hivyo kuondoa uaminifu kwa jamii, hadi ngazi ya Taifa.

"Mgongano wa maslahi hutokea pale ambapo maslahi yako binafsi (kifedha, kijamii au kindugu) yanapokinzana na majukumu yako ya kikazi. Hali hii inapaswa kuepukwa kwani inaharibu uadilifu, inasababisha upendeleo, na inaweza kuondoa uaminifu wa umma au wa taasisi tunazofanyia kazi," alisisitiza Mwaitebele.

Akitoa neno la shukran kwa niaba ya wajumbe wa kamati hiyo, Bi.Ngole Keya, Naibu Katibu wa Mheshimiwa Waziri Mkuu ameshukuru mafunzo hayo yenye lengo la kuwajengea uelewa na kuendelea kuwakumbusha masuala ya msingi katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku.

“Kipekee tunawapongeza watoa mada wametujenga na kutupa maarifa zaidi katika kuendelea kuboresha utendaji wetu ili kuendelea kutoa huduma bora na kuhakikisha tunaendelea vyema na majukumu yetu ikiwemo la kuratibu shughuli za Serikali kwa kuzingatia misingi na kanuni za kiutumishi zinavyoelekeza,” alisema Bi.Ngole.

 

Read More

Friday, June 12, 2026

SERIKALI YASISITIZA UMUHIMU WA UADILIFU KATIKA UTUMISHI WA UMMA


 SERIKALI imeendelea kusisitiza umuhimu wa kuzingatia misingi ya uadilifu katika utumishi wa umma ili kuhakikisha utekelezaji wa majukumu na mipango ya maendeleo unafanyika kwa ufanisi na kwa kuzingatia maadili ya kazi.

Hayo yamesemwa hii leo  na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, wakati akifungua Mafunzo ya Kamati ya Uadilifu yaliyolenga kuwajengea uwezo wajumbe wa Kamati Maalum ya Menejimenti katika kusimamia masuala ya uadilifu katika ofisi hiyo.

“Uadilifu ni nguzo muhimu katika ufanikishaji wa majukumu na utekelezaji wa mipango ya maendeleo katika sehemu za kazi,” amesema Dkt. Yonazi.

Dkt. Yonazi amesema kuwa ni wajibu wa kila mtumishi wa umma kuhakikisha anazingatia maadili ya kazi na kulinda misingi ya uadilifu ili kuimarisha utendaji na kuongeza imani ya wananchi kwa Serikali.

Aidha, Dkt. Yonazi amesema mafunzo hayo yanalenga kuwawezesha wajumbe kusimamia utekelezaji wa Mkakati wa Uadilifu kwa kuhakikisha unaingizwa katika mipango kazi na bajeti za mwaka za taasisi.

Vilevile, amebainisha kuwa Kamati za Uadilifu zina jukumu la kusimamia utekelezaji wa sera dhidi ya rushwa na kuhakikisha watumishi wanazingatia sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma.

“Kuna umuhimu wa kuimarisha uwazi na uwajibikaji pamoja na kuanzisha mifumo madhubuti ya kupokea na kushughulikia malalamiko ya wananchi kwa kuzingatia usiri.

Akiwasilisha mada ya masuala ya Mkakati wa Taifa Dhidi ya Rushwa na Mpango wa Utekelezaji (NACSAP IV) 2023-2030 Mkurugenzi kutoka Ofisi ya Rais Ikulu Bw. Andrew Massawe amesema, ni wajibu wa watumishi kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu na kupinga vitendo vyote vinavyoashiria mazingira ya rushwa ili kuendelea kuhudumia wananchi, na Taifa kwa ujumla katika misingi sahihi ya utumishi wa umma.

“Tufanye kazi kwa uadilifu na kuzingatia masuala ya huduma bora kwa wateja, tusihudumie watu kama favor bali tutoe huduma kwa viwango bora vinavyotakiwa,”alisema Bw. Massawe

 

Read More

Thursday, June 11, 2026

TANZANIA YAELEZA MAFANIKIO YA UJUMUISHWAJI WA WATU WENYE ULEMAVU, YAAHIDI KUIMARISHA UPATIKANAJI WA TEKNOLOJIA SAIDIZI.


Serikali ya Tanzania imeeleza mafanikio makubwa iliyoyapata katika kuimarisha ustawi na ujumuishwaji wa watu wenye ulemavu, huku ikisisitiza umuhimu wa kuongeza upatikanaji wa vifaa na teknolojia saidizi ili kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii na kiuchumi.

 Akihitimisha ushiriki wa Tanzania katika Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19-CRPD) uliofanyika New York, Marekani, Juni 11, 2026, Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, amesema teknolojia na vifaa saidizi vina mchango mkubwa katika kuwawezesha watu wenye ulemavu kuishi kwa kujitegemea na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya jamii.

“Ni muhimu kuendelea kuongeza upatikanaji na matumizi ya vifaa na teknolojia saidizi kwa watu wenye ulemavu ili kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii na kiuchumi kwa usawa pia Serikali inaendelea kutekeleza kwa vitendo dhana ya ujumuishwaji kwa kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata fursa na haki kwa usawa katika sekta mbalimbali za kijamii na kiuchumi,” alisema  Mhe. Mahundi.

 Akizungumza kwa niaba ya Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Naibu Katibu Mkuu, Dkt. James Kilabuko, amesema ushiriki wa Tanzania katika mkutano huo umeiwezesha nchi kujifunza uzoefu na mbinu mbalimbali za kukabiliana na changamoto zinazowakabili watu wenye ulemavu.

“Tanzania imepiga hatua kubwa katika uwezeshaji na ushirikishwaji wa watu wenye ulemavu hivyo Kupitia mkutano huu, tumejifunza mbinu na uzoefu kutoka mataifa mbalimbali ambazo zitatusaidia kuimarisha zaidi juhudi zetu, lakini pia Serikali itaandaa mpango kazi mahususi kwa kushirikiana na wizara, taasisi na wadau mbalimbali ili kuendeleza utekelezaji wa masuala ya watu wenye ulemavu na kushughulikia changamoto zilizobainishwa wakati wa mkutano huu.,” alisema Dkt. Kilabuko.

 Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Grace Maghembe, amesema Tanzania imeendelea kuboresha huduma za afya za msingi kwa watu wenye ulemavu kwa kusogeza huduma karibu na wananchi kuanzia ngazi ya jamii, sambamba na kuboresha miundombinu ya afya na kuwajengea uwezo watumishi wa sekta hiyo katika utoaji wa huduma jumuishi.

Aidha, ameshauri Shirika la Afya Duniani (WHO) kuangalia uwezekano wa kutumia mifumo inayotumika katika upatikanaji wa chanjo na dawa muhimu duniani ili kuboresha upatikanaji wa vifaa saidizi kwa watu wenye ulemavu, hususan katika nchi zinazoendelea.

Mkutano wa COSP19 umezikutanisha nchi wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu kujadili mafanikio, changamoto na mikakati ya kuimarisha haki, ushiriki na ustawi wa watu wenye ulemavu duniani.

 

 

 

 

 

 

Read More

OWM YATOA MAFUNZO KWA VITENDO KWA WANAFUNZI WA SHAHADA YA USIMAMIZI WA HATARI ZA MAAFA KUTOKA UDOM

KATIKA kuendelea kuimarika kwa sekta ya usimamizi wa maafa nchini na kuongezeka kwa hamasa ya kujifunza mifumo ya usimamizi wa maafa, tahadhari ya mapema na uratibu wa dharura, wanafunzi wa Shahada ya Usimamizi wa Hatari za Maafa kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) wamefanya ziara ya mafunzo kupitia Idara ya Usimamizi wa Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu).

Ziara hiyo imefanyika tarehe 10 na 11 Juni, 2026 iliyolenga kuwajengea uelewa kwa vitendo kuhusu mifumo ya usimamizi wa maafa, ufuatiliaji wa vihatarishi mbalimbali, utoaji wa taarifa za tahadhari ya mapema pamoja na uratibu wa operesheni za dharura nchini.

Katika ziara hiyo, wanafunzi walitembelea Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura kilichopo Ngome, Chumba cha Ufuatiliaji wa Mienendo ya Majanga na Tahadhari za Mapema kilichopo Mtumba pamoja na eneo la ujenzi wa Kituo Kikuu cha Taifa cha Usimamizi wa Maafa na Maghala ya Kuhifadhi Vifaa vya Dharura kilichopo Nzughuni, jijini Dodoma.

Akizungumza na wanafunzi hao, Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo Dkt. Jim Yonazi, aliwapongeza kwa uamuzi wao wa kujifunza kwa vitendo kuhusu masuala ya usimamizi wa maafa na kuonesha dhamira ya kuchangia maendeleo ya sekta hiyo nchini.

Dkt. Yonazi aliwahimiza wanafunzi kuendelea kujiongezea maarifa kupitia tafiti, ubunifu na uandishi wa machapisho mbalimbali kuhusu usimamizi wa hatari za maafa ili kuchangia katika kuimarisha uwezo wa Taifa wa kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali baada ya maafa.

Aidha, aliwahakikishia kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za elimu ya juu katika kukuza taaluma ya usimamizi wa maafa na kuahidi kutembelea Chuo Kikuu cha Dodoma siku zijazo kwa ajili ya kutoa mihadhara na kushiriki katika mijadala ya kitaaluma.

“Ziara yenu ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za elimu ya juu na Serikali katika kujenga kizazi cha wataalamu wenye uelewa wa kina kuhusu usimamizi wa hatari za maafa, tahadhari ya mapema na uratibu wa dharura. Aidha, inaonesha mafanikio ya uwekezaji uliofanywa na Serikali katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa, jambo ambalo limeendelea kuvutia wadau mbalimbali, watafiti na wanafunzi kutoka ndani na nje ya nchi kujifunza na kubadilishana uzoefu,”alisema Dkt. Yonazi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Maafa, Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, aliwaeleza wanafunzi hao kuwa wamefanya jambo la msingi kwa kutenga muda wa kujifunza na kushuhudia kwa vitendo namna Serikali inavyotekeleza majukumu yake ya usimamizi wa maafa nchini.

Alisema kuwa mifumo iliyowekwa na Serikali katika ufuatiliaji wa vihatarishi, utoaji wa tahadhari za mapema na uratibu wa operesheni za dharura ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha usalama wa wananchi na mali zao dhidi ya madhara yatokanayo na maafa mbalimbali.

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, Bi. Jane Alfred Kikunya, ambaye aliongoza mafunzo hayo, alisema ameridhishwa na hamasa na ari kubwa iliyooneshwa na wanafunzi katika kujifunza masuala ya usimamizi wa maafa na tahadhari ya mapema.

Bi. Jane alieleza kuwa ujio wa wanafunzi hao unaonesha namna sekta ya usimamizi wa maafa inavyoendelea kupata umuhimu katika jamii na taasisi za elimu ya juu. Aliongeza kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu itaendelea kufungua milango kwa wanafunzi, watafiti na wadau mbalimbali wanaotaka kujifunza kuhusu mifumo ya ufuatiliaji wa majanga, uchambuzi wa vihatarishi, tahadhari za mapema na uratibu wa operesheni za dharura kutembelea ofisi hiyo.

Kwa upande wake, Dkt. Japhet Ringo kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma ambaye aliambatana na wanafunzi hao, aliishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuwapatia wanafunzi fursa ya kujifunza kwa vitendo kuhusu mifumo ya usimamizi wa maafa nchini.

Dkt. Ringo alisema kuwa ziara hiyo imekuwa darasa muhimu lililowawezesha wanafunzi kuunganisha maarifa ya kinadharia wanayojifunza darasani na utekelezaji halisi wa shughuli za usimamizi wa maafa katika ngazi ya Taifa.

Aliongeza kuwa Chuo Kikuu cha Dodoma kitaendelea kushirikiana na Serikali katika kukuza tafiti, ubunifu na maendeleo ya taaluma ya usimamizi wa hatari za maafa ili kusaidia juhudi za Taifa za kujenga ustahimilivu dhidi ya majanga mbalimbali.

 

 

Read More

Wednesday, June 10, 2026

OWM YATOA MAFUNZO KWA VITENDO KWA WANAFUNZI WA SHAHADA YA USIMAMIZI WA HATARI ZA MAAFA KUTOKA UDOM


 KATIKA kuendelea kuimarika kwa sekta ya usimamizi wa maafa nchini na kuongezeka kwa hamasa ya kujifunza mifumo ya usimamizi wa maafa, tahadhari ya mapema na uratibu wa dharura, wanafunzi wa Shahada ya Usimamizi wa Hatari za Maafa kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) wamefanya ziara ya mafunzo kupitia Idara ya Usimamizi wa Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu).

Ziara hiyo imefanyika tarehe 10 na 11 Juni, 2026 iliyolenga kuwajengea uelewa kwa vitendo kuhusu mifumo ya usimamizi wa maafa, ufuatiliaji wa vihatarishi mbalimbali, utoaji wa taarifa za tahadhari ya mapema pamoja na uratibu wa operesheni za dharura nchini.

Katika ziara hiyo, wanafunzi walitembelea Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura kilichopo Ngome, Chumba cha Ufuatiliaji wa Mienendo ya Majanga na Tahadhari za Mapema kilichopo Mtumba pamoja na eneo la ujenzi wa Kituo Kikuu cha Taifa cha Usimamizi wa Maafa na Maghala ya Kuhifadhi Vifaa vya Dharura kilichopo Nzughuni, jijini Dodoma.

Akizungumza na wanafunzi hao, Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo Dkt. Jim Yonazi, aliwapongeza kwa uamuzi wao wa kujifunza kwa vitendo kuhusu masuala ya usimamizi wa maafa na kuonesha dhamira ya kuchangia maendeleo ya sekta hiyo nchini.

Dkt. Yonazi aliwahimiza wanafunzi kuendelea kujiongezea maarifa kupitia tafiti, ubunifu na uandishi wa machapisho mbalimbali kuhusu usimamizi wa hatari za maafa ili kuchangia katika kuimarisha uwezo wa Taifa wa kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali baada ya maafa.

Aidha, aliwahakikishia kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za elimu ya juu katika kukuza taaluma ya usimamizi wa maafa na kuahidi kutembelea Chuo Kikuu cha Dodoma siku zijazo kwa ajili ya kutoa mihadhara na kushiriki katika mijadala ya kitaaluma.

“Ziara yenu ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za elimu ya juu na Serikali katika kujenga kizazi cha wataalamu wenye uelewa wa kina kuhusu usimamizi wa hatari za maafa, tahadhari ya mapema na uratibu wa dharura. Aidha, inaonesha mafanikio ya uwekezaji uliofanywa na Serikali katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa, jambo ambalo limeendelea kuvutia wadau mbalimbali, watafiti na wanafunzi kutoka ndani na nje ya nchi kujifunza na kubadilishana uzoefu,”alisema Dkt. Yonazi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Maafa, Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, aliwaeleza wanafunzi hao kuwa wamefanya jambo la msingi kwa kutenga muda wa kujifunza na kushuhudia kwa vitendo namna Serikali inavyotekeleza majukumu yake ya usimamizi wa maafa nchini.

Alisema kuwa mifumo iliyowekwa na Serikali katika ufuatiliaji wa vihatarishi, utoaji wa tahadhari za mapema na uratibu wa operesheni za dharura ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha usalama wa wananchi na mali zao dhidi ya madhara yatokanayo na maafa mbalimbali.

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, Bi. Jane Alfred Kikunya, ambaye aliongoza mafunzo hayo, alisema ameridhishwa na hamasa na ari kubwa iliyooneshwa na wanafunzi katika kujifunza masuala ya usimamizi wa maafa na tahadhari ya mapema.

Bi. Jane alieleza kuwa ujio wa wanafunzi hao unaonesha namna sekta ya usimamizi wa maafa inavyoendelea kupata umuhimu katika jamii na taasisi za elimu ya juu. Aliongeza kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu itaendelea kufungua milango kwa wanafunzi, watafiti na wadau mbalimbali wanaotaka kujifunza kuhusu mifumo ya ufuatiliaji wa majanga, uchambuzi wa vihatarishi, tahadhari za mapema na uratibu wa operesheni za dharura kutembelea ofisi hiyo.

Kwa upande wake, Dkt. Japhet Ringo kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma ambaye aliambatana na wanafunzi hao, aliishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuwapatia wanafunzi fursa ya kujifunza kwa vitendo kuhusu mifumo ya usimamizi wa maafa nchini.

Dkt. Ringo alisema kuwa ziara hiyo imekuwa darasa muhimu lililowawezesha wanafunzi kuunganisha maarifa ya kinadharia wanayojifunza darasani na utekelezaji halisi wa shughuli za usimamizi wa maafa katika ngazi ya Taifa.

Aliongeza kuwa Chuo Kikuu cha Dodoma kitaendelea kushirikiana na Serikali katika kukuza tafiti, ubunifu na maendeleo ya taaluma ya usimamizi wa hatari za maafa ili kusaidia juhudi za Taifa za kujenga ustahimilivu dhidi ya majanga mbalimbali.

 

 

Read More

TANZANIA YAONGOZA MJADALA WA KIMATAIFA KUHUSU UIMARISHAJI WA HUDUMA NA MSAADA KWA WATU WENYE ULEMAVU


 Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Mhe. Balozi Togolani Mavura, ameongoza mjadala wa ngazi ya juu katika Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19), uliojikita katika mada ndogo ya “Jamii Imara: Kuimarisha Mifumo ya Huduma na Msaada ili Kuhakikisha Uwezeshaji, Uhuru na Kujitegemea kwa Watu Wote Wenye Ulemavu.”

 Akifungua mjadala huo, Mhe. Balozi Togolani  amesema huduma na mifumo ya msaada ni msingi muhimu wa ustawi wa watu binafsi, jamii na uchumi kwa ujumla, huku akisisitiza kuwa utekelezaji wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu umeleta mafanikio makubwa duniani katika kipindi cha miaka 20 tangu kupitishwa kwake.

 "licha ya hatua zilizofikiwa, bado watu wengi wenye ulemavu wanakabiliwa na changamoto za kupata huduma na msaada unaokidhi mahitaji yao, hali iliyodhihirika zaidi wakati wa janga la UVIKO-19 ambapo mifumo mingi ya huduma ilionekana kutokuwa imara na jumuishi vya kutosha hivyo ni muhimu  kuimarisha huduma za usaidizi binafsi, huduma za urekebishaji na uendelezaji uwezo, vifaa saidizi, mifumo ya hifadhi ya jamii pamoja na huduma za kijamii zinazotolewa katika ngazi ya jamii katika kuwawezesha watu wenye ulemavu kufanya maamuzi yao wenyewe, kuishi kwa kujitegemea na kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii, kiuchumi na kisiasa."Alisema Mhe. Balozi Togolani.

 Aidha, amesema kuwa uwekezaji katika mifumo ya huduma na msaada si suala la maendeleo pekee bali ni wajibu wa kuheshimu haki za binadamu, huku akizitaka serikali, mashirika ya maendeleo, asasi za kiraia, mashirika ya watu wenye ulemavu na wadau wengine kushirikiana kwa karibu ili kuziba mapengo yaliyopo na kuharakisha utekelezaji wa sera na programu zinazolenga kujenga jamii jumuishi na himilivu.

 Kwa upande wake Afisa  Sheria kutoka kitengo cha  Watu Wenye Ulemavu,Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Bw. Jacob C. Mwinula, akiwasilisha uzoefu wa Tanzania katika kuimarisha mifumo ya huduma na msaada kwa watu wenye ulemavu wakati wa mjadala (Roundtable Discussion) ameeleza hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kuimarisha ujumuishaji, kujitegemea na ushiriki wa watu wenye ulemavu kupitia sera, sheria, mifumo ya hifadhi ya jamii, huduma za afya, elimu jumuishi na uwezeshaji wa kiuchumi.

 


Read More