Tuesday, July 2, 2024

UJENZI WA NYUMBA ZA WANANCHI WALIOKUMBWA NA MAFURIKO HANANG WAFIKA HATUA NZURI


 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama amewapongeza SUMA JKT kwa hatua nzuri waliyofikia katika Ujenzi wa Nyumba za Makazi kwa wananchi waliokumbwa na Mafuriko ya Mawe na Matope mwezi Disemba Mwaka Jana.

Waziri ametoa Kauli hiyo wakati alipotembelea na kujionea maendeleo ya Ujenzi wa nyumba hizo   zinazojengwa katika eneo la Waret, katika Kijijiji cha Gidagamowd kata ya Mogitu wilaya ya Hanang’.

Ujenzi wa nyumba hizi ni kielelezo cha dhamira ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya uzalendo kwa Taifa lake, utu na mapenzi kwa wananchi katika kuwatumikia.

“Nimefurahi mmerithisha ujuzi wa ujenzi kwa sababu nyumba hizi zimejengwa kwa ubora wa hali ya juu na kuzingatia kanuni za kiuhandisi wakati wa ujenzi,” alisema Waziri Mhagama.

Aidha ameelekeza kwa uongozi wa Mkoa wa Manyara kuhakikisha miundo mbinu ya Elimu, Soko na Afya inakamilika kwa muda unaotakiwa kama ilivyofanywa katika urejeshaji wa hali kwa kuhakikisha huduma za maji, nishati ya umeme inapatikana sambamba na ufunguaji wa barabara.

Waziri Mhagama amesema, “Makazi yanapendeza na baada ya muda Mji huu utakuwa Mkubwa sana na utakuwa Mji wa kihistoria ni vyema tukaendelea kutuna mazingira ili kuepukana na mabadiliko ya tabia nchi.”

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Hanang’ Mhe. Halimish Issa Hazali amesema Waziri Mhagama ametembelea Nyumba za SUMA JKT nyumba 73 na 1 UWT na ameridhishwa na maendeleo ya ujenzi na pia ametembelea na kujionea maendeleo ya ujenzi wa nyumba 35 zinazosimamiwa shirika la Msalaba Mwekundu.

Nimshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo ameifanya na anaendelea kuifanya kwa wananchi wa Hanang.

Awali Kaimu Kamanda wa Ujenzi wa Nyumba Luteni Kanali Ashiraf Hassan amesema wamefarijika kwa ziara ya Waziri Mhagama na wamejipanga kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati na ubora unaotakiwa.

“Hatuwezi kumuangusha Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan katika adhima yake ya kuhakikisha anawapatia wananchi wa Hanang waliokumbwa na Mafuriko ya Matope na Mawe nyumba bora,” alisema Kaimu Kamanda wa Ujenzi Luteni kanali Hassan.

Read More

Saturday, June 29, 2024

SERIKALI KUENDELEA KUWEKA MKAZO WA KUONDOA VIJANA KWENYE URAIBU WA DAWA ZA KULEVYA

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama amesema Serikali inaendelea kuweka nguvu katika kuondoa vijana kwenye uraibu wa dawa za kulevya kwa kuhakikisha inawapa tiba vijana hao ili warudi katika hali zao za kawaida.

Kauli hiyo ameitoa wakati alipotembelea Mabanda ya Taasisi mbalimbali kuelekea Maadhimisho ya Kitaifa ya Siku ya Kupiga Vita Dawa za Kulevya Dunia 2024 zinazofanyika Jijini Mwanza katika Uwanja wa Nyamagana.

"Tumeshuhudia vijana wengi waliotoka kwenye uraibu wa dawa za kulevya wamerudi kuwa rai wazuri wanajishughulisha na shughuli za uzalishaji mali na wameamua kujitokea kuokoa vijana wenzao," alisema Waziri Mhagama

Waziri Mhagama alifafanua kwamba, serikali imeshajenga kituo Jijini Dodoma cha urekebishaji ambacho kitakuwa kinatoa tiba ya kutoa vijana kwenye uraibu wa dawa za kulevya na kufundisha mafunzo ya ujuzi.

Aidha Serikali inaendelea kutekeleza kwa nguvu kubwa kwenye matamko ya kisera ili kuweza kuhakikisha inaokoa vijana kwenye matumizi ya dawa za kulevya.

"pia tunaamini Serikali kwa kushirikiana na wadau wengine tukifanya kwa pamoja tunaweza kupata mafanikio makubwa sana," alisema

Waziri Mhagama alisema  tafiti zilizofanyika mtumiaji akitumia dawa za kulevya anatumia masaa sita kwa kilevi ambacho kinamsababishia kulala na kutojitambua masaa sita, jambo ambalo linamnyima uwezo wa kufanya kazi, anapopata fahamu anakuwa dhaifu na hawezi ufanya kazi yoyote na anapokosa fedha ya kununua madawa inamsababisha kuingia kwenye matendo ya jinai.

Awali katika zoezi hilo Waziri Mhagama aliambatana na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Ummy Nderiananga pamoja na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi.

 

 


Read More

Sunday, June 9, 2024

WAZIRI MHAGAMA AIPONGEZA SUKOS KOVA FOUNDATION KWA KUANDAA MAFUNZO YA UOKOAJI


 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama amepongeza taasisi ya Sukos Kova Foundation na taasisi ya Peaceland Foundation kwa pamoja kwa kushirikiana taasisi za uokoaji Serikalini kwa kuandaa mafunzo maalumu ya uokoaji kwenye maji.

Ametoa pongezi hizo wakati wa hafla ya kufungua mafunzo hayo yaliyohusisha vikosi vya Jeshi la Polisi Wanamaji, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji pamoja na vikundi mbalimbali vya uokoaji katika ngazi ya jamii iliyofanyika Sawasawa Bay Mikocheni, Dar es salaam.

Amesema boti iliyokabidhiwa Ofisi ya Waziri Mkuu itaenda kwenye maziwa mito na maeneo mbalimbali ili ikakutane na taasisi za uokoaji na vikundi vya jamii ambavyo vitakuwa tayari kwa mafunzo.

Waziri Mhagama amesema, “maamuzi hayo ni ya kizalendo na tutaendelea kuheshimu uwepo wa taasisi hizo binafsi, ikiwa ni pamoja na utaratibu ambao zitakuwa zimejiwekea katika kuleta tija kubwa kwa taifa na ustawi wa Watanzania.”

Aliongezea kuwa matumizi ya uokoaji yanaenda sambamba na matumizi ya vifaa hivyo na kutoa wito juu ya utoaji wa elimu kuhusu matumizi sahihi ya vifaa, kwa wakati sahihi na mahali sahihi pale ambapo vitahitajika ili viweze kukabiliana na maafa pindi yanapotokea.

"Boti iliyokabidhiwa ni boti ya kisasa na kwa sababu mambo ya uokoaji ni mambo mtambuka yataenda sambamba na uzuiaji wa uhalifu, na inaweza kutumika pia kuzuia uhalifu kwenye maeneo ya maji katika Taifa letu.”alisema Mhe. Mhagama

Ofisi ya Waziri Mkuu itaendelea kushirikiana na taasisi nyingine za kiraia ili kuweza kufika maeneo mbalimbali yenye uhitaji wa kupata mafunzo ya uokoaji.

Aidha alitoa rai kwa taasisi za uokoaji na vikundi vya uokoaji kuhakikisha wanatunza vifaa vilivyotolewa ili viweze kudumu kwa muda mrefu huku vikiendelea kutoa msaada wa uokoaji .

Watakaopokea mafunzo watumie vizuri maarifa hayo ili waweze kufunza wengine na kusaidia kundi kubwa  kunufaika na mafunzo hayo ambayo yatatolewa kwa muda wa wiki mbili, alisistiza

Waziri amesema, “ni vyema taasisi za uokoaji na vikundi vya uokoaji vikatumia elimu itakayotolewa kwa uzalendo mkubwa pindi tutakapokutana na majanga ya maafa.”

Waziri Mhagama alizikumbusha taasisi Sukos Kova Foundation kuendelea kufungua milango ili taasisi nyingine ambazo zinapenda kufanya ushirikiano na taasisi hiyo kwenye masuala ya uokoaji wawe tayari kushirikiana.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa wa Dar es Salaam Dkt, Koba Nguvila amesema Mkoa wa Dar es salaam unaguswa kwenye habari ya uokoaji na mafaa kwa sababu Mkoa huo unapata mafuriko na madhila ya kuchafuka kwa bahari.

Amesema kuwa hili ni jambo la faraja kwa taifa, pindi inapotokea jamii imezungukwa na maji unatumia vifaa vya kisasa vya uokoaji hivyo kusaidia kuimarisha usalama  wa kuokoa watu.

Naye Kamishna Mstaafu Suleiman Kova, amesema ya Sukos Kova Foundation kwa kushirikiana taasisi ya Peaceland Foundation wametoa boti Moja ili liweze kuogeza nguvu katika miundombinu iliyopo kazini.

"Tumeona tumpatie Jaketi la Uokoaji (Life JacketRais) Dkt. Samia Suluhu Hassani kwa sababu amekuwa mstari wa mbele kutoa maelekezo makubwa wakati Maafa yanapotokea," alisema

Awali Mkuu wa Wajumbe kutoka Peaceland Foundation Bi. Jing Ping, amesema nchi ya China na Tanzania wamekuwa na ushirikiano na mshikamano wa karibu kwa zaidi ya miongo sita sasa.

"Nchi zetu zimekuwa zikisaidiana katika mambo mbalimbali na tukio la leo ni moja ya ushahidi wa ushirikiano wetu, na katika hili taasisi yangu kwa kushirikiana na Sukos Kova Foundation zimejikita katika kuimarisha juhudi za kukabiliana maafa kwa kutoa vifaa mbalimbali vya kusaidia uokoaji.

Read More

Monday, June 3, 2024

“MFUMO WA UFUATILIAJI NA TATHMINI KUBADILI DHANA YA UTENDAJI SERIKALINI” WAZIRI MHAGAMA

 


Taasisi za Umma zimetakiwa kufanya tathmini za awali ya hali ya utekelezaji wa mfumo wa Ufuatiliaji na Tathmini katika taasisi zao na kuwasilisha katika Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu kabla ya tarehe 15 Julai, 2024.

Maagizo hayo yametolewa Jijini Dodoma na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama wakati wa hafla ya Uzinduzi wa nyaraka za msingi za Ufuatiliaji na Tathmini nchini na utiaji sahihi mikataba ya makubaliano katika kuimarisha shughuli za Ufuatiliaji na Tathmini nchini.

Waziri Mhagama amesema kuzinduliwa kwa mwongozo huo utasaidia kuongeza ufanisi katika Ufuatiliaji wa Tathmini na kuhimiza matumizi ya matokeo ya tathmini hizo katika kufanya maamuzi na kuboresha utekelezaji na  utendaji katika ngazi zote.

“Katika kutekeleza mwongozo huu, ninaelekeza Taasisi za Umma kuandaa taarifa ya utekelezaji wa Tathmini zote zilizofanyika kwa mwaka wa fedha 2023/24 na zinazotarajiwa kufanyika kwa mwaka wa fedha 2024/25 ili Ofisi yangu iweze kuandaa Mpango wa Tathmini wa mwaka 2024/25 na kufuatilia utekelezaji wake," amesema Mhe. Mhagama

Aidha katika kutekeleza mwongozo huo Mhagama ameelekeza yafuatayo:-Kufanya Tathmini ya Awali ya hali ya utekelezaji wa Mfumo wa Ufuatiliaji na Tathmini katika Taasisi zao (M&E Readiness Assement), Kuandaa Mwongozo wa Matumizi (Operational Manual) ambao unaeleza utekelezaji wa Ufuatiliaji na Tathmini wa kila siku katika taasisi zao. Mwongozo huo uoneshe namna ambavyo vitengo, idara au sehemu za U&T zitakavyofanya kazi kwa kuzingatia Mwongozo huu.

Maelekezo mengine ni pamoja na Kuandaa Mpango wa Ufuatiliaji (Monitoring Plan) kwa kuonesha maeneo na kazi zote zitakazofuatiliwa kila siku kulingana na Mpango Kazi wa Taasisi (Action Plan) na mipango ya utekelezaji wa afua mbalimbali, Kuandaa Mpango wa Tathmini (Evaluation Plan) kwa kuonesha tathmini za afua za maendeleo zitakazofanyika katika kipindi husika.

Sambamaba na hayo ameelekeza Kuandaliwa kwa moduli za utendaji zinazojumuisha viashiria muhimu vya kupima utendaji wa Taasisi,Kuteua wataalamu (U&T Champions) kutoka Idara na Vitengo vyote vya taasisi husika. Wataalamu hao watashirikiana na Idara/Kitengo cha U&T katika utekelezaji wa Mwongozo huu.

 Pia amewasisitiza  Makatibu Wakuu, Watendaji Wakuu, Makatibu Tawala wa Mikoa na Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa na Wakurugenzi wa Vitengo vya U$T katika Taasisi zote za Umma kuendelea kuimarisha Vitengo vya Ufuatiliaji na Tathmini vilivyoanzishwa kwa kutengewa bajeti ya kutosha kutekeleza shughuli zake na kuwajengea uwezo wa kitaalamu watumishi waliopo katika vitengo hivyo na kuhakikisha taasisi za umma zinafanya tathmini za mara kwa mara za utekelezaji wa Sera, Mipango, Miradi na Programu mbalimbali za Serikali na kuwasilisha taarifa hizo Ofisi ya Waziri Mkuu.

 Awali akitoa neno la utangulizi Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi amefafanua miongozo  iliyozinduliwa kuwa ni Jumuishi wa Ufuatiliaji na Tathmini unalenga kuziongoza taasisi za umma kuhusu namna ya kutekeleza majukumu ya Ufuatiliaji na Tathmini. Mwongozo huu umeainisha hatua za kufuata katika ufuatiliaji, ufanyaji wa Tathmini, maandalizi ya viashiria na kupima utendaji wa shughuli za Serikali.

Pia umezinduliwa Mwongozo wa Tathmini ya utayari wa Taasisi za Umma katika kutekeleza shughuli za Ufuatiliaji na Tathmini umelenga kutathmini uwezo, udhaifu, fursa na changamoto zinazokabili taasisi za umma katika kutekeleza shughuli za ufuatiliaji na tathmini na hivyo kutoa mapendekezo ya namna ya kuboresha.

Aidha Mwongozo mwingine ni Mwongozo Kitaifa wa Tathmini (National Evaluation Guideline) unalenga kutoa namna bora ya kuratibu na kusimamia tathmini nchini. Kimsingi mwongozo huu unalenga kuhakikisha mipango ya tathmini inafuatwa, matokeo ya tathmini yanatumika na utamadumi wa kufanya tathmini unajengwa.

Dkt.Yonazi amesema utekelezaji wa miongozo hiyo kwa kiasi kikubwa unategemea uwepo wa Mfumo Jumuishi wa Kielektroniki wa Ufuatiliaji na Tathmini (Government wide integrated M&E System)

“Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Mamlaka ya Serikali Mtandao, ipo katika mchakato wa maandalizi ya Mfumo huo.  Kukamilika kwa mfumo huo kutasaidia katika ukusanyaji, uchakataji na utoaji wa taarifa za Ufuatiliaji na Tathmini kwa wakati (real time data) na pia kuwezesha upimaji utendaji kazi utakaochangia katika utoaji wa huduma bora kwa wananchi,” alieleza Dkt. Yonazi.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Profesa Elisante Ole Gabriel ameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa uzinduzi huo huku akieleza kuwa hatua hii ni jambo zuri na kukumbusha kuwapa nafasi wataalamu wa masuala ya ufuatiliaji na tathmnini ili kuyafikia matarajio ya Tanzania ya sasa na ya baadae.

Naye Bw. Kadari Singo Mkuu wa Taasisi ya Uongozi amesema upo umuhimu wa kuendelea kusimamia vitengo vya Ufuatiliaji na Tathmini katika Wizara na Taasisi zetu ili kusaidia kuleta matokeo yanayokusudiwa na kuongeza ufanisi katika kutekeleza majukumu ya kila siku.

“Ni vyema kukawa na desturi ya kufanya tathmini kuanzia mtu mmoja mmoja, nafasi ya familia, jamii na katika maeneo yetu ya kazi hii iwe ni sehemu ya maisha ya kila mmoja na kusadia kujua wapi unaenda sawa na wapi urekebishe na kuepuka kuenenda bila malengo,” alieleza Bw. Singo

Aliongezea kuwa, ili kuendelea kuwa na matokeo katika utendaji kazi wa kila siku, jamii haina budi kubadili mtazamo na kuyapa umuhimu mkubwa masuala ya tathmini na ufuatiliaji kama nyenzo ya kujipa nafasi ya kufanya vizuri zaidi kuliko ambapo isingefanyika.

 

Read More

Saturday, June 1, 2024

“MAENDELEO YA SAYANSI NA TEKHNOLOJIA YAENDELEE KUTULETEA MABADILIKO CHANYA” WAZIRI MHAGAMA

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama ameomba wanawake kuendelea kuliombea Taifa na kuombea kizazi kilichopo na kizazi kijacho ili kiendelee kuwa na hofu ya Mungu.

 Ametoa kauli hiyo wakati akihutubia Kongamano la Wanawake wa Makanisa ya Kipentekoste Tanzania ambalo limefanyika Sasaba Jijini Dar es salaam likiongozwa na kauli Mbiu, yake inayosema, Mwanamke ni Jeshi kubwa kwa Kanisa na Taifa.

 Ameeleza kwamba mabadiliko ya Sayansi na Tekhnolojia yanapaswa kuendelea kutusaidia kumjua Mungu kwa haraka na hayapaswi kutuingiza kwenye changamoto za kidunia. Licha ya kwamba nchi yetu haiegemei upande wowote katika masuala ya dini (Secular State) lakini sehemu kubwa ya watu wake wanaamini katika Mungu kupitia dini na madhehebu mbalimbali.

 “Tukifanya kazi hii vizuri tutakuwa tumelitendea haki Taifa, na naomba niendelee kutoa wito kwa wakinamama na watoto (CPCT) muendelee kubaki imara kwenye kanisa na Taifa letu,” alihimiza Waziri Mhagama.

Waziri Mhagama amezungumzia pia uchaguzi wa Serikali za Mitaa ambapo ametoa rai kwa wakinamama kuombea uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwaka huu, ili chaguzi hizo zipite salama na tushawishi wanawake wenye uwezo wagombee.

 “Mwanamke akipata nafasi ya kuongoza Kijiji au Mtaa na akiwa ametoka kwenye Jeshi kubwa la kuliombea Taifa atafanya kazi weledi,” alitanabaisha

 Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Makanisa ya Kipentekoste Tanzania (CPCT) Mhashamu Askofu Dkt. Barnabas Mtokambali Amesema umoja huo uliundwa na Hayati Ali Hassani Mwinyi aliyekuwa Raisi wa awamu ya pili ambaye aliridhia kuundwa kwa Umoja wa Baraza hilo mwaka 1993 na Makao yake Makuu yalikuwa Jijini Dar es Salaam.

 “Baraza hili linabaraka zote za madhebu ya kipentekoste na Baraka za Nchi na tumeunda Idara na Mabaraza kwenye ngazi za Mikoa na Wilaya ikiwemo Idara hii ya wanawake ambayo inatimiza maono, na dhima iliyokusudiwa alisema,” Mhashamu Askofu Dkt. Barnabas Mtokambali

Ikumbukwe Baraza la Makanisa ya Kipentekoste Tanzania (CPCT) limetimiza miaka 31 tangu kuundwa kwake, na lina idara 9 ikiwemo Idara ya Wanawake wa Makanisa ya Kipentekoste Tanzania lenye maono ya kuwa na wanawake wa Kipentekoste wanaotembea katika nguvu ya Roho Mtakatifu na kuubadilisha ulimwengu kwa Injili ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo, na hili ni Kongamano la kwanza la Wanawake wa CPCT Taifa kufanyika.

Read More

Saturday, May 25, 2024

KAMPUNI YA SANKU, YAPONGEZWA KWA KUJIKITA KATIKA URUTUBISHAJI WA VYAKULA NCHINI



Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama amesema mahitaji ya virutubishi vya chakula ni ajenda kubwa ambayo itachochea katika kuongeza ajira kwa wakulima wetu na kuwa na uhakika na virutubishi tunavyovitumia hapa nchini.

Waziri amesema hayo alipotemebelea na kukagua kiwanda cha Sanku kilichopo Mwenge Jijini Dar es salaam leo tarehe 25/12/2024 na kujionea maendeleo ya kiwanda hicho cha uchanganyaji wa virutubishi kwenye unga wa mahindi na ngano kwa bei nafuu.

Naomba muendeele kufanya ufutailiaji wa karibu katika kutoa elimu ili kuondoa matatizo mengine ya udumavu, utapiamlo na shida ya kupungukiwa vitamini A kwa wakinamama wajawazito.

“Hii kazi ni kazi yenye manufaa makubwa na itaweza kutusaidia sana kama nchi tuweze kusonga mbele na kusaidia kuitangaza nchi kwa kuwa na kiwanda kikubwa cha kuchanganya virutubishi,” alisema Waziri Mhagama

Kwa upande wake Meneja Muandamizi wa Sanku Bw. Gwao Omari Gwao amesema kampuni yao inasaidia wafanyabishara wadogo na wakati kufanya urutubishaji ambazo zimefunguliwa katika Mikoa 26 Tanzania Bara na katika Halmashauri 142 Tanzania Bara.

 

 

Read More

Friday, May 24, 2024

WADAU WAOMBWA KUSHIRIKIANA NA SERIKALI KUKABILIANA NA UTAPIAMLO


Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi ametoa rai kwa wadau wa sekta binafsi kushirikiana serikali katika kukabiliana na swala la utapiamlo nchini.

 Ametoa kauli hiyo Jijini Dar e Salaam wakati kikao kilichohusisha wadau wa sekta binafsi katika kujadili maandalizi ya Mkutano wa 10 wa lishe unaotarajiwa kufanyika Jijini Mwanza Mwezi Septemba.

 Katika biashara tunahitaji watu ambao wanaoweza kufikiri haraka katika hatua za ukuaji wa kiuchumi, ili fikra hizo ziendelee tunahitaji kujenga Jamii bora.

 “Lazima tuunganishe nguvu tukabiliane na changamoto ya udumavu katika Jamii yetu ili kampuni zetu za ndani ziweze kuendelea katika ushindani na kampuni za nje,” alihimiza

 Aidha sekta binafsi imepata nafasi ya kutambulika na kushikana mkono na serikali ili kuwa na juhudi za pamoja katika kuhakikisha taifa letu linakabiliana na tatizo la lishe nchini kwa uendelevu mkubwa.

 “Tunahitaji kuwa na   taifa lenye watu wenye afya nzuri, siha njema wanaoweza kufikiri, wanaoweza kuweka mikakati na kuongeza ushawishi wa kibiashara nje ya mipaka ya nchi yetu,” alisema.

 Kwa upanda wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania Dkt. Germana Leyna amesema sekta binafsi wanayo nafasi ya kuhamasisha walaji katika kujenga hamasa ya kuleta mabadiliko chanya katika lishe kulingana na bidhaa zinazozalishwa.

 “Tatizo la utapiamlo lisipopatiwa ufumbuzi, linaweza likapunguza nguvu ya ununuaji (Purchasing Power) hata kama bidhaa zitakuwa bora na muhimu,”

Alibainisha.

 Naye Bw. Ally Sechonge kutoka kampuni ya Tanga Freshi amesema kwa mujibu wa takwimu za Bodi ya maziwa ni 4% ya Maziwa yanayotoka kwa Ng'ombe ndio yanayosindikwa na 96% yananywewa bila kusindika.

 “Tatizo kubwa ni kwamba walaji wanakuwa na maamuzi jinsi gani watatumia fedha yao, bila kuzingatia  swala la  utaratibu mzuri wa kula,” alisema.

 Naye Bw. Iddi Mvungi kutoka kutoka kampuni ya Bakhresa ameishukuru serikali kwa kujumuisha sekta binafsi katika mapambano dhidi ya utapiamlo.

 Sisi tunaendelea kuihakikisha serikali kwamba tutakuwa pamoja na Serikali na kwa kuhakikisha maelekezo yote yanayoelekweza, tunayazingatia katika uzalishaji wa bidhaa. 

Read More

Thursday, May 16, 2024

SERIKALI KUENDELEA KUBORESHA HUDUMA ZA TIBA KWA WARAIBU WA DAWA ZA KULEVYA

 


Serikali imesema itaendelea kuboresha huduma za tiba kwa waraibu wa dawa za kulevya ili kuhakikisha wanareejea katika hali zao za awali na kushiriki katika shughuli za maendeleo.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama  wakati akizungumza na waandishi kuhusu Taarifa  ya Hali ya Dawa za Kulevya nchini kwa mwaka 2023 katika Ukumbi wa Habari Bungeni Jijini Dodoma iliyoelezea mafanikio yaliyopatikana katika vita dhidi ya dawa hizo.

Mhe. Jenista alisema, mwaka 2023, Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) kwa kushirikiana na vyombo vingine vya dola vilifanikiwa kukamata jumla ya kilogramu 1,965,340.52 za dawa za kulevya aina ya heroin, cocaine, methamphetamine, bangi, mirungi, skanka na dawa tiba zenye asili ya kulevya na kuwakamata watuhumiwa 10,522.

“Takwimu za mwaka 2023 zinaonyesha mafanikio makubwa, kwani kiasi cha dawa za kulevya kilichokamatwa ni kiasi kikubwa kuliko kiasi kilichokamatwa wakati mwingine wowote nchini. Kiasi hiki ni karibu mara tatu ya kile kilichokamatwa kuanzia mwaka 2012 hadi 2022, ikiwa ni ishara ya dhamira ya dhati na utashi wa kisiasa wa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kupambana na janga hili” alisema Mhe. Jenista.

Alieleza kwamba hadi kufikia mwezi Disemba 2023, vituo vya tiba saidizi na unasihi kwa waraibu wa dawa za kulevya (MAT Clinics) vilivyohudumia waraibu 15,912 vilifikia 16, na nyumba za upataji nafuu (Sober Houses) na 56 zilizohudumia waraibu 3,488.

Waziri Jenista aliendelea kubainisha kwamba jumla ya waraibu 903,062 wa dawa za kulevya na vilevi vingine walipata huduma katika hospitali za wilaya, mikoa na rufaa nchini huku akisema Serikali imeanza ujenzi wa kituo cha Taifa cha Utengamao kwa ajili ya kuwahudumia waraibu wa dawa za kulevya waliopata nafuu.

‘Kituo hiki kitajengwa katika eneo la Itega Jijini Dodoma na kitasaidia kuwajengea uwezo waraibu wa dawa za kulevya waliopata nafuu ili waweze kujikimu kimaisha na kuepuka kurejea kwenye matumizi ya dawa za kulevya,”Alieleza.

Vilevile ameeleza kuwa, serikali imeweka jitihada kubwa katika kuzuia matumizi ya dawa za kulevya nchini kwa kuimarisha elimu na mikakati ya kukabiliana na tatizo hili kupitia vyombo vya habari, mitandao ya kijamii, semina, makongamano, mikutano, vilabu vya kupinga rushwa na dawa za kulevya shuleni na vyuoni.

Akibainisha mafanikio yaliyopatikana Waziri Jenista alieleza kwamba, mwaka 2023, Serikali ilianzisha kituo maalumu cha Habari na Mawasiliano (Call Centre) kilichopo katika ofisi za DCEA ambapo wananchi wanaweza kupiga simu namba 119 bila malipo na kutoa taarifa za wahalifu wa dawa za Akikulevya au kupata elimu juu ya madhara ya dawa za kulevya.

Serikali imefungua Ofisi mpya tano za Mamlaka katika ngazi ya kanda ambazo ni nyanda za juu kusini ambayo ofisi zake ziko Mkoa wa Mbeya inahudumia Mikoa ya Mbeya, Songwe, Katavi, Rukwa Njombe na Iringa. Kaskazini ofisi zake ziko Mkoa wa Arusha inahudumia Mikoa ya Arusha, Manyara Kilimanjaro na Tanga,”Alitaja Mhe. Jenista.

Akiendelea kutaja Mikoa hiyo alisema kuwa ni Pwani ambayo inatoa huduma  katika Mkoa wa Mtwara, Lindi, Ruvuma na Morogoro wakati  Kanda ya ziwa ambayo ofisi zake ziko Mkoani Mwanza inahudumia Mikoa ya Mwanza, Kagera, Mara, Geita, Simiyu na Shinyanga, pamoja na Kanda ya kati yenye ofisi Mkoani Dodoma inayohudumia Mikoa ya Dodoma, Kigoma Singida na Tabora. 

Pamoja na mafanikio hayo alifafanua kwamba  bado Serikali imeendelea kuwekeza katika udhibiti  wa dawa za kulevya ambapo mwaka 2023 imenunua boti yenye kasi (Speed Boat) itakayotumika kufanya doria baharini kukabiliana na uingizaji wa dawa za kulevya kama vile heroine na methamphetamine.

Katika hatua nyingine Mhe. Jenista alisema Serikali imetunga Sera ya Taifa ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya ya Mwaka 2024 ili kuhakikisha ushiriki wa wadau wote katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya.

“Sera hii itaimarisha udhibiti wa dawa za kulevya zinazozalishwa nchini kama vile bangi na mirungi. Pia itatoa maelekezo ya kufanya utafiti wa mazao mbadala katika maeneo yanayolima mazao haya ili wananchi wapate kilimo cha mazao halali. Zaidi ya hayo, sera hii inaelekeza kuwajengea uwezo wadau mbalimbali katika udhibiti wa dawa za kulevya ili kuboresha ufanisi wa mapambano haya,” alisisitiza Mhe. Jenista.

Aidha Mhe. Jenista alitoa wito kwa jamii kushiriki kikamilifu katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya na kusisitiza kuwa elimu ya kujiepusha na matumizi ya dawa za kulevya inapaswa kuanzia ngazi ya familia pamoja na  Wazazi na walezi kushiriki katika kwa  kuwajengea misingi bora watoto wao ili wasijiingize kwenye vitendo viovu na makundi hatarishi yanayoweza kuwaingiza kwenye matumizi na biashara ya dawa za kulevya.

 

 

 

 

Read More

Saturday, April 27, 2024

WANANCHI WAPEWA SHIME KUCHANGAMKIA FURSA ZA UWEKEZAJI NCHINI

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama ametoa shime kwa Baraza la Uwekezaji wa Wananchi Kiuchumi kwa kushirikiana na sekta binafsi na wadau mbalimbali kutambua mawanda makubwa ya uwekezaji yaliyo katika nchi yetu.

Kauli hiyo ameitoa wakati akizungumza katika Kongamano la Nne la Kitaifa la Ushiriki wa Watanzania katika Miradi ya kimkakati na uwekezaji lilofanyika katika ukumbi wa Benki kuu ya Tanzania (BOT) Jijini Dar es salaam.

Waziri Mhagama amesema kuwa sekta binafsi na wadau mbalimbali waendelee kutoa mapendekezo kwenye fursa mbalimbali zinazojitokeza za kiuchumi ili kuwezesha utekelezaji wa miradi ya kiuchumi kufikia malengo yaliyopo.

Ameongeza kusema wananchi wa Tanzania wako tayari, wakiongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwa ameonesha kwa vitendo kwamba yuko tayari hivyo ni vyema kumuunga mkono kwa kufanya kazi ili kujenga uchumi wa Taifa.

Aidha jukwaa hilo litasaidia kujenga uelewa wa pamoja juu ya mafanikio yaliyopatikana na katika uwekezaji na ustawi wake wa kiuchumi.

Waziri aliongezea dhana ya kongamano hilo lenye  kauli Mbiu ya “Wekeza Tanzania kuongeza thamani ya ziada” linatumika kujenga uchumi imara ambao umeshirikisha Watanzania wengi.

“Na itatutengenezea mazingira mazuri ya biashara ambayo yatachochea wananchi wengi katika uwekezaji na ushiriki wao katika kujenga uchumi,"alisema Waziri Mhagama

Baraza la Uwekezaji wa Wananchi Kiuchumi limeingia makubaliano na taasisi ya serikali inayosimamia manunuzi ya umma, katika moja ya kipengele katika sheria ya manunuzi ya umma kinachosisitiza kila asilimia 30 ya manunuzi ya umma ya kila mradi yaende kwa vijana, wanawake wazee na watu wenye ulemavu ambayo ni sehemu ya uwezeshaji wa wananchi kiuchumi.

 

Kwa upande wake Bibi, Beng’i Issa Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi wa Kiuchumi (NEEC) amesema moja ya mambo wanayosimamia ni kuangalia kampuni zinazopata kazi kwenye miradi ya kiuchumi na bidhaa zinazouzwa katika miradi hiyo  zinatoka nchini.

Aidha kwenye ajira Baraza la Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi linaangalia ajira za moja kwa moja na ajira ambazo sio za moja kwa moja katika uhaulishaji wa teknolojia kwa kusimamia teknolojia nchini na mipango ya kutoa mafunzo ya kuhaulisha inafanyika

Akizungumzia kuhusu kongamano amesema kongamano hilo la Nne limelenga katika kujenga uelewa wa pamoja kuhusu ushiriki wa watanzania katika miradi ya kimkakati na uwekezaji unaofanyika hapa nchini pamoja na kushirikishana mafanikio na changamoto zilizopo katika ushiriki wa watanzania katika uwekezaji.

Read More

Friday, April 12, 2024

WAZIRI MHAGAMA “AWATAKA WANANCHI KUONDOKA MAENEO HATARISHI”


 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama amewataka  wananchi kuondoka katika maeneo hatarishi  ili kujikinga na mafurikio ya mvua za vuli zinazoendelea kunyesha.

Kauli hiyo ameitoa wakati alipotembelea na kujionea maeneo yaliyokubwa na mafuriko ya mvua katika Halmashauri  ya Mlimba Mkoani Morogoro ambapo amewaomba wananchi kuendelea kufuatilia na kusikiliza ushauri wa serikali.

Niwaombe wananchi tuendelee kushikamana ili kupambana na majanga ya Mvua na Mafuriko, ambayo yameleta kadhia kubwa sana kwa wananchi.

“Serikali imetengeneza Mpango wa Dharura wa kukabiliana na mvua za El Nino na mvua za Masika, ambapo serikali itafanya kila linalowezekana kuzuia madhara yasitokee na hasa maisha ya watanzania,” alisema Waziri Mhagama

Ameongeza kusema mafuriko ya maji yamesababisha udongo kumomonyoka na kuharibu miundo mbinu ya reli na kuleta madhara mengine mengi niwaombe wanamlimba tuendelee kuangalia na kusikiliza ushauri wa serikali.

“Serikali itaendelea kuhakikisha inapambana dhidi ya magonjwa ya Mlipuko na uhaba wa chakula  na madhara mengine ambayo yameathiri wananchi, serikali itakuwa pamoja na nyinyi katika kutatua kadhia hizo alibainisha,” Waziri Mhagama

Niwaombe wananchi tuendelee kumuomba mwenyezi Mungu hali iliyopo mbele yetu iweze kupita kwa haraka na ipite kwa usalama mkubwa.

 Ameeleza kwamba katika utabiri wa hali ya hewa unaoendelea kutolewa unaonesha mvua hizi zinaendelea kunyesha hivyo ni vyema tukaendelea kujichukulia tahadhari sisi wenyewe.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Kilombero Mhe. Dustan Kyobya amesema changamaoto ya Mawasiliano ya barabara kwa watu wa Masagati na Utengule kwao wamekuwa kisiwa kutokana na miundo mbinu ya barabara kutopitika, lakini pia Mawasiliano kati ya Jimbo la Ifakara na Mlimba ambazo zinatengeneza wilaya ya kilombero nayo ni magumu.

Aidha Miundo mbinu ya reli ilidondokewa na udongo na kusababisha kukatika kwa makalvati ya reli hivyo kusababisha usafiri wa kutoka Mlimba kuelekea makambako kutokuwepo.

“Nimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutuma ndege kwa ajili ya kuokoa watu waliokwama na kuruhusu treni ya Mwakyembe  kuanza kubeba abiria ili kurahisisha mawasiliano,” alisema Mkuu wa wilaya

 

Awali Bi, Zainabu Makenjula Mkazi wa Mlimba ameomba serikali kushughulikia swala la barabara kwa wakati ili kurahisisha mawasiliano na kuwezesha wananchi kuendelea na shughuli za uzalishaji kwa sababu kuna maeneo magari wala pikipiki haviwezi kupita.

 

Read More

Thursday, March 21, 2024

SERIKALI YAELEKEZWA KUONGEZA NGUVU MAPAMBANO DHIDI YA VIRUSI VYA UKIMWI

 


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI imeshauri serikali kuongeza nguvu ya mapambano dhidi ya virusi vya UKIMWI katika maeneo ya migodi; vituo vya magari makubwa, maeneo ya mialo ya samaki na maeneo ya starehe kwa kuangalia namna ya bora kutoa elimu kwa wananchi ili kujenga uelewa wa pamoja.

 

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa kamati hiyo ya kudumu ya Bunge ya Afya na Masula ya UKIMWI Mhe. Mhe. Stanslaus Nyongo katika Ukumbi wa Mikutano wa Bunge Jijini Dodoma mara baada ya wajumbe kujadili na kuridhia randama ya Bajeti ya Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania –TACAIDS kwa Mwaka wa fedha 2024/2025.

 

Ameongeza kusema upo umuhimu wa kuweka vituo vya kisasa vya kusambazia mipira (kondomu) ambazo mhitaji anaweza kuweka tokeni na kupata, utaratibu ambao ni  mzuri kabisa na utaondoa utaratibu wa kuchukua mipira hiyo kiholela.

 

“Kuna baadhi ya sehemu wameanza kutumia mfumo huo wa kisasa wa kusambaza mipira, nasi tuna nafasi ya kuhimiza  kuwekwa kwa vifaa hivyo maeneo mbalimbali ya uwekezaji na maofisini  kwa sababu tumepitisha Bajeti hii ili muweze kufanya Kazi vizuri ,” alibainisha.

 

Tunahitaji malengo mliyoyakusudia yatekelezwe na yanatimizwe vizuri ili wananchi wapate mazingira mazuri ya kuishi na kuondokana na hali ya maambukizi ya UKIMWI ambayo yanafanya watu waishi katika hali ya wasiwasi.

 

Aidha niipongeze Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mapambano dhidi ya Virusi Vya UKIMWI na nimpongeze Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Mafanikio tuliyoyapata kwenye yale malengo ya 95, 95, 95.

 

“Utafiti umeonesha kwamba kiwango cha maambukizi ya Virusi Vya UKIMWI kinazidi kupungua na tunakazi kuendelea kusimamia sekta nyingine kuhakikisha mapambano dhidi ya Virusi Vya UKIMWI yanafanikiwa, “Alifafanua.

 

Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu ) Mhe. Jenista Mhagama alisema serikali inaendelea kutoa elimu kwa wananchi juu ya umuhimu wa kupima hususani kwa wanaume kwa kuwa wamekuwa wakijitokeza kwa idadi ndogo.

 

“Tunahitaji kurudisha tena ile kampeni ya FURAHA YANGU iliyoongozwa na Mhe.  Waziri Mkuu, kuanza tena kwa mwaka ujao wa fedha angalau tuhamasishe kiwango kikubwa cha wanaume wajitokeze kupima VVU,” alifafanua

 

Serikali kwa kushirikiana na Baraza la watu wanaoishi na Virusi Vya UKIMWI; Viongozi wa dini na Vongozi wa kijamii tutaendelea kutoa elimu ya kupinga unyanyapaa na ubaguzi kupitia majukwaa yao, makongamano na vipindi vya redio.

 

Awali Mhe. Dkt. Christina Mnzava aliomba serikali kutenga fedha zaidi kwa ajili ya kuongeza mapambano dhidi ya Virusi vya UKIMWI ili kufikia lile lengo la kufikia 95 ya Mwisho.

 

Naye Mhe. Cecil Mwambe aliomba serikali kuweka mazingira wezeshi kwa wakinababa WAVIU kuwa na uwezo wa kushiriki na kujihusisha katika vikundi kwenye shughuli za miradi ya maendeleo.

 

 

 

 

 

 

 

 

Read More

Wednesday, March 20, 2024

KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UTAWALA KATIBA NA SHERIA YAPITISHA MAKADIRIO YA BAJETI YA MWAKA WA FEDHA 2024/2025 KWA MAMLAKA YA KUDHIBITI NA KUPAMBANA NA DAWA ZA KULEVYA NA OFISI YA MSAJILI WA VYAMA VYA SIASA

 


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria imepitisha Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa fedha 2024/25 ya Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa.

Hayo yamesemwa na Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Florent Laurent Kyombo akikaimu nafasi ya Mwenyekiti wa Kamati hiyo hii leo  katika Ukumbi wa Mikutano wa Bunge Jijini Dodoma mara baada ya wajumbe kujadili na kuridhia Bajeti katika kikao kilichohusisha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Menejimenti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa.

Alisema baada ya majadiliano mazuri  na maelezo ya ziada kutolewa kuhusiana na  Bajeti iliyotengwa,  Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala  Katiba na Sheria imeridhia.

 “Tunawatakia matumizi mema ya fedha hizi pale zitakapokubaliwa kupitishwa katika vikao vya Bunge la Bajeti na tunahitaji kuona Bajeti ya fedha hizi inaakisi matarajio ya msingi ya nchi yetu,” alibainisha.

Kwa Upande wake Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Ummy Nderiananga akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu ameishukuru kamati kwa ushauri na kupitia Bajeti hiyo kifungu kwa kifungu na kutoa maelekezo ambayo yatasaidia Bajeti hiyo kukaa vizuri wakati kusomwa Bungeni kwenye vikao vya Bunge la Bajeti.

Read More

Sunday, January 21, 2024

SERIKALI YAAHIDI KUENDELEA KUREJESHA HALI KATIKA MIUNDO MBINU YA BARABARA ILIYOATHIRIKA NA MVUA

 Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, anayeshughulika na Sera, Bunge na Uratibu Mhe, Ummy Nderiananga amepongeza Kamati ya Maafa ya Mkoa wa Dar es salaam kwa jitihada mbalimbali za kurejesha hali katika maeneo ambayo miundo mbinu ya barabara imeathirika kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha.

Kauli hiyo ameitoa wakati wa ziara yake leo Mkoani humo alipotemebelea na kujionea athari za mvua zilizonyesha usiku wa kuamkia tarehe 20/ januari/2024 na kuathiri maeneo mabalimbali ya wilaya ya Kindondoni, Temeke, Kigamboni, Ubungo na Jiji la Ilala.

Naibu Waziri Ummy alisema anampongeza Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe.  Abert Chalamila kwa uongozi ambao wameuonesha katika kurejesha halina kazi waliyofanya.

“Naomba tufanye kazi hii usiku na mchana ili tuweze kurejesha hali mapema bila kuathiri shughuli za biashara na shughuli nyingine za uchumi zinazofanyika katika Mkoa wa Dar es saalam,” alihimiza.

Sisi kama serikali tunawahakikishia wana Dar es salamu kwamba tutafanya kazi hii ya urejeshaji wa hali kwa nguvu bila kuchoka,

Naye Mkuu wa wilaya ya Kindondoni Mhe. Saad Mtambule amesema kazi waliyofanya ni kusimamia usafishaji wa mitaro na usawishaji wa mito na hivyo kusaidia maji kutotuwama kwa muda mrefu.

“Tumeendelea kuwaeleza wananchi walio katika maeneo ya pembezoni mwa mito kama; Mto Nyakasangwa, Mto Mpiji, Mto Tegeta, Mto Mlalakuwa na Mto Ng’ombe kuhamia maeneo ya juu ili kuepeuka athari za mvua,”alibainisha

Ujenzi wa nyumba holela umesababisha Watu kujenga mpaka kwenye mapito asili ya maji na kusababisha maji kukosa sehemu za kupita na kuingia maeneo ya watu

“Lakini pia tuna kazi ya kuendelea kuwaelimisha wananchi ili wafuate misingi ya ujenzi wa maeneo kulingana na ramani ya mipango Miji,” alisisitiza

Akizungumza katika ziara hiyo Mkazi wa Ununio Bw. James Koyi ameishukuru serikali kwa kazi kubwa inayofanya ya urejeshajji wa hali katika maeneo yaliyoathirika mafuriko kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha mkoa wa Dar es salaam.

Hakuna aliyejua kama mvua itanyesha masaa ishirini na nne hata hivyo  serikali iendelee kufanya kazi katika kurejesha hali, alisema

Read More

Thursday, January 18, 2024

KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UTAWALA KATIBA NA SHERIA YAIPONGEZA SERIKALI KWA USIMAMIZI MZURI WA KUKABILIANA NA MAAFA


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria imeipongeza Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera Bunge na Uratibu kwa Usimamizi mzuri wa kukabiliana na  Maafa nchini.

Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Joseph Mhagama  wakati wa wasilisho lililohusu  namna Serikali ilivyojipanga katika kukabiliana na maafa pamoja na mfumo  wa usimamizi wa Uratibu wa maafa katika kuzuia na kupunguza madhara ya majanga na Utekelezaji wa Mpango wa Ujenzi wa Vituo vya utoaji huduma za matibabu kwa waraibu wa Dawa za kulevya nchini lililowasilishwa na Waziri wa Nchi ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama leo Bungeni Jijini Dodoma.

Mwenyekiti huyo  alisema Serikali ilifanya kazi kubwa  nayakupongezwa kutokana na jitihada zilizofanyika kuhakikisha waathirika wa mafuriko katika Halmashauri ya Wilaya ya Hanag mkoani Manyara wanaokolewa na kurejesha hali.

 “Tunapongeza sana Uongozi wa Ofisi ya Waziri Mkuu na Serikali kwa ujumla kazi mliyofanya ni kubwa ya kuokoa maisha ya wananchi na mal zao licha ya baadhi yao kupoteza maisha kama kamati tunawapongeza sana,” Alisema Mwenyekiti wa kamati hiyo.

Mhe. Dkt. Mhagama alisema, inatia moyo sana kuona Wizara ama idara inazozisimamia zinafanya kazi ambazo watanzania wanazitarajia kwa hiyo kamati nayo inajiskia kama ni sehemu ya hayo mafanikio makubwa yaliyopatikana.

“Maafa ni majanga lakini tunapokabiliana nayo na kuyafanyia kazi vizuri inatupa nguvu sasa, tunapenda tukupongeze Mhe. Waziri Jenista Mhagama, Katibu Mkuu  Dkt. Jim Yonazi na Watendaji wako wote kwa moyo wa uzalendo mliouonyesha katika kipindi kigumu ambacho Taifa lilipitia,” Alieleza Mhe. Dkt. Mhagama.

Vilevile Kamati pia ilipongeza Mamlaka ya Kudhibiti na Kukabilana na madawa ya kulevya kwa kazi nzuri inayofanya ya kujenga vituo vya Uraibu na kushauri kujengwa vituo zaidi kwa Mikoa ya kusini pamoja na kuendeleza mapambano ya uzalishaji na biashara ya Dawa za kulevya kama vile Bangi,Mirungi na dawa nyingine.

Akitoa maoni Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria Mhe. Edward Olekaita Kisau, alifafanua kwamba namna Serikali ilivyokabiliana wakati wote wa maafa na baada ya maafa ili kuhakikisha inarejesha hali na shughuli kuendelea kama ilivyokuwa awali na janga la Hanang’ ni mfano mzuri unaoweza kuchukuliwa katika uratibu mzima wa masuala ya kukabiliana na majanga nchini.

Naye  Mjumbe wa kamati hiyo Mhe. Dkt Alice Kaijage  akitoa maoni kuhusu wasilisho la Utekelezaji wa Mpango wa Ujenzi wa Vituo vya Utoaji wa Huduma za Matibabu kwa Waraibu wa Dawa za Kulevya nchini  alibainisha kuwa  ni wakati mzuri sasa kwa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za kulevya (DCEA) kuongozewa fedha za maendeleo kwani kazi inayofanywa na mamlaka hiyo ni kubwa na kuleta matokeo chanya kwa Taifa.

Awali akiwasilisha taarifa hizo mbele ya kamati hiyo Waziri wa Nchi Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama Alisema Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo  imeendelea kutoa elimu kwa jamii kupitia majukwaa mbalimbali kwa lengo la kuijengea  uelewa na uwezo wa kuzuia, kujiandaa, kukabili na kupunguza madhara yanayotokana na maafa.

“Ofisi ya Waziri Mkuu  kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa imeendelea kujenga uwezo wa usimamizi wa maafa kwa Kamati za Usimamizi wa Maafa za Mikoa na vifaa, Serikali imefanya manunuzi na kuratibu upatikanaji wa vifaa mbalimbali vya misaada ya kibinadamu kwa ajili ya msaada wakati wa dharura na kuvihifadhi katika maghala ya kuhifadhia vifaa vya misaada ya kibinadamu ili kuongeza uwezo wa nchi katika kukabiliana na maafa,” Alieleza Mhe. Jenista.

Aidha  Waziri huyo  alitoa wito kwa wananchi kutokudharau utabiri unaotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kwani mamlaka ina vifaa vinavyoendana na teknolojia ya kisasa ambapo  utabiri wa hali ya hewa  kwa wakati huu, umekuwa na  una usahihi wa asilimia 85% mpaka 95%.

 

Read More