Katibu
Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu ( Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Dkt. Jim
Yonazi (kushoto), Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano)
Bi. Mary Maganga pamoja na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu
(TAMISEMI) Bw. Sospeter Mtwale(kulia) wakifuatilia Hotuba ya Bajeti inayotolewa
na Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba kwa Mwaka 2026/2027 tarehe 1
Aprili, 2026 Bungeni Jijini Dodoma.
Wednesday, April 1, 2026
MAKATIBU WAKUU OFISI YA WAZIRI MKUU WAKIFUATILIA HOTUBA YA BAJETI
Tuesday, March 31, 2026
WANANCHI IDODI WAMLILIA LUKUVI
WANANCHI wamlilia aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu na Mbunge wa Jimbo la Isimani Marehemu William Lukuvi kwa kazi nzuri alizozifanya wakati akitekeleza majukumu yake katika sekta mbalimbali serikalini na kuwaletea maendeleo katika nyanja mbalimbali.
Hayo
yamelezwa kwa wakati tofauti hii leo wakati mwili wa marehemu Lukuvi
ulipowasili Kijijini Kwake Kata ya Idodi, Wilaya ya Iringa ambapo ndipo kunatarajiwa kuwa makazi yake ya
milele mara baada ya ibada ya mazishi kijijini hapo.
Wananchi
hao wameonesha simanzi kubwa na kumkumbuka kama kiongozi shupavu, na mtetezi wa
wanyonge hususan kwa wakazi wa Jimbo Lake la Isimani Mkoani Iringa.
Akizungumza
na waandishi wa habari Mmoja wa waombolezaji Bw. Kombo Jumbe amesema
Marehemu William Lukuvi aliasisi utaratibu wa kliniki za ardhi wakati akiwa
anahudumu kama Waziri wa Ardhi na hivyo kuwezesha wananchi kuhudumiwa kwa
urahisi na kwa haraka.
“Marehemu
Lukuvi alituwezesha sisi hupata huduma kwa haraka hasa zilizohusu masuala ya
migogoro ya ardhi na kufanya kufikiwa kwa urahisi na watoa huduma katika wizara
ya ardhi na yeye ndiye aliyezindua upatikanaji wa hati za ardhi na
kufanya zoezi lile kuwa endelevu” alieleza
Kwa
upande wake Bw. Frank Mbindile Mkazi wa Kijiji cha Magozi Wilaya ya Iringa
amesema Marehe William Lukuvi alikuwa ni mtu anayependa kusikiliza shida za
watu kwa makundi na hata shida za mwananchi mmoja mmoja na kukiri kuwa
wamepoteza mtu muhimu na Lulu kwa Taifa.
“Ni
aina ya kiongozi anayeamini katika kusimamia mambo ya msingi kwa ajili ya
maslahi mapana ya wananchi na akizungumza jambo alikuwa anauwezo wa
kulisimamia, hivyo wanaisimani tumepoteza kiongozi mkubwa,” alieleza.
Monday, March 30, 2026
MISA YA KUOMBEA NA KUAGA MWILI WA MAREHEMU MHE. LUKUVI MKOANI IRINGA
MISA Takatifu ya kuuaga Mwili wa
aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye
Ulemavu), na Mbunge wa Jimbo la Isimani, Marehemu Mhe. William Lukuvi,
iliyofanyika katika Kanisa Kuu la Moyo Mtakatifu wa Yesu lililopo Kihesa Iringa
leo tarehe 30 Machi, 2026 nakuongozwa na Askofu wa Jimbo la iringa Romanus
Mihali.
Misa hiyo imehudhuriwa na
viongozi mbalimbali wa Serikali, Viongozi wa Vyama vya Siasa, Viongozi wa dini
pamoja na Waombolezaji kutoka maeneo mbalimbali ya mkoa wa Iringa na nje ya
mkoa huo.
Mhe. Lukuvi amefariki dunia
tarehe 25 Machi, 2026 katika Hospitali ya Benjamin Mkapa Mkoani Dodoma
alipokuwa akipatiwa matibabu.
Sunday, March 29, 2026
MWILI WA MAREHEMU MHE. LUKUVI UKIWASILI KATIKA KIWANJA CHA NDEGE CHA IRINGA
Mwili wa aliekuwa Waziri wa
Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), na Mbunge
wa Jimbo la Isimani, Mhe. William Lukuvi, ukiwasili katika Kiwanja cha
Ndege cha Iringa tarehe 29 Machi, 2026.
Mwili huo umesafirishwa kutoka
Dar es Salaam leo baada ya shughuli ya kuaga iliyofanyika jana Machi 28, 2026
katika Viwanja vya Karimjee.
Saturday, March 28, 2026
NAIBU WAZIRI UMMY ASHIRIKI IBADA YA KUAGA MWILI WA MAREHEMU WILLIAM LUKUVI
NAIBU
Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Mhe. Ummy
Nderiananga akiwa katika ibada ya kuaga mwili aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya
Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Marehemu Mhe. William
Lukuvi leo katika viwanja vya Karimjee Hall Jijini Dar es salaam.
Mhe.
Lukuvi amefariki dunia tarehe 25 Machi, 2026 katika Hospitali ya Benjamin
Mkapa Mkoani Dodoma alipokuwa akipatiwa matibabu.
DKT. YONAZI AWASILISHA WASIFU WA MAREHEMU WILLIAM LUKUVI
WASIFU
WA ALIYEKUWA WAZIRI WA NCHI OFISI YA WAZIRI MKUU SERA, BUNGE, URATIBU NA WENYE
ULEMAVU MAREHEMU WILLIAM VANGIMEMBE LUKUVI
KUZALIWA
Mheshimiwa
William Vangimembe Lukuvi alizaliwa tarehe 15 Agosti 1955 katika kijiji cha
Mapogoro, Kata ya Idodi - Wilaya ya Iringa Vijijini, Mkoani Iringa.
Marehemu
William Vangimembe Lukuvi alikuwa mwanasiasa mashuhuri alieshika nyadhifa
mbalimbali za uongozi na aliesifika kwa ubunifu, uthubutu, uchapakazi,
uzalendo, mwenye uwezo wa kujitoa na kujituma katika kazi na aliweka maslahi ya
Taifa mbele na wakati wote aliamini katika matokeo chanya katika utekelezaji wa
shughuli mbalimbali za Serikali. Alijulikana kwa mtindo wake wa kazi wa
kutembelea maeneo ya miradi na kusikiliza kero za wananchi moja kwa moja, jambo
lililosaidia kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa shughuli za Serikali.
Katika kudhihirisha uchapakazi wake, siku moja kabla ya umauti kumkuta,
marehemu alihudhuria na kuratibu Serikali katika Vikao vya Kamati za Kudumu za
Bunge pamoja na kutoa maelekezo mbalimbali ya Serikali.
ELIMU
Marehemu
William Vangimembe Lukuvi alipata elimu ya Msingi katika Shule ya Msingi
Kitanewa kuanzia mwaka 1962 hadi 1970. Alijiunga na Chuo cha Ualimu Tabora
(TTC) kuanzia mwaka 1974 – 1975 ambapo alihitimu na kutunukiwa Cheti cha
Ualimu. Mwaka 1982- 1983 alijiunga na Shule ya Komsomol High School, Moscow
nchini Urusi na kutunukiwa Stashahada ya Juu ya Sayansi ya Siasa (Advanced
Diploma in Political Science). Alipata Shahada ya Masuala ya Kimatiafa na
Diplomasia yaani Bachelor of Arts in International Studies and Diplomacy kutoka
Washington International University kuanzia mwaka 1999 – 2001, na baadaye
alijiendeleza kimasomo katika ngazi ya shahada ya uzamili katika Chuo Kikuu
Huria Tanzania ambapo alihitimu na kutunukiwa Shahada ya Uzamili katika Sayansi
ya Siasa mwaka 2008 – 2011.
KAZI
NA SIASA
Marehemu
William Vangimembe Lukuvi alianza safari yake ya kisiasa mwaka 1973 alipojiunga
na Chama cha TANU akiwa mwanafunzi wa Chuo cha Ualimu Tabora (TCC) na
kuchaguliwa kuwa kiongozi wa chama katika chuo hicho mwaka 1974 - 1975.
Mnamo mwaka 1984 alichaguliwa kuwa mjumbe wa Vikao vya umoja wa Vijana wa CCM
katika Ngazi ya Wilaya hadi Taifa. Alichaguliwa kuwa Katibu wa Mkoa na Wilaya
wa chama cha CCM mwaka 1980 – 1984. Vile vile, aliteuliwa kuwa Naibu Katibu
Mkuu wa Umoja wa Vijana wa CCM mwaka 1993 – 1994. Aidha, Alichaguliwa kuwa
Mjumbe wa Halmashuari Kuu ya CCM na Mjumbe wa Kamati ya Maadili ya Chama mwaka
2010 hadi sasa.
Marehemu
William Vangimembe Lukuvi aliajiriwa kama Mwalimu katika Wizara ya Elimu
kuanzia mwaka 1975 hadi 1980.
Aliteuliwa
kuwa Mkuu wa Wilaya ya Bukoba kuanzia mwaka 1994 – 1995, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma
2006 – 2008 na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam 2008 - 2010.
Katika
uchaguzi Mkuu wa kwanza wa vyama vingi vya Siasa nchini uliofanyika mwaka 1995,
Marehemu Lukuvi alichaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Isimani na hivyo kuwa
mbunge wa kwanza wa jimbo hilo alilolitumikia kwa takribani miaka 30 hadi
umauti ulipomkuta. Akiwa mbunge aliwahi kuwa mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya
Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira kuanzia Mwaka 2005 – 2010.
Katika
maisha yake ya siasa, Marehemu Lukuvi aliingia katika Baraza la Mawaziri kwa
mara kwanza alipoteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Vijana na Ajira mwaka 1995 –
2000, na baadaye aliteuliwa kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu
anayeshughulikia Sera, Bunge na Uratibu na Mnadhimu Mkuu wa Serikali (Chief
Whip) kati ya mwaka 2000 – 2005, 2010 – 2015 na 2025 - 2026.
Halikadhalika,
Marehemu Lukuvi aliteuliwa kuwa Waziri wa Ardhi Nyumba, na Maendeleo ya Makazi
kuanzia Januari, 2015 hadi mwaka 2022.
Aidha,
mnamo Juni 2023, Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania alimteua kuwa Mshauri wa Rais kuhusu Mahusiano ya Kisiasa na Kijamii.
MAFANIKIO
KATIKA SEKTA ALIZOONGOZA KIPINDI CHA UTUMISHI WAKE
Akiwa
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu),
Alikuwa
msimamizi mahiri wa shughuli za Serikali Bungeni na alifanikiwa kuimarisha
mahusiano kati ya Serikali na Bunge, jambo ambalo lilimfanya kuwa mmoja wa
Mawaziri wenye ushawishi mkubwa katika awamu mbalimbali za uongozi, na kujenga
daraja imara kati ya Serikali, Bunge na wananchi.
Alisimamia
utekelezaji wa sera mbalimbali zilizolenga kuboresha ustawi wa wenye ulemavu
akihamasisha ushirikishwaji wa watu wenye ulemavu katika fursa za kiuchumi na
ajira na kusisitiza kuwa kundi hili ni sehemu muhimu ya nguvu kazi ya taifa.
Alisimmamia
kikamilifu Ujenzi wa Mji wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma ambao hadi sasa
umefikia wastani wa asilimia 93 na tayari Wizara 15 zimeshahamia katika mji huo
na zinatoa huduma kwa umma kutoka hapo.
Alisimamia
uimarishaji wa mifumo ya kisera kwa kufanya maboresho katika usimamizi wa maafa
nchini ikiwemo Mfumo wa Taarifa wa kielektroniki wa Usimamizi wa Maafa
(Disaster Management Information System - DMIS), hatua iliyosaidia kupunguza
Athari za maafa nchini.
Alikuwa
mstari wa mbele kwa kuhakikisha Wizara zote zinafanya kazi kwa ushirikiano ili
kuwezesha ufanisi katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM na kuhakikisha
ahadi za serikali kwa wananchi zinatekelezwa.
Akiwa
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
Alifanikiwa
kutatua migogoro ya ardhi nchini kwa kuanzisha mifumo bora ya kutatua migogoro
ya ardhi na kupeleka huduma bora na zilizo karibu na wananchi.
Alisimamia
uanzishwaji wa mifumo ya kidijitali ya usimamizi wa ardhi iliyolenga kupunguza
urasimu na kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa kodi ya pango la ardhi, hatua
iliyosaidia kuongeza mapato ya Serikali.
Alisimamia
utoaji wa hati miliki za ardhi zaidi ya 1,992,245 kwa Watanzania hatua
iliyosaidia kuwawezesha wananchi kiuchumi kwa kutumia hati hizo kama dhamana za
mikopo.
Alifanikiwa
kutenga ardhi yenye ukubwa wa ekari 224,439.4 kwa ajili ya uwekezaji kupitia
Mipango Kabambe ya miji, mipango ya matumizi ya ardhi ya Wilaya na Vijiji.
Hatua hii ilisaidia kuongeza uwekezaji nchini na kutoa ajira kwa wananchi.
Akiwa
Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa CCM
Alianzisha
mfumo wa mbio za mwenge kwa kushindanisha mikoa katika maandalizi, hamasa na
utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika Mikoa husika. Suala hili lilileta
chachu ya utekelezaji wa miradi hiyo kwa ufanisi na kuleta matokeo makubwa kwa
wananchi.
Alibuni
na kuanzisha mradi wa mabasi ya wanafunzi katika Mkoa wa Dar es Salaam jambo
ambalo lilipunguza adha kubwa ya usafiri kwa wanafunzi wa Jiji la Dar es
Salaam.
Akiwa
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma
Alifufua
na kuimarisha kilimo cha mtama na kuanzisha shamba la ushirika la zabibu
akishirikiana na benki ya CRDB ambapo mradi huo sasa unasimamiwa na Wizara ya
Kilimo ukijulikana kama BBT (Bulding a Better Tommorow).
Alihakikisha
kuwa mipango ya upanuzi wa mji wa Dodoma inazingatia sheria na taratibu za
mipango miji ili kuzuia ujenzi holela, jambo ambalo lilikuwa ni msingi muhimu
wa ukuaji wa Mji mkuu wa kisasa.
Alisimamia
Ujenzi wa Chuo Kikuu cha UDOM, hatua iliyosaidia kuongeza udahili wa Wanafunzi
wa Elimu ya Juu nchini.
FAMILIA
Enzi
za uhai wake, Marehemu Lukuvi alifunga ndoa takatifu tarehe 28 Julai, 1990 na
Bi. Germina Lukuvi katika Kanisa la Mtakatifu Petro, Jijini Dar es Salaam na
kujaaliwa kupata watoto watatu ambao ni Nobert William Lukuvi, Brown William
Lukuvi na Anifisye Vanessa William Lukuvi.
Marehemu
Lukuvi ameacha mjane, watoto watatu na mjukuu mmoja aitwae Donovan.
UGONJWA
NA KIFO
Marehemu
William V. Lukuvi alifariki dunia tarehe 25 Machi, 2026 saa 1:00 asubuhi katika
Hospital ya Benjamini Mkapa Jijini Dodoma alipokuwa akipatiwa matibabu baada ya
kupata ugonjwa wa mshtuko wa Moyo.
Tunamsukuru
mwenyezi Mungu, kwa maisha ya Willian V. Lukuvi ambaye hakika aliitumikia
nafasi yake ya Ubunge na nafasi nyingine alizoaminiwa na serikali kwa bidii,
ufanisi na uadilifu wa hali ya juu. Tunaomba Mungu ampe pumziko la Amani.
RAHA
YA MILELE UMPE EE BWANA NA MWANGA WA MILELE UMWANGAZIE, APUMZIKE KWA AMANI,
AMINA.
Thursday, March 26, 2026
SERIKALI YAIMARISHA HUDUMA KWA WENYE ULEMAVU: WATENDAJI WAJENGEWA UWEZO MATUMIZI YA MFUMO WA (PD-MIS) RUVUMA
Serikali
imeendelea kuchukua hatua madhubuti za kuboresha huduma kwa watu wenye ulemavu
kwa kuwajengea uwezo watendaji wake katika matumizi ya mfumo wa kielektroniki
wa ukusanyaji na usimamizi wa taarifa za watu wenye ulemavu (PD-MIS), hatua
inayolenga kupata takwimu sahihi kuanzia ngazi ya kaya hadi mkoa.
Mafunzo
hayo yamehusisha Maafisa Tehama na Maafisa Ustawi wa Jamii kutoka Mikoa ya
Ruvuma, Mtwara, Lindi na Njombe, yakifanyika mkoani Ruvuma kwa lengo la
kuwawezesha washiriki kutambua na kusimamia matumizi ya mfumo huo katika maeneo
yao ya kazi.
Akizungumza
wakati wa mafunzo hayo, Afisa kutoka Kitengo cha Huduma kwa Watu Wenye Ulemavu,
Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Bw. Jackob
Mwinula, alisema kuwa uwezeshaji huo ni muhimu katika kuhakikisha watendaji
wanakuwa na uelewa wa kutosha wa mfumo huo na kuwafikia wananchi kwa ufanisi
zaidi.
“Baada
ya mafunzo haya, tunatarajia kuona watu wenye ulemavu wakisajiliwa, kupata
namba za utambulisho na hivyo kuwezeshwa kufikia huduma mbalimbali za kijamii
pamoja na kuunganishwa na mifumo mingine ya Serikali,” alisema Bw. Mwinula.
Aliongeza
kuwa zoezi la usajili ni endelevu na litahusisha maafisa kuwafikia walengwa
moja kwa moja katika maeneo wanayoishi ili kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma.
Kwa
upande wake, Bi. Suzana Mayengo, mwezeshaji kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu,
alisema mafunzo hayo pia yanalenga kuwajengea watendaji uwezo wa kutambua aina
mbalimbali za ulemavu na namna ya kushirikisha kundi hilo katika mipango ya
maendeleo ili kuhakikisha ushirikishwaji jumuishi na unaozingatia mahitaji yao.
Aidha,
upatikanaji wa taarifa sahihi utaiwezesha Serikali kutekeleza kikamilifu
Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Watu Wenye Ulemavu wa mwaka 2006 unaosisitiza
kauli mbiu ya “Nothing About Us Without Us”, inayolenga ushirikishwaji wa moja
kwa moja wa kundi hilo katika maamuzi yanayowahusu.
Naye
Mchambuzi wa Mifumo kutoka Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA), Bw. Antony
Nchimbi, alieleza kuwa mfumo wa (PD-MIS) umesanifiwa kwa ushirikiano kati ya
e-GA na Ofisi ya Waziri Mkuu, na umeunganishwa na mifumo mingine 11 ya Serikali
ili kurahisisha upatikanaji na ubadilishanaji wa taarifa.
Alibainisha
kuwa mfumo huo una uwezo wa kuwasiliana na mifumo muhimu ikiwemo wa wanafunzi
(SIS) kutoka TAMISEMI, mfumo wa afya (GoTHOMIS), mfumo wa mikopo (Wezesha) na
Mfumo wa Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB), hatua itakayosaidia
kuthibitisha na kuboresha huduma kwa watu wenye ulemavu nchini.
Monday, March 23, 2026
KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UTAWALA, KATIBA NA SHERIA YAPITISHA MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA BAJETI YA OFISI YA WAZIRI MKUU KWA MWAKA WA FEDHA 2026/27
Kamati
ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria imepitisha Makadirio ya Mapato
na Matumizi ya bajeti ya kiasi cha 168,540,287,000 kwa mwaka wa fedha 2026/27
ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi zilizopo chini ya Ofisi hiyo.
Hayo
yamesemwa na Mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro (Mb.) leo katika
Ofisi za Bunge Jijini Dodoma mara baada ya wajumbe kujadili na kuridhia
makadirio hayo ya bajeti katika kikao kilichohusisha Kamati ya Kudumu ya Bunge
ya Utawala, Katiba na Sheria, Menejimenti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Wakuu wa
Taasisi zilizo chini ya Ofisi hiyo, wataalamu
kutoka Idara na Vitengo vya Ofisi ya Waziri Mkuu.
Awali
akiwasilisha Taarifa kuhusu Utekelezaji wa Bajeti ya mwaka wa fedha 2025/26 na
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa fedha 2026/27 mbele ya kamati hiyo
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera,
Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. William Lukuvi ameishukuru kamati kwa
kujadili na kupitisha makadiri ya bajeti hiyo huku akisema Ofisi yake
itaendelea kufanya kazi kwa weledi zaidi kwa kuzingatia jukumu la msingi la
Uratibu wa Shughuli zote za Serikali.
Ameongeza
kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu inaahidi kuendelea kutoa ushirikiano kwa Kamati hiyo
ikiwa ni pamoja na kutekeleza maoni na ushauri wa kamati.
Thursday, March 19, 2026
KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA AFYA NA MASUALA YA UKIMWI YAIPONGEZA SERIKALI KUWAWEZESHA KIUCHUMI WAISHIO NA VVU
Mwenyekiti
wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI ambaye pia ni Mbunge
wa Arumeru Magharibi Mhe. Johannes Lukumay ameipongeza Serikali kuendelea kusaidia kundi la Watu
waishio na Maamubikizi Virusi vya UKIMWI kupitia shughuli mbalimbali za
kiuchumi ili kujikwamua kiuchumi.
Mhe.
Lukumay ameyasema hayo mara baada ya ziara ya kutembelea Baraza la Watu waishio
na maambukizi ya Virusi vya UKIMWI akiwa ameambatana na Wajumbe wa Kamati ya
Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI katika (Konga ya Jiji)
iliyofanyika katika Viwanja vya Pugu
Mnadani Jijini Dar es Salaam.
Amesema
kuwa watu waishio na maambukizi ya Virusi vya UKIMWI ni sawa na watu wengine
hivyo yapaswa kuwapa kipaumbele katika fursa mbalimbali za kimaendeleo.Pia
Mwenyekiti huyo amelipongeza kundi hilo kwa namna wanavyojituma katika
kuhakikisha wanajikwamua kiuchumi na kuondokana na umasikini hivyo kuziagiza
sekta husika kusaidia katika kuwatafutia masoko kwa ajili ya bidhaa zao.
Kwa
upande wake Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye
Ulemavu Mhe. Ummy Nderiananga amesema kuwa Serikali chini ya uongozi wa Rais
Dkt. Samia Suluhu Hassan wataendelea kuunga mkono jitihada zao kwa kuongeza
nguvu zaidi kwa Wanakonga ili waweze kujikwamua kiuchumi.
Mhe.
Nderiananga amempongeza Mkurugenzi wa Jiji, Mkuu wa Wilaya pamoja na Katibu
Tawala wa Halmashauri ya Jiji la Dar es salaam na timu nzima kwa kuwawezesha
Wanakonga katika fursa mbalimbali na kuwataka kuendelea na desturi hiyo ya
kuwawezesha kwani mwaka huu wa fedha bado haujamalizika.
Aidha
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es salaam Elihuruma Mabelya amesema
kuwa moja ya eneo waliloliwekea nguvu ni Konga hiyo kwa kuunga mkono shughuli
zao za kiuchumi ili kuhakikisha wanainuka na kufanikiwa katika nyanja
mbalimbali za maendeleo
Wednesday, March 18, 2026
KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UTAWALA, KATIBA NA SHERIA YARIDHISHWA NA UTEKELEZWAJI MRADI WA KITUO CHA TAIFA CHA UTENGAMAO.
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria imetembelea na kukagua mradi wa ujenzi wa Kituo cha Utengamao cha Taifa unaotekelezwa na Mamlaka ya Kudhibiti na kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) katika eneo la Itega, jijini Dodoma.
Ziara
hiyo imefanyika leo na kuongozwa na Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe.
Edwin Swale (Mb) ikiwa ni sehemu ya majukumu ya kamati ya kusimamia na kukagua
utekelezaji wa miradi mbalimbali.
Akizungumza
wakati wa ziara hiyo, Mhe. Swale amesema kuwa kamati imeridhishwa na hatua ya
utekelezaji ambayo mradi umefikia kwani
unaenda kutimiza dhamira ya Serikali ya
Awamu ya Sita ya kujali Utu na Ustawi wa Watanzania.
Sambamba
na hilo, ameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu
kupitia Mamlaka ya kudhibiti na kupambana na dawa za Kulevya kwa kubuni mbinu
ya jinsi ya kusaidia waraibu watokanao na matumizi ya madawa za kulevya.
Awali,Naibu
Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. Ummy
Nderiananga amesema kuwa Mradi huo ni endelevu ikiwa ni juhudi ya Serikali
katika mapambano dhidi ya Dawa za kulevya na kuahidi kuendelea kushirikiana na
Taasisi binafsi katika mapambano dhidi ya matumizi ya Dawa za kulevya Nchini.
Tuesday, March 17, 2026
NAIBU WAZIRI UMMY ATOA MSUKUMO KWA WATUMISHI KUONGEZA UFANISI, AAGIZA UTEKELEZAJI THABITI WA BAJETI
Naibu
Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Mhe.
Ummy Nderiananga, amewahimiza watumishi wa ofisi hiyo kuendelea kufanya kazi
kwa bidii, ufanisi na weledi ili kuhakikisha malengo yaliyoainishwa katika
bajeti ya Serikali yanatekelezwa ipasavyo.
Akizungumza
wakati wa ufunguzi wa Baraza la Wafanyakazi uliofanyika leo Jijini Dodoma, Mhe.
Ummy—aliyemwakilisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu
na Wenye Ulemavu), Mhe. William Lukuvi—alisisitiza umuhimu wa watumishi
kushirikiana na kuzingatia misingi ya uwajibikaji katika utekelezaji wa
majukumu yao ya kila siku.
Alifafanua
kuwa mabaraza ya wafanyakazi yameanzishwa kufuatia Tamko Na. 1 la mwaka 1970
lililotolewa na Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, likiwa
na lengo la kuongeza ufanisi na tija mahali pa kazi.
“Kupitia
mabaraza haya, wafanyakazi na waajiri hupata fursa ya kujadili na kubadilishana
mawazo kwa manufaa ya taasisi. Ni matumaini yangu kuwa majadiliano yenu
yatajikita katika kuimarisha utendaji wa Ofisi ya Waziri Mkuu,” alisema Mhe.
Ummy.
Awali,
Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu),
Dkt. Jim Yonazi, alimshukuru Waziri wa Nchi pamoja na Naibu Waziri kwa
kushiriki katika kikao hicho muhimu cha Baraza la Wafanyakazi.
Aidha,
aliwapongeza viongozi hao kwa ushindi walioupata katika Uchaguzi Mkuu na kwa
kuendelea kuaminiwa na Mhe. Rais katika kusimamia sekta hiyo nyeti.
Dkt.
Yonazi alieleza kuwa kikao hicho kimewakutanisha Menejimenti ya Ofisi ya Waziri
Mkuu pamoja na wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi ili kujadili bajeti ya ofisi
hiyo, ikiwa ni pamoja na kupitia taarifa ya utekelezaji kabla ya kuidhinisha
hatua za kuwasilisha bajeti hiyo katika ngazi zinazofuata.
Monday, March 16, 2026
WANANCHI MKINGA WANUFAIKA NA UWEKEZAJI KATIKA KILIMO CHA MWANI
Wananchi
wa Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga wanatarajiwa kunufaika zaidi kiuchumi kupitia
uwekezaji wa Serikali katika sekta ya kilimo cha mwani, hatua inayolenga
kuongeza thamani ya mazao ya bahari na kuboresha maisha ya jamii za pwani.
Akizungumza
wakati wa uzinduzi wa kaushio jipya na mashine mbili za kisasa za kusaga mwani
uliofanyika katika Kijiji cha Kichaka Miba, Wilaya ya Mkinga, Naibu Waziri wa
Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Mhe. Ummy
H. Nderiananga, amesema mradi huo ni sehemu ya jitihada za Serikali kuimarisha
uchumi wa wananchi wa maeneo ya pwani.
Mradi
wa Kuimarisha Usalama wa Bahari unaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia
Idara ya Menejimenti ya Maafa kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja
wa Mataifa (UNDP), na unatekelezwa na Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini
(IRDP) Tawi la Mwanza kwa ushirikiano na Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga ambapo
Lengo lake ni kuimarisha ufuatiliaji na ulinzi wa bahari pamoja na kuongeza
thamani ya rasilimali za baharini kwa manufaa ya jamii.
Mhe.
Nderiananga amesema kupitia mradi huo, Serikali imenunua boti mbili za doria,
kujenga kaushio la kisasa la mwani, kusimika mashine za kusaga mwani na kutoa
mafunzo kwa vikundi vya wakulima. Ameongeza kuwa hatua hizo zitaboresha ubora
wa mwani, kupanua masoko, kuongeza kipato cha wakulima na kusaidia kuzuia
vitendo vya kihalifu baharini.
Kwa
upande wake, Mkurugenzi wa Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP), Dkt.
Guvenail Mkonoko, amesema kabla ya utekelezaji wa mradi huo wataalamu walifanya
tathmini iliyobaini changamoto za mbinu duni za kilimo, ukaushaji usio salama
na ukosefu wa miundombinu ya kisasa ya uchakataji.
Naye
mwakilishi wa wakulima wa mwani, Bi. Mwamvua Bwebwe, Ameishukuru Serikali ya
Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwawezesha kuongeza
uzalishaji, kupunguza upotevu wa mazao na kuboresha kipato chao.
SERIKALI KUIFANYA TANZANIA KITOVU CHA BIASHARA - DKT. YONAZI
KATIBU
Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. Jim Yonazi
amesema Serikali imefanya juhudi mbalimbali za Kisera, Sheria na Kimkakati ili
kuhakikisha Tanzania inakuwa kitovu cha biashara Afrika Mashariki na Kati.
Dkt.
Yonazi aliyasema hayo katika kikao cha Kikundi Kazi cha Mazingira ya
Biashara cha Baraza la Taifa la Biashara TNBC kilichofanyika jijini Dar es
salaam.
Alisema
Serikali imefanya jitihada za kukuza biashara nchini huku akizitaka sekta
binafsi kuendelea kushirikiana na serikali.
“Serikali
imefanya juhudi mbalimbali katika uwekezaji nchini ikiwemo mazingira ya
ufanyaji wa biashara ya kisera, kisheria na lengo ni kuhakikisha Tanzania
inakuwa kitovu cha biashara Afrika mashariki na kati.
Kwa
upande wake Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Biashara (TNBC) Dkt. Godwill
Wanga alisema kikao hicho kimefanyika ili kujadili maendeleo ya biashara
nchini.
Alisema
kikao hicho kimejadili vivutio ambavyo serikali inaweza kufanya uwekezaji
zaidi katika sekta ya afya ili bima ya afya kwa wote itakapoanza iweze
kuwa na faida kwa Watanzania.
“Kikao
hichi ni muendelezo wa vikao ambavyo tumekuwa tukifanya mara kwa mara katika
kujadili maendeleo ya biashara ambapo katika kikao hiki kimejadili kuhusu
miundombinu ya mtandao katika katika nchi yetu.
Aliongeza
kuwa :”Tumekubaliana kufanya utafiti kuhusu madhara ya vita katika mashariki ya
kati katika uchumi wetu.
Friday, March 13, 2026
DKT. YONAZI AONGOZA MKUTANO WA TANZANIA NATIONAL COORDINATING MECHANISM - (TNCM)
Katibu
Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim
Yonazi ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa inayosimamia na kuratibu
fedha za Global Fund inayojulikana kama Tanzania National Coordinating
Mechanism – (TNCM) ameongoza Kikao cha (TNCM) kilichofanyika katika Ukumbi wa
Serengeti, Jengo la FCC, jijini Dar es Salaam.
Katika mkutano huo, mambo mbalimbali
yamejadiliwa ikiwemo maandalizi ya awali ya kuandaa andiko la maombi ya
ufadhili wa awamu ya nane ya Mfuko wa Dunia (Global Fund Grant Cycle 8 - GC8).
Aidha, Dkt. Yonazi amesisitiza umuhimu wa kuwa na mipango madhubuti na yenye
tija ili kuhakikisha Tanzania inanufaika kikamilifu na rasilimali hizo katika
mapambano dhidi ya magonjwa ya UKIMWI, Kifua Kikuu, na Malaria, pamoja na
kuimarisha mifumo ya afya kwa ujumla.
Akifunga
mkutano huo, Dkt. Yonazi amewahimiza wajumbe na wadau wote kuendeleza
ushirikiano na uwazi (Transparency) katika hatua za maandalizi ya GC8, huku
akibainisha kuwa ufanisi wa (TNCM) unategemea sauti ya pamoja ya wadau wote
wanaowakilishwa.
Mkutano
huo uliowahusisha wadau kutoka Serikalini, Sekta Binafsi, Asasi za Kiraia, na
Washirika wa Maendeleo, umelenga kujadili masuala mtambuka ya uendeshaji wa
taasisi hiyo pamoja na kuweka misingi imara ya upatikanaji wa rasilimali katika
sekta ya afya nchini.
Mbali na hayo,
katika mkutano huo, wajumbe walimchagua Bw. Godlisten Moshi kuwa Makamu
Mwenyekiti mpya wa (TNCM) ili kukamilisha safu ya uongozi na kuongeza ufanisi
katika utendaji wa chombo hicho.
Monday, March 2, 2026
VIJANA WA VYUO VIKUU NA VYUO VYA KATI WASISITIZWA KUENDELEZA MAPAMBANO DHIDI YA VVU NA UKIMWI
Serikali
imehamasisha mapambano dhidi ya VVU na
UKIMWI kwa kundi la vijana katika Chuo
cha Uhasibu Arusha (IAA) na Taasisi ya
Maendeleo ya Jamii ya Tengeru.
Hamasa
hiyo imetolewa leo na Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge
Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. Ummy Nderiananga katika ziara yake ya
kufuatilia na kutathimini utekelezaji wa Afua za VVU na UKIMWI katika
vyuo vya kati na Vyuo Vikuu Jijini Arusha.
Mhe.
Nderiananga, ameipongeza Tume ya kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) kwa kazi kubwa ya kusimamia utekelezaji wa
Afua za VVU na UKIMWI waliofanya kwenye Taasisi 26 za vyuo vya kati na Vyuo
Vikuu nchini, na kuwapongeza vijana wa Vyuo hivyo kwa kupambana nakuchukua tahadhali na kuzungatia
elimu ya kinga na maambukiz ya Virusi
vya UKIMWI waliyoipata kupitia wataalam mbalimbali.
Pia,
Mhe. Nderiananga amesisitiza kundi la vijana haswa wa Kiume kuhamasika katika
upimaji ili watambue hali za Afya zao na kuhimiza Ufuasi mzuri wa Dawa za
kufubaza virusi vya UKIMWI kwa waathirika wapya, lakini pia amewapongeza
Waathirika wote wa VVU kote nchini kwa
matumizi sahihi ya ARV.
Awali,
Mkurugenzi wa Idara ya Mwitikio wa Kitaifa wa UKIMWI kutoka Tume ya Kudhibiti
UKIMWI Tanzania (TACAIDS) Bi Audrey Njelekera, Amesema kuwa Serikali kwa
kushirikiana na wadau mbalimbali kupitia takwimu zilizopo inamipango madhubuti
ya kupunguza na kutokomeza maambukizi ya VVU na UKIMWI nchini kote.
Ameongeza
kuwa, takwimu zinaonyesha kuwa kundi la vijana kuanzia miaka 15 hadi 24 ndio
linaloathirika zaidi na maambukizi mapya hivyo TACAIDS imeanzisha Klabu za kijamii kwenye vyuo vya kati na
vikuu ili kusaidia kupunguza unyanyapaa,
kuongeza idadi ya wanafunzi kupima na kuongeza ushiriki wa wanafunzi katika
mapamabano dhidi ya VVU. Vilevile, kuanzisha programu mbalimbali za kuhamasisha
na kuelimisha kupitia mijadala, kuandika machapisho, vibonzo, picha mjongeo na kampeni za kwenye
mitandao ya kijamii.
Nae,
Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Mipango, Fedha na Utawala wa Chuo cha Uhasibu Arusha, Dkt. Eliakira Nnko
amesema kuwa, Chuo kinaendelea kuweka
mipango na mikakati ya utekelezaji wa Afua za UKIMWI mahali pakazi kwa watumishi na wanafunzi wanaoishi na
maambukizi ya virusi vya UKIMWI, lengo kuu ni kuhakikisha Wanafunzi na
watumishi wanabaki na Afya njema, Kupunguza vifo na kutokomeza unyanyapaa ili
kuimarisha utendaji kazi na kuweka
mazingira salama kwa watumishi na
wanafunzi.
Sunday, March 1, 2026
SERIKALI YA AWAMU YA SITA YASISITIZA UWEZESHWAJI WA WATU WENYE ULEMAVU
Naibu
Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu),
Mhe. Ummy Nderiananga, amesisitiza dhamira ya Serikali ya kuendelea kuwawezesha
kiuchumi watu wenye ulemavu kupitia mikopo ya asilimia 10 ya mapato ya
Halmashauri, ikiwemo asilimia 2 inayotengwa mahsusi kwa kundi hilo.
Mhe.
Nderiananga ametoa kauli hiyo leo Jijini Arusha alipokutana na watu wenye
ulemavu ikiwa ni muendelezo wa Ziara yake iliyoanza Wilaya ya
Moshi-Kilimanjaro.
Naibu
Waziri Nderiananga, amewapongeza watu wenye ulemavu wa Mkoa wa Arusha kwa
nidhamu ya kurejesha mikopo kwa wakati na kuhimiza waliomaliza kurejesha waweze
kuomba tena ili kupanua shughuli zao za kiuchumi.
Aidha,
ameelekeza kuwa 30% ya manunuzi ya umma kwenye Halmashauri zote za Jiji la
Arusha ziende kwenye makundi haya maalum kama vile watu wenye ulemavu,
“tunapotengeneza masoko tutenge maeneo
maalumu kwaaajili ya watu wenye ulemavu, na nataka kuona miradi ya watu wenye
ulemavu kuwa ni miradi ya kielelezo Nchini’’Mhe. Nderiananga amesema
Kwa
upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Mhe. Mwinyi Ahmed Mwinyi ameishukuru
Serikali ya Awamu ya sita chini ya Mhe.
Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa juhudi za kuwakwamua kiuchumi watu wenye
ulemavu, na ameahidi kuandaa hafla
kwaajili ya kuwapongeza wanufaika wa Mikopo ya 2% waliofanya vizuri ili iwe
kama sehemu ya hamasa na kielelezo kwa wale ambao hawajafanyi vizuri na ambao
wanatamani kupata mikopo hiyo.
Awali,
Mkurugenzi wa Idara ya watu wenye ulemavu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera
Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu Bw. Kizito Wambura amesema Serikali inania
thabiti ya kuleta mabadiliko kwa watu wenye ulemavu na kutatua changamoto zilizobainishwa kupitia
mfumo wa kieletroniki wa taarifa za watu wenye ulemavu (PDMIS) ambao
tunategemea ufike kwenye maeneo yote ya Tanzania.
Saturday, February 28, 2026
WATU WENYE ULEMAVU WAJIKWAMUA KIUCHUMI KWA MIKOPO YA SERIKALI
Naibu
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe.
Ummy Nderiananga, amekutana na kundi la watu wenye ulemavu katika ziara
iliyowakutanisha na wanufaika wa mikopo
ya 10% ya mapato ya Halmashauri (2% kwa wenye Ulemavu) na wale ambao wameomba
na hawajapata.
Ziara
hiyo imelenga kujadili maslahi,Fursa na changamoto mbalimbali za watu wenye
ulemavu tukio hilo limefanyika, katika Ukumbi wa Ofisi ya Halmashauri Wilaya ya
Moshi.
"Ninamshukuru
Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu
Hassan kwa moyo wake wa upendo kwa kuweka mazingira wezeshi ya upatikanaji wa
mikopo kwa watu wenye ulemavu na ninawahimiza watu wenye ulemavu kuchangamkia
Fursa hizo na kujitokeza katika kupata zabuni za tenda za serikali kwa mfumo wa
manunuzi ya umma (30% kwa watu wenye ulemavu) zinazotolewa ili kuwaletea tija
na kujikwamua kiuchumi". Amesema hayo Naibu Waziri Mhe. Nderiananga.
Pia,
ameautaka Uongozi wa Wilaya ya Moshi kuhakikisha unaeaendelea kuwawezesha watu wenye ulemavu kwa kuwapa Fursa
za Tenda za manunuzi ya ndani kwa makampuni ya vikundi vya watu wenye ulemavu
ili kuwasaidia watu wenye ulemavu kuondoka kwenye umaskini.
Aidha,
amewapongeza Mkuu wa Wilaya ya Moshi na Uongozi wote kwa kukata kiu ya Mheshimiwaa Rais ya
kuwasikiliza wananchi na kuwaletea faraja Watanzania kwa kutoa mikopo ya
Asilimia 2% kwa kiwango cha 98% yaani shilingi 60.4M, pia hata wale ambao bado
hawajanufaika wameondoka hapa wakiwa na Matumaini.
Awali,
Mkuu wa Wilaya ya Moshi Mhe.Godfrey Mzava ameihakikishia jamii ya watu wenye
ulemavu kuwa Serikali inaendelea kufanya jitihada za kuwasaidia na kuwakwamua
kiuchumi.
Ameongeza
kuwa, Serikali iko tayari kushirikiana na Jamii na Vyama vyote vya watu wenye
ulemavu na itatetenga eneo maalumu la biashara kwaajili ya watu wenye ulemavu
ili wafanye biashara zao vizuri.
Nae,
Bw. Mwacha, Mlemavu wa viungo na mnufaika wa Mkopo aliemaliza deni lake
amemshukuru Mhe. Rais kwa kuwapa vipaumbe na kuahihidi kuendelea kuhamasishana
na kuelimishana kuhusu umuhimu wa mikopo hii ili kutoka kwenye dhana ya
utegemezi.
Friday, February 27, 2026
MRADI WA JNHPP KICHOCHEO MUHIMU KATIKA ZA FURSA ZA KIUCHUMI NA KIJAMII
Kamati ya Uongozi wa Mradi wa Bwawa la Julius Nyerere (JNHPP), tarehe 26 Februari 2026, imekagua maendeleo ya uzalishaji wa umeme katika mradi huo na kueleza kuridhishwa na usimamizi pamoja na utekelezaji wake, uliokidhi viwango vya ubora vinavyoendana na thamani ya fedha iliyowekezwa na Serikali.
Mwenyekiti
wa Kamati hiyo, ambaye pia ni Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,
Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, amesema kamati imefurahishwa na
namna bwawa hilo linavyochochea ukuaji wa uchumi kwa kuongeza uzalishaji wa
umeme unaosambazwa katika maeneo mbalimbali nchini, hatua inayochangia
kuimarika kwa upatikanaji wa nishati ya umeme.
“Tumeridhishwa
na jinsi mradi huu ulivyosimamiwa na kutekelezwa kwa ufanisi mkubwa.
Ukilinganisha na miradi mingine barani Afrika, mradi huu umejengwa kwa ubora wa
hali ya juu na umeleta unafuu katika huduma ya umeme nchini. Haya ni mafanikio
makubwa kwa Taifa,” alieleza Dkt. Yonazi.
Akizungumza
kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mkurugenzi wa Sera na Mipango,
Bw. Petro Lyatuu, amesema mradi huo umekamilika kwa asilimia 100 na
mchango wake tayari umeanza kuonekana.
Amefafanua
kuwa mwaka 2021, gridi ya taifa ilikuwa na jumla ya megawati 1,600, lakini kwa
sasa uwezo wa uzalishaji umefikia zaidi ya megawati 4,000, zaidi ya mara mbili
ya kiwango cha awali.
“Kwa
sasa bwawa linazalisha umeme na tija yake imeonekana wazi. Kuongezeka kwa
uzalishaji kumeimarisha gridi ya taifa na tunaendelea kuongeza nguvu katika
sekta ya nishati kwa ajili ya maendeleo ya nchi na ustawi wa wananchi,”
alisisitiza Bw. Lyatuu.
Aidha
kwa hatua nyingine Kamati hiyo ilitembelea kituo cha kupokea na kupoza umeme
cha Chalinze, kinachopokea umeme kutoka Bwawa la Julius Nyerere na kusambaza
katika maeneo mbalimbali ya nchi.
Akizungumza
kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Naibu
Mkurugenzi Mtendaji Uzalishaji, Mhandisi Antony Mbushi, amesema kituo hicho
kimekamilika na tayari kinafanya kazi.
Ameongeza
kuwa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme kutoka Chalinze hadi Dodoma umefikia
asilimia 71.58, huku mradi wa kusafirisha umeme kutoka Chalinze kupitia
Kinyerezi hadi Mkuranga umefikia asilimia 59.76.
SERIKALI YADHAMIRIA KUMALIZA CHANGAMOTO YA USAFIRI DAR ES SALAAM
KATIBU
Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim
Yonazi ambaye pia ni mwenyekiti wa Kamati ya Usimamizi wa Mradi wa DART amesema
Serikali imejipanga kikamilifu kuhakikisha inamaliza changamoto ya usafiri
katika Jiji la Dar es Salaam, ili wananchi waweze kupata huduma bora, ya haraka
na yenye uhakika.
Akizungumza
hii mara baada ya Kamati hiyo kufanya ziara ya kukagua miundombinu ya
usafirishaji jijini humo, Dkt. Yonazi amesema Serikali imewekeza kwa kiwango
kikubwa katika kuboresha sekta ya usafiri wa umma.
Alisema
katika ziara hiyo, kamati ilitembelea Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka Dar es
Salaam (DART) pamoja na Kampuni ya Uendeshaji wa Mabasi Yaendayo Haraka (UDART)
na kujionea maendeleo ya uwekezaji uliofanywa.
“Ni
dhamira ya Serikali kuhakikisha usafiri wa Dar es Salaam unakuwa bora, wa
kisasa na unaokidhi mahitaji ya wananchi. Tumejionea miundombinu iliyowekwa na
jitihada zinazoendelea kuboresha huduma,” alisema.
Dkt.
Yonazi alibainisha kuwa tayari kampuni zimeanza kuleta mabasi mapya, hatua
itakayoliwezesha jiji hilo kuwa miongoni mwa majiji yenye usafiri wa kisasa
barani Afrika. Aliongeza kuwa mabasi mengi yatatumia gesi asilia, huku Serikali
ikiwa imejenga miundombinu ya vituo vya gesi ili kuhakikisha huduma hiyo
inapatikana kwa urahisi.
Aidha,
alisema Serikali imewekeza katika mifumo ya TEHAMA itakayomwezesha mwananchi
kutumia kadi maalumu kulipia nauli bila kulazimika kupanga foleni, jambo
litakaloongeza ufanisi na kupunguza usumbufu.
Katika
hatua nyingine, aliwahakikishia wananchi kuwa mabasi yote yaliyoharibika
yatafanyiwa ukarabati na kurejea barabarani ili kuimarisha upatikanaji wa
huduma.
Kwa
upande wake, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka Bw. Said Tunda
alisema lengo kuu ni kurejesha furaha kwa wananchi wa Dar es Salaam kwa
kuwapatia usafiri wa uhakika.
Pia aliwataka waendesha daladala kuendelea kutoa huduma huku Serikali ikiendelea kufanya mazungumzo nao ili kupata utaratibu bora wa ushirikiano, hususan kwa zile zilizopewa kibali cha kutumia barabara ya mwendokasi.
Hatua hizo zinaonesha dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita ya inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuboresha maisha ya wananchi kupitia miundombinu imara na huduma bora za kijamii.
Tuesday, February 17, 2026
SERIKALI YAENDELEZA JITIHADA KUHAKIKISHA WENYE ULEMAVU HAWAACHWI NYUMA KATIKA MAENDELEO YA TAIFA.
Naibu
Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. Ummy
Nderiananga amebainisha jitihada mbalimbali zinazofanywa na Serikali
ikiwemo ukamilishwaji wa Mfumo tambuzi
wa Kielektroniki wa taarifa za Watu wenye Ulemavu (PD-MIS).
Pamoja
na mahitaji ya msingi ya Wenye Ulemavu yanayoendelea kutolewa, Serikali pia
imeweka vipaumbele kwa Wenye Ulemavu katika ajira, elimu, afya sambamba na
Mpango wa kunusuru Kaya Masikini (TASAF) ambao unajumuisha Kaya za Wenye
Ulemavu kama kigezo kimojawapo.
Naibu
Waziri amebainisha hayo kwenye kikao na wajumbe wa Shirika lisilo la
Kiserikali Patronage Center for Persons
with Disability (PPD), kilichofanyika leo katika ukumbi mdogo wa Waziri Mkuu
Ngome Jijini Dodoma.
Saturday, February 14, 2026
SERIKALI YAPELEKA TABASAMU KWA WANAWAKE,VIJANA NA WENYE ULEMAVU MTWARA
Serikali
kupitia Ofisi ya Halmashauri ya Mtwara
Mikindani imekabidhi vifaa saidizi na kiasi cha shilingi milioni 342 ikiwa ni
jitihada ya kujikita katika utoaji wa mikopo isiyo na riba kwa vikundi vya
wanawake, vijana na watu wenye Ulemavu.
Akizungumza
katika hafla hiyo iliyofanyika Mkoani Mtwara, Mkindani leo Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera,
Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Mhe. Ummy Nderiananga, amesema hatua hiyo ni
utekelezaji wa sera na mwelekeo wa maendeleo unaolenga kujenga uchumi jumuishi
unaowawezesha wananchi wote kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji
na maendeleo ya Taifa.
Naibu
Waziri Ummy amefafanua, “Mikopo hii inalenga kuchochea na kuinua uchumi wa
chini kwenda juu sambamba na mwelekeo wa dira ya Taifa ya kujenga uchumi
shindani, jumuishi na endelevu ifikapo mwaka 2050.”
Ameongeza
kuwa, utoaji wa vifaa saidizi ikiwemo viti mwendo, magongo, fimbo nyeupe za
wasioona pamoja na taulo za kike, ni utekelezaji wa sera ya kutomwacha mtu
nyuma katika safari ya maendeleo, sambamba na maono ya kitaifa ya kujenga jamii
yenye heshima, utu na usawa wa fursa.
Kwa
upande wake Mbunge wa jimbo la Mtwara Mjini na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais
Maendeleo ya Vijana Mhe. Dkt. Joel Arthur Nanauka, ameweka wazi kuwa Serikali
katika jitahada za kuwakwamua wananchi kiuchumi itaendelea na utekelezaji wa
kuleta miradi mikubwa ya kimkakati katika Mkoa wa Mtwara ikiwemo kuboresha
Bandari ya Mtwara, ujenzi wa reli, na uboreshaji wa uwanja wa ndege pamoja na
marekebisho ya miundombinu ya Barabara.
Waziri Nanauka amehimiza, “Wanufaika wa mikopo hiyo kutumia fedha kwa malengo yaliyokusudiwa, na kurejesha kwa wakati ili kushirikiana katika kuhakikisha mikopo hiyo inaleta matokeo chanya kwao binafsi na Taifa kwa ujumla.”
Thursday, February 12, 2026
SERIKALI KUENDELEA KUIMARISHA USHIRIKIANO BAINA YA VYUO VYA ELIMU YA JUU, TAASISI ZA UTAFITI KATIKA USIMAMIZI WA MAAFA NCHINI
Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa, imefanya kikao kazi kinacholenga kuimarisha ushirikiano kati ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Taasisi za Elimu ya Juu na Taasisi za Utafiti katika eneo la usimamizi wa maafa leo Mkoani Morogoro.
Akifungua
Kikao hicho Dkt. James Kilabuko Naibu
Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu kwa
niaba ya Dkt. Jim Yonazi Katibu Mkuu wa
Ofisi hiyo amesema;
Lengo
kuu la kikao kazi hicho ni kuandaa Hati ya Makubaliano ya Ushirikiano na Mpango
Kazi wa kuimarisha matumizi ya Sayansi, Teknolojia, Utafiti na Ubunifu katika
usimamizi wa maafa kwa pamoja nchini ili kuweza kuwasaidia wananchi katika
kujiandaa, kuzuia na kukabiliana na maafa pindi yanapotokea.
Aidha
ameeleza kuwa, Serikali inadhamira ya kuimarisha Mfumo wa Taifa wa Usimamizi wa
Maafa kwa kuzingatia mzingo mzima wa menejimenti ya maafa unaojumuisha kuzuia
na kupunguza madhara, kujiandaa, kukabiliana na maafa yanapotokea pamoja na
kurejesha hali baada ya maafa.
Amesema
Mwelekeo huu, umeainishwa wazi katika Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Maafa ya
mwaka 2004, (Toleo la Mwaka 2025) inayosisitiza matumizi ya sayansi, teknolojia
na tafiti katika kufanya maamuzi na utendaji wenye ufanisi.
"Katika
utekelezaji wa sera na sheria, Ofisi ya Waziri Mkuu imeona umuhimu wa
kuimarisha ushirikiano na Vyuo vya Elimu ya Juu na Taasisi za Utafiti nchini,
Ushirikiano huu unalenga kuhakikisha kuwa tafiti, mafunzo na teknolojia
zinajibu changamoto zinazokabili taifa letu" amesema Dkt. Kilabuko
Pamoja
na hayo, Dkt. Kilabuko amesisitiza uunganishaji wa nguvu, maarifa na rasilimali
tulizonazo, utajenga Taifa lenye
ustahimilivu dhidi ya maafa na lenye uwezo wa kufikia malengo ya maendeleo
yaliyoainishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Awali
Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu Brigedia
Jenerali Hosea Ndagala alisema, kikao
hiki kinatoa fursa ya kujenga uelewa wa pamoja kati ya wahadhiri, wataalam wa
kitaaluma na watendaji wa Serikali kuhusu mahitaji halisi ya shughuli za
usimamizi wa maafa katika ngazi ya kitaifa, mkoa hadi wilaya kwa lengo la
kuongeza ufanisi wa majibu wakati wa maafa na kuboresha mikakati ya kurejesha
hali baada ya maafa.
Wednesday, February 11, 2026
SERIKALI YAHIMIZA USHIRIKISHWAJI JAMII YA WATU WASIOONA KATIKA SHUGHULI ZA KIJAMII, KIUCHUMI NA KIUTAMADUNI ILI KUONGEZA TIJA.
Serikali
inatambua Breli si mfumo pekee wa kusoma, bali ni nyenzo ya kufungua milango ya
elimu, ujuzi, ukarimu wa jamii, na ushiriki kamili wa kijamii.
Kauli
hiyo imetolewa na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na
Wenye Ulemavu (SBUU) Mhe. Ummy Nderiananga kwa niaba ya Waziri wa Nchi wa Ofisi
hiyo Mhe. William Lukuvi leo Jijini Dodoma huku akieleza kuwa Mfumo huo
umebadilisha maisha ya mamilioni ya wasioona na wenye uoni hafifu duniani kote
ikiwemo Tanzania.
“Kwa
kutambua mchango wa Jamii ya Wasioona katika maendeleo ya taifa letu, Serikali
imeendelea kufanya jitihada mbalimbali zinazolenga kuwawezesha wasioona
kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo, miongoni mwa jitihada hizo
ni pamoja na utekelezaji wa Sera, Sheria, Mikakati na Mipango inayojumuisha
huduma na teknolojia ya breli pamoja na kuimarisha elimu jumuishi kwa kuanzisha
na kuendeleza shule na vituo maalum kwa wanafunzi wasioona, pamoja na kusambaza
vifaa vya kufundishia na kujifunzia vya Breli, vitabu maalum na teknolojia
saidizi” amefafanua Mhe. Waziri.
Aidha,
Serikali imetenga madirisha maalum ya huduma kwa watu wenye ulemavu katika
vituo vya kutolea huduma za afya, pamoja na kuboresha upatikanaji wa huduma za
uchunguzi, tiba na utengamao kwa watu wenye ulemavu wakiwemo wasioona.
Vilevile,
Serikali imeendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo katika kubuni na
kutekeleza miradi ya uwezeshaji wananchi kiuchumi, mafunzo ya ujuzi na ajira
kwa watu wasioona.
“Tunapoadhimisha
kilele cha Siku ya Kimataifa ya Breli Duniani nitoe wito kwa kila mwananchi,
taasisi za umma na binafsi, mashirika ya kiraia pamoja na wadau wa maendeleo
kushirikiana kwa pamoja katika kuimarisha mazingira jumuishi, kuondoa vikwazo
vya kijamii na kimazingira, na kuweka mifumo wezeshi itakayohakikisha Ustawi na
Maendeleo ya jamii ya wasioona yanatimizwa kikamilifu. Kwa kufanya hivyo, Taifa
letu litaendelea kujenga jamii yenye usawa, haki na mshikamano, inayothamini
mchango wa kila mmoja bila ubaguzi” ameomgeza Mhe. Nderiananga
Maadhimisho
ya Siku ya Kimataifa ya Breli huadhimishwa tarehe 12 Februari ya kila mwaka kwa
lengo la kutoa nafasi kwa mataifa yote kutafakari kuhusu mchango na nafasi ya
teknolojia ya Breli katika kuwawezesha watu wasioona kushiriki kikamilifu
katika elimu, ujuzi na maendeleo ya taifa. Kaulimbiu ya mwaka huu inasema
“Teknolojia ya Breli Husaidia Kuchochea Maendeleo kwa Wasioona na Ujenzi wa
Taifa” na kwa Tanzania maadhimisho hayo yatafanyika katika Halmashauri zote na
kwa ngazi ya Kitaifa yatafanyika mkoani Tanga.
Breli
ni mfumo ulioasisiwa na ndugu Louis Braille, ambaye alibuni njia ya maandishi
inayowawezesha watu wasioona kusoma, kuandika na kupata elimu na habari kwa
usawa na wale wanaoona. Mfumo huu unawapa watumiaji wa Breli fursa sawa za
kushiriki katika maendeleo ya kijamii, kiuchumi, na kifikra. Tanzania inaungana
na nchi nyingine duniani katika kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Breli.
MITANDAO YA KIJAMII
Popular Posts
-
Na. OWM, Dodoma. Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu, imefanya ukaguzi wa utekelezaji wa sheria Na.5 y...
-
Wataalamu wa Afya moja wakiwa katikapicha ya pamoja wakati wa mkutano wa wataalamu wa Afya moja uliojikita katika ulinzi na usalama...
-
Na. OWM, ARUSHA Wataalam wa sheria kutoka katika sekta ya Afya ya binadamu, Afya ya wanyamapori na mifugo pamoja na mazingira wameshauri...
-
Washiriki wa Mkutano wa mwaka wa Wataalamu wa Maabara wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa mkutano wa mwaka kwa wataalam wa maabara w...
-
TAMOBA wafanya wasilisho la mfumo maalum wa kielektroniki wa ulinzi na usalama wa Bodaboda na BajajiKampuni ya Tanzania Motorcycle and Bajaj Association (TAMOBA) imefanya wasilisho maaluum kwa Ofisi ya Waziri Mkuu kuhusu mfumo maalum wa ...
-
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, ajira na Watu wenye Ulemavu), Mhe. Jenista Mhagama, ambaye ndiye anayesimamia Kamati ina...
-
*Aagiza fedha zilizotengwa zikatumike katika kujengea hospitali Dodoma Rais Dkt. John Pombe Magufuli ameahirisha maadhimisho ya sik...
-
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji) Mhe. Angellah Kairuki akipokea maelezo ya namna mashine zinavyochakata mifuko chakavu na ...
-
Katika kuhakikisha malengo ya kutatua masuala ya ajira na kazi, yanafikiwa na Serikali ya Awamu ya Sita inayongozwa na Mhe. Samia Suluhu H...
-
Katibu wa Kikosi kazi cha Kitaifa cha kuratibu Mpango wa Serikali kuhamia Dodoma Bw.Meshach Bandawe akiuliza jambo kwa Kaimu Meneja wa Uwa...


.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)













.jpeg)




.jpeg)
.jpeg)
