Tuesday, September 8, 2026

AFDP YAWA CHACHU YA MAENDELEO YA WANANCHI KIPUMBWI.

Wananchi wa Kata ya Kipumbwi Wilaya ya Pangani, Mkoa wa Tanga, wameeleza kunufaika na Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) inayotekelezwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Maendeleo ya Kilimo (IFAD) chini ya uratibu wa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu.

Hayo yameelezwa na wawakilishi wa wavuvi, wachakataji na wafanyabiasha wa mazao ya uvuvi kutoka Kata ya Kipumbwi wakati wa ziara kutathmini utekelezaji wa Programu hiyo katika mapitio ya utekelezaji wa kipindi cha kati (MTR) inayofanywa na Timu ya IFAD.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Katibu wa Umoja wa Wachakata Dagaa Kipumbwi (UWADAKI), Bw. Abdallah Mohamed, amesema AFDP imelenga kuboresha maisha ya wananchi kwa kuongeza kipato, kuongeza uzalishaji wa mazao ya uvuvi, kupunguza upotevu wa mazao ya uvuvi baada ya kuvunwa, kuimarisha matumizi endelevu ya rasilimali za uvuvi, kuimarisha lishe na masuala ya jinsia.

Amesema kupitia Programu hiyo, makundi mbalimbali yamenufaika, yakiwemo Vikundi vya Usimamizi Shirikishi wa Rasilimali za Uvuvi (BMU), Vyama vya Wavuvi, wachakataji na wafanyabiashara wadogo wa mazao ya uvuvi.

Ameongeza kuwa, Programu hiyo imewezesha ujenzi wa miundombinu mbalimbali inayolenga kuboresha shughuli za uvuvi na biashara ya mazao ya uvuvi, ikiwemo ujenzi wa soko la samaki la kimataifa, vichanja vya kukaushia dagaa, mtambo wa kuzalisha barafu na chumba cha ubaridi.

Miundombinu hiyo inatarajiwa kupunguza upotevu wa mazao ya uvuvi baada ya kuvunwa, kuboresha mazingira ya biashara, kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi na kuongeza upatikanaji wa masoko, kuongeza usalama wa chakula na lishe na fursa za ajira.

Aidha, Bw. Mohamed amesema AFDP imewamepatiwa mafunzo mbalimbali, ikiwemo mafunzo ya elimu ya fedha na ujasiriamali yaliyolenga kuwezesha wavuvi, wachakataji na wafanyabiashara wadogo wa mazao ya uvuvi kuanzisha na kuendesha biashara zenye mafanikio, usimamizi bora wa fedha hususan mapato na matumizi. 

Mafunzo ya lishe yaliyolenga kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa lishe bora, hususan kwa watoto na makundi mbalimbali kulingana na umri, pamoja na uhusiano uliopo kati ya lishe bora, afya na uwezo wa kufanya kazi. 

Pia, mafunzo ya jinsia yamelenga kuongeza ushiriki wa wanawake na vijana katika shughuli za kiuchumi, maamuzi ya familia na vikundi, pamoja na kuwezesha usawa wa fursa katika uzalishaji, biashara na matumizi ya mapato.

Vilevile, AFDP inalenga kuchochea uvuvi endelevu unaozingatia mabadiliko ya tabia ya nchi na kuongeza upatikanaji wa samaki, hatua inayotarajiwa kuongeza kipato kwa wananchi katika ngazi ya jamii na Wilaya ya Pangani kwa ujumla. 

 Katika ziara hiyo, wataalamu waliendelea kuhamasisha ushirikishwaji wa makundi yote katika jamii kwa usawa, kuimarisha ushirikiano baina ya wadau wa mazao ya uvuvi na kuweka mifumo na mipango madhubuti itakayosaidia katika uendeshaji endelevu wa soko hilo la kimataifa la samaki, ili liweze kutoa mchango mkubwa katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa Kipumbwi, Pangani na Taifa kwa ujumla.

 

Read More

Sunday, September 6, 2026

RAIS DKT. SAMIA KUZINDUA MIRADI KATIKA MJI WA SERIKALI MTUMBA, DODOMA


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuzindua majengo ya Ofisi za Wizara, Taasisi za Serikali pamoja na barabara za lami zenye urefu wa kilomita 57.1 katika Mji wa Serikali Mtumba,Jijini Dodoma.

Uzinduzi huo unatarajiwa kufanyika jumanne Septemba  nane mwaka huu  katika Uwanja wa Mashujaa uliopo ndani ya Mji wa Serikali Mtumba.

Hayo yamebainishwa Jijini Dodoma leo  na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe.Profesa Palamagamba Kabudi, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maandalizi ya hafla hiyo.

Alisema uzinduzi huo utahusisha maeneo matatu makuu ambayo ni majengo ya Ofisi za Wizara 26, Taasisi 11 za Serikali na barabara za lami zenye urefu wa kilomita 57.1.

Profesa Kabudi alisema kukamilika kwa majengo hayo, kutawezesha watumishi 18,510 kutumia ofisi za Mji wa Serikali, Mtumba.

“Ujenzi wa Mji wa Serikali Mtumba ulianza kutekelezwa kwa awamu, ambapo awamu ya kwanza ilihusisha ujenzi wa majengo 23 ya Ofisi za muda.ujenzi wa majengo hayo ulianza Novemba 28 mwaka  2018 na kukamilika Machi 22 mwaka 2019, hatua iliyowezesha baadhi ya watumishi wa Wizara na taasisi kuanza kuhamia.

Aliongeza kuwa :” Awamu ya pili ya ujenzi ilianza Oktoba, 2021, ikiwa inalenga kujenga majengo ya kudumu kwa ajili ya watumishi wote wa Wizara na Taasisi zilizopangwa kuhamia Mtumba.Pia ilihusisha ujenzi wa miundombinu na huduma mbalimbali za kijamii, ikiwemo barabara za lami.

Profesa Kabudi alisema mbali na barabara hizo, miundombinu ya kudumu ya mawasiliano pamoja na Uwanja wa Mashujaa imekamilika na itakuwa sehemu ya miundombinu itakayotumika katika shughuli za Serikali.

Hata hivyo, alisema baadhi ya miradi bado iko katika hatua mbalimbali za utekelezaji, ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya umeme inayopita chini ya ardhi yenye urefu wa kilomita 42.

“Kazi ya ujenzi wa miundombinu ya maji safi na uondoshaji wa maji taka, TEHAMA, ufungaji wa mifumo ya usalama ya CCTV Camera, ujenzi wa kituo cha zimamoto pamoja na utekelezaji wa mpango wa upandaji miti na ustawishaji wa Mji wa Serikali nazo zinafanyika, "alisema.

Alisema Rais Dkt.Samia ameendelea kuweka msisitizo katika kuboresha mazingira hayo, ikiwa ni pamoja na kutoa fedha kwa ajili ya ununuzi wa samani za Wizara na taasisi 26 zinazohamia katika majengo hayo.

Profesa Kabudi alisema hatua hizo zinaendelea kuifanya Mji wa Serikali Mtumba kuwa miongoni mwa alama muhimu za utekelezaji wa dhana ya Dodoma kuwa kitovu cha shughuli za Serikali.

Alisema uwekezaji huo pia unatarajiwa kuongeza fursa za kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa Dodoma na Tanzania kwa ujumla.

Read More

Wednesday, September 2, 2026

SERIKALI YATOA MAELEKEZO 13 KUKABILIANA NA EL-NINO

 


SERIKALI imetoa maelekezo 13 kwa umma, kamati za usimamizi wa maafa, Wizara, Taasisi, Mikoa, Halmashauri na sekta mbalimbali nchini, kwa ajili ya kujiandaa na kukabiliana na madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na mvua za El-Nino.

Imeelekeza maeneo yote hatarishi yatambuliwe mapema, tathmini za vihatarishi zifanyike na hatua stahiki zichukuliwe, ikiwemo kuwahamasisha wananchi kuondoka katika maeneo hatarishi na kwenda maeneo salama.

Maelekezo hayo yametolewa hii leo  na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Profesa Palamagamba Kabudi, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kukabiliana na Madhara ya El-Nino.

Profesa Kabudi amesema Serikali imeelekeza kuhakikisha mvua hizo zinatumika kikamilifu kwa shughuli za uzalishaji, ikiwemo kilimo, ufugaji, uvunaji wa maji na uvuvi.

Aidha, amesisitiza wananchi wanapaswa kuelimishwa na kuhimizwa kuchukua hatua za kupunguza madhara yanayoweza kusababishwa na mvua hizo, ikiwemo kufanya shughuli za kiuchumi na kijamii katika maeneo salama, kuweka akiba ya chakula, kutumia mbinu bora za kilimo na kuchagua mazao pamoja na mbegu bora kwa msimu wa Vuli.

“Kuandaa rasilimali kwa ajili ya kuzuia au kupunguza madhara, kujiandaa na kukabiliana na maafa yatakayotokea na kushirikisha wadau wote wa maafa, wakiwemo wananchi, taasisi na sekta binafsi katika maeneo yao,” amesema.

Ameongeza kuwa: “Serikali imeagiza kuandaliwa na kutekelezwa kwa mipango ya kuzuia milipuko ya magonjwa kwa binadamu, wanyama na mimea.”

Profesa Kabudi amesema Wizara, Taasisi, Mikoa na wadau wengine wanaohusika na miundombinu wanapaswa kufanya ukaguzi wa miundombinu muhimu na kuhakikisha inaimarishwa na kusafishwa, ikiwemo madaraja, makaravati na mitaro.

Amesema hatua hiyo itasaidia kuhakikisha upatikanaji wa huduma muhimu kabla, wakati na baada ya maafa kutokea, zikiwemo huduma za usafirishaji, maji na umeme.

Serikali pia imeagiza kuimarishwa kwa usimamizi wa mazingira, ikiwemo udhibiti wa taka ngumu, usafishaji na uimarishaji wa njia za maji, kingo za mito na mabwawa.

Aidha, imeelekeza kuhakikisha vifaa vya uokoaji, huduma za dharura na mifumo ya mawasiliano vinapatikana na kuwa katika hali ya utayari wakati wote.

Katika hatua nyingine, Serikali imeagiza kubainisha na kutenga maeneo salama yatakayotumika kwa ajili ya makazi ya dharura pindi maafa yatakapotokea.

Kwa upande wa sekta ya utalii, Serikali imeagiza kufanyika kwa ukaguzi na ukarabati wa miundombinu iliyopo katika maeneo ya Hifadhi za Taifa na Hifadhi za Jamii ili kuhakikisha shughuli za utalii zinaendelea wakati wote.

“Wizara, Taasisi, Mikoa na Halmashauri zote zimeagizwa kufuatilia na kuzingatia maelekezo ya kitaalamu pamoja na taarifa za utabiri wa hali ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), ili hatua stahiki za kujiandaa na kukabiliana na madhara ya El-Nino zichukuliwe kwa wakati.”

KUHUSU BILIONI 730

Akizungumzia taarifa iliyosambaa katika mitandao ya kijamii kuhusu makadirio ya matumizi ya Sh. bilioni 730 katika kujiandaa na kukabiliana na El-Niño, Profesa Kabudi amesema taarifa hiyo haikutoa ufafanuzi wa kina kuhusu shughuli zilizoainishwa katika mpango huo.

Amesema Sh. bilioni 730 ni makadirio ya fedha zinazohitajika kutekeleza Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kukabiliana na Madhara ya El-Niño kabla, wakati na baada ya El-Nino kutokea.

“Kwa mujibu wa Mpango, makadirio ya fedha zinazohitajika kutumika katika kutekeleza Mpango huo ni Sh. bilioni 730,” amesema.

Hata hivyo, amesema fedha zilizotengwa katika bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli hizo katika sekta zote ni Sh. bilioni 10

Read More

Sunday, August 30, 2026

WAZIRI KABUDI AMUWAKILISHA RAIS SAMIA MKUTANO WA UA ANGOLA


WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Prof. Palamagamba Kabudi, amesisitiza haja ya nchi za Afrika kuendelea kuitumia kikamilifu mifumo ya kikanda na kibara ya ulinzi na amani ili kuimarisha juhudi za kutatua migogoro na kudumisha utulivu Barani Afrika. 

Prof. Kabudi ameyasema hayo leo Jijini Luanda, Angola, alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano Maalumu wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (UA) unaojadili mifumo ya kuzuia na kutatua migogoro barani humo.

 

Akihutubia mkutano huo kwa niaba ya Mkuu wa Nchi, Waziri Kabudi ameeleza kuwa ufanisi wa utatuzi wa migogoro unategemea kuheshimiwa na kutekelezwa kwa sheria, taratibu na mikataba iliyowekwa na nchi wanachama kupitia vyombo vya kikanda.

 

“Tunahitaji kuendelea kuweka msisitizo kupitia maamuzi yetu ya pamoja ili kuzuia migogoro na kuhakikisha tunapata matokeo chanya na ya kudumu. Tanzania inaunga mkono kikamilifu na inakubaliana na jitihada zote zinazolenga kuimarisha ulinzi, amani na usalama Barani Afrika,” amesema Prof. Kabudi.

 

Tanzania imekuwa mshirika mkuu katika juhudi za diplomasia ya amani na usuluhishi wa migogoro barani Afrika, msimamo unaoendelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.



 

 

Read More

Friday, August 28, 2026

MKATABA WA UJENZI WA MELI TATU ZA UVUVI WA BAHARI KUU WASAINIWA


Serikali kupitia Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) imesaini mkataba wa ujenzi wa meli tatu za uvuvi wa bahari kuu na Kampuni ya Rongcheng Xinyang Ship Industry Limited ya China, ikiwa ni hatua ya kuimarisha na kuongeza tija katika sekta ya uvuvi nchini.

Mkataba huo umesainiwa, Jijini Dar es Salaam kupitia Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) inayofadhiliwa na Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) ambapo Shirika la Uvuvi Tanzania - TAFICO  kuwa na meli mbili Kwa upande wa Tanzania bara na Shirika la Uvuvi Zanzibar -ZAFICO kuwa na meli moja.

Akizungumza wakati wa kushuhudia utiaji saini wa mkataba huo, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Dkt. Bashiru Kakurwa, amesema hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2025 pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, kwa lengo la kuleta mapinduzi katika sekta ya uvuvi.

Dkt. Kakurwa ameishukuru IFAD kwa ufadhili wa ujenzi wa meli hizo kupitia AFDP, huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi katika kufungua fursa zaidi za uvuvi wa bahari kuu na kukuza uchumi wa Taifa.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, amesema Ofisi ya Waziri Mkuu ikiwa Mratibu Mkuu wa AFDP, inatambua utiaji saini wa mkataba huo kuwa hatua muhimu katika utekelezaji wa programu hiyo.

Amesema ujenzi wa meli hizo ni hatua itakayochangia ukuzaji wa uchumi kupitia uvuvi wa bahari kuu, pamoja na kuongeza uwezo wa Tanzania kutumia kikamilifu rasilimali zake za bahari.

Naye Mratibu wa AFDP kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Bw. Salum Mwinjaka, amesema utiaji saini wa mkataba huo ni hatua muhimu katika kuhakikisha malengo ya programu yanafikiwa kwa wakati na utekelezaji wake unakuwa na mafanikio.

Amesema Serikali inalenga kuhakikisha walengwa wa programu pamoja na Taifa kwa ujumla wananufaika na fursa zinazotokana na utekelezaji wa AFDP.

AFDP inalenga kukuza uzalishaji endelevu wa kibiashara unaozingatia mazingira, hususan katika uzalishaji wa mbegu za mazao ya kilimo kama mahindi, alizeti, maharagwe na jamii ya mikunde, pamoja na uvuvi na ufugaji wa viumbe maji.

Programu hiyo pia inalenga kuwawezesha wanawake na kuongeza ushiriki wa vijana katika shughuli za uzalishaji.

AFDP inaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) na kutekelezwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Kilimo pamoja na Wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi Zanzibar kupitia taasisi mbalimbali, ikiwemo TAFICO, ZAFICO, Wakala wa Mbegu (ASA), TARI na TOSCI.

Hatua hiyo ya kusaini mkataba wa ujenzi wa meli tatu inatarajiwa kuongeza uwezo wa Tanzania katika uvuvi wa bahari kuu, kuchochea uwekezaji, kuongeza ajira na mapato, na hatimaye kuimarisha mchango wa sekta ya uvuvi katika uchumi wa Taifa.

Read More

Tuesday, August 18, 2026

DKT. YONAZI AWAKUMBUSHA VIJANA KULINDA AFYA ZAO KATIKA MAPAMBANO DHIDI YA UKIMWI


 Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, Amewaasa vijana kulinda afya zao na kuepuka tabia hatarishi ili kupunguza maambukizi mapya ya VVU, kwa kuzingatia kuwa ni kundi linaloongoza kuwa hatarini zaidi nchini Tanzania.

Dkt. Yonazi ameyasema hayo mwishoni mwa wiki wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa Afua za UKIMWI Wilaya ya Uvinza Mkoa wa Kigoma alipoambatana na Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania, Dkt. Adam Mrisho, timu ya wataalam kutoka Ofisi yake, Wizara ya Afya, TAMISEMI na Ofisi ya Mkoa huo.

Aidha amepata wasaa kutembelea Kituo cha Maarifa Kata ya Kazuramimba mkoani humo kinachotoa huduma za masuala ya VVU na UKIMWI, na kukutana na vijana wanaotekeleza afua za UKIMWI kupitia vikundi vya uzalishaji mali kwa lengo la kujiinua kiuchumi na kujiletea maendeleo yao.

Akiwa katika kituo hicho, Dkt. Yonazi amepokea taarifa kutoka kwa mwenyekiti wa kikundi, Billy Sekibaha, kuhusu shughuli zinazofanywa na kikundi hicho ikiwemo za biashara ndogondogo za kuuza dagaa pamoja na shunguli za ushonaji wa nguo kwa lengo la kujikwamua kiuchumi na kuondokana na dhana ya utegemezi.

Amesisitiza kuwa, kundi la vijana linategemewa na Taifa katika shughuli za uzalishaji mali na kujiletea maendeleo yao na Taifa kwa ujumla hivyo ni vyema vijana wakaendelea kujilinda na kulinda wengine kwa kutambua hali zao na endapo wakagundulika kuwa na maambukizi ya VVU inashauriwa kuanza kutumia dawa mapema.

"Mnafanya kazi nzuri sana, endeleeni kuchangamkia uwepo wa mitandao ya kijamii kutangaza bidhaa zenu ili kuwafikia wateja wengi zaidi na kujitangaza kitaifa na kimataifa," alisisitiza Dkt. Yonazi

Kwa upande wake Mtendaji  wa TACAIDS, Dkt. Adam Mrisho amewapongeza vijana hao kwa kazi nzuri wanazofanya na kusisitiza kuwa Tume itaendelea kuwawezesha vijana kiuchumi na kuwajengea uwezo ili kuendeleza mapambano dhidi ya maambukizi mapya ya VVU na kufikia lengo la kutokomeza UKIMWI ifikapo mwaka 2030.

 

Read More

Monday, August 17, 2026

WAZIRI KABUDI AKAGUA NA KUKABIDHI MIRADI YA IFAD YA KUIMARISHA UZALISHAJI WA MBEGU, NZEGA


 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Prof. Palamagamba Kabudi, leo Agosti 17, 2026, ametembelea, kukagua na kukabidhi miradi inayotekelezwa kupitia Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (Agriculture and Fisheries Development Programme – AFDP) katika Shamba la Mbegu la Wakala wa Mbegu Tanzania (ASA), Kilimi, Wilaya ya Nzega, Mkoa wa Tabora.

Programu hiyo inafadhiliwa na Shirika la Kimataifa la Maendeleo ya Kilimo (IFAD), ikiwa na lengo la kuongeza tija, kuimarisha uzalishaji wa mbegu bora na kuchochea maendeleo ya sekta ya kilimo nchini.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Prof. Kabudi amesema sekta ya kilimo ni mhimili muhimu wa ukuaji wa uchumi wa Tanzania kutokana na mchango wake katika pato la Taifa, usalama wa chakula, ajira na biashara ya nje.

“Programu hii ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi ni muhimu kwa sekta ya kilimo kwa kuwa inalenga kuongeza tija katika sekta ya kilimo ambayo ni mhimili wa maendeleo ya uchumi. Sekta hii inachangia kiasi cha nusu ya pato la Taifa, robo tatu ya bidhaa zinazouzwa nje ya nchi na ni chanzo cha chakula pamoja na kutoa fursa za ajira kwa zaidi ya asilimia 75 ya Watanzania,” amesema Prof. Kabudi.

Aidha, Waziri Kabudi amekabidhi rasmi jengo la ofisi, jengo la karakana na jengo la kukaushia mbegu kwa Wizara ya Kilimo, miradi ambayo imetekelezwa kupitia Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kwa ufadhili wa IFAD.

Kabla ya kukabidhi miradi hiyo, Prof. Kabudi alikagua miradi mbalimbali inayotekelezwa katika Shamba la Mbegu la Kilimi, ikiwemo jengo la karakana, eneo la kukaushia mazao (drying shade), ofisi na ukumbi wa mafunzo pamoja na ujenzi wa nyumba za watumishi.

Vilevile, programu hiyo imewezesha upatikanaji wa zana na vifaa vya kisasa vya kilimo, ikiwemo boom sprayer, disc harrow, matrekta, maize sheller, tiller, vifaa vya karakana pamoja na magari kwa ajili ya usimamizi na usambazaji wa mbegu.

Akihitimisha ziara hiyo, Prof. Kabudi amesisitiza umuhimu wa utekelezaji wa miradi kwa wakati, kwa kuzingatia viwango na ubora uliokusudiwa ili kuhakikisha thamani halisi ya fedha iliyowekezwa (value for money) inapatikana.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuwa na mpango mkakati madhubuti wa utekelezaji ili kuhakikisha malengo ya Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi yanafikiwa ndani ya muda uliopangwa.

Katika ziara hiyo, Waziri Kabudi ameambatana na Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. David Silinde, Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Umwagiliaji na Zana za Kilimo, Mhandisi Athumani Kilundumya, Mkurugenzi wa Sera na Uratibu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Bw. Paul Sangawe, pamoja na Mratibu wa Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Bw. Salimu Mwinjaka. ‎

Read More

“WENYE ULEMAVU CHANGAMKIENI FURSA ZA MIKOPO” NAIBU WAZIRI UMMY


 Naibu  Waziri  Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. Ummy Nderiananga amewataka watu wenye ulemavu kutumia mikopo inayotolewa na Serikali kama fursa ya kujikwamua kiuchumi na kubadili maisha yao, badala ya kuichukulia kama msaada au hisani.

Naibu Waziri aliyasema  hayo katika Ofisi za Mkoa wa Iringa, wakati wa ziara yake ya kutoa elimu kwa watu wenye ulemavu kuhusu fursa mbalimbali zinazopatikana kwa lengo la kuwawezesha kiuchumi na kijamii.

Amesemalisema  Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira wezeshi kwa watu wenye ulemavu kupata mikopo na fursa nyingine za kiuchumi, huku akibainisha kuwa kiasi kikubwa cha fedha tayari kimetolewa kwa wanufaika nchini.

“Hadi sasa watu wenye ulemavu Nchi nzima  wameshakopa shilingi Bilioni 26.8 hivyo tunapaswa kushukuru na kuipongeza Serikali kwa mikakati mizuri kuhakikisha Kundi hili linafikiwa na sisi kama watu wenye ulemavu tuchangamkie fursa hii ya mikopo tujiinue kiuchumi na tuwe waaminifu kurejesha ili kuwawezesha na wengine,”Alieleza Mhe. Ummy.

Mhe. Ummy Alieleza kwamba  ongezeko hilo ni ishara kuwa watu wenye ulemavu wameanza kutambua na kutumia fursa zinazotolewa kwa ajili ya kuanzisha na kuendeleza shughuli za kiuchumi, hivyo kuwataka kuendelea kujitokeza na kutumia fursa hizo .

"Mafanikio ya baadhi ya watu wenye ulemavu waliopata mikopo yanapaswa kutumika kama mfano na kuwahamasisha  wengine kuchangamkia fursa hii ya mikopo kwani wapo wenye ulemavu wengi wamenufaika hatimaye kupungua wimbi la utegemezi katika familia hata Taifa," Alisisitiza.

Aidha Waziri Ummy aliitaka  Halmashauri ya Manispaa ya Iringa kujitathmini katika utoaji wa mikopo kwa watu wenye ulemavu akibainisha kuwa kiwango kilichotolewa katika manispaa hiyo bado ni kidogo ikilinganishwa na mahitaji yaliyopo huku akiwapongeza watu wenye ulemavu wanaofanya shughuli zao kama vile kiwanda cha kufyatua matofali Kata ya Nduli, duka la jumla la mahitaji ya nyumbani, mnufaika wa mikopo aliyenunua bajaji ya biashara na wafanyabiashara wadogo katika Halmashauri ya Manispaa ya Iringa.

“Serikali za mitaa zinapaswa kuhakikisha fursa za mikopo zinawafikia walengwa, huku wakitenga pia maeneo maalumu ambayo watu wenye ulemavu watafanya  shughuli za uzalishaji na biashara zao bila kusumbuliwa,” Alibainisha.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Mhe. Benjamini Sitta alisema Serikali imefanya jitihada kubwa kuhakikisha inatatua changamoto ya mikopo kwa wenye ulemavu kutoka utaratibu wa kukopa kwa vikundi wa awali  hadi mtu mmoja mmoja.

Awali akitoa taarifa ya Halmashauri ya Manispaa ya Iringa ya Utoaji wa mikopo kwa vijana, wanawake na wenye ulemavu  kwa kipindi cha mwaka 2024/2025 hadi 2025/2026, Afisa Maendeleo ya Jamii ambaye ni Mratibu wa mikopo Bi. Sunday Mtamakaya alieleza kuwa vikundi 183 vimepatiwa mikopo wakiwemo wanawake, vijana na wenye ulemavu.

“Halmashauri imefanikiwa kuwawezesha wenye ulemavu mitaji, wana vikundi kuboresha hali za maisha yao na baadhi ya wanavikundi kuwaajiri watu wengine katika biashara zao. Licha ya mafanikio hayo bada ya kurejeshwa utaratibu wa mikopo bado kuna changamoto ya baadhi yao kushindwa kuejesha mikopo hiyo kwa uaminifu,” Alisema Afisa Maendeleo huyo.

Naye  Mnufaika wa mikopo hiyo mwenye ualbino  Bwa. Issa Iddi Sogoi ambaye anamiliki duka la jumla la mahitaji ya nyumbani  katika Halmashauri hiyo alimshukuru Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyoonyesha upendo, kujali na kuwaunga mkono watu wenye ulemavu kupitia mikopo hatua inayomsaidia kumudu mahitaji ya familia na kujiongezea kipato ambapo pia ametoa ajira kwa vijana wengine.

 

Read More

DKT. YONAZI AVIASA VIKUNDI VYA WAVIU KUTUMIA MITANDAO YA KIJAMII KUWAFIKIA WATEJA


 Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi  ashauri kikundi cha Paza Sauti cha Watu Wanaoishi na Maambukizi ya Virusi vya UKIMWI (WAVIU) kutumia mitandao ya kijamii kutangaza na kuuza bidhaa zao ili kuweza kufikia wateja wengi zaidi huku akiwapongeza kwa juhudi na umoja wao katika shughuli zao za uzalishaji.

Ametoa ushauri huo alipotembelea kikundi cha Paza Sauti cha wajasiliamali wanaoishi na VVU katika ziara yake ya ufatiliaji utekelezaji wa afua za VVU na UKIMWI katika Wilaya ya Nyamagana, Jijini Mwanza.

“Nikiingia kwenye simu yangu sioni kikundi cha Paza Sauti msibanwe na soko la machoni nendeni duniani kupitia mitandao ya kijamii, anzisheni akaunti ya Instagram muweze kuwafikia hata watu walipo nchi za nje" alisema Dkt. Yonazi

Vilevile, Dkt. Yonazi alitembelea Kikundi cha Peace and Love kinachojishughulisha na kilimo cha nyanya na matikiti, kinachosimamiwa na Halmashauri ya Jiji la Mwanza kupitia Mradi wa DREAMS, unaoratibiwa na TACAIDS kwa kushirikiana na ICAP, Mradi huo unalenga kuwawezesha wanawake na vijana balehe kiuchumi na kijamii ili kupunguza vishawishi vinavyoweza kupelekea maambukizi mapya kwa kundi hili.

Kwa hatua nyingine Dkt.Yonazi amepongeza Jiji la Mwanza kwa kuweza kufanikiwa kufikia lengo la kitaifa la 95-95-95 kwa kiwango cha juu na kuongeza ushirikiano na wadau wakiwemo viongozi wa dini katika mwitikio wa VVU na UKIMWI nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) Dkt. Adam Mrisho alisisitiza kuwa TACAIDS itaendelea kuwekeza katika uwezeshaji wa vijana kiuchumi kama sehemu ya juhudi za kuwaondoa katika mazingira ya changamoto na vishawishi vinavyoweza kuongeza hatari ya maambukizi mapya ya VVU.

“hongereni kwa juhudi na kazi mnazozifanya, hili ni eneo ambalo Tume tumezingatia sana ili kuwawezesha vijana kujikwamua kiuchumi”alisema

Naye, Katibu wa Baraza la Watu Wanaoishi na Maambukizi ya Virusi vya UKIMWI Wilaya ya Nyamagana Bw. Joseph Kiharate ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu kwa kuwezesha WAVIU kupata dawa katika hospitali zote na kushukuru huduma zinatolewa kwani zinazingatia ubora na weledi kwa kila siku katika juma.

“tunashukuru tunapata dawa katika hospitali zote na huduma zinatolewa siku saba za wiki kupitia nyie afya zetu zinaimarika," alisema Joseph.

 

Read More

Saturday, August 15, 2026

WAZIRI KABUDI, SERIKALI ITAENDELEA KUTHAMINI MCHANGO WA LUKUVI


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu) Mhe. Prof, Palamagamba Kabudi amesema Serikali itaendelea kuheshimu na kuthamini mchango wa kiuongozi uliotolewa na aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu) Marehemu William Lukuvi.

Hayo ameyasema leo wakati wa maadhimisho ya  ibada ya Misa Takatifu ya kumaliza Msiba  iliyofanyika nyumbani kwa Marehemu Idodi Mkoani Iringa na kuhudhuriwa na wananchi na viongozi mbalimbali wa chama na Serikali.

Alisema, “Enzi za uhai wake Waziri Lukuvi alinisaidia kufahamu shughuli mbalimbali za Bunge na serikali na hivyo kupata weledi mzuri mambo mengi kutokana na uzoefu aliyokuwa nao,”

Aidha uwezo wake wa kusimamia nidhamu ipasavyo Bungeni ikiwa ni pamoja na kuimarisha mahusiano kati ya Serikali na Bunge ilimfanya aendelee kuaminiwa katika kazi ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu.

Kwa Upande Mama Germana Lukuvi Mjane wa Marehemu ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mhe, Rais Dkt, Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kushikamana na familia tangu walipopata msiba.

Awali Mbunge wa Isimani Mhe, Emanuela Mtatifikolo alisema Marehemu Lukuvi ataendelea kuishi kwenye mioyo ya wananchi wa Isimani, kwa mageuzi makubwa ya maendeleo aliyoyafanya.

 “Uwakilishi wake kwa wananchi wa Jimbo la isimani na kwa kushirikiana na Serikali aliwezesha Jimbo la Isimani kunufaika na ujenzi wa barabara ya lami uimarishaji wa Huduma za afya na kuendelea kuboresha miundo mbinu ya elimu sambamba na umeme,” alibainisha

Read More