Thursday, July 23, 2026

PROF. KABUDI: TUMEPIGA HATUA UTOAJI HUDUMA ZA AFYA

 


Huduma za afya ya mama na mtoto katika ngazi ya Kata, Wilaya, Mkoa na Taifa zimeendelea kuimarika ikiwa ni pamoja na kuwekeza katika ununuzi wa vifaa tiba na kutoa mafunzo kwa watoa huduma ikiwemo madaktari na wauguzi.

Kauli hiyo imetolewa leo na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi wakati akizindua jengo la mama na mtoto katika Hospitali ya Vijimbweni Kigamboni Jijini Dar es salaam.

 Alisema, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alianza kusimamia jambo hili tangu akiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ndio maana Umoja wa Afrika ulimteua kuwa kinara wa afya ya mama na mtoto katika Bara la Afrika.

 Aidha, Prof. Kabudi, alifafanua “Maendeleo haya katika kipindi cha Miaka 65 ya Uhuru ni hatua kubwa ukilinganisha na kipindi ambacho Baba wa Taifa Hayati Julius Kambarage Nyerere anaichukua nchi kutoka kwa mkoloni, hali ilikuwa na tofauti na sasa, ni lazima tujivunie maendeleo tuliyofikia”.

Awali Mkuu wa wilaya ya Kigamboni Mhe. Mikaya Tumaini Dalmia ameishukuru serikali kwa kuendelea kuimarisha miundombinu ya ya afya akisema awali wananchi wa Kigamboni walikuwa wanafuata huduma katika Hospitali ya wilaya ya Temeke na Mhimbili.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Kigamboni Mhe. Haran Sanga ametoa shukrani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwarahisishia wananchi wa kigamboni kupata huduma karibu na maeneo wanayoishi.

Read More

TNCM YAPITISHA OMBI LA TANZANIA LA FEDHA KUTOKA MFUKO WA DUNIA 2027 HADI 2029


 Kamati ya Kitaifa ya Kuratibu na Kusimamia Fedha za Mfuko wa Dunia nchini Tanzania (Tanzania National Coordinating Mechanism – TNCM), imeidhinisha rasmi Ombi la Tanzania la Ufadhili wa Mzunguko wa Nane wa Mfuko wa Dunia (Global Fund Grant Cycle 8 – GC8) kiasi cha dola za Marekani milioni 538.6 kwa ajili ya kuendeleza mapambano dhidi ya UKIMWI, Kifua Kikuu (TB) na Malaria, pamoja na kuimarisha Mifumo Thabiti na Endelevu ya Afya (RSSH), katika kipindi cha utekelezaji kuanzia Januari 2027 hadi Desemba 2029.

Uidhinishaji huo umefanyika jijini Dar es Salaam katika kikao maalum cha TNCM kilichoongozwa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, ambaye pia ni Mwenyekiti wa TNCM.

Dkt. Yonazi amesema kuwa, mchakato wa maandalizi ya Ombi la GC8 ulianza rasmi tarehe 13 Machi, 2026 na umeendelea kwa zaidi ya miezi minne, ukihusisha mashauriano ya kina, majadiliano ya kitaifa, upangaji wa vipaumbele, uandishi wa andiko, mapitio ya kitaalamu na uhakiki wa nyaraka za maombi.

Aidha, alifafanua kuwa, mchakato huu umejengwa katika msingi wa ushirikishwaji mpana wa wadau, uwazi, uwajibikaji na umiliki wa kitaifa ambapo zaidi ya wadau 270 walishiriki kwa uwakilishi wa makundi mbalimbali, yakiwemo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara, Idara na Taasisi zake; Washirika wa Maendeleo, Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mashirika ya Kimataifa, Asasi za Kiraia, Sekta Binafsi, Mashirika ya Dini, watu wanaoishi na VVU, jamii zilizo katika hatari kubwa ya maambukizi na zilizoathiriwa na magonjwa hayo; pamoja na wataalamu wa sekta ya afya.

Dkt. Yonazi ameeleza kuwa uwekezaji wa Mfuko wa Dunia umeendelea kutoa mchango mkubwa katika juhudi za Serikali za kuboresha afya na ustawi wa Watanzania, na kusema utekelezaji wa GC8 utatoa fursa kwa Nchi kuendela kuzuia maambukizi mapya ya VVU, kuongeza upatikanaji wa dawa za kufubaza makali ya VVU (ARV), kuimarisha kinga, uchunguzi na matibabu ya Malaria, pamoja na kuboresha ugunduzi wa mapema na matibabu ya Kifua Kikuu.

“Kuidhinishwa kwa Ombi hili la Ufadhili ni matokeo ya kazi kubwa na ushirikiano wa wadau wetu ambao wamewekeza muda, utaalamu na rasilimali kuhakikisha kuwa vipaumbele vilivyoainishwa vinazingatia mahitaji ya nchi pamoja na sauti za jamii na makundi yanayoathiriwa na magonjwa hayo”.Alisema Dkt. Yonazi.

Aliongezea kuwa,hatua hiyo ni mafanikio muhimu yanayoonesha dhamira ya Tanzania ya kuendeleza mapambano dhidi ya magonjwa hayo matatu, sambamba na kujenga mfumo wa afya ulio imara, jumuishi na endelevu.

Dkt. Yonazi ameshukuru Sekretarieti ya Mfuko wa Dunia iliyopo Geneva (Global Fund Country Team), wajumbe wa TNCM pamoja na wadau wote walioshiriki katika maandalizi na ukamilishaji wa maombi hayo, amepongeza jitihada zao akisema zimekuwa na mchango muhimu kuwezesha kufikia hatua hii.

Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa TNCM, Bw. Kent Pius, ametoa shukrani maalum kwa Mwenyekiti wa TNCM, Mfuko wa Dunia, wajumbe na wadau wote kwa ushirikiano na uwajibikaji mkubwa katika kuhakikisha kuwa zoezi hili limefanyika kwa ufanisi na ubora uliokusudiwa na kusema kuwa, hatua hii ni matokeo ya dhamira ya dhati na juhudi za pamoja.

“TNCM itaendelea kuratibu ushirikiano kati ya Serikali, jamii, Asasi za Kiraia, Washirika wa Maendeleo, Sekta Binafsi na wadau wa kimataifa katika kuhakikisha uwekezaji wa Mfuko wa Dunia unachangia katika kufikia malengo ya Kitaifa na Kimataifa ya kutokomeza UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria kama vitisho vya afya ya jamii,” alisema Kent.

Read More

Tuesday, July 21, 2026

KAMATI YA KITAIFA YA USIMAMIZI WA MAAFA YAIDHINISHA MPANGO WA DHARURA WA TAIFA WA KUKABILIANA NA MADHARA YA EL NIÑO


 Kamati ya Kitaifa ya Wataalamu ya Usimamizi wa Maafa imeidhinisha Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kukabiliana na Madhara ya El Niño na kuzielekeza Wizara, Idara, Taasisi, Mikoa na Halmashauri kuongeza kasi ya maandalizi ili kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na mvua za El Niño zinazotabiriwa kudumu hadi mwisho wa mwaka 2026.

Akizungumza katika kikao hicho, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, ambaye pia ni Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, ameelekeza kila sekta kutenga rasilimali zitakazowezesha hatua za kuzuia, kujiandaa, kukabili na kurejesha hali katika eneo lake na pia kuandaa mipango ya dharura ya manunuzi. Pia amesisitiza umuhimu wa kutambua mapema maeneo hatarishi, kufanya tathmini za vihatarishi na kuwahamasisha wananchi wanaoishi katika maeneo hayo kuhamia maeneo salama.

Aidha, Dkt. Yonazi ameelekeza wananchi kupewa elimu kuhusu namna ya kupunguza madhara ya mvua hizo kwa kuweka akiba ya chakula, kulima mazao yanayostahimili mvua nyingi na kutumia fursa zitokanazo na mvua katika kilimo, uvunaji wa maji, ufugaji na uvuvi. Vilevile, amezitaka taasisi husika kuandaa mipango ya kuzuia milipuko ya magonjwa kwa binadamu, mifugo na mimea.

Kamati hiyo pia imeagiza ukaguzi na uboreshaji wa miundombinu muhimu ikiwemo barabara, maji na umeme, kuimarisha usimamizi wa mazingira, kuhakikisha vifaa vya uokoaji, huduma za dharura na mifumo ya mawasiliano vinakuwa tayari wakati wote, pamoja na kuhuisha mipango ya utekelezaji katika maeneo hatarishi.

Aidha, Wizara, Taasisi, Mikoa na Halmashauri zimeelekezwa kufuatilia kwa karibu utabiri na maelekezo ya kitaalamu kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ili hatua zote za maandalizi na kukabiliana na athari za El Niño zichukuliwe kwa wakati.

 

Read More

Monday, July 20, 2026

WATENDAJI MANISPAA YA UBUNGO WAPONGEZWA UBUNIFU WA UNUNUZI WA MITAMBO


 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe, Prof. Palamagamba Kabudi amepongeza watendaji wa Manispaa ya Ubungo kwa ubunifu wa ununuzi wa mitambo ya kutengeneza barabara itakayosaidia mageuzi ya uimarishaji wa mtandao wa barabara na kuchochea shughuli za maendeleo na kasi ya ukuaji wa uchumi kwa wananchi.

Prof. Kabudi ameitoa pongezi hizo leo Jijini Dar es Salaam wakati aliposhiriki katika uzinduzi wa mitambo ya malori ya Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo itakayosaidia katika kuboresha miundombinu ya bararaba katika halmashauri hiyo.

“Maamuzi haya si mepesi kufanywa na baraza la madiwani, kwa sababu imelenga kutatua changamoto za barabara zinazotukabili kwa sasa, ni lazima mitambo hii isimamiwe sawasawa ili kuleta tija kwa wananchi na kila mtendaji aone anajukumu la kuilinda mitambo hii” ameeleza Prof. Kabudi

Aidha, Prof. Kabudi amesema, “ubunifu wa namna hii unahitajika sana, kufanywa katika maeneo mengine ili Halmashauri kwa kushirikiana na Wakala wa Barabara Vijijini na Mjini (TARURA) na kwa kutumia nyenzo uwe wa faida kwa wananchi na mambo haya yanawekewa mkazo kwenye dira ya Taifa.”

Awali Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Albert Chalamila amesema malengo ya Mkoa wake ni kutoka kwenye kuwaza mambo madogo na kuwaza mambo makubwa yenye tija kwa taifa.

“Ili kufikia matarajio hayo tumeainisha kwamba maendeleo lazima yawe yanahusu watu, maendeleo yanayoweza kuchangiwa na watu na yawe maendeleo yao wenyewe,” ameeleza Mkuu wa Mkoa.

 Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Mhe. Albert Msando amesema, msukumo wa kununua mitambo hiyo ulitokana na kulenga kukarabati barabara zinazoharibika wakati wa masika na hasa barabara za mtaani ambazo ziko katika utaratibu wa kusajiliwa na Wakala wa Barabara vijijini na Mjini (TARURA).

“Imani yetu kwa ngazi ya wilaya ni kuendelea kuwekeza zaidi kwa kujipanga kununua seti nyingine ya mitambo  ili kusaidia kila jimbo kuwa na mitambo yake ili kupata matokeo mazuri,” alifafanua Mhe. Msando.

Read More

Sunday, July 12, 2026

MKUU WA MKOA WA TANGA ATOA WITO WANANCHI KUTEMBELEA BANDA LA OWM SABASABA

 

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian ametoa wito kwa wananchi kuendelea kujitokeza kupata elimu ya masuala mbalimbali katika Banda Jumuishi la Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi zake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba 2026) yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Ametoa wito huo hii leo (12 Julai, 2026) alipotembelea na kujionea namna ofisi hiyo inavyoendelea kutoa huduma kwa wananchi na kuwasihi waendelee kujitokeza kwa wingi na kupata taarifa na huduma zinazotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na taasisi zake.

Dkt. Batilda amepongeza namna Ofisi ya Waziri Mkuu ilivyojipanga na kuhakikisha inawafikia wananchi kwa utoaji wa huduma bora na kuzingatia viwango huku wakiendelea kutatua changamoto mbalimbali kwa jamii kupitia maonesho hayo.

Aidha amewakumbusha watumishi wa ofisi hiyo kuendelea kuwa na program mbalimbali za elimu kwa umma ili kuifikia jamii kwa ukumbwa wake na kuendelea kutangaza huduma zinazotolewa.

Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam yanaendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere chini ya kaulimbiu isemayo, "Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba ni Fahari ya Tanzania," yakilenga kukuza biashara, uwekezaji na ubunifu, nchini.

 

Read More

Saturday, July 11, 2026

WITO WATOLEWA KUENDELEA KUIMARISHA USHIRIKIANO WA KITAIFA KULINDA AMANI


SERIKALI imewataka Watanzania kuendelea kulinda na kudumisha amani ya nchi kwa kutambua kuwa ndiyo msingi wa maendeleo ya taifa, huku ikisisitiza kuwa jukumu hilo linamhusu kila mwananchi bila kujali dini, kabila au itikadi za kisiasa.

Wito huo umetolewa na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, katika hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, profesa Palamagamba Kabudi, wakati wa Ibada ya Siku Maalumu ya Wanaume (AMO Big Day) iliyofanyika katika Kanisa la Waadventista wa Sabato (SDA), Mwenge, tarehe 11 Julai, 2026 jijini Dar es Salaam.

Dkt. Nchemba alisema ulinzi wa amani unapaswa kupewa kipaumbele na kuwa ajenda namba moja ya kitaifa kwa kuwa ndiyo msingi wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii, unaowezesha wananchi kuishi kwa utulivu, kufanya kazi kwa bidii na kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa taifa.

Alisema kila Mtanzania ana wajibu wa kulinda amani kwa kuheshimu sheria za nchi, kuimarisha mshikamano wa kitaifa na kuepuka vitendo vinavyoweza kuhatarisha usalama na utulivu wa nchi.

“Suala la ulinzi wa amani lipewe kipaumbele na kwa kila mmoja liwe ajenda namba moja ya kitaifa. Watanzania wote tutambue kuwa tunao wajibu wa kulinda amani yetu,” alisema.Aidha, Dkt. Nchemba aliwataka viongozi wa dini kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuhamasisha wananchi kudumisha amani, upendo, mshikamano na maadili mema kupitia mafundisho yao.

Alisema viongozi wa dini wana nafasi muhimu katika kujenga jamii yenye umoja na mshikamano, hivyo wanapaswa kuendelea kuhubiri ujumbe wa amani na kuhimiza wananchi kuepuka vitendo vinavyoweza kuvuruga utulivu wa taifa.

“Viongozi wa dini endeleeni kuhubiri kuhusu umuhimu wa kudumisha amani na upendo miongoni mwa wanajamii. Ninawasihi sana katika hili, shirikianeni na Serikali kuhakikisha nchi yetu inaendelea kuwa na amani na utulivu. Suala la ulinzi wa amani halina mbadala; sote kwa pamoja tuendelee kuweka msisitizo katika kulinda amani ya nchi,” alisema.

Alisema Tanzania imeendelea kujijengea heshima ndani na nje ya nchi kutokana na historia yake ya amani, umoja na mshikamano, hali iliyowezesha kuvutia uwekezaji, kukuza biashara, kuboresha utoaji wa huduma za jamii na kuharakisha maendeleo ya wananchi.

Katika hatua nyingine, Dkt. Nchemba aliwapongeza waumini wa Kanisa la Waadventista wa Sabato (SDA) Mwenge kwa kukamilisha ujenzi wa jengo la kisasa la ibada, akisema ni ushahidi wa imani yao, mshikamano na kujitoa katika kazi ya Mungu.

“Hili ni jambo la kujivunia. Ni alama ya imani yenu thabiti, mshikamano wenu wa kijamii na bidii yenu ya kujitoa kwa kazi ya Mungu,” alisema.

 

Read More

PROF. NAGU ARIDHISHWA NA HUDUMA ZINAZOTOLEWA BANDA JUMUISHI LA OFISI YA WAZIRI MKUU SABASABA

Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Afya katika Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Prof. Tumaini Nagu, ametembelea Banda Jumuishi la Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi zake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba 2026) yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam, na kupongeza ubora wa huduma zinazotolewa kwa wananchi.

Akiwa katika ziara hiyo, Prof. Nagu amepata fursa ya kutembelea sehemu mbalimbali za banda hilo na kupokea maelezo kuhusu huduma na mifumo mbalimbali inayowezesha wananchi kupata taarifa na huduma zinazotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na taasisi zake.

Amesema banda hilo limekuwa jukwaa muhimu la kuwaelimisha wananchi kuhusu utekelezaji wa programu na miradi ya maendeleo inayolenga kuboresha utoaji wa huduma za kijamii, hususan katika sekta ya afya, elimu, utawala bora na maendeleo ya serikali za mitaa.

Prof. Nagu amewapongeza watumishi wanaohudumu katika banda hilo kwa kujituma, kutoa elimu kwa ufasaha na kuhakikisha kila mwananchi anayefika anapata huduma na taarifa sahihi zinazomwezesha kufahamu shughuli zinazotekelezwa na Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu.

Aidha, amewataka kuendelea kutumia maonesho hayo kama fursa ya kusikiliza maoni ya wananchi, kupokea changamoto zao na kutoa ufafanuzi wa kina kuhusu huduma zinazotolewa, ili kuongeza uelewa na kuimarisha uhusiano kati ya Serikali na wananchi.

"Banda Jumuishi la Ofisi ya Waziri Mkuu limeendelea kuvutia maelfu ya wananchi wanaotembelea Maonesho ya Sabasaba, ambapo wamekuwa wakipata elimu na huduma mbalimbali zinazotolewa na Ofisi hii pamoja na taasisi zake kwa lengo la kuboresha ustawi wa wananchi na kuharakisha maendeleo ya Taifa, hivyo wananchi endeleeni kuitumia fursa ya uwepo wa ofisi hii katika maonesho haya," alisema Dkt. Nagu

Aidha,ametumia nafasi hiyo kuipongeza Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE) pamoja na Taasisi nyingine zilizowezesha mafanikio ya maonesho hayo huku akiiasa jamii kuendelea kutembelea banda hilo na kupata elimu.

Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam yanaendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere chini ya kaulimbiu isemayo, "Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba ni Fahari ya Tanzania," yakilenga kukuza biashara, uwekezaji na ubunifu nchini.

Miongoni mwa Taasisi za Ofisi ya Waziri Mkuu zilizoshiriki ni pamoja na PSSSF, WCF, NSSF, OSHA, NEEC, TNBC, CMA, TACAIDS, DCEA,Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, DART, TARURA, Chuo cha Serikali za Mitaa(LGTI) pamoja na Shirika la Masoko Kariakoo.

Read More

Thursday, July 9, 2026

SERIKALI YAAHIDI KUIMARISHA MAPAMBANO DHIDI YA UKIMWI LICHA YA KUPUNGUA KWA MISAADA YA WAHISANI


Serikali imehakikisha kuwa mapambano dhidi ya Virusi vya UKIMWI (VVU) yataendelea kupewa kipaumbele, huku huduma za kinga, matibabu na upatikanaji wa dawa muhimu zikiendelea kutolewa bila kukwama licha ya changamoto zinazotokana na kupungua kwa misaada kutoka kwa wahisani wa maendeleo.

Kauli hiyo imetolewa leo, na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi, alipokutana na Mkurugenzi Mtendaji wa UNAIDS na Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Winnie Byanyima, katika Ofisi ya Waziri Mkuu, jijini Dar es Salaam.

Prof. Kabudi alisema Serikali imeendelea kuwekeza katika sekta ya afya kupitia vyanzo vya ndani vya mapato ili kuhakikisha huduma zote muhimu zinazohusiana na mapambano dhidi ya UKIMWI zinaendelea kutolewa kwa wananchi bila kuathiriwa na mabadiliko ya ufadhili kutoka nje.




Read More

Monday, July 6, 2026

OFISI YA WAZIRI MKUU YAWAWEZESHA WATU WENYE ULEMAVU KUNG'ARA MAONESHO YA SABASABA



Ofisi ya Waziri Mkuu imewezesha watu wenye ulemavu nchini kushiriki katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) kupitia Shirikisho la Vyama vya Watu Wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA).

Ushiriki huo umewawezesha kuonesha bidhaa na huduma wanazotoa pamoja na kufanya biashara katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa jijini Dar es Salaam.

Akitembelea banda la SHIVYAWATA pamoja na banda la Chama cha Wanawake Wafanyabiashara Tanzania (TWCC), Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu  Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe. Ummy Nderiananga, alisema ameridhishwa na kiwango cha ushiriki wa watu wenye ulemavu katika maonesho ya mwaka huu, akibainisha kuwa ushiriki huo umeongeza fursa za kiuchumi na kuwajengea kujiamini tofauti na miaka iliyopita.

Mhe. Nderiananga alisema Serikali imegharimia ushiriki wa watu wenye ulemavu katika maonesho hayo bila wao kubeba gharama yoyote, hatua iliyowapa nafasi ya kutangaza bidhaa zao na kufanya biashara katika mazingira yenye usawa na heshima na  kuhaidi kuwa Serikali itaendelea kuboresha ushiriki huo katika miaka ijayo ili watu wengi zaidi wenye ulemavu wanufaike na fursa hizo.

Aidha, aliipongeza Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE) pamoja na Taasisi nyingine zilizowezesha ushiriki huo, huku akizitaka Mamlaka za Serikali za Mitaa kuendelea kutenga na kutoa mikopo ya asilimia mbili kwa watu wenye ulemavu ili kuwawezesha kukuza shughuli zao za kiuchumi.

"Ni wakati sasa kwa watu wenye ulemavu kuendelea kuonesha uwezo wao katika uzalishaji na biashara. Kupitia maonesho haya tumejionea matokeo chanya ya uwezeshaji wa kiuchumi unaotokana na mikopo na fursa zinazotolewa na Serikali". alisema Mhe. Nderiananga.

Kwa upande wake, mwakilishi wa washiriki hao, Bi. Pili Bilahi, aliishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuwawezesha kushiriki katika maonesho hayo bila kulipia gharama yeyote.

Pia alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuweka mazingira wezeshi yanayowapa watu wenye ulemavu fursa za kiuchumi, ikiwemo kupitia mikopo ya asilimia mbili inayotolewa na halmashauri.

Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam yanaendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere chini ya kaulimbiu isemayo, "Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba ni Fahari ya Tanzania," yakilenga kukuza biashara, uwekezaji na ubunifu nchini.



Read More

Saturday, July 4, 2026

WAZIRI PROF. KABUDI ATEMBELEA MIRADI YA VVU NA UKIMWI MKOA WA MOROGORO INAYORATIBIWA NA TACAIDS.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu. Prof. Palamagamba Kabudi (Mb) amefanya ziara katika Mkoa wa Morogoro ili kuangalia Miradi inayotekelezwa na TACAIDS chini ya Uratibu wa  Ofisi ya Waziri Mkuu-SBUU kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro. 

Katika ziara hiyo, Waziri Prof. Kabudi aliweza kutembelea kituo cha Afya Kingolwira, kiliboreshwa kupitia miradi ya VVU na UKIMWI iliyoratibiwa na TACAIDS kwa kuongezewa jengo la maabara na jengo la kuchomea taka. Kituo hicho ni kati ya vituo 32 nchini ambavyo vilinufaika na miradi ya VVU na UKIMWI iliyoratibiwa na TACAIDS.

Aidha, katika hatua nyingine, Waziri Prof. Kabudi alitembelea mashine zinazotoa huduma za kinga na upimaji wa VVU kwenye maeneo ya vyuo vikuu vya Mzumbe na cha Kilimo SUA vilivyopo mkoani humo. Mashine hizo zinazojulikana kama Digital Vending Machine zimekua zikitoa huduma ya kondomu za kiume na za kike pamoja na Vitepe vya JIPIME. Waziri Prof. Kabudi amewaasa vijana kuendelea kutumia huduma za VVU na UKIMWI kwani serikali ya awamu ya sita inayoongozwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imefanya juhudi kubwa za kuweka mashine hizo katika vyuo hivyo ikiwa ni pamoja na chuo Mipango, CBE, UDOM pamoja na Hombolo jijini Dodoma.

 

Read More

Friday, July 3, 2026

MIAKA 50 YA MAONESHO YA SABASABA WANANCHI WAKARIBISHWA KUPATA ELIMU BANDA LA WAZIRI MKUU

Mkurugenzi wa  Idara ya  Uwezashaji Kiuchumi na Maudhui ya Ndani Bw. Condrad Millinga ametoa wito kwa wananchi kutembelea Banda Jumuishi la Ofisi ya Waziri Mkuu katika maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba kwaajili ya kupata elimu.  

Bw. Millinga ameongeza kuwa banda hilo linajumuisha Taasisi na Idara zote ambazo zipo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu hali itakayowasaidia wananchi kupunguza kutembea sana kutafuta Ofisi mojamoja, wito huo ameutoa ikiwa ni siku ya  Ufunguzi Rasmi wa maonyesho hayo.

Ambapo mgeni rasmi katika siku hii ya ufunguzi atakuwa Rais wa Msumbiji Mhe. Daniel Francisco Chapo, akiwa na Mwenyeji wake Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Read More

Thursday, July 2, 2026

PROF. KABUDI AKABIDHI BAJAJI KWA MKAZI WA MSALATO

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Mhe. Prof. Palamagamba John Kabudi, amemkabidhi bajaji Bw. John Miina Mpumpa, mkazi wa Msalato, Mkoani Dodoma, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuwawezesha watu wenye ulemavu kujitegemea kiuchumi.

 

Makabidhiano hayo yamefanyika leo, , katika Ofisi ya Waziri wa Nchi, Ngome, jijini Dodoma. Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Prof. Kabudi alisema Serikali itaendelea kuweka mbele ustawi wa watu wenye ulemavu kwa kuhakikisha wanapata fursa na mazingira jumuishi yanayowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo.

 

Alieleza kuwa uwezeshaji huo unaakisi dhamira ya Serikali ya kuboresha maisha ya wananchi wenye mahitaji maalum kupitia hatua mbalimbali za kijamii na kiuchumi.

 

Bajaji hiyo ilitolewa na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhe. Dkt. Rhimo S. Nyansaho, kufuatia ombi la msaada lililowasilishwa Serikalini na Bw. Mpumpa.

 

Prof. Kabudi pia alimpongeza Bw. Mpumpa kwa uzalendo wake na mchango alioutoa kwa taifa wakati wa kipindi chake cha utumishi, akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuthamini wananchi walioitumikia nchi kwa uadilifu na kujituma.

 

Kwa upande wake, Bw. Mpumpa aliishukuru Serikali kwa kuendelea kumjali na kumpatia msaada huo, akisema utamwezesha kujipatia kipato na kuboresha maisha yake licha ya changamoto za kiafya anazokabiliana nazo.



Read More

Wednesday, July 1, 2026

DKT.YONAZI: TUTUMIE AFCON KAMA FURSA YA KUJITANGAZA KIMATAIFA

Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Makatibu Wakuu ya Maandalizi ya Michuano ya Kombe la Mataifa Afrika (AFCON 2027),  Dkt. Jim Yonazi, amesema michuano ya AFCON ni fursa adhimu ya kuitangaza Tanzania Kimataifa kupitia sekta mbalimbali ikiwemo ya utalii na uwekezaji hivyo ni jukumu la kila sekta kuhakikisha inachangamkia na kushiriki kikamilifu katika kufanikisha michuano hiyo.


Ameyasema hayo hii leo wakati wa ziara ya Kamati hiyo inayojumuisha Makatibu Wakuu wa kisekta na baadhi ya wakuu wa Taasisi walipotembelea na kukagua maendeleo ya maandalizi kuelekea michuano hiyo ikiwemo kuangalia miundombinu na vituo vya michezo vitakavyotumika katika michuano ya Kombe la Mataifa Afrika (AFCON 2027) ili kufanikisha mashindano hayo makubwa ya soka barani Afrika.


Katika ziara hiyo, Kamati imekagua maendeleo ya maboresho katika Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Uwanja wa Mazoezi wa Shule ya Sheria (Law School Grounds), Uwanja wa Mazoezi wa Leaders Club, Uwanja wa Mazoezi wa Gymkhana (Gymkhana Club), Uwanja wa Mazoezi wa Farasi pamoja na Uwanja wa Taifa wa Benjamin Mkapa ili kujionea utayari wa miundombinu itakayotumika wakati wa mashindano hayo.

Dkt. Yonazi amesema ili kufanikisha AFCON 2027 kila sekta inapaswa kuweka nguvu ya pamoja katika kuelekea kwenye michuano hiyo kwa kuzingatia faida zake ikiwemo ya kukuza uchumi wa jamii na Nchi kwa ujumla  


"AFCON 2027 ni zaidi ya mashindano ya soka; ni jukwaa la kuitangaza Tanzania Duniani hivyo kila taasisi inapaswa kutekeleza wajibu wake ili kuhakikisha nchi inanufaika ipasavyo na fursa hii," amesema Dkt. Yonazi.

Aidha, ameielekeza Bodi ya Utaliii Tanzania (TTB) kuandaa mkakati mahsusi wa kuitangaza Tanzania kupitia mashindano hayo kwa kuonesha vivutio vya utalii, utamaduni na fursa za uwekezaji kwa wageni watakaofika nchini.


Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Maendeelo ya Michezo kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Bw. Boniface Tamba, amesema maboresho ya miundombinu yanaendelea vizuri na kwamba ujenzi wa barabara zinazoingia na kutoka katika vituo pamoja na viwanja vya michezo umefikia hatua za mwisho za ukamilishaji.

"Maandalizi yanaendelea kwa kasi na miundombinu muhimu ipo katika hatua za mwisho ili kuhakikisha Tanzania inakuwa tayari kuandaa AFCON 2027 kwa viwango vinavyotakiwa," amesema Bw. Tamba.


Kamati ya Makatibu Wakuu inaendelea na ziara ya ukaguzi wa miundombinu ya AFCON 2027, ambapo baada ya kukamilisha ukaguzi katika Mkoa wa Dar es Salaam itatembelea Zanzibar kabla ya kuhitimisha ziara hiyo itatembelea katika viwanja vilivyopo  Jijini Arusha.

Read More

Monday, June 29, 2026

OWM NA SKAUTI DODOMA MGUU SAWA USIMAMIZI WA MAAFA

Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu imefanya mafunzo ya usimamizi wa maafa kwa Uongozi wa Skauti Mkoa wa Dodoma.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (SBUU) Brig. Jen Hosea Ndagala, ameipongeza Skauti Tanzania kwa ushirikiano ambao wanaoutoa wakati wote katika kushughulikia matukio mbalimbali ambayo yamekua yakitokea nchini, hivyo mafunzo hayo ni sehemu ya kujiweka sawa juu ya kuimarisha namna bora ya mashirikiano haya.

Brig. Jen Ndagala ameongeza kuwa, Mfumo wa usimamizi wa maafa nchini ni mfumo unaoanzia ngazi ya Taifa hadi Kijiji, hivyo Mfumo huo ukifuatwa utasaidia kupunguza athari za majanga.

"Kama kamati zote katika Mfumo huu zitafanya kazi kama inavyotakiwa hatutegemei kuwa na maafa makubwa, kwani majanga mengine huwezi kuyazuia lakini kuna mambo kadhaa ya kuyazuia, na kuna mengine yakitoea unapunguza maafa kwa binadamu, miundombinu na maswala mengine hususani shughuli za kijamii na uchumi na kulinda maendeleo ambayo nchi imeshayapata ", ameeleza Brig. Jen Ndagala.

Aidha, Brig. Jen Ndagala amewataka washiriki wa mafunzo hayo kutoka skauti Mkoa wa Dodoma kutumia mafunzo hayo na  kuwa Mabalozi ili kuelimisha na  kutahadharisha jamii hatua mahususi za kuchukua tahadhari za mapema, kujikinga au kupunguza madhara ambayo yanaweza kujitokeza ili kuendelea kuhakikisha taifa linakuwa salama na matukio ya Maafa.

Nae, Kamishna wa Skauti Mkoa wa Dodoma Bi. Salama Katunda ametumia Mafunzo hayo kudhihirisha adhma ya skauti ya kuendelea kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura katika kujiandaa, kutoa elimu na kukabiliana na maafa nchini .

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo, Mkurugenzi msaidizi Idara ya Menejimenti ya Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (SBUU) Bi. Jane Kikunya amesema kuwa, mafunzo hayo ni sehemu ya kuimarisha mashirikiano yaliyopo kati ya serikali na wadau mbalimbali katika usimamizi na uratibu wa maafa nchini na kusema Ofisi ya Waziri Mkuu iko tayari kuendeleza mashirikiano hayo.

Read More

Friday, June 26, 2026

UTEKELEZWAJI WA MIPANGO NA MIKAKATI YA KUIMARISHA HAKI NA USTAWI KWA WATU WENYE ULEMAVU WASISITIZWA MWANZA.


Serikali imezitaka Mamlaka za Serikali za Mitaa, watendaji wa sekta mbalimbali pamoja na wadau wa masuala ya Watu wenye Ulemavu kuhakikisha Mpango Kazi wa Taifa wa Haki na Ustawi kwa Watu wenye Ualbino (MTHUWWU) na Mkakati wa Taifa wa Teknolojia Saidizi (NATS) vinatekelezwa kikamilifu ili kuboresha huduma na kulinda haki za Watu wenye Ulemavu nchini.

Wito huo umetolewa Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Dkt. Kheri Kagya akimwakilisha Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza Bw. Balandya Elikana, wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya usambazaji na utoaji wa elimu kuhusu Mpango Kazi wa Taifa wa Haki na Ustawi kwa Watu wenye Ualbino pamoja na Mkakati wa Taifa wa Teknolojia Saidizi kwa watendaji na wadau wenye ulemavu yaliyowakutanisha washiriki kutoka mikoa ya Mwanza, Mara na Geita katika ukumbi wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza.

Katika hotuba yake, Dkt. Kagya ameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu kwa kuendelea kuratibu utekelezaji wa sera na mipango inayolenga kuimarisha ustawi wa watu wenye ulemavu, akibainisha kuwa usambazaji wa nyaraka hizo utasaidia kuongeza uelewa kwa watendaji na viongozi wa SHIVYAWATA ili kuboresha utoaji wa huduma na kutokomeza ubaguzi, unyanyasaji na ukatili dhidi ya watu wenye ualbino.

Aidha, amesema Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kutekeleza hatua mbalimbali za kuboresha maisha ya Watu wenye Ulemavu, ikiwemo kuimarisha huduma za afya, elimu jumuishi, uwezeshaji wa kiuchumi kupitia mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri na asilimia 30 ya zabuni za manunuzi ya umma, pamoja na kuendeleza huduma za teknolojia saidizi.

Ameongeza kuwa, pamoja na umuhimu mkubwa wa teknolojia saidizi katika kuwawezesha watu wenye ulemavu na wazee kujitegemea na kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii na kiuchumi, kiwango cha upatikanaji wa vifaa hivyo bado ni cha chini, hali inayolazimu wadau wote kushirikiana katika utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Teknolojia Saidizi wa mwaka 2024–2027.

Pia, Dkt Kagya amewataka watendaji wa mikoa na halmashauri kutenga bajeti kwa ajili ya ununuzi wa mafuta kinga kwa Watu wenye Ualbino na vifaa saidizi kwa Watu wenye Ulemavu, sambamba na kuhakikisha elimu iliyotolewa katika mafunzo hayo inawafikia watendaji wengine ili kuimarisha utoaji wa huduma jumuishi nchini.

Awali, akimwakilisha Kaimu Mkurugenzi, Afisa Sheria kutoka Kitengo cha Watu wenye Ulemavu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (SBUU) Bw. Jacob Mwinula, amesema usambazwaji na utoaji wa Elimu hiyo umeshafanyika katika mikoa mitano ambayo ni Mwanza, Geita, Mara, Manyara na Kilimanjaro pia amewaomba watendaji wote wa Halmashauri, Mikoa, Sekta mbalimbali na SHIVYAWATA kuhakikisha mikakati na shughuli zote zinazofanyika katika maeneo yao zinajumuisha utekelezaji wa mpango na mkakati huu na kufanya tathimini na ufuatiliaji ili kuimarisha maisha ya Watu wenye Ulemavu kijamii, kisiasa na kiuchumi.

 

Read More

Thursday, June 25, 2026

SERIKALI YAZITAKA TAASISI ZOTE KUJIANDAA KUKABILIANA NA ATHARI ZA EL NIÑO


SERIKALI imesema itaendelea kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini ili kupunguza madhara yanayosababishwa na majanga mbalimbali ambayo yamekuwa yakigharimu maisha ya watu, kuharibu mali na kurudisha nyuma maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Kauli hiyo imetolewa hii leo na Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. James Kilabuko, wakati akifunga Jukwaa la Wadau wa Usimamizi wa Maafa lililojadili Rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kuzuia na Kukabiliana na Madhara ya El Niño Jijini Dodoma.

Amesema Tanzania imeendelea kukabiliwa na matukio ya maafa yanayosababisha athari kubwa kwa wananchi na uchumi wa Taifa, hali inayolazimu kuwepo kwa maandalizi madhubuti ya kukabiliana na changamoto hizo kabla hazijatokea.

“Nchi yetu imekuwa ikishuhudia matukio ya majanga ambayo yamekuwa yakisababisha maafa na kuathiri mfumo wa kawaida wa maisha ya jamii. Majanga hayo yamesababisha vifo, ulemavu wa kudumu, upotevu wa mali na uharibifu wa miundombinu,” amesema Dkt. Kilabuko.

Amesema kufuatia taarifa ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ya Aprili 28, 2026 kuhusu uwezekano wa kujitokeza kwa hali ya El Niño, Ofisi ya Waziri Mkuu imeandaa Rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura kwa ajili ya kuzuia na kukabiliana na madhara yanayoweza kutokea kuanzia Agosti 2026 hadi Juni 2027.

Kwa mujibu wa Dkt. Kilabuko, rasimu hiyo imejadiliwa na wadau mbalimbali ili kuiboresha kwa kuzingatia uzoefu uliopatikana wakati wa matukio ya El Niño yaliyowahi kutokea nchini, hususan ya mwaka 2023/2024.

Amesema ushirikishwaji wa wadau ni hatua muhimu itakayoiwezesha Serikali kuwa na mpango shirikishi na unaotekelezeka katika kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali endapo maafa yatatokea.

“Ni vema kushiriki kikamilifu na kutoa maoni yetu huku tukijielekeza kwenye athari tarajiwa na hatua za kuchukua ili kuwa na mpango thabiti utakaoiwezesha Serikali na wadau kuchukua hatua stahiki za kuzuia au kupunguza madhara,” amesema.

  

Read More

Wednesday, June 24, 2026

SERIKALI YAJIPANGA KUKABILIANA NA ATHARI ZA EL NIÑO

SERIKALI imesema imejipanga kikamilifu kukabiliana na madhara yanayoweza kusababishwa na hali ya El Niño kufuatia tahadhari iliyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA).

Akizungumza hii leo wakati wa ufunguzi wa kikao cha wadau wa usimamizi wa maafa, Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Operesheni na Uratibu kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Kanali Selestine Masalamado, amesema kuwa tayari Serikali imeandaa Rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura ili kuimarisha maandalizi na hatua za kukabiliana na hali hiyo.

Amesema mpango huo unalenga kuhakikisha kunakuwa na uratibu madhubuti, utekelezaji wa hatua za mapema pamoja na kupunguza athari zinazoweza kujitokeza kwa wananchi, mali zao na miundombinu.

“Kikao hiki kinatoa fursa kwa wizara, taasisi, mikoa na wadau wengine kupitia rasimu hii kwa kina na kutoa maoni yatakayosaidia kupatikana kwa mpango shirikishi na unaotekelezeka,” amesema Kanali Masalamado

Ameongeza kuwa Serikali inathamini mchango wa wadau wote katika kuboresha mpango huo ili uwe mwongozo thabiti wa kuzuia, kujiandaa na kukabiliana na madhara ya El Niño.

Aidha, amewataka washiriki kushiriki kikamilifu katika majadiliano na kutoa mapendekezo yenye kujenga yatakayosaidia kulinda maisha ya wananchi na kuhakikisha huduma muhimu zinaendelea kutolewa hata wakati wa majanga.

Katika hatua za maandalizi, amesisitiza umuhimu wa kutoa elimu kwa umma kuhusu tahadhari za kuchukua, ikiwemo kuhama katika maeneo hatarishi na kuendelea na shughuli za kiuchumi katika maeneo salama.

Read More