Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Afya Moja kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu inayoshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Salum Manyatta, amesema kuwa Mpango Mkakati wa Afya Moja umejikita kuhakikisha wananchi wananufaika kuanzia ngazi ya Kaya hadi Taifa kupitia utekelezaji shirikishi wa sekta mbalimbali nchini ili kuhakikisha malengo yake yanafikiwa na kuwa na tija kwa jamii kwa ujumla.
Dkt.
Manyatta ameyasema hayo mkoani Tanga wakati wa kikao kazi cha wataalam cha
kuandaa Mpango wa Mkoa wa Afya Moja kilichoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu
Sehemu ya Afya Moja kwa kushirikiana na Shirika lisilo la Serikali la CIHEB
Tanzania kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani.
Amesema
kuwa lengo kuu la kikao hicho ni kuwajengea uwezo Watalamu ngazi ya mkoa kuhusu
utekelezaji wa Dhana ya Afya Moja na kuwawezesha kutengeneza Mpango wa
Utekelezaji wa Afya Moja wa Mkoa ambacho kitafanyika kwa siku tano kuanzia
tarehe 13 hadi 17 Aprili 2026 katika Halmashauri ya Mji wa Korongwe, Mkoani
Tanga.
Dkt.
Manyatta ameeleza kuwa, lengo la dhana ya Afya Moja ni kupanua na kuimarisha
ushirikiano baina ya sekta/taaluma mbalimbali katika hatua zote za kuzuia,
kujiandaa na kukabiliana na milipuko ya magonjwa na hatari nyingine za afya
zinazohitaji ushiriki wa sekta zaidi ya moja na taaluma mbalimbali.
“Ushirikiano
huu pamoja na wadau wengine ikiwemo jamii, kimsingi unaongozwa na sekta/wizara
za msingi (lead Ministries) ambazo ni Afya ya Binadamu, Wanyama (Mifugo na
Wanyama Pori), Mazingira na Kilimo katika ngazi zote,” alifafanua Dkt.
Manyatta.
Alifafanua
kuwa, uwepo wa Mpango Mkakati ni muhimu kwani unatarajiwa kuweza kujibu na
kutatua changamoto zilizopo katika Mkoa wa Tanga, hivyo utumike kama fursa ya
kuhakikisha mkoa unakuwa na uelewa wa pamoja wa masuala ya Afya Moja kwa
kuunganisha nguvu ya pamoja na kuweza kufanya kazi pamoja kwani hii ndiyo maana
halisi ya dhana ya Afya Moja.
Naye
Mwakilishi wa Katibu Tawala, ambaye ni Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tanga Dkt. Japhet
Simeo amepongeza uratibu wa Ofisi ya Waziri Mkuu kwa namna inavyoendelea kutoa
elimu ya masuala ya Afya Moja, na kueleza kuwa mkoa wa Tanga utanufaika kwa
uwepo wa Mpango Mkakati wa Afya Moja na kusisitiza kuwa Tanga itautekeleza kwa
vitendo na kufanya mkoa huo kuwa wa mfano
“Ifike
mahali tutoke katika mambo ya concept to Action, yaani kuwa na mipango na
mikakati ya namna hii na kuitekeleza na hiyo ndiyo umuhimu wa dhana Afya Moja,”
alisisitiza Dkt. Simeo
Kwa
upande wake, Msimamizi wa Afya Moja na Mratibu wa Mradi wa Usalama wa
Afya Duniani unaotekelezwa na Shirika lisilo la Serikali la CIHEB
Tanzania Dkt. Irene Massawe amesema kuwa, ushirikiano uliopo utasaidia
kufanikisha malengo yaliyopo kwa nguvu ya pamoja na kuhakikisha matarajio ya
uwepo wa mpango huo yanafika hadi ngazi za chini.
Aliongezea
kuwa, sekta husika zikiungana kwa pamoja katika kutekeleza dhana ya Afya Moja
itasaidia kudhibiti vihatarishi vya afya ikiwemo magonjwa ya mlipuko hasa yale
yanayoweza kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu, yakiwemo ya kimeta, kichaa
cha mbwa kwani itarahisisha na kuleta ufanisi katika kukabiliana na changamoto
hizo.
“Tunaamini
kuwepo kwetu ndani ya siku tano hizi Korogwe kutazaa matunda kwa washiriki wote
kisha kuyaleta haya katika utekelezaji wa kila siku na kuhakikisha tunaleta
matokeo chanya ya mipango hii,” alisema Dkt. Irene.
AWALI
Afya
Moja ni Dhana ya Kimataifa iliyoridhiwa na Shirika la Afya Duniani (WHO),
shirika linaloshughulika na Afya ya Wanyama (OIE), Shirika la Chakula na Kilimo
la Umoja wa Mataifa (FAO), Programu ya Kimataifa ya Mazingira (UNEP) kupitia
“Global Health Security Agenda” (GHSA) na wadau wengine wa Afya duniani kote.
Shirika la Afya Duniani (WHO), Shirika linaloshughulika na Afya ya Wanyama
(OIE) na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) yamekuwa
yakishirikiana duniani kote na kutoa wito kwa wataalamu wa sekta za Afya ya
Binadamu, Wanyama na Mazingira kuongeza na kuimarisha ushirikiano na
mawasiliano ili kuboresha ufanisi katika kukabiliana na tishio la magonjwa ya
kuambukiza yanayoenea kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu na yanayovuka
mipaka; tatizo la usugu wa vimelea vya magonjwa na changamoto zingine
zinazokabili afya ya jamii zinazohitaji nguvu ya pamoja.

.jpeg)
.jpeg)





.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)











