Wananchi wa Kata ya Kipumbwi Wilaya ya Pangani, Mkoa wa Tanga, wameeleza kunufaika na Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) inayotekelezwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Maendeleo ya Kilimo (IFAD) chini ya uratibu wa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu.
Hayo yameelezwa na wawakilishi wa wavuvi, wachakataji na wafanyabiasha wa mazao ya uvuvi kutoka Kata ya Kipumbwi wakati wa ziara kutathmini utekelezaji wa Programu hiyo katika mapitio ya utekelezaji wa kipindi cha kati (MTR) inayofanywa na Timu ya IFAD.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Katibu wa Umoja wa Wachakata Dagaa Kipumbwi (UWADAKI), Bw. Abdallah Mohamed, amesema AFDP imelenga kuboresha maisha ya wananchi kwa kuongeza kipato, kuongeza uzalishaji wa mazao ya uvuvi, kupunguza upotevu wa mazao ya uvuvi baada ya kuvunwa, kuimarisha matumizi endelevu ya rasilimali za uvuvi, kuimarisha lishe na masuala ya jinsia.
Amesema kupitia Programu hiyo, makundi mbalimbali yamenufaika, yakiwemo Vikundi vya Usimamizi Shirikishi wa Rasilimali za Uvuvi (BMU), Vyama vya Wavuvi, wachakataji na wafanyabiashara wadogo wa mazao ya uvuvi.
Ameongeza kuwa, Programu hiyo imewezesha ujenzi wa miundombinu mbalimbali inayolenga kuboresha shughuli za uvuvi na biashara ya mazao ya uvuvi, ikiwemo ujenzi wa soko la samaki la kimataifa, vichanja vya kukaushia dagaa, mtambo wa kuzalisha barafu na chumba cha ubaridi.
Miundombinu hiyo inatarajiwa kupunguza upotevu wa mazao ya uvuvi baada ya kuvunwa, kuboresha mazingira ya biashara, kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi na kuongeza upatikanaji wa masoko, kuongeza usalama wa chakula na lishe na fursa za ajira.
Aidha, Bw. Mohamed amesema AFDP imewamepatiwa mafunzo mbalimbali, ikiwemo mafunzo ya elimu ya fedha na ujasiriamali yaliyolenga kuwezesha wavuvi, wachakataji na wafanyabiashara wadogo wa mazao ya uvuvi kuanzisha na kuendesha biashara zenye mafanikio, usimamizi bora wa fedha hususan mapato na matumizi.
Mafunzo ya lishe yaliyolenga kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa lishe bora, hususan kwa watoto na makundi mbalimbali kulingana na umri, pamoja na uhusiano uliopo kati ya lishe bora, afya na uwezo wa kufanya kazi.
Pia, mafunzo ya jinsia yamelenga kuongeza ushiriki wa wanawake na vijana katika shughuli za kiuchumi, maamuzi ya familia na vikundi, pamoja na kuwezesha usawa wa fursa katika uzalishaji, biashara na matumizi ya mapato.
Vilevile, AFDP inalenga kuchochea uvuvi endelevu unaozingatia mabadiliko ya tabia ya nchi na kuongeza upatikanaji wa samaki, hatua inayotarajiwa kuongeza kipato kwa wananchi katika ngazi ya jamii na Wilaya ya Pangani kwa ujumla.
Katika ziara hiyo, wataalamu waliendelea kuhamasisha ushirikishwaji wa makundi yote katika jamii kwa usawa, kuimarisha ushirikiano baina ya wadau wa mazao ya uvuvi na kuweka mifumo na mipango madhubuti itakayosaidia katika uendeshaji endelevu wa soko hilo la kimataifa la samaki, ili liweze kutoa mchango mkubwa katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa Kipumbwi, Pangani na Taifa kwa ujumla.


.jpg)