Sunday, August 30, 2026

WAZIRI KABUDI AMUWAKILISHA RAIS SAMIA MKUTANO WA UA ANGOLA


WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Prof. Palamagamba Kabudi, amesisitiza haja ya nchi za Afrika kuendelea kuitumia kikamilifu mifumo ya kikanda na kibara ya ulinzi na amani ili kuimarisha juhudi za kutatua migogoro na kudumisha utulivu Barani Afrika. 

Prof. Kabudi ameyasema hayo leo Jijini Luanda, Angola, alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano Maalumu wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (UA) unaojadili mifumo ya kuzuia na kutatua migogoro barani humo.

 

Akihutubia mkutano huo kwa niaba ya Mkuu wa Nchi, Waziri Kabudi ameeleza kuwa ufanisi wa utatuzi wa migogoro unategemea kuheshimiwa na kutekelezwa kwa sheria, taratibu na mikataba iliyowekwa na nchi wanachama kupitia vyombo vya kikanda.

 

“Tunahitaji kuendelea kuweka msisitizo kupitia maamuzi yetu ya pamoja ili kuzuia migogoro na kuhakikisha tunapata matokeo chanya na ya kudumu. Tanzania inaunga mkono kikamilifu na inakubaliana na jitihada zote zinazolenga kuimarisha ulinzi, amani na usalama Barani Afrika,” amesema Prof. Kabudi.

 

Tanzania imekuwa mshirika mkuu katika juhudi za diplomasia ya amani na usuluhishi wa migogoro barani Afrika, msimamo unaoendelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.



 

 

Read More

Friday, August 28, 2026

MKATABA WA UJENZI WA MELI TATU ZA UVUVI WA BAHARI KUU WASAINIWA


Serikali kupitia Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) imesaini mkataba wa ujenzi wa meli tatu za uvuvi wa bahari kuu na Kampuni ya Rongcheng Xinyang Ship Industry Limited ya China, ikiwa ni hatua ya kuimarisha na kuongeza tija katika sekta ya uvuvi nchini.

Mkataba huo umesainiwa, Jijini Dar es Salaam kupitia Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) inayofadhiliwa na Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) ambapo Shirika la Uvuvi Tanzania - TAFICO  kuwa na meli mbili Kwa upande wa Tanzania bara na Shirika la Uvuvi Zanzibar -ZAFICO kuwa na meli moja.

Akizungumza wakati wa kushuhudia utiaji saini wa mkataba huo, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Dkt. Bashiru Kakurwa, amesema hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2025 pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, kwa lengo la kuleta mapinduzi katika sekta ya uvuvi.

Dkt. Kakurwa ameishukuru IFAD kwa ufadhili wa ujenzi wa meli hizo kupitia AFDP, huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi katika kufungua fursa zaidi za uvuvi wa bahari kuu na kukuza uchumi wa Taifa.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, amesema Ofisi ya Waziri Mkuu ikiwa Mratibu Mkuu wa AFDP, inatambua utiaji saini wa mkataba huo kuwa hatua muhimu katika utekelezaji wa programu hiyo.

Amesema ujenzi wa meli hizo ni hatua itakayochangia ukuzaji wa uchumi kupitia uvuvi wa bahari kuu, pamoja na kuongeza uwezo wa Tanzania kutumia kikamilifu rasilimali zake za bahari.

Naye Mratibu wa AFDP kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Bw. Salum Mwinjaka, amesema utiaji saini wa mkataba huo ni hatua muhimu katika kuhakikisha malengo ya programu yanafikiwa kwa wakati na utekelezaji wake unakuwa na mafanikio.

Amesema Serikali inalenga kuhakikisha walengwa wa programu pamoja na Taifa kwa ujumla wananufaika na fursa zinazotokana na utekelezaji wa AFDP.

AFDP inalenga kukuza uzalishaji endelevu wa kibiashara unaozingatia mazingira, hususan katika uzalishaji wa mbegu za mazao ya kilimo kama mahindi, alizeti, maharagwe na jamii ya mikunde, pamoja na uvuvi na ufugaji wa viumbe maji.

Programu hiyo pia inalenga kuwawezesha wanawake na kuongeza ushiriki wa vijana katika shughuli za uzalishaji.

AFDP inaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) na kutekelezwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Kilimo pamoja na Wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi Zanzibar kupitia taasisi mbalimbali, ikiwemo TAFICO, ZAFICO, Wakala wa Mbegu (ASA), TARI na TOSCI.

Hatua hiyo ya kusaini mkataba wa ujenzi wa meli tatu inatarajiwa kuongeza uwezo wa Tanzania katika uvuvi wa bahari kuu, kuchochea uwekezaji, kuongeza ajira na mapato, na hatimaye kuimarisha mchango wa sekta ya uvuvi katika uchumi wa Taifa.

Read More

Tuesday, August 18, 2026

DKT. YONAZI AWAKUMBUSHA VIJANA KULINDA AFYA ZAO KATIKA MAPAMBANO DHIDI YA UKIMWI


 Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, Amewaasa vijana kulinda afya zao na kuepuka tabia hatarishi ili kupunguza maambukizi mapya ya VVU, kwa kuzingatia kuwa ni kundi linaloongoza kuwa hatarini zaidi nchini Tanzania.

Dkt. Yonazi ameyasema hayo mwishoni mwa wiki wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa Afua za UKIMWI Wilaya ya Uvinza Mkoa wa Kigoma alipoambatana na Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania, Dkt. Adam Mrisho, timu ya wataalam kutoka Ofisi yake, Wizara ya Afya, TAMISEMI na Ofisi ya Mkoa huo.

Aidha amepata wasaa kutembelea Kituo cha Maarifa Kata ya Kazuramimba mkoani humo kinachotoa huduma za masuala ya VVU na UKIMWI, na kukutana na vijana wanaotekeleza afua za UKIMWI kupitia vikundi vya uzalishaji mali kwa lengo la kujiinua kiuchumi na kujiletea maendeleo yao.

Akiwa katika kituo hicho, Dkt. Yonazi amepokea taarifa kutoka kwa mwenyekiti wa kikundi, Billy Sekibaha, kuhusu shughuli zinazofanywa na kikundi hicho ikiwemo za biashara ndogondogo za kuuza dagaa pamoja na shunguli za ushonaji wa nguo kwa lengo la kujikwamua kiuchumi na kuondokana na dhana ya utegemezi.

Amesisitiza kuwa, kundi la vijana linategemewa na Taifa katika shughuli za uzalishaji mali na kujiletea maendeleo yao na Taifa kwa ujumla hivyo ni vyema vijana wakaendelea kujilinda na kulinda wengine kwa kutambua hali zao na endapo wakagundulika kuwa na maambukizi ya VVU inashauriwa kuanza kutumia dawa mapema.

"Mnafanya kazi nzuri sana, endeleeni kuchangamkia uwepo wa mitandao ya kijamii kutangaza bidhaa zenu ili kuwafikia wateja wengi zaidi na kujitangaza kitaifa na kimataifa," alisisitiza Dkt. Yonazi

Kwa upande wake Mtendaji  wa TACAIDS, Dkt. Adam Mrisho amewapongeza vijana hao kwa kazi nzuri wanazofanya na kusisitiza kuwa Tume itaendelea kuwawezesha vijana kiuchumi na kuwajengea uwezo ili kuendeleza mapambano dhidi ya maambukizi mapya ya VVU na kufikia lengo la kutokomeza UKIMWI ifikapo mwaka 2030.

 

Read More

Monday, August 17, 2026

WAZIRI KABUDI AKAGUA NA KUKABIDHI MIRADI YA IFAD YA KUIMARISHA UZALISHAJI WA MBEGU, NZEGA


 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Prof. Palamagamba Kabudi, leo Agosti 17, 2026, ametembelea, kukagua na kukabidhi miradi inayotekelezwa kupitia Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (Agriculture and Fisheries Development Programme – AFDP) katika Shamba la Mbegu la Wakala wa Mbegu Tanzania (ASA), Kilimi, Wilaya ya Nzega, Mkoa wa Tabora.

Programu hiyo inafadhiliwa na Shirika la Kimataifa la Maendeleo ya Kilimo (IFAD), ikiwa na lengo la kuongeza tija, kuimarisha uzalishaji wa mbegu bora na kuchochea maendeleo ya sekta ya kilimo nchini.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Prof. Kabudi amesema sekta ya kilimo ni mhimili muhimu wa ukuaji wa uchumi wa Tanzania kutokana na mchango wake katika pato la Taifa, usalama wa chakula, ajira na biashara ya nje.

“Programu hii ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi ni muhimu kwa sekta ya kilimo kwa kuwa inalenga kuongeza tija katika sekta ya kilimo ambayo ni mhimili wa maendeleo ya uchumi. Sekta hii inachangia kiasi cha nusu ya pato la Taifa, robo tatu ya bidhaa zinazouzwa nje ya nchi na ni chanzo cha chakula pamoja na kutoa fursa za ajira kwa zaidi ya asilimia 75 ya Watanzania,” amesema Prof. Kabudi.

Aidha, Waziri Kabudi amekabidhi rasmi jengo la ofisi, jengo la karakana na jengo la kukaushia mbegu kwa Wizara ya Kilimo, miradi ambayo imetekelezwa kupitia Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kwa ufadhili wa IFAD.

Kabla ya kukabidhi miradi hiyo, Prof. Kabudi alikagua miradi mbalimbali inayotekelezwa katika Shamba la Mbegu la Kilimi, ikiwemo jengo la karakana, eneo la kukaushia mazao (drying shade), ofisi na ukumbi wa mafunzo pamoja na ujenzi wa nyumba za watumishi.

Vilevile, programu hiyo imewezesha upatikanaji wa zana na vifaa vya kisasa vya kilimo, ikiwemo boom sprayer, disc harrow, matrekta, maize sheller, tiller, vifaa vya karakana pamoja na magari kwa ajili ya usimamizi na usambazaji wa mbegu.

Akihitimisha ziara hiyo, Prof. Kabudi amesisitiza umuhimu wa utekelezaji wa miradi kwa wakati, kwa kuzingatia viwango na ubora uliokusudiwa ili kuhakikisha thamani halisi ya fedha iliyowekezwa (value for money) inapatikana.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuwa na mpango mkakati madhubuti wa utekelezaji ili kuhakikisha malengo ya Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi yanafikiwa ndani ya muda uliopangwa.

Katika ziara hiyo, Waziri Kabudi ameambatana na Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. David Silinde, Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Umwagiliaji na Zana za Kilimo, Mhandisi Athumani Kilundumya, Mkurugenzi wa Sera na Uratibu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Bw. Paul Sangawe, pamoja na Mratibu wa Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Bw. Salimu Mwinjaka. ‎

Read More

“WENYE ULEMAVU CHANGAMKIENI FURSA ZA MIKOPO” NAIBU WAZIRI UMMY


 Naibu  Waziri  Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. Ummy Nderiananga amewataka watu wenye ulemavu kutumia mikopo inayotolewa na Serikali kama fursa ya kujikwamua kiuchumi na kubadili maisha yao, badala ya kuichukulia kama msaada au hisani.

Naibu Waziri aliyasema  hayo katika Ofisi za Mkoa wa Iringa, wakati wa ziara yake ya kutoa elimu kwa watu wenye ulemavu kuhusu fursa mbalimbali zinazopatikana kwa lengo la kuwawezesha kiuchumi na kijamii.

Amesemalisema  Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira wezeshi kwa watu wenye ulemavu kupata mikopo na fursa nyingine za kiuchumi, huku akibainisha kuwa kiasi kikubwa cha fedha tayari kimetolewa kwa wanufaika nchini.

“Hadi sasa watu wenye ulemavu Nchi nzima  wameshakopa shilingi Bilioni 26.8 hivyo tunapaswa kushukuru na kuipongeza Serikali kwa mikakati mizuri kuhakikisha Kundi hili linafikiwa na sisi kama watu wenye ulemavu tuchangamkie fursa hii ya mikopo tujiinue kiuchumi na tuwe waaminifu kurejesha ili kuwawezesha na wengine,”Alieleza Mhe. Ummy.

Mhe. Ummy Alieleza kwamba  ongezeko hilo ni ishara kuwa watu wenye ulemavu wameanza kutambua na kutumia fursa zinazotolewa kwa ajili ya kuanzisha na kuendeleza shughuli za kiuchumi, hivyo kuwataka kuendelea kujitokeza na kutumia fursa hizo .

"Mafanikio ya baadhi ya watu wenye ulemavu waliopata mikopo yanapaswa kutumika kama mfano na kuwahamasisha  wengine kuchangamkia fursa hii ya mikopo kwani wapo wenye ulemavu wengi wamenufaika hatimaye kupungua wimbi la utegemezi katika familia hata Taifa," Alisisitiza.

Aidha Waziri Ummy aliitaka  Halmashauri ya Manispaa ya Iringa kujitathmini katika utoaji wa mikopo kwa watu wenye ulemavu akibainisha kuwa kiwango kilichotolewa katika manispaa hiyo bado ni kidogo ikilinganishwa na mahitaji yaliyopo huku akiwapongeza watu wenye ulemavu wanaofanya shughuli zao kama vile kiwanda cha kufyatua matofali Kata ya Nduli, duka la jumla la mahitaji ya nyumbani, mnufaika wa mikopo aliyenunua bajaji ya biashara na wafanyabiashara wadogo katika Halmashauri ya Manispaa ya Iringa.

“Serikali za mitaa zinapaswa kuhakikisha fursa za mikopo zinawafikia walengwa, huku wakitenga pia maeneo maalumu ambayo watu wenye ulemavu watafanya  shughuli za uzalishaji na biashara zao bila kusumbuliwa,” Alibainisha.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Mhe. Benjamini Sitta alisema Serikali imefanya jitihada kubwa kuhakikisha inatatua changamoto ya mikopo kwa wenye ulemavu kutoka utaratibu wa kukopa kwa vikundi wa awali  hadi mtu mmoja mmoja.

Awali akitoa taarifa ya Halmashauri ya Manispaa ya Iringa ya Utoaji wa mikopo kwa vijana, wanawake na wenye ulemavu  kwa kipindi cha mwaka 2024/2025 hadi 2025/2026, Afisa Maendeleo ya Jamii ambaye ni Mratibu wa mikopo Bi. Sunday Mtamakaya alieleza kuwa vikundi 183 vimepatiwa mikopo wakiwemo wanawake, vijana na wenye ulemavu.

“Halmashauri imefanikiwa kuwawezesha wenye ulemavu mitaji, wana vikundi kuboresha hali za maisha yao na baadhi ya wanavikundi kuwaajiri watu wengine katika biashara zao. Licha ya mafanikio hayo bada ya kurejeshwa utaratibu wa mikopo bado kuna changamoto ya baadhi yao kushindwa kuejesha mikopo hiyo kwa uaminifu,” Alisema Afisa Maendeleo huyo.

Naye  Mnufaika wa mikopo hiyo mwenye ualbino  Bwa. Issa Iddi Sogoi ambaye anamiliki duka la jumla la mahitaji ya nyumbani  katika Halmashauri hiyo alimshukuru Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyoonyesha upendo, kujali na kuwaunga mkono watu wenye ulemavu kupitia mikopo hatua inayomsaidia kumudu mahitaji ya familia na kujiongezea kipato ambapo pia ametoa ajira kwa vijana wengine.

 

Read More

DKT. YONAZI AVIASA VIKUNDI VYA WAVIU KUTUMIA MITANDAO YA KIJAMII KUWAFIKIA WATEJA


 Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi  ashauri kikundi cha Paza Sauti cha Watu Wanaoishi na Maambukizi ya Virusi vya UKIMWI (WAVIU) kutumia mitandao ya kijamii kutangaza na kuuza bidhaa zao ili kuweza kufikia wateja wengi zaidi huku akiwapongeza kwa juhudi na umoja wao katika shughuli zao za uzalishaji.

Ametoa ushauri huo alipotembelea kikundi cha Paza Sauti cha wajasiliamali wanaoishi na VVU katika ziara yake ya ufatiliaji utekelezaji wa afua za VVU na UKIMWI katika Wilaya ya Nyamagana, Jijini Mwanza.

“Nikiingia kwenye simu yangu sioni kikundi cha Paza Sauti msibanwe na soko la machoni nendeni duniani kupitia mitandao ya kijamii, anzisheni akaunti ya Instagram muweze kuwafikia hata watu walipo nchi za nje" alisema Dkt. Yonazi

Vilevile, Dkt. Yonazi alitembelea Kikundi cha Peace and Love kinachojishughulisha na kilimo cha nyanya na matikiti, kinachosimamiwa na Halmashauri ya Jiji la Mwanza kupitia Mradi wa DREAMS, unaoratibiwa na TACAIDS kwa kushirikiana na ICAP, Mradi huo unalenga kuwawezesha wanawake na vijana balehe kiuchumi na kijamii ili kupunguza vishawishi vinavyoweza kupelekea maambukizi mapya kwa kundi hili.

Kwa hatua nyingine Dkt.Yonazi amepongeza Jiji la Mwanza kwa kuweza kufanikiwa kufikia lengo la kitaifa la 95-95-95 kwa kiwango cha juu na kuongeza ushirikiano na wadau wakiwemo viongozi wa dini katika mwitikio wa VVU na UKIMWI nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) Dkt. Adam Mrisho alisisitiza kuwa TACAIDS itaendelea kuwekeza katika uwezeshaji wa vijana kiuchumi kama sehemu ya juhudi za kuwaondoa katika mazingira ya changamoto na vishawishi vinavyoweza kuongeza hatari ya maambukizi mapya ya VVU.

“hongereni kwa juhudi na kazi mnazozifanya, hili ni eneo ambalo Tume tumezingatia sana ili kuwawezesha vijana kujikwamua kiuchumi”alisema

Naye, Katibu wa Baraza la Watu Wanaoishi na Maambukizi ya Virusi vya UKIMWI Wilaya ya Nyamagana Bw. Joseph Kiharate ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu kwa kuwezesha WAVIU kupata dawa katika hospitali zote na kushukuru huduma zinatolewa kwani zinazingatia ubora na weledi kwa kila siku katika juma.

“tunashukuru tunapata dawa katika hospitali zote na huduma zinatolewa siku saba za wiki kupitia nyie afya zetu zinaimarika," alisema Joseph.

 

Read More

Saturday, August 15, 2026

WAZIRI KABUDI, SERIKALI ITAENDELEA KUTHAMINI MCHANGO WA LUKUVI


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu) Mhe. Prof, Palamagamba Kabudi amesema Serikali itaendelea kuheshimu na kuthamini mchango wa kiuongozi uliotolewa na aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu) Marehemu William Lukuvi.

Hayo ameyasema leo wakati wa maadhimisho ya  ibada ya Misa Takatifu ya kumaliza Msiba  iliyofanyika nyumbani kwa Marehemu Idodi Mkoani Iringa na kuhudhuriwa na wananchi na viongozi mbalimbali wa chama na Serikali.

Alisema, “Enzi za uhai wake Waziri Lukuvi alinisaidia kufahamu shughuli mbalimbali za Bunge na serikali na hivyo kupata weledi mzuri mambo mengi kutokana na uzoefu aliyokuwa nao,”

Aidha uwezo wake wa kusimamia nidhamu ipasavyo Bungeni ikiwa ni pamoja na kuimarisha mahusiano kati ya Serikali na Bunge ilimfanya aendelee kuaminiwa katika kazi ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu.

Kwa Upande Mama Germana Lukuvi Mjane wa Marehemu ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mhe, Rais Dkt, Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kushikamana na familia tangu walipopata msiba.

Awali Mbunge wa Isimani Mhe, Emanuela Mtatifikolo alisema Marehemu Lukuvi ataendelea kuishi kwenye mioyo ya wananchi wa Isimani, kwa mageuzi makubwa ya maendeleo aliyoyafanya.

 “Uwakilishi wake kwa wananchi wa Jimbo la isimani na kwa kushirikiana na Serikali aliwezesha Jimbo la Isimani kunufaika na ujenzi wa barabara ya lami uimarishaji wa Huduma za afya na kuendelea kuboresha miundo mbinu ya elimu sambamba na umeme,” alibainisha

Read More

MJI WA SERIKALI MTUMBA WAIPA TANZANIA FURSA YA KUIMARISHA DIPLOMASIA


Balozi wa Serbia nchini, Mhe. Jovica Topalović, amesema, maendeleo ya Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma, yanaipa Tanzania fursa ya kuimarisha mazingira ya shughuli za kidiplomasia na uhusiano na mataifa mbalimbali.

 Hayo yamejiri wakati wa ziara ya kukagua eneo lililotengwa kwa ajili ya ujenzi wa Ubalozi wa Serbia, ambapo alipongeza hatua za Serikali katika kuendeleza eneo hilo. Amesema anaamini ndani ya miaka 10 ijayo, balozi nyingi zitahamia Mtumba, jambo litakaloimarisha nafasi ya Dodoma kuwa kama kitovu cha shughuli za kidiplomasia nchini.

Aidha, amesema uwepo wa balozi nyingi katika eneo moja utarahisisha mwingiliano na ushirikiano wa kidiplomasia. Pia ameongeza kuwa, Serbia na Tanzania zina historia ndefu ya uhusiano na maeneo mbalimbali ya ushirikiano na akieleza matumaini ya kuimarika zaidi kwa uhusiano huo katika miaka minne ijayo.

Katika ziara hiyo, Mratibu wa Ujenzi na Uendelezaji wa Mji wa Serikali, Ofisi ya Waziri Mkuu, Bw. Noel Mlindwa, aliwasilisha taarifa kuhusu maendeleo ya ujenzi na uendelezaji wa eneo hilo. Ziara hiyo ilihudhuriwa pia na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Marekani kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Ellen Maduhu, pamoja na Maafisa wa Wizara na wataalamu kutoka Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Read More

Wednesday, August 12, 2026

PROFESA KABUDI AHIMIZA MATUMIZI SAHIHI YA ALAMA ZA TAIFA

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi, amehimiza wananchi kuendelea kuzingatia matumizi sahihi ya alama za Taifa, hususan rangi na mwonekano wa Bendera ya Taifa, kwa mujibu wa sheria.

Prof. Kabudi ametoa kauli hiyo leo, jijini Dodoma, alipofanya ziara ya kikazi katika Ofisi za Wakala wa Serikali wa Uchapishaji Tanzania, ambapo alipongeza taasisi hiyo kwa kuendelea kuelimisha umma na kusimamia matumizi sahihi ya alama za Taifa, ikiwemo Bendera na Nembo ya Taifa.

Amesema sheria inayosimamia matumizi ya alama za Taifa inaweka wajibu kwa Wakala wa Serikali wa Uchapishaji Tanzania kuhakikisha sheria hiyo inatekelezwa ipasavyo, ikiwemo kuzalisha Bendera za Taifa kwa niaba ya Serikali.

“Sheria ya Alama za Taifa inaeleza kuwa Bendera yetu ina ufito wa rangi ya dhahabu na siyo njano. Lazima tuzingatie sheria ilivyoelekeza na kuendelea kuelimisha umma kuhusu matumizi na rangi sahihi za Bendera ya Taifa,” amesisitiza Prof. Kabudi.

Aidha, Prof. Kabudi amesema mabadiliko ya Idara kuwa Wakala wa Serikali yanalenga kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali, pamoja na kuiwezesha taasisi hiyo kuendelea kupanua shughuli zake kulingana na mabadiliko ya teknolojia, uchumi na mahitaji ya kimkakati.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Wakala wa Serikali wa Uchapishaji Tanzania, Bw. George Lugome, amesema Wakala unaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ununuzi wa mashine mpya na malighafi, kulingana na mahitaji ya uzalishaji.

Amesema uwekezaji huo unalenga kuimarisha uwezo wa Wakala katika uzalishaji na utoaji wa huduma kwa ufanisi, sambamba na kuendana na mahitaji ya sasa ya kiteknolojia.

 

 

Read More

Tuesday, August 11, 2026

WAZIRI KABUDI AHIMIZA KUKAMILIKA KWA UJENZI OFISI YA MSAJILI WA VYAMA VYA SIASA


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu ( Sera Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu) Mhe, Prof. Palamagamba Kabudi ametoa wito kwa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa kuhakikisha  umaliziaji ujenzi wa Jengo  la Ofisi hiyo unakamilika kwa wakati ili kusaidia kuendelea kutoa huduma bora za Ofisi.

Waziri amesema hayo alipotembelea kujionea maendeleo ya ujenzi wa Ofisi hiyo leo Mtaa wa Kilimani Jijini Dodoma ambapo amepongeza kwa hatua za ujenzi uliofikiwa na kuelekeza Mkandarasi kuhakikisha anamaliza ujenzi wa Jengo hilo kwa wakati.

Waziri amesema, “ujenzi wa Ofisi za Umma lazima ujengwe kwa hadhi na uakisi matarajio ya muda mrefu ujao kulingana na mahitaji ya Ofisi, niwapongeze kwa kuzingatia hilo katika  ujenzi wa jengo lenu.”

Kwa upande wake Msajili wa Vyama vya Siasa Jaji Mstaafu Fransis Mutungi amemshukuru Waziri kwa maelekezo aliyotoa, ambapo amesema mipango ya Ofisi ni kuwa na watendaji wa wenye elimu ya siasa, wataalamu wa elimu jamii ambao watasaidi kuchakata na kutoa muongozo kulingana na mambo yanavyokwenda.

“Taasisi hii ni kitovu cha mambo ya siasa tunahitaji wataalamu wenye ujuzi tofauti watakaosaidia katika kufanya tafiti na kutoa taarifa zenye weledi zitakazosaidia taasisi kufanya kazi vizuri zaidi,” alieleza Jaji Mstaafu Mutungi

Awali Mkurugenzi wa Rasilimali Watu Bw,Magohu Zonzo amesema ujenzi wa jengo hilo unatekelezwa na Kampuni ya Group Six Intenational na unasimamiwa na mshauri elekezi kutoka Chuo Kikuu cha Ardhi kupitia kampuni tanzu ya (ARU) kwa ajlili usanifu na usimamizi wa mradi.

 

Read More

Saturday, August 8, 2026

KABUDI, AHIMIZA MATUMIZI YA TEKNOLOJIA ZA KISASA KATIKA UZALISHAJI


Washiriki wa Maonesho ya nane watakiwa kuendelea kuzingatia ubunifu, teknolojia mpya katika shughuli zao za uzalishaji ili zisaidie katika kutatua changamoto zinazojitokeza wakati wa kazi.

Kauli hiyo Imetolewa leo  Mkoani Morogoro na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Mhe, Prof. Palamagamba Kabudi wakati akifunga maonesho ya nanenane Kanda ya Mashariki.

 

Waziri amehimiza viongozi wa Mikoa kuhakikisha teknolojia zilizooneshwa kwenye viwanja vya Nanenane zinafikishwa kwa wananchi kupitia huduma za ugani na mashamba darasa. 

 

“tuendelee kutumia Jukwaa la Business-to-Business (B2B) ili liweze kkuweka malengo yanayopimika katika biashara, uwekezaji na masoko” alihimiza Waziri Kabudi

 

Aidha  taasisi  nyingine kama ( TBS), (SIDO) ziendelee kujikita katika kuwasaidia wajasiriamali wadogo kufikia viwango vinavyohitajika kushindana katika soko la ndani na nje ya nchi.

 

Naye Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Malima amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe, Dkt, Samia Suluhu Hassan kwa utumishi wake wa kipekee katika taifa na kwa wananchi.

 

Mkuu wa Mkoa alieleza, “Maonesho ya Mwaka yamefanyika yakiwa katika utekelezaji wa mwaka wa kwanza wa dira ya taifa 2050, nasi tumeondoka katika mafanikio ya maonesho kwa kuangalia idadi ya mabanda na sasa tumeweka vigezo maalumu kwa kuangalia elimu iliyotolewa na teknolojia iliyochukuliwa na muunganiko wa biashara iliyopatikana.”

 

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Balozi Batlida Burian amempongeza Mhe, Rais Dkt, Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha kusainiwa kwa mkataba wa kiwanda cha Usafishaji Mafuta Mkoani Tanga. 

 

“Mhe, Rais ameshaacha tabasamu kabla ya kufika mwaka 2030 mradi huo mkubwa utawezesha kunufaisha Tanga na kanda nzima ya Mashariki, tumejipanga kuhakikisha kila mtu ananufaika na fursa hii ya ujengwaji wa kiwanda ambayo imetolewa,”alibainisha

 

 

Read More

Thursday, July 23, 2026

TNCM YAPITISHA OMBI LA TANZANIA LA FEDHA KUTOKA MFUKO WA DUNIA 2027 HADI 2029


 Kamati ya Kitaifa ya Kuratibu na Kusimamia Fedha za Mfuko wa Dunia nchini Tanzania (Tanzania National Coordinating Mechanism – TNCM), imeidhinisha rasmi Ombi la Tanzania la Ufadhili wa Mzunguko wa Nane wa Mfuko wa Dunia (Global Fund Grant Cycle 8 – GC8) kiasi cha dola za Marekani milioni 538.6 kwa ajili ya kuendeleza mapambano dhidi ya UKIMWI, Kifua Kikuu (TB) na Malaria, pamoja na kuimarisha Mifumo Thabiti na Endelevu ya Afya (RSSH), katika kipindi cha utekelezaji kuanzia Januari 2027 hadi Desemba 2029.

Uidhinishaji huo umefanyika jijini Dar es Salaam katika kikao maalum cha TNCM kilichoongozwa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, ambaye pia ni Mwenyekiti wa TNCM.

Dkt. Yonazi amesema kuwa, mchakato wa maandalizi ya Ombi la GC8 ulianza rasmi tarehe 13 Machi, 2026 na umeendelea kwa zaidi ya miezi minne, ukihusisha mashauriano ya kina, majadiliano ya kitaifa, upangaji wa vipaumbele, uandishi wa andiko, mapitio ya kitaalamu na uhakiki wa nyaraka za maombi.

Aidha, alifafanua kuwa, mchakato huu umejengwa katika msingi wa ushirikishwaji mpana wa wadau, uwazi, uwajibikaji na umiliki wa kitaifa ambapo zaidi ya wadau 270 walishiriki kwa uwakilishi wa makundi mbalimbali, yakiwemo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara, Idara na Taasisi zake; Washirika wa Maendeleo, Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mashirika ya Kimataifa, Asasi za Kiraia, Sekta Binafsi, Mashirika ya Dini, watu wanaoishi na VVU, jamii zilizo katika hatari kubwa ya maambukizi na zilizoathiriwa na magonjwa hayo; pamoja na wataalamu wa sekta ya afya.

Dkt. Yonazi ameeleza kuwa uwekezaji wa Mfuko wa Dunia umeendelea kutoa mchango mkubwa katika juhudi za Serikali za kuboresha afya na ustawi wa Watanzania, na kusema utekelezaji wa GC8 utatoa fursa kwa Nchi kuendela kuzuia maambukizi mapya ya VVU, kuongeza upatikanaji wa dawa za kufubaza makali ya VVU (ARV), kuimarisha kinga, uchunguzi na matibabu ya Malaria, pamoja na kuboresha ugunduzi wa mapema na matibabu ya Kifua Kikuu.

“Kuidhinishwa kwa Ombi hili la Ufadhili ni matokeo ya kazi kubwa na ushirikiano wa wadau wetu ambao wamewekeza muda, utaalamu na rasilimali kuhakikisha kuwa vipaumbele vilivyoainishwa vinazingatia mahitaji ya nchi pamoja na sauti za jamii na makundi yanayoathiriwa na magonjwa hayo”.Alisema Dkt. Yonazi.

Aliongezea kuwa,hatua hiyo ni mafanikio muhimu yanayoonesha dhamira ya Tanzania ya kuendeleza mapambano dhidi ya magonjwa hayo matatu, sambamba na kujenga mfumo wa afya ulio imara, jumuishi na endelevu.

Dkt. Yonazi ameshukuru Sekretarieti ya Mfuko wa Dunia iliyopo Geneva (Global Fund Country Team), wajumbe wa TNCM pamoja na wadau wote walioshiriki katika maandalizi na ukamilishaji wa maombi hayo, amepongeza jitihada zao akisema zimekuwa na mchango muhimu kuwezesha kufikia hatua hii.

Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa TNCM, Bw. Kent Pius, ametoa shukrani maalum kwa Mwenyekiti wa TNCM, Mfuko wa Dunia, wajumbe na wadau wote kwa ushirikiano na uwajibikaji mkubwa katika kuhakikisha kuwa zoezi hili limefanyika kwa ufanisi na ubora uliokusudiwa na kusema kuwa, hatua hii ni matokeo ya dhamira ya dhati na juhudi za pamoja.

“TNCM itaendelea kuratibu ushirikiano kati ya Serikali, jamii, Asasi za Kiraia, Washirika wa Maendeleo, Sekta Binafsi na wadau wa kimataifa katika kuhakikisha uwekezaji wa Mfuko wa Dunia unachangia katika kufikia malengo ya Kitaifa na Kimataifa ya kutokomeza UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria kama vitisho vya afya ya jamii,” alisema Kent.

 

 

Read More