Saturday, December 2, 2023

“WAHITIMU CHUO CHA BIBLIA MUWE MABALOZI WAZURI WA KUSIMAMIA MAADILI” WAZIRI MHAGAMA


 Wahitimu wa Chuo cha Biblia cha Evengelism Church wameaswa kuwa askari wazuri wa vita dhidi ya mmomonyoko wa maadili ambao unaendelea kushamiri katika jamii zetu hususani kwa vijana.

Wito huo umetolewa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe, Jenista Mhagama wakati wa mahafali ya 83 ya chuo hicho yaliyofanyika, Sakila Katika wilaya ya Meru Mkoani Arusha.

Waziri aliwaambia wahitimu hao kwamba maendeleo ya taifa letu yanategemea sana nguvu kazi na nidhamu ya kazi, japokuwa nchi yetu haiegemei upande wowote katika maswala ya dini, lakini sehemu kubwa ya watu wake wanaamini katika dini kupitia madhehebu mbalimbal

 “ni muhimu mkawe mabalozi wazuri katika vita hii na mkashirikiane na viongozi wengine wa dini na Serikali ili kwa pamoja tuhakikishe tunalilinda taifa letu dhidi ya upotofu huu wa maadili” alibainisha.

Aidha, aliwasihi kuendelea kuliombea taifa amani, utulivu, upendo na mshikamano ili kulijenga taifa.

Waziri ametumia maandiko matakatifu, katika Injili ya Matayo (Sura ya 5:13-16) ambayo yalisema, nami pia niwasihi popote mnapokwenda, mkawe chumvi ya dunia na kamwe msipoteze ladha ya chumvi lakini pia mkawe mwanga wa ulimwengu ukaangaze mbele ya watu ili wayaone matendo yenu mema wamtukuze baba yenu aliye mbinguni.

“Sina shaka kwamba, wote mkitoka hapa mtakwenda kutekeleza jukumu la kichungaji na kufundisha watu kwa upendo, uaminifu na kuwaongoza katika kweli maana huo ndio wito mlioitiwa,” alifafanua

Kwa upande wake Dkt. Eliud Issangya, Askofu Mkuu wa International Evengelism Church na Mkuu wa Chuo cha Biblia Sakila; alisema wahitimu wa chuo cha Biblia wanapaswa  kwenda kuweka mkazo wa kufundisha maadili kwenye jamii.

“Msambaze maandiko kwa kulenga maadili na si kwa kutafuta mali, bali watu waweze kuishi kwa kuthaminiana na wawe watu wenye hekima,” alihimiza

Awali muwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe, Joshua Nassari Mkuu wa wilaya ya Monduli alisema serikali ya mkoa wa Arusha itaendelea kutoa ushirikiano wa kiroho kwa chuo hicho cha Biblia na madhehebu mengine.

“Jamii yetu imekuwa ikipitia changamoto kubwa za mabadiliko ya kimadili na kitamaduni hivyo tujikite katika kufundisha maadili mema ya kitanzania na madili mema ya Imani ili tuwe na jamii iliyostaarabika,”alihimiza

Read More

Thursday, November 30, 2023

MAANDALIZI KUELEKEA SIKU YA UKIMWI DUNIANI YAKAMILIKA

 


Viongozi wa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu wamekagua maandalizi ya kuelekea Kilele cha Maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani Desemba 1, 2023 katika Viwanja vya Morogoro Sekondari ambapo maandalizi hayo yamekamili. Katika ukaguzi huo waliongozwa na Mhe. Jenista Mhagama ambaye ndiye Waziri mwenye dhamana ya uratibu.

Ikumbukwe maadhimisho ya siku ya UKIMWI Duniani hufanyika kila mwaka ambapo kauli mbiu ya mwaka huu inasema “Jamii Iongoze Kutokomeza UKIMWI”.

Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa.

Read More

Wednesday, November 29, 2023

TAMWA YAHIMIZWA KUWEKA MKAZO AJENDA YA UHURU WA KUJIELEZA UNAOJUMUISHA SAUTI ZA WANAWAKE

 


Chama cha wahandishi wa habari wanawake Tanzania (TAMWA) kimetakiwa kuweka mkazo mkubwa katika uhuru wa kujieleza unaojumuisha sauti za wanawake ndani ya ajenda ya jumla ya haki za binadamu.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama wakati alipomuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan katika maadhimisho ya miaka 36 ya chama cha waandishi wa habari wanawake Tanzania yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam.

Waziri, ametoa wito kwa (TAMWA) kuona umuhimu wa mijadala yenye mlengo wa kijinsia na uhusiano kati ya uhuru wa vyombo vya habari, ulinzi na usalama wa waandishi wa Habari wanawake, na uhuru wa kujieleza kuwa kitovu cha kufanya maamuzi katika ngazi ya jamii kitaifa, na kimataifa.

“Tuadhimishe siku hii kutimiza ahadi zilizotolewa na kila Nchi Mwanachama wa Umoja wa Mataifa ili kuyafikia Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) yote na hasa lengo namba tano linalozungumzia usawa wa jinsia,” alihimiza.

Aidha wadau mbalimbali wa habari watumie siku hii kusherehekea kwa kuungana na TAMWA kulinda na kuthamini haki za wanawake, haki za wasichana, haki za watoto, maadili ya kitanzania, na kupinga ukatili wa jinsia majumbani, hadharani na mitandaoni.

“Wamiliki wa vyombo vya Habari na waandishi wote kwa ujumla muungane katika jitihada za ulinzi na usalama wa waandishi wa Habari wanawake na hapa niwatie moyo waandishi wa Habari wanawake kuwa kazi yenu nzuri inaonekana pale mnapoweka jitihada ya kufanya kazi kwa weledi bila kukatishwa tamaa na vikwazo vya kimazingira.”Alifafanua

Waziri amesema kama kauli mbiu inavyosema, Uongozi Bora na Mchango wa Wanawake ni Chachu Kuelekea Tanzania yenye Maendeleo endelevu.

Hatuna budi kutambua kwamba suala la jinsia sio suala la wanawake peke yao bali ni suala la kuchochea maendeleo ya taifa letu miongoni mwa wanawake na wanaume, kwani ni jambo linalohimiza ushirikishwaji na ujumuishi usioacha kundi lolote nyuma.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Mawasiliano na Technolojia ya Habari Bw, Selestine Gervas Kakele amesema inatambua Mchango wa (TAMWA) na wakati wote serikali itaendelea kuangalia ujumbe ambao TAMWA na asasi nyingine inatoa.

Tumepokea utafiti kuhusu unyanyasaji wa kijinsia: (TAMWA) kupitia utafiti huu imesaidia kuvunja ukimya, matokeo ya utafiti  hayalengi kunyoosha kidole kwa mtu, bali kushirikiana ili tuweze kuishinda vita hiyo.

“Tusimamie weledi na nidhamu ya kazi na pale vitendo hivi vinapojitokeza: wahanga wasikae kimya jitokezeni, pazeni sauti na serikali itasikia,” alifafanua.

Awali   Mwenyekiti wa chama cha waandishi wa habari wanawake Tanzania (TAMWA) Bi, Joyce Shebe amemshukuru Mhe. Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kukubali mwaliko.

“Tumeona jinsi serikali ambavyo inapitia mifumo ya kisera na kisheria ilikuja na mipango inayopimika katika kuhakikisha ushirikishwaji na uwezeshaji wa wanawake kiuchumi na masuala yanayohusu usawa wa kijinsia inatatekelezeka” alibainisha

(TAMWA) tunaahidi kumuunga mkono kivitendo kwa sababu ni jukumu ambalo tumealianza tangu miaka 36 iliyopita

 

 

Read More

Saturday, November 25, 2023

WAZIRI MHAGAMA, AHIMIZA UWEKEZAJI KATIKA SEKTA YA UTALII MBINGA

 


Imeelezwa kwamba uwekezaji wa hoteli kubwa na za kisasa unasaidia katika kuchochea shughuli za utali na kuongeza thamani ya Mji wa Mbinga, kwa sababu ya upekee wa vivutio vyake.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama wakati wa Uzinduzi wa Mradi wa Hotel ya One Pacific yenye hadhi ya nyota tatu katika wilaya ya Mbinga.

Waziri Mhagama amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.  Samia Suluhu Hassan amejipambanua kwa kuwa balozi kinara wa sekta ya utalii na uwekezaji kwa ujumla katika sekta ya utalii.

“Mkakati wa Taifa wa ROYAL TOUR na kuifungua nchi yetu Tanzania katika sekta ya utalii ni mkakati mkubwa sana, na uliotukuka na tunaungana na wawekezaji katika kutafsiri ROYAL TOUR ndani ya wilaya yetu ya Mbinga,” Alifafanua

Akieleza kuhusu vivutio vinavyopatikana, Waziri amesema, wilaya ya Mbinga inavivutio vya kutosha; kama safu za milima zilizojipanga kwa kuvutia, zenye maporomoko ya maji, uoto wa asili, unaopendezesha madhari ya milima hiyo.

Aidha hapa ndio mahali ambapo kuna mapango ya kale katika eneo la Litembo, na inaaminika wazee wetu wa zamani waliishi katika mapango hayo.

“Hii historia kama itawekezwa vizuri, ni kivutio na utalii wa kutosha sana katika eneo letu,” Alibainisha.

Kwa upande wake Dkt. Erasmo Nyika akizungumza kwa niaba ya bodi ya wawekezaji wa mradi wa Hotel hiyo amesema wamesukumwa kuja kuwekeza Mbinga kutokana na Msukumo wa Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye amejenga mazingira rafiki ya uwekezaji.

“Tumuwekeza miradi miwili ndani ya wilaya ya Mbinga yenye thamani ya zaidi ya shilingi Billioni 4, na tumeona fursa zipo na tunashukuru Ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Mbinga kwa kutushawishi kuwekeza Mbinga, mradi umelenga kuzalisha ajira nyingi kwa wazawa,” Alisema

Awali, Mhandisi Selemani Kinyaka katika taarifa yake amesema Ujenzi wa Majengo ya mraadi wa One Pacific Hotel; unavyumba vya kawaida 14, vyumba vya daraja la juu 23 vyumba vya hadhi ya kiutawala 3, Ukumbi mdogo wa mikutano, Migahawa 2, sehemu ya mazoezi, eneo la kuogelea na eneo la kufulia nguo.

 

Katika kipindi cha utekelezaji wa mradi tumetoa ajira zaidi ya 250 ambapo 30 zilikuwa ajira za kudumu, na nyingine ni ajira zilizojitokeza kila siku.

Read More

Wednesday, November 22, 2023

WAZIRI MHAGAMA AAGIZA KUIMARISHWA MIUNDOMBINU YA MAWASILIANO DAR



 Serikali kupitia Ofisi ya Rais TAMISEMI imeahidi kutoa kiasi cha shilingi Millioni  20 ili kuimarisha kivuko cha kivuko cha Magole/Mwanagati kilichopo katika kata ya Mzinga Halmashauri ya Ilala Mkoani Dar es salaam ili kiweze kupitika muda wote.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe, Jenista Mhagama wakati akizungumza na wakazi waliojitokeza katika eneo hilo la kivuko liloathirika na Mvua wakati wa ziara yake iliyolenga kupata taarifa zilizochukuliwa na Kamati ya Mkoa ya Maafa juu ya kudhibiti madhara ya zaidi mvua yanayoweza kujitokeza.

Ameongeza kusema kazi ya kuimarisha kivuko ifanywe na wakala wa barabara vijijini TARURA haraka iwezekanavyo.

“Kivuko hiki kitakapokuwa kinapitika muda wote hakitarudisha juhudi ya kwenda na Mpango wa pili wa muda mrefu wa kujenga daraja la kudumu,”alibainisha

Waziri mhagama alisema kuwa serikali inatamani kuona shughuli za wananchi zifanyika bila kusimama; tunatamani watoto wetu waende shule, tunatamani kina mama wajawazito waende kupata huduma za afya kwa wakati, tunapenda wananchi wajisikie serikali yao inawajali, alisema Waziri.

“Tunataka tutengeneze daraja livutie machoni pa watu, kile matumaini kwa watu kwamba hii ni nyota ya Mhe. Rais, Dkt, Samia Suluhu Hassan na wananchi washirikishwe kiasi cha kutosha,” alifafanua

Waziri Mhagama alielekezaTARURA kuifanya kazi hiyo  kwa uaminifu mkubwa na kwa hofu ya mungu, kwa sababu mnasimamia uhai na maisha ya watu na sisi tunawaamini na tunawategemea.

Katika hatua nyingine Waziri ameomba wananchi kuendelea kuchukua tahadhari juu ya magonjwa ya mlipuko; hali ya mvua inaweza kutupelekea kwenye magonjwa ya kuhara, magonjwa ya malaria.

Aliwaasa wananchi kuendelea kusafisa vichaka na kujenga utaratibu mzuri wa kusafisha mazingira yetu na kila mmoja awe askari wa mwenzake na kuhakikisha mifereji yetu inakuwa safi na mapito ya maji yanakuwa wazi.

Kwa upande Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Mhe. Albert Chalamila alisema Mkoa wa Dar es salaam umeathiriwa na wa ujenzi wa kutawanyika, hivyo kasi ya ujenzi wa miundombinu imekuwa gharama kubwa, lakini lazima hilo lifanyike kwa sababu ni huduma kwa watanzania.

Wataalamu wetu wamekuwa wakisanifu ramani za daraja lakini bado hatujapata fungu la fedha kwa ajili ya ujenzi wa daraja, na hapa tunahitaji mkakakati mkubwa wa kuzuia mto kutokula kingo zake.

:Tunajitahidi kuhakikisha wananchi hawajengi mabondeni; na kulinda mito dhidi ya shughuli za kibinadamu, ikiwa ni sambamba na  kuhakikisha tunaunganisha miundo mbinu ya mawasiliano ili mambo yaweze kwenda vizuri,” alifafanua Mkuu wa Mkoa.

Naye diwani wa kata ya mzinga Mhe Jackob Izack amesema kero ni kubwa na kumshukuru sana waziri kwa kuja, mipango ilikwisha pangwa, mahitaji ya wananchi ni mikubwa na kuna wananchi zaidi ya elfu ishirini wanapita kila siku.

“Imani kubwa ipo kwa mama, na wewe mama umekuja kazi yetu ni kukuombea ili haya yote yaende kutendeka ili ikawe historia mpya kwa wananchi,” alifafanua Mhe. Diwani




Read More

Wednesday, November 15, 2023

WANANCHI WAPEWA RAI KUJITOKEZA KUPIMA KWA HIARI VVU

 


Wito umetolewa kwa wananchi kuendelea kujitokeza kupima VVU kwa hiari ili kujua hali zao ili kuendelea kuishi kwa kuzingatia matokeo, kwa wale ambao hawatakutwa na maambukizi ni nafasi kwao kuendelea kuishi ili wasiambukizwe na wale ambao watakutwa na maambukizi  wana nafasi kuendelea kuishi kwa kutumia dawa za kufubaza.

Kauli hiyo imetolewa wakati wa kikao cha pamoja Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu,anayeshughulika na Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe.Adam Kighoma Malima kuhusu kuelekea maandalizi ya siku ya UKIMWI kitaifa, katika kikao kilichofanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.

Ameongeza kusema tafiti zote za miaka mitano zimeonesha wanaume hawajitokezi kupima, na hawajitokezi kuanza kupata dawa, na hivyo kusumbuliwa sana na magonjwa Nyemelezi yanayotokana na virusi vya UKIMWI.

“Virusi vya UKIMWI na UKIMWI upo ni wajibu wa kila Mwananchi kuendelea kuchukua tahadhari,” alibainisha

Aidha kauli mbiu yetu inyosema; JAMII IONGOZE KUTOKOMZEA UKIMWI inatuhamasisha jamii yenyewe ndio iongoze mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI

Akizungumzia kuhusu malezi, ametoa rai kwa wazazi kukaa na familia na kuwaelimisha uwepo wa tatizo hili la UKIMWI.

“Tunajukumu kubwa la kuendelea kutoa malezi bora kwa watoto wetu na kuwajengea misingi ya tabia njema” alifafanua

Awali Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Kighoma Malima amesema maandalizi kuelekea wiki Maadhimisho ya siku ya UKIMWI yanaendelea vizuri

“Lengo ni kupeleka ujumbe kwa wananchi, huku tukitupia jicho kwa kundi la vijana na kwa kushiriki kwao itasaidia kupeleka ujumbe kwa vijana wengine ambao hawakupata fursa ya kushiriki,” alisema

 

 

 

 

 

 

 

Read More

Tuesday, November 14, 2023

SERIKALI KUONGEZA NGUVU MAPAMBANO YA VVU KWA KUNDI LA VIJANA.

 


Imeelezwa kuwa kundi la vijana kati ya umri wa miaka 15 mpaka 24 wanaongoza kwa kuchangia maambikizi mapya ya VVU – UKIMWI ambayo ni sawa na Asilimia 40 (40%).

 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama ameyasema hayo mapema leo Ofisini kwake Jijini Dodoma alipokuwa katika Mkutano na waandishi wa Habari uliyohusu maandalizi ya kilele cha maadhimisho ya siku ya UKIMWI Duniani, yanayofanyika Disemba moja kila mwaka.

Akiongelea kuhusu maadhimisho hayo yanayotarajiwa kafanyika kitaifa Mkoani Morogoro mwaka huu, Waziri Mhagama alisema tafiti zilizopo zinaonesha kuwa kuna kila sababu ya kuongeza nguvu kubwa kwa kundi la vijana ili kuliondoa kwenye uhatarishi wa maambukizi ya vvu.

Aliendelea kusema kuwa maadhimisho ya mwaka huu yatatoa kipaombele kwa kiasi cha cha kutosha kwa vijana kushiriki kikamilifu kwenye majukwaa na matukio yaliyoandaliwa kwenye maadhimisho ya siku ya UKIMWI Duniani mwaka huu nchini kote kutokana na sababu kwamba vijana ndo waingia kwenye maambukizi mapya kwa wingi.

  “Tunapokwenda huko mbele walau kwenye maadhimisho ya wiki ya kuelekea siku ya UKIMWI Duniani, tutoe nafasi ya kuwasikiliza vijana kwa karibu zaidi wakongamane, wakutane na viongozi wa dini na viongozi wa kimila, na wakati mwingine tumekuwa tukifikiri kwamba labda, mienendo ya kimaadili kwa sasa imekuwa ikichagiza vijana wetu kujikuta wanaingia kwenye kundi la maambukizi mapya kwa hivyo kwa kipindi hiki kipaombele kitakuwa kwa kundi la vijana.” Alifafanua Waziri Mhagama.

Aidha, Waziri Mhagama alisema kuwa zaidi ya mara tano tafiti zinaonesha kuwa wanawake wamekuwa na uhiyari wa kupima ukilinganisha na wanaume; ambao hawajitokezi kupima na kuanza matumizi ya dawa, hivyo kuna kila haja ya Serikali kupaza sauti juu kuwaomba kina baba waingiwe na hali ya uhiyari katika kufanya maamuzi ya kupima.

Kwa Upande wake Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Watu wanaoishi na VVU (NACOPHA) Bw. Emmanuel Reuben Msinga alisema kuwa kupitia Kliniki ya Huduma na Kinga (CTC) vijana wanaweza kufikiwa kwa wingi na kupata hamasa ya kupima kwa hiyari, na vijana wanahamasishana kukubali hali zao na namna ya kuwafikia vijana wingine ili wakapime kwa hiayari.

Aliongeza kusema kuwa NACOPHA ina kanda zake nchini na suala la uhamasishaji kwa sasa linafanyika kuanzia ngazi ya Kata, Wilaya na Mikoa.

Kauli Mbiu kwa Maadhisho ya Siku ya Ukimwi Duniani kwa mwaka huu inasema; “JAMII IONGOZE KUTOKOMZEA UKIMWI.”

Read More

Monday, October 30, 2023

PROGRAMU YA KUENDELEZA KILIMO NA UVUVI (AFDP) YAMEWEZESHA TAFITI ZA TEKNOLOJIA YA KISASA ZA KUKABILIANA NA MABADILIKO YA TABIA NCHI.


 

Programu ya kuendeleza kilimo na Uvuvi (AFDP) imewezesha Tafiti za Kiteknolijia kupitia Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Nchini (TARI) katika kuzalisha mbegu za kisasa zenye uwezo wa kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi.

Hayo yamesemwa leo na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibi) Mhe. Ummy Nderianaga wakati wa wasilisho la Taarifa ya Utekelezaji wa Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala Katiba na Sheria, Bungeni Dodoma.

Akitolea mfano aina ya mbegu sita za mahindi ikiwa ni Pamoja na Situka M1, TMV1, STAHA, Bora, T104 na T105, kuwa zikipandwa kwa kufuata kanuni bora za kilimo zinapelekea kuleta matokeao bora na Tafiti zinaonesha kuwa mbegu hizi zina uwezo mkubwa wa ustahimilivu dhidi ya changamoto mbalimbali za mabadiliko tabianchi.

Akiongelea suala la usalama wa chakula, Naibu Waziri Nderianaga alisema kuwa suala hili linakwenda sambamba na kipengele cha Usalama wa mbengu. “tulimaliza hivi punde mkutano wa Chakula Afrika na Tanzania imeonekana kuwa ni kitovu kwenye suala la chakula hivyo kama hatutakuwa na mbegu Bora na nzuri kufikia malengo itakuwa ni kazi.” Alibainisha

Kwa upande Mratibu wa Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Bw. Salimu Mwinjaka, alisema katika sekta ya Kilimo, Programu hii ya kimkakati inalenga kuongeza uzalishaji na upatikanaji wa mbegu bora kwa wakulima, na jitihada kubwa ni kuweka miundombinu ya umwagiliaji ili kuondokana na kilimo cha kutegemea mvua sambamba na kuihamasisha jamii ya wakulima, umuhimu wa kutumia mbegu bora katika kuleta tija na mageuzi ya kilimo.

Akiongoza kikao hicho, Kaimu Mwenyetiki wa Kamati hiyo ya Kudumu ya Bunge ya Utawala Katiba na Sheria, Mhe. Florent Laurent Kyombo Alisema “Tumeona mikakati Mizuri ya Serikali ambayo imewekwa hasa katika suala la mbegu, hii ni kuhakikisha kwamba suala zima la uzalishwaji wa mbegu bora na kwa wakati linafanikiwa.”

Akiongea katika kikao hicho, Mhe. Boniphace Nyangindu Butondo (Mjumbe wa kamati) alishauri Wakala wa Mbegu za Kilimo Nchini (ASA) kuwa na mkakati wa kuzalisha mbegu zenye tija za kutosha na kuangalia mbegu za mazao mengine kama vile Mtama, Mpunga na Pamba na kuzalisha mbegu za kutosha za Asili ili kuweza kukabiliana na mabadiliko yoyote yanayoweza kutokea kwani mbegu nyingi za kisasa zinaonesha kushambuliwa na wadudu mbalimbali.

 Kwa Upande wake Mhe. Dkt. Alice Kaijage (Mjumbe wa Kamati) Alishauri Wakala wa Mbegu za Kilimo Nchini (ASA) kuongeza uwanda wa Tafiti hususani katika zao la Alizeti, kama linaweza kustawi bila tatizo katika mikoa mingine tofauti na Singida, akitolea mfano Mkoa wa Pwani.

Awali akiongelea suala la Mbegu la Asili, Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Mbegu za Kilimo Nchini (ASA) Dkt. Sophia Kashenge Kilenga, Alisema kuna nasaba nyingi sana ya benki ya Mbegu za asili Mkoani Arusha,”Ni kweli kabisa Mbegu za Asili zina sifa ambazo kila mtu anahitaji, na zina nasaba nyingi mchanganyiko zinazopelekea ukuaji wa mbegu kwenda polepole na una mipaka, hivyo kwa ukuaji wa sasa wa idadi ya watu ni vyema kuwa na maeneo maalum ambayo mbegu za asili zitatumika na kwa kulisha idadi kubwa ya watu ni vizuri kutumika kwa mbegu zinazozaa kwa wingi katika eneo dogo.

 

Read More

Thursday, October 12, 2023

KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA AFYA NA MASUALA YA UKIMWI YAIPONGEZA OFISI YA WAZIRI MKUU

 


Kamati ya kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI imeipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) kwa mafanikio makubwa katika kutekeleza afua za VVU na UKIMWI nchini.

Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Stanslaus Nyongo wakati kamati ilipofanya ziara ya kutembelea na kukagua Mpango wa Dreams kupitia Mradi wa Epidemic Control (EPIC) unaotekelezwa na Shirika la Family Health International (FHI360) kwa wasichana balehe na wanawake vijana (AGYW) katika katika Mkoa wa Shinyanga.

Akizungumza mara baada ya kukagua vikundi vya vijana vikiwemo  Sitetereki kilichopo Kata ya Old Shinyanga, Jahazi, Kata ya Ibadakuli na Tunaweza katika Kata ya Kolandoto Mhe. Nyongo amesema lengo la ziara ni kujionea maendeleo ya mradi huo na kuishauri Serikali maeneo ya kuboresha ili kuendeleza jitihada za kuwa na vijana wenye afya nzuri wanaoshiriki katika shughuli za uzalishaji na kujiletea maendeleo yao.

“Tunapongeza kazi kubwa inayofanywa na Rais wetu Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kutoa maelekezo ya kumlinda mtoto wa kike hasa katika gonjwa kubwa la UKIMWI, namna ya kumkomboa mtoto wa kike, kujifunza kazi za ujasiliamali ili kujikwamua katika maisha pamoja  kupaza sauti dhidi ya unyanyasaji wa kijinsia hivyo sisi kama wabunge tumeridhishwa na kazi inayofanywa na Serikali,”Amesema Mwenyekiti huyo.

Naye Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Ummy Nderiananga amewaomba vijana wa kike kuendelea kujiamini na kufanya kazi vizuri kwani Serrikali ya Awamu ya Sita inawajali vijana na kutambua mchango wao mkubwa katika maendeleo ya Taifa.

Akizungumzia ziara hiyo  Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI Mhe. Hassan Mtenga  ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha za kukamilisha na kujengwa kwa miradi mikubwa ya maendeleo huku akiipongeza TACAIDS na wadau wa maendeleo kuwa na mwamko wa kuwawezesha vijana kujikwamua kiuchumi.

“Tumejifunza kitu kwasababu  tunao watu wako tayari kupiga vita janga  kuu la UKIMWI na niishukuru TACAIDS, Mawaziri wenye dhamana na hawa wadada ambao  wameamua kutoka kwenye  sughuli za kuuza bar na kuanzisha biashara  zao sasa uwe mfano  wa kuigwa kwa maeneo mengine,”Amepongeza Mhe. Mtenga.

Vilevile Mjumbe wa Kamati hiyo Mhe. Christina Mnzava amesema wazazi na walezi wana wajibu wa kusimamia malezi sahihi ya watoto ili kuwakomboa katika tabia hatarishi huku  akiupongeza Mpango wa Dream kwa kuamua  kuwafikia mabinti katika maeneo yao akishauri mradi huo kuongeza wigo na kuwafikia vijana wengine  waliopo Vijijini .

“Sisi kama wazazi na walezi tunaweza kuwakomboa watoto wetu katika tabia hatarishi ambazo wanazipata mtaani kuna wengine walikuwa wanauza miili yao, lakini kutokana na mradi huu wamejikwamua wamefundishwa ujasiriamali, kuwekeza tumeona wasichana wamejitambua wanatengeneza sabuni, batiki, vyungu katika vikundi vya Kata za Old Shinyanga, Ibadakuli na Kolandoto kwa kweli wamefanya vizuri,”Ameeleza Mjumbe huyo.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe Christina Mndeme amesema Serikali ipo tayari kushirikiana na Mashirika yasiyokuwa ya kiserikali kuondoa unyanyapaa na ubaguzi kwa watu wanaoishi na VVU ambao upo juu, kuwajengea vijana uwezo wa kiuchumi ili muda mwingi wautumie kwenye uzalishaji na sio kwenye mambo yanayoweza kuwasababishai maambukizi ya VVU,kuelimisha jamii kuacha mila potofu ambazo zinasababisha ukatili wa kijinsia.

Kwa upande wake Mshauri Mwandamizi wa Mpango wa Dreams kupitia Mradi wa Epidemic Control (EPIC) unaotekelezwa na Shirika la Family Health International (FHI360) Bi. Agnes Junga amefafanua kuwa lengo la Mpango huo ni kupunguza maambukizi ya Virusi vya UKIMWI kwa wasichana kuanzia umri wa miaka Tisa hadi 24.

“Mpango huu ulizinduliwa 2014 ukilenga kupunguza maambukizi ya virusi vya UKIMWI kwa Nchi 13 za Bara la Afrika ikiwemo Tanzania ambapo tulianza na Halmashauri Sita na hadi sasa tumefikia Halmashauri 12. Shirika la (FHI360) kwenye mradi wa EPIC tunatekeleza Dreams katika Mikoa miwili ya Shinyanga ndani ya Halmashauri Tano na Iringa katika Halmashauri mbili na tunawafikia wasichana kuanzia miaka 15 hadi 25 walio nje ya shule pamoja na wazazi au walezi na jamii kwa ujumla tuhakikishe msichana anafikia ndoto zake.

Aidha akizungumza kwa niaba ya wanakikundi kutoka Vikundi vya Mabinti Balehe na Wanawake Vijana vya Sitetereki, Tunaweza na Jahazi mwanakikundi Sungi Leonard amesema uanzishwaji wa vikundi hivyo vimewasaidia kama mabinti kujitambua, kufahamu elimu ya afya, kuwajengea uwezo wa kukabiliana na vitendo vya kikatili pamoja na kuchukua tahadhari dhidi ya maambukizi mapya ya VVU na kuwawezesha kiuchumi.

“Nilikutana na mwezeshaji kiuchumi na mwelimishaji rika nikapata elimu ya ukatili wa kijinsia, umuhimu wa upimaji wa afya, matumizi sahihi ya kinga, magonjwa ya ngono na VVU ambayo imenisaidia kujitambua kama binti. Pia nilifanikiwa kujiunga katika kikundi cha Sitetereki nikajifunza kutengeneza batiki kazi ambayo inanipatia kipato na ninamudu mahitaji yangu tofauti na ilivyokuwa awali,” Ameshukuru Mwanakikundi huyo.

Read More

Wednesday, October 11, 2023

WAZIRI MHAGAMA, AZINDUA MUONGOZO WA UWEKEZAJI MKOA WA MANYARA.


 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama ametoa wito kwa watendaji wa Serikali; kujipanga na kuhakikisha Muongozo wa uwekezaji kwa Mkoa Manyara unawafikia wananchi wote ili kufanya kazi kwa tija.

Kauli hiyo ameitoa Mkoani Manyara wakati wa Ufunguzi wa wiki ya Kitaifa ya Vijana tukio alilolifanya kwa niaba ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa.

“Tunataka Muongozo huu uweze kutoa fursa nyingi kwa vijana ili uweze kujenga kizazi ambacho kitatatumia Muongozo huu kwa muda mrefu” alieleza.

Aliendelea kusema kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu italeta timu ya baraza la uwezeshaji kiuchumi, timu ambayo itasaidia kujenga uwezo kwenye dhana kutengeneza vitu asilia (Local content) ili kuongeza tija na kuweka mazingira wezeshi yatakayochochea wanawekezaji.

“Makapuni yaliyowekeza katika Mkoa wa Manyara yaone namna ya kutumia fedha zile zinazorudi kwa jamii, kwa kuwekeza katika vikundi vya vijana wabunifu ili kupitia muongozo wa uwekezaji usaidie kuleta tija kwa vijana na maendeleo ya Mkoa,” alihimiza

Akizungumza kuhusu madhimisho ya wiki ya vijana, Mhe. Waziri Mhagama amesema ubunifu aliyouona wakati alipotembelea Mabanda, hasa uliofanywa na kijana Said Mussa wa kubuni namna ya kutengeneza taa za magari zilozoharibika na kurudisha katika muonekano mpya ni ubunifu mzuri.

“Kijana Huyu wa Kitanzania akifanikiwa kuhuisha teknolojia hiyo basi tutakuwa uwezo huko mbele kujenga viwanda vidogo vidogo vingi vya kuzalisha taa za magari nakusaidia kuongeza pato la kigeni na Kubrand Tanzania ya Mhe. Samia Kupitia Ubunifu wa Vijana,” alisema.

Namshukuru sana Mhe. Mhe. Prof. Joyce L. Ndalichako na Katibu Mkuu Mhandisi Cyprian John Luhemeja kwa kuridhia kumpatia Mkopo kijana huyu ili kuhakikisha anafanya vizuri katika ugunduzi alioufanya.

Naye Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi vijana ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Joyce Ndalichako amesema wiki ya vijana inalenga kutambua Mchango wa Waasisi wa Taifa Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere na Hayati Shekh Abeid Amani Karume.

 

Ameongeza kusema Maadhimisho ya wiki ya vijana Kitaifa ya Mwaka 2023 yanayofanyika Mkoani Manyara, kauli mbiu yake ni,” Vijana na Ujuzi Rafiki kwa Mazingira na Maendeleo Endelevu”. Maadhimisho ya vijana yanakutanisha vijana na wananchi wa Mikoa yote ya Tanzania Bara na Visiwani ambapo vijana wanapata fursa ya kubadilishana uzoefu. Ni fursa kwa Serikali na Wadau kutambua mchango mzuri wa vijana kwa maendeleo ya nchi yetu.

 “Natoa shukrani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuwajali na kuthamini vijana wa Tanzania kwa matendo kwa kuhakikisha vijana wanapatiwa mitaji ya kuendeleza biashara zao au kwa kuanzisha shughuli za maendeleo,” alibainisha

Awali Mkuu wa Mkoa wa Manyara Bi, Queen Sendiga alimshukuru Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt, Samia Suluhu Hassan kwa kuchagua Manyara kuwa Mwenyeji wa Kilele cha Madhimisho ya Siku ya vijana kitaifa, Mwenyeji wa Misa Maalumu ya Kumbukizi ya Baba wa Taifa, na Mwenyeji wa Killele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru.

“Moja ya mambo makubwa yatakayoachwa katika Mkoa wa Manyara, kutokana na kuwa Mwenyeji wa kilele cha Mbio za Mwenge wa uhuru ni pamoja na Ujenzi wa uwanja Mkubwa wa kisasa wa Mpira wa Miguu ambao Umejengwa kwa hadhi,” alisema

Read More

Friday, October 6, 2023

IDARA YA MENEJIMENTI YA MAAFA NCHINI YASHIRIKISHA UJUZI KWA WANAFUNZI NA WAKUFUNZI KUTOKA MALAWI


 

Idara ya Menejimenti ya Maafa Nchini yashirikisha ujuzi wa masuala ya usimamizi wa maafa kwa wanafunzi na wakufunzi kutoka Chuo cha Ukamanda na Unadhimu Jeshi la Ulinzi la Malawi walifanya ziara yao ya mafunzo nchini Tanzania.

 Akizungumza wakati wa kikao kilifanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Waziri Mkuu Jijini Dar es salaam kilicholenga kubadilishana uzoefu katika usimamizi wa maafa kati ya wataalam wa Ofisi ya Waziri Mkuu na ujumbe wa wanafunzi na wakufunzi kutoka chuo hicho, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Luteni Kanali Selestine Masalamado amesema mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo na kubadilishana uzoefu katika masuala ya usimamizi wa maafa na kueleza kuwa ujio wao ni moja ya ishara kuwa nchi hizo mbili zimeendelea kuwa na mahusiano mazuri na kupongeza hatua hiyo.

 “Hatua hii ya kukutana pamoja na kupeana uzoefu imetufariji na inaimarisha umoja baina yetu, hivyo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaendelea kuimarisha mahusiano yaliyopo na Serikali ya Jamhuri ya Malawi katika masuala ya menejimenti ya maafa kwa kuhakikisha tunatumia fursa zilizopo katika kuyafikia malengo hayo,”alisema Kanali Masalamado.

Aidha alitumia fursa hiyo kuwaeleza kuwa, Tanzania imeendelea kuimarisha mifumo ya kiutendaji katika kukabiliana na maafa huku akisema uwepo wa Teknolojia ya TEHAMA umeendelea kurahisisha masuala ya usimamizi wa maafa nchini hasa upande wa mawasilisno wakati wa dharura kwa kuanzishwa kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharula katika Ofisi ya Waziri Mkuu ambacho kimerahisisha mawasiliano kwa ajili ya upatikanaji wa taarifa za maafa nchini.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo cha Ukamanda na Unadhimu Jeshi la Ulinzi la Malawi na kiongozi wa msafara huo kutoka chuo hicho, Brigedia Jen. Luke Mwetseni amepongeza namna nchi ya Tanzania inavyoendelea na masuala ya menejimenti ya maafa huku akishukuru namna Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilivyowasaidia wakati wa maafa ya Kimbunga Freddy kilichotokea Machi, 2023 ambapo Tanzania ilitoa misaada mbalimbali ikiwemo ya kibinadamu na fedha kwa Taifa hilo.

“Serikali ya Tanzania ilitushika mkono wakati wa maafa ya Kimbunga Freddy kwa kutupatia Mablanketi, madawa ya binadamu, fedha pamoja na ndege kutoka jeshi la Wananchi wa Tanzania zilizosafiri kuja Malawi kwa lengo la wokozi, tunashukuru sana kwa namna mlivyojali, hii inaonesha namna mlivyojipanga katika masuala ya menejimenti ya maafa hongereni sana,” alisema Brig Jen. Mwetseni

Aidha alimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake makini katika masuala ya Menejimenti ya maafa na kusema kuwa wanaitumia Tanzania kama nchi ya mfano kuja kujifunza kwa vitendo namna inavyoratibu masuala ya maafa ili kuendelea kuwa na jamii stahimilivu katika maafa.

“Kwa kutambua mchango wenu tumekuja na tuzo hii maalum kwa ajili ya kuonesha kuwa tulitambua na kujali Serikali yenu ilivyotutendea sisi watu wa Malawi wakati wa maafa, tunaahidi kuendelea kushirikiana katika kuimarisha umoja huo,” alisisitiza Brigedia Jen. Mwetseni.

Awali alisema kuwa, ujio wao nchini unatija kubwa na utasaidia wanafunzi hao kuongeza ujezi utakao wasaidia wanapoelekea kumaliza mafunzo katika chuo hicho pamoja na kuwaongezea maarifa katika utendaji kazi wao.

 

Read More

Thursday, October 5, 2023

KATIBU MKUU KIONGOZI AIPONGEZA OFISI YA WAZIRI MKUU KWA USIMAMIZI MZURI WA UJENZI WA MJI WA SERIKALI

 


Katibu Mkuu Kiongozi Mhe. Balozi Dkt. Moses Kusiluka ameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Uratibu na Usimamizi mzuri wa Ujenzi wa Mji wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma.

Ametoa pongezi hizo mapema leo, alipokuwa katika ziara maalum ya Makatibu Wakuu ya kutembelea mji wa Serikali Mtumba Dodoma ambapo alisema mafanikio ya mradi huu wa ujenzi wa Mji wa Serikali ni kukamilika kwa ukamilifu wake akitolea mfano ujenzi wa Uwanja wa Mashujaa kuwa ni alama kubwa ambao utatumika kwa mambo mengi ikiwa ni pamoja na wageni kujifunza nini ambacho Tanzania imefanya.

“Tunathamini kazi yenu kubwa sana mnayofanya, kama tulivyosema awali kwenye Wasilisho, hii kazi inahitaji Uratibu kwa Sababu ni kazi ya Serikali, siyo kazi ya mmoja kuwa amemaliza na wengine kujisikia vibaya, tunashukuru kwa kutupitisha kwenye kazi kuanzia mwanzo, tumeona juhudi kubwa za wataalamu wetu na wasimamizi lakini pia tumeona kazi kubwa iliyopo mbele na tunatambua kwamba baadhi ya wadau wanakaribia kumaliza kazi zao.” Alisema Mhe. Balozi Kusiluka.

 Aliendelea kusema kuwa bado kuna muda wa kutosha wa kutatua Changamoto ndogo zilizobainika katika ziara hiyo; na kusisitiza kuutazama mradi huo kwa ujumla wake kama Serikali moja, na kazi ya uratibu ikiendelea lakini pamoja na kuimarisha timu ya wataalamu wa ngazi zote katika ujenzi na kuwasikiliza, “Ni Fursa Pekee ambayo tumepewa ya kujenga Makao Makuu ya Serikali mapya  na Serikali imetoa fedha nyingi kwa hivyo ni lazima sisi wataalam tufanye kazi inavyopaswa.” Alisisitiza.

Alimshukuru Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha za kutekeleza mradi huo, na kuwapa uhuru wataalam kufanya kazi ya kitaalam inavyopaswa, na kushauri wadau wengi kushiriki katika kazi hiyo pamoja na kujadili mambo ya kitaalam ili watu wengi waweze kujifunza

Kwa Upande wake Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonaz alisema swala la ushirikishwaji wa wataalam katika ujenzi wa mji wa Serikali ni swala la muhimu sana, na wadau mbalimbali wanashirikishwa kwa ajili ya kuja kuwekeza katika maeneo mbali mbali  ambayo yametengwa katika mji huo wa Serikali,na majengo hayo ya Mji wa Serikali yapo katika hatua mbalimbali za ukamilishwaji.

 

Read More

Tuesday, September 26, 2023

WANANCHI WATAKIWA KUCHUKUA TAHADHARI MVUA ZA EL NINO.

 


Serikali imezitaka taasisi zinazohusika kutoa huduma wezeshi au saidizi  kuimarisha mifumo mbalimbali kama ya  usafiri, mawasiliano, nishati na maji  ili kuhakikisha shughuli za kijamii na kiuchumi haziathiriki wakati wa maafa.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama wakati alipofanya ziara ya kutembelea na kukagua miundo mbinu ya mito mikubwa na mifereji ikiwa ni hatua ya kujiandaa na mvua za El Nino zinazotarajiwa kunyesha mapema mwaka huu mara baada ya kufungua Kikao Kazi cha Kamati za Usimamizi wa Maafa ngazi ya Mkoa katika Kuzuia na Kupunguza madhara ya El Nino kilichofanyika Jijini Dar es salaam.

Mhe. Jenista amesema  matukio ya maafa yanatokea na kusababisha madhara katika ngazi ya jamii ambapo Serikali za Mitaa, kuanzia Kitongoji, Mtaa au Kijiji na Jiji, Manispaa, Mji na Wilaya zinawajibika moja kwa moja.

“Hatua za kuzuia madhara zinatekelezwa zaidi na viongozi na wataalam kwa  kushirikiana na wadau na wananchi katika maeneo haya. Tumekutana leo  kukumbushana wajibu muhimu mlio nao kwa kila mmoja kuwajibika katika  eneo lake ili kuokoa maisha na kulinda mali za wananchi. Tukumbuke kuwa  Mkoa unaingia kusaidia juhudi za Halmashauri husika pamoja na  kushirikisha uratibu wa msaada kutoka ngazi ya Taifa endapo madhara  yatakuwa yamezidi uwezo wa rasilimali katika eneo husika.

Pia  amewasisitiza wananchi  kila mmoja kuchukua hatua katika eneo lake, akisema  mfumo wa Serikali umezingatia wajibu wa sekta na taasisi yenye  jukumu kisera na kisheria kuchukua hatua ili kuokoa maisha na mali za jamii  yetu kutokana na matukio ya maafa.

Katika hatua nyingine amezitaka taasisi zinazohusika kuwa mstari wa mbele  kuchukua tahadhari na kujiandaa  kikamilifu kwa kuweka utaratibu wa pamoja ikiwa ni pamoja na kuwa na mpango wa dharura wa utendaji na utaratibu wa mawasiliano wakati wa dharura ili ziweze kuchukua hatua kwa haraka na ufanisi ili kuokoa maisha.

“Historia inaonesha madhara yanayoweza kutokea katika sekta kutokana na uwepo wa El Nino utakaosababisha mvua kubwa ni pamoja na  Mafuriko kuharibu miundombinu mbalimbali, madhara ya kiafya, kiuchumi, kijamii na upotevu wa mali,  Maporomoko ya ardhi kuathiri makazi, mazingira, mashamba, usafiri na shughuli zingine hususani uchimbaji madini, Magonjwa ya milipuko kwa binadamu na wanyama na wadudu waharibifu wa mazao na mimea,” Amesema Mhe. Jenista.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam,Albert Chalamila ameahidi kutekeleza maagizo yalyotolewa na Waziri huyo katika kuhakikisha miundo mbinu yote ya maji pamoja na maeneo hatarishi yanafanyiwa matengenezo ili kuepuka madhara makubwa yanayoweza kujitokeza wakati wa mvua za El Nino hivyo akawahimiza wananchi kutoa ushirikiano kwa wakandarasi watakapofika katika maeneo yao kufanya maboresho hayo.

“Hakikisha tunajidhatiti kutunza mazingira yetu na miundo mbinu hasa hii ya mito tunaweza kupata kipindu pindu na jambo tunalokabiliana nalo kwa sasa hapa Tabata ni wimbi la vibaka lakini tumeandaa timu  za ulinzi kupitia ulinzi shirikishi wa Sungusungu,”Ameeleza Mkuu wa Mkoa huyo.

Akitoa maoni yake mkazi wa Mji Mpya-Mnyamani ameiomba Serikali kuhakikisha inaweka miundo mbinu imara ya vivuko na barabara katika maeneo ya mitaa ili kusaidia wananchi kuvuka na kupata huduma wakati wa maafa.

Aidha Mkazi wa Tabata Bw. Shelemia Gwassy ameishukuru Serikali kupitia Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu na Mkuu wa Mkoa kwa kufanya ziara ya kushitukiza katika maeneo ya Tabata na kukagua mito inayopitisha maji ikiwemo Mto Msimbazi, Mto Mpiji, Mto Ng’ombe na Mfereji wa Jangwani huku akiiomba kuweka utaratibu mzuri wa uzoaji taka katika makazi ya wananchi.

 

Read More

Monday, September 25, 2023

KAMATI ZA MAAFA MKOA ZAJENGEWA UWEZO WA KUZUIA ,KUJIANDAA NA KUKABILIANA NA MADHARA YA EL-NINO

 


Kamati za maafa Ngazi ya Mkoa zajengewa uwezo juu Kuimarisha Uwezo wa Kuzuia na Kujiandaa Kukabiliana na Madhara ya mvua za El-nino kufuatia utabiri wa mwelekeo wa mvua za msimu wa Vuli kwa kipindi cha mwezi Oktoba hadi Desemba, 2023 kuonesha uwepo wa El-Niño itakayosababisha vipindi vya mvua kubwa kwa mwezi Oktoba mpaka Disemba 2023 na kuendelea mpaka Mwezi Januari 2024.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha utekelezaji wa Mpango wa Kuimarisha Uwezo wa Kuzuia na Kujiandaa Kukabiliana na Madhara ya mvua za El-nino kwa Kamati ya Usimamizi wa Maafa mkoa wa Morogoro Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Ummy Nderiananga amesema kuwa, Serikali ilianza kutekeleza hatua za kuzuia madhara haya toka mwezi Julai 2023 wakati taarifa ya awali ya dalili za uwezekano wa uwepo wa El Nino ilipotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania.

Kikao kazi hichi kinafanyika kwa siku mbili kuanzia tarehe 25 hadi 26 septemba, 2023 na kuhusisha wajumbe wa Kamati ya Usimamizi wa Maafa ngazi ya Mkoa wakiwemo; Wakuu wa Wilaya, Katibu Tawala wa Mkoa, Wakurugenzi wa Halmashauri, Wenyekiti wa Halmashauri pamoja na washiriki kutoka washiriki kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, wawezeshaji kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Jeshi la Polisi Tanzania, TMA na DarMAERT Pamoja na Wawakilishi wa Taasisi mbalimbali na Viongzozi wa dini.

Alisema kuwa zoezi hilo limefanyika kwa mikoa 14 inayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka ambayo ni Kagera, Geita, Mwanza, Shinyanga, Kusini mwa mkoa wa Simiyu, kaskazini mwa mkoa wa Kigoma, Dar es Salaam, Tanga, Pwani (ikiwemo visiwa vya Mafia) na kaskazini mwa mkoa wa Morogoro.

 

“Kikao kimezingatia wajibu mlio nao kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa Maafa namba 6 ya Mwaka 2022 na Kanuni zake, ambayo imeanzisha Kamati za Usimamizi wa Maafa za Mikoa, Wilaya, Kata na Vijiji au Mitaa. Jukumu la msingi la Kamati hizi ni kuchukua hatua kwa lengo la kuzuia na kupunguza madhara ya majanga ya aina zote na kujiandaa kukabili na kurejesha hali kwa ubora zaidi endapo maafa yatatokea.” alisisitiza Mhe. Nderiananga.

Naibu Waziri aliongezea kuwa, kazi hiyo imezingatia uwajibikaji wa pamoja ambapo, Ofisi ya Waziri Mkuu imeshirikiana na Wizara za kisekta na Taasisi za Serikali na Wadau kuendelea kuimarisha hatua ambazo zinaendelea kuchukuliwa na Mamlaka za Mikoa na Serikali za Mitaa katika Mikoa husika.

Ametumia nafasi hiyo kuzikumbusha kamati za maafa zote kuendelea kujiandaa na kukabili maafa nchini kwa kuimarisha mifumo ya utendaji, rasilimali zilizopo huku wakitambua masuala ya menejimenti ya maafa ni jukumu la kila mmoja hivyo upo umuhimu wa kuunganisha nguvu ya pamoja.

“Ni jukumu letu sote katika nafasi zetu kama wajumbe wa Kamati za Usimamizi wa Maafa kutekeleza kimamilifu hatua za kuchukua katika sekta zenu kwa kuzingatia kuwa madhara yanaweza kuongezeka endapo hatua stahiki hazitachukuliwa kwa wakati. Natarajia kuwa baada ya kikao kazi cha leo, Kamati hasa ngazi ya Halmashauri zote za Mkoa zitaimarisha utekelezaji wa hatua za kuzuia madhara ili kuhakikisha tunaokoa maisha na mali kwa ustahimilivu wa taifa,”alisema.

Alizikumbusha Taasisi zinazohusika kuendelea kuwa mstari wa mbele wakati wa tukio la maafa zinapaswa kujiandaa kikamilifu kwa kuweka utaratibu wa pamoja ikiwa ni pamoja na kuwa na mpango wa dharura wa utendaji na utaratibu wa mawasiliano wakati wa dharura ili ziweze kuchukua hatua kwa haraka na ufanisi ili kuokoa maisha.

“Taasisi hizo ni pamoja na zile zinazohusika na huduma ya utafutaji na maokozi, usalama wa wananchi, afya na makazi ya muda na huduma zingine za kijamii. Aidha, taasisi zinazohusika kutoa huduma wezeshi au saidizi pamoja na kuimarisha mifumo kama vile usafiri, mawasiliano, nishati na maji zinakumbushwa kujiimarisha ili kuhakikisha shughuli za kijamii na kiuchumi haziathiriki wakati wa maafa. Taasisi saidizi zina wajibu wa kuwezesha taasisi zenye jukumu ongozi katika kuokoa maisha na mali ili zitekeleze majukumu kwa ufanisi pamoja na kupunguza athari kwa jamii”,Alisisitiza

Sambamba na hilo aliwaeleza kuwa hatua hiyo ni muhimu ili kuhakikisha juhudi zinazochukuliwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, katika kuimarisha uchumi na huduma za kijamii katika ujenzi wa Taifa letu zinakuwa stahimilivu dhidi ya maafa. Ni dhahiri kuwa hatua zinazochukuliwa zitachangia katika juhudi zake katika kuongoza na kusimamia utekelezaji wa mipango ya Serikali pamoja na maelekezo ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi 2020-2025 kwa manufaa makubwa kwa wananchi na tija iliyokusudiwa.

 

“Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2020 hadi 2025 kuhusu masuala ya Menejimenti ya maafa nchini kifungu cha 107, kinaeleza katika kipindi cha miaka mitano ijayo, Chama Cha Mapinduzi kitaendelea kuhakikisha Serikali inaendelea kusimamia kikamilifu vyombo vinavyoshughulika na maafa kuwa na mpango wa utayari wa kuzuia, kujiandaa, kukabili na kurejesha hali haraka pindi maafa yanapotokea kwa kuchukua hatua mbalimbali” alibainisha Mhe. Nderiananga.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Malinyi Mhe. Sebastian Waryuba akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Morogoro ameeleza kuwa mkoa umejiandaa katika kukabiliana na maafa na kueleza wataendelea kutoa elimu kwa umma juu ya uwepo wa mvua hizo huku akitahadharisha wakazi wa Malinyi kuendelea kuchukua tahadhari kwa kuzingatia ni maeneo yanayoathiriwa na maafa ya mvua mara kwa mara.

Naye, Mkuu wa Wilaya ya Morogoro Mhe. Rebeca Nsemwa ametahadharisha wakazi wa maeneo yanayoathiriwa kwa wingi, kuendelea kuzingatia ushauri wa wataalam ikiwemo kuhama maeneo hatarishi na kutotupa taka zinazosababisha kuziba kwa mifereji ya maji na kuimarisha kingo zote.

 

 

Read More

Friday, September 22, 2023

NAIBU WAZIRI NDERIANANGA: ENDELEENI KUZINGATIA UBORA KATIKA UZALISHAJI WA MBEGU

 


Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Ummy Nderiananga ameupongeza uongozi wa Wakala wa Taifa wa Uzalishaji na Uendelezaji wa mbegu za kilimo (ASA) kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuzalisha na uendelezaji wa mbegu nchini huku akiwasihi kuendelea kuzingatia ubora na weledi katika majukumu ya kuzalisha mbegu bora hizo ili kuendelea kuwa na uhakika wa chakula cha kutosha nchini. 

Ametoa pongezi hizo wakati wa ziara yake ya kikazi kufuatili shughuli za utekelezaji wa Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo na Uvuvi ya AFDP ambayo inaratibiwa na ofisi yake na kutekeleza katika mikoa mbalimbali nchini ikiwemo Morogoro.

Akiwa katika ziara hiyo alitembelea Kituo cha Kuendeleza Ukuzaji Viumbe Maji Kingolwira, Wakala wa Taifa wa Uzalishaji na Uendelezaji wa mbegu za kilimo (ASA) Pamoja na Taasisi ya Kuthibiti Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI) zilizopo Mkoani Morogoro.

Mhe.Ummy amesema upo umuhimu wa kuendelea kuunga mkono Programu ya kuendeleza sekta ya Kilimo na Uvuvi nchini kwa kuzingatia inaongeza tija hasa katika kuhakikisha kunakuwa na mbegu bora nchini. 

“Ofisi ya Waziri Mkuu tunaendelea kufanya uratibu na kutathmini ya programu hii ambayo ni ya miaka sita hivyo endeleeni kufanya kazi vizuri, kwa weledi huku mkiunga jitihada za Mhe Rais za kuona Tanzania inakuwa ghala kubwa la chakula, Serikali haita waacha nyumba, inaendelea kuunga mkono jitihada hizi.” alisema Mhe. Nderiananga

Aidha aliwataka kuendelea kuzingatia ubora na viwango katika utekelezaji wa majukumu ya uzalishaji wa mbegu bora na zinazoendana na mahitaji halisi.

 “Eneo la mbegu ni muhimu sana, bila kuwa na mbegu nzuri hatuwezi kuwa na matokeo ya chakula kizuri, hivyo ninawapongeza mnafanya kazi nzuri endeleeni maana tunategemea sana sekta yetu ya kilimo ili kuendelea kuwa na uhakika wa chakula nchini,”alisisitiza.

Kwa upande wake Mchumi Mwandamizi kutoka wa Wakala wa Taifa wa Uzalishaji na Uendelezaji wa Mbegu za Kilimo (ASA) Bw. Edmund Kayombo akizungumza kuhusu wakala hiyo amesema umeendelea kutoka huduma za kuongeza uzalishjaji na usambazanji mbegu bora, kuhamasisha sekta binafsi kushiriki katika uzalishaji na usambazaji wa mbegu bora, kuhamasisha wakulima kutumia mbegu bora na kushirikiana na kituo cha utafiti ili kuhakikisha mbegu mpya zinazaliwashwa na kusambazwa kwa wakulima.

“Wakala wa Mbegu za kilimo una jumla ya mashamba 14 ikiwemo mashamba ya kilimi yaliyopo Nzenga, Msungula (Kasulu), Chalinze, Nane nane - Morogoro, Tanganyika, Dabaga kilosa, Arusha (Tengelu), Namtumbo (Songera), Njombe, ambayo yanajumla ya ukubwa wa hekta 16,909,” alisema Kayombo.

Read More