Saturday, February 8, 2025

WAZIRI LUKUVI AMPA KONGOLE MHE. WAZIRI MKUU

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mheshimiwa William Lukuvi amemshukuru na kumpongeza Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muugano wa Tanzania Mheshimiwa Kassim Majaliwa kwa kuendelea kusimamia na kuratibu shughuli za Serikali.

Waziri Lukuvi ametoa pongezi hizo wakati wa Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu uliofanyika katika Ukumbi wa Ofisi hiyo Ngome Jijini Dodoma.

Alisema kuwa kazi ya Waziri Mkuu kwa Mujibu wa Katiba ni kuratibu shughuli zote za Serikali na chini yake yupo Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati na watendaji wa Ofisi yake ambayo wanatekeleza majukumu hayo kwa weledi na ufanisi mkubwa.

“Wakati wa uratibu wa shughuli za Maafa watendaji mmefanya kazi kwa ushirikiano Mkubwa chini ya Uongozi wa Mhe. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa na mambo yameenda vizuri nchi nzima,” alisema Waziri Lukuvi

Aidha alifafanua kuwa kazi ya Ofisi ya Waziri Mkuu ni kuratibu Serikali ili kuwafahamisha namna Serikali inavyoendelea kutekeleza majukumu na kuhudumia wananchi.

"...kwa kuwa tuna nafasi ya kupata taarifa na kuzifanyia uchambuzi ili kujulisha umma kwa njia mbalimbali ikiwemo vyombo vya habari basi tuendelee kuratibu vyema taarifa na kuzitoa kwa usahihi ndiyo jukumu letu kubwa na lamsingi lazima tujipange ili ziweze kutoka kwa wakati alisema,” Waziri Lukuvi.

Naye Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi katika maneno ya utangulizi amesema Viongozi wa Ofisi ya Waziri Mkuu wamewatengeneza mazingira mazuri kwa watendaji kufanya kazi kwa furaha na amani.

Pia ameahidi kuimarisha ushirikiano miongoni mwao ili kuyafikia maelengo ya ofisi na Serikali kwa ujumla.

"Tuimarishe ushirikiano miongoni mwetu ili kazi zetu ziende kwa wepesi na ufanisi kwa kuamini kila mmoja ana mchango chanya kuhakikisha malengo yanatimia," alisema Dkt. Yonazi.

 


Read More

Tuesday, February 4, 2025

DKT. YONAZI AWAKUMBUSHA WATUMISHI OFISI YA WAZIRI MKUU KUENDELEA KUTEKELEZA MAJUKUMU KWA WELEDI



Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya sera, bunge na uratibu Dkt. Jim Yonazi amewakumbusha watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa ushirikiano, upendo, furaha na amani ili kuyafikia malengo ya ofisi hiyo.

Dkt. Yonazi ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na Watumishi Ofisi yake wakati wa mkutano wake na watumishi hao uliofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi iliyopo Njedengwa Jijini Dodoma.

Dkt. Yonazi amesema ipo haja ya kila mtumishi kujifanyia tathmini katika utendaji wake wa kazi huku akizingatia miongozo na kanuni za utumishi wa umma na kusema kuwa, kila mtumishi anawajibika katika kuhakikisha ofisi inapata matokeo iliyoyakusudia na kwa ufanisi.

“Ni wakati sahihi kila mmoja kuilinda furaha aliyonayo awapo mahali pa kazi, isingefaa utoke nyumbani huna furaha na ufike eneo la kazi ukose furaha, ni vyema kuja eneo la kazi na kuipata furaha mara mbili  kwa kuzingatia mazingira yaliyorafiki katika kutekeleza majukumu,” alisema Dkt. Yonazi

Aliongezea kuwa kila mtumishi wa umma awe na desturi ya kuheshimu nafasi ya mwingine bila kujali tofauti zinazoweza kuwepo miongoni mwa watumishi hao.

“Ni vyema kila mtu akajali mwingine na ikumbukwe hakuna mtu mwenye uwezo mdogo wa kufanya kazi, jambo la msingi ni kuhakikisha ule uwezo uliopewa na Mwenyezi Mungu na Mafunzo mbalimbali unatumia vizuri na kuhakikisha unaleta matunda mazuri na kuleta maendeleo kwa Nchi yetu” alisema Dkt, Yonazi.

Sambamba na hilo aliwaeleza watumishi hao kuwa kila mmoja ni kiongozi katika eneo lake la kazi hivyo abebe dhamana hiyo kwa weledi na ufanisi mkubwa.

“.....kila mtumishi aliyepo hapa ndiye Katibu Mkuu kwenye eneo lake, kwa kubeba imani ya kwamba ni Katibu Mkuu anapaswa kuwa na nidhamu na bidii katika kazi ikiwa ni pamoja na kuwa mwaminifu,” alisema.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo Dkt. James Kilabuko katika neno lake la utangulizi amewaasa Watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu kuendelea kufanya kazi kwa bidii na weledi na kuzingatia sheria za utumishi wa Umma huku akiwasihi kuimarisha umoja na mshikamano ili kuiletea Serikali maendeleo yake.

Naye Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la Ofisi ya Waziri Mkuu Bi, Numpe Mwambenja ameomba watumishi kuendelea kujitathimini mienendo yao katika utumishi wa Umma kwa kufanya kazi vizuri na nidhamu na kuheshimu viongozi huku wakiheshimiana wao kwa wao.

Bi. Numpe alitumia nafasi hiyo kuupongeza uongozi wa Ofisi ya Waziri Mkuu kwa namna unavyojali maslahi ya watumishi na ustawi wao kwa ujumla na kuwasihii watumishi kuendelea kutimiza wajibu kwa kuzingatia kauli ya “hakuna haki bila wajibu”.






Read More

Wednesday, January 8, 2025

WAZIRI LUKUVI AWEKA JIWE LA MSINGI UJENZI JENGO JIPYA LA MAHAKAMA YA WILAYA MKOANI

 


Imeelezwa kwamba hali ya amani utulivu na ushirikiano unaosimamiwa na Viongozi Wakuu wa Nchi imesaidia katika kuleta chachu kubwa ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo Tanzania Bara na Tanzania Visiwani.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera Bunge na Uratibu) Mhe. William Lukuvi ametoa kauli hiyo leo  wakati wa hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi katika ujenzi wa jengo jipya la Mahakama ya Wilaya ya Mkoani ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Miaka 61 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya mwaka 1964.

Amefafanua kwamba uongozi wao bora; hatuna budi kuendelea kuwaombea viongozi wetu, kila mmoja kwa dini yake ili Mwenyezi Mungu awape afya na nguvu ya kuendelea kutuongoza kwa mshikamano.

Waziri Lukuvi amesema, “chini ya uongozi wao Tanzania Bara imetulia na Tanzania Visiwani imetulia na hivyo kuwezesha haya kufanyika na kuendelea kuchochea maendeleo makubwa, mwenye macho haambiwi tazama.”

Sote ni mshahidi wa hatua kubwa za maendeleo zinazoendelea kutekelezwa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kupitia uongozi wa awamu ya nane chini ya Mhe. Daktari Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.

Waziri Lukuvi amesema, mafanikio ya Serikali ya awamu ya nane yanaonekana wazi katika nyanja za siasa na utawala bora, uchumi, huduma za kijamii na namna utamaduni wa watu wa Visiwa vya Zanzibar unavyoenziwa na kuheshimika wakati wote.

Aidha Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imechukua hatua za makusudi kuja na mradi wa ujenzi wa jengo hili la Mahakama ya Wilaya pamoja na majengo mengine ya Mahakama za Mikoa na Wilaya kule Unguja na hapa Pemba ili kukabiliana na changamoto za miundombinu ya majengo.

“Ujenzi wa jengo hili ni sehemu ya utekelezaji wa Mradi wa ujenzi wa majengo saba ambao ulipangwa kufanyika katika mwaka wa fedha wa 2023/2024 alisema,” Waziri Lukuvi.

Kwa upande wake Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla, Jaji Mkuu wa Zanzibar amesema Rais. Mhe. Daktari Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi amewaheshimisha kwa kuwajengea majengo saba ya Mahakama za Mkoa na wilaya katika visiwa vyote vya unguja na pemba.

“Tumekusudia kusogeza huduma kwa wananchi kwa kujenga mifumo imara ya usimamizi wa haki ili kuboresha huduma zetu za mahakama kuwa za kisasa ,” alisema Mhe, Jaji, Khamis.

Naye Mhe, Valentina Katema, Mrajis wa Mahakama Kuu Zanzibar, amesema miundo mbinu ya majengo ya mahakama ipo katika muundo zamani hivyo kusababisha kushindwa kuendesha shughuli zake katika mazingira ya kisasa.

”Ujenzi wa majengo mapya ya Mahakama itasaidia, kupunguza msongamano wakati wa utoaji wa huduma na kusaidia wananchi kupewa huduma kwa kuendana na  mahitaji ya kisasa,” alisema Mrajis.



Read More

Thursday, December 19, 2024

WANANCHI WA HANANG' WAMSHUKURU RAIS SAMIA

 


Wananchi waliokumbwa na athari za maafa ya Maporomoko ya tope na mawe kutoka Mlima Hanang wametoa shukrani za dhati kwa Rais wa Awamu ya Sita Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa wema aliowatendea kwa ujenzi wa nyumba za makazi zilizojengwa katika eneo la Waret Wilaya ya Hanang' Mkoa wa Manyara.

Wametoa salamu hizo katika kikao cha ndani walichokutana na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera Bunge na Uratibu Mheshimiwa William Lukuvi leo katika ukumbi wa Halmashauri Hanang' ikiwa ni maandalizi ya kuwakabidhi wananchi nyumba 109 zilizojengwa na Serikali tukio litakaloongozwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa.

Bw, Kizito Joackimu Mkazi wa Katesh "A" amesema Serikali iliweka jitihada kubwa kusimamia urejeshaji wa hali wakishirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama nchini na kazi imefanyika kwa ubora na weledi.

“Mama Samia ni zaidi ya Mama hakulazimishwa na mtu kututendea wema alioufanya kwa wananchi wa Hanang', angeweza kutoa salamu za pole lakini akaona haitoshi, atoe vyakula vya kutosha, magodoro, matibabu ndugu zetu wametibiwa kwa kiwango kikubwa,” alieleza Bw, kizito.

Alifafanua, kwamba Kuna wananchi nyumba zao zilizoharibika zikiangaliwa thamani yake hazilingani na hizi zilizojengwa kwa ubora na kwa kuzingatia upatikanaji wa huduma muhimu za kibinadamu.

"nyumba hizi zitatufaa sana na kimsingi kuna watu walikuwa hawana ndoto za kuwa na nyumba zilizokatika mtaa mmoja wenye maji wenye umeme na eneo la biashara, tumebebwa sana na Serikali lazima tuwe na moyo wa shukrani," alisisitiza.

Wakitoa neno la shukrani wakati wa kikao hicho Bi. Fausta Magasa Mkazi wa Katesh, "A"amesema jambo hilo limewaletea furaha katika maisha yao na kusema ni la neema na baraka ambalo hawakulitegemea kutokea.

“Tunapenda kutoa shukrani za dhati kwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mbegu ya upendo aliyoipanda kwa watu 109 ambayo itazaa vizazi na vizazi" alieleza Bi, Magasa.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. William Lukuvi amesema wananchi watakaopewa funguo za nyumba kesho wataamua wao wenyewe siku watakayohamia kwenye nyumba  zao walizojengewa na serikali.

“Nimepokea Salamu za Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nitaziwasilisha lakini naamini muwakilishi wenu atasema salamu zenu pia kesho wakati mnapokea hati ya nyumba, funguo za nyumba zenu na majiko ya gesi" alieleza Waziri Lukuvi.





Read More

Monday, December 16, 2024

DKT. YONAZI AMPONGEZA MHE. BALOZI MUTATEMBWA

 


Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Dkt Jim Yonazi amempongeza Aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo Bw. Anderson Mutatembwa kwa Kuteuliwa kuwa Balozi.

Dkt. Yonazi Ametoa pongezi hizo wakati akimuaga Mhe. Balozi Mutatembwa na Kumakaribisha Naibu katibu Mkuu mpya Dkt. James Kilabuko.

Dkt. Yonazi amempongeza Balozi Mutatembwa kwa kufanya kazi ya ushauri kwa utulivu aliyotokana hekima aliyojijengea na kujaliwaa na Mwenyezi Mungu kuwa nayo “Na ndiyo maana Mhe. Rais ameweza kukuamini na kukuteuwa katika nafasi ya Ubalozi ili uweze kumuwakilisha yeye pamoja na Nchi katika maeneo ambayo atakayoona inampendeza.” Alifafanua

Aliendelea kusema kuwa, nafasi ya ubalozi ni nafasi nyeti na adhimu sana na ni fursa inayopatikana kwa watu wachache sana, “umepata fursa nyeti sana ya kuitumikia Taifa naamini utaendelea kufanya kazi kama ambavyo umekuwa ukifanya hapa na utakaoenda kufanya nao kazi watafaidika na kufurahia kama tulivyo faidika sisi.” Alibainisha Dkt. Yonazi

Akimkaribisha Naibu Katibu Mkuu mpya Dkt. James Kilabuko, Katibu Mkuu Dkt. Yonazi alisema Ofisi ya Waziri Mkuu ni Ofisi yenye majukumu mazito yenye watumishi wachapakazi wenye kutizama tija katika utendaji wa majukumu yao ya kila siku.

Naibu Katibu Mkuu, Dkt. James Kilabuko Alimshukuru Mhe. Rais kwa kumteuwa katika nafasi hiyo na kuona kwamba anaweza kumsaidia Katibu Mkuu Kiongozi katika nafasi hiyo, aliendea kusema kuwa anategemea kupata ushirikiano kutoka kwa Watumishi na Menejimenti ya Ofisi ya Waziri Mkuu katika kumsaidia Katibu Mkuu Dkt. Jonazi kiutendaji na kufikia malengo yanayotegemewa na mamlaka za juu.

Kwa Upande wake Mhe. Balozi Anderson Mutatembwa, alimshukuru Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea Kumuamini na kumteuwa katika nafasi hiyo.

Aidha, Ameishukuru Menejimenet ya Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu pamoja na watumishi wa Ofisi hiyo kwa ushirikiano waliomupatia wakati wa utekelezaji wa majukumu yake ofisini hapo, aliendelea kusema kuwa ni sehemu ambayo atapakumbuka kwani amefanya kazi kwa amani na Utulivu wa hali ya juu.

 

Read More

Saturday, December 14, 2024

MAFUNZO YA UFUATILIAJI NA TATHMNI KWA WIZARA, IDARA ZINAZOJITEGEMEA, WAKALA WA SERIKALI NA MASHIRIKA YA UMMA YAFANYIKA JIJINI TANGA

 


Afisa Muandamizi wa Ufuatiliaji na Tathmini kutoka kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Bw.Charlton Charles Meena amewataka washiriki wote wa mafunzo ya awamu ya kwanza ya ufuatiliaji na tathmni yaliyoshrikisha wizara, idara zinazojitegemea, wakala wa serikali na mashirika ya umma kuwa na mundelezo mzuri wa mafunzo ya awamu zote tatu ili kuweza kujipambanua vizuri katika utendaji wa kazi zao.

Kauli hiyo ameitoa Jijini Tanga wakati wa kuahirisha mafaunzo ya ufutiliaji na tathimini yaliyofanywa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania kupitia kitengo chake maalumu cha ushauri wa kitaalam na kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) pamoja na washirika wengine Ofisi ya Msajili wa Hazina, yaliyofanyika katika ukumbi wa New Kiboko Hall Jijini Tanga kwa muda wa siku tatu.

Ameeleza kwamba Mafunzo yameshirikisha watumishi wa umma zaidi ya 200, na yamewawezesha washiriki kujifunza kutofautisha na kutumia ipasavyo aina tofauti za Ufuatiliaji na Tathmini, kuamua jinsi ya kufuatilia na kutathmini miradi, mipango ya kimaendeleo na sera ikiwa ni pamoja na kuweka bayana matokeo muhimu katika ngazi ya programu kwa kutumia mfumo wa kimantiki (Logical Framework) au miundo ya nadharia ya mabadiliko (Theory of Change).

Bw, Meena, alisema “mafunzo yamelenga kuunda viashiria sahihi (SMART), kwaajili Ufuatiliaji na Tathmini, kutumia zana mbalimbali za Ufuatiliaji na Tathmini kwaajili ya ukusanyaji na uchanganuzi wa takwimu, kubuni na kusimamia Tathmini kwa kutumia kanuni za Kiafrika za Tathmini na vigezo vya OECD-DAC na kuandaa ripoti bora za Ufuatiliaji na Tathmini kwaajili ya matumizi ya Serikali, Idara, Wizara, Mashirika na Wakala za Serikali.

Aidha kutokana na umuhimu wa mafunzo hayo, Chuo Kikuu Huria kitaendelea kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, pamoja na Msajili wa Hazina kuandaa awamu nyingine ya mafunzo ya awamu ya kwanza ili kuweza kuzifikia baadhi ya Wizara, Idara zinazojitegemea, mashirika na wakala za serekali ambazo zilishindwa kuleta watumishi kwenye awamu hii ya kwanza ya mafunzo.

“ni vyema kujenga uelewa wa pamoja  sasa,  kwasababu kutakua na awamu ya pili na ya tatu ambazo zitawezesha  watumishi kubobea katika eneo la Ufuatiliaji na Tathmini wa shughuli za Serikali na hivyo kuboresha utendaji kazi wa serikali na utoaji huduma kwa wananchi,” alibainisha.

 

Read More

Friday, November 29, 2024

WAZIRI MHAGAMA AZINDUA USAMBAZAJI WA RIPOTI YA UTAFITI WA VIASHIRIA NA MATOKEO YA UKIMWI 2022-2023

 


Waziri Afya Mheshimiwa Jenista Mhagama amezindua Usambazaji wa Ripoti ya Utafiti wa Viashiria na Matokeo ya UKIMWI 2022-2023 Mkoani Ruvuma.

 Akizungumza katika uzinduzi huo uliofanyika Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma alieleza mafanikio makubwa yaliyopatikana katika juhudi za kudhibiti maambukizi ya UKIMWI nchini Tanzania ambapo imeelezwa kuwa kiwango cha Maambukizi Mapya kimepungua huku akipongeza juhudu zinazofanywa na Tume ya Kudhibiti UKIMWI Nchini

"Kwa mujibu wa ripoti hiyo, kiwango cha maambukizi ya UKIMWI nchini kimepungua kwa kiasi kikubwa kutoka asilimia 7 mwaka 2022 hadi asilimia 4.4 mwaka 2023. Aidha, juhudi za kupunguza maambukizi ya mama kwenda kwa mtoto zimezaa matunda, ambapo kiwango cha maambukizi kimepungua kutoka asilimia 18 mwaka 2010 hadi asilimia 8.1 mwaka 2023," alisema Waziri Mhagama

Waziri Mhagama alieleza kuwa mafanikio haya yametokana na juhudi za Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo, sekta binafsi, na jamii katika kuimarisha programu za utoaji elimu, upimaji wa hiari, na matumizi ya dawa za kufubaza makali ya virusi vya UKIMWI (ARVs).

Alisisitiza umuhimu wa kuendelea na juhudi hizi ili kufikia malengo ya kumaliza maambukizi mapya ya UKIMWI, hasa kwa watoto, ifikapo mwaka 2030. Vilevile, aliwahimiza wananchi kuendelea kuchukua hatua za kujikinga na maambukizi na kufuata ushauri wa kitaalamu.

Aidha alitoa wito kwa jamii kuunga mkono mikakati ya kitaifa ya kupambana na UKIMWI ili kuhakikisha maendeleo ya afya ya jamii na uchumi wa taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mheshimiwa Ummy Nderiananga, amesema Watanzania wamepiga hatua kubwa katika mapambano dhidi ya maambukizi ya Virusi vya UKIMWI (VVU)ambapo asilimia 98 ya Watanzania wanaohitaji dawa za kufubaza makali ya virusi hivyo (ARVs) sasa wanatumia dawa hizo, hatua ambayo imevuka malengo yaliyowekwa kitaifa na kimataifa.

Mhe. Ummy alibainisha kuwa mafanikio haya ni matokeo ya jitihada za serikali chini ya Mhe. Dkt . Samia Suluhu Hassan, kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, ikiwemo utoaji wa elimu ya afya, upimaji wa hiari, na utoaji wa dawa kwa urahisi katika vituo vya afya.

Pia ametumia nafasi hiyo kuhimiza wananchi kuendelea kuchukua hatua za kujikinga na kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa kuendelea kutumia dawa kwa walioambukizwa ili kuboresha maisha yao na kupunguza maambukizi mapya.

Serikali inaendelea kuweka mikakati imara kuhakikisha kila Mtanzania anayehitaji huduma za matibabu anazipata kwa wakati.

Maadhimisho ya Wiki ya UKIMWI Duniani yanaadhimishwa Kitaifa mkoani Ruvuma yenye kauli Mbiu isemayo "Chagua Njia Sahihi, Tokomeza UKIMWI"



Read More

Thursday, November 21, 2024

DKT. YONAZI ASHUKURU MICHANGO INAYOENDELEA KUTOLEWA, AFAFANUA NAMBA SAHIHI YA KUTUMA MICHANGO MAAFA KARIAKOO

 

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera,Bunge na Uratibu  Dkt. Jim Yonazi amewashukuru wadau mbalimbali wanaoendelea kujitolea na kutoa michango kwa ajili ya maafa ya Kuporomoka kwa ghorofa eneo la Kariakoo kusema ni moyo wa upendo unaoneshwa kwa matendo mbalimbali walioguswa na maafa hayo.

Ametoa shukrani hizo wakati akiongea na waandishi wa habari kuhusu hatua zinavyoendelea katika eneo lililopatwa na ajali ya kuporomoko kwa jengo la ghorofa mtaa wa Agrey Kariakoo Jijini Dar es Salaam.

Dkt. Yonazi ametumia nafasi hiyo kutangaza “Control Number” kwa ajili ya kuwawezesha wananchi ambao wataguswa na maafa hayo kwa kutuma michango yao kwa ajili ya kuendelea kusaidia katika hatua baada ya kutokea maafa hayo.

" Control number ni 987320001709 ambapo namba hii inatumika kwa mitandao yote ,mwananchi anaweza kuchangia kuanzia 1000 na kuendelea na fedha hizi zinaingia moja kwa moja kwenye akaunti ya Maafa au kuchangia kupitia akaunti ya National Relief Fund yenye namba 9921159801 ambayo ipo Benki Kuu ya Tanzania,” amesema Dkt.Yonazi.

Kwa hatua nyingine Dkt. Yonazi amepokea msaada kutoka Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) lililokabidhi kiasi cha shilingi za Kitanzania Milioni Ishirini kwa lengo la kusaidia kufuatia maafa hayo.

Akizungumza kabla ya kukabidhi hundi hiyo Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya TANAPA, Jenerali mstaafu George Waitara amesema kuwa tukio hilo limesababisha maafa makubwa ikiwemo vifo,uharibifu wa mali pamoja na matatizo ya kisaikolojia kwa waathirika wa tukio hilo.

"TANAPA ni sehemu ya wananchi wa Tanzania,hivyo janga hili tumetugusa tukaona tutoe chochote kusaidia uokoaji wa maafa haya na Watanzania wasiwe na taharuki kwani tumeona shughuli za uokoaji zinakwenda vizuri, kikubwa wawe wanafuatilia taarifa kupitia mamlaka husika na si vyanzo vingine " amesema Jenerali Mstaafu Waitara.











Read More

Tuesday, November 19, 2024

SERIKALI YAONGEZA SAA 24 ZA ZIADA ZA UOKOZI KARIAKOO

Mkurugenzi wa Idara ya Habari-Maelezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali Bw. Thobias Makoba, amesema zoezi la uokoaji wa watu walionasa kwenye jengo lililoporomoka Jumamosi ya Novemba 16, 2024 Kariakoo kwenye Mtaa wa Congo na Mchikichi Jijini Dasr es Salaam, litaendelea tena kwa saa 24 za ziada baada ya saa 72 za kawaida za kiwango cha kimataifa kumalizika.

Bw. Makoba ameyasema hayo, wakati akizungumza na waandishi wa habari Kariakoo kwenye eneo la tukio, ambapo amesema kuongezeka kwa saa hizo 24 za ziada, ni agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, alilolitoa kupitia kwa Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa, katika kikao cha tathmini kuhusu zoezi hilo la uokoaji ambapo amelitaka jeshi la zimamoto na uokoaji, kuendelea na shughuli hiyo ili kunusuru uhai wa watu ambao bado wamekwama kwenye jengo hilo.

“Tukiwa kwenye kikao cha tathmini cha kazi inayoendelea, moja ya ajenda iliyozungumzwa ni kuhusiana na utaratibu wa uokoaji, kulianza kutokea maneno kwenye mitandao ya kijamii kwamba baada ya masaa 72 kwa kawaida kwa viwango vya kimataifa, zoezi la uokoaji kwenye maeneo kama haya linabadilika, na wanaanza kutumia mashine pale inapolazimu, sasa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan muda huu ametoa maelekezo kupitia kwa Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa, na maelekezo hayo yaje kwa kikosi chetu cha Zimamoto na Uokoaji kwamba zoezi hili liendelee kwa saa zingine 24 za ziada, ni kwamba wasisitishe, kabla ya kubadili hatua yoyote, kwa hiyo zoezi hili linaendelea, halitasitishwa kama ambavyo wananchi wengine wameanza kuwa na hofu” amesema Bw. Makoba.

Amesema lengo ni kuhakikisha maisha ya watu walioko kwenye jengo hilo yanalindwa na kwamba hakuna kifusi kitakachowaangukia.

“Imempendeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwamba, tutaendelea kutumia mbinu ambazo zilikuwa zikitumika za weledi na ustadi zaidi katika kuhakikisha kwamba, kwanza tunaridhika kwamba hakuna ambaye aliyepo hai atasumbuliwa au ataangushiwa kifusi huko chini, au kwa namna yoyote ile itamkuta ili kumsababishia kupoteza maisha, baada ya masaa 24 tutatangaza utaratibu unaofuata” amesema Bw. Makoba.

Zoezi la uokoaji wa watu walionaswa kwenye jengo lililoporomoka linaendelea kwa kasi kubwa kwa siku ya nne sasa ambapo Serikali inafanya jitihada zote kuhakikisha hakuna madhara yatakayowapata watu walionasa kwenye jengo hilo.

 

Read More

NAIBU WAZIRI UMMY AWASHUKURU RED CROSS NA TPA KWA MISAADA YA VIFAA SAIDIZI MAAFA KARIAKOO


Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mheshimiwa Ummy Nderiananga amewashukuru wadau kutoka Shirika la Msalaba Mwekundu (Red Cross Tanzania) pamoja na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania TPA kwa kutoa misaada ya vifaa saidizi kwa ajili ya kuendelea kusaidia katika zoezi la uokoaji linaloendelea kufuatia janga la kuporomoka jengo la ghorofa eneo la Congo na Mchikichi Kariakoo Wilaya ya Ilala Jijini Dar es Salaam.

Ametoa shukrani hizo hii leo na kueleza kuwa miongoni mwa vifaa vilivyokabidhiwa ni pamoja na machela tisa (9) mashuka 100 kutoka Shirika la Msalaba Mwekundu (Red Cross Tanzania) Pamoja na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania TPA, reflectors pamoja na  cover white.

Naibu Waziri huyo ameendelea kutoa rai kwa wadau mbalimbali kuendelea kujitokeza kuchangia huku akipongeza namna zoezi la uokoaji linavyoendelea kwa kushirikiana na wadau.








 

Read More

Monday, November 18, 2024

MAPITIO YA PROGRAMU YA KUENDELEZA KILIMO NA UVUVI (AFDP), YAWAKUTANISHA WATAALAMU PAMOJA NA UJUMBE KUTOKA- (IFAD) MJINI ZANZIBAR

 


Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Uratibu wa Shughuli za Serikali, kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Bw. Paul Sangawe ameongoza Kikao cha Ujumbe kutoka Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), wakurugenzi wa sekta zinazotekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) inayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu pamoja na timu ya wataalamu.

Pamoja na mambo mengine kikao hicho pia kimehusu mapitio ya Mipango na Bajeti ya Programu kwa kipindi cha miaka minne ya utekelezaji iliyobakia.

Kikao  hicho kimefanyika Zanzibar, katika ukumbi wa Mkutano wa Wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi.



Read More

MISAADA KWA AJILI YA WAATHIRIKA WA KUPOROMOKA KWA JENGO KARIAKOO ITOLEWE KWENYE AKAUNTI MOJA- DKT. YONAZI

 


Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi amesema msaada wa kifedha kwa ajili ya kusaidia walioathirika na kuporomoka kwa jengo la ghorofa Kariakoo Jijini Dar es Salaam unatolewa kwa akaunti maalum ya maafa ya 9921159801 ambayo ipo Benki Kuu ya Tanzania na kushughulikiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu.

Dkt. Yonazi ameyasema hayo leo wakati akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu hali inayoendelea katika zoezi la uokoaji.

Amesema akaunti hiyo ni pekee nchini ambayo inakusanya misaada ya kifedha kwa ajili ya maafa.

"Kuna watu wana nia njema kabisa ya kuwasaidia Watanzania, lakini naomba tujizuie kabisa kukusanya michango ya kifedha kutoka kwa mtu yeyote bila kupitia akaunti hii". Amesema Dkt. Yonazi.

Aidha amesema akaunti hiyo ni maalumu imethibitishwa na serikali ili kuweza kuhakikisha misaada inawafikia walengwa na inatimiza malengo ya kutoa misaada hiyo.

Amesema kwa sasa operesheni inaendelea mpaka pale watakapokamilisha zoezi la kuokoa baadhi ya watu ambao bado hawajaokolewa.



Read More

Sunday, November 17, 2024

KATIBU MKUU WA CCM DKT. EMMANUEL NCHIMBI AFIKA KARIAKOO, AUNGANA NA VIONGOZI WENGINE WAKATI WA ZOEZI LA UOKOAJI

 


Katibu Mkuu wa CCM Dkt. Emmanuel Nchimbi afika Kariakoo Leo Novemba 17,2024 na kushuhudia zoezi la uokoaji akiwa ameongozana na viongozi wa Serikali na kujionea zoezi hilo linaloendelea  mara baada ya  kuporomoka kwa jengo la ghorofa Kariakoo kwenye mtaa wa Congo na Mchikichi Jijini Dar es Salaam.

Mawaziri hao ni pamoja na  Waziri wa Viwanda na Biashara Dkt. Selemani Jafo, Naibu Waziri wa Afya Dkt. Godfrey Mollel, Naibu Waziri wa TAMISEMI Mhe. Zainab Katimba pamoja na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Ummy Nderiananga.



Read More

MAWAZIRI WAHAMIA KARIAKOO; KAZI YA UOKOZI INAENDELEA

 


Mawaziri wa kisekta wakiongozwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Mhe. William Lukuvi Leo Novemba 17,2024 wamekutana kwa ajili ya kuendelea na zoezi la uokoaji wa watu waliokwama kwenye jengo lililoporomoka Kariakoo kwenye mtaa wa Congo na Mchikichi Jijini Dar es Salaam.

Mawaziri hao ni pamoja na Waziri wa Viwanda na Biashara Dkt. Selemani Jafo, Naibu Waziri wa Afya Dkt. Godfrey Mollel, Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Mwanaidi Khamis na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Ummy Nderiananga.



Read More

Thursday, November 14, 2024

TANZANIA YAVUTIA MATAIFA UWEPO WA KITUO CHA UFUATILIAJI WA MAJANGA

 

 

TANZANIA imeendelea kutolewa mfano wa kuwa na Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura (National Emergency Operation and Communication Center Situation Room) na kuelezwa kuwa nchi nyingine ziendelee kuiga mfano wa Tanzania na kuendelea kuwekeza katika mifumo ya tahadhali za mapema -early warning systems kwa kutumia vyanzo vya ndani, kushirikisha jamii na sekta binafsi.

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi ameyasema hayo 13 Novemba, 2024 wakati wa Mkutano wa 29 wa nchi Wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (COP-29) unaoendelea mjini Baku, nchini Azerbaijan.

Dkt. Yonazi amesema kuwa,Tanzania imeendelea kuwa kinara katika masuala ya menejimenti ya maafa hususan katika kuzuia, kupunguza kujiandaa na kukabili maafa pindi yanapotokea, huku akitaja mafanikio ya uwepo wa kituo cha ufuatiliaji wa majanga (situation room) ikiwemo ya kurahisisha ufuatiliaji wa mwenendo wa janga lililotabiriwa na kufanya uchambuzi wa kiwango cha madhara kwa jamii, miundombinu na mazingira.

Pia kituo hicho kimesaidia kuandaa taarifa za tahadhari ya mapema ya hatua za kuchukua ili kuzuia, kujiandaa na kukabili maafa, kuandaa taarifa ya mwenendo wa tukio na kusambaza kwa wadau mbalimbali kwa ajili ya kusaidia uratibu na utekelezaji wa shughuli za kukabili na kurejesha hali pindi maafa yanapotokea.

Aidha alitumia fursa hiyo kuwahamasisha wadau kuwezesha utekelezaji wa afua za usimamizi wa maafa katika eneo la mifumo ya tahadhali ya mapema.

Dkt. Yonazi ametumia jukwaa hilo kuyakaribisha Mataifa mbalimbali kuja kujifunza Tanzania namna Kituo hicho kinavyofanya kazi katika kuratibu mwenendo wa majanga kwa umahiri wa hali ya juu.

“Uwepo wa kituo hiki umewavutia wadau wengi kuja kujifunza huku wengine wakiahidi kuunga mkono juhudi za Tanzania katika masuala ya menejimenti ya maafa,” alisema Dkt. Yonazi






Read More

Tuesday, November 12, 2024

AU YAIPATIA TANZANIA DOLA ZA KIMAREKANI 200,000 MCHANGO WA MAAFA HANANG

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, na Uratibu) Mhe. William Lukuvi ameishukuru Umoja wa Afrika kwa kutoa kibali cha kuichangia nchi ya Tanzania Dola za Kimarekani 200,000 kama ishara ya mshikamano kutokana na maafa makubwa yaliyotokea Wilaya ya Hanang’ mkoani Manyara.

Waziri Lukuvi ametoa shukrani hizo leo katika Ofisi za Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu zilizopo Jijini Dodoma na kubainisha kuwa mchango huo ni muhimu kwa kuwa utasaidia juhudi zinazofanywa na Serikali za kurejesha hali ikiwemo ujenzi wa shule, kituo cha afya na soko katika eneo lililoathirika.

 Akipokea mchango wa fedha hizo kutoka kwa Mheshimiwa Balozi Tabelelo Alfred Boang, Balozi wa Jamhuri wa Muungano wa Botswana nchini Ethiopia na Mwakilishi wa kamati ya Mabalozi (Permanent Representative Sub Committee on refugees, Returnees and IDPs), Mhe. Lukuvi amemweleza kuwa, mwaka 2023/2024 Tanzania ilikumbwa na El-Niño ambayo ilisababisha kuwepo kwa mvua kubwa zilizofululiza kwa kipindi kirefu na kusababisha mafuriko, upepo mkali, maporomoko ya tope na udongo.

Ameeleza, pamoja na juhudi zilizofanywa na Serikali katika kuzuia na kupunguza madhara, bado El-Niño ilileta madhara makubwa ikiwemo maafa ambayo yaliyosababisha vifo, kuharibu makazi ya watu na miundombinu muhimu.

 “Maporomoko ya tope wilayani Hanang’ yaliathiri maisha ya watu, miundombinu, shughuli za kiuchumi na kijamii, takwimu zinaonesha kuwa watu wapatao 89 walipoteza maisha na watu wapatao 139 waliumia kutokana na maporomoko hayo. Aidha, tathmini iliyofanyika inaonesha jumla ya nyumba 261 ziliathirika kwa namna moja au nyingine ambapo nyumba 95 zilibomoka kabisa na zingine kuzungukwa na tope, Watu wapatao 1576 kutoka 526 waliachwa bila makazi katika kipindi cha tukio” ameeleza Mhe. Lukuvi.

 Aidha, ameongeza kuwa, katika kukabiliana na maafa, Serikali ilifanya juhudi za kurudisha hali ambapo mpaka sasa imewezesha kujengwa nyumba 108 za makazi ya watu, kati ya nyumba hizo 73 zimejengwa kwa fedha za Serikali na nyumba 35 zimejengwa na Shirika la Msalaba Mwekundu, ujenzi wa nyumba hizo 108 umekamilika. 

 “Ninaelewa kuwa ujumbe wako utatembelea Wilaya ya Hanang’ tarehe 14 Novemba, 2024, katika safari yenu mtashuhudia juhudi kubwa za Serikali kwa kushirikiana na wadau zinazoendelea za kurejesha hali ikiwemo miundombinu muhimu kama vile barabara, umeme, maji na ujenzi wa nyumba 108 za makazi, ameeleza Mhe. Lukuvi.

Kwa upande wake Mheshimiwa Balozi Tabelelo Alfred Boang, Balozi wa Jamhuri wa Muungano wa Botswana nchini Ethiopia na Mwakilishi wa kamati ya Mabalozi (Permanent Representative Sub Committee on refugees, Returnees and IDPs), ameeleza kuwa, ujumbe huo umeagizwa na Kamati ya Mabalozi kufanya tathmini ya uharibifu uliotokea katika maeneo yaliyoathiriwa ikiwa dhamira kubwa ni Mkoa wa Manyara, aidha muhimu zaidi ni kusikia kutoka kwenye mamlaka na ndio maana wamekutana na Mheshimiwa Waziri na timu yake.

 “Muhimu zaidi kama Umoja wa Afrika kwa hakika kila kidogo tulicho nacho huwa tunainuka tunajivunia kuwa tumejitolea na kusema tunaenda kutafuta suluhu ya Afrika, matatizo au changamoto za Afrika” amebainisha Balozi Tabelelo.



Read More

Wednesday, November 6, 2024

UJUMBE WA MFUKO WA KIMATAIFA WA MAENDELEO YA KILIMO "IFAD" WATEMBELEA PROGRAMU YA KUENDELEZA KILIMO NA UVUVI "AFDP" TANZANIA


Ujumbe kutoka Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) ukiwa umeambatana na watumishi wa Programu ya kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP), kutoka  Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) pamoja na watekelezaji wa programu hiyo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Wizara ya Uchumi wa Buluu na uvuvi Zanzibar  wamekitembelea Kikundi cha Ufugaji wa samaki kiitwacho UWASAMO, katika kata ya Mzinga Mtaa wa Konga Manispaa ya Morogoro, ili kuona mafanikio ya ufugajiwa samaki kwa wanakikundi baada ya kupata mafunzo ya Ufugaji samaki, biashara na utunzaji wa kumbukumbu kutoka  kituo cha Kingolwira.

Ziara hiyo imefanyika leo tarehe 6/11/2024 kwenye Kituo kinachojishughulisha na utoaji mafunzo ya ufugaji samaki, pamoja na uuzaji wa vifaranga vya samaki.

Akizungumza kwa niaba ya wanakikundi ndugu Asungushe Patrick Msugupakulya amesema, wao kama kikundi wanaishukuru serika kwa kuwaletea mradi wa IFAD, ambao umewasaidia katika kuunda ushirika wao ambao mpaka sasa wanaendelea kupata msaada wa Elimu ya ufugaji wa samaki kwa wakati.

Pamoja na hayo wanakikundi cha UWASAMO, wamefurahishwa na ziara ya viongozi, ambapo wanaamini kwa kutembelewa huko, misaada zaidi watapata ili kuendeleza mtaji wao wa ufugaji wa samaki na kuleta maendeleo yenye tija kwa familia na Tanzania kwa ujumla wake.





Read More

TUONGEZE NGUVU YA PAMOJA KATIKA KUTEKELEZA DHANA YA AFYA MOJA - DKT. YONAZI

 


SERIKALI imedhamiria kuendelea kushirikiana na wadau  katika kutekeleza dhana ya Afya Moja nchini hasa maeneo ya kuzuia, kujiandaa na kukabiliana na milipuko ya magonjwa na hatari nyingine za afya zinazohitaji ushiriki wa sekta zaidi ya moja na taaluma mbalimbali.

Akizungumza leo Jumatano Novemba 6, 2024 wakati akifunga Mkutano wa Afya Moja uliofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa wa Arusha (AICC) Jijini Arusha, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala Sera, Bunge na Uratibu, Dkt. Jim Yonazi amesema lengo la Dhana ya Afya Moja ni kupanua na kuimarisha ushirikiano baina ya sekta pamoja na taaluma mbalimbali katika hatua zote za kuzuia, kujiandaa na kukabiliana na milipuko ya magonjwa na hatari nyingine za afya zinazohitaji ushiriki wa sekta zaidi ya moja na taaluma mbalimbali  katika kutekeleaji wa Afua hizo.

“Ni wakati sahihi kuendelea kushirikiana kwa pamoja na wadau wengine ikiwemo jamii, kwa kuongozwa na wizara za msingi ambazo ni Afya ya Binadamu, Wanyama (Mifugo na Wanyama Pori), Mazingira na Kilimo katika ngazi zote ili kuhakikisha nguvu ya pamoja inatuvusha hapa tulipo na kuendelea kuipa nguvu dhana ya afya moja,” alisema Dkt. Yonazi

Aliongezea kuwa, Dawati la Uratibu wa Afya Moja lipo chini ya Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo utekelezaji wa majukumu yake unaongozwa na Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Maafa ya Mwaka 2004 inayoweka umuhimu katika usalama wa maisha ya watu na mali zao kwa kupunguza athari za kiuchumi na kijamii katika kuipa nguvu Sera ya Usimamizi wa Maafa ya mwaka 2004, Serikali ilitunga Sheria ya Usimamizi ya Maafa Namba 7 ya Mwaka 2015 inayosimamia utekelezaji wa shughuli za idara.

Dkt. Yonazi alizikumbusha sekta zote kuendelea kushirikiana katika kutatua changamoto ya magonjwa ya zoonotiki, usalama wa chakula, mabadiliko ya tabia nchi na usugu wa dawa dhidi ya vimelea vya magonjwa.

Aidha ameyataja maeneo ya kuimarisha ushirikiano kwa sekta pamoja na wadau wote wanaotekeleza Dhana hiyo ikiwemo ya kuongeza ushiriki wa sekta ya mazingira na sekta ya kilimo katika utekelezaji wa dhana ya Afya Moja, kuandaa miongozo ya namna sekta zitakavyobadilishana taarifa za magonjwa na matukio yenye athari kwa binadamu, wanyama na mazingira chini ya uratibu wa Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na kuhuisha orodha ya magonjwa ya kizoonotoki na kutekeleza miongozo na mipango mbalimbali ya kudhibiti magonjwa hayo.

Maeneo mengine ni kuendelea kuzijengea uwezo Kamati za Usimamizi wa Maafa kuhusu uratibu na utekelezaji wa dhana ya Afya Moja, kuendelea kutekeleza Mpango Mkakati wa Afya Moja (2022-2027) katika maeneo yote pamoja na kuendelea kushiriki katika tafiti na uchunguzi wa pamoja kuhusu milipuko ya magonjwa na matukio mbalimbali nchini.

Kwa hatua nyingine Dkt. Yonazi amepongeza washiriki wote ikiwemo wawasilisha mada kwa siku zote na kueleza kuwa zitaendelea kuongeza tija katika miradi mbalimbali nchini ikiwemo ya kichaa cha mbwa, kimeta  na homa ya bonde la ufa.

“Mmetoa michango mingi na mizuri hakika itatufaa katika utekelezaji wa dhana ya Afya Moja na kuboresha afya za binadamu, wanyama, mimea na mifumo yaikolojia ,”alieleza Dkt. Yonazi.

Aidha amewashukuru wadau waliofanikisha kufanyika kwa mkutano huo muhimu huku akiwasihii kuendelea kuimarisha mashirikiano yaliyopo ili kuendelea kuipa nguvu Dhana ya Afya Moja na kuyafikia malengo yake.

“Kipekee niwashukuru COHESA, FAO, USAID na One Health Society kwa kusaidia na kufanikisha mkutano huu. Aidha, niwapongeze USAID kupitia mradi wao wa Breakthrough Action, MDH, Chuo cha Nelson Mandela kupitia mradi wa CEREBLAM, AFROHUN, KCMC/KCRI na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kwa kushiriki kikamilifu katika maonesho ya Mkutano huu,” Alisisitiza

Kwa upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Arusha Ndugu Missaile Musa ameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuratibu Mkutano huo wenye tija kwa Mkoa na Taifa kwa ujumla huku akisema mkutano huo umefanikiwa kukutanisha wadau na kujengewa uwezo pamoja na kuweka mikakati itakayowezesha kuyafikia malengo yaliyokusudiwa.

“Malengo na mkutano huu yamefanikiwa sana, kama mkoa tunaamini kuwa yote yaliyowasilishwa hapa yanamchango katika kuimarisha afya zetu pamoja na za wanyama, tutaendelea kuwa salama endapo haya tutayapa kipaumbele hivyo tuendelee kuwalinda na kujilinda kuwa na jamii salama,”alisema Missaile

Katika Mkutano huo uliofanyika kwa muda wa siku tatu kuanzia  Novemba 4  hadi 6, 2024 na kuhudhuriwa na zaidi ya washiriki 320 kutoka ndani na nje ya nchi ikiwemo; Kenya, Uganda, Zimbabwe, Namibia, Rwanda, Nigeria, Ghana, Sudani ya Kusini, Cameroon, Senegal, Scotland na Ujerumani umekuwa ni muhimu sana.



Read More