Sunday, May 25, 2025

ASKOFU MSAIDIZI TABORA AWEKWA WAKFU, WAZIRI LUKUVI AMWAKILISHA RAIS SAMIA

 


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Mhe. William Lukuvi, amemuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika ibada maalum ya kuwekwa wakfu kwa Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Tabora, Mhashamu Josephat Jackson Bududu.

Ibada hiyo ya Misa Takatifu imefanyika leo, katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Theresia, Jimboni Tabora, na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali, Kanisa na waumini kutoka maeneo tofauti.

Katika hotuba iliyosomwa kwa niaba ya Rais Samia, Mhe. Lukuvi amempongeza Askofu Bududu kwa kuteuliwa kushika nafasi hiyo, akieleza kuwa Serikali inaendelea kuthamini mchango wa taasisi za dini katika kuimarisha maadili, amani na maendeleo ya jamii.

Sherehe hiyo imehudhuriwa pia na viongozi wa madhehebu mbalimbali, ikionyesha mshikamano wa kidini na kijamii katika mkoa wa Tabora.

Read More

Wednesday, May 21, 2025

DKT. KILABUKO AZINDUA MWONGOZO WA KITAIFA KWA WATOA HUDUMA ZA MAENDELEO YA BIASHARA


 

Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Dkt. James Kilabuko amezindua rasmi Mwongozo wa Kitaifa kwa Watoa Huduma za Maendeleo ya Biashara katika hafla iliyofanyika kwenye Hoteli ya Four Points by Sheraton, Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza hii leo wakati wa uzinduzi  huo kwa niaba ya Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi, Naibu Katibu Mkuu huyo amesema kuwa Mwongozo huo unaweka msingi wa mabadiliko makubwa ambayo yatawawezesha wafanyabiashara wadogo na wa kati ikiwa ni pamoja na wafanyabiashara wakubwa kukuza biashara zao na kuchangia kikamilifu kwenye uchumi wa Taifa.

“Uwepo wa Mwongozo huo unalenga kuweka viwango, mwelekeo na uratibu wa huduma zinazotolewa kwa wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo na wa kati nchini, hivyo umekuja kwa wakati sahihi na tunaamini utaleta matokeo chanya kama ilivyokusudiwa,” alisema Dkt. Kilabuko.

Aidha alitumia nafasi hiyo kumpongeza Mheshimiwa Dkt Samia Suluhu Hassan kwa jitihada anazozifanya katika kuhakikisha mazingira ya wafanyabiashara na wawekezaji nchini yanaendelea kuwa bora.

“Kwa umuhimu wa pekee napenda kumshukuru kwa dhati, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jitihada anazofanya katika kufungua uchumi na kuchochea biashara na uwekezaji nchini.Rais wetu ameboresha mazingira ya biashara nchini na kuchochea kuanzishwa kwa shughuli za kiuchumi nyingi katika sekta mbalimbali. Shughuli hizo pia zinahitaji huduma za maendeleo ya biashara ili kuwa shindani.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wanamanchi Kiuchumi (NEEC) Bi. Beng'i Issa ameleeza kuwa Mwongozo wa Huduma za Maendeleo ya Biashara kwa Watoa Huduma za Maendeleo ya Biashara Tanzania unalenga kuboresha utoaji wa huduma za biashara ikiwa ni pamoja na: ushauri, mafunzo, msaada wa kiufundi, ujuzi, uatamizi, uhusiano baina ya wafanyabiashara, mawasiliano, na usimamizi wa biashara.

“Tunategemea, Mwongozo huu unakwenda kutoa dira ya namna bora ya utoaji wa huduma za biashara Tanzania zinazoweza kuboresha biashara na hivyo kuchochea ukuaji wa uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujuml,” alisema Bibi. Beng’i.

Alifafanua kuwa, mwongozo huo utaleta matokeo chanya na kuwasihi watoa huduma za maendeleo ya biashara nchini kutumia Mwongozo huu kama nyenzo katika kuwahudumia wafanyabiashara wadogo na wa kati wanaotekeleza shughuli za kiuchumi katika sekta mbalimbali.

 

Read More

Thursday, May 15, 2025

WAELIMISHA RIKA WATAKIWA KUTUMIA MBINU ZA KISASA KATIKA KUELIMISHA MASUALA YA AFYA KAZINI

 


Waelimisha rika Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) watakiwa kutumia mbinu mbadala na zinazokwenda na mazingira ya sasa katika kufikisha elimu ya afya kwa watumishi wenzao kazini huku wakijitolea kwa uzalendo na weledi ili kuendelea kuwa na mazingira mazuri ya utendaji wa kazi kwa kuzingatia afya zao.

Hayo yamebainishwa Kaimu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Bw. Eleuter Kihwele kwa niaba ya Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Dkt. Jim James Yonazi hii leo, wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya siku mbili kwa waelimisha rika mahala pa kazi, yanayofanyika mjini Morogoro.

Kihwele amesema kuwa mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo waelimisha rika katika utoaji wa elimu, hasa katika kipindi hiki ambapo jamii inakumbwa na ongezeko la magonjwa yasiyoambukizwa pamoja na changamoto nyingine za kiafya.

“Mafunzo haya yatakuwa na mada muhimu. Zingatieni ili kuwawezesha watumishi wenzenu kupata uelewa wa kina kuhusu masuala ya VVU na UKIMWI pamoja na magonjwa yasiyoambukizwa,” alisema Bw. Kihwele.

Aidha, amepongeza maandalizi ya mafunzo hayo, akisisitiza kuwa yatatoa mwanga na mwelekeo mpya wa kuhakikisha Ofisi ya Waziri Mkuu inakuwa mfano wa kuigwa katika kueneza elimu ya afya kwa watumishi wake.

Kwa mujibu wa Kihwele, mafunzo kwa waelimisha rika hufanyika kila mwaka ili kutathmini utekelezaji wa mwongozo uliopo, kubaini changamoto na kuja na mikakati bora ya kudhibiti magonjwa katika Idara na Vitengo husika.

Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Menejimenti ya Anuai za Jamii, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora;Bi. Mwanaamani Mtoo, ameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuendeleza utekelezaji wa mwongozo wa waelimisha rika kwa mafanikio makubwa.

“Sisi kama wasimamizi wa rasilimali watu, tunawapongeza kwa hatua mliyoifikia. Kuendeleza juhudi hizi ni hatua muhimu ya kudhibiti maambukizi ya VVU na UKIMWI pamoja na magonjwa yasiyoambukizwa kazini,” alisema Bi. Mtoo.

Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu imeendelea kuweka kipaumbele katika afya na ustawi wa watumishi wake, ikiwemo kutoa mafunzo ya stadi za afya kwa waelimisha rika na kuwawezesha kuwa mabalozi wa mabadiliko ya kiafya katika maeneo yao ya kazi.

 

Read More