Wednesday, March 18, 2026

KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UTAWALA, KATIBA NA SHERIA YARIDHISHWA NA UTEKELEZWAJI MRADI WA KITUO CHA TAIFA CHA UTENGAMAO.


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria imetembelea na kukagua mradi wa ujenzi wa Kituo cha Utengamao cha Taifa unaotekelezwa na Mamlaka ya Kudhibiti na kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) katika eneo la Itega, jijini Dodoma.

Ziara hiyo imefanyika leo na kuongozwa na Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Edwin Swale (Mb) ikiwa ni sehemu ya majukumu ya kamati ya kusimamia na kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Swale amesema kuwa kamati imeridhishwa na hatua ya utekelezaji  ambayo mradi umefikia kwani unaenda kutimiza  dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kujali Utu na Ustawi wa Watanzania.

Sambamba na hilo, ameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu kupitia Mamlaka ya kudhibiti na kupambana na dawa za Kulevya kwa kubuni mbinu ya jinsi ya kusaidia waraibu watokanao na matumizi ya madawa za kulevya.

Awali,Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. Ummy Nderiananga amesema kuwa Mradi huo ni endelevu ikiwa ni juhudi ya Serikali katika mapambano dhidi ya Dawa za kulevya na kuahidi kuendelea kushirikiana na Taasisi binafsi katika mapambano dhidi ya matumizi ya Dawa za kulevya Nchini.

Kwa upande wake Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na kupambana na Dawa za kulevya Bw. Aretas Lymo ameongeza kuwa kituo hiko kinatarajia kutoa huduma za matibabu, urekebishaji wa kitabia pamoja programu za kuwawezesha waathirika kurejea katika jamii wakiwa na uwezo wa kujitegemea



Read More

Tuesday, March 17, 2026

NAIBU WAZIRI UMMY ATOA MSUKUMO KWA WATUMISHI KUONGEZA UFANISI, AAGIZA UTEKELEZAJI THABITI WA BAJETI

Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Mhe. Ummy Nderiananga, amewahimiza watumishi wa ofisi hiyo kuendelea kufanya kazi kwa bidii, ufanisi na weledi ili kuhakikisha malengo yaliyoainishwa katika bajeti ya Serikali yanatekelezwa ipasavyo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Baraza la Wafanyakazi uliofanyika leo Jijini Dodoma, Mhe. Ummy—aliyemwakilisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Mhe. William Lukuvi—alisisitiza umuhimu wa watumishi kushirikiana na kuzingatia misingi ya uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Alifafanua kuwa mabaraza ya wafanyakazi yameanzishwa kufuatia Tamko Na. 1 la mwaka 1970 lililotolewa na Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, likiwa na lengo la kuongeza ufanisi na tija mahali pa kazi.

“Kupitia mabaraza haya, wafanyakazi na waajiri hupata fursa ya kujadili na kubadilishana mawazo kwa manufaa ya taasisi. Ni matumaini yangu kuwa majadiliano yenu yatajikita katika kuimarisha utendaji wa Ofisi ya Waziri Mkuu,” alisema Mhe. Ummy.

Awali, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, alimshukuru Waziri wa Nchi pamoja na Naibu Waziri kwa kushiriki katika kikao hicho muhimu cha Baraza la Wafanyakazi.

Aidha, aliwapongeza viongozi hao kwa ushindi walioupata katika Uchaguzi Mkuu na kwa kuendelea kuaminiwa na Mhe. Rais katika kusimamia sekta hiyo nyeti.

Dkt. Yonazi alieleza kuwa kikao hicho kimewakutanisha Menejimenti ya Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi ili kujadili bajeti ya ofisi hiyo, ikiwa ni pamoja na kupitia taarifa ya utekelezaji kabla ya kuidhinisha hatua za kuwasilisha bajeti hiyo katika ngazi zinazofuata.



Read More

Monday, March 16, 2026

WANANCHI MKINGA WANUFAIKA NA UWEKEZAJI KATIKA KILIMO CHA MWANI

 


Wananchi wa Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga wanatarajiwa kunufaika zaidi kiuchumi kupitia uwekezaji wa Serikali katika sekta ya kilimo cha mwani, hatua inayolenga kuongeza thamani ya mazao ya bahari na kuboresha maisha ya jamii za pwani.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kaushio jipya na mashine mbili za kisasa za kusaga mwani uliofanyika katika Kijiji cha Kichaka Miba, Wilaya ya Mkinga, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Mhe. Ummy H. Nderiananga, amesema mradi huo ni sehemu ya jitihada za Serikali kuimarisha uchumi wa wananchi wa maeneo ya pwani.

Mradi wa Kuimarisha Usalama wa Bahari unaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), na unatekelezwa na Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP) Tawi la Mwanza kwa ushirikiano na Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga ambapo Lengo lake ni kuimarisha ufuatiliaji na ulinzi wa bahari pamoja na kuongeza thamani ya rasilimali za baharini kwa manufaa ya jamii.

Mhe. Nderiananga amesema kupitia mradi huo, Serikali imenunua boti mbili za doria, kujenga kaushio la kisasa la mwani, kusimika mashine za kusaga mwani na kutoa mafunzo kwa vikundi vya wakulima. Ameongeza kuwa hatua hizo zitaboresha ubora wa mwani, kupanua masoko, kuongeza kipato cha wakulima na kusaidia kuzuia vitendo vya kihalifu baharini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP), Dkt. Guvenail Mkonoko, amesema kabla ya utekelezaji wa mradi huo wataalamu walifanya tathmini iliyobaini changamoto za mbinu duni za kilimo, ukaushaji usio salama na ukosefu wa miundombinu ya kisasa ya uchakataji.

Naye mwakilishi wa wakulima wa mwani, Bi. Mwamvua Bwebwe, Ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwawezesha kuongeza uzalishaji, kupunguza upotevu wa mazao na kuboresha kipato chao.



Read More

SERIKALI KUIFANYA TANZANIA KITOVU CHA BIASHARA - DKT. YONAZI

KATIBU Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. Jim Yonazi amesema Serikali imefanya juhudi mbalimbali za Kisera, Sheria na Kimkakati ili kuhakikisha Tanzania inakuwa kitovu cha biashara Afrika Mashariki na Kati.

Dkt. Yonazi aliyasema hayo katika kikao  cha Kikundi Kazi cha Mazingira ya Biashara cha Baraza la Taifa la Biashara TNBC kilichofanyika jijini Dar es salaam.

Alisema Serikali imefanya jitihada za kukuza biashara nchini huku akizitaka sekta binafsi kuendelea kushirikiana na serikali.

“Serikali imefanya juhudi mbalimbali katika uwekezaji nchini ikiwemo mazingira ya ufanyaji wa biashara ya kisera, kisheria na lengo ni kuhakikisha Tanzania inakuwa kitovu cha biashara Afrika mashariki na kati.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Biashara (TNBC) Dkt. Godwill Wanga  alisema kikao hicho kimefanyika ili kujadili maendeleo ya biashara nchini.

Alisema kikao hicho kimejadili vivutio  ambavyo serikali inaweza kufanya uwekezaji zaidi katika sekta ya afya  ili bima ya afya kwa wote itakapoanza iweze kuwa na faida kwa Watanzania.

“Kikao hichi ni muendelezo wa vikao ambavyo tumekuwa tukifanya mara kwa mara katika kujadili maendeleo ya biashara ambapo katika kikao hiki kimejadili kuhusu miundombinu ya mtandao katika  katika nchi yetu.

Aliongeza kuwa :”Tumekubaliana kufanya utafiti kuhusu madhara ya vita katika mashariki ya kati katika uchumi wetu.

 

 

Read More

Friday, March 13, 2026

DKT. YONAZI AONGOZA MKUTANO WA TANZANIA NATIONAL COORDINATING MECHANISM - (TNCM)

Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa inayosimamia na kuratibu fedha za Global Fund inayojulikana kama Tanzania National Coordinating Mechanism – (TNCM) ameongoza Kikao cha (TNCM) kilichofanyika katika Ukumbi wa Serengeti, Jengo la FCC, jijini Dar es Salaam.

 Katika mkutano huo, mambo mbalimbali yamejadiliwa ikiwemo maandalizi ya awali ya kuandaa andiko la maombi ya ufadhili wa awamu ya nane ya Mfuko wa Dunia (Global Fund Grant Cycle 8 - GC8). Aidha, Dkt. Yonazi amesisitiza umuhimu wa kuwa na mipango madhubuti na yenye tija ili kuhakikisha Tanzania inanufaika kikamilifu na rasilimali hizo katika mapambano dhidi ya magonjwa ya UKIMWI, Kifua Kikuu, na Malaria, pamoja na kuimarisha mifumo ya afya kwa ujumla.

Akifunga mkutano huo, Dkt. Yonazi amewahimiza wajumbe na wadau wote kuendeleza ushirikiano na uwazi (Transparency) katika hatua za maandalizi ya GC8, huku akibainisha kuwa ufanisi wa (TNCM) unategemea sauti ya pamoja ya wadau wote wanaowakilishwa.

Mkutano huo uliowahusisha wadau kutoka Serikalini, Sekta Binafsi, Asasi za Kiraia, na Washirika wa Maendeleo, umelenga kujadili masuala mtambuka ya uendeshaji wa taasisi hiyo pamoja na kuweka misingi imara ya upatikanaji wa rasilimali katika sekta ya afya nchini.

Mbali na hayo, katika mkutano huo, wajumbe walimchagua Bw. Godlisten Moshi kuwa Makamu Mwenyekiti mpya wa (TNCM) ili kukamilisha safu ya uongozi na kuongeza ufanisi katika utendaji wa chombo hicho.


Read More

Monday, March 2, 2026

VIJANA WA VYUO VIKUU NA VYUO VYA KATI WASISITIZWA KUENDELEZA MAPAMBANO DHIDI YA VVU NA UKIMWI


Serikali imehamasisha  mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI kwa kundi la vijana katika  Chuo cha Uhasibu Arusha  (IAA) na Taasisi ya Maendeleo ya Jamii ya Tengeru.

Hamasa hiyo imetolewa leo na Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. Ummy Nderiananga katika  ziara yake ya  kufuatilia na kutathimini utekelezaji wa Afua za VVU na UKIMWI katika vyuo vya kati na Vyuo Vikuu Jijini Arusha.

Mhe. Nderiananga, ameipongeza Tume ya kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS)  kwa kazi kubwa ya kusimamia utekelezaji wa Afua za VVU na UKIMWI waliofanya kwenye Taasisi 26 za vyuo vya kati na Vyuo Vikuu nchini, na kuwapongeza vijana wa Vyuo hivyo kwa  kupambana nakuchukua tahadhali na kuzungatia elimu  ya kinga na maambukiz ya Virusi vya UKIMWI waliyoipata kupitia wataalam mbalimbali.

Pia, Mhe. Nderiananga amesisitiza kundi la vijana haswa wa Kiume kuhamasika katika upimaji ili watambue hali za Afya zao na kuhimiza Ufuasi mzuri wa Dawa za kufubaza virusi vya UKIMWI kwa waathirika wapya, lakini pia amewapongeza Waathirika wote wa VVU  kote nchini kwa matumizi sahihi ya ARV.

Awali, Mkurugenzi wa Idara ya Mwitikio wa Kitaifa wa UKIMWI kutoka Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) Bi Audrey Njelekera, Amesema kuwa Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali kupitia takwimu zilizopo inamipango madhubuti ya kupunguza na kutokomeza maambukizi ya VVU na UKIMWI nchini kote.

Ameongeza kuwa, takwimu zinaonyesha kuwa kundi la vijana kuanzia miaka 15 hadi 24 ndio linaloathirika zaidi na maambukizi mapya hivyo TACAIDS imeanzisha  Klabu za kijamii kwenye vyuo vya kati na vikuu ili kusaidia  kupunguza unyanyapaa, kuongeza idadi ya wanafunzi kupima na kuongeza ushiriki wa wanafunzi katika mapamabano dhidi ya VVU. Vilevile, kuanzisha programu mbalimbali za kuhamasisha na kuelimisha kupitia mijadala, kuandika machapisho,  vibonzo, picha mjongeo na kampeni za kwenye mitandao ya kijamii.

Nae, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Mipango, Fedha na Utawala wa  Chuo cha Uhasibu Arusha, Dkt. Eliakira Nnko amesema kuwa, Chuo kinaendelea kuweka  mipango na mikakati ya utekelezaji wa Afua za UKIMWI mahali pakazi  kwa watumishi na wanafunzi wanaoishi na maambukizi ya virusi vya UKIMWI, lengo kuu ni kuhakikisha Wanafunzi na watumishi wanabaki na Afya njema, Kupunguza vifo na kutokomeza unyanyapaa ili kuimarisha utendaji kazi na kuweka  mazingira salama kwa watumishi na  wanafunzi.



Read More

Sunday, March 1, 2026

SERIKALI YA AWAMU YA SITA YASISITIZA UWEZESHWAJI WA WATU WENYE ULEMAVU

 

Naibu Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Mhe. Ummy Nderiananga, amesisitiza dhamira ya Serikali ya kuendelea kuwawezesha kiuchumi watu wenye ulemavu kupitia mikopo ya asilimia 10 ya mapato ya Halmashauri, ikiwemo asilimia 2 inayotengwa mahsusi kwa kundi hilo.

Mhe. Nderiananga ametoa kauli hiyo leo Jijini Arusha alipokutana na watu wenye ulemavu ikiwa ni muendelezo wa Ziara yake iliyoanza Wilaya ya Moshi-Kilimanjaro.

Naibu Waziri Nderiananga, amewapongeza watu wenye ulemavu wa Mkoa wa Arusha kwa nidhamu ya kurejesha mikopo kwa wakati na kuhimiza waliomaliza kurejesha waweze kuomba tena ili kupanua shughuli zao za kiuchumi.

Aidha, ameelekeza kuwa 30% ya manunuzi ya umma kwenye Halmashauri zote za Jiji la Arusha ziende kwenye makundi haya maalum kama vile watu wenye ulemavu, “tunapotengeneza masoko  tutenge maeneo maalumu kwaaajili ya watu wenye ulemavu, na nataka kuona miradi ya watu wenye ulemavu kuwa ni miradi ya kielelezo Nchini’’Mhe. Nderiananga amesema

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Mhe. Mwinyi Ahmed Mwinyi ameishukuru Serikali ya  Awamu ya sita chini ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa juhudi za kuwakwamua kiuchumi watu wenye ulemavu, na  ameahidi kuandaa hafla kwaajili ya kuwapongeza wanufaika wa Mikopo ya 2% waliofanya vizuri ili iwe kama sehemu ya hamasa na kielelezo kwa wale ambao hawajafanyi vizuri na ambao wanatamani kupata mikopo hiyo.

Awali, Mkurugenzi wa Idara ya watu wenye ulemavu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu Bw. Kizito Wambura amesema Serikali inania thabiti ya kuleta mabadiliko kwa watu wenye ulemavu na  kutatua changamoto zilizobainishwa kupitia mfumo wa kieletroniki wa taarifa za watu wenye ulemavu (PDMIS) ambao tunategemea ufike kwenye maeneo yote ya Tanzania.




Read More