Monday, June 8, 2026

DKT. YONAZI AONGOZA KIKAO CHA MAKATIBU MAKUU CHA MAANDALIZI YA AFCON 2027


 Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Dkt.Jim Yonazi ameongoza Kikao cha Makatibu Wakuu cha Maandalizi ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) kwa ajili ya kupitia hatua mbalimbali zilizofikiwa katika maandalizi ya michuano hiyo mikubwa itakayofanyika mwaka 2027 katika nchi za Tanzania, Uganda na Kenya.

Dkt. Yonazi ameongoza kikao hicho leo katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ndogo ya Waziri Mkuu Magogoni jijini Dar es Salaam.

Ametumia nafasi hiyo kuwasihi wajumbe wa kikao hicho kuendelea kufanya maandalizi kwa weledi huku wakishirikisha sekta zote muhimu katika kufanikisha michuano hiyo na kufikia malengo yanayotarajiwa ili kuipa nchi heshima inayostahili.

“Kila sekta iendelee kutekeleza jukumu lake kwa ufanisi ili kuleta matokeo chanya, “ alisema Dkt. Yonazi

Aidha, Dkt. Yonazi amewashukuru wajumbe wote na kusema kuwa Ofisi yake itaendelea kuratibu shughuli hizo kwa ushirikiano wa pamoja.

Read More

SERA ZA KISEKTA ZATAKIWA KUENDANA NA DIRA 2050


Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) imewakumbusha wataalamu wa uchambuzi wa sera nchini kuimarisha jitihada za kuhakikisha sera zote zinaendana na Dira 2050 ili kuwezesha utekelezaji wenye tija na kuleta matokeo tarajiwa kwa wananchi.

Wito huo umetolewa leo Jijini Arusha na Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Uratibu wa Shughuli za Serikali, Bw. Paul Sangawe, alipokuwa akifungua kikao kazi maalum cha kuwajengea uwezo wataalamu wa uchambuzi wa sera kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu.

Bw. Sangawe amesema kuwa, sera zina mchango mkubwa katika kufanikisha malengo ya maendeleo ya Taifa, hivyo ni muhimu kuendana na Dira 2050.

“Ni muhimu sera zetu ziendane na Dira 2050 ili kuhakikisha utekelezaji wake unakuwa hai na matokeo yanayokusudiwa yanaonekana kwa wananchi na taifa kwa ujumla,” amesema Bw. Sangawe.

Aidha, ameipongea Taasisi ya Uongozi kwa mchango wanaotoa katika kuratibu sera na kujenga uwezo wa wataalam wa uchambuzi wa sera. 

Katika kikao kazi hicho, mada mbalimbali zimewasilishwa ikiwemo Dira 2050, hatua iliyofikiwa katika mapitio ya sera, nafasi ya sheria katika utekelezaji wa sera na uzoefu kutoka nchi nyingine.

Washiriki wa kikao hicho kutoka taasisi mbalimbali za Serikali na zisizo za Serikali wameishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuandaa mafunzo hayo na kueleza umuhimu wa mafunzo hayo kuwa endelevu. Aidha, akitoa ufafanuzi Mkurugenzi alieleza kuwa, mafunzo hayo yatakuwa endelevu. 

Vilevile, amewahakikishia wajumbe hao kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu itaendelea kushirikiana na wadau wote ikiwemo Tume ya Mipango katika kuhakikisha uratibu wa sera unaimarishwa nchini.

 





Read More

OWM, DIT YAINGIA MAKUBALIANO KUIMARISHA USIMAMIZI WA MAAFA NCHINI

 


SERIKALI kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) imeingia Makubaliano ya Ushirikiano (MoU) na Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam (DIT) yenye lengo la kuimarisha usimamizi wa maafa nchini kwa kutumia sayansi, teknolojia na ubunifu.

Akizungumza mapema hii leo (08 Juni, 2026) katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo Katibu Mkuu wa ofisi hiyo, Dkt. Jim Yonazi, amesema hatua hiyo ni utekelezaji wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa  Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kujenga mifumo madhubuti ya kiutendaji inayoongozwa na maarifa, sayansi na teknolojia ikiwemo matumizi ya Akili Unde (AI) katika kukabiliana na maafa.

Amesema makubaliano hayo yanatekeleza pia mapendekezo ya Mkutano wa Nane wa Umoja wa Mataifa wa Jukwaa la Dunia la Upunguzaji wa Vihatarishi vya Maafa uliofanyika Geneva, Uswisi, mwezi Juni 2025, na yanaashiria mabadiliko ya kimkakati katika namna Serikali inavyoshughulikia changamoto za maafa kutoka mfumo wa kusubiri majanga hadi mfumo wa kujikita katika kinga, maandalizi na tahadhari.

“Vyuo vikuu na taasisi za utafiti, ikiwemo Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam, zina jukumu muhimu la kuzalisha maarifa na suluhisho za kisayansi zitakazosaidia kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini,”amesema.

Ameongeza kuwa ili kuhakikisha utekelezaji madhubuti wa makubaliano hayo, Serikali itaandaa Mpango Kazi wa utekelezaji pamoja na Agenda ya Kitaifa ya Utafiti wa Usimamizi wa Maafa itakayobainisha maeneo ya kipaumbele yanayohitaji ufumbuzi wa kisayansi na kiteknolojia.

Dkt. Yonazi amesisitiza kuwa mafanikio ya makubaliano hayo yatapimwa kwa matokeo halisi yatakayochangia kuongeza usalama wa wananchi, kulinda rasilimali za taifa na kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya maafa.

Ushirikiano huo unaendana na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayoweka msisitizo katika matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu kama nguzo kuu ya maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii.

Kwa upande wake Mkuu wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam Prof.Preksedis Marco Ndomba amesema kuwa taasisi imeandika historia kwa kusaini hati ya ushirikiano na Ofisi ya Waziri Mkuu ambapo ameeleza kuwa mchakato huu ulianza muda mrefu na matunda yake yameanza kuonekana jambo ambalo ni mafanikio makubwa.

“Tunaahidi juu ya kufanikisha  makubaliano hayo kwa kuwa, uwezo huo tunao, utalaam upo wa kutosha kwa kushirikiana kwenye masuala ya viatarishi kitaifa ili kufanikisha adhima hii ya Serikali,” Alisema Profesa Ndomba.

 

Read More

Friday, June 5, 2026

SERIKALI YAZINDUA KITUO CHA OPERESHENI NA MAWASILIANO YA DHARURA MWANZA


SERIKALI imezindua rasmi Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura cha Mkoa wa Mwanza, hatua inayolenga kuimarisha uratibu wa shughuli za usimamizi wa maafa na majanga katika mkoa huo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo leo , Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mheshimiwa Said Mtanda, amesema kituo hicho ni nyenzo muhimu katika kufuatilia na kudhibiti matukio ya dharura kwa ufanisi zaidi.

Amesema kupitia kituo hicho, mkoa unaweza kufuatilia matukio ya dharura kwa karibu, kukusanya na kuchambua taarifa kwa wakati pamoja na kuimarisha mawasiliano kati ya wadau mbalimbali wa usimamizi wa maafa.

“Kupitia kituo hiki, taarifa muhimu zinafika kwa mamlaka husika kwa haraka ili kuwezesha maamuzi stahiki kufanyika kwa wakati,” anasema Mhe.Mtanda.

Ameongeza kuwa kituo hicho kinaunganishwa moja kwa moja na Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, hatua inayorahisisha mtiririko wa taarifa na kuimarisha uratibu wa shughuli za kukabiliana na maafa kati ya ngazi ya mkoa na taifa.

Kwa mujibu wa Mhe. Mtanda, hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za serikali kujenga mfumo jumuishi wa usimamizi wa maafa wenye uwezo wa kutoa mwitikio wa haraka na wenye ufanisi katika kukabiliana na majanga.

Aidha, amewataka watumishi na viongozi kutumia mafunzo wanayopata kujenga uelewa, kubadilishana uzoefu na kuimarisha mshikamano wa kiutendaji ili kuboresha zaidi usimamizi wa maafa katika Mkoa wa Mwanza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, amesema kituo hicho kina umuhimu mkubwa kwa mkoa wa Mwanza na taifa kwa ujumla.

Amesema kituo hicho kinakuwa kitovu cha ukusanyaji, uchambuzi na usambazaji wa taarifa za matukio ya dharura na maafa, ambapo kinaunganishwa moja kwa moja na Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, hivyo kuwezesha upatikanaji wa taarifa kwa wakati na kufanya maamuzi ya haraka na sahihi.

“Kupitia kituo hiki, Serikali inaweza kufuatilia vihatarishi mbalimbali, kutoa tahadhari za mapema, kuratibu rasilimali za kukabiliana na maafa na kuimarisha mawasiliano kati ya wadau wote wanaohusika na usimamizi wa maafa,”alisema.

Ameongeza kuwa, “Huu ni uwekezaji muhimu katika kuimarisha utayari wa mkoa na taifa kwa ujumla. Sambamba na hilo, timu ya mkoa ya kukabiliana na dharura tunayoizindua leo ndiyo nguzo kuu ya kukabiliana na matukio ya maafa kwa wakati.”

Vilevile amesema uzinduzi wa kituo hicho unakuja katika wakati muafaka ambapo serikali inaendelea kujiandaa na kuimarisha mifumo ya tahadhari ya mapema kufuatia taarifa kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania kuhusu uwezekano wa kutokea kwa hali mbaya ya hewa, ikiwemo athari zinazoweza kusababishwa na El Niño.

Read More

Thursday, June 4, 2026

TIMU KUTOKA OFISI YA WAZIRI MKUU YAFANYA MAZUNGUMZO NA KATIBU TAWALA MWANZA KUHUSU MASUALA YA USIMAMIZI WA MAAFA


 Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa Mwanza Bw. Henry Mwaijega amekutana na kufanya mazungumzo timu ya Idara ya Usimamizi wa Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu walipomtembelea ofisini kwake leo Jijini Mwanza.

Timu hiyo ipo mkoani Mwanza kwa lengo la kuongoza mafunzo ya usimamizi wa maafa kwa Kamati za Usimamizi wa Maafa mkoa pamoja na wadau mbalimbali, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha utayari, uratibu na uwezo wa kukabiliana na majanga katika ngazi ya mkoa.

Pamoja na mafunzo hayo, wanatarajia kuzindua Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura cha mkoa wa Mwanza tarehe 05 juni, 2026.

Read More

Friday, May 15, 2026

MHE.MMUYA AONGOZA UJUMBE WA TANZANIA KATIKA MKUTANO WA MAWAZIRI WANAOSHUGHULIKIA MAAFA NCHI ZA SADC ULIOFANYIKA ZIMBABWE

 


Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Mmuya ameongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa Sita (6) wa Kawaida wa Kamati ya Mawaziri Wanaohusika na Usimamizi wa Maafa kwa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu Mheshimiwa Profesa Palamagamba Kabudi unaofanyika Masvingo, Zimbabwe.

Aidha, Mkutano huo pamoja na masuala mengine umejadili maendeleo yaliyopatikana katika utekelezaji wa programu za kikanda na masuala ya kimkakati katika utekelezaji wa afua mbalimbali katika usimamizi wa maafa, pia mkutano huo utatumika kama jukwaa kwa Mawaziri kuimarisha ushirikiano na Washirika wa Maendeleo wa Kimataifa na Jumuiya ya Wafadhili kuhusu uwekezaji katika Usimamizi wa Maafa ili kujenga ustahimilivu wa kikanda.

Naibu Waziri Ameongozana na mwenyeji wake ambaye ni Balozi wa Tanzania nchini Zimbabwe Mhe. CP-Suzan Kaganda, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Brig.Jenerali Hosea Ndagala, Mkurugenzi Msaidizi Urasimishaji Makazi kutoka ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bw. Nicholaus Mwakasege, Mratibu wa Maafa Dkt. Baltazar Leba, Bw. Abubakar Juma kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,Msaidizi wa naibu waziri Bw. Blastus Kahemela, Msaidizi wa katibu mkuu Bw. Januari Kitunsi, pamoja na afisa habari Ofisi ya Waziri Mkuu, Bi. Nyamagory Kitwara.

Read More

Thursday, May 14, 2026

JUMUIYA YA UMOJA WA ULAYA YASHIRIKIANA (EU) NA SERIKALI KUKABILIANA NA MABADILIKO YA TABIA NCHI KIGOMA.


 Ofisi ya Waziri Mkuu-Sera, Bunge na Uratibu na wenye Ulemavu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya (EU) imeanza utekelezaji wa mradi wa Mwitikio wa Kikanda dhidi ya Uhamaji Unaotokana na Mabadiliko ya Tabia nchi  (Regional Responses to Climate Displacement in Subsaharan Africa- RE2CLID) unaolenga kujenga uhimilivu wa jamii zinazoishi maeneo yanayozunguka Ziwa Tanganyika mkoani Kigoma dhidi ya athari za mabadiliko ya tabia nchi.

 Mradi huo unafadhiliwa na Jumuiya ya Umoja wa Ulaya(EU) Unatekelezwa na mashirika ya IOM UN migration, Enabel na kusimamiwa na Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara za kisekta pamoja na Mashirika yasiyo ya kiserikali kama vile RedCross umezinduliwa rasmi na Mkurugenzi Msaidizi kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa Bw. Vonyvako Luvanda kwaniaba ya Naibu Katibu Mkuu Dkt.James Kilabuko, katika Hoteli ya Morena, Jijini Dodoma.

 Akizungumza katika uzinduzi huo Bw. Luvanda amesema, mradi huo unalenga kusaidia jamii zilizoathirika na kuhamishwa kutokana na kuongezeka kwa kina cha maji ya Ziwa Tanganyika pamoja na kuimarisha mifumo ya uratibu wa maafa na usimamizi wa rasilimali za asili.

 Pia, ameeleza kuwa mradi huo unaotekelezwa kwa kipindi cha miaka minne kuanzia mwaka 2025 hadi Septemba 2029 utaongeza uwezo wa jamii kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi huku ukipewa kipaumbele na Serikali pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo.

 Kwa upande wake, Mkuu wa Ushirikiano wa Jumuiya ya Umoja wa Ulaya (EU) Tanzania Bw. Marc Stalmans amesema EU imefadhili mradi huo wenye thamani ya Euro milioni 13 kwa lengo la kusaidia jamii zilizoathirika zaidi na mabadiliko ya tabia nchi, hususan wananchi wanaoishi maeneo yanayozunguka Ziwa Tanganyika.

 Ameongeza kuwa, ongezeko la kina cha maji limeharibu makazi, mashamba, barabara pamoja na huduma muhimu kama maji safi na umeme, hali inayosababisha wananchi wengi kupoteza maeneo yao ya kuishi.

 Aidha, amesema mradi huo utasaidia kutambua maeneo hatarishi na kuweka mipango ya muda mrefu ya kuhimili athari za mafuriko pamoja na kugharamia ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya kijamii ikiwemo shule, hospitali, miradi ya maji na barabara zilizoathirika.

 Naye, Katibu Tawala Msaidizi Mipango na Uratibu Mkoa wa Kigoma Bw. Justin Njuu, amesema kuwa mradi huu  umekuja wakati muafaka kwani wananchi wengi wameendelea kuathirika kutokana na kuongezeka kwa kina cha maji ya Ziwa Tanganyika, hali iliyoharibu maeneo ya kilimo na makazi na kuwalazimu baadhi yao kuhama kwenda maeneo mengine.

 

 

Read More

Wednesday, May 13, 2026

TANZANIA YATOA SOMO KWA NCHI ZA SADC KUHUSU USIMAMIZI WA MAAFA


 TANZANIA imeendelea kung’ara katika Ukanda wa Kusini mwa Afrika baada ya kutajwa kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza kwa mifumo madhubuti ya usimamizi wa maafa, hatua inayozifanya nchi nyingine wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kujifunza kupitia uzoefu wake.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Mmuya wakati akimwakilisha  Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe.Prof. Palamagamba Kabudi wakati wa Mkutano wa Sita wa Kawaida wa Kamati ya Mawaziri Wanaohusika na Usimamizi wa Maafa kwa nchi wanachama wa SADC unaofanyika mjini Masvingo, Zimbabwe.

Amesema Tanzania imefanikiwa kuimarisha mifumo ya kuzuia, kupunguza madhara, kujiandaa na kurejesha hali baada ya maafa kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa katika sekta ya uratibu wa maafa nchini.

Kwa mujibu wa Mhe. Mmuya amesema moja ya mafanikio makubwa ni kuanzishwa kwa Kituo cha Ufuatiliaji wa Mwenendo wa Majanga na Tahadhari ya Mapema (National Emergency Operation and Communication Center Situation Room), ambacho kinafanya kazi saa 24 kila siku kufuatilia na kuchambua taarifa za majanga.

“Kwa kupitia kituo hiki, Serikali imeweza kupata taarifa za mapema kuhusu majanga yanayoweza kutokea, kufanya uchambuzi wa madhara na kuweka mikakati ya haraka ya kukabiliana nayo,” alisema Mhe Mmuya.

Aliongeza kuwa matumizi ya teknolojia ya kisasa katika ukusanyaji na uchambuzi wa takwimu za wakati halisi yamechangia kuongeza ufanisi wa maamuzi na kurahisisha utoaji wa taarifa rasmi kwa wananchi kuhusu namna ya kujiandaa dhidi ya maafa.

“Tunatumia takwimu za sasa na za zamani kutabiri hatari zinazoweza kujitokeza, jambo ambalo linaisaidia Serikali kupanga kwa usahihi hatua za kurejesha hali na kuendelea kulinda maisha ya wananchi,” alisisitiza

Aidha, aliwaalika wajumbe kutoka nchi wanachama wa SADC kutembelea Tanzania ili kujionea namna mifumo hiyo inavyofanya kazi pamoja na ubunifu unaotumika katika usimamizi wa maafa.

Mkutano huo wa siku nne umezikutanisha nchi 16 wanachama wa SADC pamoja na wataalamu wa kitaifa na mashirika ya kimataifa kujadili utekelezaji wa programu za kikanda za usimamizi wa maafa na namna ya kuimarisha ushirikiano wa kikanda.

Pamoja na mambo mengine, mkutano huo unatarajiwa kuwa jukwaa muhimu kwa mawaziri na washirika wa maendeleo kujadili uwekezaji katika sekta ya usimamizi wa maafa kwa lengo la kujenga ustahimilivu wa kikanda dhidi ya majanga mbalimbali yanayoendelea kujitokeza duniani.

Read More

Tuesday, May 12, 2026

NAIBU WAZIRI MMUYA AWASILI ZIMBABWE KUSHIRIKI MKUTANO WA SITA WA MASUALA YA MAAFA NCHINI ZIMBABWE



Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Mmuya (Mb), amewasili nchini Zimbabwe kushiriki Mkutano wa Sita (6) wa Kawaida wa Kamati ya Mawaziri Wanaohusika na Usimamizi wa Maafa kwa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu Mheshimiwa Profesa Palamagamba Kabudi unaofanyika Masvingo, Zimbabwe kuanzia tarehe 11 haadi 14 Mei, 2026.

Mara baada ya kuwasili, Mhe. Mmuya amepokelewa na Balozi wa Tanzania nchini humo, Mhe. Balozi Suzan S. Kaganda na kuipongeza Tanzania kushiriki katika mkutano huo unaolenga kujadili maendeleo yaliyopatikana katika utekelezaji wa programu za kikanda na masuala ya kimkakati katika utekelezaji wa afua mbalimbali katika Usimamizi wa maafa kwa nchi za SADC.

Masuala mengine yaliyoelezwa na Mheshimiwa Balozi Suzani ni  pamoja na Tanzania kuendelea kuzitangaza fursa zilizopo ikiwemo sekta ya utalii, uchukuzi pamoja na kilimo  huku akiahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano uliopo baina ya Tanzania na Zimbabwe.

Sambamba na hayo, mkutano huo utahudhuriwa na wadau mbalimbali wa masuala ya Usimamizi wa Maafa kutoka Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) ambapo ni fursa kwa Tanzania kuendelea kujitangaza Kimataifa kwa kuwa na mifumo thabiti ya Usimamizi wa Maafa pamoja na  kubadilishana uzoefu kuhusu masuala ya Menejimenti ya maafa.

Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizoshiriki katika Mkutano huo wa siku Nne ambapo umekutanisha wadau wa  masuala ya maafa kutoka nchi kumi na sita wakiwemo wataalamu kutoka  katika ngazi za Kimataifa pamoja na Mashirika ya Umoja wa Kitaifa.

Read More

SERIKALI YAPOKEA VIFAA VYA TEHAMA KUIMARISHA MFUMO WA KUKABILIANA NA MAAFA


 Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa imepokea vifaa vya TEHAMA vyenye thamani ya shilingi milioni 120 kutoka Shirika la Chakula Duniani (WFP), kwa lengo la kuimarisha vituo vya operesheni na mawasiliano ya dharura pamoja na utekelezaji wa mfumo wa Anticipatory Action (AA).

 Vifaa hivyo vinavyojumuisha kompyuta za mezani, runinga kubwa tatu za inchi 100 pamoja na mashine za kuchapisha, vimekabidhiwa leo  katika hafla iliyofanyika katika ofisi za WFP jijini Dodoma na kuzinduliwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule.

 Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Senyamule amesema Serikali inaendelea kuwekeza katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia ya nchi na majanga mbalimbali, huku akisisitiza umuhimu wa taarifa kuwafikia wananchi kwa wakati na kwa ufanisi.

 “Vifaa hivi vitaongeza ubora na ufanisi wa taarifa zinazowafikia wananchi kwa haraka ili waweze kuchukua tahadhari dhidi ya maafa yanayoweza kutokea,” amesema Mhe. Senyamule huku akiishukuru (WFP) kwa mchango wake katika kuimarisha sekta ya menejimenti ya maafa nchini.

 Kwa upande wake, Naibu Mwakilishi Mkazi wa (WFP) Bi. Christine Mendes amesema tafiti zinaonyesha kuwa uwekezaji katika maandalizi na kinga dhidi ya majanga ni nafuu zaidi kuliko gharama za kukabiliana na madhara baada ya majanga kutokea. Amesema ushirikiano huo unalenga kujenga ustahimilivu na maendeleo endelevu ya jamii.

Awali, Mkurugenzi Msaidizi wa Operesheni na Uratibu wa Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (SBUU), Kanali Selestine Masalamando amesema vifaa hivyo ni sehemu ya jitihada za Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuimarisha mfumo wa Taifa wa menejimenti ya maafa na kuongeza uwezo wa kukabiliana na majanga yanayoikumba nchi.

 Kanali Masalamando ameongeza kuwa vifaa hivyo vitasaidia kuimarisha ufuatiliaji wa vihatarishi, utoaji wa tahadhari za mapema, ukusanyaji na uchambuzi wa taarifa za maafa pamoja na kuboresha uratibu na mawasiliano kati ya ngazi ya Taifa, mikoa na wilaya wakati wa majanga.

 

Read More

Monday, May 11, 2026

TANZANIA KUENDELEA KUTUMIA AKILI UNDE KATIKA KUKABILIANA NA MAAFA

TANZANIA imesema itaendelea kutumia teknolojia ya Akili Unde (AI) katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini ili kuongeza ufanisi wa utoaji wa tahadhari za mapema na kupunguza madhara yanayosababishwa na majanga mbalimbali.

Hayo yameelezwa na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, wakati wa mkutano wa maandalizi ya Mkutano wa Sita wa Kawaida wa Kamati ya Mawaziri Wanaohusika na Usimamizi wa Maafa kwa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) uliofanyika  mjini Masvingo, Zimbabwe.

Alisema matumizi ya AI yatasaidia uchakataji na ufuatiliaji wa taarifa mbalimbali zinazoripotiwa kuhusu masuala ya maafa nchini, hatua inayolenga kuongeza uwezo wa Serikali katika kufanya maamuzi ya haraka wakati wa majanga.

“Matumizi ya teknolojia ya Akili Unde yatawezesha uchambuzi wa taarifa kwa haraka, kutabiri hatari zinazoweza kujitokeza na kusaidia hatua za mapema za kukabiliana na maafa,” alisema Dkt. Yonazi.

Dkt. Yonazi alisema Serikali inaendelea kuweka mkazo katika maeneo muhimu yatakayosaidia kuwa na usimamizi wenye tija wa maafa ikiwemo utafiti wa kisayansi, matumizi sahihi ya Akili Unde, ushirikiano katika uhifadhi wa taarifa za matukio pamoja na matumizi ya menejimenti ya maarifa.

Aidha alisema Tanzania imeendelea kuwa mfano katika ukanda wa Kusini mwa Afrika kutokana na uwezo wake wa kuratibu na kusimamia maafa kwa mafanikio huku ikiendelea kuzuia, kupunguza madhara, kujiandaa na kurejesha hali pindi majanga yanapotokea.

Alifafanua kuwa mafanikio hayo yamechangiwa na uwepo wa Kituo cha Ufuatiliaji wa Mwenendo wa Majanga na Tahadhari ya Mapema ambacho hufanya kazi saa 24 kupokea, kufuatilia na kuchambua taarifa za majanga kwa wakati halisi.

“Kituo cha Operesheni ya Maafa kimekuwa msaada mkubwa kwani kimerahisisha upatikanaji wa taarifa za mapema, uchambuzi wa takwimu za wakati halisi na upangaji wa mikakati ya kurejesha hali pamoja na kutoa elimu kwa umma kuhusu namna ya kujiandaa na kukabiliana na maafa,” alisisitiza.

 

 

Read More

Wednesday, May 6, 2026

URASIMISHAJI WA UKALIMANI WA LUGHA YA ALAMA WASISITIZWA


Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Watu Wenye Ulemavu), Mhe. Ummy H. Nderiananga (Mb), amesisitiza umuhimu wa kuharakisha urasimishaji wa tasnia ya ukalimani wa Lugha ya Alama ya Tanzania, ili kuhakikisha watu wenye ulemavu wa kusikia wanapata huduma kwa usawa.

Akifungua kikao cha mashauriano kilichoandaliwa na Chama cha Viziwi Tanzania (CHAVITA), na kuhudhuriwa na viongozi wa Shirikisho la Vyama vya Watu Wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA), Wabunge pamoja na wadau mbalimbali, Jijini Dodoma, Mhe. Nderiananga amesema hatua hiyo itasaidia kuweka viwango vya taaluma, kuboresha mafunzo, na kutambua rasmi wakalimani wa Lugha ya Alama nchini.

Aidha, Mhe. Nderiananga amesema kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuandaa miongozo na kanuni zitakazosaidia kusimamia taaluma hiyo, huku akihimiza jamii kuongeza uelewa wa matumizi ya Lugha ya Alama, ili kuondoa vikwazo vya mawasiliano.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa CHAVITA, Bi. Selina Mlemba amesema, urasimishaji wa tasnia ya ukalimani wa Lugha ya Alama ni hatua muhimu katika kuhakikisha haki za watu wenye ulemavu wa kusikia zinalindwa na kutekelezwa kwa vitendo.

Aidha Bi. Mlemba ameongeza kuwa CHAVITA itaendelea kushirikiana na Serikali pamoja na wadau wengine ili kuhakikisha kunakuwepo na miongozo, mafunzo, pamoja na mfumo rasmi wa usajili wa wakalimani wa Lugha ya Alama nchini, sambamba na hilo amesisitiza kuwa hatua hiyo itachangia kuongeza ubora wa huduma katika sekta mbalimbali na kuwezesha ushiriki kamili wa watu wenye ulemavu wa kusikia katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Washiriki wa kikao hicho wameitaka Serikali kuipa kipaumbele tasnia hiyo, wakisisitiza umuhimu wa ajira kwa wakalimani wa Lugha ya Alama katika sekta zote, pamoja na kuimarisha mafunzo na utambuzi wa taaluma hiyo ili kuboresha huduma kwa watu wenye ulemavu wa kusikia.

Read More

Friday, May 1, 2026

OFISI YA WAZIRI MKUU YASHIRIKI MAADHIMISHO YA MEI MOSI 2026 DODOMA

Watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) wameungana na watumishi wengine wa Serikali kusherehekea Siku ya Wafanyakazi Duniani leo, Mei 1, 2026, katika Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma.

Maadhimisho hayo yameongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, ambapo alisisitiza umuhimu wa wafanyakazi kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na kujituma ili kuchochea maendeleo ya taifa.

Amesema kuwa mchango wa wafanyakazi ni msingi muhimu katika kufanikisha malengo ya maendeleo ya nchi, hasa katika kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Kaulimbiu ya mwaka huu ni: “Kazi Zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050”, ikilenga kuhamasisha mazingira bora ya kazi na ustawi wa wafanyakazi nchini.



Read More

Thursday, April 30, 2026

SERIKALI YASISITIZA MATUMIZI YA MFUMO WA PD-MIS MKOANI ARUSHA


 Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu-Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu imehimiza watendaji wa Halmashauri zote za Jiji la Arusha matumizi ya Mfumo wa ukusanyaji na usimamizi wa taarifa za watu wenye ulemavu.

Hayo yamesemwa katika Mafunzo yavitendo yaliyofanyika katika kata nne za jiji hilo ikiwa ni muendelezo na hitimisho la mafunzo ya mfumo wa PD-MIS yaliyowakutanisha wataalamu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu na maafisa ustawi wa jamii na TEHAMA jutoka Halmshauri zote za jiji la Arusha, yaliyochukua siku tatu ambapo makundi ya watu mbalimbali ya watu wenye ulemavu yamejitokeza kuitikia wito wa kujisajili katika mfumo.

Akizungumza wakati wa kilele cha mafunzo hayo, Afisa kutoka kitengo cha huduma kwa watu wenye ulemavu Ofisi ya Waziri Mkuu Bw.Gerold Komba ametoa shukrani za dhati Uongozi wa Mkoa na Maafisa ustawi wa jamii na Maafisa TEHAMA kwa kushiriki kikamilifu katika mafunzo hayo tangu siku ya kwanza, Aidha aliwapongeza baadhi ya watu wenye ulemavu waliojitokeza kushiriki .

Amesisitiza kuwa ujuzi uliopatikana utakuwa nguzo muhimu katika kutekeleza majukumu ya msingi ya ukusanyaji wa na usimamizi wa taarifa za watu wenye ulemavu.

Mafunzo haya yanatazamwa kama hatua ya kimkakati ya kuhakikisha Maafisa na Watendaji  wanakuwa na uelewa mpana wa kutekeleza majukumu yao katika kuwahudumia watu wenye ulemavu ikiwa ni pamoja na kukusanya na kusimamia taarifa za watu wenye ulemavu mkoani humo,jambo litakalosaidia kuimarisha  upatikanaji wa takwimu sahihi na kuimarisha na kuobresha upatikanji wa huduma kwa watu wenye ulemavu na kuinua Uchumi kwa watu wa Kundi hili.



Read More

Wednesday, April 29, 2026

SERIKALI YASISITIZA USHIRIKI WA VIJANA KATIKA UKUAJI WA UCHUMI


Serikali imesisitiza kuwa, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inatoa kipaumbele cha pekee kwa ushiriki wa vijana katika maendeleo, kwa lengo la kuinua vipaji, uwezo, na ari yao katika kufanikisha ukuaji wa uchumi jumuishi.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Prof. Palamagamba Kabudi,  leo jijini Dodoma wakati akifungua kongamano la kwanza la kisayansi la vijana kuhusu VVU/UKIMWI, afya ya uzazi, jinsia na masuala mtambuka. Kongamano hilo limeandaliwa na Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS).

Akizungumza katika hafla hiyo, Prof. Kabudi alisisitiza kuwa dhamira kuu ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ni kujenga taifa lenye nguvukazi iliyoelimika, yenye ujuzi na maono.

"Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inatoa kipaumbele kwa vijana kwa kutumia vipaji na uwezo wao katika kufanikisha maendeleo endelevu. Nguvukazi hii itajengwa katika misingi imara ya ubunifu, ujasiriamali, na uwajibikaji," amesema Prof. Kabudi.

Katika hatua nyingine, Waziri Kabudi amebainisha kuwa, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeweka kipaumbele katika kushughulikia changamoto za ukatili wa kijinsia na afya ya akili.

Ameeleza kuwa, serikali imeanzisha madawati maalum ya ulinzi katika maeneo mbalimbali, ikiwemo shuleni, vyuoni, na kwenye ngazi ya jamii ili kuhakikisha huduma za kinga na msaada zinawafikia wahitaji kwa wakati.

Awali, akimkaribisha Waziri, Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. James Kilabuko, amebainisha umuhimu wa kongamano hilo kwa ustawi wa vijana.

"Kongamano hili ni chachu ya mabadiliko ya fikra na utendaji, tunatarajia elimu watakayopata itakuwa mwanzo wa safari ya kujenga jamii yenye afya, matumaini, na uwezo wa kufanya maamuzi sahihi kwa mustakabali wao," amesema  Dkt. Kilabuko.

Kongamano hilo la siku mbili linaongozwa na kaulimbiu; ‘’Kuunganisha Sayansi na Ubunifu katika Kukabiliana na Janga la VVU, Afya ya Uzazi na Jinsia, Kukuza Ustawi Kuelekea Dira 2050”.




Read More

KAGERA KUNUFAIKA NA MPANGO WA MKOA WA AFYA MOJA

KAIMU Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Bw. Salum Kimbau amesema maandalizi ya Mpango wa Afya Moja kwa mkoa wa Kagera utaunufaisha mkoa huo kwa kuzingatia malengo yake ya kuboresha uratibu na utekelezaji wa Dhana ya Afya ya Moja na kuendelea kutatua changamoto zilizopo na zenye mwingiliano kati ya binadamu, wanyama na mazingira

Amezungumza hayo wakati akifungua kikao kazi cha wataalamu wa masuala ya Afya Moja kutoka sekta mbalimbali zikiwemo za afya, mifugo, mazingira, wanyamapori na kilimo ambao wamekutana katika Halmashauri ya Wilaya ya Muleba mkoani Kagera kwa siku tano kuanzia tarehe 27 Aprili hadi 01 Mei, 2026 ili kuandaa Mpango huo utakaotumika kubaini rasilimali zitakazosaidia kutatua changamoto na vihatarishi vya afya ya binadamu, wanyama na mazingira.

Bw. Kimbau amesema kuwa, mkoa utanufaika kwa uwepo wa Mpango huo kwani utaongeza tija katika kutatua changamoto zinazokabili sekta hizo hususan katika kuendelea kutatua changamoto za mwingiliano wa magonjwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu na binadamu kwenda kwa wanyama.

“Tunashukuru kuufikia mkoa wetu wa Kagera, tunajua kuwa asilimia 75 ya magonjwa yanatokana na mwingiliano ulipo kati ya wanyama na binadamu, hivyo kuandaliwa kwa mpango kutasaidia utekelezaji wa Dhana ya Afya Moja kwa kushirikiana pamoja, hivyo utatusaidia kutatua changamoto zilizopo na kuwa na jamii salama,” alisema Bw. Kimbau

Aliongezea kuwa ufanisi wa mpango huu unategemea ushirikishwaji wa sekta zote zinazohusika ili kuleta matokeo chanya.

Naye Mratibu wa Maafa kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa sehemu ya Afya Moja kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Valentina Sanga amesema kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Shirika lisilo la Serikali la CIHEB Tanzania kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani imeratibu maandalizi ya uwepo wa mpango huo huku akisihi kuunganisha nguvu ya pamoja katika kuhakikisha utekelezaji wake unaleta matunda yanayotarajiwa.

Aidha, aliwasihi wataalamu wa Masuala ya Afya Moja kutumia fursa hiyo kuja na Mpango utakaoinufaisha Kagera, kwa kuzingatia ni miongoni mwa Mikoa inayokumbwa na majanga ya mlipuko mengine yakichangiwa na mwingiliano wa wanyama na binadamu.

“Dhana ya Afya Moja (One Health) inatoa fursa ya kutambua uhusiano wa karibu kati ya afya ya binadamu, wanyama, na mazingira. Inasisitizwa kuendelea kujifunza zaidi dhana hii ili kutatua changamoto zilizopo zikiwemo za milipuko ya magonjwa na kuweza kuyakabili endapo yanatokea katika maeneo yetu,” alisisitiza Bi. Valentina

Aliongezea kuwa, Mpango huo utasaidia kutatua changamoto za masuala ya kiafya zinazotokea katika Halmashauri za mkoa wa Kagera, kujiandaa na kukabili majanga hayo ili kuwa na jamii salama kwa maendeleo ya Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Shirika la CIHEB Tanzania, Bw. Mark Lwakatare alisema mradi wa Usalama wa Afya Duniani utaendelea kushirikiana na mikoa husika katika kuimairisha utekelezaji wa dhana ya Afya Moja ili nchi iweze kukabiliana na vihatarishi vya majanga mbalimbali.

“Mradi huu unashirikiana na Serikali kuboresha na kuimarisha utekelezaji wa afua mbalimbali kupitia dhana ya Afya Moja nchini, hivyo mradi utaendelea kushirikiana katika kujiandaa na kukabili athari katika afya ya binadamu, manyama na mazingira,” alisisitiza Lwakatare.

Read More

Tuesday, April 28, 2026

SERIKALI YAENDELEA KUIMARISHA MATUMIZI YA MFUMO WA PD-MIS KWA WATENDAJI ARUSHA


Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu imeendelea kuimarisha huduma kwa watu wenye ulemavu kwa kutoa mafunzo ya matumizi ya Mfumo wa Kielektroniki wa Ukusanyaji na Usimamizi wa Taarifa za Watu Wenye Ulemavu (PD-MIS) kwa watendaji wa mkoa wa Arusha.

Mafunzo hayo yametolewa na Wataalamu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu kwenda kwa Maafisa Ustawi wa Jamii pamoja na Maafisa TEHAMA kutoka halmashauri mbalimbali za Mkoa wa Arusha kwa lengo la kuwajengea uwezo na kuimarisha matumizi ya mfumo huo katika ukusanyaji, uhifadhi na usimamizi wa taarifa sahihi za watu wenye ulemavu yamefanyika, katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Afisa kutoka Kitengo cha Huduma kwa Watu Wenye Ulemavu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Bw. Gerold Komba, alisema Serikali inaendelea kuhakikisha inaendelea kuweka mipango yake vizuri katika kuhakikisha kwamba kundi hili la watu wenye ulemavu linahudumiwa ipasavyo nchi nzima.

Alisema Mfumo huu wa PD-MIS kwasasa umeshasambazwa katika mikoa mbalimbali ambapo kwasasa mikoa yote ya Kanda ya ziwa, Magharibi na Kanda ya Kusini imeshafikiwa na Mfumo huu, na kwasasa Mfumo umeanza kanda ya kaskazini katika mkoa wa Arusha.

Kwa upande wake Afisa Ustawi wa jamii Mkoa wa Arusha Bw. Dennis Mgie ameishukuru Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuandaa mafunzo haya kwani kupitia Mfumo huu takwimu za mkoa zinakua zenye ufanisi lakini pia zitawaongoza kwenye kutoa huduma kwa watu wenye ulemavu.

"Takwimu hizi zitatusaidia kuweza kuwaunganisha watu wenye ulemavu na huduma na fursa mbalimbali ambazo serikali inawezesha watu wenye ulemavu ambao tutawatambua kwa hali zao na kazi zao kupitia mfumo huu". Amesema Bw. Mgie.

 

 





 

Read More

Saturday, April 18, 2026

WATUMISHI OFISI YA WAZIRI MKUU WAJENGEWA UWEZO UENDESHAJI HUDUMA NATIONAL CALL CENTER

Watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) wamejengewa uwezo katika usimamizi wa mawasiliano kwa wananchi na mbinu bora za kuhudumia wananchi pamoja na matumizi ya mifumo ya kisasa ya National call centre.

Mafunzo hayo yamefanyika Jijini Dar es Salaam ambapo Muwezeshaji Bw. Willynevilline Msamo kutoka Benki ya NMB alieleza umuhimu uwezo wa kushughulikia mawasiliano kwa ufanisi na kuongeza kasi ya utoaji wa huduma ili kuhakikisha kila mwananchi anayewasiliana na taasisi anapata msaada unaostahili kwa wakati.

“Uanzishwaji na uimarishaji wa huduma za call centre, Ofisi ya Waziri Mkuu unalenga kutatua changamoto za wananchi kwa haraka kwa kuweka mfumo rahisi na wa moja kwa moja wa kupokea na kushughulikia maoni, malalamiko na mapendekezo yao,” alifafanua

Aidha huduma hii itawawezesha wananchi kupata mrejesho kwa wakati, kufuatilia masuala yao kwa ufanisi, pamoja na kuongeza uwazi na uwajibikaji katika utoaji wa huduma za serikali.

Bw, Msamo alisema, “hatua hii inaonesha dhamira ya Ofisi ya Waziri Mkuu ya kuendelea kuboresha mifumo ya mawasiliano na kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi kwa haraka, kwa ufanisi na kwa viwango vya juu zaidi”.


Read More