Sunday, March 29, 2020

MAJALIWA ASHIRIKI MAZISHI YA WAZIRI KIONGOZI MSTAAFU WA ZANZIBAR

Rais wa Zanzibar, Dkt. Ali  Mohamed Shein akizungumza na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  katika mazishi ya Waziri Kiongozi  Mstaafu wa Zanzibar, Brigedia Jenerali Mstaafu, Ramadhani Haji Faki yaliyofanyika  Mkwajuni  Zanzibara Machi 29, 2020.

Askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), wakiwa wamebeba jeneza la  Waziri Kiongozi Mstaafu wa Zanzibar, Brigedia Jenerali Mstaafu, Ramadhani Haji Faki katika mazishi yaliyofanyika Mkwajuni , Zanzibar, Machi 29, 2020. Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alihudhuria mazishi hayo.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiweka udongo kwenye kaburi la Waziri Kiongozi wa Zanzibar Mstaafu, Brigedia Jenerali Mstaafu, Ramadhani Haji Faki yaliyofanyika  Mkwajuni  Zanzibar,  Machi 29, 2020.


Read More

MAJALIWA ATOA POLE KWA FAMILIA YA SOKOINE

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Balozi Joseph Sokoine (katikati) na Mkuu wa Wilaya Mstaafu, Kipuyo Lemburs wakati alipotoa pole kwa familia ya aliyekuwa Waziri Mkuu wa Tanzania,  Hayati Edward Moringe Sokoine iliyoondokewa na Lazaro Edward Sokoine jijini Dar es salaam Machi 29, 2020.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na familia ya Waziri Mkuu wa zamani wa Tanzania, Hayati Edward Moringe Sokoine wakati alipokwenda kutoa pole kwa familia hiyo imeondokewa  na Lazaro Edward Sokoine jijini Dar es salaam, Machi 29, 2020. Kutoka kushoto ni Balozi Joseph Sokoine ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu,Ofisi ya Makamu wa Rais, Halima Jama, Mama Napono Sokoine , Christina Towo Sokoine na Kulia ni Mkuu wa Wilaya Mstaafu, Kivuyo Lemburs.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Balozi Joseph Sokoine (katikati) na Mkuu wa Wilaya Mstaafu, Kipuyo Lemburs wakati alipotoa pole kwa familia ya aliyekuwa Waziri Mkuu wa Tanzania,  Hayati Edward Moringe Sokoine ambayo imeondokewa na Lazaro Edward Sokoine, jijini Dar es salaam Machi 29, 2020.


Read More

Thursday, March 26, 2020

MAJALIWA: KAMATI ZA MAAFA ZIUNGANE NA WARATIBU WA KUKABILIANA NA CORONA


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameziagiza kamati za Maafa katika ngazi za mikoa na wilaya ziungane na waratibu wa kupambana na ugonjwa wa homa kali ya mapafu inayosababishwa na virusi vya corona (COVID-19) waliopo katika maeneo yao.

Pia, Waziri Mkuu amewasisitiza Watanzania waendelee kujikinga na ugonjwa huo kwa kuhakikisha wanajiepusha na misongamano isiyokuwa ya lazima na hata wakienda kwenye maeneo ya kutolea huduma kama sokoni, vituo vya mabasi wapeane nafasi kati ya mtu mmoja na mwingine.

Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo (Alhamisi, Machi 26, 2020) wakati akiongoza kikao cha Kamati ya Kitaifa cha Kukabiliana na homa kali ya mapafu inayosababishwa na virusi vya corona (COVID-19) ofisini kwake Mlimwa jijini Dodoma. Kikao hicho kimehusisha wajumbe kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Waziri Mkuu ameiagiza Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ipeleke wataalamu katika maeneo yenye mahitaji makubwa kama kwenye viwanja vya ndege, vituo vya mabasi na bandarini.

“Lengo letu ni kuhakikisha nchi inabaki salama hivyo Watanzania tuendelee kuwa na tahadhari ya kutosambaa kwa ugonjwa huu na pale tunapokwenda kwenye maeneo ya kutolea huduma tujipe nafasi kati ya mtu mmoja na mwingine.”

Waziri Mkuu amesema kamati hiyo inatakiwa ifuatilie na isimamie vizuri ili kuhakikisha watu wote wanaoingia nchini wanapimwa na wanafuatilia ili kujua historia zao za safari katika kipindi cha siku 14, lengo likiwa ni kuzuia maambukizi hayo yasisambae kwa jamii.

Amesema watu wote waliopewa dhamana ya kuratibu zoezi la kupeleka watu walioko kwenye karantini, wahakikishe wahusika wanafika kwenye hoteli walizozichagua. Pia Serikali inafanya utaratibu wa kutenga maeneo ambayo watu watakuwa wanakaa bila gharama na yatakuwa na huduma zote muhimu.

Pia, Waziri Mkuu amevishukuru vyombo vya habari nchini kwa ushirikiano wanaoutoa kwa Serikali katika kuelimisha umma namna ya kujikinga na virusi vya corona, ambapo amevitaka viendelee na utaratibu huo kwani utasaidia wananchi kupata elimu na kuweza kujikinga na maabukizi hayo.

Machi 23, 2020, Waziri Mkuu aliunda kamati tatu kwa ajili ya kukabiliana na homa kali ya mapafu inayosababishwa na virusi ya corona (COVID-19).

 

Kamati hizo ni ya Kitaifa ambayo inaongozwa na Waziri Mkuu na itahusisha Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Ajira na Wenye Ulemavu, Waziri wa Ulinzi na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia.

 

Wengine ni Waziri Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Waziri wa Mambo ya Nje ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

 

Pia, Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Msemaji Mkuu wa Serikali, Waziri wa Fedha na Mipango wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na Waziri wa Fedha wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.


Katika kikao cha leo, Waziri Mkuu ameongeza wajumbe wawili ili waongeze nguvu katika kukabiliana na virusi vua corona ambao ni Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Vikosi vya SMZ wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

 (mwisho)

 

Read More

MAJALIWA AONGOZA KIKAO CHA KAMATI YA KITAIFA YA KUKABILIANA NA CORONA

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na wajumbe wa Kamati ya Kitaifa ya Kukabiliana na ugonjwa wa Corona,  ambayo yeye ni Mwenyekiti wake, katika kikao  kilichofanyika ofisini kwa Waziri Mkuu, Mlimwa jijini Dodoma, Machi 26, 2020.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na wajumbe wa Kamati ya Kitaifa ya Kukabiliana na ugonjwa wa Corona,  ambayo yeye ni Mwenyekiti wake, katika kikao  kilichofanyika ofisini kwa Waziri Mkuu, Mlimwa jijini Dodoma, Machi 26, 2020.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na wajumbe wa Kamati ya Kitaifa ya Kukabiliana na ugonjwa wa Corona,  ambayo yeye ni Mwenyekiti wake, katika kikao  kilichofanyika ofisini kwa Waziri Mkuu, Mlimwa jijini Dodoma, Machi 25, 2020.


Read More

Tuesday, March 24, 2020

MAJALIWA AONGOZA KIKAO KAZI CHA MAWAZIRI NA MAKATIBU WAKUU KUHUSU CORONA

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  akizungumza katika kikao kazi cha Mawaziri na Makatibu Wakuu   kuhusu ugonjwa wa Corona (COVID – 19) nchini kwenye ukumbi wa Hazina jijini Dodoma, Machi 23, 2020.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  akizungumza katika kikao kazi cha Mawaziri na Makatibu Wakuu   kuhusu ugonjwa wa Corona (COVID – 19) nchini kwenye ukumbi wa Hazina jijini Dodoma, Machi 23, 2020.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  akizungumza katika kikao kazi cha Mawaziri na Makatibu Wakuu   kuhusu ugonjwa wa Corona (COVID – 19) nchini kwenye ukumbi wa Hazina jijini Dodoma, Machi 23, 2020.
 Baadhi ya Mawaziri na Makatibu Wakuu wakimsikiliza Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wakati alipoungumza nao katika kikao kazi  kuhusu ugonjwa Corona  (COVIC -19) nchini kwenye ukumbi wa Hazina jijini Dodoma, Machi 23, 2020.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  akizungumza katika kikao kazi cha  Mawaziri na Makatibu Wakuu  cha kujadili ugonjwa  wa Corona (COVID- 19) nchini kwenye ukumbi wa Hazina jijini Dodoma, Machi 23, 2020. Katikati ni Waziri wa Afya,  Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu na kulia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia , Wazee na Watoto, Dkt. Zainab Chaula.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  akizungumza katika kikao kazi cha  Mawaziri na Makatibu Wakuu  cha kujadili ugonjwa  wa Corona (COVID- 19) nchini kwenye ukumbi wa Hazina jijini Dodoma, Machi 23, 2020. Katikati ni Waziri wa Afya,  Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu na kulia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia , Wazee na Watoto, Dkt. Zainab Chaula.


Read More

Monday, March 23, 2020

KAMATI YA USIMAMIZI MAAFA RUFIJI YATAKIWA KUREJESHA MIUNDOMBINU ILIYOATHIRIKA NA MAFURIKO


Mkurugenzi Idara ya Uratibu wa shughuli za Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Jimmy Matamwe akisiistiza umuhimu wa kurejesha miundombinu iliyoathirika na maafa ya mafuriko wakati akiongea na Kamati ya maafa ya wilaya ya Rufiji, tarehe 23 Machi, 2020.
Mkurugenzi Idara ya Uratibu wa shughuli za Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Jimmy Matamwe akimkabidhi Mkuu wa wilaya ya Rufiji, Mhe.  Juma Njwayo,  misaada,  ikiwa ni magodoro, mikeka, sabuni, vyandarua  na ndoo, kwa ajili ya waathirka wa  maafa ya mafuriko wilayani humo, tarehe 23 Machi, 2020.
Mkurugenzi Idara ya Uratibu wa shughuli za Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Jimmy Matamwe akiongozwa na Mbunge wa Jimbo la Rufiji Mhe. Mohamed Mchengerwa kukakagua maeneo yaliyoathirika na maafa ya mafuriko katika kata ya Muhoro kijiji cha Shela tarehe 23 Machi, 2020, takribani  Watu elfu ishirini wameathirika  na maafa hayo.
Baadhi ya wakazi wa kata ya Muhoro, kijiji cha shela wilayani Rufiji wakishuka kwenye mtumbwi wanaoutumia kuvuka na kuyafikia makazi yao baada ya barabara kujaa maji kutokana na athari ya maafa ya mafuriko. Miundombinu ya barabara , shule na zahanati katika wilaya hiyo imeathirika na maafa hayo.
Baadhi ya misaada, kwa ajili ya waathirika wa maafa ya  mafuriko wilayani Rufiji, ikiwa imepelekwa wilayani humo na Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu Maafa tarehe 23 Machi, 2020, ambapo misaada  hiyo ni  magodoro, mikeka, vyandarua, sabuni na ndoo. Takribani kaya elf sita zinakadiriwa kuathirika na maafa hayo.
Mkurugenzi Idara ya Uratibu wa shughuli za Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Jimmy Matamwe akiandika taarifa alizokuwa akielezwa na  Mbunge wa Jimbo la Rufiji Mhe. Mohamed Mchengerwa huku akimulikiwa kwa kutumia tochi ya simu wakati giza lilipotanda wakati wakiendelea na shughuli ya  kukakagua maeneo yaliyoathirika na maafa ya mafuriko katika kata za Muhoro  na Chumbi tarehe 23 Machi, 2020. Kata hizo ni kata zilizoathirika sana kati ya kata zote 13 za  wilaya hiyo.
Baadhi ya Nyumba zikiwa zimezingirwa na maji  kutokana na athari za maafa ya mafuriko katika kata ya Muhoro, kijiji cha Shela wilayani Rufuji, tarehe 23 Machi, 2020. Jumla ya kaya elfu sita zimeathirika na maafa hayo katika wilaya hiyo.


               KAMATI YA USIMAMIZI MAAFA RUFIJI YATAKIWA KUREJESHA                                                 MIUNDOMBINU ILIYOATHIRIKA NA MAFURIKO

Na. OWM, RUFIJI

Kufuatia miundombinu ya barabara, shule na Zahanati kuathirika kutokana na maafa ya mafuriko wilayani Rufiji. Kamati za Usimamizi wa maafa za wilaya hiyo zimeshauriwa kuchukua hatua za haraka katika kukabiliana na maafa hayo kwa kurejesha hali ya kawaida ya miundombinu iliyoathirika na maafa hayo katika kata zote 13 za wilaya hiyo.

 Kata ya Muhoro na Chumbi ni miongoni mwa kata zilizoathirika sana na maafa hayo, ambapo kwa sasa madaraja matatu yaliyopo barabara ya Nyamwage- Utete inayoelekea makao makuu ya wilaya hiyo tayari yameathirika, Daraja lililopo kwenye barabara ya kuelekea Mradi wa kufua Umeme wa Mwalimu Nyerere nalo limeathirika pamoja na Daraja la Mkapa nalo limeanza kupata athari ya mafuriko hayo.

Akiongea mara baada ya kukagua athari za maafa  na kukabidhi misaada kwa waathirika wa maafa hayo tarehe 23 Machi 2020, Mkurugenzi Idara ya Uratibu wa shughuli za Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Jimmy Matamwe, ameeleza kuwa  Kamati za Usimamizi wa kuanzia ngazi ya kijiji hadi wilaya, kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa maafa Na. 7 ya mwaka 2015 zinawajibika kutekeleza operesheni za dharura.

Nimezishauri kamati za usimamizi wa  maafa katika wilaya hii kuwa na mipango ya muda mfupi ya kuhakikisha barabara zinapitika kipindi chote ili wananchi wasishindwe kutumia miundombinu hiyo, kwani zipo barabara zinaunganisha mikoa ya kusini na zipo barabara zinawasaidiia wananchi kuweza kuzifikia huduma za kijamii”amesisitiza Kanali Matamwe.

Awali akiongea mara baada ya kupokea misaada kutoka kwa Idara ya Uratibu wa maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Mkuu wa wa wilaya hiyo, Mhe.  Juma Njwayo amefafanua kuwa misaada hiyo itakuwa ni msaada mkubwa kwa kuwa hadi sasa wapo watu zaidi ya elfu ishirini wameathirika na maafa hayo kwa kuwa zidi ya nyumba mia moja zimezingirwa na maji.

“Tunaishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kutuletea Magodoro, Mikeka, Vyandarua, Ndoo na Sabuni na naamini kamati za maafa zitawajibika kugawa vifaa hivi kwa mujibu wa taratibu za menejimenti ya maafa. Wilaya tunaendelea na kukabiliana  na maafa kwa kaya takribani elfu sita,  kama tulivyoshauriwa kuhusu miundombinu, kwa kushirikiana na TANROADS tunaendelea kwa kasi kuchukua hatua za kurejesha miundombinu yote iliyo athirika ” Amesisitiza  Mhe. Njwayo.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Rufiji, Mhe. Mohamed Mchengerwa, ameeleza kuwa tangu maafa ya mafuriko yatokee wilayani humo, wamekuwa wakipata ushirikiano wa kutosha kutoka kwa Ofisi hiyo,  kupitia Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu mwenye dhamana ya masuala ya maafa Mhe. Jenista Mhagama, ambapo amekuwa akiwatuma wataalamu na kufika kwa wakati kwa ajili ya kuzisaidia kamati za usimamizi wa maafa.

“Wananchi wa Rufiji wanafarijika sana kwa jinsi serikali yao inavyowajali, tunatambua mafuriko yamewaathiri sana ikiwemo na kuharibika kwa vyakula vyao, tunaomba  mtuletee mbegu ama chakula cha bei nafuu na wananchi hawataki chakula cha bure, sisi tunataka tufanye kazi na tukipata mbegu tutafanya kazi ya kilimo mara mafuriko yakiisha” amesisitiza , Mhe. Mchengerwa.

Kwa mujibu wa Taarifa ya Mamlaka ya Hali hewa iliyotolewa mwezi Februari mwaka huu imeeleza kuwa kutakuwa na mvua za juu ya wastani katika eneo kubwa la nchi kati ya mwezi Machi hadi mwezi Mei, mwak huu, ambapo mvu ahizo zilitarajiwa kuanza kati ya wiki ya kwanza au ya pili ya mwezi Machi na kutaraji akumaliziaka kati ya wiki ya kwanza au ya pili yamwezi Mei. Hivyo kutokana na mvua hizo wananchi hawanbudi kuchukua tahadhari za athari za mvua hizo.
MWISHO.

Read More

KATIBU MKUU MWALUKO AWAASA WATUMISHI OFISI YA WAZIRI MKUU KUENDELEA KUCHUKUA TAHADHARI DHIDI YA VIRUSI VYA CORONA

Mjumbe wa baraza kutoka Idara ya Mipango na Bajeti Ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Dudu Malima akiwapitisha wajumbe wa kikao cha baraza la wafanyaka kuhusu Mapitio ya Utekelezaji wa Bajeti ya Ofisi hiyo kwa mwaka wa fedha 2019/2020 na Makadirio ya Mpango na Bajeti ya Ofisi hiyo kwa mwaka 2020/2021  wakati wa kikao hicho.

Mjumbe wa Baraza la Wafanyakazi Ofisi ya Waziri Mkuu Bi. Ernajoyce Hallo akichangia jambo wakati wa kikao cha baraza la wafanyakazi Jijini Doodma.
Baadhi ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la Ofisi ya Waziri Mkuu hoja wakati wa kikao cha Baraza hilo.
Baadhi ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la Ofisi ya Waziri Mkuu wakifuatilia hoja wakati wa kikao hicho kilichofanyika Ukumbi wa Mikutano wa ofisi hiyo Jijini Dodoma.
Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Paschal Vyagusa akizungumza wakati wa kikao cha baraza hilo kilichofanyika Machi 23, 2020 Jijini Dodoma.
Mjumbe wa Baraza la Wafanyakazi Ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Augustino Tendwa akichangia jambo wakati wa kikao cha baraza hilo kilichofanyika Machi 23, 2020 Jijini Dodoma.
Read More

KATIBU MKUU MWALUKO AWAASA WATUMISHI OFISI YA WAZIRI MKUU KUENDELEA KUCHUKUA TAHADHARI DHIDI YA VIRUSI VYA CORONA


NA. MWANDISHI WETU
Katibu Mkuu Ofisi ya Waziti Mkuu anayeshughulikia Sera, Uratibu na Uwekezaji Bi. Dorothy Mwaluko amewaasa watumishi wa ofisi yake kuendelea kuchukua tahadhari dhidi ya mlipiko wa homa kali ya mapafu inayosababishwa na virusi vya Corona nchini ili kuendelea kupambana na maambukizi ya virusi hivyo.
Ametoa kauli hiyo alipokuwa akifungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi kilichohusu Mapitio ya Utekelezaji wa Bajeti ya Ofisi hiyo kwa mwaka wa fedha 2019/2020 na Makadirio ya Mpango na Bajeti ya Ofisi hiyo kwa mwaka 2020/2021kilichofanyika Ukumbi wa mikutano wa Ofisi hiyo Jijini Dodoma tarehe 23 Machi, 2020.
Katibu Mkuu aliwaeleza watumishi kuendelea kujilinda katika mazingira yote kwa kuhakikisha wanafuata maelekezo yanayotolewa na Serikali ili kulinda na janga hilo lililopo nchini.
“Watumishi lazima muwe kielelezo kwa kuzingatia ofisi hii ndiyo inayoratibu na kusimamia shughuli zote za Serikali hivyo lazima mzingatie tahadhari zote ili kuepuka mlipuko wa virusi vya Corona katika nchi yetu ”alisema Mwaluko
Aliongezea kuwa, kila Mtanzania ana nafasi ya kujilinda kuanzia ngazi ya mtu mmoja hadi Taifa kwa kuangalia namna ugonjwa ulivyoathiri nchi zingine na kusababaisha vifo vya watu wengi.
Mwaluko aliwaasa watumishi waendelee kunawa mikono na kuepuka makusanyiko yasiyo ya lazima huku wakijihadhari kwa kuzingatia matumizi sahihi ya vifaa saidiizi katika kujikinga na maambuki ya virusi vya Corona.
Aliongezea kuwa, nchi imeendelea kuchukua hatua mbalimbali ili kuona inakabiliana na mlipuko wa COVID 19 kwa kutoa elimu kwa umma juu ya kujikinga na maambukizi na kuhakikisha idadi ya wanaoathiriwa na Corona inapungua badala ya kuongezeka.
“Kila mtumishi aelewe kuwa hadi sasa hakuna dawa wala chanjo ya virusi hivyo, na ugonjwa huu upo nchini, hili silipuuzwe na lazima tuzingatie tuwapo kazini kila mmoja wetu awe makini na endapo ukiona una dalili moja wapo ya ugonjwa huu ni vyema kutoa taarifa ili kuepuka madhara kwa wengine,”alisisitiza Mwaluko
Kwa upande wake Mwenyekiti wa TUGHE wa ofisi hiyo, Bw. Mohamed Athuman alimpongeza Katibu Mkuu kwa kuchukua fursa ya kuwakumbusha watumishi na kuendelea kutoa elimu juu ya kujikinga na kuwalinda wengine.
“Leo tumepata nafasi ya kukumbushwa na kiongozi wetu kuhusu namna bora ya kuendelela kuwa makini na kuzingatia maelekezo ya Serikali ili kuepuka maambukizi ya virusi vya Corona,”alisema Athuman
Aidha aliendelea kutoa wito kwa watumishi wa ofisi hiyo kuona namna bora ya kuyazingatia maelekezo yanayotolewa ili kuendelea kuwa na  afya bora katika utekelezaji wa majukumu wawapo kazini.
“Sisi viongozi wa TUGHE tunaunga mkono tahadhari zinazotolewa na viongozi wetu , hivyo ni vyema tukazingatia na kukumbuka kuwa kinga ni bora kuliko tiba,”alieleza
Sambamba na hilo alieleza kuwa kila mtumishi wa umma ana nafasi nzuri ya kuendelea kuunga mkono na kuwa kinara namba moja katika vita kwa kuachana na mizaa na kuendelea kuelimishana kuanzia ngazi ya familia hadi Taifa kwa ujumla kwa kuzingatia ukubwa wa tatizo hilo.
Naye mmoja wa wajumbe wa Baraza la wafanyakazi Ofisi ya Waziri Mkuu Bi. Numpe Mwambenja alieleza wameendelea kuchukua tahadhari zote zinazotolewa kwa kuzingatia mchango wa watumishi wa umma katika nchi na maendeleo kwa ujumla.
“Ofisi imetimiza wajibu wake kwetu, na sisi tunapaswa kuwajibika na tuhakikishe tunapambana na wanaopotosha umma kwa kuhakikisha tunasambaza taarifa sahihi zinazotolewa na Serikali yetu,”alifafanua Bi.Numpe.
Read More

Sunday, March 22, 2020

KAMATI YA USIMAMIZI MAAFA KILOMBERO YATAKIWA KUFANYA TATHMINI YA ATHARI ZA MAAFA YA MAFURIKO

Mkurugenzi Idara ya Menejimenti ya maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Jimmy Matamwe akifafanua  umuhimu wa Kamati ya maafa kufanya tathmini ya awali ya athari za maafa katika kijiji cha Nyange Wilayani Kilombero wakati Mkurugenzi huyo alipokutana na kamati hiyo, tarehe 20 Machi 2020.


Mkurugenzi Idara ya Menejimenti ya maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Jimmy Matamwe akimkabidhi Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. James Ihunyo,blanketi kwa ajili ya waathirika wa mafuriko wa Kijiji cha Nyange waliohifadhiwa katika shule ya sekondari Nyange, wilayani Kilombero, tarehe 20 Machi 2020.
Mkurugenzi Idara ya Menejimenti ya maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Jimmy Matamwe akiongea na baadhi ya  waathirika wa mafuriko wa Kijiji cha Nyange waliohifadhiwa katika shule ya sekondari  Nyange, wilayani Kilombero, tarehe 20 Machi 2020.
Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. James Ihunyo akiongea na baadhi ya  waathirika wa mafuriko wa Kijiji cha Nyange waliohifadhiwa katika shule ya sekondari  Nyange, wilayani Kilombero, tarehe 20 Machi 2020.
Baadhi ya vifaa vya nyumbani vya wakazi wa Kijiji cha Nyange vikiwa vimehifadhiwa kwenye shule ya sekondari Nyange,  baada ya kijiji hicho kupata atthari ya maafa ya mafuriko, kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha maeneo mbalimbali hapa nchini, tarehe 20 Machi 2020.
Waokoaji wanaoratibiwa na Kamati ya Usimamizi wa Maafa ya Wilaya ya Kilombero, wakiwa katika kijiji cha Nyange, ili kuwaokoa wakazi wa kijiji hicho kilichozingirwa na maji, ambapo takribani watu 350 tayari wameokolewa kutoka kata ya Mbanane na Kichangani hadi kufikia tarehe 20 Machi 2020.
Baadhi ya wakazi wa kijiji cha Nyange, wilayani Kilombero, wakitoa vifaa vyao kwenye makazi yao yaliyozingirwa na maji kutokana na athari ya maafa ya mafuriko
Baadhi nyumba za wakazi wa  kijiji cha Nyange, wilayani Kilombero, zikiwa zimezingirwa na maji kutokana na athari ya maafa ya mafuriko. Jumla ya Kaya 250 zilizokuwa zimezingirwa na maji zimeokolewa na kuhifadhiwa shule ya sekondari Nyange, tarehe 20 Machi 2020.
Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. James Ihunyo, akimhakikishia Mkurugenzi Idara ya Menejimenti ya maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Jimmy Matamwe kufuatilia Kamati ya maafa kufanya tathmini ya awali ya athari za maafa katika kijiji cha Nyange Wilayani Kilombero wakati Mkurugenzi huo alipokutana na kamati hiyo, tarehe 20 Machi 2020.
Mkurugenzi Idara ya Menejimenti ya maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Jimmy Matamwe akimueleza  Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. James Ihunyo, umuhimu wa Kamati ya maafa kufanya tathmini ya awali ya athari za maafa katika kijiji cha Nyange Wilayani Kilombero wakati Mkurugenzi huo alipokutana na kamati hiyo, tarehe 20 Machi 2020.


Na. OWM, MOROGORO

Kufuatia Kaya 250 katika kata ya Msolwa Stesheni katika kijiji cha Nyange Wilayani Kilombero kuathirika na athari za maafa ya  mafuriko. Kamati ya Usimamizi wa Maafa ya Wilaya hiyo imeelekezwa kufanya tathmini ya awali kwa kata ya Mbanane na Kichangani ambazo takribani watu 350 wameathiriika na maafa hayo yaliyosababishwa na mvua zinazoendelea kunyesha hapa nchini.

Akiongea mara baada ya kukagua athari za maafa katika kata hizo Machi 20, 2020, wilayani Kilombero, Mkurugenzi Idara ya Menejimenti ya maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Jimmy Matamwe, amesema tathmini ya awali ya athari za maafa katika kata hizo hainabudi kufanyika kwa haraka ili kubaini hatua za kuchukua katika kukabiliana na maafa hayo.

“Kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa maafa Na. 7 ya mwaka 2015, inaainisha  majukumu ya  kamati za usimamizi wa Maafa kuanzia ngazi ya Kijiji hadi mkoa, ambapo kwa mujibu wa sheria hiyo, jukumu la msingi ni kutafuta rasilimali kwa ajili ya usimamizi wa maafa katika ngazi husika, pamoja na  Kuratibu na kusimamia shughuli za usimamizi wa maafa na operesheni za dharura ndani ya Kijiji  wilaya au mkoa. Hivyo kamati hii haina budi kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria.”amesisitiza Kanali Matamwe

Awali akieeleza hatua ambazo kamati ya Menejimenti Usimamizi wa Maafa ya Wilaya hiyo ilizo zichukua, Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. James Ihunyo, amefafanua kuwa hadi kufikia tarehe 20 Machi 2020, kamati hiyo ilikuwa imefanikiwa kuwaokoa watu 350 ambao wamehifadhiwa kwenye shule ya sekondari Nyange.

“Tunaishukuru serikali kupitia, Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya uratibu wa shughuli za maafa  kwa miongozo, lakini pia na kufika kwa wakati katika kata zetu, tumefurahi na mmetuletea blanketi ambayo naamini yatawasaidia waathirika wa maafa haya ambao tumewahifadhi hapa shuleni. Kwa sasa wapo wanaume 172 na wanawake 178 huku watoto ni 30 ambao tumewahifadhi” Ameeleza  Mhe. Ihunyo.

Kwa mujibu wa Taarifa ya Mamlaka ya Hali hewa iliyotolewa mwezi Februari mwaka huu imeeleza kuwa kutakuwa na mvua za juu ya wastani katika eneo kubwa la nchi kati ya mwezi Machi hadi mwezi Mei, mwak huu, ambapo mvu ahizo zilitarajiwa kuanza kati ya wiki ya kwanza au ya pili ya mwezi Machi na kutaraji akumaliziaka kati ya wiki ya kwanza au ya pili yamwezi Mei. Hivyo kutokana na mvua hizo wananchi hawanbudi kuchukua tahadhari za athari za mvua hizo.
MWISHO.

Read More

Saturday, March 21, 2020

WAZIRI MKUU AONYA WANAOPOTOSHA KUHUSU CORONA



WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameonya juu ya upotoshwaji na utoaji holela wa taarifa kuhusu ugonjwa wa homa ya mapafu unaosababisha na virusi vya corona (COVID 19) unaofanywa na watu mbalimbali nchini.

Amesema kuanzia sasa taarifa hizo zitatolewa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto na ikilazimika zitatolewa na Waziri Mkuu na ikilazimika sana zitatolewa na viongozi wakuu wa nchi ili kuepusha mikanganyiko.

Waziri Mkuu ametoa onyo hilo leo (Jumamosi, Machi 21, 2020) wakati akizungumza na Wakuu wa Mikoa yote nchini, Makatibu Tawala wa Mikoa na Waganga Wakuu wa Mikoa kwa njia video kutokea ofisini kwake Mlimwa, jijini Dodoma.

Kufuatia hali hiyo, Waziri Mkuu ameiagiza Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) ifuatile watu wote wanaofanya upotoshaji kwa kupitia mitandao ya kijamii ili hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yao.

“Watu wote wanaopotosha umma na kuleta taharuki kuhusu ugonjwa wa corona badala ya kuelimisha namna ya kujikinga, wafuatiliwe na kuchukuliwa hatua,” amesisitiza.

Waziri Mkuu amesema licha ya hali ya maambukizi ya corona nchini kutia matumaini, viongozi hao hawana budi kupeana taratibu za namna ya kukabiliana na tatizo hilo. 

“Wakuu wa mikoa kila mmoja ahakikishe eneo lake linakuwa salama na endapo kutakuwa na mgonjwa tumieni zahanati ambazo bado hazijaanza kutumika kwa ajili ya kutolea huduma kwa wagonjwa wa corona,” amesema.

Amewataka wakuu hao wa mikoa waimarishe utoaji wa elimu kwa umma na ikiwezekana watumie magari ya matangazo ili wananchi waelewe athari za ugonjwa huo na namna ya kujikinga pamoja na kuwaondolea hofu ili waweze kuendelea na shughuli zao za kimaendeleo. 

Pia amewataka watumie redio za kijamii katika maeneo yao kutoa elimu kwa umma juu ya kujikinga na ugonjwa huo na wasimamie maeneo ya utoaji huduma kama vituo vya mabasi na kuhakikisha kila abiria anakaa kwenye kiti. 

“Nendeni kwenye maeneo ya mikusanyiko, vituo vya mabasi kutoa elimu kwa umma na kuwaondoa hofu. Upande wa maofisini, viwandani na kwenye mgodi kuwe na utaratibu wa kutoa elimu kwa wafanyakazi kila siku asubuhi watumie hata robo saa kabla ya kuanza kazi waelekezwe namna ya kujikinga.”

Waziri Mkuu amesema kwa wanaoishi katika maeneo ya makambi, viongozi wao waelekezwe namna ya kutoa elimu ya kujikinga na corona na pia wadhibiti utorokaji na Serikali kwa upande wake inaendelea kuimarisha udhibiti mipakani, uwezo wa kupima sampuli na upatikanaji wa vifaa.

Amewataka wakuu hao wa mikoa, wawashirikishe wakuu wa wilaya kwenye mikoa yao ili wasimamie utekelezaji wa maagizo hayo.

Wakati huohuo,Waziri Mkuu amewaagiza wakuu hao wa mikoa wahakikishe wanawafuatilia na kuwachukulia hatua wafanyabiashara wote watakaobainika kuongeza bei kwa bidhaa ambazo zinatumika katika udhibiti wa maambukizi ya ugonjwa wa corona.

Kuhusu viongozi wa dini, Waziri Mkuu amewaomba waendelee kushirikiana na Serikali katika kuwaelimisha waumini wao wote kuzingatia tahadhari za ugonjwa huu. Pia awaendelee kuliombea Taifa.

(mwisho)

Read More

MAJALIWA AZUNGUMZA NA WAKUU WA MIKOA KWA NJIA YA VIDEO

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akijadili jambo na Afisa Mtendaji  Mkuu wa Kampuni  ya Simu Tanzania (TTCL), Waziri Kindamba kabla ya kuanza mkutano kwa njia  ya video na  Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala wa Mikoa na Waganga Wakuu wa Mikoa  akiwa ofisini kwake, Mlimwa jijini Dodoma, Machi  21, 2020.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Wakuu wa Mikoa , Makatibu Tawala wa Mikoa  na Waganga Wakuu wa Mikoa kwa njia ya video akiwa ofisini kwake Mlimwa jijini Dodoma, Machi 21, 2020. 
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Wakuu wa Mikoa , Makatibu Tawala wa Mikoa  na Waganga Wakuu wa Mikoa kwa njia ya video akiwa ofisini kwake Mlimwa jijini Dodoma, Machi 21, 2020. 


Read More

Tuesday, March 17, 2020

SERIKALI YAZIFUNGA SHULE ZOTE KUANZIA LEO SABABU YA CORONA





TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

SERIKALI YAZIFUNGA SHULE ZOTE KUANZIA LEO SABABU YA CORONA

SERIKALI imesema shule zote za awali, msingi na sekondari zitafungwa kwa siku 30 kuanzia leo Machi 17, 2020.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa leo (Jumanne, Machi 17, 2020) wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Magogoni, jijini Dar es Salam.

Amesema wanafuzi wa kidato cha sita walipaswa kuanza mitihani Mei 4, 2020 lakini nao pia watapaswa kusibiri Wizara ifanye utaratibu mwingine kulingana na matokeo ya hali ya maambukizi.

Amesema mikusanyiko yote mikubwa ya ndani na nje isiyo ya lazima imesitishwa kuanzia sasa ikiwemo shughuli za michezo, matamasha ya muziki, mikutano mbalimbali ikiwemo ya shughuli za kisiasa, mahafali na shughuli nyingine za kijamii.

Amezitaka wizara na taasisi zizitishe semina, warsha, makongamano na mikutano yote hapa nchini ambayo inahusisha washiriki toka nchi zenye maambukizi makubwa. “Watanzania wenye safari zisizo za lazima kwenye nchi zenye maambukizi makubwa, wanashauriwa wasitishe safari hizo,” amesisitiza.

Akielezea hatua nyingine zinazochukuliwa na Serikali ili kudhibiti ugonjwa huo, Waziri Mkuu amesema: “Serikali imesitisha michezo yote inayokusanya makundi ya watu ikiwemo Ligi Kuu ya Tanzania Bara (VPL), Ligi Daraja la Kwanza (FDL), Ligi Daraja la Pili (SDL) na aina nyngine. Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo iziandikie taasisi zake.”

Pia amewataka Wakuu wa Mikoa na Wilaya wahakikishe maeneo yote yaliyobainishwa na kutengwa (vituo vya huduma na ufuatiliaji) kwa ajili ya kuwahudumia wagonjwa endapo watajitokeza katika maeneo yao yanakuwa na mahitaji yote muhimu na yanahudumiwa ipasavyo.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali tayari imetoa shilingi milioni 500 kati ya sh. bilioni moja zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya Mbio za Mwenge wa Uhuru zilizokuwa zianze Aprili 2, mwaka huu.

“Rais Dkt. John Pombe Magufuli ameahirisha Mbio za Mwenge wa Uhuru zilizokuwa zianze Aprili 2, mwaka huu na kuagiza shilingi bilioni moja zilizokuwa zimeandaliwa kwa ajili ya shughuli hiyo, zipelekwa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa ajili ya maandalizi ya kujiweka tayari kudhubiti maambukizi ya CORONA. Serikali tayari imetoa shilingi milioni 500.”

Akielezea hatua zilizochukuliwa baada ya mgonjwa wa kwanza kubainika kuwepo nchini Tanzania, Waziri Mkuu amesema Serikali imechukua hatua kwa kumchukua mgonjwa huyo na kumhifadhi kwenye eneo maalum kwa ajili ya kumpatia huduma (isolation).

“Pia, Serikali imefanya ufuatiliaji wa watu waliokutana na mgonjwa huyu tangu aingie nchini na kuwaweka kwenye karantini ya siku 14, na pia kuchukua sampuli kwa lengo la kubaini kama wameambukizwa virusi hivi,” amesema.

Ugonjwa huu umeingia nchini baada ya Mtanzania mwenye miaka 46 aliyesafiri kwenda nchi za Ubeligiji, Sweden na Denmark hivi karibuni, kupimwa na kuthibitika kuwa na virusi vya Corona (COVID-19).

Akielezea hatua zaidi zinazochukuliwa, Waziri Mkuu amesema licha ya hatua ambazo zimechukuliwa na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Serikali itaimarisha ukaguzi na ufuatiliaji wa wasafiri wanaoingia nchini kupitia viwanja vya ndege, bandari na mipaka ya nchi kavu ili kuwabaini wasafiri wenye dalili za ugonjwa na viashiria vyenye hatari.

“Tutaimarisha uwezo wa kupima sampuli kwa watu wanaohisiwa kuwa na viashiria au dalili za ugonjwa huu ambapo maabara yetu ya Taifa kwa sasa inao uwezo wa kutoa majibu kwa haraka.”

Amesema Serikali inaendelea kuwajengea uwezo (mafunzo) watumishi wa sekta ya afya katika kukabiliana na magonjwa ya milipuko ikiwemo jinsi ya kutoa tiba, kuchukua sampuli, uelimishaji na kuzingatia kanuni za afya.

“Serikali imetenga hospitali maalum za Mloganzila (DSM), Kituo cha Buswelu (Mwanza) na Hospitali ya Mawenzi (Kilimanjaro), Mnazi Mmoja (Zanzibar) na ChakeChake (Pemba) kwa ajili ya kutoa huduma kwa waathirika.”

Ameiagiza Wizara ya Afya ihakikishe vifaa vya kinga ikiwemo vimiminika vya kudhibiti maambukizi (hand sanitizer) vinapatikana katika maduka yote husika na kwa bei ya kawaida na kuongeza kwamba Serikali itachukua hatua kwa wafanyabiashara watakaobainika kufanya ulanguzi wa vifaa hivyo.

Amewataka Watanzania wazingatie ushauri unaotolewa na Serikali na kupuuza taarifa za uzushi zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii. “Watanzania tuache mzaha wa kutumia mitandao ya kijamii kufanya upotoshaji wa tahadhari katika jambo hili,” ameonya.

Amewaomba viongozi wa dini waendelee kushirikiana na Serikali katika kuwaelimisha waumini wao wote kuzingatia tahadhari za ugonjwa huu. Pia amevitaka vyombo vyote vya habari vishirikiane na Serikali katika utoaji wa elimu kwa umma kuhusu kujikinga na Corona bila kufanya upotoshaji wala kuipa jamii hofu.

Amewataka wananchi watoe taarifa kuhusu uwepo wa mgonjwa au kupata ufafanuzi kuhusu ugonjwa huu kupitia namba za bure za 0800110124, 0800110125 na 0800110037.

(mwisho)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMANNE, MACHI 17, 2020.


Read More