Sunday, January 29, 2023

DKT.JINGU: MATOKEO YA SENSA YA WATU NA MAKAZI YATUMIKE KATIKA MIPANGO YA MAENDELEO.

 


Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Utatibu Dkt. John Jingu ameeleza ni muhimu kuyatumia matokeo ya sensa ya watu na maakazi ya mwaka 2022 katika mipango mbalimbali ya maendeleo ya nchi yetu.

Ameyasema hayo wakati akiongoza kikao cha 9 cha Kamati ya Ushauri ya Taifa ya Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 kwa ajili ya kupitia baadhi ya ripoti za matokeo ya Sensa zilizo kamilika kabla ya kuzinduliwa.Kikao kilifanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Dar es Salaam.

Jukumu kubwa la Kamati hiyo ni kuishauri Kamati Kuu ya Taifa ya Sensa inayoongozwa na Mhe. Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar namna bora ya utekelezaji wa masuala ya sensa.

=MWISHO=

Read More

Thursday, January 26, 2023

WAZIRI SIMBACHAWENE: IMARISHENI MIFUMO WA USHUGHULIKIAJI WA MATUKIO YA UKATILI DHIDI YA WANAWAKE NA WATOTO.

Serikali yahimiza jamii  kuanzia ngazi ya familia kuimarisha mfumo wa ushughulikiaji wa matukio ya ukatili dhidi ya watoto ndani na nje ya shule unaowajumuisha wasimamizi wa shule, wazazi, walezi na jamii kwa lengo kuendelea kutokomeza matukio ya ukatili nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulika na Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene katika Mkutano wa Kitaifa wa tafakuri ya Utekelezaji wa Mpango Kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto (MTAKUWWA) uliofanyika katika Ukumbi wa Saint Gaspar Jijini Dodoma.

Waziri ameeleza kwamba Mfumo wa Ushughulikiwaji wa matukio ya ukatili utasaidia Taifa kupunguza kwa kiasi kubwa changamoto iliyopo katika jamii ya ukatili wa kijinsia na unyanyasaji wa Watoto.

“tuendelee kuunga mkono juhudi za Serikali kwa hali na mali ili kuhakikisha makundi yote ndani ya jamii yanalindwa dhidi ya ukatili wa kijinsia na unyanyasaji wa watoto alisema,” alisema Waziri Simbachawene.

Akieleza kuhusu Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Mtoto wa mwaka 1989, wa Sera ya Maendeleo ya Mtoto 2008 na Sheria ya Mtoto Na. 21, 2009, ambao unaoelezea masuala ya ukatili kwa watoto ni kinyume cha haki zao za msingi za kuishi, kuendelezwa, kulindwa na kutokubaguliwa.

Aidha umeeleza kuwa,vitendo vya ukatili vinarudisha nyuma jitihada za Serikali katika kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu ya mwaka 2030 na Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Mtoto wa mwaka 1989 ambayo nchi imeridhia kutekeleza.

Waziri amehimiza kuendeleza juhudi za kukabiliana na ukatili huo katika zama za utandawazi kuwa na msukumo mpya na wa pamoja ili kuwalinda watoto dhidi ya ukatili.

Amesema kuwa, athari za utandawazi zimedhoofisha mifumo ya ulinzi na usalama wa watoto hivyo kufanya kundi hilo kutokuwa salama kwani tatizo la ukatili bado ni changamoto katika ngazi zote.

Kwa upande wake, Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake  na Makundi Maalum  Mhe. Dorothy Gwajima amesema wizara ya Maendeleo ya jamii imekuwa ikiratibu utekelezaji wa MTAKUWWA toka kuzinduliwa kwake mwaka 2016, na baada ya kukamilika kwake Wizara pamoja na Wadau wa maendeleo walifanya tathimini ya utekelezaji wake kuanzia 2017/2018 hadi 2021/2022 kupitia Mtaalam mwelekezi Chuo Kikuu cha Dodoma.

Waziri amesema taarifa ya tathimini imekamilika na imebainisha utekelezaji wa MTAKUWWA kwenye maeneo yote nane yalliyopo kwenye mpango huu, na imebainishwa maeneo muhimu yatakayoenda kutekelezwa kwenye mpango kazi ujao.

“Niwaombea wadau tuwe na subira tukiwa tunaendelea mapitio ya pamoja mpaka itakapotangazwa kwamba serikali pamoja na wadau,”aliomba Waziri Gwajima

Naye Mkurugenzi wa Shirika la ICS Tanzania Bwn.  Kudely Sokoine  Joram amesema wataendelea kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuhakikisha mapambano haya yanatokomezwa huku akiipongeza Serikali kwa hatua inazochukua katika kukabiliana na changamoto ya ukatili wa makundi haya muhimu huku akitaja maeneo muhimu ikiwemo la kuimarisha mifumo ya ulinzi wa Wanawake na Watoto, kujenga uwezo wa Kamati za ulinzi wa Wanawake na watoto pamoja na kusaidia uratibu wa Masuala yote.

Read More

Thursday, January 19, 2023

"TATUENI CHANGAMOTO ZA WANANCHI," WAZIRI SIMBACHAWENE.

Waziri wa Nchi Ofisi ya waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene amewataka watendaji wa Serikali kuendelea kutatua changamoto za wananchi zinazowakabili ili kuchochea kasi ya maendeleo nchini.

Waziri ametoa kauli hiyo wakati akifungua mafunzo ya siku mbili ya kujenga uwezo kwa Menejimenti ya Ofisi ya Waziri Mkuu yaliyolenga kuwajengea uelewa kuhusu Idara ya  Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji wa Shughuli za Serikalini yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi uliopo Njedengwa Jijini Dodoma Januari 19, 2023.

Waziri alihimiza kila mtendaji wa Serikali kuhakikisha anatekeleza majukumu yake kwa ufanisi huku akitatua changamoto za wananchi katika eneo lake la kazi.

Aliongezea kuwa ni muhimu kwa watendaji kuwajibika kwa kuyafikia malengo ya Serikali ya Awamu ya Sita huku wakileta matokeo chanya yatokanayo na utendaji mzuri wa kazi zao za umma.

"Hakikisheni mnakuwa watu wa  msaada kwa wengine katika kuyatekeleza majukumu yenu, muwe watengeneza furaha na hii iwe kipimo kwa kila mwenye kukufikia huku ukizingatia taratibu za utumishi wa umma na sheria zilizopo,"alisema Waziri Simbachawene

Aidha aliwaasa waendelee kutumia taaluma zao kuleta matokeo chanya kwa Serikali na jamii huku wakijitathimini utendaji wa kila siku.

 “Ni sahihi kujitathimini kila iitwapo leo ili kuona namna unavyoleta matokeo chanya kwenye utendaji wako wa kila siku, matokeo utayoyapata  yatatusaidia kuongeza tija ,” alisisitiza Waziri Simbachawene.

Akieleza umuhimu wa mafunzo hayo aliwataka kuhakikisha mafunzo  yanawafikia watendaji katika ngazi zote ili kuendelea kuongeza uelewa kwa watumishi wa umma.

" Mafunzo haya yawafikie watumishi wote katika Idara na vitengo vyetu bila kumuacha nyuma mtu yeyote ili kuleta chachu katika utendaji na  kuondokana na tabia ya mazoea," alisema.

Aliongezea kuwa matokeo ya Mafunzo haya yatumike kuboresha mifumo ya uratibu, usimamizi na ufuatiliaji wa shughuli za Serikali ili kuwa na uwezo wa kupima utendaji wa Wizara na Taasisi mbalimbali za Serikali kisayansi.

Aidha uwekwe utaratibu ambao utawezesha uchambuzi wa Taarifa za kisekta na kutoa mrejesho wa maeneo yanayohitaji kuboreshwa au kupewa msukumo zaidi.

 "Ili kuendelea kuboresha shughuli za uratibu naamini uwepo Idara mpya ya Ufuatiliaji na Tathmini itasimamia hili na kuhakikisha kunakuwa na mrejesho kwa Wizara na Taasisi zote ili kuimarisha uwajibikaji," alihimiza.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Dkt. John Jingu  amesema mafunzo haya yanalenga watendaji wa serikali kufanya kazi kwa ufanisi kwa weledi na kwa namna ambayo itakidhi mahitaji pia yatajikita katika majukumu ya Ofisi ya Waziri Mkuu  katika eneo la uratibu wa shughuli za serikali, na jukumu la kufanya kazi ya ufuatiliaji na tathmini ya utendaji wa  shughuli za Serikali.

 

Read More

Tuesday, January 17, 2023

WAZIRI SIMBACHAWENE, ARIDHISHWA NA HATUA ZA UJENZI KIWANDA KIPYA CHA MPIGA CHAPA MKUU WA SERIKALI

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu  ameridhishwa na kasi ya ujenzi wa kiwanda  cha kupiga chapa cha serikali ambacho mpaka sasa msingi wa jengo na ujenzi wa boma la jengo; kuta, kupiga plasta na kupauwa vimeshafanyika.

“Hiki kiwanda tunatarajia kukifunga mitambo na mashine za kisasa ili kiweze kufanya jukumu la kuchapa nyaraka za Serikali na  shughuli za Mpiga Chapa ziweze kufanyika kwa ufanisi.”

Kauli hiyo ameitoa alipotembelea na kujionea maendeleo ya ujenzi wa kiwanda hicho cha Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali kilichopo Kisasa katika Jiji la Dodoma.

Ofisi hii ni muhimu sana kwa nchi, ni lazima iwe Ofisi bora kwa sababu nyaraka nyingi za siri za serikali zinapaswa kuchapwa na Ofisi ya Mpiga Chapa wa Serikali,

Waziri Simbachawene amempongeza Rais Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa kiwanda hicho cha mpiga chapa wa serikali kwa kiasi cha billioni 1.88

“Serikali imetoa pia kiasi cha million kiasi cha millioni 350 ambazo zitatumika kufanyia ukarabati kiwanda na Mashine za Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali Jijini Dar es Salaam ikiwa ni pamoja na kiasi kingine cha shilingi billioni 1.4 kwa ajili ya kununua malighafi kwa viwanda vinavyondelea na uzalishaji, cha Dodoma na Dar es salaam.”

Amefafanua kiwanda kipya cha Dodoma cha Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali imetoa kiasi cha shilingi billioni 3.9 ambayo itasaidia kununua mitambo mipya na ya kisasa ili kuhakikisha nyaraka zote muhimu za serikali zinachapishwa katika kiwanda hicho.

“Nembo ya Taifa, Bendera ya Taifa na Mhuri ni vitu ambavyo vimewekwa katika uangalizi wa Ofisi ya Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali.”

Naye Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali Bwn. George Lugome ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kutoa fedha kwa ajili ya kuboresha idara ya Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali  kwa kuiwekea majengo yenye uwezo wa kuwa na miundo mbinu mizuri na mashine za kisasa ambazo zitasaidia kuchapa nyaraka zenye alama ya siri.

“Sheria ya alama za Taifa ya mwaka 1971 inatamka wazi kabisa kwa yoyote anayekiuka au anaibadili nembo ya Taifa au alama za Taifa anastahili kupewa adhabu ya kifungo cha miaka miwili jela,” amesema Bwn, Lugome.

Ametoa wito kwa taasisi binafsi zinazotaka kujihusisha na uchapaji wa nyaraka  kuhakikisha wanathibitishwa na Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Usalama ya Serikali ili waweze kupata kibali.

 



Read More

JAMII YA WATANZANIA IPEWE ELIMU YA KUTOSHA JUU YA URAHIBU WA DAWA ZA KULEVYA.

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe.  George Simbachawene ametoa wito kwa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Nchini kuongeza nguvu katika kutoa elimu kwa umma juu ya athari za dawa za kulevya kwa vijana na wanachi wote kwa ujumla.

Hayo ameyasema alipotembelea na kujionea eneo la Hekta saba ambalo linatarajiwa kujengwa jengo la Makao Makuu ya Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Kanda ya Kati, katika eneo la Itega Jijijni Dodoma.

 “lazima tuvunje ukimya na tuongeze udhibiti wa matumizi ya bangi, hatuwezi kudhibiti matumizi ya bangi kwa kutegemea mamlaka pekee yake lazima tuweke mfumo na uratibu kwa kuanza kudhibiti kuanzia ngazi ya kijiji, Kata na Wilaya.” Amesema Simbachawene.

 Tufike mahali tuone tunauwa Taifa; Vitu vingi vinavyotokea kwenye familia, na matokeo ya ajabu ya unyanyasaji msukumo wake ni matumizi ya madawa ya kulevya na ukipata urahibu unashindwa kuisadia jamii, unashindwa kuwajibika kwenye familia unashindwa kufanya shughuli za uzalishaji mali.

Waziri Simbachawene, ameongeza kuwa aina mpya ya Urahibu wa kucheza Kamari (Kubeti) ambayo inawakumba watu wote, na ina madhara kama urahibu wa madawa ya kulevya, lazima tujipange.

Kila mmoja ni shahidi watu wanapokuwa wanafanya Kamari ya kubahatisha, kwenye michezo ya mpira, hata kufanya kazi hawawezi, muda wote ni kuangalia mkeka tuu(kubeti)

Aidha kuna umuhimu wa kuziunganisha kwa kuziimarisha Taasisi zetu hizi za Hospitali ya Taifa ya Afya ya Akili Mirembe na Mamlaka wa Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya kisera na kisheria ili ziweze kushirikiana vizuri katika utendaji wa kazi.

Naye Kamishna wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya  Jenerali Gerald Kusaya amesema  katika Mwaka huu wa fedha serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu imeweza kupeleka Vyuo vya Ufundi warahibu  walioachana na matumizi ya  dawa za kulevya wapatao 245 wanaolipiwa ada zote na Ofisi ya Waziri Mkuu na kila mmoja amechagua kitu anachotaka kusoma ili watakapomaliza warudi mtaani na waweze kuanza kujitegemea na kujenga uchumi wa nchi.

Katika kuhitimisha ziara hiyo kamishna Jenerali Kusaya ameomba serikali kuwasaidia  warahibu wanaohitimu mafunzo ya Ufundi stadi na stadi za kazi kupewa vitendea kazi vitakavyowasaidia pindi watakaporudi kwenye jamii yao

Jumla ya warahibu wapatao 12,800 wanatarajia kuhitimu mafunzo kutoka kwenye vyuo vya ufundi wakiwa na ujuzi wa stadi mbalimbali za kazi na kuweza kujitegemea na kujenga uchumi.

 

 

Read More

Monday, January 16, 2023

TAASISI ZINAZOENDELEA NA UJENZI WA OFISI ZATAKIWA KUKAMILISHA MAJENGO YAO KWA WAKATI JIJINI DODOMA


Serikali imeziagiza Taasisi zote zinazoendelea na ujenzi wa majengo ya Ofisi zao Jijini Dodoma kuhakikisha ujenzi huo unakamilika kwa kuzingatia taratibu zote za ujenzi ikiwemo ubora, muda, bajeti iliyotengwa na thamani ya fedha ili kuleta tija inayotarajiwa.

Maagizo hayo yametolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George simbachawene wakati wa hafla ya kukabidhi Vibali vya Ujenzi wa Ofisi za Taasisi za Serikali Dodoma iliyofanyika katika Ukumbi wa Hazina mapema.

 

Waziri Simbachawene amesema, kila Taasisi ya Serikali ihakikishe inajenga majengo ya Ofisi zake ili kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali za kuhamishia Makao makuu yake Dodoma na kuifanya Dodoma kuwa eneo lenye ufanisi.

 

“Taasisi zote zilizoelekezwa kuhamia Dodoma kwa mujibu wa ratiba niliyoitoa leo zihakikishe zinatekeleza maagizo hayo na Makatibu Wakuu wa Wizara husika wahakikishe wanasimamia mpango kazi wa utekelezaji wake,”alisema Mhe.Simbachawene.

 

Aliongezea kuwa, Mpango huu ni utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2015 kama ilivyoainishwa katika Ibara ya 151 chini ya kifungu (a), (b) na (c) vinavyoielekeza Serikali kutunga Sheria ya kuitambua Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi na kuhakikisha kwamba majengo ya Wizara na Taasisi yanajengwa Dodoma badala ya Dar es Salaam.

Aidha Waziri ameagiza Ofisi ya Katibu Mkuu – Sera, Bunge na Uratibu kwa kushirikiana na Mamlaka husika kuendelea kuratibu Mpango wa Serikali na taasisi zake kuhamia Dodoma pamoja na ujenzi wa miundombinu ya kiuchumi na uboreshaji wa huduma mbalimbali za kijamii Dodoma.

Sambamba na hilo, Serikali imekamilisha ratiba na mwongozo utakaowezesha Taasisi za Serikali ambazo bado zinaendelea kutekeleza majukumu yake Dar es Salaam kuweza kuhamishia shughuli zao Jijini Dodoma kwa awamu.

“Katika utekelezaji wa suala hili, Mheshimiwa Waziri Mkuu ametoa maelekezo kwamba Taasisi 42 zihamie Dodoma ndani ya mwaka huu wa fedha wa 2022/23; Taasisi 36 zitahamia Dodoma katika mwaka ujao wa fedha wa 2023/24 na Taasisi 19 zitahamia katika mwaka 2024/25 wakati Taasisi 27 zimeelekezwa, kwa kuzingatia aina ya majukumu zilizonazo, kuendelea kutekeleza majukumu yake Mkoani Dar es Salaam.” Alieleza.

Alisisitiza kuwa, hatua hii itakamilisha sehemu kubwa ya Mpango wa Serikali wa kuhamia Dodoma ambapo hadi sasa tayari Taasisi 65 zilishahamia Dodoma tangu mwaka 2016 hadi 2022.

Waziri ameziagiza Taasisi nyingine ambazo bado hazijaanza maandalizi ya ujenzi wa Ofisi za serikali Dodoma ziwasilishe Ofisi ya Waziri Mkuu Mahitaji ya Viwanja vya ujenzi wa Ofisi za taasisi Dodoma kwa ajili ya uratibu wa pamojal.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule, ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi wa miundo mbinu ya kuwezesha taasisi kuwepo.

 

“Tunaishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kazi kubwa mnayoifanya kwa kupanga makao makuu ya serikali yetu yanakuwa ni mji wa kisasa na mji uliopangwa.”alisema Mhe. Rosemary

 

Awali Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Dkt, John Jingu akitoa taarifa ya utekelezajia amesema Ofisi ya waziri Mkuu imeidhinisha vibali 55 kwa nyakati tofauti kuanzia mwaka 2018 kati ya hizo taasisi 20 zimekamilisha ujenzi, taasisi 16 zinaendelea na ujenzi na taasisi 19 zimeanza maandalizi ya ujenzi.

“Majengo haya yanajengwa katika maeneo mbalimbali, na ujenzi huu unazingatia mpango kabambe wa Jiji la Dodoma.”

Read More

Wednesday, January 11, 2023

SERIKALI YATOA MSAADA KWA WAATHIRIKA WA MAFURIKO YA MAJI MKOANI MBEYA

Serikali Kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu imetoa msaada kwa wananchi walioathirika na Maafa ya Mafuriko ya Maji Mkoani Mbeya, yaliyosabisha nyumba kubomoka, kuharibika kwa vifaa, vyakula, uharibifu wa mifugo na mazao yaliyoko mashambani.

“Msaada huo unajumuisha Magodoro 300 kwa kuanzia, mablanketi 1200 ya wakubwa na wadogo, mikeka 600, madumu ya maji, sufuria bakuli sahani pamoja na vijiko kwa kila familia ambayo imeathirika.”

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene alipotembelea maeneo yaliyoathirika wa mafuriko ya mvua katika kata saba Mkoani Mbeya kutokana na Mvua zilizonyesha  terehe 07/01/2023.

“Kwa mujibu wa sheria no. 6 ya Maafa ya Mwaka 2022 sisi kama Ofisi ya Waziri Mkuu tunayo dhamana ya kuwaunganisha wadau ili kuwasaidia watu walioathirika na tutafanya hivyo kwa kutumia Ofisi zetu za Mkoa na wilaya, naomba wadau wote wa ndani na nje ya Mkoa wa Mbeya kutusaidia ili kuhakikisha watu hawa wanarudi katika hali yao.”

Natoa pole kwa wote walioathirika, TARURA kwa kushirikiana TANROAD Halmashauri ya jiji  la Mbeya na Halmashauri ya Mbeya vijijini wahakikishe wanaenda kuona kwenye vyanzo kuangalia ni eneo gani maji yametoka kwenye mkondo wake wa asili.

Akimkaribisha Waziri wa Nchi, Mbunge wa jimbo la Mbeya Mjini na Spika wa Bunge la jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Tulia Ackson ameishukuru serikali kwa mchango iliyoutoa kwa  waathirika wa mafuriko ya Mvua Mkoani Mbeya .

“Naomba sisi kama Halmashauri tusitoe vibali vya ujenzi kwenye  maeneo ambayo ni mikondo ya maji, kwa sababu athari za mafuriko zinarudisha nyuma  maendeleo ya uchumi kwa wananchi”

Naye Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe. Juma Homera katika taarifa yake amesema watu waliopata athari za mafuriko ya maji, kaya 281 zenye watu idadi ya watu 1405 ambao wanahitaji chakula takribani tani 50 kwa miezi mitatu ili ziweze kuwasaidia.

 

Read More

Friday, January 6, 2023

WAZIRI SIMBACHWENE AHIMIZA MAPAMBANO DHIDI YA UDHALILISHAJI WANAWAKE NA WATOTO


 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene ametoa wito kwa Walezi na jamii kwa ujumla kupiga vita dhidi ya udhalilishaji kwa Wanawake na Watoto mambo ambayo yanapoteza heshima na haiba kwa nchi yetu.

 “tushirikiane katika kutokomeza udhalilishaji kupinga, kuwafichua na kuwafikisha katika vyombo vya Sheria wale wote wanaofanya unyama huu kwa wanawake na Watoto, lakini pia hatunabudi kurejesha utamaduni wetu wa malezi ya pamoja ili kulidhibiti janga hili kwa jamii na Taifa kwa ujumla.”

wito huo ameutoa wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi ujenzi wa kituo cha afya Shehia ya Uzi Mkoa wa Kusini Unguja katika sherehe ya kuadhimisha miaka 59 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.

Katika shughuli yetu kuu ya uwekaji wa jiwe la msingi la mradi   wetu huu, ambayo tayari tumeshaifanya kwa ukamilifu wake, hivyo iliyobaki kwetu ni kuhakikisha mradi huu   unakamilika kwa hatua zilizobakia ili kukidhi  malengo tuliyoyakusudia. 

tunaendelea kushuhudia mapinduzi makubwa ya kiuchumi yanayoendelea kufanyika nchi nzima na hii inathibitisha kauli ya mwaka huu isemayo “Mapinduzi yetu ndio Amani yetu tuyalinde kwa Maendeleo yetu”.

Aidha  serikali zetu zote mbili ya SMT na SMZ zimeendelea kusogeza huduma mbalimbali kwa wananchi wake na tunashuhudia ujenzi wa Miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo huu wa ujenzi wa Kituo cha Afya katika Shehia zetu za Uzi na Ng’ambwa. Mradi ambao unafadhiliwa na Serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii -TASAF ambao ni miongoni mwa matunda ya Mapinduzi yetu yaliyofanyika Januari 12 mwaka 1964.

“ujenzi huu wa Kituo cha Afya umekuja baada ya kuona upo uhitaji mkubwa wa jengo hili kwa wanajamii wa Shehia zetu za Uzi na Ng’ambwa, hali ambayo itarahisisha upatikanaji wa huduma bora ya afya kwa wananchi hususani mama na watoto,”alisema Waziri.

Waziri amesisitiza ushirikiano wa hali na mali katika ufuatiliaji, usimamizi na utekelezaji wa mradi ili uweze kukamilika kwa wakati na kwa ubora wa hali ya juu. Pia, amewaomba viongozi  wa  Mkoa, Wilaya, Baraza la Mji Kati na Shehia zote kuwa karibu katika kusimamia utekelezaji wa  mradi huo muhimu kwa jamii na Taifa kwa ujumla na kuendelea  kutoa msaada pale unapohitajika  ili kufanikisha ukamilishaji wa  mradi kwa wakati.

Akimkaribisha Mgeni Rasmi Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja Mhe Rashid Hadid Rashid amewapongeza TASAF kwa jinsi wanavyoshirikiana na serikali katika kutekeleza Miradi ya maendeleo.

“Katika kipindi kifupi cha miaka miwili wameweza kujenga ukumbi wa mitihani, Kizimkazi Dimbani na katika Maswala ya Kilimo cha Mwani, wazee wetu wanashughulika na kilimo hicho na walikuwa wanapata tabu kuchukua Mwani baharini kuja juu TASAF imewajengea ngazi  ili iwe rahisi kufika juu.”

Naye Mkurugenzi Mtendaji - Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Tanzania (TASAF) Bwn. Ladisius Joseph Mwamanga amesema TASAF inajenga uwezo wananchi kwa kukuza rasilimali watu  katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

“Napenda kuwapongeza wananchi kwa ushirikiano mkubwa ambao wameuonesha katika ujenzi wa kituo cha afya uzi, mradi umesimamiwa kwa ukaribu na wananchi wenyewe wa Shehia ya Uzi na Ng’ambwa.”

Awali katika risala ya wananchi iliyosomwa Bi. Lemi Khalifa amesema utekelezaji wa mradi ulianza mwezi wa nane 2022 kwa kusimamiwa na kamati kuu mbili; kamati ya Shehia na kamati ya usimamizi ngazi ya jamii CMC.

“Mradi ulitengewa kiasi cha million 184,8 21,428 kati ya hizo shilingi million 134,270.261 zimetumika na ujenzi unaendelea.”

Read More