Friday, October 7, 2022

KAMATI ZA USIMAMIZI WA MAAFA ZATAKIWA KUJA NA MIPANGO KUSAIDIA MAENEO YATAKAYOPATA KIWANGO KIDOGO CHA MVUA ZA VULI

 


Kamati za usimamizi wa Maafa zatakiwa kuandaa mipango ya dharura itakayoelekeza hatua za kuchukua kwa kila taasisi na wananchi kwenye maeneo yanayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka ambapo, mvua zinatarajiwa kuwa chini ya wastani hadi wastani.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene katika Mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika Mjini Dodoma. taarifa ya utabiri huo inahusu maeneo ya  Mikoa ya Kagera, Geita, Mwanza, Mara, Shinyanga, Simiyu, Kigoma, Arusha, Kilimanjaro, Manyara, Tanga, Dar es Salaam, Pwani, Morogoro pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba. 

“kutakuwa na upungufu mkubwa wa unyevunyevu katika udongo katika maeneo mengi unaoweza kuathiri ukuaji wa mazao, kusababisha uwepo wa visumbufu vya mazao na magonjwa,” amesema Waziri.

Kina cha maji katika mito, mabwawa na hifadhi ya maji ardhini kinatarajiwa kupungua               hususani katika maeneo mengi ya yanayotegemea mvua za Vuli hivyo kusababisha upungufu wa maji kwa matumizi mbalimbali.

“Mlipuko wa magonjwa unaweza kujitokeza kutokana na upungufu wa upatikanaji wa maji safi na salama.”

Waziri ametoa rai kwa kamati za usimamizi wa Maafa katika ngazi zote kushirikisha wadau wa maafa kuhakikisha upatikanaji wa mbegu zinazokomaa kwa muda mfupi pamoja na utunzaji wa chakula cha binadamu na malisho ya mifugo ikiwemo kupanda mazao yanayokomaa mapema na kuvuna maji.

“Kamati za usimamizi wa maafa, zichukue hatua za kuzuia milipuko ya magonjwa yanayoweza kujitokeza kutokana na upungufu wa upatikanaji wa maji safi na salama ikiwa ni pamoja na Kushirikiana na sekta za maji na umeme kuweka mipango yao ya tahadhari ili kuhakikisha kuwa usumbufu unaotokana na ukosefu wa maji na nishati unapewa ufumbuzi mapema”.

Waziri amehimiza Kuimarisha udhibiti wa maeneo ya hifadhi za wanyama pori ikiwa ni pamoja na kuzuia muingiliano  kadri inavyowezekana; sambamba na kuainisha na kuandaa rasilimali za usimamizi wa maafa na kila sekta kushiriki kikamilifu katika eneo lake.

Read More

Sunday, October 2, 2022

WAZAZI WAASWA KUENDELEA KUSIMAMIA MALEZI YA VIJANA


Wazazi wahimizwa kusimamia misingi ya malezi kwa vijana wanapohitimu kidato cha nne kwa kuhakikisha vijana hao wanaendelea na masomo ya kidato cha tano na cha sita ili kuendelea kuwafuatilia kwa ukaribu mienendo ya tabia zao.

Wito huo umetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene katika mahafali ya nane ya kidato cha nne katika shule ya sekondari ya Mtakatifu Catherine iliyopo Lushoto Tanga.

Elimu hii inaushindani mkubwa katika kazi, msome kwa ajili ya uelewa na msome kwa ajili ya kuja kushiriki udahili katika ushindani wa kupata kazi na uwezo wa kujitegemea.

“Katika kipindi hiki ambacho wanasubiria matokeo, wazazi msiwape uhuru vijana kwa sababu umri walionao bado ni mdogo na bado wanahitaji malezi. Wekeni utaratibu wa kutumia simu janja katika kipindi hiki ili waweze kuweka mkazo katika kutimiza malengo yao,” alisema Waziri.

Sitegemei kumwona mmoja wa wahitimu hawa akipotea katika maadili mabovu na matumizi ya madawa ya kulevya bali ni matumaini yangu wote mtasonga mbele na kufikia ngazi za juu kabisa za taaluma. Hii ni kwa manufaa yenu binafsi na taifa letu kwasababu bado tuna uhitaji mkubwa wa wataalamu na ninyi ni sehemu ya wataalamu tunaowahitaji hapo baadaye.

Naye Sr. Fokas Mjema, Msaidizi wa Mama Mkuu wa Shirika la Masister wa Usambara na Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Mtakatifu Catherine, amewashukuru walimu na wanafunzi kwa kufanya mitihani ya majaribio kwa bidii na ungalifu na kuwa makini.

“Wahitimu wetu wa kidato cha nne wanafunzi 65; wameandaliwa vizuri, tunategemea kutokana na maandalizi wapate ufaulu wa daraja la kwanza na ufaulu wa daraja la pili”

Akieleza namna shule ya Mtakatifu Catherine ilivyojiaanda na Mtihani wa Taifa Mwalimu wa Taalumu Nyandwi Mathias Marko amesema; shule inautaratibu wa kufanya mitihani ya majaribio, mitihani ya majaribio kwa vitendo, mitihani ya mwaka, mitihani ya kila wiki, mitihani ya ushirikano na shule nyingine na mazoezi.

“Tunatumia mitihani hiyo kufanya tathimini kwa kuangalia udhaifu ili kuwasogeza sehemu inayostahili,” alisema Mwalimu wa Taaluma.

Akitoa nasaha kwa niaba ya wazazi wengine, Dkt. Wambuka Rangi ametoa rai kwa wanafunzi kuendelea kuwa wachamungu ili kuepukana na matendo maovu ambayo yanapoteza ndoto hasa za watoto wa kike.

“Tunaomba muwe waadilifu na wasikivu kwa wazazi mtakapokuwa nyumbani, ilimuweze kufanikiwa katika maisha yenu ya baadae”

Read More

Tuesday, September 20, 2022

GLOBAL FUND YAUNGA MKONO SERIKALI KUKABILIANA NA MAGONJWA NCHINI

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Dkt. John Jingu amekutana na kufanya mazungumzo na Meneja Mkaguzi kutoka Mfuko wa Kimataifa wa Kupiga Vita UKIMWI, TB na Malaria (GLOBAL FUND) Bwa. Andrew Hammond ofisini kwake Jijini Dodoma.

Dkt. Jingu amesema mazungumzo hayo yalilenga kujadili masuala mbalimbali kuhusu sekta ya afya nchini ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora ya afya katika maeneo yao.

Ameongeza kuwa serikali ya Tanzania itaendelea kushirikana na mfuko huo kwani umekuwa na mchango mkubwa katika kuwezesha vifaa tiba kama ilivyo azima ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Rais Samia  Suluhu  Hassan  ya kujenga miundo mbinu ya  na kuboresha masuala ya tiba kwa wananchi.

Naye Meneja Mkaguzi kutoka Mfuko wa Kimataifa wa kusaidia mapambano  dhidi ya  UKIMWI, TB na Malaria (GLOBAL FUND) Bwa. Andrew Hammond ameishukuru Tanzania kwa kushirikiana na Mfuko huo katika kupiga vita maradhi ya Kifua Kikuu, Malaria na Ukimwi.

Ameahidi kuwa Mfuko wa Dunia utaendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kukabiliana na magonjwa hayo hapa nchini kwa kuelekeza rasilimali fedha kwa ajili ya kununua dawa pamoja na kuboresha mifumo ya utoaji huduma ya afya.

 

Read More

Tuesday, September 6, 2022

SERIKALI KUJA NA MAPENDEKEZO YA SHERIA MPYA YA USIMAMIZI WA MAAFA

 


Serikali imeandaa mapendekezo ya kutungwa kwa  sheria mpya ya usimamizi wa maafa ili kuweka mfumo  wa udhibiti na uratibu wa maafa  kwa ajili ya hatua za kuzuia na kupunguza madhara ya majanga, kujiandaa kukabili na kurejesha hali pindi maafa yanapotokea.

Akizungumza katika kikao cha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria iliyokutana katika Ukumbi wa Bunge Jijini Dodoma kujadili Muswada wa Sheria ya Usimamizi wa Maafa, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene alisema  kutungwa kwa sheria hiyo  ni kuifuta sheria iliyopo sasa ya mwaka mwaka 2015 sura  ya 242. 

Mhe. Simbachawene alieleza kwamba awali masuala ya maafa hayakuwa na mfumo wa kisheria wa uratibu hali ambayo imekuwa ikisababisha mgongano wa majukumu hivyo kutungwa kwa sheria hiyo kutaainisha madaraka, wajibu, maamuzi, utunzaji wa rasilimali na muono unaozingatia taarifa za hali ya hewa.

“Awali masuala ya maafa yalikuwa na daraja fulani la watu, masuala ya kisheria yalikuwa kama yako juu hata ikitokea maafa ngazi ya Wilaya au Kijiji wanasema tumuone Mkuu wa Wilaya sasa tunataka sheria iseme yanapotokea maafa ijulikane kamati gani inahusika  na kuweka mfumo wa ugatuaji kuanzia; madaraka, maamuzi na utunzaji wa rasilimali,”Alisema Mhe. Simbachawene.

Pia aliongeza kwamba sababu nyingine ya kutunga sheria mpya ya Usimamizi wa Maafa ni kuimarisha mfumo wa kiutendaji wakati wa maafa na upatikanaji wa taarifa na takwimu za matukio ya maafa na kuweka mfumo mpya wa kitaasisi unaozingatia mfumo wa kiutawala utakaowezesha ushiriki wa wadau wote muhimu  kabla, wakati na baada ya maafa kutokea nchini..

“Eneo lingine ni kuhakikisha  kamati  hizi zinakuwa za kitendaji na siyo bodi ambapo itasaidia katika kutafuta ufumbuzi yanapotokea maafa pamoja na kuwezesha kurejesha hali ya awali baada ya madhara ya majanga kujitokeza,” aliongeza.

Aidha alieleza kwamba utungwaji wa sheria  utasaidia kutumia taarifa za hali ya hewa na majanga ambapo kamati zitatakiwa kukutana pamoja na utunzaji wa rasilimali ambazo hutumika kukabili na kurejesha hali pamoja na kuzingatia usalama wa wananchi na mali zao.

Kwa upande wake Makamu  Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Mhe. Najma Giga aliipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuendelea  kushirikiana na Kamati  kuhakikisha  sheria mpya inatungwa kama hatua ya kuzuia na kukabili maafa ambayo husabababisha athari kubwa.

Naye Mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo Mhe. Zainabu Katimba alishauri uundwaji wa Kamati Elekezi ya Kitaifa uzingatie sekta badala ya Wizara ambayo huwa na usimamizi wa jumla wa  utekelezaji wa maafa.

Read More

Friday, August 26, 2022

WAZIRI SIMBACHAWENE: MZEE KUSILA AMEFANYA MAMBO MENGI YA KUIGWA


Waziri wa Nchi Ofisi ya waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene amesema Mzee William Kusila alipenda kuona viongozi wanazingatia miiko, na kuishi kwa kuwa mfano mwema kwa jamii.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene alipokuwa akitoa salamu za serikali katika ibada ya mazishi ya Mzee Williamu Jonathan Kusila aliyezaliwa Mwaka 28/02/1944 na kufariki 21/08/2022,  iliyofanyika nyumba kwake kata ya Mtitaa-Bahi Dodoma 26/August/2022.

“Mzee kusila ni kipimo cha mtu muadilifu; mtu mwenye Upendo, na mtu aliyefanya mambo mengi mazuri ambayo tunapaswa kuyaiga na kuyaenzi.”

Tumepoteza kiongozi wa kisiasa aliyeshika nafasi mbalimbali za umma na kutimiza majukumu yake ipasavyo, ni mtu aliyepinga na kukataa rushwa, alisema Waziri.

Aidha ametoa rai kwa Watoto wa Mzee Kusila kuzidi kushirikiana na kushikamana ili kutunza jina na heshima ya baba.

“Amefafanua watu hawazaliwi sawa, mtatofautiana kwa uwezo wa elimu, uwezo wa kipato na mambo mengine lakini wote ni Watoto wa mzee Kusila ni lazima mtengeneze mamlaka itakayosaidia kuwaongoza kama familia”

Naye  Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule amesema  Mzee William Kusila alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Saba wa Dodoma kati ya Mwaka (1993-19995) alikuwa Mbunge wa jimbo la Bahi na katika vipindi tofauti amekuwa waziri wa kilimo, Waziri wa Mawasiliano na Uchukuzi na amewahi kuwa Mwenyekiti wa chama cha Mapinduzi Mkoa wa Dodoma.

 “Alifanya kazi kwa upendo Mkubwa; aliokuwa nao kwa wananchi wa Dodoma, Baba yetu aliongoza kwa Vitendo na sio kwa kuagiza, kama alisema limeni nayeye alikuwa analima”

Naye Mbunge Mstaafu wa jimbo la Chilowa Mhe. Hezekiah Chibulunje akitoa salamu za rambirambi amesema anamkumbuka mzee Kusila kwa jitihada zake za kuondoa Njaa Dodoma na kuhakikisha tunapanda mazao yanayostahimili ukame.

“Alikuwa na uchungu sana katika kuondoa njaa na vile vile katika swala la zima la kusimamia elimu, nimefanya naye kazi kwa ushirikiano mkubwa sana bila nongwa”

 

Read More

Wednesday, August 24, 2022

JITOKEZENI KWENYE ZOEZI LA SENSA ILI MUHESABIWE


 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu  Mhe. George  Simbachawene amehimiza wananchi kujitokeza kuhesabiwa katika zoezi la sensa ya watu na makazi kwa ajili ya maendeleo yetu wenyewe.

“Unapohesabiwa unakuwa upo katika mpango wako wa maendeleo, katika sehemu yako unayoishi na Nchi kwa ujumla”

Hayo yamesemwa na waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene baada ya kushiriki zoezi la sensa ya watu na makazi jimboni kwake Kibakwe katika Halmashauri ya wilaya ya Mpwapwa.

Amefafanua kwamba usipohesabiwa, unakosa lile fungu lako katika miaka 10 ijayo kwa ajili ya mipango ya maendeleo.

“Bado tuna siku tano mbele kwa ajili ya kuhesabiwa hakikisha umeacha kumbukumbu za watu walilolala usiku wa kuamkia tarehe 23 Agusti 2022, alisema  Waziri”

Read More

Saturday, August 20, 2022

WATENDAJI WAHIMIZWA KUONGEZA KASI UTEKELEZAJI WA MRADI WA AFDP


 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene amehimiza kuwa na vikao vya uratibu vya pamoja kati ya wizara na taasisi zinazotekeleza mradi wa mradi wa AFDP ili kuongeza kasi ya utekelezaji wa mradi.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe.  George Simbachawene alipotembelea shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) Kigamboni Jijini Dar es salaam ambalo linatekeleza programu ya kuendeleza kilimo na uvuvi katika mradi wa AFDP unaoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu sera Bunge na Uratibu na kutekelezwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Kilimo na Wizara ya Uchumi wa Bluu na Uvuvi – Zanzibar.

Waziri Smbachawene amesema programu AFDP ni ya miaka sita kuanzia 2021/2022 hadi 2027/2028 ambayo itagharimu jumla ya Dola za Kimarekani 77.4 millioni (Mkopo toka IFAD USD 58.8 millioni; Serikali USD 7.7 millioni; Sekta Binafsi 8.4 millioni na Wananchi USD 2.4 millioni).

 “Mradi huu wa  uchumi wa bluu ukisimamiwa vizuri utaibua shirikia la TAFICO, na utaibua uchumi wa biashara ya uvuvi zinazofanywa na sekta binafsi.“

Lazima tutengeneze kikosi kazi kitakachokuwa kinaashughulikia changamoto zinazojitokeza kutoka taasisi moja kwenda nyingine pamoja na wizara moja kwenda nyingine katika utekelezaji wa mradi, alisema Waziri.

“Eneo hili linaloshughulikiwa na shirika la TAFICO linaenda kujibu ahadi za ilani ya uchaguzi ya mwaka 2020-2025.”

Naye Katibu Mkuu Ofisi ya waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Dkt. John Jingu amesema mradi huu ni mradi mkubwa sana na ni mradi wa kimkakati.

“Tuone namna ambavyo tutautekeleza huu mradi kikamilifu, spidi na kasi ya utekelezaji wa mradi bado hairidhishi.”

Kwa upande wake Mwenyekiti wa bodi ya shirika la TAFICO Profesa Yunus Mgaya amesema wanalichukulia shirika la TAFICO kama shirika la kimkakati hasa katika dhana ya kutekeleza uchumi wa blue.

“Shirika linajukumu la kuwasaidia wavuvii wadogo wadogo hasa katika kunyanyua  vipato vyao, kuwawezesha kuhifadhi mazao yao ya uvuvi kuingia ubia na wananchi mbalimbali katika shughuli za uvuvi bahari kuu,”

Read More

Thursday, August 18, 2022

WATENDAJI WA SENSA WATAKIWA KUFANYA KAZI KWA BIDII

Watendaji wa Sensa wapewa wito kufanya kazi kwa bidii ili kuweza kukamilisha kwa ufanisi  zoezi la Sensa ya watu na Makazi inayotarajiwa kufanyika 23 August 2022, wito huo imetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene.

“baada ya zoezi la sensa ya watu na makazi kuna kazi kubwa ya Mchakato lazima tuwe tayari kusimama pamoja na kufanya kazi usiku na mchana ili zoezi liweze kukamilika”

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene katika kikao cha saba cha kamati kuu ya Taifa Sensa ya Watu na Makazi 2022 kilichofanyika ukumbi wa Julius Nyerere Convection Centre, Dar es saalam.

Waziri Simbachawene ameipongeza kamati ya Sensa ya Watu na makazi ya mwaka 2022 kwa kufanya kazi zake vizuri na hivyo kufanikisha maamuzi ya kamati kuu ya Taifa ya Sensa.

“Vilevile napongeza Wizara zote, Wadau wa Maendeleo na Sekta binafsi kwa ushirikiano mkubwa  walioonesha wakati wote wa maandalizi ya sensa ya watu na makazi”

Mtakwimu Mkuu wa Serikali Dkt, Alibina Chuwa amesema kwa wakuu wa kaya ambao hawatakuwa nyumbani wameandaa fomu maalumu ambayo itakuwa na maswali 11 ambayo itasambazwa kwa wakuu wote wa kaya kupitia kwa makarani wao wa sensa.

“Wakuu wa kaya waandike taarifa za watu ambao watakuwa wamelala usiku wa kuamkia siku ya sensa ili kumrahisishia karani kujaza taarifa kwenye kishikwambi atakapofika kuchukua taarifa”

Read More

Monday, August 15, 2022

MAANDALIZI YA SENSA YA WATU NA MAKAZI YAPAMBA MOTO


 

Serikali imesema maandalizi ya Sensa ya Watu na Makazi yamefika zaidi ya asilimia 95 hivyo ni vyema kuendelea kushirikiana kwa pamoja kwa kuzingatia muda uliobaki ili kulifikia lengo lililopo.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene katika Mkutano Maalum wa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa alipokutana na sekta binafsi kwa lengo la kutambua mchango wao katika kuelekea siku hiyo ikiwemo ya rasilimali fedha, huduma na vifaa kwa ajili ya zoezi la Sensa ya watu na makazi ya Mwaka 2022.

Alisema kuwa, Serikali inatambua mchango wa sekta binafsi hivyo ni vyema kwa kila mdau kushirikia katika zoezi hili  kwa kadri awezavyo kwa kuchangia  rasilimali fedha, huduma na vifaa vitakavyosaidia kufanikisha zoezi la sensa.

“Karibu kila mdau ameshiriki katika maandalizi ya sensa kupitia taasisi ya sekta binafsi (TPSF) na tumekutana hapa ili kuonesha mshikamano wetu na kutambua michango yenu ninawapongeza sana," alisema Simbachawene.

Naye katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Dkt. John Jingu amesema serikali imeshirikiana sekta binafsi  katika maandalizi ya kuelekea siku ya sensa kwa namna mbalimbali ikiwemo, kugharamia matangazo yanayotoka kwenye vyombo vya habari.

“Kampuni za simu zilisaidia kutoa ujumbe mfupi wa kuhamasisha wananchi na kuelimisha wananchi juu ya zoezi la sensa ya watu na makazi na baadhi kuahidi kuchangia fedha na vifaa mbalimbali ili kufanikisha zoezi la sensa ya watu na makazi” alisisitiza Dkt. Jingu

Naye Kamisaa wa Sensa ya Watu na Makazi Mhe. Anne Makinda ameshukuru sekta binfasi kwa mchango wao katika kuwezesha maandalizi ya kuelekea siku ya sensa ya watu na makazi inayotarajiwa kufanyika tarehe 23 Agosti, 2022.

“Tumejipanga kusimamia matumizi yote tunayopewa na kuhakikisha tunapata matunda tunayotegemea.” aliesema Mhe. Makinda

Read More

Sunday, August 14, 2022

WAUMINI WAOMBWA KUENDELEA KUIOMBEA NCHI

 


Waumini waombwa kuiombea nchi dhidi ya majanga mbalimbali likiwemo janga la njaa, changamoto za kiuchumi zinazo sababishwa ama na sisi wenyewe au mataifa mengine, magonjwa, dhiki na mmomonyoko wa maadili.

“Uwekezaji katika familia imara ni jambo la msingi, bila kwekeza katika familia hakuna nchi hakuna mataifa hakuna dunia.Msukumo wa watu wanaosimamia dhambi kutumia rasilimali fedha kwenye mambo maovu ni mkubwa  kuliko msukumo wa kutetea mambo mema.”

Wito huo umetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene ufunguzi rasmi wa sikukuu za vibanda (makambi) za kanisa la waadventista wa sabato Magomeni Mwaka 2022, Kwembe Jijini Dar es Salaam yaliyokuwa na Kauli mbiu “NITAKWENDA KWA NGUVU ZA MUNGU.”

Amefafanua kwamba pamoja na kumtegemea Mungu, bado maandiko matakatifu yanatuhimiza kufanya kazi kwa bidii. Katika hili niendelee kuwasihi ndugu Waumini kufanya kazi kwa bidiii huku tukimtumainia Mungu na kuomba baraka zake katika kila kitu. Licha ya kwamba nchi yetu haiegemei upande wowote katika masuala ya dini (Secular State) lakini sehemu kubwa ya watu wake wanaamini katika Mungu kupitia dini na madhehebu mbalimbali.

“Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan inatambua mchango wa Kanisa la Waadventista wa Sabato katika Sekta ya elimu kupitia taasisi zake za elimu; Sekta ya afya kupitia hospitali na vituo vya afya; pamoja na Sekta ya habari kupitia vyombo vya Habari vinavyomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa. Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi na rafiki kwa ustawi wa taasisi hizo ili ziendelee kuwa sehemu ya kuliletea maendeleo Taifa letu.”

Naye Mchungaji Fidelis Mngwabi, Askofu wa Jimbo la Mashariki Kati mwa Tanzania (ECT), katika neno lake la shukrani ameishukuru serikali kwa kutambua mchango wa kanisa la  waadventista wa Sabato katika kulinda umoja amani na Upendo.

“kanisa litaendelea kuwa na msimamo wa Mungu katika kusaidia waumini kwenda katika njia iliyo sahihi.”



Read More

Thursday, August 11, 2022

WIZARA ZAHIMIZWA UFUTAILIAJI WA TAARIFA ZA MPANGO KAZI

Viongozi wa Wizara wapewa rai kufuatilia na kusimamia kwa karibu maafisa viungo ambao wanahusika kuweka taarifa kwenye mfumo ili Viongozi wawe na umiliki (ownership) wa taarifa zilizo katika mfumo huo.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene katika kikao kazi cha Mawaziri kilichofanyika katika Ukumbi wa Kambarage Hazina Jijini Dodoma.

“Kwa upande wa uwasilishaji wa Taarifa ya Ilani ya Chama Tawala, uchambuzi umeonesha kuwa kwa kipindi cha mwaka 2022 ni Wizara 14 zilizowasilisha Mpango Kazi wa Utekelezaji wa Ilani kwa mwaka 2022 na Wizara 13 hazijawasilisha. Taarifa za Mpango kazi hutakiwa kuwasilishwa kwenye Mfumo wa ‘DASHBOARD’ mwezi Januari kila mwaka. Aidha, kwa upande wa Taarifa ya Utekelezaji wa Ilani kwa kipindi cha nusu mwaka, ambazo hutakiwa kuwasilishwa Julai 2022 ni wizara 4 zilizowasilisha.”

Kwa mwaka 2022 tumepokea maelekezo yako kuwa Taarifa ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuhusu Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2020 na Taarifa ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, kuhusu Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2020 itawasilishwa mwezi Novemba, 2022. Ili kuratibu taarifa hiyo vyema na kwa wakati, napenda Mawaziri kuratibu taarifa katika maeneo yanayowahusu na kuhakikisha zinawasilishwa kwa wakati kupitia mfumo huo, alisema Waziri.

 

 

Read More

Monday, August 8, 2022

WADAU WA KILIMO WAHIMIZWA KUTUMIA TEKNOLOJIA KUTATUA CHANGAMOTO ZA KILIMO

 


Serikali imetoa rai kwa wadau wa kilimo kuendelea kutambua Ubunifu na Teknolojia mpya zinazooneshwa katika maonesho ya Nanenane ili kuweza kuzikuza na kuzisambaza kwa walengwa wakiwemo Wakulima, Wafugaji na Wavuvi

“Maonesho ya Nanenane yawe ni kitovu cha teknolojia mpya (innovation hub) kwa kuhakikisha kuwa wadau wote wa Sekta za Kilimo, Mifugo na Uvuvi wanashiriki Maonesho haya, ili kuonesha na kujifunza teknolojia zote zinazotoa majawabu ya changamoto za Sekta hizo,”

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene alipokuwa akihutubia katika kilele cha maonesho ya siku ya Nanenane kanda ya Mashariki yaliyofanyika Uwanja wa Mwl. Julius Nyerere Mjini Morogoro kwa niaba ya mgeni rasmi katika maadhimisho hayo Mhe. Hemed Suleiman Abdulla, Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Sote tunatambua mchango mkubwa wa Sekta za Kilimo, Mifugo na Uvuvi katika kuchangia pato la Taifa, ajira, usalama wa chakula na malighafi za viwandani. Ndiyo maana kauli mbiu ya maonesho ya mwaka huu inasema “Ajenda ya Kilimo  ni Biashara, Shiriki Kuhesabiwa kwa Mipango Bora ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

“Waoneshaji wanatakiwa kuhakikisha kuwa takwimu na taarifa sahihi zenye ulinganifu kuhusu teknolojia na bidhaa wanazoonesha zinakuwepo ili ziweze kuwasaidia walengwa kufanya maamuzi sahihi, alisema Waziri” 

Aidha Maonesho ya Nanenane yatumike kutangaza fursa za uwekezaji zilizopo katika Sekta za Kilimo, Mifugo na Uvuvi ili kuvutia wawekezaji wengi.

Amefafanua kila ngazi kwa maana ya Kanda, Mikoa, Halmashauri na Wadau wengine ifanye tathmini kwa kuangalia mambo mbalimbali ikiwemo hali ya ushiriki na uhalisia wa teknolojia zinazooneshwa kama zinatumika katika maeneo wanayotoka.

Naye naibu waziri wa kilimo Mhe. Anthony Mavunde amesema bajeti ya kilimo imetoka billioni 294 (2021-2022) mpaka kufikia billioni 954 kwa mwaka wa fedha (2022-2023). Wizara ya kilimo tumejipanga kuleta mapinduzi ya kweli katika kufikia ajenda ya 2030 kwa ushirikiano wa wadau wote kuikuza sekta ya kilimo kufikia 10%.

“Bajeti ya umwagiliaji imepanda kutoka billioni 46 ya mwaka wa fedha uliopita hadi kufikia billioni zaidi ya 400 kwa mwaka huu wa fedha (2022-2023).  Mikakati ni kuwa na mfumo mzuri wa Umwagiliaji na utekelezaji wake umeanza kwa kupitia mabonde yote 22 ya umwagiliaji ili kufanya upembuzi yakinifu na usanifu ili tuanze kufanya kilimo cha umwagiliaji katika maeneo hayo, alisema Naibu waziri.”

Amebainisha katika Utafiti bajeti imepanda kutoka billioni 11.7 kwenda billioni 40 ili kuviwezesha vituo vya utafiti kuja na mbegu bora na mbegu ambazo zinastahimili ukame, sambamba na kujengea uwezo vituo vyetu hasa katika maabara za kupima afya ya udongo.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Fatma A. Mwasa amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kurudisha pembejeo kwa wakulima. Kupitia ruzuku hiyo mkulima hata nunua kwa bei ya kawaida  bali kutakuwa na punguzo ili kumuwezesha mkulima azalishe kwa tija.

“Maonesho haya yana umuhimu mkubwa na yanatoa elimu kubwa kwa wakulima, tumedhamiria kuichukua teknolojia tuliyoipata kuihamishia vijijini alisema mkuu wa mkoa wa Morogoro.”

Read More

Tuesday, July 26, 2022

HALMASHAURI YA MERU YAPATA ELIMU YA KUKABILIANA NA MAAFA

 


Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa, Luteni Kanali Selestine Masalamado amesema elimu ya usimamizi wa Maafa itaendelea kutolewa kwa wananchi  kwa maeneo yanaoathirika kwa matukio ya tofauti tofauti ya maafa.

“Tunatoa elimu kwa wananchi ili kujenga uelewa wanamna ya kukabiliana na maafa, kwa kueleza dhana ya maafa, kueleza maana ya majanga ikiwa pamoja na kuangalia mzingo wa maafa kwa ujumla”

Hayo yamesemwa na Luteni Kanali Selestine Masalamado Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu kwa kushirikiana na shirika la kimataifa la uhamiaji (IOM) katika kikao cha mafunzo ya Udhibiti wa Maafa kwa jamii yaliyofanyika Halmashauri ya Wilaya ya Meru na kuhusisha wananchi wa kata ya Mbuguni na Shambaray Bruka.

 “Washiriki wameelewa mfumo mzima wa Kudhibiti Maafa kwa kuanzia ngazi ya taifa hadi kufikia ngazi ya Kijiji, alisema Luteni Kanali”

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru Mwl.Zainabu Makwinya ameshukuru Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu kwa kufanya mafunzo hayo Halmashauri ya wilaya ya Meru.

“Tunashukuru kwa kutuongezea  wataalamu wa maafa kupitia mafunzo yaliyoyotolewa ili kutusaidia namna ya kukabiliana  na Maafa.”

Mwl. Makwinya amefanunua kata ya Shambaray Bruka na Mbuguni yamekuwa yakiathirika na mafuriko na ukame,

Ametoa wito kwa washiriki kutoa elimu kwa wananchi ili kuongeza maarifa kwa  kusaidia maeneo mengine yanayoyoathirika na maafa.

Naye Mshiriki Fanael Kaaya Mshiriki kutoka kata ya Mbuguni amesema mafunzo ya kukabiliana na maafa waliyopata imesaidia kuchukua tahadhari ya kujikinga na maafa kabla hajatokea ikiwemo kutengeneza matuta ya kuzuia maji kwenye maeneo yanayoathirika na mafuriko na pamoja kufukua mifereji iliyoziba pamoja na mito ili mafuriko ya maji yanapokuja yaweze kupita.

Read More

Wednesday, July 20, 2022

SERIKALI YAHIMIZA USHIRIKIANO KATIKA KUIMARISHA UTENDAJI WA KAZI SEKRETARIETI YA SADC

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya waziri Mkuu sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene ameishauri sekretarieti ya SADC kwa Kushiriiana katika kuimarisha  utendaji wa kazi wa Kituo cha udhibiti wa Maafa.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu katika Mkutano wa kamati ya Mawaziri wanaoshughulika na udhibiti wa maafa kwa Nchi wanachama wa SADC uliofanyika Lilongwe Nchini Malawi.

Katika kikao hicho waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu aliaambatana na Mkurugenzi wa Idara ya Maafa, Ofisi ya waziri Mkuu Meja Jenerali Michaeli .M. Mumanga aliyeongeoza ujumbe wa Tanzania katika Kikao hicho.

Read More

Monday, July 18, 2022

Katibu Mkuu Dkt. Jingu ahimiza ufanisi ujenzi wa Mji wa Serikali


 Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Dkt. John Jingu azitaka Wizara zote kuhakikisha zinasimamia ufanisi na weledi katika ujenzi Awamu ya Pili wa majengo ya Ofisi zao katika Mji wa Serikali Mtumba.

Ameyasema hayo mapema alipokutana na Wakurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu wa Wizara zote katika Ukumbi wa mikutano wa ofisi yake Jijini Dodoma kwa lengo la kujadili maendeleo ya ujenzi wa Ofisi za Wizara hizo zinzojengwa Mtumba Jijini Dodoma.

Dkt. Jingu alisema,kila wizara inajukumu la kuhakikisha majengo yanajengwa kwa viwango vinavyoendana na thamani ya fedha huku akiwataka kuendelea kufanya kazi kwa uzalendo kama ilivyoelekezwa.

“Viongozi wetu na wananchi kwa ujumla wana matarajio makubwa kuona mji wa Serikali unakamilika kwa wakati na kwa ubora unaotakiwa hatutarajii kuwa na delays,”alisema Dkt. Jingu

Aidha alizitaka kila Wizara kuendelea kuzingatia ubora katika kulifanikisha zoezi hilo huku wakiwasimamia wakandarasi na kuhakikisha kila vifaa vinavyonunuliwa vinakaguliwa na timu husika kabla ya matumizi.

Aliwasihii viongozi hao kuongeza rasilimali watu, vifaa na wataalamu ili kuweza kukamilisha ujenzi wa majengo hayo.

“kazi ya ujenzi izingatie viwango vilivyopo, katika hili tumeunda timu mbalimbali za kupitia na kukagua viwango ambapo tumewapa kazi BICO ya kufanya Quality assurance kuona mihimili ya majengo na mifumo mbalimbli ikiwemo ya maji, umeme na TEHAMA inakidhi vigezo hivyo naomba tuwape ushirikiano ili watimize kazi zao,”Alisisitiza

Hata hivyo Dkt. Jingu aliwasisitiza kuendelea kutoa taarifa za maendeleo ya ujenzi huo kila ifikapo tarehe 30 ya mwisho wa mwezi na kuwasilishwa katika Ofisi ya Waziri Mkuu ili kujua na kuwa na uhakikika wa kazi inavyoendelea.

Katika hatua nyingine aliwasihi kuendelea kutunza miti iliyopandwa katika maeneo ya ofisi zao kwa kuzingati umuhimu wake wa kuboresha mazingira na kuupamba mji huo.

“Kila Wizara ihakikishe inatunza miti iliyopandwa na kuzingatia mikataba ya upandaji wa miti katika Mji wa Serikali,”alisisitiza Dkt. Jingu

Read More

Friday, July 15, 2022

TANZANIA YAPIGA HATUA KUBWA KATIKA KUDHIBITI NA KUPAMBANA NA UKIMWI



Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene amesema vifo vitokanavyo na UKIMWI vimepungua kwa 50% kutoka vifo 64,000 mwaka 2010 hadi 32,000 mwaka 2020.

“ Maambukizi mapya ya VVU kwa watu wazima (miaka 15 na zaidi) yameshuka kutoka 110,000 mwaka 2010 hadi 68,000 mwaka 2020; na Maambukizi mapya kutoka kwa Mama kwenda kwa Mtoto (Mother to child transmission) yameshuka kutoka 18% mwaka 2010 hadi 7% mwaka 2020.”

Hayo yamesemwa na waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene kwenye harambee ya uchangishaji wa fedha za kupanda Mlima kilimanjaro ili kuendeleza mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI mwaka 2022.

Alieleza Matumizi ya dawa za kufubaza VVU (ARV) kwa WAVIU wanaojua hali zao za maambukizi yameongezeka kutoka 95% mwaka 2016 hadi 98% mwaka 2020;

Aidha maambukizi mapya ya VVU kwa watu wazima (miaka 15 na zaidi) yameshuka kutoka 110,000 mwaka 2010 hadi 68,000 mwaka 2020.

“Serikali, tayari imetenga fedha Bilioni 1.88 kwenye bajeti ya 2022/2023 ili iendelee kuchangia AIDS TRUST FUND alisema waziri”

Amefafanua serikali itaendelea kuwa mstari wa mbele kuhakikisha kuwa afua zinazotekelezwa za Mwitikio wa VVU na UKIMWI zinaleta tija kwa makundi mbalimbali katika jamii.

Amesema ili kufikia malengo haya pamoja na mengine katika kuishinda vita hii dhidi ya VVU na UKIMWI, kunahitaji nguvu ya pamoja kati ya serikali na wadau wengine, hususan sekta binafsi ili kupata rasilimali fedha ya kutosha.

 “Kili challenge inalenga kupunguza athari za kupungua kwa misaada ya wahisani na kuiwezesha Nchi kuimarisha uwezo wa ndani kwa ajili ya kudhibiti UKIMWI”

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti UKIMWI Dkt. Leonard Maboko, amesema kutakuwa na wapanda baiskeli 28 kuuzunguka Mlima Kilimanjarao na wapandaji mlima kwa Mguu 24.

Kwa muda wa miaka 20 zoezi hili limekuwa likifanywa na kuchangia kiasi cha dola za kimarekani million 7 zimekusaywa na zimesaidia sana katika makabilia kuendeleza mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI mwaka.

Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro Mhe. Stephen Kagaigai, ameshukuru wadau wote walioshiriki kwa lango la kutafuta  fedha za muitikio wa VVU na UKIMWI.

“Nimatumaini yangu kwamba ushirikiano huu utaendelea ili kufikia malengo ya sifuri tatu, kufikia mwaka 2030 ya kutokuwa na maambukizi mapya, unyanyapaa na vifo vitokanavyo na UKIMWI. Kushuka kwa maambukizi ya UKIMWI ni matokeo ya pamoja ya Wadau wa sekta ya Umma na Binafsi”

Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania; Dkt. Leornad Maboko amesema fedha zinazopatikana katika harambee zitasaidia sana katika kuendeleza mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI.

“Tumeunda kill Trust Fund, wajumbe wa bodi wanatoka upande (GGM) Geita Gold Mine na wengine wanatoka Tume ya Kudhibiti na Kupambana na UKIMWI, bodi imesaidia sana katika kuja na mikakati ya kufanya mara baada ya kukusanya Fedha”

Naye Makamu  wa Rais wa Kampuni ya Mgodi wa Geita Gold Mine Bwn. Simon Shayo, Makamu wa Rais wa Kampuni ya Mgodi wa Geita (GGM);  amesema tumekuwa tukikusanya fedha zinazosaidia maeneo mabalimbali, baadhi ya taasisi zimeasisiwa kutokana na uwepo wa mfuko huo ikiwemo kituo cha kulelea Watoto yatima Mkoani Geita.

“Kituo kilianza na Watoto 13 lakini sasa kina Watoto zaidi ya 170 ambao wanapata elimu wanapata huduma za afya kutokana na watu wanajitolea kuchangia kupitia Mfuko. Kundi la kwanza la Watoto walioingia kwenye kituo hicho wengi wao wako chuo kikuu”


 

Read More

Saturday, July 2, 2022

Mhe. Hemed Suleiman: “Tanzania kufanya Sensa ya aina yake”

 


Makamu wa Pili wa Rais, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdullah ameeleza kuwa Nchi ya Tanzania imejipanga kufanya ya sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 kwa njia ya kidijitali ambapo itarahisisha ukusanyaji wa taarifa wakati wa zoezi hilo.

Ametoa kauli hii wakati akifunga mafunzo ya Wakufunzi wa sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 ngazi ya Taifa uliofanyika katika Ukumbi wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Mkwawa Mkoani Iringa tarehe 01 Julai, 2022.

Makamu wa Pili wa Rais alisema kuwa, sensa ya mwaka huu itaendeshwa kwa mifumo ya kitehama ambapo itakuwa ni mara ya kwanza kwa nchi kuwa na mfumo mpya utakaongeza ufanisi.

“Sensa ya mwaka huu ni ya sita itakayobebwa na upekee wa aina yake kwani inaunganisha matukio mawili makubwa ya kitaifa ikiwemo la ukusanyaji wa taarifa za majengo yote nchini pamoja na taarifa za idadi ya watu,” alieleza.

Aidha alisema hadi sasa maandalizi yake yamefiki asilimia 87 na hii inaonesha ni hatua nzuri kwa taifa hivyo watu waendelee kupewa elimu kwa wingi.

“Kuhesabu watu kitaalam itasaidia kupata taarifa kwa urahisi, na kazi hii itafanyika kwa umakini mkubwa hivyo tuifanye kwa weledi na viwango vinavyotakiwa,”aliongezea Mhe. Abdallah

Sambamba na hilo alitoa rai kwa wakufunzi hao kuendelea kuzingatia uzalendo katika utekelezaji wa majukumu yao.

“Wahitimu wetu wote zingatieni uzalendo na muwe vielelezo vizuri kwa kuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha wananchi kujitokeza katika zoezi hili la sensa  ili kuleta matokeo makubwa,”alisisitiza.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene alieleza kuhusu utekelezaji wa zoezi la Operesheni Anwani za Makazi kuwa  umefikia asilimia 95, hii ikiwa ni muunganiko wa utekelezaji wa shughuli zote zilizopangwa.

Aidha alisema kuwa, Kazi zinazoendelea kufanyika kwa sasa ni kuhakiki na kusafisha taarifa za anwani pamoja na kuweka miundombinu ya anwani za makazi inayojumuisha nguzo za majina ya barabara na kubandika vibao vya namba za nyumba/anwani kwenye majengo.

“ Licha ya kuwa hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa Operesheni hii kuwezesha zoezi la Sensa kufanyika kwa tija, Operesheni hii imeacha alama katika kuimarisha ustawi wa jamii, Vijiji na Miji, Mamlaka za Serikali za Mitaa, Mikoa na Taifa katika nyanja mbalimbali ikiwemo Uchumi wa Kidijitali,”alisema Mhe. Simbachawene

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Hamad Hassan Chande alisema kuwa, zoezi la sensa ya watu na makazi ni nyenzo muhimuu kwa kuzingati tija iliyopo hususan katika masuala ya mipango ya maendeleo ya nchi yetu kwa kuzingatia uwepo wa bajeti yenye kukidhi mahitaji yaliyopo.

“Matokeo ya sensa ya mwaka 2022 yatatoa mwelekeo mzima wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mhe Samia Suluhu Hassan kuhusu utekelezaji wa ahadi zilizotolewa kwa wananchi wetu kupitia ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020-2025, na matokeo haya ni nyenzo muhimu kwa wizara yangu kwani yatasaidia kufuatilia utekelezeaji wa bajeti katika sekta zote,”alisisitiza.

AWALI

Wakufunzi zaidi ya 500 wamehitimu mafunzo ya Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 kwa ngazi ya Taifa yaliyofanyika katika Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Mkwawa Mkoani Iringa tarehe 01 Julai, 2022 ambapo wakufunzi hao walitumia jumla ya siku 21 kupatiwa ujuzi huo.

Read More

WADAU WA MTAKUWWA WALENGA KUNGANISHA NGUVU DHIDI YA VITENDO VYA UKATILI WA KIJINSIA

 


 

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu, Dkt. John Jingu ametoa wito kwa, Taasisi mbalimbali za serikali, kiraia na wadau mbalimbali wa maendeleo kuunganisha nguvu  dhidi ya ukatili wa wanawake na Watoto.

“Tumefanya tathimini kuhusu hali halisi jinsi ilivyo kuhusu ukatili, changamoto bado zipo na tumekubaliana tuunganishe jitihada, kwa kufanya kazi kama timu katika kupambana dhidi ya ukatili wa wanawake na Watoto.”

Wito huo umetolewa katika kikao cha dharura cha Makatibu Wakuu wa Wizara za Kisekta wa Mpango wa Taifa wa Kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto (MTAKUWWA) kilichoongozwa na Mwenyekiti Dkt, John Jingu Mjini Dodoma.

“Aidha tumekubaliana kuongeza kasi ya utekelezaji katika maazimio mbalimbali ambayo tumekubaliana na jitihada hizi tutaendelea kuzifanyia kazi na tathimini kila wakati ili kutokomeza ukatili dhidi ya Watoto, alisema Dkt. Jingu”

Awali Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Zainabu Chaula amesema tunapaswa kupaza sauti dhidi ya ukatili wa wanawake na Watoto kuanzia umri usiojitambua mpaka umejitambua.

 “Janga hili liko kwenye ngazi ya kifamilia, tafiti zinaonyesha ukatili mwingi unaofanyika dhidi ya watoto unazimwa katika ngazi ya kifamilia kwa sababu ya kuogopa kuleta migogoro. Watoto hawa ambao hawana hatia unawasababishia kupata sonona, na utuuzima usioeleweka, alisema Dkt. Chaula.”

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bi, Mary Makondo amesema wamejipanga kuhakikisha wanafanya mapitio ya sheria,  sheria ya haki ya mtoto, sheria ya ndoa kwenye umri wa mtoto na kuangalia wadau wote kwenye uendeshaji wa kesi.

Tunaamini kupitia wadau katika huduma za msaada wa kisheria, tukienda pamoja kuwezesha huduma za msaada wa kisheria lakini pia kutoa elimu ili kuona swala hili ni janga la kitaifa na Watoto wanapaswa kulindwa.

“Mahakama kama muhimili imekuwa ukitoa adhabu stahiki, lakini bado tunahitaji kuangalia mapitio ya sheria za makossa ya jinai lakini pia mwenendo wa makossa ya jinai ili kuhakikisha adhabu zinazotolewa zinaendana ili ziwe mafunzo kwa jamii katika kuhakikisha haki za Watoto na wanawake  zinalindwa alisema Katibu Mkuu Bi, Makondo.”

 

Read More

Wednesday, June 29, 2022

VIJANA JIKINGENI NA MAAMBUKIZI YA VVU- MHE. SIMBACHAWENE

 


Serikali imetoa rai kwa vijana nchini kufanya juhudi za kujikinga na maambukizi mapya ya Virusi vya   UKIMWI (VVU) pamoja na walio shuleni kuhakikisha wanazingatia masomo na kujiepusha na tabia hatarishi zitakazosababisha kupata maambukizi na kushindwa kuyafikia malengo yao.

Rai hiyo ilitolewa na Waziri wa  Nchi  Ofisi ya Waziri Mkuu  Sera, Bunge na Uratibu Mhe. George Simbachawene  wakati  wa hafla ya uzinduzi wa Ugawaji Vishikwambi kwa walimu wa Shule za Msingi na Sekondari kupitia mradi wa Timiza Malengo.

Mhe. Simbachawene alisema lengo la mradi huo ni kusaidia vijana wenye umri wa miaka 10 hadi 24 kutimiza ndoto zao pamoja na kuwasaidia vijana walio  ndani na nje ya shule  kwa kuwajengea uwezo wa fikra , maarifa na maadili ili wawe salama dhidi ya maambukizi ya VVU.

“Kama Taifa tuna kila sababu ya kulinda kundi la vijana kuimarisha nguvu kazi ya Taifa , kukuza uchumi pia kujenga Taifa imara na lenye nguvu . Nia ya Serikali ni kuhakikisha tunakuwa na vijana wazalendo wanaotambua mchango wao katika jamii , wenye kujitolea katika shughuli za maendeleo ,” alisema Mhe. Simbachawene .

Pia aliongeza kuwa mradi huo unaogharimu takribani bilioni 55 unafadhiliwa na Mfuko wa Dunia wa UKIMWI , Kifua Kikuu na Malaria (Global Fund) wasichana balehe na wanawake vijana  wapatao 1,000,000,000 watafikiwa na mradi huo.

“Niwapongeze wadau wa maendeleo kwa kutambua umuhimu wa mapambano haya  na udhibiti wa maambukizi ya VVU hususani kwa vijana  na ndani ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mhe Rais Samia Suluhu Hassan inaridhishwa  na utekelezaji wa mradi  kwani umefanikiwa kutoka mikoa mitatu hadi mitano  na Halmashauri 10 hadi 18 nchini,”aliongeza.

Aidha aliwataka Wakurugenzi Watendaji wa Halmashauri zinazotekeleza mradi kusimamia kwa ufanisi pamoja na kuanisha Klabu za UKIMWI shuleni, kusimamia na kufuatilia  uwajibikaji wa Maafisa Ugani katika usimamizi wa maendeleo ya utekelezaji wa mradi  kwa walengwa  na kusimamia matumizi sahihi ya zana  kwa uendelevu wa mradi katika Halmashauri husika.

Kwa upande wake Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda alibainisha kwamba kukithiri kwa vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia shuleni na katika maeneo mbalimbali huchangia kwa kiasi kikubwa maambukizi mapya ya UKIMWI na afya za watoto na vijana kuathirika.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) Dk. Leonard Maboko alieleza kuwa ni kusudi la tume hiyo chini ya mradi wa Timiza Malengo kuwezesha wasichana balehe na wanawake vijana kukaa shuleni kutimiza malengo yao na walio nje ya shule kupatiwa elimu ya ujasiriamali na kupewa ruzuku kuanzisha miradi midogo midogo kujikwamua kiuchumi.

Read More