Tuesday, April 30, 2019

WAZIRI MKUU: SERIKALI IMETOA SH. BILIONI 118 KUIMARISHA MAWASILIANO


*Ahimiza wananchi walinde minara ya mawasiliano popote pale ilipo

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema tangu Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote uanzishwe, Serikali imechangia shilingi bilioni 118 ili kuimarisha huduma za mawasiliano ambapo wakazi zaidi ya milioni tano kwenye kata 703 zenye vijiji 2,501 wameweza kufikiwa.

Ametoa kauli hiyo hilo leo (Jumanne, Aprili 30, 2019) wakati akizungumza na mamia ya wakazi wa Dodoma waliohudhuria kilele cha maadhimisho ya miaka 10 ya Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) yaliyofanyika kwenye viwanja vya Mwl. Nyerere, jijini Dodoma.

“Ninayo furaha kubwa moyoni mwangu, ninaposhuhudia mfuko huu ukitimiza miaka 10 huku sehemu kubwa ya nchi yetu ikiwa na mawasiliano ya uhakika. Napenda niwakikishie kwamba Serikali itaendelea kupeleka mawasiliano kwenye sehemu zilizobakia hapa nchini ili wananchi wote waweze kunufaika na uwepo wa mawasiliano,” amesema.

Amesema Serikali inatambua mchango wa watoa huduma za mawasiliano katika kufikisha huduma hiyo sehemu mbalimbali, kwani kwa sasa kuna baadhi ya minara imejengwa kwa ushirikiano baina ya kampuni za simu. “Nitoe rai kwa wananchi wahakikisha mnailinda minara ya mawasiliano, na tena mhakikishe popote ilipo inalindwa kwa mguvu zote ili tusirudishe nyuma juhudi za maendeleo,” amesisitiza.

Waziri Mkuu ameipongeza Bodi na menejimenti ya mfuko huo kwa kupeleka vifaa vya TEHAMA katika shule zaidi ya 500 nchini pamoja na kutoa mafunzo ya TEHAMA kwa walimu 800.

Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na hadhira hiyo, Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye alisema mfuko huo umejenga vituo 10 vya TEHAMA huko Zanzibar (Pemba na Unguja) ili viwe ni vituo vya mafunzo ya TEHAMA.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote, Mhandisi Peter Ulanga alisema mpaka sasa takribani asilimia 94 ya Watanzania wanapata huduma za mawasiliano mijini na vijijini.

“Kama unavyotambua kwa ukubwa wa nchi yetu, bado kuna maeneo yenye changamoto za mawasiliano. Mfuko umekwishaainisha jumla ya kata 234 ambazo zabuni yake inatarajiwa kutangazwa Mei 2019,” amesema.

Alisema Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote pamoja na kupeleka huduma za mawasiliano vijijini umeweza kuanzisha matumizi ya TEHAMA katika shule za msingi na sekondari nchini ikiwa ni utekelezaji wa majukumu yake kama yalivyoainishwa katika sheria iliyoanzisha mfuko huo.

“Katika kipindi cha miaka 10, Mfuko umeweza kupeleka vifaa vya TEHAMA katika shule za Serikali. Kupitia mradi wake wa kuunganisha shule na mtandao wa Internet, mfuko huo umepeleka vifaa hivyo kwenye shule za serikali 503, ambapo kila shule ilipata kompyuta tano. Aidha, printa zaidi ya 150 zimeweza kutolewa katika shule za umma za msingi na sekondari, alisema Mhandisi Ulanga.
         
Alisema kupitia mradi wa kuunganisha shule za umma na mtandao wa internet, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano na kampuni ya Satelaiti ya Avanti Communications, imeweza kuunganisha shule 301 na mtandao wa internet.

Aidha, Mhandisi Ulanga alisema Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote kwa kushirikiana na TAMISEMI na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia umeweza kutoa mafunzo ya TEHAMA kwa walimu 583 katika mwaka wa fedha 2017/2018 wa shule za umma kwa ajili ya kuufanya mradi wa kupeleka vifaa vya tehama uwe endelevu.

“Lengo hasa la mafunzo haya ni kutoa elimu ya kutatua matatizo ya awali katika vifaa mbalimbali vya TEHAMA, ili kupunguza gharama za uendeshaji kwa vifaa vinavyopelekwa shuleni na kuboresha namna ya kuandaa na kufundisha masomo mbalimbali. Mwaka huu wa fedha 2018/2019 tumetoa mafunzo kwa idadi hiyo hiyo ya walimu,” alisema.

Alitumia fursa hiyo kuwashukuru TAMISEMI, Wizara ya Elimu, Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam (DIT) na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kwa kufanikisha mafunzo hayo.

(mwisho) 


Read More

WAZIRI MKUU AHIMIZA WAKAZI DODOMA WACHANGIE DAMU



*Asisitiza wanaume wapime VVU ili wajue hadhi zao, wasitegemee wake zao

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka wakazi wa Dodoma wajitokeze kwa wingi kuchangia damu ili iweze kutumika kuokoa maisha ya wengine.

Ametoa kauli hiyo hilo leo (Jumanne, Aprili 30, 2019) wakati akizungumza na mamia ya wakazi wa Dodoma waliohudhuria kilele cha maadhimisho ya miaka 10 ya Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) yaliyofanyika kwenye viwanja vya Mwl. Nyerere, jijini Dodoma.

Amesema Serikali inaendelea na kampeni ya kuhakikisha vituo vya afya na hospitali vinakuwa na akiba ya kutosha ya damu kwa ajili ya wagonjwa wenye kuhitaji damu.

“Tunawasihi Watanzania waende kuchangia damu ili benki ya damu iwe na akiba ya kutosha endapo mtu ataenda pale kufanyiwa upasuaji na akapoteza damu nyingi, au awe amepata ajali au ameenda kujifungua, apate damu kwa haraka kutoka kwenye benki yetu,” amesisitiza.

Akitumia wingi wa watu kwenye hafla hiyo, Waziri Mkuu amesema: “Leo hii hapa Dodoma kuna hospitali kubwa ya Benjamin Mkapa kule UDOM, tuna vituo vya afya kama kile cha Makole vyote vinahitaji kutoa huduma hii lakini haitoshi. Tuliagiza kila penye mkusanyiko wa watu wengi, lazima kujengwe banda la kupima afya na kuchangia damu.”

Akizungumziai kuhusu upimaji wa virusi vya UKIMWI (VVU), Waziri Mkuu amesema kampeni inafanyika lakini kasoro iliyopo ni kwamba wanaojitokeza kwa wingi kupima afya zao ni wanawake na wanaume hawapimi. “Takwimu zilizopo zinaonyesha hivyo,” amesema.

“Mimi ndiye balozi wenu akinababa kwenye kampebi ya kitaita ya upimaji VVU. Nataka niwahimize twende leo tukapime, tusitegemee matokeo ya vipimo vya mke. Wengi mnasubiri matokeo ya mke, akisharudi kutoka kupima na kusema niko safi, basi na wewe unaanza kufurahi unasema niko safi, hapana!”

“Wanaume msijidanganye, nenda ukapime wewe mwenyewe ujijue afya yako na mkeo naye apime ajijue ili nyumba nzima iwe na uhakika kwamba mko salama. Kwa hiyo wanaume tukitoka hapa, twende tukapime,” alisema.

Mapema, Mkuu wa Kitengo cha Damu Salama Mkoa wa Dodoma, Dk. Leah Kitundya alimweleza Waziri Mkuu kwamba Hospitali ya Mkoa wa Dodoma ina upungufu wa damu kwa sababu kuna matukio mengi yanayosababisha upungufu wa damu,

“Tukisema kuwa tunakusanya chupa za kutosha, tunahitaji tuwe na chupa 1,000 hadi 1,500 za damu lakini katika hali ya kawaida huwa tunakusanya chupa za damu 850 hadi 950 tu,” alisema.

(mwisho) 
Read More

KILELE CHA MAADHIMISHP YA MIAKA(10) YA MFUKO WA MAWASILIANO KWA WOTE (UCSAF)


Waziri  Mkuu Kassim Majaliwa, akisalimiana na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye, katika kilele cha maadhimisho ya miaka (10) ya mfuko wa mawasiliano kwa wote (UCSAF) , kwenye viwanja vya Nyerere Square, jijini Dodoma Aprili 30, 2019.
Waziri  Mkuu Kassim Majaliwa, Meneja wa Kanda wa TCRA, Anthonio Manyanda, wakati akikagua mabanda, kwenye kilele cha maadhimisho ya miaka (10) ya mfuko wa mawasiliano kwa wote (UCSAF) , yaliyofanyika katika viwanja vya Nyerere Square, jijini Dodoma Aprili 30, 2019.
Waziri  Mkuu Kassim Majaliwa, akiteta jambo na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye, katika kilele cha maadhimisho ya miaka (10) ya mfuko wa mawasiliano kwa wote (UCSAF) , yaliyofanyika katika viwanja vya Nyerere Square, jijini Dodoma Aprili 30, 2019.
Waziri  Mkuu Kassim Majaliwa, akihutubia, katika kilele cha maadhimisho ya miaka (10) ya mfuko wa mawasiliano kwa wote (UCSAF) , kwenye viwanja vya Nyerere Square, jijini Dodoma Aprili 30, 2019.

Waziri  Mkuu Kassim Majaliwa, akihutubia, katika kilele cha maadhimisho ya miaka (10) ya mfuko wa mawasiliano kwa wote (UCSAF) , kwenye viwanja vya Nyerere Square, jijini Dodoma Aprili 30, 2019.
 Wajasiriamali wadogo wadogo (Wamachinga) wakimsikiliza Waziri  Mkuu Kassim Majaliwa, wakati akihutubia, katika kilele cha maadhimisho ya miaka (10) ya mfuko wa mawasiliano kwa wote (UCSAF) , yaliyofanyika katika viwanja vya Nyerere Square, jijini Dodoma Aprili 30, 2019.


Read More

WAZIRI MHAGAMA AWAONYA WAAJIRI WOTE KUTONYANYASA WANAWAKE


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Uratibu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe.Jenista mhagama amewataka waajiri wote nchini kutonyanyasa wanawake katika masuala ya kazi ili kuwa na usawa maeneo ya kazi.
Ameitoa kauli hiyo hii leo tarehe 30 Aprili, 2019 alipokuwa akifungua semina ya siku moja ya viongozi wanawake kutoka vyama mbalimbali vya wafanyakazi nchini walipokutana kujadili masuala yanayowahusu wawapo kazini ikiwemo; haki na wajibu wao wawapo kazini iliyofanyika katika Ukumbi wa mikutano wa Paradise Inn Jijini Mbeya.
Waziri alieleza kuwa waajiri hawana budi kubadili mitazamo hasi iliyopo katika jamii ya kuona wanawake ni viumbe dhaifu na wenye majukumu mengi yanayoweza kukwamishi jitihada zao wawapo kazini badala yake wawaone kuwa ni viungo muhimu katika kuchangia uzalishaji na maendeleo nchini.
“Mchango wa wanawake ni mkubwa endapo utatambuliwa na kuthamini katika nyanja zote za ukuaji wa uchumi, hivyo ni vyema maeneo ya kazi waajiri watimize wajibu wao kwa kundi hili kwa kuzinigatia sheria zilizopo na wasinyanyaswe na waendelee kuheshimiwa na kupewa haki na stahiki zao kama wafanyakazi wengine.”alisisitiza Waziri Mhagama.
Waziri alieleza jitihada za serikali ni kuhakikisha inasimamia vyema sheria na taratibu za kazi nchini kwa kuliangalia kundi hili ili kuwa na waajiriwa wenye kuzingatia usawa wa kijinsia.
“Ninakemea vitendo vya unyanyasaji wa haki za wanawake kazini ikiwemo kukoseshwa haki zao na vyama hivi vya wafanyakazi viendelee kuleta tija katika kukemea matendo hayo,”alisistiza Waziri Mhagama.
Aidha Waziri aliwataka wanawake kuendelea kuvitumia vyama vya wafanyakazi kama jukwaa maalum la kueleza na kutatua changamoto zao.
Aliongezea kuwa, pamoja na changamoto wanazokutana nazo wanawake hawana budi kujiendeleza kielimu ili kuendana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia yaliyopo katika masuala ya kazi.
“Wanawake umefika wakati kuendelea kujiendeleza katika eneo la elimu ili kuwa na vigezo mahususi vitakavyo wapa nafasi nzuri katika maeneo yenu ya kazi.”alisisema Waziri Mhagma.
Naye rais wa Shirikizo la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA) Bw. Tumaini Nyamhokya alimpongeza waziri pamoja na changamoto zilizopo katika kufikia haki sawa kwa wote , alieelza umuhimu wa kuendelea kuliinua kundi hili ili kuwasaidia wanawake wa Kitanzania katika kupata haki na usawa kwenye maeneo yao ya kazi.
“Wanawake wana uwezo mkubwa hivyo tuendelee kujali na kutunza nafasi zao wawapo kazini ili kuwezesha Taifa kuendelea kuwa na maendeleleo,” alisisitiza Nyamhokya.
Kwa upande wake Mwenyekiti Kamati ya Wanawake Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Bi. Rehema Ludanga alieleza kuwa, ni wakati sahihi kuendelea kuchangamkia fursa za maendeleo ikiwemo uanzishwaji wa viwanda vya wanawake vitakavyosaidia kuondokana na hali ya utegemezi na kuchangia katika ongezeko la uzalishaji nchini.
Washiriki wa semina hiyo wakifuatilia hotuba mgeni rasmi, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe.Jenista mhagama (hayupo pichani) wakati wa semina hiyo.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe.Jenista Mhagama pamoja na baadhi ya viongozi wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi wakipokea dua maalumu ya kufungua semina hiyo Jijini Mbeya.
Rais wa Shirikizo la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA) Bw. Tumaini Nyamhokya akisalimia washiriki wa semina hiyo.
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA) Dkt. Yahya Msingwa akieleza jambo wakati wa semina hiyo.

Mwenyekiti Kamati ya Wanawake Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA) Bi. Rehema Ludanga akichangia jambo wakati wa semina hiyo.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe.Jenista mhagama (katikati) pamoja na viongozi wa Vyama vya wafanyakazi nchini, wakifuatilia hoja wakati wa semina maalum kwa wanawake kutoka katika vyama mbalimbali vya wafanyakazi nchini iliyofanyika Aprili 30, 2019 Jijini Mbeya.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe.Jenista mhagama pamoja na baadhi ya washiriki wa semina hiyo wakiimba wimbo wa umoja na mshikamano wakati wa semina hiyo.
Washiriki wa semina hiyo wakiimba wimbo wa kumshukuru mgeni rasmi kwa kujumuika nao katika semina hiyo.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe.Jenista mhagama (katikati walio kaa) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya washiriki wa semina hiyo mara baada ya ufunguzi rasmi Aprili 30, 2019 Mkoani Mbeya.


Read More

Monday, April 29, 2019

WAZIRI MHAGAMA AWAASA WAFANYAKAZI KUTIMIZA WAJIBU WAO.

 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista mhagama amewaasa wafanyakazi nchini kufanya kazi kwa bidii na uzalendo ili kuendelea kutimiza wajibu wao na kujiletea maendeleo nchini.
Ametoa kauli hiyo mapema hii leo Aprili 29, 2019 alipokuwa akihutubia wafanyakazi walioshiriki katika semina maaalum ya wafanyakazi iliyowakutanisha wajumbe kutoka vyama mbali mbali vya wafanyakazi ili kujadili chimbuko la sherehe za wafanyakazi (Mei Mosi) na kujadili masuala ya sheria za kazi katika ukumbi wa Mkapa Jijini Mbeya.
Akizungumza na wajumbe wa semina hiyo, waziri Mhagama aliwaasa wafanyakazi kuendelea kufanya kazi kwa weledi na tija ili kuendelea kuwa na taifa lenye maendeleo kwa kuzingatia mchango wa wafanyakazi nchini.
“Wafanyakazi endeleeni kufanya kazi kwa umoja, weledi huku mkizingatia kanuni, taratibu na sheria zinazowaongoza katika kutekeleza majukumu yenu pasipo kukiuka masuala ya msingi yanayowahusu,”alisema Waziri Mhagama.
Aliongezea kuwa, katika kuhakikisha Taifa linakuwa na maendeleo endelevu ni vyema wafanyakazi wakaendelea kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi kwa kuzingatia mchango mkubwa wa wafanyakazi nchini katika kujiletea maendeleo kwa kuzingatia tija walioyonayo nchini.
“Niwakumbushe kuwa nyie ni wadau muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu na Serikali inawategemea katika kuchangia maendeleo ya nchi hivyo mnapaswa kujali maeneo yenu ya kazi na kuendelea kuvitumia vyama vya wafanyakazi katika kueleza masuala yenu na kutumia vyama vyenu kutatua changamoto zinazowakabili,”alisisitiza Waziri Mhagama

Sambamba na hilo Waziri aliwataka wafanyazkai kuendelea kuzingatia uwajibikaji wenye misingi ya haki na usawa ili kuwa na mazingira salama ya kiutendaji pasipo kuvunja sheria za wafanyakazi ili kuwa na matokeo chanya kama inavyotarajiwa.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa TUICO Taifa Bw. Paulo Sangeze alieleza shukrani zake kwa namna serikali inavyoendelea kuunga mkono uwepo wa Vyama vya wafanyakazi na kuahidi kutoa ushiorikiano kila itakapohitajika.
“Kwa dhati ya moyo wangu na kwa niaba ya TUCTA ninatoa shukrani kwa Serikali kwa namna inavyounga mkono shughuli za vyama vya wafanyakazi na hakika kumekuwa na mabadiliko makbwa tofauti na ilivyokuwa awali,”alisisitiza bw. Sangeze
Sehemu ya wajumbe walioshiriki semina hiyo wakiimba wimbo wa umoja na mshikamano.
Mwenyekiti wa TUICO Taifa Bw. Paulo Sangeze akitoa neno la shukran kwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu) Mhe.Jenista Mhagama (hayupo pichani) wakati wa semina.
Mwenyekiti Kamati ya Wanawake Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Bi. Rehema Ludanga akichangia jambo wakati wa semina hiyo.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu) Mhe.Jenista Mhagama akiimba wimbo wa umoja na mshikamano pamoja na baadhi ya viongozi wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi walipokutana wakati wa Semina kwa wafanyakazi kuhusu masuala ya Sheria za wafanyakazi na chimbuko la Siku ya Wafanyakazi Duniani iliyoandaliwa na TUICO Taifa na kufanyika Aprili 29, 2019 ukumbi wa Mkapa Jijini Mbeya.
Sehemu ya wajumbe walioshiriki semina hiyo wakiimba wimbo wa umoja na mshikamano.
Sehemu ya wajumbe wa semina hiyo wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu) Mhe.Jenista Mhagama (hayupo pichani) wakati wa semina hiyo.

Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA) Bw. Tumaini Nyamhokya akichangiua jambo wakati wa semina hiyo.
Read More

MAANDALIZI YA SHEREHE ZA MEI MOSI YAPAMBA MOTO SOKOINE MBEYA.

NA.MWANDISHI WETU
Waziri wa Nchi Ofisi anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama amekagua maandalizi ya Sherehe za Mei Mosi na kusema ameridhishwa na hatua zilizofikiwa.
Ametoa kauli hiyo Aprili 29, 2019 baada ya kupokea taarifa ya mbalimbali za Kamati ya Maandalizi walipokutana kujadili na kupanga mipango katika kuelekea kilele cha sherehe hizo zinazotarajiwa kuadhimishwa katika Viwanja vya Sokoine Jijini Mbeya.
Waziri amesema Kamati ya Mkoa kwa kushirikiana na Ofizi yake imeendelea na maandalizi hayo na kuendelea kutoa wito kwa wananchi wa Mkoa huo kufika kwa wingi katika viwanja hivyo siku ya tarehe 1 Mei, 2019.
“Hadi sasa maandalzi yamefikia hatua nzuri na watu wanafanya kazi kwa umoja ili kuhakikisha shughuli hii inafana, wito wangu wananchi wajitokeze kwa wingi kuja kuunga mkono wafanyakazi wa Tanzania katika siku yao hii muhimu.”Alisema waziri Mhagama.
Waziri aliwataka wanakamati hao wahakikishe wanasimamia vizuri wageni, pamoja na shughuli zote zitakazofanyika uwanjani hapo ili kuhakikisha wanaifikia siku hiyo kwa ushindi mkubwa.
Aidha Waziri aliongezea kuwa, uwepo wa maadhimisho hayo Jijini Mbeya wanachi wayatumie kama fursa ya kimaendeleo kwa kuwa mkoa utapokea wageni wengi hivyo waendelee kuwahudumia vyema.
Aidha kwa Upande wake rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA) Bw. Tumaini Nyamhokya aliendelea kuhamasisha wananchi hususan wafanyakazi wote kujitokeza kwa wingi kuja kuiadhimisha siku hiyo.
 “Ni wakati sahihi kwa wafanyakazi wote nchini kuitumia siku hii maalum katika kuiadhimisha na kuienzi ikiwa ni sherehe ya upekee sana hivyo mjitokeze kwa wingi pamoja na wananchi wote kwa ujumla.”Alisisitiza Nyamhokya.
Maadhimisho ya Sherehe za Mei Mosi yatahadhimishwa Kitaifa katika Mkoa wa Mbeya ambapo Mgeni Rasmi anatarajiwa kuwa Mhe.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.John Pombe Magufuli, aidha maonesho hayo yatapambwa na shughuli mbalimbali ikiwemo; Maandamano ya wafanyakazi na magari, Kwaya maalum, Nyimbo maalum kutoka kwa Vyama vya Wafanyakazi, wimbo maalum kutoka kwa wasanii wa kizazi kipya, vikundi vya ngoma kutoka mikoa mbalimbali, Nyimbo maalum kutoka Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).
Kauli mbiu ya maonesha ya mwaka huu inasema; “Tanzania ya Uchumi wa Kati Inawezekana, Wakati wa Mishahara na Masilahi Bora kwa Wafanyakazi ni SASA”

=MWISHO=
Read More

Friday, April 19, 2019

MARA WATAKA KAMATI ZA MAAFA NGAZI YA KIJIJI HADI MKOA

Mkuu wa Mkoa wa Mara, Adam Malima akifafanua umuhimu wa Kamati za Usimamizi wa Maafa wakati wa Mafunzo ya Usimamizi wa Maafa mjini Musoma, tarehe 18 Aprili, 2019, Mafunzo hayo yaliratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu wa shughuli za maafa, kushoto kwake ni Mkurugenzi wa Idara hiyo, Kanali Jimmy Matamwe.

Na. OWM, MUSOMA.
Wajumbe wa Kamati ya Usimamizi wa Maafa Mkoani Mara wameiomba ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu wa maafa kuwajengea uwezo wa  kuunda kamati za Usimamizi wa Maafa mkoani humo. Wajumbe hao wamebainisha kuwa wanataka kamati hizo ziundwe kuanzia ngazi ya kijiji hadi ngazi ya mkoa ili mkoa huo uwe na uwezo wa kujiandaa, kuzuia, kukabili na kurejesha hali kama maafa yatatokea.
Kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa maafa Na. 7 ya mwaka 2015, inaainisha  majukumu ya  kamati za usimamizi wa Maafa kuanzia ngazi ya Kijiji hadi mkoa, ambapo kwa mujibu wa sheria hiyo, jukumu la msingi ni kutafuta rasilimali kwa ajili ya usimamizi wa maafa katika ngazi husika, pamoja na  Kuratibu na kusimamia shughuli za usimamizi wa maafa na operesheni za dharura ndani ya Kijiji  wilaya au mkoa. Pia kutoa taarifa za tahadhari ndani ya eneo husika, hivyo kila mkoa hauna budi kuwa na kamati hizi.
Akiongea wakati akifungua mafunzo ya Usimamizi wa Maafa mjini Musoma, tarehe 18 Aprili, 2019, Mkuu wa Mkoa wa Mara, Adam Malima, amesema kuwa yeye na wajumbe wa Kamati ya Usimamizi wa Maafa ya mkoa wameamua kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu Idara ya Uratibu Maafa, ili wawejengee uwezo utakao wawezesha kuanzisha kamati hizo kuanzia ngazi ya Kijiji, ili  Kamati ya Usimamizi wa Maafa ya mkoa ambayo  ilianzishwa rasmi kisheria kwa ajili ya  kumshauri Mkuu wa mkoa masuala ya Usimamizi wa maafa iweze kumshauri kwa weledi na  kwa wakati. 
“Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu Maafa ikishatujengea uwezo sisi jukumu letu ni moja tu, ni kuhakiksha tunajiimarisha juu ya usimamizi wa maafa kuanzia ngazi ya kijiji ili haya majanga ya Upepo mkali, Ukame, Ajali za vyombo vya usafiri wa majini na nchi kavu, moto, Uharibifu wa mazao unaofanywa na tembo, tuwe na uwezo wa kuyazuia au kupunguza madhara yake  pindi yanapotokea  mkoani hapa na hatutapata vifo, uharibu wa mali na ulemavu wa kudumu kwa wananchi” Amesisitiza Malima.
Naye, Mkurugenzi wa Idara ya Uratibu wa Shughuli za Maafa  Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Jimmy Matamwe, amefafanua kuwa ili kamati hizo ziwe na ufanisi katika usimamizi wa shughuli za maafa zinapaswa  kuandaa Mkakati wa Kupunguza madhara  ya maafa pamoja na Mpango wa kujiandaa na kukabili maafa.
“Ofisi ya waziri Mkuu tutaendelea kuendesha mafunzo haya  ili kuzijengea uwezo kamati hizi ambazo ni chombo cha kisheria hapa nchini kwa ajili ya kutathimini na kutekeleza masuala ya kitaalam kuhusu usimamizi wa maafa, kuzuia na kupunguza madhara ya majanga ya aina zote katika mkoa lakini mkishapata mafunzo haya hakikisheni mnaweka masuala y amaafakatika mipango yenu ya maendeleo.”
Mafunzo hayo yaliyoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu wa shughuli za maafa, yamehudhuriwa na wajumbe wote wa Kamati ya Usimamizi wa maafa wa mkoa pamoja  kwa kuzingatia Kifungu cha 13 cha sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 7 ya mwaka 2015,  pamoja na baadhi ya wananchi wa kawaida walioalikwa katika kikao  mafunzo hayo. . 
MWISHO.
Mkurugenzi wa Idara ya Uratibu wa Shughuli za Maafa  Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Jimmy Matamwe akifafanua umuhimuwa Kamati za Usimamizi wa Maafa wakati wa Mafunzo ya Usimamizi wa Maafa mjini Musoma, tarehe 18 Aprili, 2019, Mafunzo hayo yaliratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu wa shughuli za maafa,
Baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Usimamizi wa Maafa Mkoani Mara,  wakifuatilia Mafunzo ya Usimamizi wa Maafa mjini Musoma, tarehe 18 Aprili, 2019, Mafunzo hayo yaliratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu wa shughuli za maafa.

Mratibu wa Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Maafa, Charles Msangi  akifafanua umuhimu wa Kamati za Usimamizi wa Maafa wakati wa Mafunzo ya Usimamizi wa Maafa mjini Musoma, tarehe 18 Aprili, 2019, Mafunzo hayo yaliratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu wa shughuli za maafa.
Baadhi ya wananchi walioalikwa kutoka katika Halmashauri za wilaya mkoani Mara,  wakifuatilia Mafunzo ya Usimamizi wa Maafa mjini Musoma, tarehe 18 Aprili, 2019, Mafunzo hayo yaliratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu wa shughuli za maafa.
Mkuu wa Wilaya ya Butiama ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Usimamizi wa Maafa ya Mkoa wa Mara, Bi. Annarose Nyamubi, akieleza umuhimu wa Kamati za Usimamizi wa Maafa wakati wa Mafunzo ya Usimamizi wa Maafa mjini Musoma, tarehe 18 Aprili, 2019, Mafunzo hayo yaliratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu wa shughuli za maafa.
Wajumbe wa Kamati ya Usimamizi wa Maafa ya Mkoa wa Mara, wakifuatilia  Mafunzo ya Usimamizi wa Maafa,  mjini Musoma, tarehe 18 Aprili, 2019, Mafunzo hayo yaliratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu wa shughuli za maafa.

Read More

Thursday, April 18, 2019

WAZIRI MKUU AITAKA PSSSF IONGEZE MAKUSANYO

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameitaka menejimenti ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) ijizatiti na kuweka mbinu mpya za kuongeza makusanyo.

Ametoa agizo hilo leo jioni (Alhamisi, Aprili 18, 2019) wakati alipokutana na menejimenti ya mfuko huo kwenye kikao kilichofanyika ukumbi wa mikutano wa PSSSF jijini Dodoma. 

Waziri Mkuu ambaye aliamua kutembelea ofisi za mfuko huo ili afahamiane na menejimenti hiyo, amesema amepokea taarifa ya Mkurugenzi Mkuu na kubaini kuwa ukusanyaji wa michango hauridhishi. 

“Mfuko huu ni wa tofauti na wa NSSF kwa sababu umeunganisha mifuko mingine ya GEPF, PSPF, LAPF na PPF. Mifuko yote hii ilikuwa na malengo na majukumu yake ya awali, lakini sasa imeunganishwa kwa hiyo jukumu letu ni moja,” amesema.

“Natambua mna kazi kubwa ya kusajili wanachama wapya lakini pia tunayo kazi ya kuwafikia wanachama wa zamani ambao tumewachukua kutoka mifuko mingine na kuhakikisha kuwa wanaingizwa katika mfuko mpya,” amesisitiza.

“Napenda kusisitiza kuwa jukumu la kukusanya michango ni la muhimu sana. Ni lazima mjue wastani wa makusanyo kwa mwezi ni kiasi gani, na kama zimepungua, ni kwa kiasi gani na pia mtafute ni kwa nini zimepungua,” amesema.

Ameitaka menejimenti hiyo pia ijiridhishe juu ya uhakiki wa mali walizorithi kutoka mifuko mingine na izitambue ziko katika hali gani. “Menejimenti peke yenu hamuwezi kufuatilia mali zote, kwa hiyo wapeni hiyo kazi wajumbe wa Bodi, wagawane maeneo ili waende kuzitathmini hizo mali na kisha nipate hiyo taarifa,” amesema.

Mapema, akiwasilisha taarifa ya utendaji wa mfuko huo kuanzia Agosti Mosi 2018 hadi Machi 31, 2019, Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, Bw. Hosea Kashimba alimweleza Waziri Mkuu kwamba majukumu makuu wa mfuko huo ni kusajili wanachama, kukusanya michango, kuwekeza na kulipa mafao kwa wanachama.

Alisema baada ya kuunganishwa kwa mifuko, uandikishwaji wa wanachama uliendelea ambapo hadi kufikia Machi 2019, jumla ya wanachama wapya 7,575 walikuwa wamesajiliwa.


“Hapo awali mfuko ulikuwa na wanachama 962,871. Kati ya hao, wanachama 279,564 wanatoka sekta binafsi ambao wamehamishiwa NSSF. Hadi kufikia Machi 31, 2019, mfuko ulikuwa na jumla ya wanachama 750,943 ambao ni watumishi wa umma ikijumuisha na wanachama 67,636 waliohamia kutoka NSSF,” alisema.

Kuhusu ukusanyaji wa michango, Bw. Kashimba alisema moja ya jukumu la mfuko ni kukusanya michango na tangu Agosti 2018 hadi Machi 2019, mfuko huo ulikuwa umekusanya jumla ya sh. bilioni 928.31 ikilinganishwa na lengo la lililowekwa la kukusanya sh. trilioni 1.05 sawa na asilimia 88.62.

Kuhusu malipo ya mafao, Bw. Kashimba alisema katika kipindi kilichoishia Machi 31, 2019, mfuko huo umelipa mafao ya jumla ya sh. trilioni 1.65.

Alisema mfuko huo hivi sasa una wafanyakazi 839 ambao kati yao, wanaume ni 470 na wanawake ni 369.

Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Waziri wa Nchi, (OWM – Sera, Uratibu, Bunge na wenye Ulemavu), Bibi Jenista Mhagama.
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, akizungumza na Menejimenti ya PSSSF, katika jengo la ofisi hiyo, jijini Dodoma Aprili 18, 2019. 

Read More

Wednesday, April 17, 2019

MATUKIO BUNGENI LEO TAREHE 17.04.2019

Waziri Mkuu ,Kassim Majaliwa akizungumza na Mbunge wa Mtwara Mjini (CUF), Maftah Nachuma, katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma Aprili 17, 2019.
Waziri Mkuu ,Kassim Majaliwa akizungumza na Naibu Spika wa Bunge la Tanzania, Tulia Ackson (kulia), na Mbunge wa Sumve, Richard Ndasa Bungeni jijini Dodoma Aprili 17, 2019. 
Waziri Mkuu ,Kassim Majaliwa akizungumza na Mbunge wa viti Maalum, Upendo Peneza, Bungeni jijini Dodoma Aprili 17, 2019.
Waziri Mkuu ,Kassim Majaliwa akizungumza na Mbunge wa Wawi (CUF) Ahmed Ngwali, katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma Aprili 17, 2019. Katikati ni Mbunge wa Mafinga Cosato Chumi.
 
Read More