Home
All posts
Sunday, July 16, 2017
Saturday, July 15, 2017
WATANZANIA KUACHANA NA NGUO ZA MITUMBA-MAJALIWA
WATANZANIA KUACHANA NA NGUO ZA MITUMBA-MAJALIWA
| Waziri Mkuu Kassim Majaliwa katikati akionyeshwa Ubora wa Kanga zinazo tengenezwa hapa nchini katika kiwanda cha NIDA wakati alipofanya ziara Jumamosi 15 july 2017 katika kiwanda hicho kilichopo Jijini Dar es salaam,kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa Kiwanda cha NIDA Bwana Muhammadhamza Rafiki na kushoto ni Meneja Mkuu NIDA Bwana Muhammad Waseem. |
Thursday, July 13, 2017
WAZIRI MKUU AUPONGEZA UONGOZI WA NHC KWA UTENDAJ
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameupongeza uongozi wa Shirika la Nyumba (NHC) kwa kukamilisha ujenzi wa zahanati ya kijiji cha Mnolela mkoani Lindi kwa muda mfupi.
Amesema ujenzi wa zahanati hiyo ya kisasa mwezi Machi,
2017 na sasa tayari kimekamilika, jambo ambalo litarahisisha upatikanaji
wa huduma za afya kwa wananchi wa eneo hilo na wa jirani.
Waziri Mkuu alitoa pongezi hizo
jana jioni (Alhamisi, Julai 13, 2017) alipozungumza na wananchi wa kijiji cha
Mnolela baada ya kuzindua zahanati hiyo iliyosimamiwa na NHC.
Alisema ujenzi wa zahanati hiyo ni muendelezo wa mkakati
wa Serikali ya awamu ya tano wa kuboresha huduma za afya kwa kusogeza huduma karibu kwa wananchi wake.
“Rais wetu Dkt.
John Magufuli amedhamiria kuwaondolea wananchi changamoto za mbalimbali
zikiwemo za huduma za afya, hivyo tuendelee kumuunga mkono.”
Kwa upande wake Mkurugenzi wa NHC, Bw. Nehemia Mchechu
alisema mradi wa ujenzi wa zahanati hiyo ulisimamiwa na NHC na umegharimu sh.
milioni 65.5.
“Shilingi milioni 15 zilitolewa na Rais. Dkt. Magufuli,
sh. milioni 10 zilitolewa na Mheshimiwa Mbunge wa jimbo la Mtama, Nape Nnauye,
NHC ilitoa sh. milioni 10 na kiasi kilichosalia ni mchango wa halmashauri.”
Awali Mbunge wa jimbo la Mtama, Mheshimiwa Nape
alimshukuru Rais Dkt. Magufuli kwa mchango mkubwa alioutoa katika mradi wa
ujenzi wa zahanati hiyo.
Mheshimiwa Nape alisema zahanati hiyo ni mkombozi kwa
wakati wa kijiji cha Mnolela na wananchi wengine wanaoishi kwenye maeneo yaliyo
jirani na kijiji hicho.
WAZIRI MKUU ATEMBELEA MRADI WA KUSAFIRISHA UMEME LINDI
* Asema changamoto ya
kukatika umeme Mkoa wa Lindi kuwa historia
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema
changamoto ya kukatika umeme katika mkoa wa Lindi kuwa historia baada ya
kukamilika kwa mradi wa kusafirisha umeme wa kilovolti 132 Mtwara-Lindi.
Amesema
hayo leo (Alhamisi, Julai 13, 2017) alipotembelea mradi huo wa kuzalisha umeme
unaojengwa katika kijiji cha Mahumbika wilayani Lindi.
Waziri Mkuu amesema kukamilika kwa mradi huo uliogharimu sh. bilioni
16 kutamaliza changamoto ya upatikanaji wa umeme katika mkoa wa Lindi.
Amesema mkakati wa Serikali ni kuongeza kiwango cha uzalishaji wa
umeme ili Watanzania wapate umeme mwingi utakaosambazwa hadi vijijini kwa
gharama nafuu.
“Mikoa wa Lindi ulikuwa na shida kubwa ya kukatika kwa umeme,
kukamilika kwa mradi huu ni mkombozi kwetu, tunawakaribisha wawekezaji waje kuwekeza
kwa sababu sasa tunanishati ya uhakika.”
Kwa upande wake Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati
na Madini, Profesa James Mdoe amesema kuimarika kwa upatikanaji wa umeme
kutawezesha safari ya kuelekea kwenye uchumi wa viwanda.
Katika hatua nyingine Waziri Mkuu amesema atahakikisha anapambana
na watu wote watakaokwamisha jitihada za Rais Dkt. John Magufuli za kuwahudumia
wananchi.
Pia ameahidi kusimamia shughuli
za maendeleo ya wananchi wote Tanzania bila ya kujali maeneo wanakotoka wala itikadi
zao za kisiasa na kidini.
Ameyasema hayo wakati akizungumza
kwa nyakati tofauti na wananchi wa kata za Nanganga, Nyangao, Mtama na Nyengedi
alipowasilisi wilayani Lindi, akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani Lindi.
“Tunataka fedha zinazotolewa na Serikali kwa
ajili ya kuwahudumia wananchi zitumike ipasavyo na hatutakubali kuona mtu
napewa fedha na kuzitumia atakavyo.”
Pia Waziri Mkuu amewataka
wananchi hao kuweka pembeni itikadi zao
za kisiasa na badala yake washirikiane kwa pamoja katika kufanya shughuli za
maendeleo kwenye maeneo yao.
“Rais Dkt. Magufuli amesema
Watanzania kwa sasa hatuhitaji kufanya siasa, sasa ni kazi tu, hivyo tutumie
muda wetu mwingi kwa kufanya kazi za maendeleo. Tupunguze muda wa kubishana
hakuna tija watu wanataka maji, afya.”
Awali Mbunge wa jimbo la Mtama
Mheshimiwa Nape Nnauye kwa niaba ya wananchi wa jimbo hilo aliishukuru Serikali
kwa kuboresha huduma mbalimbali kwenye jimbo hilo.
Wednesday, July 12, 2017
MBUNGE WA CHADEMA AWAOMBA WANANCHI WALIOMBEE TAIFA AMANI
MBUNGE viti Maalumu Chadema, Mheshimiwa Upendo Peneza amewaomba wananchi waliombee Taifa liendelee kuwa na amani pamoja na kuwaombea viongozi wa kisiasa wawe na uvumilivu ili wazidi kusonga mbele kimaendeleo.
Aliyasema hayo jana (Jumatano, Julai 12, 2017), katika mkutano wa hadhara uliofanyika uwanja wa shule ya msingi Likangara wilayani Ruangwa wakati wa ziara ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa mkoani Lindi.
“Wananchi wa Ruangwa nawatakia maisha mema ili mzidi kusonga mbele, tuombee amani ya nchi yetu na mtuombee viongozi tuwe na uvumilivu wa kisiasa.”
Mbali na Mheshimiwa Upendo, pia mkutano huo uliudhuriwa na wabunge wengine ambao ni Mheshimiwa Hassan Masala (Nachingwea), Mheshimiwa Zubery Kuchauka (Liwale), Mheshimiwa Hassan Kaunje (Lindi Mjini) na Mheshimiwa Hamida Abdalaah (Viti Maalumu).
Kwa pamoja wabunge hao walisema lengo la kushiriki kwenye ziara hiyo ni kuunga mkono jitihada zinazofanywa na Serikali ya awamu ya Tano katika kuwaletea wananchi maendeleo.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Bw. Godfrey Zambi aliwataka wananchi wa mkoa huo kuhakikisha wanaendelea kudumisha na kuilinda amani iliyoko kwa sababu ndiyo inayowawezesha kufanya shughuli zao za kimaendeleo.
Alisema licha ya kuwepo kwa matukio machache ya uhalifu yanayojitokeza katika baadhi ya maeneo vyombo vya ulinzi na usalama kwa kushirikiana na mikoa jirani limejizatiti kukabiliana na wahalifu wa aina yoyote kwa mtu mmoja mmoja au vikundi.
WAZIRI MKUU KASSIM MAJALIWA AKIWA RUANGWA
| Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza na wananchi wakati alipo tembelea hospitali ya Wilaya Ruangwa, akiwa kwenye ziara ya kikazi ya siku nne Mkoani Lindi, Julai 12, 2017. |
| Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akikata utepe wakati alipo kabidhi gari mbili za kisasa za kubebea wagonjwa,katika hospitali ya Wilaya Ruangwa, akiwa kwenye ziara ya kikazi ya siku nne Mkoani Lindi, Julai 12, 2017. |
WAZIRI MKUU AKIWA MKOANI LINDI
WAZIRI MKUU AKABIDHI ‘AMBULANCE’ MBILI RUANGWA
WAZIRI MKUU
Kassim Majaliwa amefanya ziara katika hospitali ya wilaya ya Ruangwa na amekabidhi
magari mawili ya kubebea wagonjwa.
Amesema kati
ya magari hayo moja ni kwa ajili ya hospitali hiyo ya wilaya na la pili litapelekwa
katika kituo cha afya cha Mandawa.
Waziri
Mkuu amekabidhi magari hayo leo (Jumatano, Julai 12, 2017), alipotembelea
hospitali hiyo, ikiwa ni siku ya tatu ya ziara yake ya kikazi Mkoani Lindi.
Amesema magari hayo ni muendelezo wa mkakati wa Serikali
ya awamu ya tano wa kuboresha huduma za afya kwa wananchi wake.
“Rais wetu Dkt.
John Magufuli amedhamiria kuwaondolea wananchi kero mbalimbali zinazowakabili zikiwemo
za huduma za afya, hivyo tuendelee kumuunga mkono.”
Waziri Mkuu amesema magari hayo ya kisasa yatasaidia kurahisisha
usafiri kwa wagonjwa wanaohitaji
matibabu ya dharura katika hospitali kubwa.
Kabla ya kukabidhi magari hayo, Waziri Mkuu
alitembelea wodi ya akina mama na ya watoto waliolazwa katika hospitali hiyo na
amesema kwamba ameridhishwa na hali ya utoaji huduma.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya
ya Ruangwa, Mheshimiwa Rashid Nakumbya amesema magari hayo ni faraja kwao kwa
kuwa walikuwa na changamoto ya usafiri kwa wagonjwa wa dharura.
“Tunatambua
na kuthamini jitihada kubwa zinazofanywa na Serikali ya awamu ya tano katika
halmashauri yetu na Taifa kwa ujumla, nasi tutayatumia magari haya kama
ilivyokusudiwa.”
Awali, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya
Wilaya ya Ruangwa, Dkt. Regan Rajuu amesema hali ya upatikanaji wa dawa na
vifaa tiba katika hospitali hiyo umeongezeka kutoka asilimia 80 Desemba, 2016
na kufikia asilimia 90 Juni 2017.
Pia Waziri Mkuu
alitembelea shule ya Sekondari ya Kassim Majaliwa iliyoanza kujengwa Desemba,
23, 2016 kwa michango ya Halmashauri, fedha za mfuko wa jimbo pamoja na wadau
mbalimbali wa maendeleo.
Kaimu Mkuu wa
shule hiyo, Mwalimu Emmanuel Sechawe alisema msingi wa kuanzisha shule hiyo
ulitokana na uwepo wa wanafunzi 319 waliofaulu darasa la saba mwaka 2016 kukosa
nafasi ya kujiunga na kidato cha kwanza katika shule zilizopo.
Mbali na
kutembelea shule hiyo, pia Waziri Mkuu alifanya ukaguzi wa maendeleo ya mradi
wa ujenzi wa gereza la wilaya ya Ruangwa, ambalo litakapokamilika litapunguza
msongamano wa wafungwa na mahabusu katika gereza la wilaya ya Nachingwea.
MAJALIWA: HAKUNA KIJIJI TANZANIA KITAKACHOACHWA BILA YA UMEME
*Asema vilivyo mbali na gridi kufungwa
sola
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema hakuna kijiji nchini
kitakachoachwa bila ya kuunganishiwa umeme katika awamu ya tatu ya Mradi wa Nishati
Vijijini (REA).
Amesema Serikali imetenga shilingi trilioni moja kwa
ajili ya kusambaza umeme katika vijiji 8,000 ambavyo bado havijaunganishiwa
nishati hiyo.
Waziri Mkuu alitoa kauli hiyo jana jioni (Jumanne, Julai
11, 2017) alipozungumza kwa nyakati tofauti na wananchi wa wilaya ya Ruangwa.
Waziri Mkuu ambaye ameambatana na mkewe Mama Mary
Majaliwa aliyasema hayo katika mikutano aliyoifanya kwenye vijiji vya Chiapi, Nandanga,
Mbecha na Luchelegwa, ikiwa ni siku ya pili ya ziara yake ya kikazi ya siku nne
Mkoani Lindi.
“Rais wetu Dkt. John Magufuli anajali sana wananchi wake,
hivyo ametenga fedha nyingi zitakazotosheleza kusambaza umeme katika vijiji
vyote vikiwemo na wilaya ya Ruangwa. Gharama za kuunganishiwa umeme huo ni sh.
27,000 tu.”
Pia Waziri Mkuu amesema
mwananchi hawatowajibika tena katika kulipia nguzo wala fomu za maombi
ya kuunganishiwa umeme, kwa sababu tayari gharama hizo zimeshabebwa na Serikali.
Waziri Mkuu
aliongeza kwamba lengo la Serikali ni
kufikisha umeme kwenye vijiji vyote Tanzania na kwa vile ambavyo viko kwenye
maeneo yaliyo mbali na gridi vitafungiwa sola, jambo ambalo litafungua fursa za
ajira na kukuza uchumi.
Waziri Mkuu alisema huduma hiyo ni muhimu kwani mbali ya kutumiwa
majumbani lakini pia kwa kusogezwa karibu na maeneo ya pembezoni
itawezesha zahanati,shule ,viwanda na vituo vya afya kuwa na umeme.
Kwa upande wake Meneja wa Tanesco Mkoa wa Lindi Mhandisi,
Johnson Mwigune alimuhakikishia Waziri
Mkuu kwamba hadi kufikia mwishoni mwa mwezi huu mkandarasi aliyepangiwa katika
vijiji hivyo atakuwa tayari ameanza kazi ya kusambaza umeme.
Tuesday, July 11, 2017
WAZIRI MKUU ATEMBELEA UJENZI WA DARAJA MTO LUKULEDI
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ametembelea mradi
wa ujenzi wa daraja la mto Lukuledi lenye urefu wa kilomita 30.45 linalounganisha
mikoa ya Lindi na Mtwara na na kusema kwamba
ameridhishwa na maendeleo ya ujenzi wake.
Amesema ujenzi wa daraja hilo unatakaogharimu
sh. bilioni 5.4 ni mkombozi kwa wananchi wa mikoa hiyo hasa wa wilaya za
Ruangwa na Masasi ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakishirikiana katika masuala mbalimbali yakiwemo kilimo na
huduma za kijamii.
Waziri Mkuu amesema hayo leo (Jumanne, Julai
11, 2017) alipotembelea mradi huo wa ujenzi wa daraja hilo katika kijiji cha
Nandanga alipowasili wilayani Ruangwa akiwa katika siku ya pili ya ziara yake
ya kikazi ya siku nne Mkoani Lindi.
“Watu wengi wamepoteza maisha kwa kuliwa na
mamba walipokuwa wakikatiza katika eneo hilo. Ujenzi wa daraja hili ni muhimu, watu
wengi wa Ruangwa wanavuka kufuata matibabu katika hospitali ya Ndanda, wilayani
Masasi na wakazi wa Ndanda wanavuka kufanya shughuli za kilimo wilayani
Ruangwa.”
Pia Waziri Mkuu amewaomba wananchi wa maeneo
hayo kuhakikisha wanatoa ushirikiano kwa mkandarasi anayejenga daraja hilo ili
aweze kutekeleza majukumu yake ipasavyo na kumaliza mradi huo kwa wakati.
Kwa
upande wake Mbunge wa jimbo la Ndanda, Mheshimiwa Cecil Mwambe ameipongeza na
kuishukuru Serikali kwa jitihada zake za kuwaletea wananchi maendele0 na
kubadilisha maisha yao.
Amesema mradi wa ujenzi wa daraja hilo ni faraja
kwa wananchi wa mikoa hiyo kwa kuwa eneo hilo ni makazi ya mamba, hivyo
kukamilika kwake kutaokoa maisha ya watu pamoja na kurahisisha usafiri wa watu
na bidhaa.
Katika
hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema changamoto ya upatikanaji wa huduma ya maji safi
na salama katika vijiji vya Litama, Luchelegwa, Nandanga, Ipingo na Chiapi kuwa
historia baada kuungwanishwa na mradi wa maji wa Mbwinji.
Ameyasema hayo leo wakati akizungumza kwa
nyakati tofauti na wananchi wa vijiji vya Litama, Chiapi, Nandanga, Luchelegwa
alipowasili wilayani Ruangwa akiwa katika siku ya pili ya ziara yake ya kikazi
ya siku nne Mkoani Lindi.
Waziri Mkuu amesema Serikali inatekeleza Kampeni yake ya kumtua mama ndoo, hivyo itahakikisha wananchi
katika maeneo yote nchini, hususan ni ya vijijini wanapata huduma ya maji safi
na salama katika umbali usiozidi mita 400.
Ameitoa kauli hiyo baada ya wananchi wa
vijiji hivyo kumueleza changamoto mbalimbali zinazowakabili kwenye maeneo yao
zikiwemo za maji, barabara, umeme, ambapo aliwahakikishia kwamba Serikali
imeshaanza kuboresha huduma hizo.
Wakati huo huo, Waziri Mkuu amezindua
Zahanati ya Nandanga ambayo imejengwa
kwa fedha kutoka mfuko wa jimbo umegaharimu kiasi cha sh. milioni 73.47 na
kuwahakikishia kwamba Serikali itawapelekea wataalam wa kutosha ili kuwahudumia.
HABARI PICHA : WAZIRI MKUU AKIWA KIJIJI CHA LIKWACHU MKOANI LINDI
| Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akisalimiana na Wananchi wa kijiji cha Likwachu, Wilaya ya Ruangwa, akiwa katika ziara ya kikazi ya siku tano Mkoani Lindi, Julai 11, 2017. |
| Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza na Wananchi wa kijiji cha Likwachu, Wilaya ya Ruangwa, akiwa katika ziara ya kikazi ya siku tano Mkoani Lindi, Julai 11, 2017. |
| Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza na Wananchi wa kijiji cha Likwachu, Wilaya ya Ruangwa, akiwa katika ziara ya kikazi ya siku tano Mkoani Lindi, Julai 11, 2017. |
| Wananchi wa kijiji cha Likwachu, Wilaya ya Ruangwa, wakimsikiliza Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alipo ongea nao, wakati akiwa kwenye ziara ya kikazi ya siku tano Mkoani Lindi, Julai 11, 2017. |
Monday, July 10, 2017
HAKUNA MGONJWA ATAKAYEKOSA DAWA-MAJALIWA
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali imetenga fedha nyingi kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba na kwamba hakuna mgonjwa atakayekwenda kutibiwa katika hospitali, vituo vya afya au zahanati bila ya kupatiwa dawa.
Ameyasema hayo jana jioni (Jumatatu, Julai 10, 2017), wakati akizungumza na wananchi wa wilaya ya Liwale katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa Michezo wa Wilaya.
Waziri Mkuu ambaye ameambatana na mkewe Mama Mary Majaliwa katika ziara yake ya kikazi ya siku nne Mkoani Lindi, alisema Serikali haitaki kusikia wananchi wanakwenda hospitali, Vituo vya afya au zahanati na kukosa dawa.
Alisema moja kati ya ajenda muhimu ya Serikali ya awamu ya Tano ni kuboresha huduma za afya kwa wananchi wake, ambapo kila mwezi halmashauri zote nchini zinapelekewa fedha za ununuzi wa dawa.
“Serikali hii ya Rais Dkt. John Magufuli inatoa fedha za kununulia dawa kila mwezi katika halmashauri zote nchini. Sasa kama hapa Liwale kuna malalamiko ya wananchi kukosa dawa katika hospitali yetu, Mkuu wa Wilaya kafuatilie huko Halmashauri ili kujua wanapeleka wapi fedha za dawa.”
Katika bajeti ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ya mwaka wa fedha 2017/2018 jumla ya shilingi bilioni 236 zimetengwa kwenye ununuzi wa dawa, vifaa, vifaa tiba na vitendanishi.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Bw. Godfrey Zambi alisema hali ya upatikanaji wa dawa muhimu kwa kipindi cha mwaka 2016/2017 iliongezeka kwa asilimia 50 ikilinganishwa na ile ya mwaka 2015/2016.
Bw. Zambi alisema katika kipindi cha kuanzia Julai mwaka 2016 hadi Februari 2017 mkoa wa Lindi ulipokea sh milioni 538 kwa ajili ya ununuzi wa dawa kupitia Bohari ya Dawa (MSD).
“Hospitali ya mkoa ilipokea sh. milioni 195,328,186 kwa ajili ya ununuzi wa dawa na pia ilitumia sh. Milioni 127,171,700 toka fedha za uchangiaji kwa ununuzi wa dawa.”
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu aliwaagiza watendaji wa Halmashauri kwenda vijijini na kuwaelimisha wananchi umuhimu wa utunzaji wa mazingira ili kuliepusha Taifa kugeuka jangwa.
Pia amewaagiza Maofisa Kilimo wote kuhakikisha wanaacha kushinda maofisini na badala yake waende mashambani kwa ajili ya kuwaelimisha wakulima namna bora ya kulima kwa kufuata njia za kisasa ili kupata tija.
Kila ofisa kilimo awe na shamba lake ambalo litatumika kama darasa kwa wananchi
WALIOKULA FEDHA ZA USHIRIKA WATAZILIPA-MAJALIWA
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali haitahusika na ulipaji wa deni la fedha za Ushirika na badala yake kila aliyekula fedha hizo atazilipa mwenyewe.
Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumatatu, Julai 10, 2017), wakati akizungumza na wananchi wa wilaya ya Liwale katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa michezo wa wilaya.
Waziri Mkuu ambaye yuko katika na ziara ya kikazi ya siku nne Mkoani Lindi, amesema Serikali haiwezi kukubali Ushirika ukafa nchini kwa ajili ya watu wachache wasiokuwa waaminifu.
Amesema watu wote waliopewa dhamana ya kuongoza Vyama vya Ushirika na kuamua kujinufaisha kwa kula fedha za vyama watazilipa.
Waziri Mkuu amewaagiza Viongozi wa Mkoa wa Lindi kufanya ukaguzi katika Vyama vyote vya Ushirika vya Msingi (AMCOS) ili kubaini ni wakulima wangapi wanadai.
Amesema baada ya kufanya uchunguzi na kubaini idadi ya wakulima wanaodai na kiasi cha fedha wawachukulie hatua wahusika wote kwa mujibu wa sheria.
Awali, Waziri Mkuu alizungumza na Watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Liwale katika Ukumbi wa Tengeneza, ambapo amewataka Watumishi wa Umma Nchini kutojihusisha na vitendo vya rushwa katika utoaji wa huduma kwa Wananchi.
Amesema Watumishi wanawajibu wa kuwahudumia Wananchi bila ya kutengeneza mazingira ya kuomba rushwa na atakayebainika atachukuliwa hatua kali za kisheria.
Amesema Watumishi wa Umma wanatakiwa kufanya kazi kwa weledi na kwa kuzingatia maadili ya kiutumishi jambo litakaloondoa malalamiko kutoka kwa Wananchi.
“Lazima Wananchi waone na wanufaike na kazi inayofanywa na Serikali yao, hivyo ni wajibu wa Watumishi kuwatumikia Wananchi popote walipo na si kukaa maofisini.”
Pia amewataka Watumishi hao kupanga mipango itakayoleta tija kwa Wananchi na si vinginevyo.
UFUTA KUUZWA KWA MFUMO WA STAKABADHI GHALANI-MAJALIWA
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali imemuagiza Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Dkt. Charles Tizeba akutane na Bodi ya mazao mchanganyiko kwa ajili ya kuliondoa zao la ufuta na kuliingiza katika mfumo wa stakabadhi ghalani.
Pia amewaagiza wakuu wa mikoa yote inayolima zao la ufuta kukutana na Dkt. Tizeba kwa ajili ya kupanga mfumo mzuri wa uuzaji katika msimu wa mwaka 2016/2017 wakati Serikali ikijipanga kuliingiza zao hilo katika mfumo wa stakabadhi ghalani.
Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Jumatatu, Julai 10, 2017) wakati akisalimiana na wananchi katika vijiji vya Nangano, Kibutuka na Kiangara alipowasili katika wilaya ya Liwale kwa ajili ya ziara ya kikazi ya siku nne mkoani Lindi.
Ametoa kauli hiyo baada ya mbunge wa jimbo la Liwale, Mheshimiwa Kuchauka pamoja na wananchi kuiomba Serikali iwasaidie kuboresha bei ya zao la ufuta ambayo imekuwa ikiyumba.
Waziri Mkuu amesema “tatizo lipo kwenye mfumo wa uuzaji zao la ufuta, unauzwa kwa bei ya rejareja, wanunuzi wako huru. Serikali imemuagiza Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi kuliondoa zao katika bodi ya mazao mchanganyiko na kuliingiza katika mfumo wa stakabadhi ghalani ili kuboresha bei yake.”
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amemwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Liwale Bw. Justine Monko kuhakikisha anamaliza tatizo la maji katika vijiji vya Nangano,Kibutuka na Kiangara.
Amesema Serikali imedhamiria kuondoa tatizo la maji kwa kuhakikisha kuwa wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama katika umbali usiozidi mita 400. “Ndio maana Serikali imekuja na Kampeni inayosema mtue mama ndoo kichwani.”
Pia amemtaka Mhandisi wa Maji Bw. Andrew Kilembe kuandika barua ya kufuatilia fedha za maji sh. milioni 76 kwa ajili ya kijiji cha Kiangara walizopangiwa katika bajeti ya mwaka 2016/2017 kwa Waziri wa Maji ili waweze kukamilisha uchimbaji wa kisima.
WAZIRI MKUU AWASILI MKOANI LINDI KWA ZIARA YA KIKAZI
Sunday, July 9, 2017
MAADHIMISHO YA MIAKA 60 YA AGAKHAN
| Waziri Mkuu,Kassim Majaliwa akisalimiana na mama Zakia Megji wakati wa maadhimisho ya miaka 60 tangu Mtukufu Agakhan alipo chaguliwa kuwa Imamu mkuu wa madhehebu ya Shia Ismailia duniani, akiwa amemuwakilisha Rais Dkt. John Magufuli, (kushoto) ni Rais wa Jumuiya ya Shia Ismailia Amin Lakhani Julai 9, 2017. |
| Waziri Mkuu,Kassim Majaliwa akipokea maandano ya maadhimisho ya miaka 60 tangu Mtukufu Agakhan alipo chaguliwa kuwa Imamu mkuu wa madhehebu ya Shia Ismailia duniani yaliyofanyika katika viwanja vya Diamond Jubilee, Waziri Mkuu amemuwakilisha Rais Dkt. John Magufuli katika sherehe hiyo, Julai 9, 2017. |
WAZIRI MKUU AWAHAKIKISHIA WAWEKEZAJI MAFANIKIO
*Asema nchi ina utulivu wa kisiasa na uchumi
unaokuwa kwa kasi
WAZIRI
MKUU Kassim Majaliwa amewahakikishia uwekezaji wenye tija wawekezaji
watakaokuja nchini kwa kuwa Tanzania ni nchi yenye amani, utulivu wa kisiasa na
uchumi wenye kukua kwa kasi.
Ameyasema
hayo leo (Jumapili, Julai 09, 2017) alipomuwakilisha
Rais Dkt. John Magufuli katika maadhimisho ya miaka 60 tangu Mtukufu Aga Khan
alipochaguliwa kuwa Imamu Mkuu wa madhehebu ya Shia Ismailia duniani.
Waziri
Mkuu amesema Serikali inatambua na kuthamini shughuli
mbalimbali zinazofanywa na mtandao wa taasisi za Aga Khan zilizopo hapa nchini,
hivyo Serikali itaendelea kushirikiana nao.
Ameupongeza mtandao wa taasisi za Aga Khan kwa kumuunga mkono
Rais Dkt. Magufuli katika kutoa kipaumbele cha kuwapa fursa watu wenye kipato cha chini kushiriki katika uzalishaji ili
waweze kujikwamua kiuchumi.
“Nawahakikishia
kwamba uwekezaji wenu hapa nchini utakuwa na baraka kwa sababu nchi imetulia kisiasa na uchumi
wake unakua kwa kasi. Nawaomba muendelee kuwaalika wanajumuia wa madhehebu ya Shia
Ismailia popote walipo duniani waje kuwekeza nchini fursa bado zipo.”
Kwa
upande wake Rais wa Jumuiya ya Madhehebu ya Shia
Ismailia Tanzania, Bw. Amin Lakhani ameishukuru Serikali kwa ushirikiano
inaowapa na kwamba ameahidi kuendelea kushirikiana nayo katika kuboresha sekta
mbalimbali nchini.
Amesema
mtandao wa maendeleo wa Aga Khan unatoa huduma mbalimbali zikiwemo za afya,
elimu, kilimo na kunaendesha miradi katika mabara ya Afrika na Asia kwa kuwapa
fursa watu wenye kipato cha chini kushiriki katika uzalishaji ili kujikwamua
kiuchumi.
Awali, Mkuu wa wilaya ya Ilala, Bi. Sophia Mjema aliipongeza
taasisi hiyo kwa mpango wake wa upanuzi
wa hospitali na kuongeza vituo 35 vya afya kutoka 15 walivyonavyo.
Subscribe to:
Posts (Atom)
MITANDAO YA KIJAMII
Popular Posts
-
Na. OWM, Dodoma. Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu, imefanya ukaguzi wa utekelezaji wa sheria Na.5 y...
-
Wataalamu wa Afya moja wakiwa katikapicha ya pamoja wakati wa mkutano wa wataalamu wa Afya moja uliojikita katika ulinzi na usalama...
-
Na. OWM, ARUSHA Wataalam wa sheria kutoka katika sekta ya Afya ya binadamu, Afya ya wanyamapori na mifugo pamoja na mazingira wameshauri...
-
Washiriki wa Mkutano wa mwaka wa Wataalamu wa Maabara wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa mkutano wa mwaka kwa wataalam wa maabara w...
-
TAMOBA wafanya wasilisho la mfumo maalum wa kielektroniki wa ulinzi na usalama wa Bodaboda na BajajiKampuni ya Tanzania Motorcycle and Bajaj Association (TAMOBA) imefanya wasilisho maaluum kwa Ofisi ya Waziri Mkuu kuhusu mfumo maalum wa ...
-
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, ajira na Watu wenye Ulemavu), Mhe. Jenista Mhagama, ambaye ndiye anayesimamia Kamati ina...
-
*Aagiza fedha zilizotengwa zikatumike katika kujengea hospitali Dodoma Rais Dkt. John Pombe Magufuli ameahirisha maadhimisho ya sik...
-
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji) Mhe. Angellah Kairuki akipokea maelezo ya namna mashine zinavyochakata mifuko chakavu na ...
-
Katika kuhakikisha malengo ya kutatua masuala ya ajira na kazi, yanafikiwa na Serikali ya Awamu ya Sita inayongozwa na Mhe. Samia Suluhu H...
-
Katibu wa Kikosi kazi cha Kitaifa cha kuratibu Mpango wa Serikali kuhamia Dodoma Bw.Meshach Bandawe akiuliza jambo kwa Kaimu Meneja wa Uwa...
Formulir Kontak
Contributors
Powered by Blogger.






