Wednesday, July 12, 2017

WAZIRI MKUU AKABIDHI ‘AMBULANCE’ MBILI RUANGWA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amefanya ziara katika hospitali ya wilaya ya Ruangwa na amekabidhi magari mawili ya kubebea wagonjwa.

Amesema kati ya magari hayo moja ni kwa ajili ya hospitali hiyo ya wilaya na la pili litapelekwa katika kituo cha afya cha Mandawa.

Waziri Mkuu amekabidhi magari hayo leo (Jumatano, Julai 12, 2017), alipotembelea hospitali hiyo, ikiwa ni siku ya tatu ya ziara yake ya kikazi Mkoani Lindi.

Amesema magari hayo ni muendelezo wa mkakati wa Serikali ya awamu ya tano wa kuboresha huduma za afya kwa wananchi wake.

 “Rais wetu Dkt. John Magufuli amedhamiria kuwaondolea wananchi kero mbalimbali zinazowakabili zikiwemo za huduma za afya, hivyo tuendelee kumuunga mkono.”

Waziri Mkuu amesema magari hayo ya kisasa yatasaidia kurahisisha usafiri kwa  wagonjwa wanaohitaji matibabu ya dharura katika hospitali kubwa.

 Kabla ya kukabidhi magari hayo, Waziri Mkuu alitembelea wodi ya  akina  mama na ya  watoto waliolazwa katika hospitali hiyo na amesema kwamba ameridhishwa na hali ya utoaji huduma.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Ruangwa, Mheshimiwa Rashid Nakumbya amesema magari hayo ni faraja kwao kwa kuwa walikuwa na changamoto ya usafiri kwa wagonjwa wa dharura.

“Tunatambua na kuthamini jitihada kubwa zinazofanywa na Serikali ya awamu ya tano katika halmashauri yetu na Taifa kwa ujumla, nasi tutayatumia magari haya kama ilivyokusudiwa.”

Awali, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya ya Ruangwa, Dkt. Regan Rajuu amesema hali ya upatikanaji wa dawa na vifaa tiba katika hospitali hiyo umeongezeka kutoka asilimia 80 Desemba, 2016 na kufikia asilimia 90 Juni 2017.

Pia Waziri Mkuu alitembelea shule ya Sekondari ya Kassim Majaliwa iliyoanza kujengwa Desemba, 23, 2016 kwa michango ya Halmashauri, fedha za mfuko wa jimbo pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo.

Kaimu Mkuu wa shule hiyo, Mwalimu Emmanuel Sechawe alisema msingi wa kuanzisha shule hiyo ulitokana na uwepo wa wanafunzi 319 waliofaulu darasa la saba mwaka 2016 kukosa nafasi ya kujiunga na kidato cha kwanza katika shule zilizopo.

Mbali na kutembelea shule hiyo, pia Waziri Mkuu alifanya ukaguzi wa maendeleo ya mradi wa ujenzi wa gereza la wilaya ya Ruangwa, ambalo litakapokamilika litapunguza msongamano wa wafungwa na mahabusu katika gereza la wilaya ya Nachingwea.



EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.