Wednesday, August 30, 2017

WAZIRI MKUU AKUTANA NA MAKAMU WA RAIS WA KAMPUNI YA UTENGENEZAJI MELI UFARANSA

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza na Makamu wa Raisi wa Kampuni (Uendelezaji Bibiashara) wa Kampuni ya PIRIOU ya  utengenezaji na ukarabati wa  meli nchini Ufaransa. Bwana Michel Perrin .kulia ni Balozi wa Tanzania Nchini Ufaransa Bwana Samweli Shelukindo.Waziri Mkuu amekuana naye leo Agost 29/2017 Parisi Ufaransa

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza na Makamu wa Raisi wa Kampuni (Uendelezaji Bibiashara) wa Kampuni ya PIRIOU ya  utengenezaji na ukarabati wa  meli nchini Ufaransa. Bwana Michel Perrin .kulia ni Balozi wa Tanzania Nchini Ufaransa Bwana Samweli Shelukindo.Waziri Mkuu amekuana naye leo Agost 29/2017 Parisi Ufaransa

Read More

MIVARF YAWEZESHA HALMASHAURI 73 KUPUNGUZA UMASIKINI WA KIPATO

Programu ya Miundo Mbinu ya Masoko, Uongezaji thamani na Huduma za Kifedha Vijijini(MIVARF), imefanikiwa kupunguza umasikini wa kipato na kuimarisha uhakika wa chakula katika Halmashauri 73 zinazotekeleza program hiyo kwa Tanzania Bara na Visiwani.

Akiongea wakati wa Mkutano wa wadau wa MIVARF wa siku mbili tarehe 29 hadi 30, Agosti, 2017  mjini Dodoma, Mkurugenzi wa Idara ya uratibu wa shughuli za serikali Ofisi ya Wazir Mkuu, Obey Assery alifafanua kuwa lengo la Program hiyo inalenga kuongeza uzalishaji na tija kwa walengwa.

“Program imelenga kuwajengea uwezo wazalishaji ambao huwa katika vikundi kwa kuvifiki vikundi 2,331 vyenye walengwa 81,677. Kimsingi Programu imelenga kumuwezesha mkulima aweze kufanya  kilimo cha kibiashara” alisema Assery.

Naye Mratibu wa Program Kitaifa, Walter Swai alibainisha kuwa Program imelenga kuwajengea uwezo walengwa kuyafikia masoko ya uhakika ili waweze kupunguza umasikini wa kipato.

“Programu imelenga kuboresha 1,000km za  barabara hadi sasa 9991.8km zimeshakamilika sawa na asilimia 92. Lakini pia kwa upande wa miundo mbinu ya masoko tunajenga maghala, hadi sasa kati ya maghala 29 yaliyo kwenye malengo tayari tumekamilisha maghala 24 sawa na asilimia 83 ” alisistiza Swai.

Swai aliongeza kuwa Program hiyo imepanga kukarabati maghala 6 ambapo tayari yote yamekamilika, pia tumelenga  kujenga masoko 16 ambapo hadi sasa masoko 7 yamekamilika ambayo ni asilimia 44.
   
MIVARF;  ni Programu ya Miundo Mbinu ya Masoko na Huduma za Kifedha Vijijini  iliyobuniwa  na serikali ya Tanzania  kwa  kushirikiana na Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo yaani (IFAD) na Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB).


Read More

MIVARF YAWEZESHA HALMASHAURI 73 KUPUNGUZA UMASIKINI WA KIPATO

Mkurugenzi Idara ya Uratibu wa Shughuli za serkali Obey Assery akisistiza jambo wakati wa Mkutano wa wadau wa MIVARF Agosti 30, Agosti, 2017  mjini Dodoma.

 Wataalamu kutoka Program ya MIVARF wakifuatilia majadiliano ya wadau wa Program hiyo wakati wa mkutano wa wadau wa MIVARF Agosti 30 Mjini Dodoma.
Baadhi ya wadau wa MIVARF wakifuatilia mkutano wa wadau wa MIVARF unaofanyika mjini Dodoma Agost, 2017.
Baadhi ya wadau wa MIVARF wakifuatilia mkutano wa wadau wa MIVARF unaofanyika mjini Dodoma Agost, 2017.

Read More

Tuesday, August 29, 2017

WAZIRI MKUU AWATAKA WAWEKEZAJI KUFUATA SHERIA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka watu wote wenye nia ya kutaka kuwekeza katika miradi mbalimbali nchini Tanzania kuhakikisha wanafuata sheria, kanuni na taratibu.

Ametoa kauli hiyo leo (Jumanne, Agosti 29, 2017) wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Makamu wa Rais (Uendelezaji Bishara) wa kampuni ya PIRIOU, Bw. Michel Perrin.

Waziri Mkuu amekutana na Bw. Perrin jijini Paris nchini Ufaransa kupitia ofisi ya ubalozi wa Tanzania nchini Ufaransa. Kampuni ya PIRIOU inataka kuja nchini kuwekeza katika utengenezaji na ukarabati wa meli.

Akizungumza na muwekezaji huyo Waziri Mkuu alimshukuru kwa nia yake ya kutaka kuwekeza nchini, ambapo alimtaka afuate sheria, kanuni na taratibu za uwekezaji nchini.

“Tanzania ni sehemu nzuri ya uwekezaji kwa sababu kuna fursa nyingi. Pia ni nchi yenye amani na utulivu wa kisiasa pamoja na mazingira mazuri ya uwekezaji hivyo nakukaribisha sana.”

Kwa upande wake Bw. Perrin amesema ameamua kuja kuwekeza nchini kwa kuwa Tanzania ni nchi salama na kwamba anauhakika wa kupata soko ndani ya nchi pamoja na mataifa jiraji.

Amesema anaamini uwekezaji wake nchini Tanzania utakuwa na tija, hivyo ameahidi kufanya kazi kwa ushirikiano wa karibu na Serikali na pia atahakikisha anafuata sheria zote za nchi.

Pia Bw. Perrin alitumia fursa hiyo kumshukuru Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Balozi Samwel Shelukindo kutokana na ushirikiano anaompa kuhusu masuala ya uwekezaji nchini.

Naye Balozi Shelukindo amesema atahakikisha anaendelea kutafuta wafanyabiashara mbalimbali na kuwashawishi waje kuwekeza katika sekta mbalimbali nchini
Read More

Sunday, August 27, 2017

WAZIRI MKUU KASSIM MAJALIWA AKIMUAGA NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE CUBA

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa  akiagana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Cuba  Bi. Ana Teressa Jana Agosti 27/2017 katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Havana ,baada ya kumaliza ziara ya kikazi Nchini Cuba. Katikati ni Mke wa Waziri Mkuu Mama Mary Majaliwa.

Read More

Saturday, August 26, 2017

WAZIRI MKUU KASSIM MAJALIWA AKUTANA NA MAKAMU WA RAISI WA CUBA

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amekutana na kufanya mazungumzo ya Kikazi na Makamu wa Rais wa Cuba, Bi. Gladys Bejarano. katika Mji wa Havana Nchini Cuba jana August 26/2017

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amekutana na kufanya mazungumzo ya Kikazi na Makamu wa Rais wa Cuba, Bi. Gladys Bejarano. katika Mji wa Havana Nchini Cuba jana August 26/2017
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amekutana na kufanya mazungumzo ya Kikazi na Makamu wa Rais wa Cuba, Bi. Gladys Bejarano. katika Mji wa Havana Nchini Cuba jana August 26/2017


Read More

Thursday, August 24, 2017

WAZIRI MKUU AKUTANA NA RAIS WA VIWANDA VYA SUKARI CUBA

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akipata maelezo ya ukarabati wa kiwanda  cha Sukari cha UGB . kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Sukari Nnchini Cuba Bwana Francisco Martin, jana August 24/2017 kiwanda hicho kipo katika Mji wa San Nicola's de Bari Nnchini Cuba.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akiangalia shehena ya sukari iliyozalishwa katika kiwanda cha UGB Central Azucarero 30 Noviembre, Wakati alipotembelea kiwanda hicho jana August 24/2017 kilichopo katika mji wa San Nicola's de Bari Nchini Cuba

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amekutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Shirika la Viwanda vya Sukari nchini Cuba, Bw. Francisco Lled, ambaye amekubali kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kuongeza uzalishaji wa sukari nchini.

Shirika la Sukari la nchini Cuba linauwezo wa kuzalisha tani milioni nne za sukati kwa mwaka huku mahitaji ya ndani ni tani 700,000, ambapo kiasi kinachobaki huuzwa nje ya nchi. Kwa sasa shirika hilo linazalisha tani milioni mbili tu katika viwanda vyake 56.

Waziri Mkuu alikutana na Bw. Lled jana (Alhamisi, Agosti 24, 2017), wakati alipofanya ziara katika kiwanda cha kuzalisha sukari cha UGB Central Azucarero 30 de Noviembre katika mji wa San Nicola’s de Bari ambacho ni kati ya viwanda 27 vya shirika hilo linalomilikiwa na Serikali ya Cuba kwa asilimia 100.

Katika mazungumzo yao Waziri Mkuu alimshawishi Bw. Lled kuja nchini kwa ajili ya kuwekeza katika ujenzi wa viwanda vya kuzalisha sukari. Alisema kwa sasa Tanzania kuna viwanda vikubwa vitano vya sukari ambavyo uzalishaji wake hautoshelezi mahitaji ya ndani.

Waziri Mkuu alivitaja viwanda hivyo ambavyo ni Mtibwa na Kilombero (Morogoro), Mahonda (Zanzibar), TPC (Kilimanjaro) na Kagera  ambavyo vyote vinazalisha jumla ya tani 320,000 za sukari kwa mwaka huku mahitaji yakiwa ni zaidi ya tani 400,000.

Hata hivyo, Waziri Mkuu alisema Serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi inatarajia kujenga viwanda vitatu vya kuzalisha sukari, ambavyo vitazalisha sukari itakayotosheleza mahitaji na ndani ya nchi na kiasi kitakachosalia kitauzwa nje.

Kwa upande wake Bw. Lled alisema sera za Cuba haziruhusu shirika kwenda kuwekeza nje ya nchi na badala yake wanaruhusiwa kuzisaidia nchi zinazohitaji kujenga viwanda hivyo kwa kutoa ushauri na usimamizi wa ujenzi wa miradi hiyo.

Alisema Shirika lake lipo tayari kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika usimamizi na kutoa ushauri wa ujenzi wa miradi ya viwanda vya kuzalisha sukari na kwamba walishatoa huduma kama hiyo katika nchi mbalimbali zikiwemo Brazil na Bolivia.

Katika hatua nyingine, Bw. Lled alisema mbali na uzalishaji sukari pia shirika hilo kupitia viwanda vyake vya sukari wanazalisha vyakula vya mifugo, asali ambayo inatumika katika viwanda vya kutengeneza vinywaji vikali pamoja nishati ya umeme.

Alisema miwa ya kuzalishia sukari katika viwanda vyao wanaipata kutoka kwenye vikundi vya ushirika wa kulima wa miwa vilivyoko katika mikoa yote nchi nzima kasoro mkoa wa Havana na Pañar del Rio na kwa mkulima mmoja mmoja ambao kwa pamoja hukusanya miwa katika vituo ambavyo hupeleka kiwandani.

Hata hivyo alisema kuwa viwanda vyao vinanunua miwa kwa bei tofauti kulingana na ubora wa miwa na kwamba shirika lao linawasaidia wakulima kwa kuwaelimisha namna bora ya kulima pamoja na kuwaazima mashine za kuvunia wakati wa mavuno. Miwa yote nchini Cuba inavunwa kwa kutumia mashine.

Read More

Wednesday, August 23, 2017

WAZIRI MKUU AITAKA WIZARA YA UTALII KUONGEZA UBUNIFU : MAJALIWA

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa (mwenye miwani)na Mama Mary Majaliwa (kulia). Pamoja na Ujumbe wa Serekali ya Tanzania wakipata maelezo jana August 23/2017kutoka kwa Kiongozi wa Utalii katika Mkoa wa Matanzas ,Bwana Luis Martines. jinsi fukwe za Bahari zinavyo tunzwa nakuwa kivutio kwa Watalii wanao tembelea Mji wa Varadero Mkoa wa Matanzas Nnchini Cuba
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ,kushoto akikabidhi  Jarida la kutangaza Utalii wa Tanzania KwaKiongozi wa masuala ya Utalii katika Mkoa wa Matanzas . Bwana  Luis Marines , jana August 23/2017 wakati alipokuwa katika Ziara yakikazi kwenye Mji  wa Varadero Mkoa wa Matanzas Nnchini Cuba katikati katika picha ni Mama Mary Majaliwa.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa (mwenye shati jeupe) na Mama Mary Majaliwa (kushoto)pamoja na ujumbe wa serekali ya Tanzania jana August 23/2017, wakipata maelezo kutoka kwa muongoza wa Talii Bibi Yanseli Marrero kuhusu  biashara ya Boti za Utalii  kwenye fukwe za Bahari katika Mji wa Varadero  Mkoa wa Matanzas Nnchini Cuba
Read More

WAZIRI MKUU AITAKA WIZARA KUONGEZA MBINU ZA KUVUTIA WATALII


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii kutafuta mbinu bora za kutangaza vivutio mbalimbali vya utalii vilivyopo nchini ili kukuza sekta hiyo.

Amesema licha ya Tanzania kuwa na vivutio vingi vya utalii lakini idadi ya watalii wanaoingia nchini kwa mwaka ni ndogo, hivyo kuna haja ya kuboresha matangazo.

Waziri Mkuu aliyasema hayo jana (Jumatano, Agosti 23, 2017) wakati alipofanya ziara katika mji wa kitalii wa Varadero ulioko kwenye mkoa wa Matanzas nchini Cuba.

Alisema mji wa Varadero tu unaingiza watalii zaidi ya milioni moja kwa mwaka na unategemea kivutio kikubwa kimoja tu cha fukwe ambayo ina urefu wa kilomita 22.

Alisema idadi  hiyo ni tofauti na Tanzania ambayo imejaliiwa kuwa na vivutio vingi vya utalii huku watalii wanaovitembelea ni wachache. “Tunatakiwa kujitangaza zaidi.”

Waziri Mkuu alitaja baadhi ya vivutio vya utalii ambavyo ni mlima Kilimanjaro, mbuga za wanyama, miji ya kihistoria ya Kilwa, Bagamoyo, Stone Town pamoja na Mikindani.

Vivutio vingine ni eneo la Oldvai George ambako binadamu wa kwanza aliwahi kuishi, hifadhi ya Gombe ambako kuna sokwe ambao wanaishi kama binadamu.”

Alisema Serikali itahakikisha jitihada zinafanyika katika kukuza sekta ya utalii ikiwa ni pamoja na kutangaza vivutio vilivyoko nchini ili kuweza kuongeza idadi ya watalii.

Pia Waziri Mkuu aliwahamasisha Watanzania kujenga tabia ya kutembelea vivutio vyeo vya utalii na kujifunza mambo mbalimbali na si kuwaachia wageni pekee.

Kwa upande wake, Kiongozi wa Sekta ya Utalii katika mkoa wa Matanzas, Bw.  Luis Martinez de Armas alisema mji wa Varadero ni kivutio kikubwa cha utalii nchini Cuba.

Alisema kivutio kingine cha utalii ni hoteli zilizojengwa ndani ya bahari, maeneo ya kihistoria na migahawa inayouza vyakula vya asili vya nchi hiyo.

Bw. Luis alisema mwaka 1990 ndio walianza kuendeleza sekta ya utalii katika mkoa wao na ulikuwa na hoteli 4,436 ambazo kwa sasa zimeongeza na kufikia hoteli 20,696.

Hata hivyo Bw. Luis alisema Tanzania inavivutio vingi vya utalii na kwamba anavutiwa na mlima Kilimanjaro pamoja na wanyama na viumbe vingine vilivyoko katika mbuga mbalimbali. Alisema wako tayari kushirikiana na Serikali katika kukuza sekta ya utalii.
Read More

Tuesday, August 22, 2017

WAZIRI MKUU AWAKARIBISHA WACUBA KUJENGA VIWANDA TANZANIA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Cuba nchini Tanzania, Balozi Lucas Domingo Polledo, ambapo amewakaribisha wafanyabiashara wa Cuba kuja kuwekeza katika ujenzi wa viwanda vya dawa.

Amesema kwa sasa Serikali ya Tanzania inaagiza dawa kutoka nje ya nchi jambo ambalo linasababisha kutumia fedha nyingi, hivyo uwepo wa kiwanda utasaidia katika kupunguza gharama. Pia wawekezaji watakuwa na uhakika wa soko la bidhaa zao.

Waziri Mkuu aliyasema hayo jana jioni (Jumanne, Agosti 22, 2017) wakati akizungumza na Balozi Polledo mjini Havana. Waziri Mkuu yuko nchini Cuba kwa ajili ya ziara ya kikazi yenye lengo la kudumisha ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.

Alisema Serikali imedhamiria kuendeleza sekta ya viwanda nchini kama mkakati wa kukuza uchumi na kufikia uchumi wa kati, hivyo wafanyabiashara kutoka nchini Cuba wanakaribishwa kuja kuwekeza nchini, hususani katika viwanda vya dawa na sukari.

Waziri Mkuu alisema licha ya Tanzania kuwa ni nchi ya amani na yenye utulivu wa kisiasa, pia imeweka mazingira mazuri ya uwekezaji jambo ambalo litawawezesha watakaokuja kuwekeza nchini kupata tija.

Pia alitumia fursa hiyo kuishukuru Serikali ya Cuba kwa ushirikiano mzuri na Serikali ya Tanzania kwa sababu Cuba ni mojawapo kati ya nchi zenye ushirikano wa muda mrefu na Tanzania hususani katika masuala ya Kisiasa, Kijamii, Kielimu na Kiuchumi.

“Tanzania na Cuba zina historia ya kutosha. Tunatambua mahusiano mazuri yaliyopo kati nchi zote mbili, ambayo yalikuwepo kuanzia Serikali ya Awamu ya kwanza chini ya uongozi wa Baba wa Taifa Hayati Mwl. Julius Nyerere.”

Kwa upande wake, Balozi Polledo alisema Serikali ya Cuba itahakikisha uhusiano wake na Serikali ya Tanzania unaendelea kuimarishwa. Pia alipongeza jitihada zinazofanywa na Serikali katika kuboresha maendeleo pamoja na kukuza uchumi.

Alisema licha ya kuwahi kufanya kazi kama Balozi katika nchi mbalimbali za Afrika, baada ya kufika Tanzania amefurahishwa na kasi ya ukuaji wa uchumi pamoja na kuimarika kwa hali ya siasa na amani.”Hali hii ni tofauti na mataifa mengine  ya Afrika.”

Pia Balozi Polledo alisema kwamba Serikali ya Cuba itaendelea kushirikiana na Tanzania katika uboreshaji wa Sekta za Afya na Elimu, ambapo alisema jumla ya madaktari 50 wa Cuba wakiwemo maprofesa 11 wako nchini wakihudumia wananchi katika mikoa mbalimbali.

Read More

Monday, August 21, 2017

WAZIRI MKUU AWATAKA WATANZANIA KUIMARISHA UZALENDO



WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka Watanzania wote wahakikishe wanaboresha mshikamano wao pamoja na kuimarisha uzalendo kwa Taifa lao.

Ametoa kauli hiyo jana jioni (Jumapili, Agosti 20, 2017) wakati akizungumza na wanafunzi wa Kitanzania wanaosomea udaktari nchini Cuba.

Waziri Mkuu yuko nchini Cuba kwa ajili ya ziara ya kikazi yenye lengo la kudumisha ushirikiano kati ya nchi hizo mbili. Alisema uzalendo kwa Taifa ni jambo muhimu.

 “Uzalendo ni muhimu sana kwa sababu tumekosa fursa nyingi za kimaendeleo kutokana na baadhi ya wananchi kutokuwa wazalendo kwa Taifa lao.”

Kutokana na hali hiyo Serikali inawasisitiza Wananchi kuwa wazalendo na washirikiane kuhakikisha fursa za kimaendeleo zilizoko nchini zinaendelezwa.

Alisema Serikali inatekeleza miradi mingi kwa lengo la kukuza uchumi kutoka wa chini kwenda wa kati, ni vema wananchi wakashirikiana nayo ili kufanikisha adhma hiyo.

Pia Waziri Mkuu alitumia fursa hiyo kuwasihi wanafunzi hao kuzingatia sheria za nchini waliyoko pamoja na kukumbuka kurudi nyumbani mara wamalizapo masomo yao.

Alisema Serikali inatambua uwepo wao wa kimasomo nchini Cuba na kwamba inatarajia kupata mchango mkubwa kutoka kwao punde wamalizapo masomo yao.

 “Nawaomba msome kwa bidii na mfaulu mitihani yenu. Elimu yenu iwasaidie katika ajira na muweze kurejesha mikopo mliyopewa na Serikali ili iwanufaishe wengine.”

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu aliwataka Mabalozi wote wanaoiwakilisha Tanzania katika mataifa mbalimbali kuhakikisha wanatangaza vivutio vya utalii.

Alisema Tanzania imejaaliwa kuwa na vivutio vingi vya utalii, hivyo ni vema Mabalozi wakavitangaza jambo ambalo litasaidia kuongeza idadi ya watalii wanaokuja nchini.

Miongoni mwa vivutio vya utalii vilivyoko nchini ni pamoja na mlima Kilimanjaro, visiwa vya Zanzibar, mbuga mbalimbali zenye wanyama wa aina tofauti tofauti.

Awali Mwenyekiti wa wanafunzi hao, Bw. Goodchance Tarimo alimuhakikishia Waziri Mkuu kwamba watarejea nyumbani mara baada ya kumaliza masomo yao nchini humo.

Alisema wao wanaimani kubwa na Serikali na wanaunga mkono jitihada zinazofanywa na viongozi wa Taifa kwa lengo la kuboresha maendeleo pamoja na kukuza uchumi.

“Tunapongeza jitihada za Serikali ya Awamu ya Tano katika  kujenga uchumi wa viwanda, mapambano dhidi ya rushwa, ufisadi na ujenzi wa miundombinu ya kisasa.”
Read More

Sunday, August 20, 2017

WAZIRI MKUU AWATAKA WATANZANIA KUIMARISHA UZALENDO

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa . katikati akiongea na wanafunzi wanao somea fani ya Udaktari nchini Cuba , katika Hotel ya Nacional de Cuba .jana August 20/2017 kushoto ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanafunzi Cuba,Bwana Goodchance Tarimo,  kulia ni Ofisa wa  Ubalozi wa Tanzania Nnchini Canada na Cuba.Bwana Leonce Bilauri

Waziri Mkuu Kassim Mjaliwa .kulia akisalimiana na Eshe Hemed Rashid Mwanafunzi wa  Kitanzania anaye Soma fani ya Udaktari  Nnchini Cuba .katikakati ni Nasra Sheikhan. Waziri Mkuu alikutana na wanafunzi wa Kitanzania wanao soma Udakatari Cuba. katika Hoteli ya Nacional de Cuba .Jana August 20/2017

Waiziri Mkuu Kassim Majaliwa akiwa katika picha ya pamoja na wanafunzi Wakitanzania wanao somea fani ya Udaktari Nchi Cuba .Waziri Mkuu yupo Havana Cuba kwa Ziara ya Kikazi

Read More

Thursday, August 17, 2017

TUTAENDELEZA MAHUSIANO YA KIDIPLOMASIA YALIYOJENGWA NA AWAMU ZILIZOTANGULIA-MAJALIWA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Magufuli inayatambua na kuyathamini mahusiano mazuri ya kidiplomasia yaliyojengwa na awamu zilizotangulia baina ya Tanzania na mataifa mbalimbali ikiwemo Jamuhuri ya Cuba na kwamba itayaendelea.

Ametoa kauli hiyo jana jioni (Alhamisi, Agosti 17, 2017), alipozungumza na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Cuba, Bi Anna Teressa mara baada ya kuwasili nchini Cuba kwa ajili ya ziara ya kikazi yenye lengo la kudumisha ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.

“Tanzania na Cuba zina historia ya kutosha. Tunatambua mahusiano mazuri yaliyopo kati nchi zote mbili, ambayo yalikuwepo kuanzia Serikali ya Awamu ya kwanza chini ya uongozi wa Baba wa Taifa Hayati Mwl. Julius Nyerere.”

Amesema katika ziara yake hiyo anatarajia kufanya mazungumzo na viongozi mbalimbali waandamizi wa Serikali ya Cuba kwa lengo la kukuza ushirikiano katika sekta za Afya, Elimu, Utalii na Kilimo.

Waziri Mkuu amesema Cuba ni mojawapo kati ya nchi zenye ushirikano wa muda mrefu na Tanzania kisiasa, kijamii, kiafya na kiuchumi.”Mfano katika Sekta ya Afya, madaktari wengi kutoka Cuba walikuwa wanakuja Tanzania kutibu wagonja waliokuwa na maradhi makubwa.”

Pia Waziri Mkuu amesema katika ziara hiyo anatarajia kukutana na Jumuya ya Wafanyabiashara wa Cuba ili kuwaelezea fursa za uwekezaji zilizopo nchini Tanzania hususan  katika Sekta ya Viwanda pamoja na kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo nchini.

Kwa upande wake Bi. Anna ambaye alimpokea Waziri Mkuu kwa niaba ya Serikali ya Cuba alitumia fursa hiyo kuishukuru Serikali ya Tanzania kwa kuendelea ushirikiano mzuri baina ya nchi hizo mbili, hivyo alimuhakikishia kwamba wataendelea kuudumisha.

Pia Bi. Anna ametumia fursa hiyo kuupongeza uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Magufuli kwa namna inavyopambana na rushwa, ufisadi, kuhimiza uwajibikaji pamoja na kutetea wanyonge.

Read More

WAZIRI MKUU KASSIM MAJALIWA AWASILI NCHINI CUBA KWA ZIARA YA KIKAZI

Waziri Mkuu Kassim  Majaliwa  akiwa na mazungumzo na Naibu Waziri wa Mambo ya Nnje wa CUBA Bibi Ana Teresa mara baada ya kuwasili jana  August 17/2017 katika Uwanja wa  Ndege wa kimataifa wa Havana   kwa ajili ya ziara ya kikazi Nchini Cuba.
Waziri Mkuu Kassim Majliwa na Mkewe Mary Majaliwa wakipata makaribisho Nchini Cuba jana August 17/2017 kutoka kwa Naibu  Waziri wa Mambo ya Nnje wa CUBA Bibi Ana Teresa mara baada ya kuwasili  katika Uwanja wa  Ndege wa  kimataifa wa Havana   kwa  ziara ya kikazi Nchini Cuba.


Read More

TUMEDHAMIRIA, TUNARATIBU KWA MATOKEO CHANYA NCHINI.

Napenda kuwahakikishia watanzania serikali yangu itafanya kazi kwa ajili ya watu wote, watanzania wa maisha ya juu na wa maisha ya chini, ninachoomba watanzania tuendelee kushirikiana, Sisi sote lengo letu liwe ni moja, kuleta maendeleo ya watanzania wote” 

Rais Dkt. John Pombe Magufuli, wakati akizindua Bunge la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Novemba, 2015.
Hiyo ni kauli ambayo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amekuwa akiirudia mara kwa mara pale anapopata fursa ya kuwahutubia wananchi. Lengo lake ni kuwadhihirishia watanzania kuwa Serikali ya awam ya Tano anayoingoza imedhamiria kutekeleza sheria, Sera, Mipango na mikakati ili kila mtanzania apate matokeo chanya ya utekelezaji huo.

Bila shaka msomaji wa Makala hii tunaposema matokeo chanya ya utekelezaji wa serikali ya awam ya tano utakubaliana na mimi kuwa unayafahamu, baadhi ya matokeo hayo ni kuimarika uwajibikaji na nidhamu katika Utumishi wa Umma; kuboresha huduma za kiuchumi na za kijamii; na kutekeleza Awamu ya Kwanza ya Mpango wa Serikali Kuhamia Dodoma.

Kimsingi matokeo hayo ni chanya lakini pia yanamgusa kila mtanzania ambaye ni wa hali ya juu na chini. Hii ni kutokana na uongozi mahiri, uzalendo uliotukuka na dhamira njema aliyonayo Mhe. Rais kwa Watanzania.

 Ili dhamira hiyo iwe endelevu lazima kuwepo na uratibu imara, unaofanywa kiufanisi katika kuhakikisha kuwa sheria, Sera, Mipango na mikakati ya serikali inaratibiwa na inatekelezwa kwa manufaa ya Watanzania.

Ifahamike tu, Ofisi ya Waziri Mkuu ndiyo yenye majukumu ya kuratibu na kusimamia shughuli za Serikali katika sekta zote na Bungeni. Ofisi hii imepata jukumu hilo kwa mara kwa mujibu wa katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ibara (52).Pamoja na majukumu hayo ya msingi wa kikatiba, Aidha, Ofisi hii inahusika na kuratibu masuala yote mtambuka, ambapo ni yale masuala yanayuhusisha sekta Zaidi ya moja kama vile; (UKIMWI, Madawa ya Kulevya, Uendelezaji wa Makao Makuu ya Nchi Dodoma, Uchaguzi, Bunge, Vyama vya siasa, Kazi, Ajira, Vijana na Watu wenye ulemavu).

Makala hii itajikita katika kuangalia jinsi ofisi hii ilivyodhamiria kutekeleza majukumu yake ya kuratibu na kusimamia shughuli zote za serikali ndani na nje ya Bunge na masuala mtambuka, ili kuleta matokea chanya nchini na hatimaye kufanikisha adhima ya serikali ya awam ya tano ya kujenga uchumi wa viwanda.

Mfumo wa Ufuatiliaji wa Shughuli za Serikali

Hatuwezi kuzungumzia matokeo chanya ya shughuli za serikali bila kuwa na nyenzo bora za kusimamia na kuratibu shughuli hizo kuanzia katika ngazi ya kijiji, kata, wilaya, mkoa na kitaifa.

Kwa kulitambua hilo Ofisi ya Waziri Mkuu imeanzisha Mfumo wa Wazi wa Kielektroniki wa kufuatilia uwajibikaji na utendaji Serikalini. Mfumo huo utasaidia kuongeza ufanisi katika uratibu wa shughuli za Serikali kwa kuwawezesha Viongozi kutoa maelekezo na kufuatilia utekelezaji wake.

Kama tunavyojua serikali hii inaongozwa na falsafa ya “HAPA KAZI TU” hivyo mfumo huu unajikita katika dhana hiyo ya kuona kazi inafanyika kwa kutekeleza maagizo ya viongozi wakuu na Mpango wa Taifa wa Maendeleo.

Ofisi ya Waziri Mkuu imedhamiria kuratibu kwa matokeo chanya kwa kupitia mfumo huo ambao utaongeza kasi ya utoaji taarifa za utekelezaji wa kazi za Serikali kwa wakati na pia kuongeza uwajibikaji kwa watumishi wa Umma.

Wizara na Taasisi zote za Serikali zinatakiwa kuutumia Mfumo huo kikamilifu ili kurahisisha ufuatiliaji wa utekelezaji wa kazi za Serikali na kusaidia viongozi kutatua vikwazo pale vinapojitokeza.


“Mfumo huu utasaidia sisi waratibu washughuli za serikali kuangalia maagizo na ahadi zilizotolewa na viongozi wakuu wa serikali ambazo zitakuwa zinawekwa katika mfumo huo na wasaidizi wao. Mfumo huo utaainisha mhusika wa kutekeleza agizo hilo, kama limetekelezwa ama bado halijatekelezwa hivyo unakuwa unauwezo wa kuangalia nini kilielekezwa na utekelezaji wake, tunataka utekelezaji wa shughuli za serikali ziwe za ufanisi na kwa wakati”

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Jenista Mhagama, Machi 2017, Dodoma, alipokuwa akizindua Mfumo huo.

 


Ikiwa ni zaidi ya miaka 40 tangu serikali kuwa na dhamira ya kuhamia Dodoma, serikali ya awam ya Tano kupitia Ofisi ya Waziri mkuu imeweza kuratibu uamuzi wa kuhamishia rasmi Shughuli za Serikali Kuu Dodoma kwa awamu.

Ninafurahi kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba tayari watumishi 2,069 wakiwemo Mawaziri, Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu, Naibu Makatibu Wakuu, baadhi ya Wakuu wa Idara na Vitengo na watumishi wengine wamekwishahamia Dodoma kama ilivyopangwa. Vilevile, Wizara zote zimepata majengo ya Ofisi yatakayotumika katika kipindi cha mpito”

Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa, Julai, 2017 Bungeni.
Katika kuhakikisha matokeo chanya ya zoezi hili yanapatikana, Ofisi ya Waziri Mkuu inaendelea kuratibu zoezi la kuupitia upya Mpango Kabambe wa Mji wa Dodoma. Mapitio hayo yatasaidia sana kuepuka makosa yaliyofanyika katika miji mingi hususan ujenzi holela unaochangia katika uchafuzi wa mazingira na kuharibu mandhari ya miji.
Ni wazi kwamba, Ili Mji wa Dodoma uweze kuendelezwa kwa mpangilio mzuri wenye kukidhi uchumi wa viwanda unaokusudiwa na serikali ya awam ya Tano. ujenzi wa Mji wa Dodoma hautafanywa na Serikali pekee, bali serikali inaendelea kuhamasisha Sekta binafsi na wadau wengine kuwekeza Dodoma.

Kwa upande wa serikali kupitia Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), limejenga nyumba 300 za makazi ambazo watumishi wanaweza kununua au kupangishwa. Manispaa ya Dodoma na Taasisi nyingine za Serikali.zinaendelea na zoezi la upimaji wa viwanja, kuboresha miundombinu na kudhibiti ujenzi holela kwa kushirikiana.

Msomaji wa Makala hii utakubaliana nami kuwa dhamira ya kuratibu uamuzi wa kuhamishia rasmi Shughuli za Serikali Kuu Dodoma, inaleta matokeo chanya nchini kwani serikali itakuwa imetoa fursa kwa wananchi kutoka pande zote nchini kupata huduma zote za serikali bila kusafiri umbali mrefu hadi Dar es salaam kama ilivyokuwa awali.

Lakini pia uamuzi wa kuhamishia rasmi Shughuli za Serikali Kuu Dodoma wananchi watapata fursa ya kupata huduma hizo kwa wakati na kwa pamoja mara tu serikali itakapo kamilisha ujenzi wa maeneo ya mji wa serikali ambao utakuwa na ofisi zote za serikali mahali pamoja.

Siasa

 

Ukiniuliza siasa nini? Kwa ufupi nitakwambia neno siasa linaashiria mambo yanyaoihusu jamii, tunaweza kueleza kwa ufupi kuwa hiyo ndiyo maana ya siasa. Kwani siasa hubeba taswira nzima ya jamii katika; Uchumi, elimu, mfumo wa, haki, wajibu na sheria, mgawanyo wa mali katika jamii, mila, utamaduni, desturi, imani na mahusiano miongoni mwa jamii au nje ya jamii husika.

 

Kwakuwa siasa inahusu maisha ya wanadamu na wanasiasa wanajishughulisha na mambo yanayoihusu jamii, hatuna budi kujenga jamii inayoheshimu na kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za nchi pamoja na kuwa na uvumilivu wa kisiasa, ili kuendelea kuboresha demokrasia hapa nchini.

 

Ofisi ya Waziri Mkuu ndiyo yenye dhamana ya Kuratibu shughuli za siasa nchini kupitia ofisi ya Msajili wa vyama vya siasa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi.

 

“Ninatoa rai kwa wadau wa siasa kote nchini kujenga utamaduni wa masikilizano na kuendesha siasa za maendeleo badala ya siasa za malumbano; siasa za kuunganisha watu wetu badala ya kuwagawa; na siasa za uwajibikaji badala ya siasa za mazoea. Serikali itaendelea kulinda na kuheshimu misingi ya siasa zinazolenga kuleta ustawi wa wananchi na zinazotanguliza maslahi ya nchi na wananchi” Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa, Julai, 2017 Bungeni.

 

Katika misingi ya kuboresha demokrasia nchini, ofisi hiyo imeweza kuratibu Chaguzi Ndogo zilizofanyika tarehe 22 Januari, 2017 katika Jimbo la Dimani - Zanzibar na Udiwani katika kata 20 Tanzania Bara kwa kushirikisha wagombea kutoka vyama 15 vya siasa.

 

Katika kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata uwakilishi, tayari Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa kushirikiana na Mwanasheria Mkuu wa Serikali imeweza kuendesha kesi kwa kasi na weledi za baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.

 

Mashauri yaliyofunguliwa baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 yalikuwa ni mashauri 53 ya kupinga ushindi wa Ubunge na mashauri 194 ya kupinga ushindi wa Udiwani, Mashauri hayo yamekwisha sikilizwa na hukumu kutolewa.

 

Tukiacha masuala ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, bila shaka msomaji wa Makala hi utakuwa unaufikiria pia uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020. Tayari Ofisi ya Waziri Mkuu katika dhana ya kuratibu kwa matokeo chanya imeshaanza kuratibu zoezi hilo kupitia Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).

Serikali imetenga shilingi bilioni 10 kwa ajili ya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la wapiga Kura kwa mwaka wa fedha wa 2017/2018. Tume ya Taifa ya Uchaguzi imeanza maandalizi ya kufanya uboreshaji wa daftari hilo utakaojikita katika kufanya mapitio ya mifumo ya menejimenti ya Uchaguzi.

Tume hii ni huru, hivyo Bunge limepitisha fedha hizo kwa ajili ya Tume kuanza kufanya maadalizi ya kuboresha Daftari la kudumu la Wapiga Kura kwa mara ya kwanza na itafanyika tena mara ya pili kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020. Lazima Tume ipitie upya mifumo yake na kuiboresha lakini pia kuangalia na vifaa ilivyonavyo. Nimeridhika na mpango kazi wa tume wa kukamilisha kazi hiyo kwa ufanisi na weledi mkubwa, sisi kama serikali tutawasaidia katika maeneo yote ambayo kikatiba tunaruhusiwa kushirikiana nao katika utekelezaji wa majukumuyao”

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Jenista Mhagama Agosti, 2017, alipotembelea Ofisi za Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).

 

Bunge

Nikukumbushe msomaji wa Makala hii, kuwa nchi yetu inayo mihimili mitatu ya nchi ambayo ni Serikali, Bunge na Mahakama. Wajibu wa serikali ni kuendesha utawala  na utekelezaji kila siku wa shughuli za umma, Bunge linao wajibu wa kujali sera na kutunga sheria na mahakama zinao wajibu wa kusikiliza na kuamua kesi na pia kutoa tafsiri ya sheria na katiba ya nchi.


Ofisi ya Waziri Mkuu kama lilivyo jukumu la kikatiba la kuratibu shughuli za serikali, hata ndani ya Bunge ofisi hii ndiyo inayoratibu shughuli za serikali Bungeni, Shughuli hizo zinazojumuisha mikutano minne kwa mwaka pamoja na Kamati zake zimeratibiwa kwa mafanikio makubwa.

 Ofisi hii huakikisha inakuwa kiungo kati ya serikali na Bunge kama ilivyo mihimili tofauti na yenye mamlaka yake ya kikatiba.  miswada 10 ya sheria ya serikali ilijadiliwa na kupitishwa na Bunge pamoja na matoleo 41 ya Gazeti la serikali na nyongeza zake yaliwasilishwa Bungeni.

Na hapa ndipo msomaji utaweza kunielewa kwa nini tumedhamiria kwa matokeo chanya hapa nchini kwani ofisi hii ndiyo kiungo cha serikali na wananchi kupitia Bungeni ambapo wabunge huwawakilisha wananchi.

 

Wabunge kama wawakilishi wawanachi wamewawakilisha vyema Bungeni nahasa katika kutetea maslah yao. Katika mkutano ulioisha  wa saba wa Bunge umefanikisha kuundwa kwa kamati maalum ya Wabunge tisa itakayotathmini mfumo wa uchimbaji, usimamizi, umiliki na udhibiti wa madini ya almasi nchini.

Kuundwa kwa Kamati hiyo kumetokana na pendekezo la kuunda Tume ya kuchunguza na kufuatilia madini ya Almasi alilolitoa Rais Dk. John Magufuli Juni 12 mwaka huu wakati akipokea taarifa ya pili ya kamati ya kuchunguza masuala ya kiuchumi na kisheria kuhusu usafirishaji wa makinikia.

Kamati hiyo pia itaandaa mapendekezo mahsusi kwa ajili ya kuishauri Serikali kuhusiana na uendeshaji bora wa biashara ya Madini hapa Nchini. Ofisi ya waziri Mkuu kama mratibu wa shughuli za serikali Bungeni tumedhamiria kuratibu mapendekezo hayo kwa matokeo chanya kwa watanzania wote.

 

Lakini pia, Ofisi hii huratibu maswali ya serikali Bungeni, suala ambalo huipa fursa ofisi ya waziri mkuu kujua na kutambua nini mahitaji hasa ya watanzania na kuweza kuelelekeza kwa watekelezaji husika kuweza kuyapatia majibu.

 

Katika   Mkutano wa nne, wa tano na wa sita wa Bunge la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania maswali ya msingi 330 ya Wabunge yaliulizwa na kujibiwa na Serikali pamoja na maswali 865 ya nyongeza

Aidha, Ofisi ya Waziri Mkuu hupokea malalamiko rufani, kwa maana ya malalamiko ambayo mhusika hakupata suluhisho katika ngazi zote, kuanzia ngazi ya kijiji, kata, wilaya, mkoa na kitaifa, ofisi hii huya pokea kama mratibu wa shughuli zote za serikali na kuyapatia ufumbuzi kwa wakati.


Tayari Ofisi imeshapokea na kushughulikia jumla ya kero na malalamiko ya wananchi 278 na kuyapatia ufumbuzi na nyingine zimewasilishwa katika mamlaka mbalimbali ili kupatiwa ufumbuzi.

Tutoe wito kwa watanzania amabao wanayo malalamiko ya aina hiyo kufika ofisi ya Waziri Mkuu, milago huwa wazi kuanzia saa mbili asubuhi hadi saa Saba Mchana kwa siku zote za kazi.

 

Hata hivyo; kutokana na matokeo chanya ya serikali ya awam ya Tano, ni wazi kuwa wananchi wenye malalamiko ya aina hiyo wamepungua kwa kiasi kikubwa kufika ofisini, hii inadhihirisha kuwa uwajibikaji na uadilifu umeongezeka serikalini.

 

Uratibu wa Maafa

Kimsingi maafa yanapotokea huathiri maisha ya watu na kuharibu mali na mazingira. Maafa pia, hayachagui yanapotokea iwe Vijijini au Mijini, na iwe nchi za dunia ya kwanza au dunia ya tatu wote wanaathirika. Ili kuweza kupunguza athari zinazoletwa na maafa ni lazima kuchukua hatua za tahadhari mapema.

Hapa nchini jukumu la kuratibu shughuli za maafa lipo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu katika Idara ya Uratibu wa shughuli za maafa. Idara hii ilianzishwa kwa mujibu wa Sheria Na.9 ya mwaka 1990 ya Uratibu wa Misaada ya Maafa.

Serikali wakati wote inahakikisha kuwa nchi ipo katika hali ya utayari wa kukabiliana na maafa na pia kutoa misaada ya kibinadamu ikiwemo huduma za matibabu, ushauri wa kisaikolojia, na vifaa pale maafa yanapotokea.

 

Kufuatia tetemeko la ardhi lililotokea katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa mwezi Septemba 2016, Serikali kwa kushirikiana na wadau iliechukua hatua za kushughulikia athari zilizotokana na tetemeko hilo. Huduma za afya na tiba na za kibinadamu za chakula na malazi zilitolewa kwa walioathirika.

 

Changamoto ambayo hupatikana wakati wa uratibu wa shughuli za maafa ni kuwa wananchi wachache kushindwa kuelewa kuwa maafa ya asili ni vigumu kuyazuia lakini pia ni vigumu hata kuyatabiri kama ilivyo maafa ya tetemeko la ardhi.

 

Kwa mantiki hiyo ni vigumu serikali kuwa na makadirio sahihi ya bajeti ya kukabili na kurejesha hali pindi maafa yanapotokea. Lakini kwa kuwa serikali hujali ustawi wa jamii yake huchukua jukumu la moja kwa moja kurejesha hali, ambayo itaweza kuwaweka wananchi wake kwa mara moja  na kwa wakati katika hali ya kawaida na kuendelea na uzalishaji kama ilivyo kuwa kabla ya maafa.

 

Tukiangalia maafa ya tetemeko la ardhi mkoani Kagera serikali ilichukua jukumu la kurejesha hali ya miundo mbinu ya umma badala ya miundo mbinu ya kila mwananchi mmoja moja isipokuwa kwa wale wazee, wajane/wagane, yatima na watu wenye ulemavu pamoja na watu ambao nyumba zao zilibomoka kabisa na kubaki bila makazi. Serikali ilitoa maturubai 6,237, mahema 367, mabati 7,300 na mifuko ya saruji 1,825 kwa walioathirika.

 

Katika kuhakikisha jamii iliyoathirika inarejea katika hali ya kawaida Serikali ilirejesha hali ya miundombinu iliyobomoka, yakiwemo majengo ya Serikali na Taasisi za Umma 686, Kituo cha wazee Kilima Kituo cha afya Kabyaile Ishozi pamoja na ukarabati wa Omumwani.

 

Serikali inaendelea na ujenzi wa Shule ya Ihungo, Nyakato na Zahanati mpya ya kijiji cha Rwele. Ofisi ya Waziri Mkuu imeshakabidhi shughuli za kuratibu maafa hayo kwa kwa Mwenyekiti wa kamati ya maafa ya mkoa huo ambaye ni Katibu Tawala wa Mkoa huo, kwa mujibu wa Sheria ya Maafa ya mwaka 2015 sehemu ya 13(1).


Bila shaka msomaji wa Makala hii unakubaliana na mimi kuwa Maafa ni tukio kubwa ambalo husababisha upotevu wa maisha ya watu, wanyama, majeraha, uharibifu wa mali na mazingira na kuvuruga kabisa mfumo wa kawaida wa maisha ya jamii iliyoathirika na hatimaye jamii kushinwa kukabili hali hiyo kwa uwezo wake wenyewe bila msaada toka sehemu tofauti.

 

Ili kuhakikisha menejimenti ya maafa inakuwa na matokeo chanya, tayari Ofisi ya waziri mkuu inao mradi wa utoaji wa taarifa za tahadhari zinazohusu mabadiliko ya tabia nchi, ili kuchukua hatua za ufuatiliaji, kufanya tathimini na mbinu mbalimbali za kukakabiliana na hali hiyo wakati wa kujenga maendeleo ya nchi.

Lengo la Mradi, ni kuimarisha mifumo ya utoaji tahadhari na taarifa kwa ajili ya kuweka mipango thabiti ya kukabiliana na madhara ya  mabadiliko ya tabia nchi nchini.

Kupitia mradi huo vimejengwa vituo vipya 20 vya upimaji wa hali ya hewa katika Halmashauri 11 za Tarime, Nyamagana, Muleba, Longido, Geita, Maswa, Kigoma, Sikonge, Kongwa, Serengeti, na Kahama. Kuwepo kwa vituo hivyo kutaongeza ufanisi katika upatikanaji wa taarifa za tahadhari hasa kwa majanga ya mafuriko na ukame.

 

Ili matokeo chanya ya shhughuli za uratibu maafa kuwa endelevu jamii lazima iweze kushiriki kikamilifu katika kupunguza athari za Maafa, Serikali haina budi kuijengea jamii husika uwezo wa kupunguza athari hizo.

 

Kupitia mradi huu ofisi ya Waziri mkuu imeandaa  Mipango ya kujikinga na Usaidiaji wakati wa Majanga ambayo imewashirikisha  wadau katika ngazi ya Vijiji, Kata na Wilaya Kama vile katika  wilaya za Liwale (Lindi) na Arumeru (Arusha).

 

Vijana, Kazi na Ajira

Tunafahamu kuwa Vijana ndio wenye nguvu zaidi za kufanya kazi, Vijana ni wabunifu, Vijana ndio chachu ya mabadiliko chanya katika jamii na Vijana ndio warithi wa Taifa.


Hapa nchini asilimia 56 ya nguvu kazi ya Taifa ni vijana. Hivyo, Serikali inatekeleza Programu ya Kukuza Ujuzi na Stadi za Kazi.


Ili kuwawezesha vijana kushiriki katika ujenzi wa uchumi wa viwanda pamoja na kuinua ari ya vijana kupenda kufanya kazi, lakini pia ili kutimiza adhima ya matokeo chanya, Serikali imeshaanza kuchukua hatua za kufanya mapitio ya Sera ya maendeleo ya vijana ya mwaka 2007 kutokana na kupitwa na wakati.

 

Kwa kutambua nafasi ya Vijana katika kuleta maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini, Serikali imetoa mafunzo kwa vijana 9,120 katika fani za stadi za kushona nguo na kutengeneza bidhaa za ngozi.

 

Wapo vijana wenye ujuzi katika fani mbali mbali lakini hawakuwahi kupata mafunzo rasmi, ili kufanya shughuli zao kuwa endelevu serikali imefanya mafunzo ya kurasimisha ujuzi huo uliopatikana kwa mfumo usio rasmi kwa kuwapatia mafunzo ya kukuza ujuzi na stadi za kujiajiri takribani vijana 1,469 wamehitimu mafunzo hayo na kupata ajira.

 

Vijana wengine 7,651 wanaendelea kupata mafunzo kupitia viwanda vya TOOKU GARMENTS, MAZAVA FABRICS, Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT), VETA na Don Bosco.

 

Ni vyema ikaeleweka serikali inalenga kutoa mafunzo ya kukuza ujuzi wa kujiajiri na stadi za kazi kwa vijana 15,350 katika fani mbalimbali katika mwaka huu wa fedha 2017/2018.

 

Shime kijana huna budi kuchangamkia furs hizi na hatimaye kuwa mshirki kikamilifu katika kujenga uchumi wa viwanda.

 

Serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana, imetoa mikopo yenye thamani ya Shilingi bilioni 1.5 kwa vikundi vya vijana 297 katika Halmashauri mbalimbali nchini.

 

Aidha, Mamlaka za Serikali za Mitaa kupitia mapato yake ya ndani zimetoa Shilingi bilioni 4.6 ikiwa ni mikopo yenye masharti nafuu kwa vikundi vya vijana 2,356.

 

Hatua hizi zimekwenda sanjari na utengaji wa maeneo maalum yenye jumla ya ekari 85,603 kwa ajili ya shughuli za vijana za kilimo, biashara ndogo ndogo, burudani na michezo.

 

Haiwezekani vijana wawe wanashinda vijiweni wanacheza pool, wakati wazee na akina mama wapo mashambani wanalima. Kawahimizeni wafanye kazi, wasipofanya kwa hiari walazimisheni kufanya kazi”

Rais Dkt. John Pombe Magufuli, mara bada ya kuwaapisha wakuu wa mikoa, Machi, 2016.

Kwa kauli hiyo ya Mhe. Rais Dkt. John Magufuli tungependa kutoa wito kwa Halmashauri zote nchini kutenga asilimia tano (5) ya mapato yao kwa ajili ya vijana na asilimia tano (5) kwa wanawake, ili waweze kutengeneza ajira zao.


Ifahamike tu, kuwa hadi Machi 2017, jumla ya ajira 418,501 zimezalishwa nchini. Kati ya ajira hizo, ajira 239,017 sawa na asilimia 57 zimezalishwa katika sekta binafsi wakati ajira 179,484 sawa na asilimia 43 zimezalishwa kutokana na shughuli za sekta ya umma ikiwemo miradi ya maendeleo.

Msomaji, huna budi kutambua kuwa ili shughuli ambazo huratibiwa na ofisi ya Waziri Mkuu ziwe na matokeo chanya kwa watanzania hakuna budi ya kuhimiza mahusiano mazuri mahala pa Kazi aidha katika sekta binafsi au Sekta ya umma.

Serikali imefanya utafiti na kubaini kuwa asilimia 58 ya migogoro ya kikazi inatokana na kutozingatiwa kwa taratibu za kuachisha kazi. Sekta zinazoongoza kwa migogoro ya kazi ni usafirishaji, ujenzi, ulinzi binafsi, elimu, huduma za hoteli na viwanda.

Katika kupunguza migogoro mahali pa kazi, Serikali imefanya kaguzi na kusimamia uundwaji wa Mabaraza ya Wafanyakazi.

Aidha, Tume ya Usuluhishi na Uamuzi imeendelea kutimiza wajibu wake wa kusuluhisha migogoro ambapo katika kipindi cha Julai 2016 hadi Februari 2017, Tume imesajili jumla ya migogoro 8,832 kati ya hiyo migogoro 3,319 sawa na asilimia 37.6 ya migogoro yote iliyosajiliwa imesuluhishwa.

 “Waajiri na waajiriwa wote nchini, zingatieni Sheria za Kazi na imarisheni uhusiano mzuri kwenye maeneo ya kazi, ili muda mwingi zaidi utumike kwenye uzalishaji mali badala ya kutatua migogoro. Vilevile, ni muhimu sana muimarisha kaguzi za kazi na kuendelea kusaini mikataba ya kuunda na kusajili mabaraza ya wafanyakazi ili kuimarisha zaidi mahusiano mahali pa kazi

Rais Dkt. John Pombe Magufuli, Siku ya Wafanyakazi Duniani, Mei, 2017.

 

Huduma kwa Watu Wenye Ulemavu

Ofisi ya Waziri Mkuu kama mratibu wa shughuli za serikali imeendelea kutoa huduma pamoja na kuongeza upatikanaji wa haki na fursa kwa watu wenye ulemavu, tayari imewaagiza Wakuu wa Mikoa kuhakikisha kuwa Kamati za Watu wenye Ulemavu zinaanzishwa katika ngazi za Mikoa, Wilaya, Mitaa na Vijiji.

 

 

 Baadhi ya wanajamii huwanyanyapaa watu wenye ulemavu, kwa  kulitambua hilo tunaendelea kuratibu  kampeni za kupinga unyanyapaa na vitendo vya kikatili dhidi ya watu wenye ualbino katika mikoa ya Shinyanga, Mwanza, Geita, Simiyu, Kagera, Tabora, Kigoma, Mara, Mbeya, Katavi na Rukwa na kampeni hiyo itaendelea nchi nzima.

 

Tunatambua kuwa Mawasiliano ni njia pekee ya kuifanya jamii kushiriki kikamilifu kwa maendeleo. Kama tujuavyo baadhi ya wana jamii wenye ulemavu wa kutosikia wamekuwa wanashindwa kupata huduma ya mawsiliano hasa kupitia Vituo vya Televisheni kwa kuwa hutumia lugha ya alama.

 

Serikali inahakikisha kwamba watumiaji wa lugha ya alama wanapata haki ya kupata habari na vituo vyote vya televisheni vimeelekezwa kutumia wakalimani wa lugha ya alama.

 

Watu wenye ulemavu wanaendelea kupata huduma ikiwa ni pamoja na kutoa vifaa saidizi kwa wanafunzi wenye ulemavu shuleni na vifaa vya kufundishia.

 

 


Katika masuala mtambuka ambayo Ofisi hii huyaratibu ni Vita dhidi ya UKIMWI, Kwa kuwa suala hili linahitaji jitihada elekezi za wadau mbalimbali ili kuweza kushinda vita hii.

 

Ili kuishinda vita hii nyenzo ya msingi ni rasilimali fedha, Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Tume ya Kudhibiti UKIMWI, Tazania (TACAIDS), mnamo Desemba 2016 ilizindua Mfuko wa Udhamini wa UKIMWI ulioanzishwa na Serikali miaka miwili iliyopita.

 

Kupitia harambee iliyofanyika kwa ajili ya kuchangia Mfuko huo, shilingi milioni 347 zilipatikana kama ahadi. Vilevile, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 5.6 kwa ajili ya Mfuko wa UKIMWI.

 

Serikali inaendelea kutoa huduma kwa Watu Wanaoishi na Virusi vya UKIMWI (WAVIU) ambapo hadi Desemba, 2016 WAVIU 839,574 sawa na asilimia 63 ya WAVIU wote, walikuwa wamepatiwa dawa. Juhudi zinaendelea kufanyika ili kuwahamasisha WAVIU kujitokeza na kuingia kwenye Mpango wa Tiba ya Kufubaza Athari za UKIMWI.

 

Ili vita hii tuweze kuishinda lazima tuwe na mikakati endelevu, tayari serikali imekamilisha uandaaji wa miongozo minne ya Taifa ya Kudhibiti UKIMWI ikijumuisha Mpango Kazi wa Kinga, Mkakati wa Kondomu, Mkakati wa Uwekezaji na Mpango kazi wa jinsia.

 

Tunatambua kuwa suala la UKIMWI ni mtambuka na ambalo huihitaji juhudi za makusudi kupambana nalo kwa sekta zote za umma na binafsi, ili vita hii iwe na matokeo chanya,  serikali imeirisha uratibu wa afua za UKIMWI kwa wadau wote wa sekta ya umma na binafsi na kupitia mifumo ya uratibu iliyoanzishwa.

 

Serikali kwa kushirikiana na wadau pia inaendelea kujenga uwezo Kamati zilizo katika ngazi ya jamii hususan vijiji na kata ili kufikia malengo ya kitaifa na kimataifa ya kupunguza na kumaliza UKIMWI ifikapo mwaka 2030 kwa kutumia mfumo ulio katika jamii.

 

Vilevile, Serikali itakamilisha utafiti wa nne wa kubainisha viwango vya maambukizo ya UKIMWI nchini na kuboresha ushiriki wa sekta binafsi ili kuleta ufanisi katika kuchangia mwitikio wa Taifa dhidi ya UKIMWI.

 

Tunatoa wito kwa watanzania wote kushirikiana katika kutokomeza maabukizi mapya ya UKIMWI nchini.

 

Takwimu zinaonesha kuwa maabukizi mapya yameshuka kwa asilimia 50 mkwa watoto miongoni mwa watoto duniani 290,000 wapya walioambukizwa mwaka 2010 na watoto wapya 150,000 waliambukizwa mwaka 2015. Maambukizo mapya kwa watu wazima hayajashuka tangu 2010 duniani.

 

Tuungane Kutokomeza Maambukizo Mapya ya Virusi vya UKIMWI”

 

 

Vita Dhidi ya Dawa za Kulevya

Dawa za kulevya zinaathiri maisha ya vijana wetu wengi na hivyo kuzima ndoto za maisha yao na kupunguza nguvu kazi ya Taifa. Suala hili linaoneka kumgusa Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, wakati wa hafla ya kuwaapisha Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania ambapo alitoa wito kwa vyombo vya ulinzi kuendeleza vita dhidi ya biashara haramu ya dawa za kulevya nchini.

 

“Madawa ya Kulevya yanapoteza nguvu kazi za watanzania hasa vijana, hivyo hii kazi si ya mtu mmoja ni ya wanzania wote kushirikiana kwa pamoja katika kupambana na jambo hili kwa manufaa ya nchi”


Rais Dkt. John Pombe Magufuli, Februari, 2017.

 

Katika kuhakikisha matokeo chanya katika hili la kupambana na janga hilo, Ofisi ya waziri Mkuu kama mratibu wa shughuli za serikali Bungeni, Tayari Bunge limefanya marekebisho ya Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya Na. 5 ya Mwaka 2015.

 

Marekebisho hayo yameipa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nguvu ya kukamata, kupeleleza na kushitaki watuhumiwa wanaohusika na biashara ya dawa za kulevya.

 

katika kipindi cha Julai, 2016 hadi Januari, 2017 watuhumiwa 11,303 walikamatwa kwa tuhuma za kujihusisha na uzalishaji, usambazaji, uuzaji na matumizi ya dawa za kulevya katika sehemu mbalimbali nchini.

 

Kati ya watuhumiwa hao, watu 9,811, walikutwa na kesi za kujibu ambapo 9,174 wametiwa hatiani, 238 hawakukutwa na hatia na wengine 478 upelelezi wa kesi zao unaendelea. Pia tangu Tume mpya iundwe Februari mwaka huu, jumla ya watuhumiwa 79 wametiwa mbaroni na uchunguzi wa kesi zao unaendelea.

 

Tunaamini kwa jinsi tulivyo dhamiria kkutratibu kwa matokeo chanya kwa watanzania wote , ni imani yetu  kuwa, Mamlaka ya Udhibiti wa Dawa za Kulevya itaendeleza kwa kasi zaidi juhudi za kupambana na uingizaji, uzalishaji, usambazaji na matumizi ya dawa za kulevya hapa nchini.

 

Pamoja na kuwa shughuli za uratibu kuwa imara lakini bila jamii kushiriki kikamilifu hatuwezi kufanikiwa hivyo tunatoa wito wazazi kuwa karibu na vijana wao na kufuatilia nyendo zao ili wasiingie kwenye mtego huu wa dawa za kulevya.

 

Tunahitaji taifa la watu wenye afya njema ili waweze kushiriki kikamilifu katika kujenga uchumi wa viwanda kama ilivyo dhamira ya seerikali ya awam ya tano amabao pia inasisitiza watu kufanya kazi.

 

Tunaamini msomaji wa Makala hii umeweza kuelewa kwa jinsi tulivyodhamiria na kuweza kuratibu shughuli za serikali ndani nan je ya Bunge pamoja na masula mtambuaka. Aidha , kwa kuwa Makala hizi zinaendelea Kutolewa na Taasisi za serikali hasa nasi tunaamini taasisi amabazo zipo chioni ya Ofsis ya Waziri Mkuu zitafafanua kwa kina utekelezaji wa mipango na mikakati yao.


Tataendelea kukuhudumia kwani Dira yetu ni kutoa huduma bora za Serikali kwa umma na dhima inayotekelezwa sasa ni kuhakikisha malengo ya Serikali yanafikiwa kwa kuratibu sekta zote kwa ufanisi na tija.


“Tumedhamiria, Tunaratibu Kwa Matokeo Chanya nchini.”
Read More