Sunday, December 17, 2023

PAROKIA YA KIWANJA CHA NDEGE YAWAKUMBUKA WAATHIRIKA HANANG

 


Padre Emmanuel Mtambo wa Kanisa Katoliki Parokia ya Mwenyeheri Maria Theresa Ledochowaska amesema Kanisa linawajibu wa kuchangia watanzania wenzetu waliopata janga la mafuriko ya Mawe na Matope kutoka Mlima Hanang’.

Alisema Parokia ya Mwenyeheri Maria Theresa Ledochowaska Kiwanja cha Ndege kupitia kamati ya Caritas ambayo inashughulikia wanaohitaji, leo  jijini Dodoma imetoa hundi ya shilingi milioni 5 ikiwa ni sehemu ya kushirikiana na serikali kusaidia waathirika.

“Kama Parokia na Kanisa; tunapaswa kufanya sehemu yetu, kupitia michango yetu tunayotoa katika akaunti ya Caritas” alifafanua

Mchango huo umepokelewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya waziri Mkuu, (Sera Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama


Read More

Thursday, December 14, 2023

WATUMISHI WA OFISI YA WAZIRI MKUU, WAASWA KUFANYA KAZI KWA KUSHIRIKIANA

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama ametoa wito kwa watumishi walio chini yake kufanya kazi kwa kutegemeana na kushirikiana bila kutengeneza makundi.

Ametoa rai hiyo Mkoani Morogoro wakati akifungua kikao cha Baraza la wafanyakazi la Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na uratibu kilicholenga kujadili Taarifa ya Bajeti ya 2023-2024 ya Ofisi hiyo.

Waziri Mhagama alisema, Kuna kila sababu ya kufanya maamuzi ya pamoja ya ushirikishwaji ili kuweza kupata mafanikio kwenye idara na vitengo, kama viongozi wenu wanavyofanya kazi vizuri kwa kushirikiana.

Aliendelea kusema kuwa hata kama inafikia wakati Mtendaji hayupo kwenye Idara au kitengo kuwe kuna Mtu anayeweza kufanya kazi kwa viwango na uwezo huo huo ili mambo yaweze kwenda vizuri.

“Tukifanya kazi kwa umoja na ushirikiano tukifanikiwa tuwe tumefanikiwa wote na tukianguka tujue tumeanguka wote na tujipange ili kujua sababu ya kuanguka na tuweze kujipanga." Alibainisha.

Aidha, Waziri Mhagama alisema anafarijika na utendaji wa kitaasisi na kuwaomba watumishi kuendelea kuimarisha utendaji wa kitaasisi ambao unatoa fursa kwa kila mtu kuwa ni sehemu ya mafanikio na ufanisi wa taasisi.

“Wale ambao Mnamadaraka kwenye Idara Vitengo au Taasisi zetu Muhakikishe Mnajenga moyo wa kukuza watumishi walio chini yenu, kwa kuwapa fursa ya kukua kielimu ndani ya ofisi, kukua kiujuzi na kukua kiubobezi." Alihimiza.

Alibainisha kuwa Watumishi wa umma ni rasilimali muhimu, ya kuendesha rasilimali nyingine na kusema kuwa ni lazima tuiratibu vizuri Rasilimali hiyi na kuilinda kwa nguvu zote ili kuweza kupata mafanikio tuliyoyakusudia.

Waziri alisema; Rais wa awamu ya tatu Mhe. Benjamini Mkapa aliwahi kusema,” jambo muhimu kwa mfanyakazi si muda anaotumia kufanya kazi,bali kiasi cha kazi anachoweza kufanya katika muda aliopewa."

Alisema Kuna kila sababu ya kuanzaa kujipima wenyewe hasa katika kuelekea kuanza mwaka 2024, ili kujua kiasi cha kazi tuliyoifanya na ufanisi wake kila siku anayoshiriki kama mtumishi wa umma katika ofisi ya waziri Mkuu.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi, amesema vikao vya wafanyakazi ni tamko la kisheria ambalo chimbuko lake ni Hayati Baba wa Taifa mwalimu Julius Nyerere, Rais wa awamu ya Kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alilolitoa katika tamko no 1 la mwaka 1970 linalohimiza ushirikishwaji kupitia Baraza la wafanyakazi.

 

"Baraza ni kiungo muhimu kati ya wafanyakazi na Menejimenti na Ofisi ya Waziri Mkuu, tutaendele kuwa vikao hivi vya baraza la wafanyakazi kwa mujibu ya miongozo.

Awali akitoa salamu Katibu wa TUGHE Mkoa wa Dodoma Bw. Samwel Nyungwa ameipongeza Menejimenti ya Ofisi ya Maziri Mkuu, kwa kutekele za Sera ya ushrikishwaji kikamilifu,

Chama cha wafanyakazi kinaamini hakuna haki bila wajibu, tunaangalia namna tunavyopata haki na namna ambavyo tunatekeleza wajibu katika kuhakikisha mipango iliyopangwa inakamilika sawasawa.

Read More

Wednesday, December 13, 2023

SERIKALI YAAHIDI KUFANYA JITIHADA ZAIDI KATIKA UREJESHAJI HALI KATIKA MITAA, HANANG


 

Serikali imesema zoezi la ufunguaji wa mitaa katika mji wa Kateshi limefika 85% na mkazo mkubwa umewekwa katika kutoa udongo kwenye vipenyo vya vya mtaa kwa mtaa na nyumba kwa nyumba.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama katika mahojiano maalumu aliyoyafanya na shirika la utangazaji la Taifa TBC leo Hanang Manyara

Waziri alisema katika zoezi hilo malori makubwa zaidi ya 30 yalisaidia kutoa tope lenye mawe miti pamoja na udongo, katika barabara kuu ya Katesh Singida.

“Malori yenye uwezo wa kubeba magunia 130 yamefanya safari zaidi ya 400 ya kutoa Tope kutoka kwenye viunga vyote vya Mji wa Katesh,” alibainisha.

Waziri amefafanua kwamba, vifaa tulivyonavyo haviwezi kuingia kwenye vipenyo vya mtaa kwa mtaa au nyumba kwa nyumba na hivyo tunalazimika kutumia nguvu kazi, na tunafanikiwa.

Halikadhalika tunafikiria kushirikisha wananchi kujitokeza kusaidia zoezi la uondoaji wa tope hasa kwenye hifadhi ya barabara ili tuweke hali katika usalama zaidi.

“Tunafanya tathimini na kuendelea kuchukua tahadhari mvua nyingine ikinyesha, ikiwa ni pamoja na kurudisha mto uliopokea mawe na matope ambao njia yake ilifunga na kutengeneza mapito mengine,”alifafanua.

Kwa upande wake Mkazi wa Katesh, Bi, Halima Rashidi amesema Mawe na tope yaliyoletwa na Mlima Hanang yaliathiri kwa kiasi kikubwa miundo mbinu na makazi ya watu.

“Msaada wa serikali umekuja kwa wakati na haraka, watu wana moyo wa kufanya kazi kwa sababu jitihada zao zimeokoa maisha ya watu na mali,” alibainisha

Read More

Tuesday, December 12, 2023

UREJESHAJI WA MIUNDOMBINU YA BARABARA KATIKA MJI WA KATESH WAFIKIA ASILIMIA 75


Naibu Waziri wa Ujenzi, Eng. Godfrey Kasekenya amesema hadi sasa urejeshaji wa miundombinu ya barabara na makalvati iliyokuwa imeharibiwa na maporomoko ya tope na mawe yaliyotokea Disemba 3, 2023 kwenye Mji wa Katesh wilayani Hanang mkoani Manyara umefikia asilimia 75.

Kasekenya amesema hayo Mkoani Manyara mara baada ya kukagua maendeleo ya utekelezaji wa kazi hizo zinazofanywa na Wakala ya Barabara (TANROADS) wakishirikiana na Wakala ya Barabara za  Vijijini na Mijini (TARURA).

"Hadi sasa tumefikia karibu asilimia 75 ya kuirejesha Katesh katika hali yake na tutakachofanya kabla ya kuondoka tutakuwa tumehakikisha tumesafisha barabara zote na kuzirudisha katika hali yake ya awali kama tulivyokuwa tumeagizwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan", amesema Kasekenya.

Kasekenya ameongeza kuwa mitambo na magari imeshafika eneo la Katesh ambapo kuna magari 32 yenye uzito wa tani 13, vijiko 12, doza 3, magari ya kishindilia barabara mawili, mitambo ya kubeba matope (roller) mawili, na mitambo yote hiyo inaendelea kufanya kazi usiku na mchana.

"Ninaposema magari yenye uzito wa tani 13 na yale yenye uwezo wa kubeba magunia 130 kwa wakati mmoja na mpaka sasa magari hayo yameweza kubeba Tripu za tope na mawe zaidi ya 4,000 na kazi bado inaendelea", amefafanua Kasekenya

Amesema Wizara hiyo kupitia Wakala hizo wanaendelea kufungua barabara za mitaa kwa ajili ya kuhakikisha njia zinafunguka kwa kutoa mawe na magogo ili kuhakikisha kama kuna mali za watu zilisalia katika makazi yao wanaweza kuingia na kufanya usafi.

"Kwahiyo kazi kubwa ambayo tunafanya sisi Wizara, TANROADS na TARURA ni tumejipangia mpaka kufikia kesho tuwe tumefikia walau asilimia 95 katika kurejesha hali", amesisitiza Eng. Kasekenya.

Naye Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Mhe. Jenista Mhagama amesema kuwa mbali na Serikali kurejesha miundombinu pia imeendelea kuwa bega kwa bega na Wananchi sambamba na kutoa maagizo kwa Wataalamu wa Satellite kuanza kuangalia Kaya zote na kuona zipi zimeathirika zaidi huku ikiendelea kutoa msaada zaidi.

"Kiu ya Mhe. Rais ni kuona wale ambao wamepoteza makazi tunaipata hesabu yao vizuri ili Serikali ianze mchakato wa makazi mapya kwa waathirika hao", amefafanua Mhe. Jenista.

Aidha, Waziri Jenista ametoa shukrani zake kwa juhudi kubwa za uokoaji lakini pia kwa ushirikiano  wa Viongozi wote wa Mkoa, Wilaya na Serikali za mitaa kwa kuendelea kutatua changamoto sambamba na kuwapatia mahitaji muhimu ya kibinadamu waathirika wote wa maporomoko ya tope na mawe waliopo kambini lengo likiwa ni kurejesha faraja tena," amesema Jenista.

Wakati huo huo, Naibu Waziri Ofisi ya Rais - TAMISEMI anayeshughulikia masuala ya Afya Dkt. Festo Dugange amesema kuwa waathirika wa Maafa ya maporomoko ya tope 117 wameendelea kupatiwa matibabu bure tangu kutokea kwa maafa hayo hadi leo  kwa gharama ya Serikali katika Hospitali ya Mkoa, Wilaya na Kituo cha Afya cha Gendabi.

"Mhe. Rais tayari amekwishaleta fedha zaidi ya Milioni 560 kwa ajili ya kununua dawa na vifaa tiba lakini pia kununua madaawa kwa ajili ya kinga ya mlipuko wa magonjwa", amesema Dkt. Dugange.

Wakitoa neno la shukrani kwa Serikali wakazi wa Katesh akiwemo Emmanuael Joseph ameipongeza Serikali kwa namna ilivyoratibu suala hilo na kueleza kuwa imewapa faraja na matumaini mapya kwa kuzingatia misaada waliyopewa na namna walivyohudumiwa.

“Tunamshukuru Mhe Rais alivyotusaidia wakati wa maafa na wamefungua barabara sasa tunaweza kufanya biashara zetu ili kujiletea maendeleo yetu na Taifa kwa ujumla,” alisema

Naye Mkazi wa Katesh A, Budila Mkenda ameeleza namna Serikali ilivyowasaidia ikiwemo kuwafikiwa kwa haraka na kupata misaada kwa wakati hii inaonesha namna viongozi wetu wanajali.

 

Read More

Monday, December 11, 2023

UREJESHAJI HALI HANANG’ WAENDELEA

Wananchi wapokea kwa muitikio chanya zoezi la kuhifadhi waathirika wa Maporomoko ya mawe na matope kutoka Mlima Hanang kwa kushrikiana na serikali. Uratibu wa zoezi hilo unaenda sanjari na ugawaji wa vifaa vya msaada wa kibinadamu kwa waathirika wa maafa hayo.

Hatua hiyo inaenda sambamba na hali ya urejeshaji hali katika Mji wa Katesh, Halmashauri ya wilaya ya Hanang Mkoani Manyara, huku shughuli ya uondoaji wa tope katika barabara na mitaa ya Mji wa katesh ikiendelea.

Read More

Saturday, December 9, 2023

UMOJA WA MAKANISA YA CPCT YAFARIJI WAATHIRIKA WA MAAFA HANANG’

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama ameishukuru uongozi wa umoja wa Makanisa ya Kipentencoste Tanzania (CPTC) kwa namna walivyoendelea kuonesha upendo kwa kuchangia mifuko 500 ya saruji kwa waathirika wa maafa ya maporomoko ya tope na mawe kutoka Mlima Hanang’ mkoani Manyara na kuendelea kuwaombea waathirika hao.

Ameyasema hayo mapema katika ibada iliyoandaliwa na umoja wa makanisa hayo iliyofanyika katika kanisa la DNPC-Katesh.

Waziri Mhagama alishukuru namna kanisa linavyoendelea kusaidia jamii katika malezi ikiwemo kuwalea kiroho na kusema hii inasaidia Serikali kuwa na vijana na Taifa lenye maadili mema.

“Kanisa ni taasisi muhimu sana, endeleeni kutushauri pale inapobidi na ninawashukuru namna mmeendelea kuungana nasi katika maafa haya kwa kutoa mifuko ya Saruji nasi tutaiwasilisha niwahakikishie itatumika kwa malengo yaliyokusudiwa na kwa usimamizi mzuri wa Serikali yetu,” alisema Mhe Mhagama

Mwenyekiti wa Makanisa ya Kipentencoste Tanzania (CPTC) Dkt. Barnabas Mtokambali ameshauri jamii kuendelea kuwaombea waathirika wa maafa hayo huku akitoa rai kuona umuhimu wa kuwapa msaada kwa namna yoyote ili kusaidia na kuonesha upendo kwa matendo lengo ni kuendelea kushikamana kama Watanzania.

“Ni wakati sahihi kuwakimbilia ndugu zetu hawa, tuwaoneshe upendo na Serikali imechukua jukumu hili nasi tuungane nao kwa kuwasaidia ndugu zetu na tukumbuke bado serikali inawahudumia hata wakiwa katika makazi yetu,” alisema Mchungaji Mtokambali

Ametahadharisha uwepo wa changamoto kadhaa zinazoweza kusababishwa na mikusanyiko ikiwemo magonjwa ya milipuko, mmomonyoko wa maadili na tabia zingine zisizofaa na kuwaomba waumini na jamii kwa ujumla kuendelea kuwaombea na kuwastiri kwa namna mbalimbali.

 Naye Mbunge wa Hanang’ Mhe. Mhandisi Samwel Hayuma alieleza kuwa amefarijika kwa namna kanisa lilivyowakimbilia na kuendelea kuwaombea katika mapito ya maafa yaliyotokea Wilayani Hanang’.

Aidha alimshuku Mhe Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kujali na kutoa maelekezo kwa viongozi wake kuratibu na kuhakikisha hali inarejea katika nafasi yake.”

 “Mhe Waziri mhagama wewe ni mpambanaji kweli, umefanya kazi kubwa katika kuratibu maafa haya, hakika Serikali inafanya kazi nzuri sana na hii imetupa faraja kubwa kuona Serikali yote ipo hapa Hanang’ tunasema asanteni sana,” alisisitiza Mhandisi Hayuma

Aidha alitumia nafasi hiyo kuwaasa Watanzania kuungana Pamoja kuendelea kumuombea mbeba maono wa nchi hii ambaye ni Mheshimiwa Rais kwa namna anavyotuongoza Pamoja na wasaidizi wake wote.

“Tuone umuhimu na haja ya kuendelea kumuombea sana Rais wetu na viongozi wote wa nchi yetu, Tanzania ni nchi nzuri yenye upendo wa hali ya juu, Tuendelee kuiombea Hanang’ yetu, Manyara yetu na Nchi kwa ujumla,” alisema

 

 

Read More

SPIKA WA BARAZA LA WAWAKILISHI ZANZIBAR AWAPA POLE WANA HANANG’


Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar Mhe. Zubeir Maulid ameipongeza kazi kubwa iliyofanywa na Serikali na Wananchi waliojitolea kusaidia Waathirika wa maafa ya maporomoko ya mawe na tope kutoka Mlima Hanang’ mkoani Manyara.

Ametoa kauli hiyo alipongoza ujumbe kutoka baraza la wawakilishi kutoa Msaada wa kibinadamu kwa waathirika wa maporomoko hayo katika Halmashauri ya wilaya ya hanang yaliyotokea Disemba 3, 2023.

Alieleza kwamba, jambo hili limeonesha kiasi gani nchi yetu ina umoja hususan tunapopata matatizo na namna gani tunashirikiana kama ndugu kulitatua.

“Tumekuja tumeleta kiasi cha shilingi milllioni 30 tunajua mahitaji ni makubwa lakini kidogo kidogo, tukiunganisha nguvu zetu jambo litakuwa kubwa ili isaidie waathirika, “alibainisha.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama amewashukuru, baraza la wawakilishi kwa msaada wa kibinadamu walioutoa kwa waathirika.

“Jambo hili limeonesha kwamba Muungano wetu si Muungano wa maneno bali ni Muungano  wa vitendo,” alifafanua Waziri Mhagama

Aliongezea kuwa Serikali itaendelea kuratibu vyema suala hilo na kuhakikisha kila mchango unatumika kwa lengo lililokusudiwa na si vinginevyo na kuongezea kwamba watadhibiti kila mianya ya ubadhilifu na kusisitiza kuwa kwa yeyote atakayefuja michango hiyo hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake.

Read More

Friday, December 8, 2023

“HAKUNA HAKI YA MUATHIRIKA WA MAAFA YA HANANG’ ITAKAYOPOTEA,” SERIKALI


 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama ametoa wito kwa wananchi kushirikiana na serikali kuwahifadhi waathirika wa Maporomoko ya Mawe na Matope kutoka Mlima Hanang’ mkoani Manyara.

Kauli hiyo ameitoa wakati wa kikao na viongozi wa Serikali, Wazee na Waathirika wa Maporomoko hayo katika Kijiji cha Gendabi Halmashauri ya wilaya ya Hanang’ Mkoani humo.

Alitumia fursa hiyo kuwakumbusha kuwa Serikali itaendelea kutoa huduma zote muhimu kwa kila aliyeathirika na maafa hayo na kipaumbele ni wale waliohifadhiwa katika Kambi za muda zilizopo na endapo kuna mazingira rafiki ya kuhifadhiwa na ndugu, jamaa na marafiki wanapaswa kufuata utaratibu zilizopo.

“Tunahitaji kupunguza mikusanyiko mikubwa kwenye makambi kiafya siyo sahihi tutahakikisha tunamhudumia kila Muathirika popote atakapokuwa amehifadhiwa na ndugu au Jamaa na hakuna haki yake itakayopotea,” alibainisha 

Aidha alishauri kuwa, Wananchi wawapokee waathirika wa Maporomoko ya Mawe katika makazi yao na hata kama nyumba itakuwa haitoshi serikali itawezesha kujenga mahema ili waweze kujitosheleza.

Alifafanua zaidi kuwa lengo la serikali ni kuhakikisha vifaa vya msaada wa kibinadamu vinawafikia waathirika katika maeneo yao kwa kuhakikisha wanapata mahitaji muhimu ikiwemo chakula, magodoro pamoja na mablanketi.

“Sio kweli kwamba Muathirika wa maporomoko ya Mawe na Matope akienda kwa ndugu zile stahiki zake atakosa, cha msingi ni kuainisha eneo analokwenda kwa anuani, majina viongozi wake pamoja na mawasiliano yao,”alifafanua.

Kwa upande wake Nyerere Izrael Mwenyeji wa kijiji cha Gendabi ameomba serikali kutuma wataalamu kuangalia tabia za Mlima Hanang’ ili janga hilo lisije likajirudia.

 

“Wataalamu watasaidia kutupa taarifa za awali kama eneo ni salama au si salama kuendelea kuishi bila kuleta taharuki kwa wananchi” alizungumza

Awali Bwana Steven Sulle Mwenyekiti wa CCM Kata Gendabi, amemshaukuru, Mhe Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema ni Rais wa kipekee kabisa ameonesha upendo na kutoa faraja katika madhila haya.

“Niipongeze Serikali kwa kutukimbilia sisi tunawashukuru sana, ila nashauri wale waathirika wenye uwezo wa kwenda kwa ndugu , jamaa na marafiki watumie utaratibu uliopo na ni sahihi kuwapokea kwa upendo, tunavyoendelea kuwaacha katika eneo la Kambi, wataendelea kuwa wapweke zaidi,” alisema.

Read More

Wednesday, December 6, 2023

WANANCHI KATESH, WAISHUKURU SERIKALI KWA VIFAA VYA MSAADA WA KIBINADAMU

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama amesema misaada yote inayotolewa na wadau mbalimbali itawafikia walengwa walioathirika wa poromoko ya matope kutoka Mlima Hanang’.

Kauli hiyo ameitoa wakati alipozindua zoezi la ugawaji wa vifaa vya msaada wa kibinadamu kwa familia 205 zilizoweka makazi ya muda katika shule ya sekondari ya Katesh iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Hanang Mkoani Manyara.

Chochote tutakachokipata tutakigawa kwa walengwa kwa sababu hili zoezi ni sehemu ya majukumu yetu na tutalitekeleza kwa uaminifu mkubwa.

“Atakayefanya ubadhilifu wa aina yoyote, serikali haitakuwa na uvumilivu naye, tutachukua hatua,” alibainisha Waziri

Serikali ipo pamoja na nyie, tunajua maswahibu mliyoyapata: wengi wenu mlishapiga hatua za kimaisha, lakini janga hili limeturudisha nyuma, kikubwa tuwe na moyo wa subira kwa mwenyezi Mungu kwa kuendelea kutulinda.

“Kazi kubwa ilikuwa ilikuwa ya kukabiliana na janga lilipotokea na hatua ya pili ni kurudisha huduma za kijamii na miundo mbinu ya mawasiliano, katika hali ya kawaida,” alifafanua

katika hatua nyingine waziri Mhagama ameishukuru shirika la umeme TANESCO kwa kurudishia transfoma 76 zilizokuwa zimeharibika na nguzo zaidi ya 60 na hivyo kusaidia kijiji cha Gendabi kilichoathirika na Maporomoko.

“Niwaombe sasa muanze kufanya ufuatilaiji wa nyumba zote zilizokuwa zinapata nishati ya umeme ili wananchi wandelee kupata huduma hiyo alisema,” Waziri.

Awali Luteni Kanali Selestine Masalamadu Mkurugenzi Msaidizi idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, amesema kila familia itapata magodoro 3; masufuria 5, sabuni za miche pamoja na sabuni za unga na nguo za watoto.

Kwa upande wa Bi, Betha Mmari Mwananchi aliyepata adha ya mafuriko ameishukuru serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na kwa Mama Samia kwa Kujali.

“Tunaomba muendele kutuhudumia katika kipindi hiki kigumu kwetu na msituache” alisema

 

Read More

Tuesday, December 5, 2023

WADAU WAENDELEA KUJITOKEZA KUCHANGIA MAAFA HANANG’


 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama ameelekeza watendaji wa Idara ya Menejimenti ya Maafa katika ofisi hiyo kuhakikisha wanaweka utaratibu wa kimfumo ili misaada yote iingie kwenye mfumo rasmi ili iweze kuwafikia wale waliokusudiwa.

 

Ametoa kauli hiyo wakati akipokea vifaa vya msaada wa kibinadamu vilivyowasilishwa na wadau mbalimbali kusaidia wahanga wa maafa yaliyotokana na maporomoko ya mawe na tope kutoka mlima Hanang Mkoani Manyara.

 

Waziri Mhagama alisema Serikali imepokea misaada hiyo huku akishukuru kwa niaba ya Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan na kuwahakikisha kuwa misaada hiyo itasimamiwa kwa ukaribu ili kuhakikisha inaleta tija kwa wahusika.

 

“kipekee niwapongeze na kuwashukuru sana kwa namna mlivyoguswa na kuungana na Serikali katika kuwanusuru ndugu zetu waliopatwa na maafa haya, Hanang Tunawashukuru sana,” alisisitiza

 

Alitumia nafasi hiyo kutoa onyo kwa yeyote atayejaribu kufanya utapeli au kujinufaisha isivyo halali katika kipindi hiki.

“Tumewaonya matapeli wasije wakathubutu kutengeneza akaunti za utapeli kwa sababu tutawakamata na serikali itachukua hatua kali za kisheria,” alibainisha

 

Waziri Mhagama alitumia nafasi hiyo kueleza umma kuwa Serikali imetoa akaunti sahihi ya kutuma michango ya kifedha kwa ajili ya masuala ya maafa ambapo ni kwa akaunti ya bank yoyote ya ndani au nje ya nchi.

“Kwa ajili ya kukabiliana na maafa ya Katesh itatumika  Akounti ya Mfuko wa Taifa wa Usimamizi wa Maafa (National Disaster Management Fund Electronic Account) Na. 9921151001 kwa kuandika neno maafa likifuatiwa jina la Wilaya ya Hjanang’.

 

Halikadhalika alitoa rai kwa watumishi watakaohusika na misaada itakayotolewa kuhakikisha wanafanya kazi kwa uaminifu ili misaada iwafikie walengwa.

 

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Kupitia Chama Cha Mapinduzi Mhe.Mary Chatanda alisema anatoa pole kwa niaba ya Umoja wa wanawake Tanzania kwa tukio hilo lenye kuleta majonzi na huzuni kubwa kwa wana Hanang’,  jamii na Taifa kwa ujumla.

 

Tunashukuru wafadhili mbalimbali wameweza kutuchangia, tumekuja na Mablanketi 120, mashuka 300, mashuka ya kimasai 500, madira ya kuvaa wanawake 520, kanga 1000, katoni za sabuni na mafuta ya kupaka,” alisema

 

Aidha alitoa rai kwa jamii, wadau mbalimbali kuendelea kujitokeza kusaidia ili kuwapa nafuu waliofikwa na maafa hayo.

 

“Wabunge wetu wa viti maalum nao wamesaidia kuchangia kupitia kwa Ktibu wao wa wabunge na fedha hizo tutawasilisha baadae,” alieleza Mhe. Chatanda
Read More

Saturday, December 2, 2023

“WAHITIMU CHUO CHA BIBLIA MUWE MABALOZI WAZURI WA KUSIMAMIA MAADILI” WAZIRI MHAGAMA


 Wahitimu wa Chuo cha Biblia cha Evengelism Church wameaswa kuwa askari wazuri wa vita dhidi ya mmomonyoko wa maadili ambao unaendelea kushamiri katika jamii zetu hususani kwa vijana.

Wito huo umetolewa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe, Jenista Mhagama wakati wa mahafali ya 83 ya chuo hicho yaliyofanyika, Sakila Katika wilaya ya Meru Mkoani Arusha.

Waziri aliwaambia wahitimu hao kwamba maendeleo ya taifa letu yanategemea sana nguvu kazi na nidhamu ya kazi, japokuwa nchi yetu haiegemei upande wowote katika maswala ya dini, lakini sehemu kubwa ya watu wake wanaamini katika dini kupitia madhehebu mbalimbal

 “ni muhimu mkawe mabalozi wazuri katika vita hii na mkashirikiane na viongozi wengine wa dini na Serikali ili kwa pamoja tuhakikishe tunalilinda taifa letu dhidi ya upotofu huu wa maadili” alibainisha.

Aidha, aliwasihi kuendelea kuliombea taifa amani, utulivu, upendo na mshikamano ili kulijenga taifa.

Waziri ametumia maandiko matakatifu, katika Injili ya Matayo (Sura ya 5:13-16) ambayo yalisema, nami pia niwasihi popote mnapokwenda, mkawe chumvi ya dunia na kamwe msipoteze ladha ya chumvi lakini pia mkawe mwanga wa ulimwengu ukaangaze mbele ya watu ili wayaone matendo yenu mema wamtukuze baba yenu aliye mbinguni.

“Sina shaka kwamba, wote mkitoka hapa mtakwenda kutekeleza jukumu la kichungaji na kufundisha watu kwa upendo, uaminifu na kuwaongoza katika kweli maana huo ndio wito mlioitiwa,” alifafanua

Kwa upande wake Dkt. Eliud Issangya, Askofu Mkuu wa International Evengelism Church na Mkuu wa Chuo cha Biblia Sakila; alisema wahitimu wa chuo cha Biblia wanapaswa  kwenda kuweka mkazo wa kufundisha maadili kwenye jamii.

“Msambaze maandiko kwa kulenga maadili na si kwa kutafuta mali, bali watu waweze kuishi kwa kuthaminiana na wawe watu wenye hekima,” alihimiza

Awali muwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe, Joshua Nassari Mkuu wa wilaya ya Monduli alisema serikali ya mkoa wa Arusha itaendelea kutoa ushirikiano wa kiroho kwa chuo hicho cha Biblia na madhehebu mengine.

“Jamii yetu imekuwa ikipitia changamoto kubwa za mabadiliko ya kimadili na kitamaduni hivyo tujikite katika kufundisha maadili mema ya kitanzania na madili mema ya Imani ili tuwe na jamii iliyostaarabika,”alihimiza

Read More

Thursday, November 30, 2023

MAANDALIZI KUELEKEA SIKU YA UKIMWI DUNIANI YAKAMILIKA

 


Viongozi wa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu wamekagua maandalizi ya kuelekea Kilele cha Maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani Desemba 1, 2023 katika Viwanja vya Morogoro Sekondari ambapo maandalizi hayo yamekamili. Katika ukaguzi huo waliongozwa na Mhe. Jenista Mhagama ambaye ndiye Waziri mwenye dhamana ya uratibu.

Ikumbukwe maadhimisho ya siku ya UKIMWI Duniani hufanyika kila mwaka ambapo kauli mbiu ya mwaka huu inasema “Jamii Iongoze Kutokomeza UKIMWI”.

Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa.

Read More

Wednesday, November 29, 2023

TAMWA YAHIMIZWA KUWEKA MKAZO AJENDA YA UHURU WA KUJIELEZA UNAOJUMUISHA SAUTI ZA WANAWAKE

 


Chama cha wahandishi wa habari wanawake Tanzania (TAMWA) kimetakiwa kuweka mkazo mkubwa katika uhuru wa kujieleza unaojumuisha sauti za wanawake ndani ya ajenda ya jumla ya haki za binadamu.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama wakati alipomuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan katika maadhimisho ya miaka 36 ya chama cha waandishi wa habari wanawake Tanzania yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam.

Waziri, ametoa wito kwa (TAMWA) kuona umuhimu wa mijadala yenye mlengo wa kijinsia na uhusiano kati ya uhuru wa vyombo vya habari, ulinzi na usalama wa waandishi wa Habari wanawake, na uhuru wa kujieleza kuwa kitovu cha kufanya maamuzi katika ngazi ya jamii kitaifa, na kimataifa.

“Tuadhimishe siku hii kutimiza ahadi zilizotolewa na kila Nchi Mwanachama wa Umoja wa Mataifa ili kuyafikia Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) yote na hasa lengo namba tano linalozungumzia usawa wa jinsia,” alihimiza.

Aidha wadau mbalimbali wa habari watumie siku hii kusherehekea kwa kuungana na TAMWA kulinda na kuthamini haki za wanawake, haki za wasichana, haki za watoto, maadili ya kitanzania, na kupinga ukatili wa jinsia majumbani, hadharani na mitandaoni.

“Wamiliki wa vyombo vya Habari na waandishi wote kwa ujumla muungane katika jitihada za ulinzi na usalama wa waandishi wa Habari wanawake na hapa niwatie moyo waandishi wa Habari wanawake kuwa kazi yenu nzuri inaonekana pale mnapoweka jitihada ya kufanya kazi kwa weledi bila kukatishwa tamaa na vikwazo vya kimazingira.”Alifafanua

Waziri amesema kama kauli mbiu inavyosema, Uongozi Bora na Mchango wa Wanawake ni Chachu Kuelekea Tanzania yenye Maendeleo endelevu.

Hatuna budi kutambua kwamba suala la jinsia sio suala la wanawake peke yao bali ni suala la kuchochea maendeleo ya taifa letu miongoni mwa wanawake na wanaume, kwani ni jambo linalohimiza ushirikishwaji na ujumuishi usioacha kundi lolote nyuma.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Mawasiliano na Technolojia ya Habari Bw, Selestine Gervas Kakele amesema inatambua Mchango wa (TAMWA) na wakati wote serikali itaendelea kuangalia ujumbe ambao TAMWA na asasi nyingine inatoa.

Tumepokea utafiti kuhusu unyanyasaji wa kijinsia: (TAMWA) kupitia utafiti huu imesaidia kuvunja ukimya, matokeo ya utafiti  hayalengi kunyoosha kidole kwa mtu, bali kushirikiana ili tuweze kuishinda vita hiyo.

“Tusimamie weledi na nidhamu ya kazi na pale vitendo hivi vinapojitokeza: wahanga wasikae kimya jitokezeni, pazeni sauti na serikali itasikia,” alifafanua.

Awali   Mwenyekiti wa chama cha waandishi wa habari wanawake Tanzania (TAMWA) Bi, Joyce Shebe amemshukuru Mhe. Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kukubali mwaliko.

“Tumeona jinsi serikali ambavyo inapitia mifumo ya kisera na kisheria ilikuja na mipango inayopimika katika kuhakikisha ushirikishwaji na uwezeshaji wa wanawake kiuchumi na masuala yanayohusu usawa wa kijinsia inatatekelezeka” alibainisha

(TAMWA) tunaahidi kumuunga mkono kivitendo kwa sababu ni jukumu ambalo tumealianza tangu miaka 36 iliyopita

 

 

Read More

Saturday, November 25, 2023

WAZIRI MHAGAMA, AHIMIZA UWEKEZAJI KATIKA SEKTA YA UTALII MBINGA

 


Imeelezwa kwamba uwekezaji wa hoteli kubwa na za kisasa unasaidia katika kuchochea shughuli za utali na kuongeza thamani ya Mji wa Mbinga, kwa sababu ya upekee wa vivutio vyake.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama wakati wa Uzinduzi wa Mradi wa Hotel ya One Pacific yenye hadhi ya nyota tatu katika wilaya ya Mbinga.

Waziri Mhagama amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.  Samia Suluhu Hassan amejipambanua kwa kuwa balozi kinara wa sekta ya utalii na uwekezaji kwa ujumla katika sekta ya utalii.

“Mkakati wa Taifa wa ROYAL TOUR na kuifungua nchi yetu Tanzania katika sekta ya utalii ni mkakati mkubwa sana, na uliotukuka na tunaungana na wawekezaji katika kutafsiri ROYAL TOUR ndani ya wilaya yetu ya Mbinga,” Alifafanua

Akieleza kuhusu vivutio vinavyopatikana, Waziri amesema, wilaya ya Mbinga inavivutio vya kutosha; kama safu za milima zilizojipanga kwa kuvutia, zenye maporomoko ya maji, uoto wa asili, unaopendezesha madhari ya milima hiyo.

Aidha hapa ndio mahali ambapo kuna mapango ya kale katika eneo la Litembo, na inaaminika wazee wetu wa zamani waliishi katika mapango hayo.

“Hii historia kama itawekezwa vizuri, ni kivutio na utalii wa kutosha sana katika eneo letu,” Alibainisha.

Kwa upande wake Dkt. Erasmo Nyika akizungumza kwa niaba ya bodi ya wawekezaji wa mradi wa Hotel hiyo amesema wamesukumwa kuja kuwekeza Mbinga kutokana na Msukumo wa Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye amejenga mazingira rafiki ya uwekezaji.

“Tumuwekeza miradi miwili ndani ya wilaya ya Mbinga yenye thamani ya zaidi ya shilingi Billioni 4, na tumeona fursa zipo na tunashukuru Ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Mbinga kwa kutushawishi kuwekeza Mbinga, mradi umelenga kuzalisha ajira nyingi kwa wazawa,” Alisema

Awali, Mhandisi Selemani Kinyaka katika taarifa yake amesema Ujenzi wa Majengo ya mraadi wa One Pacific Hotel; unavyumba vya kawaida 14, vyumba vya daraja la juu 23 vyumba vya hadhi ya kiutawala 3, Ukumbi mdogo wa mikutano, Migahawa 2, sehemu ya mazoezi, eneo la kuogelea na eneo la kufulia nguo.

 

Katika kipindi cha utekelezaji wa mradi tumetoa ajira zaidi ya 250 ambapo 30 zilikuwa ajira za kudumu, na nyingine ni ajira zilizojitokeza kila siku.

Read More

Wednesday, November 22, 2023

WAZIRI MHAGAMA AAGIZA KUIMARISHWA MIUNDOMBINU YA MAWASILIANO DAR



 Serikali kupitia Ofisi ya Rais TAMISEMI imeahidi kutoa kiasi cha shilingi Millioni  20 ili kuimarisha kivuko cha kivuko cha Magole/Mwanagati kilichopo katika kata ya Mzinga Halmashauri ya Ilala Mkoani Dar es salaam ili kiweze kupitika muda wote.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe, Jenista Mhagama wakati akizungumza na wakazi waliojitokeza katika eneo hilo la kivuko liloathirika na Mvua wakati wa ziara yake iliyolenga kupata taarifa zilizochukuliwa na Kamati ya Mkoa ya Maafa juu ya kudhibiti madhara ya zaidi mvua yanayoweza kujitokeza.

Ameongeza kusema kazi ya kuimarisha kivuko ifanywe na wakala wa barabara vijijini TARURA haraka iwezekanavyo.

“Kivuko hiki kitakapokuwa kinapitika muda wote hakitarudisha juhudi ya kwenda na Mpango wa pili wa muda mrefu wa kujenga daraja la kudumu,”alibainisha

Waziri mhagama alisema kuwa serikali inatamani kuona shughuli za wananchi zifanyika bila kusimama; tunatamani watoto wetu waende shule, tunatamani kina mama wajawazito waende kupata huduma za afya kwa wakati, tunapenda wananchi wajisikie serikali yao inawajali, alisema Waziri.

“Tunataka tutengeneze daraja livutie machoni pa watu, kile matumaini kwa watu kwamba hii ni nyota ya Mhe. Rais, Dkt, Samia Suluhu Hassan na wananchi washirikishwe kiasi cha kutosha,” alifafanua

Waziri Mhagama alielekezaTARURA kuifanya kazi hiyo  kwa uaminifu mkubwa na kwa hofu ya mungu, kwa sababu mnasimamia uhai na maisha ya watu na sisi tunawaamini na tunawategemea.

Katika hatua nyingine Waziri ameomba wananchi kuendelea kuchukua tahadhari juu ya magonjwa ya mlipuko; hali ya mvua inaweza kutupelekea kwenye magonjwa ya kuhara, magonjwa ya malaria.

Aliwaasa wananchi kuendelea kusafisa vichaka na kujenga utaratibu mzuri wa kusafisha mazingira yetu na kila mmoja awe askari wa mwenzake na kuhakikisha mifereji yetu inakuwa safi na mapito ya maji yanakuwa wazi.

Kwa upande Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Mhe. Albert Chalamila alisema Mkoa wa Dar es salaam umeathiriwa na wa ujenzi wa kutawanyika, hivyo kasi ya ujenzi wa miundombinu imekuwa gharama kubwa, lakini lazima hilo lifanyike kwa sababu ni huduma kwa watanzania.

Wataalamu wetu wamekuwa wakisanifu ramani za daraja lakini bado hatujapata fungu la fedha kwa ajili ya ujenzi wa daraja, na hapa tunahitaji mkakakati mkubwa wa kuzuia mto kutokula kingo zake.

:Tunajitahidi kuhakikisha wananchi hawajengi mabondeni; na kulinda mito dhidi ya shughuli za kibinadamu, ikiwa ni sambamba na  kuhakikisha tunaunganisha miundo mbinu ya mawasiliano ili mambo yaweze kwenda vizuri,” alifafanua Mkuu wa Mkoa.

Naye diwani wa kata ya mzinga Mhe Jackob Izack amesema kero ni kubwa na kumshukuru sana waziri kwa kuja, mipango ilikwisha pangwa, mahitaji ya wananchi ni mikubwa na kuna wananchi zaidi ya elfu ishirini wanapita kila siku.

“Imani kubwa ipo kwa mama, na wewe mama umekuja kazi yetu ni kukuombea ili haya yote yaende kutendeka ili ikawe historia mpya kwa wananchi,” alifafanua Mhe. Diwani




Read More

Wednesday, November 15, 2023

WANANCHI WAPEWA RAI KUJITOKEZA KUPIMA KWA HIARI VVU

 


Wito umetolewa kwa wananchi kuendelea kujitokeza kupima VVU kwa hiari ili kujua hali zao ili kuendelea kuishi kwa kuzingatia matokeo, kwa wale ambao hawatakutwa na maambukizi ni nafasi kwao kuendelea kuishi ili wasiambukizwe na wale ambao watakutwa na maambukizi  wana nafasi kuendelea kuishi kwa kutumia dawa za kufubaza.

Kauli hiyo imetolewa wakati wa kikao cha pamoja Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu,anayeshughulika na Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe.Adam Kighoma Malima kuhusu kuelekea maandalizi ya siku ya UKIMWI kitaifa, katika kikao kilichofanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.

Ameongeza kusema tafiti zote za miaka mitano zimeonesha wanaume hawajitokezi kupima, na hawajitokezi kuanza kupata dawa, na hivyo kusumbuliwa sana na magonjwa Nyemelezi yanayotokana na virusi vya UKIMWI.

“Virusi vya UKIMWI na UKIMWI upo ni wajibu wa kila Mwananchi kuendelea kuchukua tahadhari,” alibainisha

Aidha kauli mbiu yetu inyosema; JAMII IONGOZE KUTOKOMZEA UKIMWI inatuhamasisha jamii yenyewe ndio iongoze mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI

Akizungumzia kuhusu malezi, ametoa rai kwa wazazi kukaa na familia na kuwaelimisha uwepo wa tatizo hili la UKIMWI.

“Tunajukumu kubwa la kuendelea kutoa malezi bora kwa watoto wetu na kuwajengea misingi ya tabia njema” alifafanua

Awali Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Kighoma Malima amesema maandalizi kuelekea wiki Maadhimisho ya siku ya UKIMWI yanaendelea vizuri

“Lengo ni kupeleka ujumbe kwa wananchi, huku tukitupia jicho kwa kundi la vijana na kwa kushiriki kwao itasaidia kupeleka ujumbe kwa vijana wengine ambao hawakupata fursa ya kushiriki,” alisema

 

 

 

 

 

 

 

Read More

Tuesday, November 14, 2023

SERIKALI KUONGEZA NGUVU MAPAMBANO YA VVU KWA KUNDI LA VIJANA.

 


Imeelezwa kuwa kundi la vijana kati ya umri wa miaka 15 mpaka 24 wanaongoza kwa kuchangia maambikizi mapya ya VVU – UKIMWI ambayo ni sawa na Asilimia 40 (40%).

 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama ameyasema hayo mapema leo Ofisini kwake Jijini Dodoma alipokuwa katika Mkutano na waandishi wa Habari uliyohusu maandalizi ya kilele cha maadhimisho ya siku ya UKIMWI Duniani, yanayofanyika Disemba moja kila mwaka.

Akiongelea kuhusu maadhimisho hayo yanayotarajiwa kafanyika kitaifa Mkoani Morogoro mwaka huu, Waziri Mhagama alisema tafiti zilizopo zinaonesha kuwa kuna kila sababu ya kuongeza nguvu kubwa kwa kundi la vijana ili kuliondoa kwenye uhatarishi wa maambukizi ya vvu.

Aliendelea kusema kuwa maadhimisho ya mwaka huu yatatoa kipaombele kwa kiasi cha cha kutosha kwa vijana kushiriki kikamilifu kwenye majukwaa na matukio yaliyoandaliwa kwenye maadhimisho ya siku ya UKIMWI Duniani mwaka huu nchini kote kutokana na sababu kwamba vijana ndo waingia kwenye maambukizi mapya kwa wingi.

  “Tunapokwenda huko mbele walau kwenye maadhimisho ya wiki ya kuelekea siku ya UKIMWI Duniani, tutoe nafasi ya kuwasikiliza vijana kwa karibu zaidi wakongamane, wakutane na viongozi wa dini na viongozi wa kimila, na wakati mwingine tumekuwa tukifikiri kwamba labda, mienendo ya kimaadili kwa sasa imekuwa ikichagiza vijana wetu kujikuta wanaingia kwenye kundi la maambukizi mapya kwa hivyo kwa kipindi hiki kipaombele kitakuwa kwa kundi la vijana.” Alifafanua Waziri Mhagama.

Aidha, Waziri Mhagama alisema kuwa zaidi ya mara tano tafiti zinaonesha kuwa wanawake wamekuwa na uhiyari wa kupima ukilinganisha na wanaume; ambao hawajitokezi kupima na kuanza matumizi ya dawa, hivyo kuna kila haja ya Serikali kupaza sauti juu kuwaomba kina baba waingiwe na hali ya uhiyari katika kufanya maamuzi ya kupima.

Kwa Upande wake Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Watu wanaoishi na VVU (NACOPHA) Bw. Emmanuel Reuben Msinga alisema kuwa kupitia Kliniki ya Huduma na Kinga (CTC) vijana wanaweza kufikiwa kwa wingi na kupata hamasa ya kupima kwa hiyari, na vijana wanahamasishana kukubali hali zao na namna ya kuwafikia vijana wingine ili wakapime kwa hiayari.

Aliongeza kusema kuwa NACOPHA ina kanda zake nchini na suala la uhamasishaji kwa sasa linafanyika kuanzia ngazi ya Kata, Wilaya na Mikoa.

Kauli Mbiu kwa Maadhisho ya Siku ya Ukimwi Duniani kwa mwaka huu inasema; “JAMII IONGOZE KUTOKOMZEA UKIMWI.”

Read More

Monday, October 30, 2023

PROGRAMU YA KUENDELEZA KILIMO NA UVUVI (AFDP) YAMEWEZESHA TAFITI ZA TEKNOLOJIA YA KISASA ZA KUKABILIANA NA MABADILIKO YA TABIA NCHI.


 

Programu ya kuendeleza kilimo na Uvuvi (AFDP) imewezesha Tafiti za Kiteknolijia kupitia Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Nchini (TARI) katika kuzalisha mbegu za kisasa zenye uwezo wa kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi.

Hayo yamesemwa leo na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibi) Mhe. Ummy Nderianaga wakati wa wasilisho la Taarifa ya Utekelezaji wa Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala Katiba na Sheria, Bungeni Dodoma.

Akitolea mfano aina ya mbegu sita za mahindi ikiwa ni Pamoja na Situka M1, TMV1, STAHA, Bora, T104 na T105, kuwa zikipandwa kwa kufuata kanuni bora za kilimo zinapelekea kuleta matokeao bora na Tafiti zinaonesha kuwa mbegu hizi zina uwezo mkubwa wa ustahimilivu dhidi ya changamoto mbalimbali za mabadiliko tabianchi.

Akiongelea suala la usalama wa chakula, Naibu Waziri Nderianaga alisema kuwa suala hili linakwenda sambamba na kipengele cha Usalama wa mbengu. “tulimaliza hivi punde mkutano wa Chakula Afrika na Tanzania imeonekana kuwa ni kitovu kwenye suala la chakula hivyo kama hatutakuwa na mbegu Bora na nzuri kufikia malengo itakuwa ni kazi.” Alibainisha

Kwa upande Mratibu wa Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Bw. Salimu Mwinjaka, alisema katika sekta ya Kilimo, Programu hii ya kimkakati inalenga kuongeza uzalishaji na upatikanaji wa mbegu bora kwa wakulima, na jitihada kubwa ni kuweka miundombinu ya umwagiliaji ili kuondokana na kilimo cha kutegemea mvua sambamba na kuihamasisha jamii ya wakulima, umuhimu wa kutumia mbegu bora katika kuleta tija na mageuzi ya kilimo.

Akiongoza kikao hicho, Kaimu Mwenyetiki wa Kamati hiyo ya Kudumu ya Bunge ya Utawala Katiba na Sheria, Mhe. Florent Laurent Kyombo Alisema “Tumeona mikakati Mizuri ya Serikali ambayo imewekwa hasa katika suala la mbegu, hii ni kuhakikisha kwamba suala zima la uzalishwaji wa mbegu bora na kwa wakati linafanikiwa.”

Akiongea katika kikao hicho, Mhe. Boniphace Nyangindu Butondo (Mjumbe wa kamati) alishauri Wakala wa Mbegu za Kilimo Nchini (ASA) kuwa na mkakati wa kuzalisha mbegu zenye tija za kutosha na kuangalia mbegu za mazao mengine kama vile Mtama, Mpunga na Pamba na kuzalisha mbegu za kutosha za Asili ili kuweza kukabiliana na mabadiliko yoyote yanayoweza kutokea kwani mbegu nyingi za kisasa zinaonesha kushambuliwa na wadudu mbalimbali.

 Kwa Upande wake Mhe. Dkt. Alice Kaijage (Mjumbe wa Kamati) Alishauri Wakala wa Mbegu za Kilimo Nchini (ASA) kuongeza uwanda wa Tafiti hususani katika zao la Alizeti, kama linaweza kustawi bila tatizo katika mikoa mingine tofauti na Singida, akitolea mfano Mkoa wa Pwani.

Awali akiongelea suala la Mbegu la Asili, Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Mbegu za Kilimo Nchini (ASA) Dkt. Sophia Kashenge Kilenga, Alisema kuna nasaba nyingi sana ya benki ya Mbegu za asili Mkoani Arusha,”Ni kweli kabisa Mbegu za Asili zina sifa ambazo kila mtu anahitaji, na zina nasaba nyingi mchanganyiko zinazopelekea ukuaji wa mbegu kwenda polepole na una mipaka, hivyo kwa ukuaji wa sasa wa idadi ya watu ni vyema kuwa na maeneo maalum ambayo mbegu za asili zitatumika na kwa kulisha idadi kubwa ya watu ni vizuri kutumika kwa mbegu zinazozaa kwa wingi katika eneo dogo.

 

Read More

Thursday, October 12, 2023

KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA AFYA NA MASUALA YA UKIMWI YAIPONGEZA OFISI YA WAZIRI MKUU

 


Kamati ya kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI imeipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) kwa mafanikio makubwa katika kutekeleza afua za VVU na UKIMWI nchini.

Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Stanslaus Nyongo wakati kamati ilipofanya ziara ya kutembelea na kukagua Mpango wa Dreams kupitia Mradi wa Epidemic Control (EPIC) unaotekelezwa na Shirika la Family Health International (FHI360) kwa wasichana balehe na wanawake vijana (AGYW) katika katika Mkoa wa Shinyanga.

Akizungumza mara baada ya kukagua vikundi vya vijana vikiwemo  Sitetereki kilichopo Kata ya Old Shinyanga, Jahazi, Kata ya Ibadakuli na Tunaweza katika Kata ya Kolandoto Mhe. Nyongo amesema lengo la ziara ni kujionea maendeleo ya mradi huo na kuishauri Serikali maeneo ya kuboresha ili kuendeleza jitihada za kuwa na vijana wenye afya nzuri wanaoshiriki katika shughuli za uzalishaji na kujiletea maendeleo yao.

“Tunapongeza kazi kubwa inayofanywa na Rais wetu Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kutoa maelekezo ya kumlinda mtoto wa kike hasa katika gonjwa kubwa la UKIMWI, namna ya kumkomboa mtoto wa kike, kujifunza kazi za ujasiliamali ili kujikwamua katika maisha pamoja  kupaza sauti dhidi ya unyanyasaji wa kijinsia hivyo sisi kama wabunge tumeridhishwa na kazi inayofanywa na Serikali,”Amesema Mwenyekiti huyo.

Naye Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Ummy Nderiananga amewaomba vijana wa kike kuendelea kujiamini na kufanya kazi vizuri kwani Serrikali ya Awamu ya Sita inawajali vijana na kutambua mchango wao mkubwa katika maendeleo ya Taifa.

Akizungumzia ziara hiyo  Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI Mhe. Hassan Mtenga  ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha za kukamilisha na kujengwa kwa miradi mikubwa ya maendeleo huku akiipongeza TACAIDS na wadau wa maendeleo kuwa na mwamko wa kuwawezesha vijana kujikwamua kiuchumi.

“Tumejifunza kitu kwasababu  tunao watu wako tayari kupiga vita janga  kuu la UKIMWI na niishukuru TACAIDS, Mawaziri wenye dhamana na hawa wadada ambao  wameamua kutoka kwenye  sughuli za kuuza bar na kuanzisha biashara  zao sasa uwe mfano  wa kuigwa kwa maeneo mengine,”Amepongeza Mhe. Mtenga.

Vilevile Mjumbe wa Kamati hiyo Mhe. Christina Mnzava amesema wazazi na walezi wana wajibu wa kusimamia malezi sahihi ya watoto ili kuwakomboa katika tabia hatarishi huku  akiupongeza Mpango wa Dream kwa kuamua  kuwafikia mabinti katika maeneo yao akishauri mradi huo kuongeza wigo na kuwafikia vijana wengine  waliopo Vijijini .

“Sisi kama wazazi na walezi tunaweza kuwakomboa watoto wetu katika tabia hatarishi ambazo wanazipata mtaani kuna wengine walikuwa wanauza miili yao, lakini kutokana na mradi huu wamejikwamua wamefundishwa ujasiriamali, kuwekeza tumeona wasichana wamejitambua wanatengeneza sabuni, batiki, vyungu katika vikundi vya Kata za Old Shinyanga, Ibadakuli na Kolandoto kwa kweli wamefanya vizuri,”Ameeleza Mjumbe huyo.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe Christina Mndeme amesema Serikali ipo tayari kushirikiana na Mashirika yasiyokuwa ya kiserikali kuondoa unyanyapaa na ubaguzi kwa watu wanaoishi na VVU ambao upo juu, kuwajengea vijana uwezo wa kiuchumi ili muda mwingi wautumie kwenye uzalishaji na sio kwenye mambo yanayoweza kuwasababishai maambukizi ya VVU,kuelimisha jamii kuacha mila potofu ambazo zinasababisha ukatili wa kijinsia.

Kwa upande wake Mshauri Mwandamizi wa Mpango wa Dreams kupitia Mradi wa Epidemic Control (EPIC) unaotekelezwa na Shirika la Family Health International (FHI360) Bi. Agnes Junga amefafanua kuwa lengo la Mpango huo ni kupunguza maambukizi ya Virusi vya UKIMWI kwa wasichana kuanzia umri wa miaka Tisa hadi 24.

“Mpango huu ulizinduliwa 2014 ukilenga kupunguza maambukizi ya virusi vya UKIMWI kwa Nchi 13 za Bara la Afrika ikiwemo Tanzania ambapo tulianza na Halmashauri Sita na hadi sasa tumefikia Halmashauri 12. Shirika la (FHI360) kwenye mradi wa EPIC tunatekeleza Dreams katika Mikoa miwili ya Shinyanga ndani ya Halmashauri Tano na Iringa katika Halmashauri mbili na tunawafikia wasichana kuanzia miaka 15 hadi 25 walio nje ya shule pamoja na wazazi au walezi na jamii kwa ujumla tuhakikishe msichana anafikia ndoto zake.

Aidha akizungumza kwa niaba ya wanakikundi kutoka Vikundi vya Mabinti Balehe na Wanawake Vijana vya Sitetereki, Tunaweza na Jahazi mwanakikundi Sungi Leonard amesema uanzishwaji wa vikundi hivyo vimewasaidia kama mabinti kujitambua, kufahamu elimu ya afya, kuwajengea uwezo wa kukabiliana na vitendo vya kikatili pamoja na kuchukua tahadhari dhidi ya maambukizi mapya ya VVU na kuwawezesha kiuchumi.

“Nilikutana na mwezeshaji kiuchumi na mwelimishaji rika nikapata elimu ya ukatili wa kijinsia, umuhimu wa upimaji wa afya, matumizi sahihi ya kinga, magonjwa ya ngono na VVU ambayo imenisaidia kujitambua kama binti. Pia nilifanikiwa kujiunga katika kikundi cha Sitetereki nikajifunza kutengeneza batiki kazi ambayo inanipatia kipato na ninamudu mahitaji yangu tofauti na ilivyokuwa awali,” Ameshukuru Mwanakikundi huyo.

Read More