Saturday, July 1, 2017

MAJALIWA:HAKUNA MSAMAHA KWA WANAOUIBIA USHIRIKA


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali haitamsamehe mtu yeyote atakayejihusisha na ubadhilifu wa mali za fedha za Ushirika nchini.

“Kwa Serikali hii ya awamu ya Tano tutachua hatua kali kwa wezi wa mali na fedha za ushirika na tunaendelea kufanya usafi wa wabadhilifu hadi tupate viongozi waadilifu,”.

 Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Jumamosi, Julai Mosi, 2017), katika Maadhimisho ya Siku ya Ushirika Duniani (SUD), iliyoadhimishwa kitaifa mjini Dodoma kwenye ukumbi wa Jakaya Kikwete.

Amesema miongoni mwa changamoto zinazoukabili Ushirika nchini ni pamoja na wizi na ubadhilifu wa rasilimali za Ushirika unaofanywa na baadhi ya viongozi na wanachama wasiokuwa waaminifu.

 Waziri Mkuu amesema changamoto nyingine ni baadhi ya viongozi wa vyama vya Ushirika kutoheshimu miongozo ya vyama vyao na kujifanyia mambo kwa maslahi yao binafsi.

Amesema katika kukabiliana na changamoto hizo Serikali itaendelea kutimiza wajibu wake na kuweka mazingira rafiki ya kustawisha Ushirika nchini ili kutoa fursa ya Ushirika kushamiri na kuwawezesha Watanzania kumiliki uchumi wa nchi yao.

“Haikubaliki hata kidogo kuona sekta hii inayosadifu maisha ya Mwafrika hamnufaishi ipasavyo , hivyo naelekeza Tume ya Maendeleo ya Ushirika nchini ihakikishe kuwa vyama vya Ushirika vinaendeshwa kisayansi na kwa mujibu wa sheria,” amesema.

Pia amezielekeza Kamati za Ushauri za Mikoa na Wilaya nchini, ziingize agenda ya Maendeleo ya Ushirika kama moja ya agenda muhimu inayopaswa kujadiliwa na kuwekewa maazimio ya utekelezaji. Pia wawe na takwimu za vyama vya Ushirika na Wanaushirika.

Hata hivyo Waziri Mkuu amezielekeza mamlaka zote zinazohusika na Ushirika nchini zijiwekee malengo yanayopimika ya namna ya kuboresha sekta ya Ushirika.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameelekeza kwamba masuala yote yanayohusu Ushirika wa kilimo nchini lazima yaratibiwe na Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Aidha, Waziri Mkuu amezielekeza Wizara za Kilimo, Mifugo na Uvuvi na Ofisi ya Rais-TAMISEMI zifanye mapitio kubaini elimu na ujuzi katika ngazi zote za Ushirika kwa ajili ya kuwaandalia kozi za muda mfupi za kuongeza ujuzi au kubainisha aina ya watumishi wanaohitajika kwenye sekta hiyo.

Pia amewaagiza Maofisa Ushirika nchini kuhakikisha wanasimamia vizuri uchanguzi wa Vyama vya Ushirika vya Msingi (AMCOS) na kuwaondoa wagombea wote waliowahi kuwa viongozi, ambao waliondolewa madarakani kutokana na ubadhilifu wa mali na fedha za Ushirika.

Awali, Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Dkt. Charles Tizeba alisema wizara itaendelea kusima na kuchukua hatua kwa viongozi wote wa vyama vya Ushirika watakaobainika kufuja mali na fedha za Ushirika.


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.