Tuesday, October 31, 2017

KUWENI WAZALENDO, WAZIRI MKUU AHIMIZA


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka Watanzania waishio Canada wadumishe mshikamano wao na wawe na uzalendo kwa Taifa lao.

Ametoa wito huo jana (Jumanne, Oktoba 31, 2017) wakati akizungumza na Watanzania waishio Toronto, Canada.

Waziri Mkuu ambaye yuko Canada kwa ziara ya kikazi, alisema kila Mtanzania anapaswa ahubiri utaifa wake. “Tembea huku ukiringia nchi yako, wakati wote ringia nchi yako, unapotakiwa kuisemea nchi yako, isemee vizuri kama ambavyo wengine wanasemea vizuri nchi zao licha ya matatizo waliyonayo.”

Aliwataka wakumbuke kuweka akiba na wanapopata fursa watume fedha zao nyumbani ili zisaidie kuleta maendeleo. “Ukipata kitu kidogo, rusha nyumbani; ukipata mtu anayeweza kuleta tija, mlete nyumbani, nasi tutawapokea wewe na yeye,” alisisitiza.  

“Tunawasisitiza muitangaze nchi yetu kwa mataifa mengine ili nao waone Tanzania ni mahali pa fursa, na akitaka kuwekeza ajue kuwa anawekeza mahali ambapo ni salama,” alisema.

Alisema Serikali inasisitiza wananchi waishio nje ya nchi, wawe wazalendo na washirikiane kuhakikisha wanazitumia vizuri fursa za kimaendeleo kwa manufaa ya nchi yao.
  
Awali, Balozi wa Tanzania nchini Canada, Mhe. Jack Nzoka, alitumia fursa hiyo kuwasihi Watanzania waishio nchini humo wazingatie sheria za nchi hiyo.


“Wote sisi tunawatambua kama mabalozi katika nafasi zenu hapa Canada. Tunawashauri muwe raia wema, na muishi kwa kufuata sheria na taratibu za nchi hii na msisahau mlipotoka, kwani hakuna mahali pazuri kama nyumbani,” alisisitiza.
Read More

Thursday, October 26, 2017

VITUO VYA KUTOA TAHADHARI YA MAAFA YA MAFURIKO NA UKAME VYAFUNGWA NCHINI

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Ajira na Watu wenye Ulemavu) Mhe.Jenista Mhagama akisisitiza umuhimu wa vituo vya hali ya hewa vilivyofungwa na Ofisi ya Waziri Mkuu chini ya usimamizi wa mamlaka ya hali ya hewa Tanzania ambapo kutokana na uwezo wa vituo hivyo taarifa zake zinatumika kutoa tahadhari ya uwepo wa maafa ya mafuriko na Ukame nchini, kushoto kwake ni Mkurugenzi Idara ya Uratibu maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Brigedia Jenerali Mbazi Msuya, Meneja Kanda ya Kusini, Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania,  Daudi Amas na Mratibu Mradi wa mifumo ya Tahadhari za mapema, Alfei Daniel, wakati alipokuwa anakagua vituo hivyo mkoani Ruvuma.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Ajira na Watu wenye Ulemavu) Mhe.Jenista Mhagama akipata maelezo kutoka kwa  Mhandisi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania,  David CChilambo, juu ya jinsi vituo vya hali ya hewa vilivyofungwa na Ofisi ya Waziri Mkuu chini ya usimamizi wa mamlaka ya hali ya hewa Tanzania ambapo kutokana na uwezo wa vituo hivyo taarifa zake zinatumika kutoa tahadhari ya uwepo wa maafa ya mafuriko na Ukame nchini, , wakati alipokuwa anakagua vituo hivyo mkoani Ruvuma, katikati ni Mkuu wa Wilaya Namtumbo, Luckness Amlima.


Moja ya Kituo cha hali ya hewa kati ya vituo 36  vilivyofungwa na Ofisi ya Waziri Mkuu nchi nzima kwa  usimamizi wa mamlaka ya hali ya hewa Tanzania ambapo kutokana na uwezo wa vituo hivyo taarifa zake zinatumika kutoa tahadhari ya uwepo wa maafa ya mafuriko na Ukame nchini, , kutokana na uwezo wa vituo hivyo vinavyopatikana  hapa nchini na Ethiopia kwa bara la Afrika, vimeongeza uwezo wa ufanisi wa utabiri wa Mamlaka ya Hali ya Hewa kutoka asilimia 82 hadi asilimia 87 kwa sasa.

Read More

Wednesday, October 25, 2017

MHAGAMA : HAYATI ASKOFU CASTOR MSEMWA ALIKUWA KIUNGO MUHIMU KWA MIRADI YA KANISA KUWEZESHA HUDUMA ZA SERIKALI

Waziri wa Nchi Ofisi ya  Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Ajira na Watu wenye ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama akisaini kitabu cha rambi rambi wakati alipofika kushiriki maziko ya aliyekuwa askofu wa jimbo la Katoliki Tunduru Masasi Hayati Castor Msemwa yaliyofanyika katika  jimbo hilo, mkoani Ruvuma, leo tarehe 25 Oktoba, 2017.
Waziri wa Nchi Ofisi ya  Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Ajira na Watu wenye ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama  akiwa na spika mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania , Anna Makinda, wakati wa misa ya  maziko ya aliyekuwa askofu wa jimbo la katoliki Tunduru Masasi Hayati Castor Msemwa yaliyofanyika katika  jimbo hilo, mkoani Ruvuma, leo tarehe 25 Oktoba, 2017



Waziri wa Nchi Ofisi ya  Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Ajira na Watu wenye ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama akitoa salaam za serikali wakati wa maziko ya aliyekuwa askofu wa jimbo la katoliki Tunduru Masasi Hayati Castor Msemwa yaliyofanyika katika  jimbo hilo, mkoani Ruvuma, leo tarehe 25 Oktoba, 2017.

Spika mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania , Anna Makinda, akinena kuhusu kifo cha Hayati askofu wa jimbo la katoliki Tunduru Masasi Hayati Castor Msemwa wakati wa maziko yake yaliyofanyika katika  jimbo hilo, mkoani Ruvuma, leo tarehe 25 Oktoba, 2017.

Read More

Tuesday, October 24, 2017

WATUMISHI WA OFISI YA WAZIRI MKUU WAJENGEWA UWEZO KUKABILI MAAFA

Watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu wameshiriki Warsha ya kujengewa uwezo kuhusu kugharamia maafa na matumizi ya Bima za majanga ili kutumia fursa zilizopo za kukabili maafa pindi yanapotokea kwa kushirikisha wadau mbalimbali  ikiwemo Taasisi zilizopo chini ya Umoja wa Afrika .

Akizungumza wakati wa Warsha hiyo iliyofanyika Oktoba 24, 2017 Mjini Dodoma kwa niaba ya Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera na Bunge, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimaliwatu Bw. Issa Nchasi alisema kuwa warsha hiyo inalenga kutoa uelewa kuhusu utaratibu utaotumiwa na African Risk Capacity (ARC) ambayo ni Taasisi chini ya Umoja wa Afrika.

“Serikali imekuwa ikifanya kazi ya kuboresha mazingira ili kujenga uwezo wa kukabili madhara yatokanayo na maafa nchini” Alisisitiza Nchasi

Akifafanua amesema kuwa, warsha hiyo itasaidia watumishi wa Idara ya Uratibu wa Maafa kuwa na uwezo katika Menejimenti ya Maafa hali itayorahisisha Kujikinga, kukabili na kurejesha hali.

Washa hiyo ya siku moja imelenga kuwajengea uelewa Watumishi wa Ofisi hiyo kuhusu utaratibu unaotumiwa na Taasisi yaAfrica Risk Capacity katika kuhudumia na kugharamia maafa na Bima za majanga.

Kuwawezesha Serikali kutambua maeneo ya ushirikianao katika huduma na kugharimia maafa na Bima za majanga.

Kwa upande wake Mkuu wa Huduma kwa Serikali kwa nchi za Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika kutoka Shirika la “Africa Risk Capacity” bi. Lucy Nyirenda amesema kuwa mpango huo uko chini ya nchi wanachama wa Umoja wa Afrika (AU) na takribani nchi 9 zimeshajiunga katika mfumo wa Bima za majanga.

“Takribani nchi 32 zimeshajengwewa uwezo kuhusu umuhimu wa kuwa na bima ya majanga ili kuimarusha uwezo wa kuyakabili pale yanapotokea kwa kushirikiana na wadau.” Alisisitiza Lucy

Akifafanua Lucy amesema kuwa, ni vyema nchi za Afrika zikaungana ili kuweza kuzuia majanga katika Bara la Afrika kwa kushirikishana mbinu mbalimbali zikiwemo fursa zinazoweza kusaidia kukabiliana na majanga hayo .

Warsha hiyo ya siku moja iliyoandaliwa na Taasisi ya Africa Risk Capacity (ARC ) iliyopo chini ya Umoja wa Afrika kwa kushirikiana na Idara ya Uratibu wa Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu  imewashirikisha  Watumishi kutoka  Wizara za kisekta na Idara zinazojitegemea Takribani 42.
Read More

WATUMISHI WA OFISI YA WAZIRI MKUU WAJENGEWA UWEZO KUKABILI MAAFA

Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Ofisi ya Waziri Mkuu Bw.Issa Nchasi akifungua Warsha ya siku moja kwa niaba ya Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Uratibu) iliyofanyika Oktoba 24, 2017 Dodoma Warsha hiyo iliandaliwa na Taasisi ya Africa Risk Capacity (ARC) iliyopo chini ya Umoja wa Afrika

Mkuu wa Huduma kwa Serikali kwa nchi za Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika kutoka Shirika la “Africa Risk Capacity” Bi. Lucy Nyirenda akieleza umuhimu wa Bima za Majanga kwa wajumbe walioudhuria warsha ya kujengewa uwezo kuhusu Gharama za  Maafa na Matumizi ya Bima za Majanga iliyofanyika Mjini Dodoma Oktoba 24, 2017

Mkuu wa Huduma kwa Serikali kwa nchi za Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika kutoka Shirika la “Africa Risk Capacity” Bi. Lucy Nyirenda akifafanua jambo wakati wa Warsha ya Kugharamia Maafa na Matumizi ya Bima za Majanga iliyofanyika Mjini Dodoma kwa lengo la kutoa elimu kwa Watumishi wa Serikali juu ya masuala ya Maafa.

Meneja Kanda ya Kati Mamlaka ya BIMA Tanzania Bi. Stella Rutaguza akichangia hoja kuhusu umuhimu wa Bima za Majanga wakati wa Warsha ya siku moja juu ya Kugharamia Maafa na Matumizi ya Bima za Majanga iliyoandaliwa na Taasisi ya Africa Risk Capacity kushirikiana na Idara ya Uratibu wa Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu.

Washiriki wa Warsha ya Kugharamia Maafa na Matumizi ya Bima za Majanga wakifuatilia mada iliyowasilishwa na Mkuu wa Huduma kwa Serikali kwa nchi za Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika kutoka Shirika la “Africa Risk Capacity” Bi. Lucy Nyirenda Mjini Dodoma Oktoba 24, 2017.

Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Issa Nchasi (wanne kutoka kulia) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa Warsha  hiyo mapema leo mjini Dodoma

Read More

Tuesday, October 17, 2017

SERIKALI YAKAMILISHA UJENZI WA KITUO CHA OPERESHENI NA MAWASILIANO YA DHARURA KWA AJILI YA KUFUATILIA MAAFA NCHINO

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu(Sera, Bunge, Ajira na  Watu wenye Ulemavu) Jenista Mhagama akipata maelezo kutoka kwa Mratibu wa Maafa  Ofisi ya Waziri Mkuu, Jane Alfred, namna mtambo unavyosaidia kupatikana kwa taarifa za dharura kwa ajili ya kufuatilia maafa nchini, leo tarehe 17 Oktoba, 2017, Dar es salaam.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge, Ajira na  Watu wenye Ulemavu) Jenista Mhagama akiangalia mitambo inayotumika kutunza takwimu za taarifa za dharura kwa ajili ya kufuatilia maafa nchini, leo tarehe 17 Oktoba, 2017, Dar es salaam.
Mkurugenzi wa Idara ya Uratibu wa Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Brig. Jen. Mbazi Msuya akieleza umuhimu wa mpango wa uendeshwaji wa kituo Cha Operasheni na Mawasiliano ya Dharura kwa ajili ya kufuatilia maafa nchini kwa  Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge, Ajira na  Watu wenye Ulemavu) Jenista Mhagama, leo tarehe 17 Oktoba, 2017, Dar es salaam.



Mkurugenzi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini Dkt. Agnes Kijazi akimueleza Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge, Ajira na  Watu wenye Ulemavu) Jenista Mhagama,jinsi Mradi wa Uboreshaji wa Mifumo ya Tahadhari za Awali na Mabadiliko ya Tabianchi ulivyoboresha utabiri wa hali ya hewa nchini, alipotembelea mamlaka hiyo, leo tarehe 17 Oktoba, 2017, Dar es salaam.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge, Ajira na  Watu wenye Ulemavu) Jenista Mhagama (walio kaa katikati) akiwa na Menejimenti ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini mara baada ya kutembelea mamlaka hiyo kwa ajili ya kuona jinsi Mradi wa Uboreshaji wa Mifumo ya Tahadhari za Awali na Mabadiliko ya Tabianchi ulivyoboresha utabiri wa hali ya hewa nchini, , leo tarehe 17 Oktoba, 2017, Dar es salaam.

Read More

Monday, October 16, 2017

MAWAZIRI TUMIENI MADARAKA YENU KWA MASLAHI YA TAIFA-MAJALIWA

*Asisitiza Uwaziri si fursa ya kujitajirisha

                                        
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka Mawaziri watumie madaraka yao kwa manufaa ya Taifa na kamwe wasiyatumie kama fursa ya kujitajirisha wao binafsi.

Ameyasema hayo leo (Jumatatu, Oktoba 16, 2017) alipozungumza na baadhi ya Mawaziri, Manaibu na Makatibu Wakuu katika kikao kilichofanyika jijini Dar es Salaam.

Amesema Mheshimiwa Rais Dkt. John Magufuli amesisitiza kwamba amewateua ili wafanye kazi na kamwe wasitumie madaraka waliyopewa kwa maslahi yao binafsi.

“Madaraka haya ya Uwaziri si fursa ya kujipatia utajiri, tunatakiwa tufanye kazi kwa weledi, uadilifu, bidii na uaminifu mkubwa ili kuondoa kero za wananchi kwa wakati.”

Amesema Mawaaziri na Manaibu Waziri wazingatie Katiba ya nchi, Kanuni, Taratibu na Miongozo mbalimbali ya Serikali katika utekelezaji wa majikumu yao ya kila siku.

Waziri Mkuu amesema Mawaziri hao wanatakiwa wasimamie utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa miaka kuanzia mwaka 2016/2017 hadi 2020/2021.

Pia utekelezaji wa ahadi zote zilizopo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015 pamoja na ahadi alizozitoa Rais Dkt Magufuli wakati wa kampeni za uchaguzi.

Waziri Mkuu amewaagiza Mawaziri wahakikishe wanakwenda kufanya ufuatiliaji wa tathmini ya utekelezaji wa mipango mbalimbali ya maendeleo inayohusu sekta zao.

Pia amewataka Mawaziri hao wakasimamie kikamilifu ukusanyaji wa mapato na kuanzisha vyanzo vipya vya ukusanyaji pamoja na kudhibiti mianya ya upotevu.

Hata hivyo Waziri Mkuu amewataka Mawaziri hao wakapunguze urasimu katika utekelezaji wa malengo ya Serikali kwa sababu wananchi wanahitaji kuhudumiwa kwa wakati.

Mawaziri waliohudhuria kikao hicho ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais –TAMISEMI Bw. Suileiman Jaffo pamoja na Manaibu wake Bw. Joseph Kandege na Bw. George Kakunda, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bi Ummy Mwalimu na Naibu wake Dkt. Faustine Ndungulile.

Wengine ni Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mhandisi Isack Kamwelwe na Naibu wake Bw. Jumaa Aweso, Waziri wa Viwanda na Biashara Bw. Charles Mwijabe na Naibu wake Mhandisi Stella Manyanya.

Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Hamisi Kigwangalla na Naibu wake Bw. Josephat Hasunga, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako na Naibu wake Bw. William Ole Nasha, Naibu waziri wa Mifugo na Uvuvi Bw. Abdallah Ulega pamoja na Makatibu Wakuu wa Wizara hizo.

Read More

Saturday, October 14, 2017

SERIKALI YAWEKA MIKAKATI MADHUBUTI KUKABILI MAAFA NCHINI

Serikali imejipanga kikamilifu katika kuhakikisha inayakabili maafa yanayotokea nchini kwa kuangalia sheria, Kanuni na Taratibu mbalimbali zinazohusika na masuala ya Menejimenti ya Maafa ili kuepuka madhara yatokanayo na maafa nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi Masaidizi Idara ya Uratibu wa Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Bashiru Taratibu wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Kupunguza Maafa yaliyofanyika Kitaifa mjini Dodoma na Kuwashirikisha wananchi, wanafunzi na wadau mbalimbali.

Katika kuhakikisha wananchi wanakuwa salama na kuepuka madhara yatokanayo na maafa tayari Serikali imepima Viwanja zaidi ya milioni moja na nusu katika Halmashauri mbalimbali hapa nchini ikiwa ni moja ya mikakati ya kuondoa makazi holela na kuepusha maafa yanayotokana na matumizi ya ardhi yasiyozingatia sheria kanuni na taratibu zinazosimamia sekta ya Ardhi.

“Wananchi wazingatie sheria, Kanuni, na Taratibu kwa kuepuka kujenga maeneo hatarishi kama mabondeni, maeneo yenye mafuriko na mengine yote yanayokatazwa kisheria ili kuepuka maafa” Alisisitiza Taratibu

Akifafanua Taratibu amesema kuwa Viongozi wa Serikali katika maeneo yote hapa nchini wanajukumu la kusimamia sheria zilizopo ili kuepusha maafa kwa kuzingatia Kauli mbiu ya mwaka huu inayosema “MAKAZI SALAMA: Punguza Makazi katika Maeneo Hatarishi, Punguza kuhama kutokana na maafa”.

Akizungumzia mikakati ya Serikali kuondoa maafa na kupunguza uwezekano wa kutokea kwa maafa amesema kuwa Idara ya Maafa imekuwa ikitoa elimu kwa Umma ili kuwasaidia wananchi kuwa na uelewa utakaosaidia kuepuka athari za maafa.

Aidha alitaja hatua nyingine zilizochukuliwa na Serikali kuwa ni kutungwa kwa sheria ya maafa ya mwaka 2015, Miongozo, Kanuni na kuwekwa kwa taratibu mbalimbali  za kusimamia masuala ya maafa hapa nchini.

Kwa upande wake Mratibu wa Maafa Wilaya ya Chamwino Bi Lilian Zakaria amesema kuwa wamekuwa wakitoa elimu kuanzia ngazi ya Wilaya hadi Vijjiji wakishirikisha Kamati za Maafa katika ngazi zote ili kuwajengea wananchi uwezo wa kupambana na maafa pale yanapotokea na pia kuzuia viashiria vyake.

Pia Bi Zakaria amewataka wananchi kuepuka kujenga na kuishi katika maeneo hatarishi na kuzingatia taratibu zote zilizowekwa na Serikali kuepuka maafa.

Naye Mwakilishi wa Asasi za Kirai Bw. Mussa Mussa amesema kuwa  wanaunga mkono juhudi za Serikali katika kupambana na maafa hali inayosababisha wananchi kuishi salama katika maeneo mbalimbali hapa nchini.

AWALI:
Chimbuko la Siku ya Kimataifa ya Kupunguza Maafa ilitokana na Azimio Na. 64/200 lililopitishwa na Baraza la Umoja wa Mataifa tarehe 21 Desemba, 2009 ambapo iliamuliwa Oktoba 13 ya kila mwaka ni Siku ya Kimataifa ya Kupunguza Maafa ikiwa na lengo la Kukuza utamaduni wa kupunguza madhara ya maafa kimataifa, ikiwa ni pamoja na kuzuia, kupunguza madhara, Kujitayarisha, Kukabili na Kurejesha hali kuwa bora zaidi na mwaka huu kaulimbili inasema: “MAKAZI SALAMA: Punguza Makazi katika Maeneo Hatarishi, Punguza Kuhama kutokana na Maafa

Read More

TUMUENZI BABA WA TAIFA KWA KUIGA MAISHA YAKE-MAJALIWA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewaomba Watanzania waendelee kumuenzi Hayati Baba wa Taifa Mwl. Julius Nyerere kwa kuiga maisha yake na utendaji wake.

Ameyasema hayo leo (Jumamosi, Oktoba 14, 2017) aliposhiriki ibada maalumu ya kumuombea Mwl. Nyerere iliyofanyika katika Kanisa Katoliki la Minara Miwili Zanzibar.

Ibada hiyo ya kumbukumbu ya miaka 18 ya kifo cha Mwl. Nyerere ni sehemu ya maadhimisho ya kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru uliozimwa leo katika mkoa wa Mjini Magharibi visiwani Zanzibar.

Katika Idaba hiyo Waziri Mkuu amewasisitiza wananchi kuhakikisha wanamuenzi Mwl. Nyerere kwa kuendeleza mambo mema yote aliyoyafanya enzi za uhai wake.

Awali, Katibu wa Jimbo Katoliki Zanzibar Padri Cosmas Shayo ambaye aliongoza ibada hiyo aliwaomba waamini wamuenzi Mwl. Nyerere kwa kudumisha umoja na mshikamano wa Taifa.

“Hayati Baba wa Taifa Mwl. Nyerere aliwapenda watu wote bila kujali Imani zao wala itikadi zao. Alikuwa mzalendo na alitaka Watanzania waishi maisha bora.”

Padri Shayo aliongeza kuwa tunu za amani na umoja zilikuwa miongoni mwa falsafa kuu ya Mwl. Nyerere, ambapo matokeo yake ni umoja na mshikamano wa Taifa uliopo.

Ibada hiyo ilihudhuriwa na Makamu wa Pili wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Balozi Seif Ally Idd, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Bi Jenista Mhagama, Mke wa Waziri Mkuu Mama Mary Majaliwa.


Wengine ni Waziri wa Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Vijana, Wanawake na Watoto Bi. Mauldine Castico, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira Bw. Anthony Mavunde, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Walemavu Bi. Stella Alex Ikupa na mwakilishi wa familia ya Mwl. Bw. Makongoro Nyerere.
Read More

HABARI PICHA WAZIRI MKUU

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwa kwenye ibada maalum ya kumuombea Mwalimu Julius Nyerere, iliyofanyika katika Kanisa Katoliki la Minara Miwili Zanzibar (katikati) ni Makamu wa pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi (kushoto) ni Mke wa Waziri Mkuu mama Marry Majaliwa. Oktoba 14, 2017.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na waumini waliyo hudhuria kwenye ibada maalum ya kumuombea Mwalimu Julius Nyerere, iliyofanyika katika Kanisa Katoliki la Minara Miwili Zanzibar, Oktoba 14, 2017.

Read More

RAIS MAGUFULI AKABIDHI TAARIFA YA MWENGE KWA UTEKELEZAJI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimkabidhi Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu(Sera, Binge na Watu kwenye Ulemavu) taarifa ya Mbio za Mwenge kwa mwaka huu, Leo tarehe 15 Oktoba, 2017, Zanzibar. Jana tarehe 14, Oktoba , 2017, Mhe. Rais aliahidi kuhakikisha taarifa hiyo inatekelezwa kikamilifu .

Read More

Thursday, October 12, 2017

TUTAENDELEA KUIMARISHA USHIRIKIANO WETU NA UGANDA-MAJALIWA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali ya Tanzania itaendelea kuimarisha ushirikiano wake wa kiuchumi na kidiplomasia baina yake na Uganda.

Amesema Tanzania na Uganda zinauhusiano wa muda mrefu na kwamba Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Magufuli inafarijika na ushirikiano huo.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Alhamisi, Oktoba 12, 2017) alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Uganda nchini Tanzania, Bw. Richard Kaonero jijini Dar es Salaam.

“Tunaimani kubwa na ushirikiano wetu na Serikali ya Uganda. Tutaendelea kuimarisha miradi mbalimbali ya maendeleo tunayoitekeleza kwa pamoja ukiwemo ujenzi wa bomba la gesi.”

Hivyo ametumia fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji kutoka nchini Uganda ili waje kuwekeza kwenye viwanda mbalimbali vikiwemo  vya kuchakata mazao ya  kilimo.

Pia amewakaribisha raia wa Uganda kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii vilivyoko nchini Tanzania kama mlima wa Kilimanjaro, fukwe, mali kale na mbuga za wanyama.

Kwa upande wake, Balozi Kaonero  ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa kuwa na dhamira ya dhati ya kuimarisha uchumi wake kupitia sekta ya viwanda.

Pia Balozi huyo ameiomba Serikali ya Tanzania kupitia Shirika la Ndege Tanzania 
(ATCL) kuanzisha safari ya kwenda Entebe nchini Uganda ili kuimarisha usafiri kati ya nchi hizo mbili.

Akizungumzia kuhusu ushirikiano baina ya nchi hizo mbili, Balozi Kaonero amesema Serikali ya Uganda na Tanzania zinaundugu wa damu na kwamba wataendelea kuudumisha.

Read More

Wednesday, October 4, 2017

MARUFUKU KUWAKAMATA WAUGUZI BILA YA KUFUATA TARATIBU-MAJALIWA

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akisalimiana na Katibu Mwenezi msaidizi wa Chama cha Wauguzi Tanzania (TANNA) Johari Yusuf, baada ya ufunguzi wa Mkutano wa chama cha wauguzi leo Oktoba 4,2017 Mkoani Lindi.katikati  ni mweye beji shigoni ni Rais wa Chama cha Wauguzi Tanzania Bwana Poul Magesa .kulia kwa katibu mwenezi ni Katibu Mkuu wa Chama cha Wauguzi Tanzania Sebastian Luziga.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa  akisoma Hotuba ya Ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Chama cha Wauguzi Tanzania (TANNA) ambao umeanza leo Oktoba 4,2017 Mkoani Lindi.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa  akisoma Hotuba ya Ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Chama cha Wauguzi Tanzania (TANNA) ambao umeanza leo Oktoba 4,2017 Mkoani Lindi.


Read More

MARUFUKU KUWAKAMATA WAUGUZI BILA YA KUFUATA TARATIBU-MAJALIWA



WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amepiga marufuku tabia ya baadhi ya viongozi  katika maeneo mbalimbali nchini kuwakamata na kuwaweka ndani watumishi wakiwemo wauguzi bila ya kufuata taratibu.

Pia amewataka wauguzi nchini kufanya kazi kwa weledi, uaminifu pamoja na kufuata maadili ya taaluma yao kwa kuwa maisha ya wagonjwa yako chini yao.

Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo (Jumatano, Oktoba 04, 2017) wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa 45 wa Chama cha Wauguzi Tanzania, mkoani Lindi.

“Naagiza viongozi wote kufuata na kuzingatia sheria. Kama kuna makosa ya kitaaluma, Mabaraza husika yashughulikie jambo hilo na ni marufuku kuwaweka ndani watumishi kwa tuhuma za kitaaluma.” 

Amesema kwamba katika sekta ya afya bila wauguzi ambao ni kundi kubwa kati ya Wanataaluma wa Afya, Serikali haitaweza kutekeleza ipasavyo mikakati mbalimbali iliyopangwa kwa ajili ya kuboresha sekta hiyo.

Katia hatua nyingine Waziri Mkuu amewaasa wauguzi wote nchini kuhakikisha wanazingatia kiapo cha maadili ya kazi yao na kwamba Serikali haitamvumilia yeyote atakae bainika kwenda kinyume.

“Nanyi Wauguzi mnao wajibu wa kutoa huduma kwa wananchi kwa kuzingatia kiapo na miiko ya taaluma yenu. Tunazo taarifa kuhusu baadhi ya Wauguzi kutoa lugha chafu kwa wagonjwa, kuomba rushwa na wengine kujihusisha na vitendo vya wizi wa dawa.”

Amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha afya za Watanzania wote zinaimarika ili kuendana na kasi ya utendaji kazi wa Serikali ya kuinua uchumi na kufikia wa kiwango cha kati, hivyo ni lazima watoe huduma bora kwa wananchi. 

Pia amewaomba waunge mkono kwa nguvu zote jitihada za Serikali katika kuhakikisha miundombinu na vifaa vyote havihujumiwi na watu wachache ili viwe msaada mkubwa hususani kwa akina mama wajawazito ili wajifungue salama.

Akizungumzia kuhusu upungufu wa wauguzi nchini, Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kuajiri watumishi wa kada mbalimbali wakiwemo Wauguzi na Wakunga na kuwapanga katika maeneo yenye upungufu zaidi.

Awali, Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Khamis Kigwangalla alisema baadhi ya viongozi katika maeneo mbalimbali wamekuwa wakiwakamata na kuwachukulia hatua watumishi wa Sekta ya Afya bila ya kufuata taratibu, jambo ambalo si sahihi.

Mkutano huo umehudhuriwa Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Kigwangalla,  Rais wa Chama cha Wauguzi Tanzania Bw. Paul Magesa, Mbunge wa Lindi Mjini Bw. Hassan Kaunje, Mbunge wa Kuteuliwa  Mama Salma Kikwete(MB) Viti maalum.

Wengine ni Mkurugenzi wa Huduma za Uuguzi na Ukunga Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bw. Gustav Moyo, Mwenyekiti wa Baraza la Uuguzi na Ukunga Tanzania Bw. Stewart Mbelwa.

Wengine ni Mbunge wa Viti Maalumu, Hamida Abdallah, Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo ya Uuguzi Bw. Ndementria Vermund, Rais wa Chama cha Madaktari Tanzania Dkt. Obadia Nyongolena wawakilishi wa wauguzi kutoka mikoa yote nchini.
Read More

WANAFUNZI WA KIKE MSISHAWISHIKE SOMENI KWA BIDII-MAJALIWA

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akisalimia na wanafunzi Kike wanaosoma WAMA_SHARIF Sekondari .iliyopo Mkoani Lindi .Kushoto ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) Mama Salma Kkikwete (MB) Waziri Mkuu ametembelea shule hiyo jana Oktoba 4,2017 alipokuwa katika ziara ya siku moja katika Mkoa wa Lindi jana

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa  ahamasisha utunzaji wa mazingira Nchini kwakupanda Mti jana  Oktoba 4/2017 katika Shule ya WAMA_ SHARIF SEKONDARI.iliyopo Mkoani Lindi ,kushoto mwenye fimbo ni Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto Daktari Hamisi Kigwangala na kulia kwa Waziri Mkuu ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA)  Mama Salma Kikwete (MB) Waziri Mkuu alifanya ziara ya siku moja jana Mkoani Lindi .

Read More

WANAFUNZI WA KIKE MSISHAWISHIKE SOMENI KWA BIDII-MAJALIWA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka wanafunzi wa kike wanaosoma katika shule mbalimbali nchini kusoma kwa bidii na wasikubali kushawishika.

Pia Waziri Mkuu amesema Serikali imeweka sheria kali kwa wote watakaobainika kukatisha masomo ya watoto wa kike kwa kuwapa ujauzito au kuwaozesha.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo jana (Jumatano, Oktoba 04, 2017) wakati akizungumza na wanafunzi wa shule ya Sekondari ya Wasichana na WAMA Sharaf.

Shule ambayo ipo wilayani Lindi inamilikiwa na Taasisi ya WAMA ambapo inasomesha watoto wa kike ambao ni yatima na wanaotoka katika mazingira magumu.

Waziri Mkuu amewataka wanafunzi hao wa kike kuhakikisha wanatumia muda wao vizuri kwa kusoma kwa bidii na hatimaye watimize malengo yao.

Amesema ni vema wanafunzi hao wakatumia vizuri fursa hiyo ya elimu wanayoipata shuleni hapo kwa kusoma kwa bidii na wafuate ratiba itakayokuwa inapangwa.

“Nawasihi mtumie muda huu kusoma kwa bidii ili muweke msingi imara ya kujenga maisha yenu ya baadae. Msikubali kushawishika na kukatisha masomo yenu.”

Naye, Mwenyekiti wa Taasisi ya WAMA, Mama Salma Kikwete ambaye pia ni mbunge wa Kuteuliwa alisema shule hiyo inasomesha watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu kutoka mikoa yote nchini.
Read More

Sunday, October 1, 2017

HABARI PICHA WAZIRI MKUU WA TANZANIA

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na waumini wa Jumuiya ya waislamu wa Ahmadiya Tanzania, kabla ya kufungua mkutano mkuu wa 48 wa Jumuiya hiyo huko Mbande, Temeke, Jijini Dar es salaam Oktoba 1, 2017.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimiana na kiongozi na mbashiri mkuu wa Jumuiya ya waislamu wa Ahmadiya Tanzania,Tahir Mahmood, kabla ya kufungua mkutano mkuu wa 48 wa jumuiya hiyo Mbande, Temeke, Jijini Dar es salaam Oktoba 1, 2017.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na waumini wa Jumuiya ya waislamu wa Ahmadiya Tanzania, kabla ya kufungua mkutano mkuu wa 48 wa Jumuiya hiyo huko Mbande, Temeke, Jijini Dar es salaam Oktoba 1, 2017.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipokea kitabu kutoka kwa Katibu wa Malezi Jumuiya ya waislamu wa Ahmadiya Tanzania, Mahmood Hamsin, baada ya kufungua mkutano mkuu wa 48 wa jumuiya hiyo Mbande, Temeke, Jijini Dar es salaam Oktoba 1, 2017. (kulia) ni. kiongozi na mbashiri mkuu wa Jumuiya ya waislamu wa Ahmadiya Tanzania,Tahir Mahmood.


Read More