Saturday, October 14, 2017

SERIKALI YAWEKA MIKAKATI MADHUBUTI KUKABILI MAAFA NCHINI

Serikali imejipanga kikamilifu katika kuhakikisha inayakabili maafa yanayotokea nchini kwa kuangalia sheria, Kanuni na Taratibu mbalimbali zinazohusika na masuala ya Menejimenti ya Maafa ili kuepuka madhara yatokanayo na maafa nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi Masaidizi Idara ya Uratibu wa Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Bashiru Taratibu wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Kupunguza Maafa yaliyofanyika Kitaifa mjini Dodoma na Kuwashirikisha wananchi, wanafunzi na wadau mbalimbali.

Katika kuhakikisha wananchi wanakuwa salama na kuepuka madhara yatokanayo na maafa tayari Serikali imepima Viwanja zaidi ya milioni moja na nusu katika Halmashauri mbalimbali hapa nchini ikiwa ni moja ya mikakati ya kuondoa makazi holela na kuepusha maafa yanayotokana na matumizi ya ardhi yasiyozingatia sheria kanuni na taratibu zinazosimamia sekta ya Ardhi.

“Wananchi wazingatie sheria, Kanuni, na Taratibu kwa kuepuka kujenga maeneo hatarishi kama mabondeni, maeneo yenye mafuriko na mengine yote yanayokatazwa kisheria ili kuepuka maafa” Alisisitiza Taratibu

Akifafanua Taratibu amesema kuwa Viongozi wa Serikali katika maeneo yote hapa nchini wanajukumu la kusimamia sheria zilizopo ili kuepusha maafa kwa kuzingatia Kauli mbiu ya mwaka huu inayosema “MAKAZI SALAMA: Punguza Makazi katika Maeneo Hatarishi, Punguza kuhama kutokana na maafa”.

Akizungumzia mikakati ya Serikali kuondoa maafa na kupunguza uwezekano wa kutokea kwa maafa amesema kuwa Idara ya Maafa imekuwa ikitoa elimu kwa Umma ili kuwasaidia wananchi kuwa na uelewa utakaosaidia kuepuka athari za maafa.

Aidha alitaja hatua nyingine zilizochukuliwa na Serikali kuwa ni kutungwa kwa sheria ya maafa ya mwaka 2015, Miongozo, Kanuni na kuwekwa kwa taratibu mbalimbali  za kusimamia masuala ya maafa hapa nchini.

Kwa upande wake Mratibu wa Maafa Wilaya ya Chamwino Bi Lilian Zakaria amesema kuwa wamekuwa wakitoa elimu kuanzia ngazi ya Wilaya hadi Vijjiji wakishirikisha Kamati za Maafa katika ngazi zote ili kuwajengea wananchi uwezo wa kupambana na maafa pale yanapotokea na pia kuzuia viashiria vyake.

Pia Bi Zakaria amewataka wananchi kuepuka kujenga na kuishi katika maeneo hatarishi na kuzingatia taratibu zote zilizowekwa na Serikali kuepuka maafa.

Naye Mwakilishi wa Asasi za Kirai Bw. Mussa Mussa amesema kuwa  wanaunga mkono juhudi za Serikali katika kupambana na maafa hali inayosababisha wananchi kuishi salama katika maeneo mbalimbali hapa nchini.

AWALI:
Chimbuko la Siku ya Kimataifa ya Kupunguza Maafa ilitokana na Azimio Na. 64/200 lililopitishwa na Baraza la Umoja wa Mataifa tarehe 21 Desemba, 2009 ambapo iliamuliwa Oktoba 13 ya kila mwaka ni Siku ya Kimataifa ya Kupunguza Maafa ikiwa na lengo la Kukuza utamaduni wa kupunguza madhara ya maafa kimataifa, ikiwa ni pamoja na kuzuia, kupunguza madhara, Kujitayarisha, Kukabili na Kurejesha hali kuwa bora zaidi na mwaka huu kaulimbili inasema: “MAKAZI SALAMA: Punguza Makazi katika Maeneo Hatarishi, Punguza Kuhama kutokana na Maafa


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.