Wednesday, February 11, 2026

SERIKALI YAHIMIZA USHIRIKISHWAJI JAMII YA WATU WASIOONA KATIKA SHUGHULI ZA KIJAMII, KIUCHUMI NA KIUTAMADUNI ILI KUONGEZA TIJA.


Serikali inatambua Breli si mfumo pekee wa kusoma, bali ni nyenzo ya kufungua milango ya elimu, ujuzi, ukarimu wa jamii, na ushiriki kamili wa kijamii.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu (SBUU) Mhe. Ummy Nderiananga kwa niaba ya Waziri wa Nchi wa Ofisi hiyo Mhe. William Lukuvi leo Jijini Dodoma huku akieleza kuwa Mfumo huo umebadilisha maisha ya mamilioni ya wasioona na wenye uoni hafifu duniani kote ikiwemo Tanzania.

“Kwa kutambua mchango wa Jamii ya Wasioona katika maendeleo ya taifa letu, Serikali imeendelea kufanya jitihada mbalimbali zinazolenga kuwawezesha wasioona kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo, miongoni mwa jitihada hizo ni pamoja na utekelezaji wa Sera, Sheria, Mikakati na Mipango inayojumuisha huduma na teknolojia ya breli pamoja na kuimarisha elimu jumuishi kwa kuanzisha na kuendeleza shule na vituo maalum kwa wanafunzi wasioona, pamoja na kusambaza vifaa vya kufundishia na kujifunzia vya Breli, vitabu maalum na teknolojia saidizi” amefafanua Mhe. Waziri.

Aidha, Serikali imetenga madirisha maalum ya huduma kwa watu wenye ulemavu katika vituo vya kutolea huduma za afya, pamoja na kuboresha upatikanaji wa huduma za uchunguzi, tiba na utengamao kwa watu wenye ulemavu wakiwemo wasioona.

Vilevile, Serikali imeendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo katika kubuni na kutekeleza miradi ya uwezeshaji wananchi kiuchumi, mafunzo ya ujuzi na ajira kwa watu wasioona.

“Tunapoadhimisha kilele cha Siku ya Kimataifa ya Breli Duniani nitoe wito kwa kila mwananchi, taasisi za umma na binafsi, mashirika ya kiraia pamoja na wadau wa maendeleo kushirikiana kwa pamoja katika kuimarisha mazingira jumuishi, kuondoa vikwazo vya kijamii na kimazingira, na kuweka mifumo wezeshi itakayohakikisha Ustawi na Maendeleo ya jamii ya wasioona yanatimizwa kikamilifu. Kwa kufanya hivyo, Taifa letu litaendelea kujenga jamii yenye usawa, haki na mshikamano, inayothamini mchango wa kila mmoja bila ubaguzi” ameomgeza Mhe. Nderiananga

Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Breli huadhimishwa tarehe 12 Februari ya kila mwaka kwa lengo la kutoa nafasi kwa mataifa yote kutafakari kuhusu mchango na nafasi ya teknolojia ya Breli katika kuwawezesha watu wasioona kushiriki kikamilifu katika elimu, ujuzi na maendeleo ya taifa. Kaulimbiu ya mwaka huu inasema “Teknolojia ya Breli Husaidia Kuchochea Maendeleo kwa Wasioona na Ujenzi wa Taifa” na kwa Tanzania maadhimisho hayo yatafanyika katika Halmashauri zote na kwa ngazi ya Kitaifa yatafanyika mkoani Tanga. 

 

Breli ni mfumo ulioasisiwa na ndugu Louis Braille, ambaye alibuni njia ya maandishi inayowawezesha watu wasioona kusoma, kuandika na kupata elimu na habari kwa usawa na wale wanaoona. Mfumo huu unawapa watumiaji wa Breli fursa sawa za kushiriki katika maendeleo ya kijamii, kiuchumi, na kifikra. Tanzania inaungana na nchi nyingine duniani katika kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Breli.

Read More

TGPA YAPOKEA UGENI WA WACHAPISHAJI KUTOKA UGANDA KUIMARISHA USHIRIKIANO

 


Wakala wa Serikali wa Uchapishaji Tanzania (TGPA) leo umepokea ugeni wa watu 24 kutoka Shirika la Uchapishaji la Uganda (Uganda Printing and Publishing Corporation – UPPC) waliowasili nchini kwa ziara ya kikazi yenye lengo la kubadilishana uzoefu na kuimarisha ushirikiano katika sekta ya uchapishaji wa serikali.

Ujumbe huo umeongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa UPPC, Profesa Joackim Buwembo, ukijumuisha wajumbe wa bodi, Mpigachapa Mkuu wa Serikali ya Uganda, Profesa Sudi Nangoli, pamoja na watumishi kutoka idara mbalimbali za shirika hilo.

Kwa mujibu wa taarifa za TGPA, ziara hiyo imelenga kujifunza na kubadilishana uzoefu katika uchapishaji wa nyaraka za serikali, hususan Gazeti la Serikali, pamoja na uchapishaji wa nyaraka zenye alama za usalama (security printing).

Katika ziara hiyo, pande zote mbili zimefanya vikao vya kitaalamu na majadiliano yaliyolenga kuimarisha mifumo ya uchapishaji, kuongeza ubora wa huduma na kuzingatia viwango vya usalama katika uchapishaji wa nyaraka nyeti za serikali.

Aidha, TGPA na UPPC zimekubaliana kushirikiana katika maeneo ya uchapishaji, kuandaa mafunzo kwa watumishi wao, pamoja na kuanzisha utaratibu wa kubadilishana uzoefu kwa lengo la kuongeza ufanisi na kuimarisha mahusiano ya kitaasisi kati ya Tanzania na Uganda.

Ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za taasisi hizo kuendeleza ushirikiano wa kikanda katika sekta ya uchapishaji wa serikali na kuhakikisha huduma bora zinatolewa kwa kuzingatia viwango vya kimataifa.



Read More