Thursday, January 29, 2026

WANANCHI KUNUFAIKA NA MRADI WA RAMANI ZETU, SAUTI ZETU


 Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu imezindua mradi wezeshi wa “Ramani Zetu, Sauti Zetu”, unaolenga kuwajengea uwezo Wananchi wa Mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro na Pwani katika kukabiliana na Majanga.

Akizungumza katika Uzinduzi huo uliofanyika leo Jijini Morogoro Mkurugenzi Msaidizi wa Operesheni na Uratibu wa Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu) Kanali Selestine Masalamado amesema, mradi huo umekuja wakati mufaka ambao jitihada kubwa zikiwa zinaendelea za kuzuia majanga ya asili maeneo mbalimbali ya nchi.

Aidha, ameeleza kuwa “tunahitaji uwepo wa data sahihi za wakati bila kusahau ushirikishwaji wa moja kwa moja wa jamii katika kuendelea kukabiliana na majanga ya asili na athari zake”

“Mpango huu unaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 inayolenga kujenga taifa lenye jamii imara yenye uwezo wa kutumia maarifa ya teknolojia katika kufanya maamuzi ya maendeleo” aliongeza Kanali Masalamado.

Naye, Mkurugenzi wa Taasisi ya OpenMap Development Tanzania (OMDTZ) Bw. Innocent Maholi, amesema Mradi huo unalenga kuimarisha mifumo ya tahadhari za mapema, ikiwa ni pamoja maandalizi na usimamizi wa maafa kwa kutumia teknolojia na ushiriki wa wananchi katika ukusanyaji wa taarifa muhimu za maeneo yao.

“serikali itaendelea kuuunga mkono juhudi hatua za usimamizi madhubuti wa maafa ambazo sehemu muhimu ya safari ya kuelekea maendeleo endelevu na uchumi imara wa wananchi,” alibainisha

Read More

Tuesday, January 27, 2026

DKT. KILABUKO AZINDUA NYARAKA ZA USIMAMIZI WA MAAFA NKASI


Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. James Kilabuko amezindua nyaraka za usimamizi wa maafa katika Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi mkoani Rukwa huku akisisistiza nyaraka hizo kutekelezwa kwa vitendo.

Dkt. Kilabuko amesema hayo wakati wa uzinduzi huo na kusema kuwa, hatua hiyo ni mwanzo wa kuanza kazi rasmi endapo kutatokea janga lolote, na kutoa wito kwa idara, vitengo na taasisi ngazi ya wilaya kuzingatia nyaraka hizo kwa kuhakikisha zinakuwa chachu ya kuongeza ushirikishwaji wa jamii na wadau katika masuala ya menejimenti ya maafa.

Ameongeza kuwa, hatua hiyo itasaidia kujenga uelewa wa jamii kuhusu masuala ya usimamizi wa maafa, kuimarisha mfumo wa utoaji wa tahadhari awali, kujenga uwezo wa kuzuia, kupunguza madhara na kujiandaa na kurejesha hali pindi maafa yanapotokea.

Dkt. Kilabuko alifafanua kuwa, nyaraka hizo zimekuja wakati sahihi kwa  kuzingatia kuwa, Wilaya imekuwa ikikabiliwa na maafa yanayosababishwa na majanga hasa ya upepo mkali, magonjwa ya mlipuko kwa binadamu na wanyama, mafuriko pamoja na mgongano wa wanyamapori na binadamu ambayo yamekuwa yakijirudia mara kwa mara.

“Nimeelezwa kuwa matokeo ya tathmini ya maafa iliyofanyika katika Halmashauri ya Nkasi mwezi Januari, 2026 yalionesha kuwa yapo majanga mengine ambayo yamekuwa yakijitokeza japo hayajaleta athari kubwa ikiwemo wadudu waharibifu wa mazao, ajali za barabarani, moto, ajali za majini, tetemeko la ardhi, radi pamoja na maporomoko ya ardhi.Natambua kuwa Wilaya imekuwa ikikabiliwa na mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu,nitumie fursa hii kuwapongeza kwa jitihada mnazoendelea nazo katika kukabiliana na ugonjwa huo,”Alisema Dkt. Kilabuko

Kwa hatua nyingine, Ameshukuru Shirika la Kuhudumia Watoto la Umoja wa Mataifa (UNICEF) kwa ufadhili ambao umewezesha kuchangia jitihada za Serikali katika kuandaa Mpango wa Kujiandaa na Kukabiliana na Maafa pamoja na Mkakati wa Kupunguza Vihatarishi vya Maafa kwa Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi.

Naye Mkurugenzi Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Brigedia Generali Hosea Ndagala amesema Idara hiyo imekuwa ikichukua hatua za kuzuia, kujiandaa na kukabiliana na maafa na kurejesha hali pindi maafa yanapotokea kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu zilizopo.

Aliongezea kuwa,Serikali kwa kutambua hilo na katika kuhakikisha nchi inakuwa stahimilivu dhidi ya maafa, imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali. Jitihada hizo ni pamoja na kuweka utaratibu mzuri wa kushughulikia masuala ya maafa kwa kutunga Sera ya Taifa ya Menejimenti ya Maafa ya mwaka 2004, Toleo la Mwaka 2025 na Sheria ya Usimamizi wa Maafa Sura ya 242 ambayo imeweka mfumo mzuri wa usimamizi wa maafa kutoka ngazi ya Taifa hadi Kijiji/Mtaa.

“Ni muhimu kwa Halmashauri kuendelea kutenga fedha katika bajeti juu ya utekelezaji wa Mpango huu uliozinduliwa leo na kuendelea kutoa elimu kuhusu namna bora ya wananchi kuendelea kuchua hatua za awali kwa kuzingatia maafa ni suala mtambuka na linaanza na mtu mmoja,” alisisitiza

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Nkasi Mheshimiwa Peter Lijualikali ameishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu na UNICEF kwa kazi nzuri ya uandaaji wa nyaraka za usimamizi wa maafa na kutoa elimu juu ya masuala ya menejimenti ya maafa kwa Wilaya ya Nkasi na kuahidi kuzifanyia kazi nyaraka hizo.

“Wilaya imepata kitu chema kitakachotufaa, nasi tunaahidi kuzitumia kama miongozo sahihi ya kuleta matokeo kwa kuzingatia Serikali imeweka fedha katika kuhakikisha mipango inaleta matokeo yaliyokusudiwa, hivyo tusiwe nyuma, tufanyie kazi kwa tija ya Halmashauri nzima,” alisema Lijualikali

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Nkasi Mheshimiwa Richard Leonard Masai akitoa Salam ameshukuru uratibu mzuri wa uandaaji wa nyaraka hizo na kutoa rai kwa wananchi kuendelea kuchukua tahadhali za awali na kuzingatia taarifa za tahadhali zinazotolewa na wataalamu ili kuendeala kuwa na jamii iliyo salama na yenye kujiletea maendeleo yake.

 

Read More

Friday, January 23, 2026

KAMATI YAPONGEZA JUHUDI ZA SERIKALI UBORESHWAJI HUDUMA ZA AFYA

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Afya na Masuala ya UKIMWI Mhe. Dkt. Lembulung Lukumay ameipongeza Serikali kwa kuwekeza fedha katika ujenzi wa miundombinu ya sekta ya afya pamoja na uboreshaji wa upatikanaji vifaa tiba.

Dkt. Lukumay ametoa pongezi hizo leo Jijini Dodoma wakati akipokea taarifa ya Muundo na Majukumu ya Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) iliyo chini Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu.

 “Serikali imeongeza idadi ya madaktari wabobezi katika jitihada za kuboresha huduma za afya ikiwemo kuweka utaratibu mzuri wa kuendelea kuwezesha afua za UKIMWI kwa kutegemea fedha zetu za ndani ili kuendeleza upatikanaji wa dawa,” alieleza Dkt. Lukumay.

 Aidha, amebainisha kuwa, wananchi hawana budi kuelezwa juhudi zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mhe. Rais, Dkt, Samia Suluhu Hassan katika uimarishaji wa huduma za afya, katika ngazi ya Zahanati, Vituo vya afya, hospitali za Wilaya na hospitali za Mikoa.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. William Lukuvi ameahidi kuendelea kushirikiana na kamati kwa ukaribu  na kufanyia kazi kwa ukamilifu ushauri na maelekezo yatakayotolewa na kamati




Read More

Thursday, January 22, 2026

NDUMBARO AIPONGEZA OFISI YA WAZIRI MKUU KWA UTENDAJI BORA


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Damas Daniel Ndumbaro, ameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) pamoja na taasisi zake kwa utendaji mzuri katika kuratibu shughuli za Serikali zinazogusa maisha ya wananchi.

Pongezi hizo zimetolewa leo jijini Dodoma wakati wa uwasilishaji wa taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Ofisi ya Waziri Mkuu mbele ya Kamati hiyo ya Bunge.

Mhe. Ndumbaro amesema maeneo ya uratibu wa maafa na uwezeshaji wa wananchi kiuchumi yanahitaji kuendelea kupewa kipaumbele ili Serikali iendelee kuwafikia wananchi kwa ufanisi.

Kwa upande wake, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Mhe. Ummy Nderiananga, amesema Serikali imetenga fungu maalum la fedha kwa ajili ya afua za UKIMWI pamoja na kushughulikia masuala ya maafa kila mwaka wa bajeti, hatua itakayohakikisha utekelezaji endelevu wa majukumu hayo nchini.



Read More

Wednesday, January 21, 2026

SERIKALI KUSHIRIKIANA NA VYUO VIKUU KUIMARISHA UWAJIBIKAJI KATIKA UTEKELEZAJI WA SHUGHULI ZA UMMA


 

Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, kupitia Idara ya Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji wa Serikali, imesaini Hati za Mashirikiano (MoU) na Vyuo Vikuu vinne ambavyo ni Chuo Kikuu cha Dodoma, Chuo Kikuu cha Mzumbe, Chuo Kikuu cha Usimamizi wa Fedha na Taasisi ya Uhasibu Tanzania kwa lengo la kuimarisha mfumo wa ufuatiliaji na tathmini unaotumia ushahidi katika kupanga na kutekeleza sera, mipango, programu na miradi ya maendeleo. 

Akizungumza wakati wa hafla hiyo iliyofanyika leo  jijini Dodoma, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (SBUU) Dkt. Jim Yonazi amesema kupitia mashirikiano hayo, Serikali na Vyuo Vikuu vitashirikiana katika kuimarisha uwezo wa wataalamu wa ufuatiliaji na tathmini, kufanya tathmini za pamoja za miradi ya maendeleo, kuendeleza tafiti bunifu na kuhakikisha maarifa yanayozalishwa vyuoni yanatumika kuboresha utendaji wa Serikali.

"Mafanikio ya MoU hizo yatapimwa kwa utekelezaji wake, kwa kuzingatia maelekezo ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, yenye msisitizo wa matokeo yanayopimika na manufaa halisi kwa wananchi" ameongeza Dkt. Yonazi.

Awali, akizungumza kwa niaba ya Makamu Wakuu wa Vyuo Vikuu vilivyoshiriki katika hafla hiyo, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma Prof. Lughano Kusiluka amesema kuwa, Ufuatiliaji na Tathmini ni eneo muhimu kwa ajili ya maendeleo ya taifa na Vyuo Vikuu vinaahidi kushirikiana na serikali katika kuhakikisha tunafanya vizuri katika eneo hilo ili nchi zinazotuzunguka wajifunze kutoka Tanzania.

Aidha, Mkurugenzi wa Idara ya Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji wa Serikali Bi. Sakina Mwinyimkuu amesema kuwa ushirikiano huo wenye nia ya pamoja una malengo ya kuongeza nguvu ya kusaidia taifa na kujenga tamaduni ya uwajibikaji.

Read More

Tuesday, January 20, 2026

MHE. LIJUALIKALI ATOA NENO KWA KAMATI ELEKEZI YA WILAYA YA USIMAMIZI WA MAAFA

 


Mkuu wa Wilaya ya Nkasi, Mheshimiwa Peter Lijualikali amepongeza Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu kwa namna ilivyoratibu zoezi la uandaaji wa Rasimu za Nyaraka za Usimamizi wa Maafa kwa Wilaya yake huku akiwasihi wajumbe wa kamati kuzitumia kama ilivyokusudiwa mara baada ya uzinduzi utakaofanyika hivi karibuni.

Ameyasema hayo leo wakati wa kikao cha Kamati Elekezi ya Wilaya ya Usimamizi wa Maafa ikihudhuriwa na timu ya wajumbe hao wakiongozwa na mkuu wa Wilaya huyo ambaye ndiye Mwenyekiti wa Kamati.

“Kipekee nawapongea Ofisi ya Waziri Mkuu na UNICEF kwa kuona umuhimu wa kuja katika Wilaya yetu ya Nkasi, na tutahakikisha kile mlichokifanya hapa Nkasi kinaleta matokeo chanya hasa kwa elimu tuliyoipata ya masuala ya usimamizi wa maafa hususani katika kuzuia na kujiandaa ili kusiwe na athari kubwa endapo majanga yatatokea,” alieleza Mhe. Lijualikali.

Naye Mratibu wa Maafa Mkoa wa Rukwa Bi. Aziza Kalyatila amesema ipo haja ya kuendelea kupewa elimu zaidi ya masuala ya usimamizi wa maafa kwani itasaidia katika kuwajengea uwezo wa kuzuia, kujiandaa, kukabili, na kurejesha hali pindi maafa yanapotokea.

Kikao hicho kimeandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) pamoja na timu ya wataalamu kutoka ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi kikilenga kuwapitisha katika nyaraka zilizoandaliwa kwa ajili ya matumizi ya Halmashauri ambazo ni Tathmini ya Vihatarishi vya Majanga, Uwezekano wa Kuathirika na Uwezo wa Kukabiliana na Majanga, rasimu ya Mpango wa Kujiandaa na Kukabiliana na Maafa pamoja na rasimu ya Mkakati wa kupunguza vihatarishi vya maafa.

 

Read More

Monday, January 19, 2026

NKASI YAJENGEWA UWEZO MASUALA YA MENEJIMENTI YA MAAFA


Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu imewajengea uwezo wajumbe wa Kamati ya Wataalamu ya Usimamizi wa Maafa ya Wilaya ya Nkasi Mkoani Rukwa ili kuhakikisha jamii inakuwa stahimilivu wakati wa majanga.

Elimu hiyo imetolewa na timu ya wataalamu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu wakati wa kikao cha kupitia Rasimu za Nyaraka za Usimamizi wa Maafa za Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi kwa Kamati za Usimamizi wa Maafa wilayani humu ikiongozwa na  na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo.

Kikao hicho kimeandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu kwa kushirikiana na timu ya wataalamu kutoka ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi kikilenga kuwapitisha katika nyaraka zilizoandaliwa kwa ajili ya matumizi ya Halmashauri ambazo ni Tathmini ya Vihatarishi vya Majanga, Uwezekano wa Kuathirika na Uwezo wa Kukabiliana na Majanga, Mpango wa Kujiandaa na Kukabiliana na Maafa pamoja na Mkakati wa kupunguza vihatarishi vya maafa.

Akitoa neno la shukran mara baada ya kikao hicho Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi Bw. Eliud Njogellah amepongeza kazi iliyofanyika na timu ya kuandaa nyaraka hizo huku akieleza kuwa zimekuja kwa wakati sahihi ambapo Halmashauri imekuwa ikikumbwa na majanga na maafa mbalimbali hivyo zitatumika kwa uzito wake na tija iliyokusudiwa.

Read More

WAJUMBE BARAZA KUU JUMUIYA YA WAZAZI CCM TAIFA WAIPONGEZA SERIKALI KWA UJENZI WA MJI WA SERIKALI MTUMBA

 


Wajumbe wa Baraza Kuu la Jumuiya ya Wazazi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Taifa, wakiongozwa na Mwenyekiti Fadhili Maganya, wameipongeza Serikali ya Awamu ya Sita kwa ujenzi wa mji wa Serikali, Mtumba.

Bw. Maganya ametoa pongezi hizo alipoongoza ujumbe wa Baraza Kuu la Jumuiya ya Wazazi ya CCM Taifa kutembelea Mji wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma.

"Tunaona namna Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais na Mwenyekiti wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan inavyotekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwa ujenzi wa Mji huu wa kisasa ambao sio tuu watu kuja kufanya kazi bali hata kukuza  utalii wa ndani" amesema Bw. Maganya.

Aidha, Bw. Maganya ameongeza kuwa, ujenzi wa barabara, majengo ya kisasa na matumizi ya samani zilizotengenezwa ndani ya nchi vinaonesha thamani ya fedha zinazotolewa na Serikali na kuahidi kushirikiana na Serikali katika upandaji wa miti ili kuwa sehemu ya kutimiza malengo ya utunzaji wa mazingira katika mji huo.

 Awali, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Mheshimiwa Ummy Nderiananga amesema, Ofisi ya Waziri Mkuu (SBUU) itaendelea na uratibu wa ujenzi wa mji wa Serikali kwa kiwango kinachohitajika na amewashukuru Jumuiya ya Wazazi Taifa kwa  kutenga muda wa kutembelea Mji wa Serikali ili kujionea kwa macho utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Akiwakaribisha Wajumbe hao, Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Uratibu wa Shughuli za Serikali kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Paul Sangawe amesema, Ofisi ya Waziri Mkuu inapokea wageni mbalimbali wanaotaka kutembelea Mji wa Serikali Mtumba na kuufanya Mji huo kuwa kivutio cha utalii.

Read More

Monday, December 1, 2025

DAWA ZA KUFUBAZA MAKALI YA VVU (ARV) ZIPO KWA ASILIMIA 100- WAZIRI LUKUVI

 


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe. William Lukuvi, amewahakikishia Watanzania kuwa dawa za kufubaza makali ya Virusi vya UKIMWI (ARVs) zinapatikana kwa asilimia 100 nchini na zinatolewa bila malipo kwa watu wote wanaoishi na VVU (WAVIU).

Amesema hayo leo Jijini Dar es Salaam wakati akitoa Tamko la Serikali kuhusu Maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani ambapo kwa mwaka 2025 yamefanyika chini ya kaulimbiu: “Imarisha Mwitikio, Tokomeza UKIMWI”.

 Waziri Lukuvi amesema upatikanaji wa dawa hizo umeendelea kuimarika, huku idadi ya WAVIU wanaotumia Dawa za ARV ikiongezeka kutoka asilimia 98 mwaka 2024 hadi asilimia 98.5 mwaka 2025, hatua inayochochea kupungua kwa athari za UKIMWI na kuboresha afya za wananchi.

 Aidha, Waziri Lukuvi amebainisha kuwa Serikali imeongeza idadi ya vituo vinavyotoa huduma za tiba na matunzo kwa WAVIU ili kurahisisha upatikanaji wa huduma za VVU na UKIMWI nchini. Vituo hivyo vimeongezeka kutoka vituo 7,805 mwaka 2024 hadi vituo 8,203 mwaka 2025.

 Ameongeza kuwa, huduma za ufuatiliaji wa matibabu kwa WAVIU zinaendelea kuimarishwa, huku serikali ikiboresha upatikanaji wa huduma za maabara kwa kuongeza mashine za kupima wingi wa VVU mwilini. Kwa sasa, zipo mashine kubwa 50 kutoka 43 mwaka 2024, na mashine ndogo 127, hivyo kufanya kuwa na jumla ya mashine 177 zinazoendelea kutoa huduma nchini.

 Katika tamko lake, Waziri Lukuvi amesisitiza kuwa Siku ya UKIMWI Duniani ni muhimu kwa kutathmini hali na mwelekeo wa kudhibiti VVU na UKIMWI nchini na kimataifa, kuhamasisha jamii kushiriki kikamilifu katika mapambano dhidi ya maambukizi mapya, kuwakumbuka waliopoteza maisha kutokana na ugonjwa wa UKIMWI, na kuwaenzi watu wanaoishi na VVU pamoja na yatima wanaotokana na athari za UKIMWI.

 Amesema Serikali inaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha kuwa ajenda ya kudhibiti UKIMWI inaendelea kupewa kipaumbele katika ngazi zote za uongozi na utungaji sera


Read More

Thursday, November 27, 2025

WANANCHI WAASWA KUWAUNGA MKONO WATU WENYE ULEMAVU

 


Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. Ummy Nderiananga ametoa wito kwa wananchi kuendelea kuwaunga mkono Watu Wenye Ulemavu ili kuendelea kuvumbua vipaji vyao katika maeneo mbalimbali.

Naibu Waziri ametoa wito huo leo Jijini Dodoma katika Ukumbi PSSSF wakati wa uzinduzi wa Msimu wa Pili wa Mashindano ya kusoma Quran kwa Watu Wenye Ulemavu yaliyoandaliwa na Taasisi ya Lulida.

Ameeleza kwamba, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kushirikiana na Wenye Ulemavu bega kwa bega ili kuhakikisha masuala mbalimbali yanayowahusu yanapewa kipaumbele.

“Nipo kwenye hatua ya kupita katika makundi mbalimbali ili kusikiliza changamoto na kuweka mikakati ya muda mrefu na muda mfupi katika kuzifanyia kazi,” alisema Naibu Waziri Nderiananga.

 Aidha, aliongeza kusema, “nimefurahishwa na taasisi ya Lulida kwa kuanzisha jambo hili kwa sababu ni sehemu ya kujali Watu Wenye Ulemavu kuona vipaji vyao na vipawa vyao”.

Naye Mwenyekiti wa Taasisi ya Lulida Mhe. Hajjat Riziki Lulida ametoa rai kwa vyombo vya habari  kuendeleza upendo na kujikita katika kuandika habari zenye kujenga misingi ya umoja na ushirikiano kwa jamii.



Read More

Thursday, October 23, 2025

“WAKUU WA VITENGO VYA UFUATILIAJI NA TATHMINI WA SEKRETARIETI ZA MIKOA WAJENGEWA UWEZO WA MASULA YA UFUATILIAJI NA TATHMINI NCHINI”


 Wakuu vitengo vya Ufuatiliaji na Tathmini kwa Mikoa wajengewa uwezo ili kuimarisha ufanisi katika Ufuatiliaji, Tathimini na upimaji wa Utendaji wa shughuli za Serikali katika ngazi ya Mikoa na Halmashauri ili kuweza kujipima katika utendaji wa kazi.

Akizungumza wakati wa Ufunguzi wa kikao hicho kilichofanyika Mkoani Singida Mkurugenzi Msaidizi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) kutoka Idara ya Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji wa Serikali (Sehemu ya Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa Bw. John Bosco Quman amesema Ufuatiliaji na Tathmini huratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuzingatia ibara ya 52 (1) (3) inayokasimu Madaraka kwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa msimamizi Mkuu wa Shughuli za Serikali siku hadi siku.

“Ni muhimu kuelewa dhana mbalimbali zinazohusiana na masuala ya Ufuatiliaji, Tathmini kwa kuzingatia Upimaji na Utendaji wake, pamoja na kufanya ufuatiliaji wa afua mbalimbali za Serikali zinazojumuisha; Sera, Mipango, Mikakati, Miradi na Programu zinazotekelezwa kwenye Ofisi za Wakuu wa Mikoa na Halmashauri zote nchini, alieleza Bw, Quman.

Aidha Serikali inaendelea kukamiikisha Sera ya Kitaifa ya Ufuatliaji na Tathmini Nchini ambayo ipo katika hatua za Uandishi baada ya kupita katika kamati ya Kitaifa ya uchambuzi wa Sera.

Bw. Quman amesema, jitihada zinaendelea katika Mashirika ya Umma pamoja na Makampuni ya Serikali ili kuwa na Idara za Ufuatiliaji na Tathmini zinazojitegemea kama ambavyo msisitizo ulivyowekwa katika ngazi ya Mikoa na Halmshauri ili kuhakikisha vitengo hivi vinajitegemea na kutekeleza majukumu yake.

Read More

Wednesday, October 15, 2025

SERIKALI YATANGAZA FURSA ZA UWEKEZAJI WA UTALII WA MIKUTANO KATIKA MJI WA SERIKALI MTUMBA

Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) imetangaza rasmi fursa za uwekezaji katika Mji wa Serikali Mtumba, hususan katika sekta ya utalii wa mikutano, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kukuza shughuli za kiuchumi katika Makao Makuu ya Nchi, Dodoma.

 Tangazo hilo limetolewa na Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Uratibu wa Shughuli za Serikali, Bw. Paul Sangawe, wakati wa mazungumzo rasmi na Mtendaji Mkuu wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC), Bi. Christine Mwakatobe yaliyofanyika leo Jijini Arusha.

 Katika mazungumzo hayo, Bw. Sangawe ameeleza kuwa Serikali imetenga maeneo maalum katika Mji wa Serikali kwa ajili ya ujenzi wa Kituo Kikubwa cha Kimataifa cha Mikutano, hoteli za kisasa, na maeneo ya huduma za kifedha, biashara na burudani. Amesisitiza kuwa uboreshaji wa miundombinu mikubwa kama reli ya kisasa (SGR) na uwanja wa ndege wa kimataifa wa Msalato ni miongoni mwa sababu kuu zitakazochochea mahitaji ya huduma hizo.

 “Kituo hiki kitasaidia kuimarisha hadhi ya Dodoma kama Makao Makuu ya Nchi, na pia kuifanya Tanzania kuwa kivutio kikubwa cha mikutano ya kikanda na kimataifa,” alisema Bw. Sangawe.

Kwa upande wake, Bi. Mwakatobe ameahidi AICC kuipa Dodoma kipaumbele katika uwekezaji, na kueleza kuwa taasisi hiyo iko tayari kushirikiana na Serikali kuhakikisha miradi hiyo inatekelezwa kwa viwango vya kimataifa.

 Ujenzi wa kituo hicho unatarajiwa pia kuambatana na maeneo ya maonesho ya biashara, hoteli za nyota tano, maduka, ofisi na maeneo ya kupumzikia, hatua inayolenga kuongeza mchango wa sekta binafsi katika maendeleo ya Mji wa Serikali.

 

Read More

Monday, September 29, 2025

DKT. YONAZI: TUIMARISHE LISHE, TUPUNGUZE MAGONJWA SUGU

 


KATIBU Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi amewataka wadau kushirikiana na Serikali katika kuimarisha hali ya lishe nchini ili kupunguza kasi ya kuenea kwa magonjwa yasiyo ya kuambukiza.

Amesema ulaji usio faa na mitindo mibaya ya maisha vimechangia kuongezeka kwa magonjwa sugu yasiyo ya kuambukiza jambo linalohatarisha maendeleo ya Taifa.

Dkt. Yonazi ameyasema hayo jijini Dar es salaam leo katika Mkutano Mkuu wa 11 wa Wadau wa Lishe unaoendelea katika kituo cha mikutano cha APC Bunju.

 Dkt. Yonazi amesema tafiti zinaonesha kuwa uzito uliozidi na uliokithiri ni chanzo kikuu cha magonjwa sugu yasiyo ya kuambukiza yakiwemo  kisukari, moyo, figo na baadhi ya saratani.

“Napenda kukumbusha wadau, taasisi na wataalam kushirikiana na serikali kufanya tafiti zitakazosaidia kuleta majibu ya changamoto za lishe, pamoja na kusaidia watu kubadili tabia za ulaji na mtindo wa maisha ili kuzuia magonjwa sugu yasiyo ya kuambukiza yanayohusiana na ulaji usiofaa na ambayo ni tishio kwa Taifa letu,”alisema Dkt. Yonazi

Dkt.Yonazi ameongeza kuwa  Takwimu zinaonesha  licha ya hali ya lishe nchini kuendelea kuimarika bado kuna changamoto hususani kwenye uzito uliozidi na kiriba tumbo hii kutokana maendeleo tunayoyapata na mabadiliko ya mtindo wa maisha hususani  ulaji usiofaa hivyo jitihada za pamoja kati ya wadau na serikali zinahitajika ili kukabiliana na tatizo hili.

Akizungumza kuhusu mkutano huo Dkt. Yonazi amesema lengo ni kupokea na kujadili hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa afua za lishe kwa kipindi cha Mwaka wa Tatu 2024/2025 katika maeneo mahsusi yaliyoanishwa kwenye Mpango Jumuishi wa Kitaifa wa Lishe (2021/22-2025/26).

Vilevile amesema mkutano huo unatoa fursa kwa wadau wote wa lishe kujadili namna utekelezaji ulivyofanyika, changamoto na mikakati ya kufanikisha utekelezaji katika kipindi kilichobaki cha utekelezaji wa mpango huo hususan mwaka 2025/26.

Kwa mujibu wa Dkt. Yonazi mkutano huo unatazamiwa kuongeza msukumo mpya wa utekelezaji wa afua za lishe miongoni mwa wadau kama moja ya nguzo muhimu kwa maendeleo ya Taifa.

“Uwepo wenu hapa, ni uthibitisho tosha wa ushirikiano mlionao na utayari wenu katika kuhamasisha uboreshaji wa hali ya lishe kwa Watanzania, hususani makundi yanayoathirika zaidi ambayo ni watoto wadogo na wachanga, watu wenye mahitaji maalum, wanawake wajawazito na wale walio katika umri wa uzazi,”amesema Dkt. Yonazi.

Dkt. Yonazi amewashukuru  wadau wote walitoa mchango wa fedha na ushauri wa kitaalamu katika kufanikisha maandalizi ya mkutano huo na amewahakikishia kuwa serikali itaendelea kuunga mkono juhudi za wadau ili kuhakikisha Taifa linapata mafanikio dhidi ya mapambano ya tatizo la utapiamlo.

 


Read More

Thursday, September 25, 2025

DKT. YONAZI ATOA WITO WATUMISHI KUBEBA MAONO YA DIRA YA TAIFA 2050

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Dkt. Jim Yonazi, ametoa wito kwa Viongozi, Menejimenti na Watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zake kubeba malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 kama sehemu ya wajibu wao wa kitaifa ili kuweza kufikia maono yaliyopo kufikia mwaka 2050.

 Dkt. Yonazi ametoa wito huo wakati ufunguzi wa Kikao cha Mazingativu ya Menejimenti, Wakuu wa taasisi na Watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu na taasisi zake kinachofanyika leo Jijini Arusha.

 “Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 tayari imeshazinduliwa, Dira hii ni ramani ya mustakabali wa nchi yetu, ikitupa taswira ya nchi ambayo tunaihitaji kuwa nayo katika ndani ya miaka 25 ijayo, ili kufanikisha maono haya kila mmoja wetu anawajibu na anajambo la kulifanya, ni wajibu wetu kujiuliza kwamba nitachangia nini kuhakikisha nchi yangu inafikia maono haya kufikia mwaka 2050” ameeleza Dkt. Yonazi.

 Aidha, amebainisha kuwa, kila mmoja mahali pake pa kazi anawajibu kwa kuhakikisha nchi ya Tanzania inakuwa nchi bora na mahali bora pa kuishi kwa kuweka misingi bora ifikapo mwaka 2050.

 Akizungumza kuhusu kikao hicho, Dkt. Yonazi amebainisha kuwa, kikao hicho ni sehemu ya utamaduni wa Ofisi ya Waziri Mkuu kutenga muda kila mwaka kwa ajili ya kujitafakari, kujifunza na kujipanga upya kwa lengo la kuboresha utendaji katika kutekeleza majukumu ya Ofisi hiyo.

 Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Arusha, Joseph Mkude akimuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Arusha CPA. Amos Makalla ametoa wito kwa Watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu kuwa wabunifu katika kufikiri na kutekeleza majukumu yao, ili kuweza kutoa huduma zinazokidhi mahitaji na matarajio ya wananchi kwa ufanisi zaidi.

“Dunia ya sasa inabadilika kwa kasi kubwa na changamoto zake zinahitaji mbinu mpya za kuzikabili, ni wajibu wetu kuwa wabunifu katika kufikiri na kutekeleza majukumu yetu, ili tuweze kutoa huduma zinazokidhi mahitaji na matarajio ya wananchi kwa ufanisi zaidi. Hivyo, kubadilika kulingana na wakati ni muhimu ili kuendana na mabadiliko ya kidunia, kitaifa na kijamii, tukizingatia misingi hii, tutakuwa na Ofisi yenye weledi, inayothamini maendeleo endelevu na inayokabiliana na changamoto kwa mafanikio” alisema.

 Aidha, Mkuu wa Wilaya huyo amebainisha kuwa “Kwa kuwa jukumu la uratibu, ufuatiliaji na tathmini ya shughuli zote za Serikali lipo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, nitumie fursa hii kutoa rai kuwa tuendelee kulitekeleza jukumu hili kwa ufanisi wa hali ya juu. Kila taasisi inapaswa kuonesha matokeo halisi katika maeneo yake ya utekelezaji, tuweke mkazo zaidi katika kuhakikisha kwamba kazi zetu zinajikita kwenye matokeo yanayogusa maisha ya wananchi, badala ya kuishia kwenye michakato au utekelezaji usioonesha matokeo”.

Mbali na hayo Mhe. Mkude ametoa wito wa kushiriki uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani kwani Uchaguzi huo ni fursa ya kipekee kushiriki katika kuimarisha misingi ya demokrasia na utawala bora.

 “Kila Mtanzania anatakiwa kutimiza haki na wajibu wake wa kikatiba kwa kupiga kura, ili kuchagua viongozi watakaoliongoza Taifa letu katika ngazi zote, aidha, ni wajibu wa kila mmoja wetu kuhakikisha tunadumisha amani, mshikamano na utulivu katika kipindi chote cha uchaguzi, ili Tanzania iendelee kubaki kuwa mfano bora wa utulivu, mshikamano na demokrasia barani Afrika” ameongeza.

 Kikao hicho kinaendelea Jijini Arusha, na mada mbalimbali zitawasilishwa ikiwemo ikiwemo Matumizi ya Akili Unde (AI) mahala pa kazi na mustakabali wa ajira kutokana na maendeleo ya kasi ya sayansi na teknolojia, masuala ya afya ya akili, fursa za uwekezaji kwa watumishi na maandalizi ya maisha baada ya kustaafu, masuala ya itifaki na ustaarabu na Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050, ili kuweza kujiimarisha katika nyanja mbalimbali kitaaluma, kimaisha na kiutumishi.



Read More

Sunday, September 21, 2025

UBUNIFU UENDELEZAJI MAKAO MAKUU, MJI WA SERIKALI WAHITAJIKA- DKT. YONAZI

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi amesisitiza ubunifu katika uendelezaji wa Makao Makuu na Mji  Serikali ili kuweza kuvutia watalii wa ndani na nje.

Dkt. Yonazi ametoa msisitizo huo wakati wa ziara yake nchini Malaysia alipotembelea Mji Mkuu wa Utawala wa Malaysia uitwao Putrajaya.

"Ni muhimu wataalam kuzingatia masuala yanayofanya mji wa Serikali kuwa kivutio kwa wananchi na watalii kutoka nje. Masuala hayo ni ubunifu katika majengo, utunzaji wa mazingira na miundombinu na huduma muhimu hasa nyumba za ibada, huduma za fedha na maeneo ya kupumzika" amesema Dkt. Yonazi.

Aidha, Dkt.  Yonazi ameahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano na taasisi za Kimataifa ili kubadilishana uzoefu na kujifuza masuala ambayo yataongeza tija na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Serikali kwa ujumla.

Katika ziara hiyo Dkt. Yonazi ameambata na Balozi wa Tanzania nchini Malaysia Mhe. Dkt. Mahadhi Maalim, Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Uratibu wa Shughuli za Serikali Bw. Paul Sangawe, Wataalam kutoka Ubalozi wa Tanzania Nchini Malaysia na kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu.


Read More

Tuesday, September 16, 2025

DKT. YONAZI ATANGAZA FURSA ZILIZOPO MAKAO MAKUU YA MJI WA SERIKALI DODOMA NCHINI KOREA.


 Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi leo tarehe 16 Septemba, 2025 ameshiriki Mkutano wa Kimataifa wa Uendelezaji Miundombinu unaofanyika Jijini Seoul nchini Korea.

Katika Mkutano huo Dkt. Yonazi amepata fursa ya kuwasilisha mada kuhusu hatua iliyofikiwa katika zoezi lakuhamisha Makao Makuu na fursa za uendelezaji wa Jiji la Dodoma pamoja na Mji wa Serikali.

Aidha, Dkt. Yonazi amekutana na Mwenyekiti wa KFINCO na taasisi inayoratibu uendelezaji wa Mji wa Serikali Korea (National Agency For Administrative City Construction of KOREA-NA ACC) kwa lengo la kuimarisha ushirikiano katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo pamoja na utekelezaji wa makubaliano ya ushirikiano baina Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) na Taasisi ya NAACC.

Katika mkutano huo, Dkt. Jim Yonazi ameongozana na Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Uratibu wa Shughuli za Serikali Bw. Paul Sangawe na wajumbe wengine kutoka Tanzania.



Read More

Saturday, September 6, 2025

AFDP YADHAMIRIA KUONGEZA UPATIKANAJI WA MBEGU BORA NCHINI

 


Ujumbe wa Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kwa kushirikiana na Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), umesema utaendelea kuwekeza katika uzalishaji na upatikanaji wa mbegu bora ili kuongeza tija kwa wakulima nchini.

Kauli hiyo imetolewa na kiongozi wa ujumbe huo, Bi. Nester Mashingaidze, alipozungumza na wakulima wa Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro, alipokuwa akikagua utekelezaji wa programu hiyo inayolenga kuongeza uzalishaji wa mahindi, alizeti, maharage na mimea jamii ya mikunde.

“Tunalenga kuongeza upatikanaji wa mbegu bora kwa kushirikiana na taasisi kama TARI, ASA, na TOSCI ili kuwafikia wakulima wengi zaidi kwa wakati,” alisema Bi. Mashingaidze.

Kwa upande wake, Bw. Salum Mwinjaka – Mratibu wa Programu hiyo kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, alisema AFDP inatekelezwa katika mikoa 11 ya Tanzania Bara pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba. Alibainisha kuwa programu inajikita katika kilimo kinachohimili mabadiliko ya tabianchi, lishe na usawa wa kijinsia.

Naye, Mhandisi Enock Nyanda kutoka TAMISEMI, alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na wizara za kisekta kufikisha huduma kwa wananchi kwa ushirikiano na wadau wa maendeleo.

Wakulima waliopokea mafunzo kutoka kwenye programu hiyo wamesema imewasaidia kuachana na kilimo cha mazoea na kuhamia kwenye kilimo chenye tija kwa kutumia mbegu bora na za kisasa.



Read More

Tuesday, September 2, 2025

WAZALISHAJI WA MBEGU MKALAMA WAOMBA SERIKALI KUIMARISHA UFUNGASHAJI

 


Wazalishaji wa mbegu za alizeti katika Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama, mkoani Singida, wameiomba Serikali kuongeza juhudi katika kuwawezesha kuandaa vifungashio bora vya mbegu ili kuongeza thamani ya mazao yao sokoni. 

 Wito huo umetolewa  wakati wa ziara ya ujumbe wa Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kwa kushirikiana na wawakilishi kutoka IFAD katika Kijiji cha Ilunda, waliokuja kufuatilia utekelezaji wa programu hiyo. 

Bw. Athumani Ramadhani, mzalishaji wa mbegu aina ya Record, alisema: “Tunaomba Serikali itupe msaada wa kitaalamu kuandaa vifungashio bora vitakavyotangaza mbegu zetu na kuongeza thamani sokoni.” 

Naye Bi. Aziza Ramadhani aliongeza kuwa uzalishaji huo umeimarisha ushirikiano wao na taasisi za Serikali kama ASA na TOSCI, zinazopima ubora kabla ya mbegu kuingia sokoni. 

 Kwa Upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mkalama, Bi. Asia, alisema Serikali inalenga kuifanya Mkalama kuwa mfano bora katika utekelezajiwa Programu ya Kilimo na Uvuvi (AFDP), huku akisisitiza umuhimu wa kuongezwa nguvu katika sekta hiyo.

 


Read More

Monday, September 1, 2025

DKT. KILABUKO: OFISI YA WAZIRI MKUU ITAENDELEA KUSHIRIKIANA NA IFAD

 


Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Dkt. James Kilabuko, amesema Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) katika utekelezaji wa miradi ya kilimo na uvuvi nchini. 

Ametoa kauli hiyo Jijini Dodoma wakati wa kikao na ujumbe wa IFAD waliopo nchini kufuatilia utekelezaji wa mradi wa programu ya kuendeleza sekta ya Kilimo na uvuvi (AFDP). 

“Nawahakikishia kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu ipo tayari kutoa ushirikiano wote unaohitajika ili kuhakikisha miradi mnayoitekeleza inaleta matokeo chanya,” amesema Dkt. Kilabuko.



Read More

Saturday, August 23, 2025

SERIKALI KUGHARAMIA MAZISHI YA WALIOFARIKI KATIKA AJALI YA MGODI NYANDOLWA.

 


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge na Uratibu Mhe. William Lukuvi, amemfikishia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, salamu za pole kufuatia ajali ya kufukiwa kwa mafundi katika Mgodi wa Dhahabu wa Nyandolwa, iliyotokea tarehe 11 Agosti 2025 katika Mkoa wa Shinyanga.

Waziri Lukuvi ameeleza kuwa Serikali imepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za ajali hiyo, na kwa niaba ya Rais Samia, ametoa pole kwa familia zilizopoteza wapendwa wao katika tukio hilo la kusikitisha. Aidha, ameeleza kuwa Serikali itagharamia kikamilifu gharama za mazishi kwa waathirika wa ajali hiyo pamoja na matibabu kwa waliofikwa na tukio hilo.

Akizungumza na wanandugu wa marehemu na wale waliokwama mgodini, Mhe. Lukuvi amewatia moyo na kuwahakikishia kuwa Serikali ipo pamoja nao katika kipindi hiki kigumu. Ametoa wito kwa timu za uokoaji kuongeza juhudi na kasi ya uokoaji ili kuwaokoa mafundi waliokwama kwa haraka na usalama zaidi.

“Tunaamini kuwa kazi kubwa imefanyika lakini bado tunahitaji jitihada zaidi. Serikali inatambua uzito wa tukio hili na itaendelea kutoa ushirikiano wa karibu kwa kuhakikisha kila jitihada zinafanyika kwa ufanisi,” amesema Lukuvi.

Kwa upande wake, Msimamizi wa Mgodi huo, Fikiri, ameiambia Serikali kuwa ndani ya kipindi cha siku tatu hadi nne zijazo, zoezi la kuwaokoa wahanga waliokwama litakuwa limekamilika. Ameeleza kuwa vifaa vya kutosha vimeletwa eneo la tukio na wataalamu wanaendelea na kazi kwa umakini mkubwa kuhakikisha mafanikio ya haraka.

Kabla ya kuwasili katika eneo la mgodi, Mhe. Lukuvi alifanya ziara katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita, ambapo alipokea taarifa ya kina kuhusu maendeleo ya sekta ya madini katika mkoa huo pamoja na hali ya sasa ya shughuli za uokoaji zinazoendelea katika mgodi wa Nyandolwa.

Akizungumza kwa niaba ya ndugu wa wanasubiri waliofukiwa na kifusi Bw.Furaha Enock aliishukuru Serikali kwa namna ilivyoratibu zoezi na inavyowahudumia katika kipindi chote toka tukio kutokea na kueleza kuwa imefanya jambo la kipekee, la heshima na la uungwana kuwashika mkono na kuhudumia kwa hali na mali na kuwasihi wanandugu kuendelea kuwa na utulivu.

"Kipekee ninaipongeza Serikali Yetu imetufanyia wema na imetupa faraja kwa namna wanavyoratibu tukio zima, tunakosa neno zaidi ya Asante sana kwa Rais Dkt. Samia pamoja na uongozo wake wote," alisema Enock

AWALI

Ziara ya Waziri Lukuvi ni sehemu ya juhudi za Serikali za Uratibu na kutoa maelekezo kwa karibu katika kipindi hiki cha majonzi, huku ikilenga kuimarisha utendaji wa shughuli za uokoaji na kuhakikisha haki na heshima kwa waathirika wote wa ajali hiyo.

Read More

Thursday, August 21, 2025

SERIKALI YAENDELEA NA JITIHADA ZA UOKOAJI MGODI WA NYANDOLWA


Imeelezwa kuwa, jitihada za kuendelea kuokoa maisha baada ya ajali ya mgodi kutokea eneo la Nyandolwa Mkoani Shinyanga zinaendelea usiku na mchana ambapo hadi kufikia Leo Agosti 21,2025 mafundi 10 kati ya 25 waliokuwa wamekwama chini ya ardhi wameokolewa, huku wanne wakiwa hai, mmoja kati yao akifariki dunia muda mfupi baada ya kufikishwa hospitalini, na saba wakikutwa wamefariki dunia.

Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita wakati akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake Mkoani humo ambapo amethibitisha taarifa hizo na kusema kuwa tukio hilo lilitokea takribani siku 10 zilizopita, likisababisha shughuli za uokoaji kuendelea kwa muda mrefu katika mazingira magumu.

Amesema ajali hiyo ilitokea baada ya ardhi kutitia ghafla na kusababisha kifusi kuporomoka katika mashimo (maduara) matatu tofauti yaliyokuwa yakikarabatiwa na mafundi ndani ya mgodi huo, unaomilikiwa na kikundi cha Wachapakazi chini ya leseni ya uchimbaji mdogo.

"Tunaendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali kuhakikisha mafundi waliobaki wanatolewa salama. Hili ni tukio la huzuni kubwa kwa mkoa wetu na Taifa kwa ujumla," amesema Mhe. Mhita.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Dkt. James Kilabuko, ametoa wito kwa timu ya uokoaji kuongeza kasi na juhudi katika shughuli za uokoaji, akisisitiza kuwa kila sekunde ina maana katika kuokoa maisha ya waliobaki chini ya kifusi.

“Natoa pongezi kwa kikosi kizima cha uokoaji kwa moyo wao wa kujitolea, lakini ni muhimu sasa kuongeza kasi bila kuhatarisha usalama wa waokoaji wenyewe,” amesema Dkt. Kilabuko.

Naye, Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Dkt. Janet Lekashingo, amefika eneo la tukio na kutoa salamu za pole kwa familia za marehemu na wote walioathirika na ajali hiyo. Ametoa rai kwa waokoaji kuendelea kuwa na umakini mkubwa na kutanguliza usalama katika operesheni ya uokoaji.

“Hii ni ajali ya kusikitisha mno. Tume ya Madini inatoa pole kwa familia za wahanga, na tutaendelea kufuatilia kwa karibu kuhakikisha taratibu zote za usalama katika migodi zinasimamiwa ipasavyo ili kuepusha ajali kama hizi siku za usoni,” amesema Dkt. Lekashingo.

Aliongezea kuwa, Timu za uokoaji zinajumuisha maafisa kutoka Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Polisi, Tume ya Madini, Wizara ya Madini, wachimbaji wenzao, Mgodi wa Barrick Bulyanhulu, Serikali ya Mkoa na Wilaya ya Shinyanga, ambao wote wanaendelea kushirikiana kuhakikisha mafundi waliobaki wanatolewa salama.

Hadi sasa, juhudi za uokoaji bado zinaendelea katika eneo hilo la mgodi, huku matumaini yakiwa bado hayajapotea kwa familia na ndugu wa mafundi waliobaki chini ya kifusi. Serikali imeahidi kutoa usaidizi wa karibu kwa waathirika na kuhakikisha uchunguzi wa kina unafanyika kubaini chanzo cha ajali hiyo.



Read More

SERIKALI YA ZAMBIA YAPATA MAFUNZO KUTOKA TANZANIA: YAPONGEZA UJENZI WA MJI WA SERIKALI DODOMA


Maofisa waandamizi kutoka Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ya Zambia wametembelea Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma, kwa lengo la kujifunza namna Tanzania ilivyofanikiwa kutekeleza mradi mkubwa wa kitaifa wa kuhamishia shughuli za serikali katika mji huo.

Wakiwa katika ziara hiyo, maofisa hao walipokelewa na Mratibu wa Ujenzi wa Mji wa Serikali, Bw. Noel Mlindwa, ambaye alieleza kuwa Tanzania imeweka historia kwa kuanzisha na kutekeleza kwa mafanikio makubwa ujenzi wa mji wa serikali, chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.

Bw. Mlindwa alifafanua kuwa mji huo umejengwa kwa kuzingatia mipango bora ya kisasa, usimamizi makini wa rasilimali na matumizi ya teknolojia, hali iliyowavutia wageni hao kutoka Zambia.

Kwa upande wao, maofisa wa Zambia waliipongeza Serikali ya Tanzania kwa hatua kubwa ilizopiga na walisisitiza kuwa Mji wa Serikali Dodoma si tu ni kielelezo cha maendeleo, bali pia ni kivutio cha kiutalii na mfano wa kuigwa kwa mataifa mengine barani Afrika.



Read More

Saturday, August 16, 2025

UZINDUZI WA MFUMO WA ANUANI ZA MAKAZI ZANZIBAR WAFANA


Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Mhe. Ummy Nderiananga, ameshiriki katika hafla ya uzinduzi wa mfumo wa anuani za makazi, unaolenga kutoa huduma ya barua ya utambulisho wa mkazi kwa njia ya kidijitali.

Uzinduzi huo umefanyika leo katika Mkoa wa Mjini Magharibi, Zanzibar, ukiongozwa na Mgeni Rasmi, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Ummy amepongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, kwa jitihada zao za kuimarisha huduma za kijamii kupitia mifumo ya kidijitali.

"Niwapongeze kwa kuendelea kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi kwa urahisi zaidi kupitia teknolojia. Mfumo huu utarahisisha utambuzi wa makazi na uboreshaji wa utoaji wa huduma mbalimbali serikalini," alisema Mhe. Ummy.

Aidha, amezipongeza wizara zote za kisekta kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa ushirikiano wao uliowezesha utekelezaji wa mfumo huo muhimu kwa maendeleo ya Taifa.



Read More