Saturday, February 17, 2018

MAJALIWA AWEKA JIWE LA MSINGI LA KIWANDA CHA MIFUKO NA STEEL WIRE MAGU

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa  kiwanda cha Lakairo Industries, Daniel Lameck wakati alipotembelea na kukagua  uzalishashaji wa mifuko  na steel wire kiwandani hapo,  eneo la Isangijo wilayani Magu Februari 17, 2018. Wapili kulia ni Mkuu wa mkoa wa Mwanza, John Mongella.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiweka jiwe la msingi la kiwanda cha Lakairo Industries kwenye eneo la Isangijo wilayani Magu Februari 17, 2018.  Wapili kulia ni Mwenyekiti  wa makampuni ya Lakairo na Mbunge wa Rorya, Mhe. Lameck Airo, wanne kulia  ni Mkurugenzi Mtendaji, Daniel Lameck. Wapili kushoto ni Mkuu wa mkoa wa Mwanza, John Miongella .
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa kiwanda cha  Lakairo Industries, Daniel Lameck wakati alipotembelea na kukagua   uzalishaji wa mifuko  na steel wire  katika kiwanda hicho, eneo la Isangijo wilayani Magu Februari 17, 2018. Kulia ni Mkuu wa wilaya ya Magu,  Khadija Nyembo.

 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa kiwanda cha Lakairo Industries, Daniel Lameck  wakati alipotembelea na  kukagua uzalishaji wa mifuko  na steel wire  kwenye kiwanda  hicho, eneo la Isangijo wilayani Magu Februari 17, 2018.

 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa kiwanda cha Lakairo Industries, Daniel Lameck  wakati alipotembelea na  kukagua uzalishaji wa mifuko  na steel wire  kwenye kiwanda  hicho, eneo la Isangijo wilayani Magu Februari 17, 2018.

 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipiga kakofi baada ya kuweka jiwe la msingi la kiwanda cha  Lakairo Industries kwenye eneo la Isangijo wilayani Magu Februari 17, 2018.  Wapili kulia ni Mwenyekiti  wa makampuni ya Lakairo na Mbunge wa Rorya, Mhe. Lameck Airo, wanne kuila ni Mkurugenzi Mtendaji wa kiwanda hicho , Daniel Lameck. Wapili kushoto ni Mkuu wa mkoa wa Mwanza, John Miongella .

Read More

WAZIRI MKUU AWEKA JIWE LA MSINGI VIWANDA VYA LAKAIRO

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ametembelea na kuweka jiwe la viwanda vya Makampuni ya Lakairo Investment vyenye thamani ya sh. bilioni 25, ambavyo vipo katika kijiji cha Isangijo kata ya Kisesa wilayani Magu.

Ameweka jiwe la msingi la viwanda hivyo leo (Jumamosi, Februari 17, 2018) akiwa katika siku ya tatu ya ziara yake ya kikazi mkoani Mwanza. Viwanda hivyo  vinatengeneza steel wire, pipi, vifungashio aina ya viroba

“Nampongeza Bw. Lameck Airo mbunge wa Rorya na Mwenyekiti wa Makampuni ya Lakairo Investment kwa kuunga mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Tano za kukuza uchumi kupitia sekta viwanda.”

Waziri Mkuu amesema Serikali ya Awamu ya Tano inatekeleza sera ya uchumi wa viwanda na inahamasisha wawekezaji wa ndani na nje kuwekeza katika viwanda mbalimbali.

Amesema Serikali itamuunga Bw. Airo mkono ili viwanda hivyo viweze kuzalisha kwa mafanikio makubwa. Pia aliwataka wananchi nao wamuunge mkono muwekezaji huyo kwa sababu viwanda hivyo vinazalisha bidhaa muhimu na kutoa ajira kwa wananchi wengi.

Pia amewaagiza viongozi wa mkoa na halmashauri wahakikishe wanatoa kipaumbe kwa wawekezaji kwa kuwasogezea miundombinu ya huduma mbalimbali zikiwemo za maji na umeme ili waweze kutekeleza majukumu yao vizuri.

Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa Makampuni ya Lakairo Investment, Bw. Daniel Lameck alisema mbali na ujenzi wa viwanda hivyo vinavyotarajiwa kutoa ajira 200 hadi 300, pia wanatarajia kujenga viwanda vingine vya kutengeneza mafuta ya kupaka, dawa za viatu na kusaga nafaka.

Bw. Lameck alisema mbali na mafanikio wanayoyapata pia wanakabiliwa na tatizo la upatikanaji wa fedha kwa ajiali ya uwekezaji, ambapo alitolea mfano  mpango wao wa kutaka kujenga viwanda vingine viwili ambao umekwama kutokana na upatikanaji wa fedha.

 Mkurugenzi huyo alitumia fursa hiyo kuishauri Serikali iweke mfumo rafiki kwa ajili ya kuwawezesha wawekezaji wa ndani ili viwanda wanavyovianzisha viwe endelevu na vipanuke zaidi.
Read More

Friday, February 16, 2018

MAJALIWA AKAGUA MASHAMBA BORA YA PAMBA KATIKA VIJIJI VYA KILYABOYA NA SOLWE WILAYANI KWIMBA

  Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Pamba, Marco Mtunga (watatu kulia) kuhusu zao la pamba lililostawi vizuri wakati alipotembelea shamba darasa  katika kijiji cha Kilyaboya wilayani Kwimba Februari 16, 2018. Wanne kulia ni Mkuu wa mkoa wa Mwanza, John Mongella na kushoto ni Afisa Kilimo wa wilaya ya Kwimba, Magreth Kavalo.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikagua shamba la pamba la Bw. Dotto Masomi  (kushoto) katika kijiji cha Solwe wilayani Kwimba Februari 16, 2018, Kushoto kwake ni Mkuu wa wilaya ya Kwimba Mtemi Simon Msafiri.


Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikagua shamba la pamba la Bw. Dotto Masomi  (kushoto) katika kijiji cha Solwe wilayani Kwimba Februari 16, 2018, Kushoto kwake ni Mkuu wa wilaya ya Kwimba Mtemi Simon Msafiri.

 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimpongeza, Dotto  Masomi baada ya kutembelea shamba la pamba la mkulima huyo katika kijiji cha Solwe wilayani Kwimba na kufurahishwa na ubora wa shamba hilo Februari 16, 2018.

Read More

WANANCHI WAMKATAA MKUU WA WILAYA MBELE YA WAZIRI MKUU

WANANCHI wa wilaya ya Kwimba wamemuomba Waziri Mkuu Kassim Majaliwa aondoke na mkuu wa wilaya hiyo Bw. Mtemi Msafiri baada ya kutoridhishwa na utendaji wake.

Wametoa ombi hilo leo (Ijumaa, Februari 16, 2018) walipozuia msafara wa Waziri Mkuu alipowasili katika Ofisi za Halmashauri ya wilaya Kwimba zilizopo Ngudu kwa ajili ya kuzungumza na watumishi akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani Mwanza.

Wananchi hao walimkataa mkuu wao wa wilaya Bw. Msafiri kupitia ujumbe wa mabango 17, ambapo Waziri Mkuu amewataka wananchi hao wawe watulivu wakati Serikali inafanyia kazi malalamiko yao.

Wananchi hao wanadai kwamba Mkuu huyo wa Wilaya anatabia ya kuamrisha polisi wawakamate kwa kisingizio cha uzururaji na kisha wanawekwa mahabusu, ambapo baada ya muda wanatolewa na kwenda kulima kwenye shamba lake.

Waziri Mkuu amesema Serikali inahitaji kila mtumishi atambue majukumu yake na ayatekeleze. “Hakuna atakayeonewa, haki zenu zote tunazitekeleza nanyi mnatakiwa kutenda haki kwa kuwatumikia wananchi.”

Hata hivyo, Waziri Mkuu amewataka Mkuu huyo wa wilaya Bw. Msafiri, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Kwimba Bibi Pendo Malebeja na wakuu wote wa Idara wajitathmini kama kweli wanatekeleza majukumu yao ipasavyo na kuwatumikia wananchi.

“Mkurugenzi katika kipindi chako chote cha utendaji kuanzia mwaka 2013 hadi leo, fedha nyingi za Serikali zilizoletwa Kwimba zimepotea na hazijulikani zilipo huku miradi mingi bado haijakamilika na muda wote huo Halmashauri imekuwa inapata hati chafu.”


Pia Waziri Mkuu amewataka watumishi wote wa Halmashauri ya wilaya ya Kwimba wabadilishe mienendo yao na wawatumikie vizuri wananchi pamoja na kuishi nao vizuri.
Read More

ZIARA YA MAJALIWA WILAYANI KWIMBA

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akitoka ndani ya pantoni ya MV Kigongo baada ya kuvuka ziwa Victoria akitoka  Sengerema kwenda Kwimba Februari 16, 2018. Watatu kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongell.

 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimtwika ndoo ya maji, Esther Balele baada ya kuweka jiwe la msingi la mradi wa maji wa kijiji cha Igumambogo  wilayani Kwimba Februari 16, 2018.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimtwika ndoo ya maji , Scolastica Odiria baada ya kuweka jiwe la msingi la mradi wa maji wa kijiji cha Igumambogo wilayani Kwimba Februari 16, 2018.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikagua shamba la pamba katika kijiji cha Igumambogo wilayani Kwimba akiwa katika ziara ya mkoa wa Mwanza Februari 16, 2018.  Kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella.

 Baadhi ya watumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Kwimba wakimsikiliza Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wakati alipozungumza nao kwenye ukumbi wa Halmashauri hiyo katika mji mdogo wa Ngudu Februari 16, 2018. 

 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba kwenye ukumbi wa Halmashauri hiyo  katika mji mdogo wa Ngudu, Februari 16, 2018. Kulia ni Mwenyekiti wa CCM wa mkoa wa Mwanza, Dkt. Anthony Diallo.

Read More

WAZIRI MKUU AAGIZA KUKAMATWA KWA MKANDARASI WA KAMPUNI YA PALIMON

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemuagiza Kamanda wa TAKUKURU mkoa wa Mwanza Mhandisi Ernest Makale kumkamata mkandarasi wa kampuni ya Palimon baada ya kushindwa kukamilisha mradi wa mradi wa maji wenye thamani ya sh. bilioni 2.06 wilayani Kwimba.

Ametoa agizo leo (Ijumaa, Februari 16, 2018) wakati akizungumza na watumishi na wananchi kwenye kijiji cha Igumangobo wilayani Kwimba. Mkandarasi huyo alianza ujenzi wa mradi huo Oktoba 28, 2013 na alitakiwa kukamilisha Mei 28, 2014.

Waziri Mkuu amesema kitendo cha mkandarasi kutokamilisha mradi huo kwa wakati licha ya kupewa fedha hakivumiliki, hivyo amemtaka kamanda wa TAKUKURU kutafuta popote alipo na kumuhoji.

Waziri Mkuu alitoa agizo hilo baada ya wananchi wa vijiji vya Mhande, Shirima na Izizimba ‘B’ ambao mradi huo unatekelezwa katika vijiji vyao. Wananchi hao walimuomba Waziri Mkuu awasaidie ili mradi wao ukamilike na wao wapate huduma ya maji.

Wakati huo huo, Waziri Mkuu amelitaka Baraza la Madiwani la Halmashauri ya wilaya ya Kwimba kutotumia fedha za miradi ya maendeleo kulipana posho.

“Fedha zinazopelekwa si za kulipana posho ni za maboresho na Serikali inataka wananchi wahudumiwe wasipate shida.”

Waziri Mkuu amesema watumishi wahakikishe wanawahudumia wananchi ipasavyo, ikiwa ni pamoja na kusimamia vizuri matumizi ya fedha za maendeleo.

Amesema wilaya hiyo imegeuka kama shimo la kuteketeza fedha za Serikali kwa sababu miradi mingi inayotekelezwa haikamili, hivyo ameitaka ijipange. Alitolea mfano sh. milioni 94 za ujenzi wa mradi wa kliniki ya mifugo ambayo haijakamilika na fedha zimekwisha.


Awali, Waziri Mkuu alifungua mradi wa maji wa kijiji cha Igumangobo kilichopo katika Tarafa ya Mwamashimba wilayani Kwimba. Chanzo cha maji hayo ni ziwa Victoria.
Read More

WAZIRI MKUU AKEMEA VITENDO VINAVYOHARIBU UBORA WA PAMBA

*Awataka wasiweke mchanga wala maji ili kuongeza uzito 

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka wakulima wa pamba kutochanganya pamba na mchanga au maji kwa sababu watakosa wanunuzi.

Pia amesema Serikali itapambana na watu wote wanaotaka kuvuruga zao hilo, hivyo amewataka wakulima waendelee kuwa na imani na Serikali yao.

Waziri mkuu alitoa kauli hiyo jana (Ijumaa, Februari 16, 2018) wakati akizungumza kwa nyakati tofauti na wananchi wa wilaya ya Kwimba.
                                                   
“Wakulima msichezee pamba kwa kuichanganya na chochote ili kuiongezea uzito kwa sababu mtaharibu sifa nzuri ya pamba ya Tanzania ndani nan je ya nchi.”

Alisema kumekuwa na tabia ya baadhi ya wakulima wasiokuwa waaminifu ambao kabla ya kuipeleka pamba sokoni wanachanganya na maji au mchanga.

Waziri Mkuu alisema Serikali imeanza kuona tija tangu ilipoagiza Maofisa Kilimo katika mikoa inayolima pamba wasimamie kilimo hicho kuanzia ngazi za awali.

Akizungumzia kuhusu suala la wanunuzi wa pamba, Waziri Mkuu alisema tayari Serikali imeweka mikakati ya kutosha itakayowezesha pamba yote kununuliwa.

Kuhusu suala la bei alisema wataangalia katika soko la Dunia na kisha watawashawishi wanunuzi wanunue kwa bei nzuri itakayowanufaisha wakulima.

Alisema Serikali itaendelea kusimamia zao hilo kuanzia hatua za maandalizi ya shamba kwa kulima kitaalam, upatikanaji wa pembejeo hadi masoko.

Awali, Waziri Mkuu alitembelea mashamba ya mfano ya pamba katika kijiji cha Kilyaboya na Igumangobo ambapo alisema ameridhishwa mashamba hayo.

Pia aliweka jiwe la msingi la ujenzi wa zahanati ya kijiji cha Kadashi, mradi ambao ulioibuliwa na Diwani wa Kata ya Maligisu, Bw. Tabu Mapembe.

Kata ya Maligisu yenye vijiji vine ina zahanati moja tu, kukamilika kwa ujenzi wa zahanati hiyo kutasaidia kupunguza tatizo la utoaji wa huduma za afya.


Read More

IDARA YA URATIBU WA SHUGHULI ZA SERIKALI YAENDESHA KIKAO CHA TATHIMINI NA UFUATILIAJI JUU YA UKATILI DHIDI YA WANAWAKE NA WATOTO.

Mwenyekiti wa kikao cha Kujadili Rasimu ya Mpango wa Tathimini na Ufuatiliaji wa Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto kwa miaka mitano  2017/18-2021/22 Bw.Joseph Kiraia akichangia hoja wakati wa kikao hicho kilichoratibiwa na Idara ya Uratibu wa Shughuli za Serikali Ofisi ya Waziri Mkuu Februari 16, 2018. 

Mshauri Mwelekezi wa Mambo ya Tathimini na Ufuatiliaji Bw.Luhuvilo Sanga aliwasilisha mada wakati wa kujadili Rasimu ya Mpango wa Tathimini na Ufuatiliaji wa Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto kwa miaka mitano   katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu Dodoma.

Mtendaji Mkuu wa Mtandao wa Malezi, Makuzi, Maendeleo ya Watoto Wadogo Tanzania Bw.Bruno Ghumpi akiuliza swali wakati wa kikao cha kujadili Rasimu ya Mpango wa Tathimini na Ufuatiliaji wa Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto kilichoandaliwa na Idara ya Uratibu wa Shughuli za Serikali Ofisi ya Waziri Mkuu Februari 16, 2018

Mchambuzi wa Masuala ya Sera Bw. Ezekiel Swema akitoa maelezo kwa baadhi ya wanakikundi cha Kujadili Rasimu ya Mpango wa Tathimini na Ufuatiliaji wa Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto wakati wa kikao hicho.

Mtendaji Mkuu wa Mtandao wa Malezi, Makuzi, Maendeleo ya Watoto Wadogo Tanzania Bw.Bruno Ghumpi akichangia hoja wakati wa kazi za vikundi ili kujadili Rasimu ya Mpango wa Tathimini na Ufuatiliaji wa Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto.

Afisa Kazi Mwandamizi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu) Bi. Pendo Berege akichangia hoja wakati wa kikao cha kujadili Rasimu ya Mpango wa Tathimini na Ufuatiliaji wa Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto kilichofanyika Ukumbi wa mikutano Ofisi ya Waziri Mkuu Dodoma.

Read More

Thursday, February 15, 2018

WATENDAJI TENGENI MUDA WA KUWAHUDUMIA WANANCHI-MAJALIWA



 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwapungia wananchi wa Buchosa wakati alipoingia kwenye uwanja wa michezo wa Nyehunge wilayani Sengerema kuhutubia mkutano wa hadhara Februari 15, 2018.

 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwapungia wananchi wa Buchosa wakati alipoingia kwenye uwanja wa michezo wa Nyehunge wilayani Sengerema kuhutubia mkutano wa hadhara Februari 15, 2018.

 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  akipata maelezo kutoka kwa mmiliki wa kiwanda kidogo  cha Dotto Posho Mill, Bw.  Alexander Dotto  (kushoto) kuhusu  unga na Mchele unaozalishwa na kiwanda hicho kilichopo eneo la Bukara, Sengerema Februari 15, 2018. Kulia ni Mkuu wa mkoa wa Mwanza, John Miongella.



Na mwandishi wetu
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka watendaji na wakuu wa idara mbalimbali kuhakikisha wanatenga muda na kwenda vijijini kuwahudumia wananchi.

Amesema wananchi hususani waishio maeneo ya vijijini wanachangamoto mbalimbali ambazo zinatakiwa kupatiwa ufumbuzi na watendaji hao.

Aliyasema hayo jana (Alhamisi, Februari 15, 2018) alipozungumza kwa nyakati tofauti na watumishi na wananchi katika kata ya Nyehunge na Ibisabageni wilayani Sengerema akiwa katika ziara ya mkoa wa Mwanza.

Alisema Serikali imedhamiria kwa dhati kuwatumikia kwa lengo la kuwaondolea kero mbalimbali zinazowakabili, hivyo hakuna sababu ya watendaji kukaa maofisini.

“Watumishi wanawajibu wa kuwafuata wananchi katika maeneo yao hasa vijijini kwa sababu si kila mwananchi anauwezo wa kufuata huduma katika ofisi zenu na atakayeshindwa kufanya hivyo hatutomvumilia.”

Waziri Mkuu aliongeza kuwa Serikali inawawezesha watumishi wake kwa kuwapatia vitendea kazi kama usafiri ili waweze kuwahudumia wananchi ipasavyo.

Alisema kwa sababu ya kutotekeleza wajibu wao ipasavyo kumekuwa na kero na malalamiko mengi kutoka kwa wananchi na hivyo kusababisha wananchi kuwasilisha kero na malalamiko hayo wakati wa ziara za viongozi wakuu.

Katika hatua nyingine Waziri Mkuu aliwataka wananchi wanaofanya kazi katika kiwanda cha kuongeza thamani ya mazao ya nafaka cha Doto Alex Posho Meel kuwa waaminifu.


Waziri Mkuu alisema wafanyakazi hao wanatakiwa wawe waaminifu na wafanye kazi kwa bidii ili kukiwezesha kiwanda hicho kuendelea na uzalishaji.
Read More

MADIWANI WA BUCHOSA WAMKATAA MKURUGENZI WAO MBELE YA WAZIRI MKUU


MADIWANI wa Halmashauri ya Buchosa wilayani Sengerema wamemuomba Waziri Mkuu Kassim Majaliwa aondoke na Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Bw. Cyprian Luanda baada ya kutoridhishwa na utendaji wake.

Wametoa ombi hilo leo (Alhamisi, Februari 15, 2018) katika kikao cha Waziri Mkuu na watumishi Halmashauri ya Buchosa akiwa katika siku ya kwanza ya ziara yake ya kikazi mkoani Mwanza.

Waziri Mkuu baada ya kupokea ombi hilo alimuagiza Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Bw. John Mongella kwenda katika halmashauri hiyo na kufanya kikao cha pamoja kati ya Madiwani, Mkurugenzi na watumishi ili kubaini changamoto zilizopo na kuzitafutia ufumbuzi.

Awali, Waziri Mkuu  aliweka jiwe la msingi la hospitali ya Halmashauri ya Buchosa wilayani Sengerema, ambapo ujenzi wake hadi kukamilika unatarajiwa kugharimu sh. bilioni 10.55.

Pia Waziri Mkuu amezindua madarasa manne ya Kidato cha Tano na Sita katika Shule ya Secondari ya Nyehunge wilayani Sengerema na kuwata wanafunzi wasome kwa bidii.

Waziri Mkuu amesema wanafunzi hao wanatakiwa wasome sana kwa sababu Rais Dkt. John Magufuli amewaondolea wazazi michango  ya hovyo ili wao wapate fursa ya kusoma.

Pia amewasisitiza walimu wasijiingize katika masuala ya michango ili wajikite na masuala ya taaluma. Kama kuna michango kutoka mtu mmoja mmoja, vikundi au Taasisi yote sasa itafikishwa kwa Mkurugenzi wa Halmashauri.

Amesema awali wanafunzi walikuwa wanatumika kama njia ya kutengeneza fedha, ambapo wazazi au walezi wanaposhindwa kutoa michango hiyo watoto wao walikuwa wanarudishwa nyumbani. Waziri Mkuu amesema kila mwezi Serikali inapeleka moja kwa moja shuleni sh. bilioni 20.8 kwa ajili ya kugharamia Elimumsingi bila malipo.


Read More

MAJALIWA AWEKA JIWE LA MSINGI LA HOSPITALI YA HALMASHAURI YA BUCHOSA


 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiweka jiwe la msingi la Hospitali ya Halmashauri ya Buchosa wilayani Sengerema akiwa katika siku ya kwanza ya ziara ya mkoa wa Mwanza Februari 15, 2018 .Kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella na kulia ni Mbunge wa Buchosa na Waziri wa Kilimo, Dkt. Charles Tizeba.
Read More

Tuesday, February 13, 2018

WAZIRI MKUU AZINDUA MPANGO MKAKATI WA AFYA MOJA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Mpango Mkakati wa Afya Moja na Dawati la Kuratibu Afya Moja nchini ni muhimu katika kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa mahala safi na salama kwa kuishi na kufanya kazi za kimaendeleo.

Ametoa kauli hiyo leo (Jumanne, Februari 13, 2018) wakati akizindua mpango mkakati huo katika ukumbi wa Karimjee jijini Dar es Salaam, ambapo amesema dhana ya Afya Moja inafaa kutumika zaidi katika nchi zinazoendelea.

Waziri Mkuu amesema mbali na mpango kufaa kutumika katika nchi zinazoendelea pia hata kwa nchi zinazokaribia maeneo ya wanyama pori kama Tanzania kutokana na kukabiliwa na changamoto ya upungufu wa rasilimali.


Amesema kwa upande wa nchi za Afrika hali ni hatarishi zaidi kwa kuwa Bara hilo, lina sehemu nyingi zinazokaribia mapori makubwa ya wanyama kama Bonde la Mto Kongo, ambalo mazingira yake yamekuwa ni kitovu cha magonjwa ya mlipuko kama vile Ebola, Homa ya Bonde la Ufa (RVF), Marburg na mengineyo.

Waziri Mkuu amesema kwa kutambua hilo, Serikali kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Marekani (USAID) na wadau wengine wa Maendeleo, imeendelea kutekeleza agenda ya Afya Moja nchini tangu mwaka 2013 ilipozinduliwa kwa mara ya kwanza mjini Arusha na  Makamu wa Rais Mstaafu, Dkt. Mohamed Gharib Bilal.

“Utekelezaji wa Mpango huu unakwenda sambamba na maelekezo ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (2015-2020) ya kujenga Taifa lenye watu wenye afya bora itakayowawezesha kuzalisha mali na kutoa huduma mbalimbali ambayo ni muhimu sana katika kufikia azma ya Serikali ya kujenga Uchumi wa Viwanda.”

Awali, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge,Kazi,Vijana,Ajira na Wenye Ulemavu, Bibi Jenista Mhagama alisema uzinduzi wa mkakati huo ni ngao tosha kwa nchi katika kuzuia na kudhibiti magonjwa.

Alisema pamoja na kutekeleza kanuni za Kitaifa, Kikanda na Kimataifa ambazo zinahitaji ushirikiano  wa sekta mbalilmbali kwa kutumia dhana ya afya moja, mpango mkakati huo unaleta msukumo katika Ofisi ya Waziri Mkuu  kuendelea kushirikiana na Taasisi mbalimbali kudhibiti magonjwa.

Bibi Jenista alisema uratibu wa afya moja unakwenda sambamba na matakwa ya Shirika la Afya Duniani (WHO), Shirika linaloshughulika na Afya ya Wanyama (IOE) na Shirika la Kimataifa la Chakula la Kilimo (FAO) ambayo yanashirikiana katika kudhibiti magonjwa yanayoambukiza na usugu wa dawa.
Read More

BAHARI KUU, VIWANJA VYA NDEGE VYABAINIKA KUPITISHA DAWA ZA KULEVYA-MAJALIWA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali imebaini kwamba maeneo ya bahari kuu, bandari, vituo vya mabasi na viwanja vya ndege yanayotumika sana katika kupitisha dawa za kulevya.

Hata hivyo Waziri Mkuu amesema wafanyabiashara, wasambazaji na watumiaji wa dawa za kulevya wameendelea kukamatwa, lengo ni kuhakikisha biashara hiyo inamalizika nchini.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Jumanne, Februari 13, 2018) wakati akikabidhi gari kwa Kamishna Generali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Bw. Rogers Siyanga  kwenye viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam.

Amesema mbali na kukamata meli, pia Serikali imewakamata wasambazaji pamoja na kundi kubwa la wafanyabiashara wanaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya sambamba na watumiaji, lengo ni kuhakikisha Tanzania inakuwa salama na kizazi chenye uwezo wa kuzalisha mali.  

Waziri Mkuu amesema Serikali imepiga hatua kubwa katika vita dhidi ya dawa za kulenya, ambapo hivi karibuni imekamata meli nyingi, moja ilikiwa inatokea pwani ya Msumbiji na ilikamatiwa maeneo ya Mtwara ikiwa na dawa nyingi za kulevya.

“Niwakati wa Serikali kuendelea kuiwezesha Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya na leo hii tunawakabidhi gari hili jipya kabisa ili iweze kuendelea na utekelezaji wa majukumu yake ipasavyo.”

Pia Waziri Mkuu amewataka Watanzania waachane na biashara ya dawa za kulevya ikiwa ni pamoja na  kazi ya kusambaza, kuzalisha na kutumia na watakaokamatwa wakijihusisha nayo watachukuliwa hatua kali za kisheria.

Amesema kwa sasa Serikali inajenga maabara ambayo itatumiwa na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa dawa wanazozikamata.

Waziri Mkuu amesema wananchi wanatakiwa kushirikiana na Serikali katika vita dhidi ya dawa za kulevya kwa kutoa taarifa mara wanapowabaini wafanyabiashara, watumiaji na wasambazaji wa dawa hizo. Pia wahakikishe wanawalinda vijana ili wasijihusishe na dawa za kulevya.

Kwa upande wake Siyanga aliishukuru Serikali kwa kuipatia mamlaka hiyo gari, ambapo alitumia fursa hiyo kuwataka wananchi waachane na biashara ya dawa za kulevya. Alisema wanapambana kuhakikisha dawa za kulevya ili zisiingie nchini.

Alisema mbali na kudhibiti biashara hiyo, pia wanatoa elimu juu ya madhara ya matumizi ya dawa za kulevya vikiwemo vitendo viovu vinavyofanywa na watumiaji ili wachukie na waache kutumia dawa hizo.

Pia wanafanya kazi ya kuwahudumia watu walioathirika na matumizi ya dawa za kulevya, hivyo aliwaomba wananchi kutowanyanyapaa waathirika na badala yake wawapeleke katika vituo maalumu vya kutolea huduma za methadone.

Read More

WAZIRI MKUU AKABIDHI GARI KWA MAMLAKA YA KUPAMBAMBANA NA DAWA ZA KULEVYA

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa( Aliye vaa miwani)leo (Jumanne, Februari 13, 2018) amekabidhi gari kwa Kamishna Generali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Bw. Rogers Siyanga kwa ajili ya Mamlaka hiyo. Makabidhiao hayo yamefanyika katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam.

Read More

Friday, February 9, 2018

WAZIRI MKUU KUZINDUA MPANGO MKAKATI WA AFYA MOJA NA DAWATI LA URATIBU AFYA MOJA NCHINI

"Afya moja ni dhana inayojumuisha sekta ya binadamu,wanyama pori na wafugwao na mazingira katika kujiandaa,kufuatilia na kukabili magonjwa yanayoathiri sekta hizo "

Read More

SERIKALI YAFANIKIWA KUREJESHA MALI ZA NCU, SHIRECU

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali imefanikiwa kurejesha mali tisa kati ya 10 za Chama Kikuu cha Ushirika cha Nyanza (NCU) ambazo zilichukuliwa kinyume cha taratibu na kuagiza watuhumiwa wachukuliwe hatua za kisheria.

Amesema mali moja iliyobakia bado inafanyiwa uchunguzi na mali mbili za Chama Kikuu cha Ushirika cha Shinyanga (SHIRECU) nazo pia zimepatikana lakini bado ziko kwenye hatua ya makabidhiano.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Ijumaa, Februari 9, 2018) bungeni mjini Dodoma wakati akitoa hoja ya kuahirisha mkutano wa 10 wa Bunge la 11. Bunge limeahirishwa hadi Aprili 3, mwaka huu.

Waziri Mkuu amezitaja mali za Chama Kikuu cha Ushirika cha Nyanza (NCU) zilizorejeshwa kuwa jengo la Nyanza Cooperative Union (1984) Ltd. maarufu kwa jina la “Transport House” au KAUMA House, lililopo katika kiwanja namba 242, Kitalu T, Mtaa wa Stesheni; kiwanda cha kusindika mafuta cha New Era Oil Mill, kilichopo katika eneo la Igogo; na jengo na viwanja vya Ashock Industries vilivyopo eneo la viwanda Igogo.

Nyingine ni majengo ya kilichokuwa kiwanda cha mkonge na dengu kilichopo eneo la Igogo kwenye kiwanja namba 41 na 79; jengo lililopo katika kiwanja kilichopo Isamilo namba 80, kitalu “D”; jengo lililopo katika kiwanja kilichopo Isamilo namba 110, kitalu “D” na ghala moja katika kiwanja namba 104, kitalu “A” kilichopo eneo la Igogo.

“Mali nyingine zilizorejeshwa ni jengo moja lililopo mjini Geita katika kiwanja namba 8 Kitalu “K”; jengo moja lililopo mjini Geita, katika kiwanja namba 24, Kitalu “K” na jengo lililopo Isamilo katika kiwanja namba 89 Kitalu “D”,” amesema Waziri Mkuu.

Kwa upande wa mali za SHIRECU, Waziri Mkuu amezitaja mali zilizopo kwenye hatua ya makabidhiano kuwa ni ghala lililopo Kurasini, Dar es Salaam na nyumba ya ghorofa tatu iliyopo kiwanja namba 1001 “BB” Ilala, jijini Dar es Salaam.

“Katika kusimamia misingi ya utawala bora na uwajibikaji wa watendaji wa vyama vya ushirika, Serikali inaendelea kufanya uchunguzi maalum kuhusu mikataba mibovu ya Chama Kikuu cha Ushirika cha Nyanza (NCU), Chama Kikuu cha Ushirika cha Shinyanga (SHIRECU), Chama Kikuu cha Ushirika cha Kagera (KCU) na Chama Kikuu cha Ushirika cha Kilimanjaro (KNCU). Vilevile, tunachunguza kushikiliwa kwa mali za ushirika bila kufuata utaratibu,” amesema.

Amesema Serikali itaendelea kuviamsha vyama vya ushirika vya msingi na vyama vikuu vilivyosinzia katika mikoa yote ili kujenga ushirika imara na kwamba juhudi na hatua hizo zinazochukuliwa na Serikali, zinalenga kuongeza imani, hamasa na uzalishaji wa mazao na kusimamia masoko yake, na hivyo, kuinua kipato cha wakulima sambamba na kuwapatia fursa ya kujiajiri wenyewe katika sekta ya kilimo.
Read More

VIWANJA ZAIDI YA 15,000 VIMEPIMWA DODOMA- MAJALIWA

*Kuanza kuuzwa Machi 30, mwaka huu

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Manispaa ya Dodoma imekamilisha upimaji wa viwanja vipya zaidi ya 15,000 na vitaanza kugawiwa Machi, 30 mwaka huu.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Ijumaa, Februari 9, 2018) bungeni mjini Dodoma wakati akitoa hoja ya kuahirisha mkutano wa 10 wa Bunge la 11. Bunge limeahirishwa hadi Aprili 3, mwaka huu.

“Kutokana na agizo la Serikali la kuhamishia makao makuu ya nchi Dodoma, mahitaji ya viwanja hadi Februari 2018 yalikuwa ni viwanja 24,602.Manispaa ya Dodoma hivi sasa inatekeleza mkakati wake wa kuzalisha viwanja 30,000 kwa kushirikiana na wadau mbalimbali. Tayari upimaji wa viwanja vipya 15,316 umekamilika na vitaanza kugawiwa kuanzia tarehe 30 Machi 2018,” amesema Waziri Mkuu.

Amelieleza Bunge kwamba kiasi kilichobaki cha viwanja 14,684 kitakamilika ifikapo Juni, 2018 na wananchi watauziwa viwanja hivyo kwa bei elekezi itakayotolewa na Manispaa hiyo.

Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwasihi wananchi na watumishi wa umma watakaohitaji viwanja kufuata taratibu za maombi ya viwanja pindi vitakapotangazwa rasmi na kusisitiza kuwa zoezi la kubadilisha hati zilizotolewa na iliyokuwa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Dodoma (CDA) na kupata hatimiliki za miaka 99 linaendelea. “Wenye hati za CDA mnasisitizwa kuendelea na taratibu za kuzibadilisha,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema jumla ya watumishi 3,829 kutoka wizara na taasisi mbalimbali za Serikali tayari wamehamia Dodoma akiwemo Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan.

“Napenda kulifahamisha Bunge lako tukufu kuwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na ofisi yake walihamia rasmi Dodoma tarehe 15 Desemba, 2017 kama ilivyopangwa,” amesema.

Kuhusu mpango wa kuifanya Dodoma kuwa ya kijani, Waziri Mkuu amesema Serikali imedhamiria kuifanya Dodoma iwe na ukanda wa kijani (Green Belt) kupitia mpango wa kuendeleza, kutunza na kuhifadhi maeneo ya msitu wa Mahomanyika wenye ukubwa wa hekta 2,000; msitu wa Chimwaga Nzuguni (hekta 300) na msitu wa Mbwenzelo (hekta 3,500) pamoja na vilima vya Image na Nyankali.

“Katika kutimiza malengo hayo ya kuifanya Dodoma kuwa ya kijani, Serikali imeendelea kutoa elimu ya upandaji miti na uhifadhi wa misitu hususan miti adimu ya asili na makao ya wanyamapori mbalimbali katika kata nane za Ipala, Nzuguni, Kikombo, Ng’ong’ona, Chahwa, Zuzu, Hombolo na Kikuyu Kaskazini ambapo kila kata imepewa lengo la kupanda miti isiyopungua 40,000,” amesema.

Kuhusu zoezi la upandaji miti, Waziri Mkuu amesema miche 34,000 yenye thamani ya sh. milioni 34 ilitolewa bure katika kata mbalimbali na kupitia mradi wa TASAF miche mingine 138,000 inaendelea kusambazwa kwa wananchi. “Kwa sasa, Manispaa ya Dodoma inaendelea na maandalizi ya kuotesha miche mingine 200,000 kwa ajili ya msimu ujao,” ameongeza.

Ametumia fursa hiyo kuwashukuru Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Bonde la Wami Ruvu, Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) ambao kwa kushirikiana na Manispaa ya Dodoma wamefanikisha upandaji wa miche 79,000 katika maeneo ya UDOM, Mzakwe, Iseni Park, Nala na Mahomanyika.

Katika kuhakikisha zoezi la upandaji miti linakuwa endelevu, Waziri Mkuu ameziagiza Halmashauri zote nchini zihakikishe zinaandaa miche ya kutosha na kuweka utaratibu wa kila kaya kupanda na kutunza miti isiyopungua mitano.

“Taarifa za utendaji na maendeleo za Halmashauri zote zioneshe mafanikio yaliyopatikana kutokana na zoezi la upandaji miti. Utendaji wa Wakurugenzi na Wakuu wote wa Mikoa na Wilaya, utapimwa kutokana na uendelezaji na utunzaji wa mazingira katika maeneo yao,” amesisitiza.
Read More