Wednesday, June 18, 2025

SERIKALI YAWEKA MIKAKATI YA KUIMARISHA SEKTA YA KILIMO KUPITIA ASDP II

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Uratibu wa Shughuli za Serikali kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge na Uratibu, Bw. Omary Ilyas, ameongoza kikao maalum cha Wakurugenzi wa Wizara na Taasisi zinazotekeleza Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo awamu ya pili (ASDP II).

Kikao hicho kilichofanyika jijini Dodoma kimejadili utekelezaji wa programu hiyo kwa kipindi cha Julai 2024 hadi Machi 2025, sambamba na kuanza maandalizi ya mpango wa mwaka ujao wa 2025/2026.

Bw. Ilyas amesema ASDP II inalenga kuimarisha usalama wa chakula, kuongeza tija kwa wakulima na kusaidia ukuaji wa uchumi wa vijijini kupitia ushirikiano wa kisekta.

Kikao kimehusisha wadau kutoka sekta ya kilimo, mifugo, uvuvi, pamoja na taasisi za fedha na maendeleo, ili kuhakikisha utekelezaji wa pamoja unaolenga mafanikio ya mkakati wa Taifa wa kilimo.

Read More

Tuesday, June 17, 2025

DKT. YONAZI AMEONGOZA KIKAO CHA KAMATI YA TAIFA YA USHAURI YA SENSA YA WATU NA MAKAZI YA MWAKA 2022


 Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi (mwenyekiti wa kikao) cha Kamati ya Taifa ya Ushauri ya Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 kilichofanyika tarehe 17 Juni, 2025 katika ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere JIjini Dar es Salaam.

 Kikao hicho kimeudhuriwa na Matibu Wakuu wa Wizara za Kisekta, Makamisaa wa Sensa pamoja na baadhi ya wakuu wa Taasisi.Lengo la kikao hicho ni kupokea na kujadili ripoti mbalimbali za utekelezaji wa Awamu ya Tatu na ya Mwisho ya Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022.

 Aidha miongoni mwa ripoti hizo ni pamoja na ile ya Utekelezaji wa Mwongozo wa Kitaifa wa Matumizi ya Matokeo ya Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 kwa kipindi cha kuanzia Desemba 2024 hadi Mei 2025, na Hali ya Utekelezaji wa Anwani za Makazi.

 Pia kikao kimejadili na kupokea Rasimu za Ripoti Tano za kina za Matokeo ya Sensa, na Ripoti ya Makadirio ya Idadi ya Watu kuanzia mwaka 2023 hadi 2050 ngazi ya Mikoa.





Read More

WAZIRI SIMBACHAWENE ATEMBELEA BANDA LA OFISI YA WAZIRI MKUU






Waziri wa Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene (Mb) leo June 17, 2025 ametembelea banda la Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu lililopo katika maonesho ya Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park Jijini Dodoma ambapo Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) ikijumuisha idara na taasisi zilizo chini yake inashiriki maonesho hayo. 






 

Read More

Saturday, June 14, 2025

SERIKALI KUIMARISHA MIKAKATI YA KUKABILIANA NA MAAFA NCHINI

 

Serikali y


a Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imepiga hatua kubwa kwa kuweka mifumo, sera na mikakati madhubuti ya kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali ya pindi baada ya maafa yanapotokea, ili kuimarisha usalama na ustawi wa wananchi.

Kauli hiyo imetolewa jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu, Dkt. Jim Yonazi, wakati wa hafla ya kufunga mafunzo ya wakufunzi kuhusu usimamizi wa hatari zitokanazo na maafa Mafunzo hayo yaliandaliwa na Jumuiya ya Nchi Zilizopo kwenye Mwambao wa Bahari ya Hindi (IORA) kwa ushirikiano na Shirika la Maendeleo la Uturuki (TİKA), Shirika la Msalaba Mwekundu la Uturuki, na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ya Tanzania.

Dkt. Yonazi amesema kuwa mafunzo hayo yamekusudia kuimarisha uwezo wa kitaifa na wa kikanda katika kudhibiti maafa na kuwalinda wananchi. Alibainisha kuwa mafunzo hayo yanaonesha umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa katika kupunguza hatari za maafa (DRR), sambamba na kujenga jamii imara na endelevu.

“Kuwajengea uwezo viongozi wa jamii ni jambo la msingi, kwani wao ndiyo wahusika wa kwanza kutoa mwitikio wakati wa majanga, kusaidia kuratibu misaada na kuhakikisha usalama na ustawi wa jamii,” amesisitiza Dkt. Yonazi.

Aidha, amewapongeza wadau wote waliowezesha mafunzo hayo kufanyika kwa mafanikio, akiwemo TİKA, Sekretarieti ya IORA, Msalaba Mwekundu wa Uturuki, pamoja na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, kwa mchango wao mkubwa na ushirikiano thabiti.

“Ni faraja kubwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa mwenyeji wa mafunzo haya muhimu kwa maendeleo ya ukanda huu. Nawatakia kila la heri na natumai mmefurahia uwepo wenu hapa Dar es Salaam na Tanzania kwa ujumla. Tunawakaribisha tena na tena,” amesema.

Kwa upande wake, Balozi wa Uturuki nchini Tanzania, Mheshimiwa Bekir Gezer, alieleza kuwa Serikali ya Uturuki itaendelea kushirikiana na Tanzania, hasa katika masuala yahusuyo maafa. Amesisitiza kuwa nchi yao iko tayari kusaidia kwa kutoa vifaa muhimu vya kukabiliana na maafa.

Naye, Bi. Filiz Sahinci, Mkurugenzi wa Shirika la Maendeleo la TİKA nchini Tanzania, amesema shirika hilo limejikita kusaidia juhudi za kukabiliana na maafa kwa kubadilishana uzoefu na kuimarisha ushirikiano katika kutatua changamoto zinazotokana na maafa.

Mafunzo hayo yamehusisha wakufunzi kutoka Mataifa Kumi na Moja zilizopo kwenye Mwambao wa Bahari ya Hindi na yameweka msingi muhimu wa kuimarisha utayari wa jamii dhidi ya majanga na magonjwa ya kuambukiza, hususan katika mazingira ya baada ya maafa.



Read More

Monday, June 9, 2025

TUME HURU YA UCHAGUZI YAPONGEZWA MAANDALIZI UCHAGUZI MKUU 2025

 




Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Dkt. Jim Yonazi ameipongeza Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi kwa kukamilisha zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na kuendelea vyema na maandalizi ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

 Dkt. Yonazi ametoa pongezi hizo leo tarehe 09 Juni, 2025 Kisiwani Unguja, Zanzibar wakati wa kufungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi la INEC, ambapo imewaasa viongozi wa Tume kuendelea kuwa imara na kufanya kazi kwa bidii na ushirikiano ili kuhakikisha kuwa uchaguzi unakwenda vizuri.

 “Kwanza niwapongeze sana kwa kukutekeleza jukumu hili kubwa ambalo mmekabidhiwa na Taifa letu na kwa namna ya pekee kabisa Mwenyekiti wa Baraza unifikishie salamu za pongezi kwa Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele pamoja na wajumbe wa Tume kwa kazi kubwa ambayo mmeifanya katika kuhakikisha kuwa shughuli za uchaguzi nchini kwetu zinakwenda vizuri,” amesema Dkt. Yonazi.

 Ameeleza kuridhishwa na jinsi Tume ilivyotekeleza kwa ufanisi zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na kuongeza kuwa ni matarajio ya Serikali kuwa utendaji huo mzuri wa Tume utaendelea kwa viwango vya juu kwa mujibu wa katiba, sheria na taratibu mbalimbali ambazo zimewekwa.

 Awali akimkaribisha mgeni rasmi, Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi ambaye pia ni Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Ndugu. Kailima Ramadhan amesema tayari Tume imekamilisha awamu ya kwanza ya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ambapo kwa sasa inaendelea na uboreshaji wa awamu ya pili.

 “Tume imeshakamilisha uboreshaji wa awamu ya kwanza na imeshachakata na kutoa daftari la awali na imeshakamilisha uboreshaji wa awamu ya pili mzunguko wa kwanza na mzunguko wa pili. Tunategemea kuanzia tarehe 28 mwezi huu (tarehe 28 Juni, 2025) tutaanza mzunguko wa tatu wa uboreshaji katika Vyuo vya Mafunzo Tanzania Zanzibar na Magereza Tanzania Bara kwa wanafunzi na wafungwa waliohukumiwa kifungo chini ya miezi sita,” amesema Kailima.

 Katibu huyo wa Baraza amesema mzunguko huo wa tatu utahusisha vituo 140 vya kuandikisha wapiga kura ambapo 130 vipo kwenye magereza Tanzania Bara na vituo 10 vipo kwenye vyuo vya mafunzo Tanzania Zanzibar. Zoezi hilo linatarajiwa kufanyika kwa siku saba hadi tarehe 04 Julai, 2025.

 Ameongeza kuwa Tume imekamilisha maandalizi ya nyaraka mbalimbli kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 ikiwa ni pamoja na Kanuni za Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani za Mwaka 2025, Kanuni za Maadili ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani za Mwaka 2025 na maelekezo mbalimbali kwa ajili ya watendaji wa uchaguzi na wadau wa uchaguzi kupata miongozo kwa ajili ya utekelezaji wa uchaguzi.

 Alimkumbusha mgeni rasmi kuwa tayari Tume imekamilisha zoezi la ugawaji wa majimbo na kwamba kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 kutakuwa na jumla ya majimbo 272 yatakayofanya uchaguzi wa wabunge katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kata 3960 kwa ajili ya uchaguzi wa madiwani kwa Tanzania Bara.

 


Read More

Friday, June 6, 2025

MAMLAKA YA HALI YA HEWA DUNIANI KUENDELEA KUUNGA MKONO JITIHADA ZA TANZANIA KUKABILIANA NA MAAFA

 


Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Duniani (World Meteorological Organization - WMO) Bi. Celeste Saulo ameahidi kushirikiana na Tanzania katika kuimarisha mfumo wa Tahadhari ya mapema (early warning systems) kwa ajili ya kuchukua hatua za haraka kuzuia na kukabiliana na maafa pindi yanapotokea.

Ameyasema hayo wakati wa kikao cha pembezoni mwa Jukwaa la Nane la Dunia la Kupunguza Madhara ya Maafa na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, na Uratibu, Dkt. Jim Yonazi pamoja na ujumbe alioongozana nao kwa lengo la kuzungumza mikakati na mipango ya kuendeleza ushirikiano mapema 05 Juni 2025 mjini Geneva Uswizi.

Bi. Celeste Saulo amesema wapo tayari kuwezesha maeneo mbalimbali ikiwemo ya kuongeza ueleza kupitia mafunzo kwa wataalam kwenye masuala ya Matumizi ya Taarifa za  hali ya hewa pamoja na masuala muhimu kama elimu na kuona namna wanavyoweza kuunga nguvu za Pamoja katika matumizi ya vifaa vya kisasa vya utabiri wa hali ya hewa na matumizi ya taarifa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya hewa kwa lengo la kuendelea kuwa na tahadhari za mapema.

“Tunaendelea kushirikiana na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania kwa kuwa tuna ushirikiano wa muda mrefu.Aidha, tunazingatia umuhimu wa kuimarisha usimamizi wa maafa kwa kuzingatia hatua zinazochukuliwa na Tanzania ya kujenga uwezo pamoja na kushirikiana na nchi zingine na kuandaa miradi ambayo inazingatia vipaumbele vyenye maslahi kwa wote,” alisisitiza Bi. Saulo

Kwa hatua hiyo Bi. Saulo ameipongeza Tanzania kwa namna imeendelea kuwa ya mfano katika kuratibu, masuala ya menejimenti ya maafa na kuhakikisha wanakuwa na mifumo ya tahadhari za mapema inayowasaidia katika kupeana taarifa za mapema zinazosaidia kuzuia madhara yanayoweza kutokea wakati wa maafa.

Aidha alifafanua kuwa mifumo ya tahadhari za mapema ni muhimu kwani inasaidia kuandaa mifumo jumuishi ya kupeana taarifa za tahadhari za mapema; kupata taarifa mapema zinazosaidia kupunguza madhara ya majanga, kuwezesha upatikanaji wa taarifa za awali zitakazosaidia kuimarisha mfumo wa maisha ya jamii ambayo iko katika hatari ya kuathirika na majanga na kupunguza madhara katika kujiandaa kwa ajili ya maafa yanayoweza kutokea.

Katika mazungumzo hayo, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, na Uratibu, Dkt. Jim Yonazi amesisitiza dhamira ya Serikali ya Tanzania kuendeleza ushirikiano na Mamlaka ya Hali ya Hewa Duniani katika kuimarisha masuala ya usimamizi wa maafa inayolenga kuwawezesha kuwa na jamii stahimilivu na majanga na kuifanya Dunia kuwa sehemu salama ya kuishi.

 

Akiongelea namna Tanzania inavyoendelea kuratibu masuala ya Menejimenti ya maafa kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizopo ili kuendela kulinda jamii isipatwe na madhara yatokanayo na maafa huku akiainishsa mafanikio makubwa ikiwemo la uwepo wa Kituo cha Ufuatiliaji wa Mwenendo wa Majanga na Tahadhari ya Mapema (National Emergency Operation and Communication Center Situation Room) katika Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura nchini Tanzania chenye tija kwa Taifa kwani kimerahisisha utekelezaji na utendaji wa haraka katika masuala ya maafa.

Viongozi hao wamejadili umuhimu wa kuweka mikakati madhubuti ya maendeleo jumuishi ili kuhakikisha juhudi za pamoja katika kukabiliana na maafa kwa kushirikiana na wadau wengine ili kuinufaisha jamii nzima.

Read More

Tuesday, June 3, 2025

“USHIRIKI WA TANZANIA JUKWAA LA DUNIA WAONGEZA FURSA ZA KIMATAIFA KUKABILIANA NA MAAFA” DK. YONAZI



TANZANIA imeshiriki Jukwaa la Nane la Dunia la Kupunguza Madhara ya Maafa lenye jukumu muhimu katika kuhamasisha na kukuza ushirikiano kati ya Serikali, Wadau na Mfumo wa Umoja wa Mataifa ili kuharakisha utekelezaji wa hatua za kupunguza madhara ya maafa.

Akizungumza wakati wa Mkutano huyo unaoendelea Mjini Geneva Uswisi kuanzia tarehe 02 hadi 6 Juni 2025, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri, Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu Dkt.Jim Yonazi alisema jukwaa hilo ni chombo cha kutathmini, kujadili maendeleo ya utekelezaji na kuimarisha masuala ya usimamizi wa maafa kimataifa kupitia makubaliano ya hiyari ya nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa ambayo yameridhiwa na Makubaliano ya hiyari ya kimataifa yanayotekelezwa kwa sasa ni Mkakati wa Sendai wa Kupunguza Madhara ya Maafa 2015 – 2030

“Jukwaa hili hutumika kama chombo muhimu cha kukuza ushirikiano katika utekelezaji wa ajenda nyingine za kimataifa zinazochangia kupunguza madhara ya maafa, ikiwa ni pamoja na mkataba wa Paris kuhusu mabadiliko ya tabianchi na malengo ya maendeleo endelevu.

Aliongeza kuwa, Matokeo ya jukwaa hilo yanatumika katika kutoa muelekeo wa masuala ya usimamizi wa maafa katika maazimio ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, baraza la umoja wa mataifa la kiuchumi na kijamii na jukwaa kuu la kisiasa la umoja wa mataifa kuhusu maendeleo endelevu.

Kwa mujibu wa Dkt. Yonazi ameelezwa kuwa, ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kupunguza Madhara ya Maafa imepewa jukumu la kuandaa Jukwaa la Dunia na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa. Jukwaa hufanyika kila baada ya miaka miwili ambapo tangu mwaka 2007, limefanyika mara saba.

Vilevile alisema jukwaa hilo limejumuisha ajenda kuhusu kuimarisha utekelezaji wa mkakati wa Sendai kwa kuzingatia maendeleo na changamoto zilizoainishwa katika mapitio yake ya muda wa kati na Azimio lake kupitia Baraza la Umoja wa Mataifa 2023,

Ajenda nyingine ilihusu kuimarisha mikakati ya kitaifa na serikali za mitaa na mipango ya kupunguza madhara ya maafa, kwa kuzingatia athari za maafa ya hivi karibuni;

“Jukwaa limejadili namna ya kuimarisha mitandao iliyopo na kuanzisha ushirikiano mpya katika ngazi za kimataifa, kitaifa na wadau wa ndani, kubadilishana ujuzi, teknolojia na uzoefu kuhusu sera, programu na uwekezaji kuhusu kupunguza hatari ya maafa.

Dk.Yonazi alisema matokeo ya ushiriki wa jukwaa hilo ni kuimarisha utekelezaji wa Mkakati wa Sendai kupitia Sheria na Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Maafa kwa kupata uzoefu na fursa za kimataifa na wadau.

Matokeo mengine ni kuimarisha uratibu na ushiriki wa pamoja wa sekta na mtazamo wa wadau katika kutekeleza shughuli za maeneo ya maendeleo endelevu, kuibua fursa za rasilimali fedha na mipango ya kiuchumi, kuimarisha miundombinu, hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kulinda mifumo wa ikolojia katika maeneo ya kupunguza hatari ya maafa, tahadhari ya mapema na kurejesha hali.

“Jukwa hili litasaidia kuongeza uwekezaji katika usimamizi wa maafa na tahadhari ya mapema kwa wote kupitia ushirikiano na taasisi za Umoja wa Mataifa na Kimataifa,”alisema.



Read More

Monday, June 2, 2025

DKT. YONAZI ATEMBELEA UWAKILISHI WA KUDUMU WA TANZANIA KATIKA OFISI ZA UMOJA WA MATAIFA GENEVA, AAZIMIA KUIMARISHA USHIRIKIANO

 



Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi ametembelea Ofisi za Ubalozi wa Tanzania nchini Uswisi, ikiwa ni ziara yake ya kikazi nchini humo, lengo ni kushiriki Jukwaa la Nane la Dunia la Kupunguza Madhara ya Maafa linalofanyika kuanzia tarehe 2 hadi 6 Juni, 2025 Jijini Geneva Nchini Uswisi.

Dkt. Yonazi ameongoza ujumbe wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania unaoshiriki Mkutano huo huku akiambatana na Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu, Ofisi hiyo Bi. Stella Mwaiswaga, Mkurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini, Ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Charles Msangi pamoja na Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Menejimenti ya Maafa sehemu ya Utafiti, Ofisi hiyo Bw. Vonyvaco Luvanda.

Aidha, amepokelewa na kufanya mazungumzo na Balozi na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Ofisi za Umoja wa Mataifa na Mashirika mengine ya Kimataifa Geneva Uswisi Mhe. Dkt. Abdallah Possi na kumweleza kuwa ushiriki wa Tanzania katika Jukwaa hilo unatija na manufaa makubwa kwa Taifa.

Alifafanua kuwa Jukwaa hilo linalenga kutathmini, kujadili maendeleo ya utekelezaji wake na kuimarisha masuala ya usimamizi wa maafa kimataifa kupitia makubaliano ya hiyari ya nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa ambayo yameridhiwa.

Sambamba na hilo, Dkt. Yonazi ameupongeza ubalozi huo na kuahidi kuendeleza ushirikiano masuala mbalimbali ili kuona fursa zilizopo Uswisi na kuzichangamkia fursa za kibiashara sambamba za zinazoendana na mabadiliko ya Kiteknolojia.

Akitoa maelezo kuhusu utekelezaji wa shughuli za ubalozi, Mhe. Dkt. Possi amesema amepongeza ushiriki wa Tanzania katika Jukwaa hilo la Nane na kusisitiza kuwa Tanzania ina kila sababu ya kuendelea kushiriki katika mikutano hiyo ili kuwa na mwendelezo mzuri utakaowezesha nchi kupata na kutumia fursa mbalimbali zinazotokana na Majukwaa hayo.



 

Read More

Sunday, May 25, 2025

ASKOFU MSAIDIZI TABORA AWEKWA WAKFU, WAZIRI LUKUVI AMWAKILISHA RAIS SAMIA

 


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Mhe. William Lukuvi, amemuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika ibada maalum ya kuwekwa wakfu kwa Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Tabora, Mhashamu Josephat Jackson Bududu.

Ibada hiyo ya Misa Takatifu imefanyika leo, katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Theresia, Jimboni Tabora, na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali, Kanisa na waumini kutoka maeneo tofauti.

Katika hotuba iliyosomwa kwa niaba ya Rais Samia, Mhe. Lukuvi amempongeza Askofu Bududu kwa kuteuliwa kushika nafasi hiyo, akieleza kuwa Serikali inaendelea kuthamini mchango wa taasisi za dini katika kuimarisha maadili, amani na maendeleo ya jamii.

Sherehe hiyo imehudhuriwa pia na viongozi wa madhehebu mbalimbali, ikionyesha mshikamano wa kidini na kijamii katika mkoa wa Tabora.

Read More

Wednesday, May 21, 2025

DKT. KILABUKO AZINDUA MWONGOZO WA KITAIFA KWA WATOA HUDUMA ZA MAENDELEO YA BIASHARA


 

Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Dkt. James Kilabuko amezindua rasmi Mwongozo wa Kitaifa kwa Watoa Huduma za Maendeleo ya Biashara katika hafla iliyofanyika kwenye Hoteli ya Four Points by Sheraton, Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza hii leo wakati wa uzinduzi  huo kwa niaba ya Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi, Naibu Katibu Mkuu huyo amesema kuwa Mwongozo huo unaweka msingi wa mabadiliko makubwa ambayo yatawawezesha wafanyabiashara wadogo na wa kati ikiwa ni pamoja na wafanyabiashara wakubwa kukuza biashara zao na kuchangia kikamilifu kwenye uchumi wa Taifa.

“Uwepo wa Mwongozo huo unalenga kuweka viwango, mwelekeo na uratibu wa huduma zinazotolewa kwa wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo na wa kati nchini, hivyo umekuja kwa wakati sahihi na tunaamini utaleta matokeo chanya kama ilivyokusudiwa,” alisema Dkt. Kilabuko.

Aidha alitumia nafasi hiyo kumpongeza Mheshimiwa Dkt Samia Suluhu Hassan kwa jitihada anazozifanya katika kuhakikisha mazingira ya wafanyabiashara na wawekezaji nchini yanaendelea kuwa bora.

“Kwa umuhimu wa pekee napenda kumshukuru kwa dhati, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jitihada anazofanya katika kufungua uchumi na kuchochea biashara na uwekezaji nchini.Rais wetu ameboresha mazingira ya biashara nchini na kuchochea kuanzishwa kwa shughuli za kiuchumi nyingi katika sekta mbalimbali. Shughuli hizo pia zinahitaji huduma za maendeleo ya biashara ili kuwa shindani.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wanamanchi Kiuchumi (NEEC) Bi. Beng'i Issa ameleeza kuwa Mwongozo wa Huduma za Maendeleo ya Biashara kwa Watoa Huduma za Maendeleo ya Biashara Tanzania unalenga kuboresha utoaji wa huduma za biashara ikiwa ni pamoja na: ushauri, mafunzo, msaada wa kiufundi, ujuzi, uatamizi, uhusiano baina ya wafanyabiashara, mawasiliano, na usimamizi wa biashara.

“Tunategemea, Mwongozo huu unakwenda kutoa dira ya namna bora ya utoaji wa huduma za biashara Tanzania zinazoweza kuboresha biashara na hivyo kuchochea ukuaji wa uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujuml,” alisema Bibi. Beng’i.

Alifafanua kuwa, mwongozo huo utaleta matokeo chanya na kuwasihi watoa huduma za maendeleo ya biashara nchini kutumia Mwongozo huu kama nyenzo katika kuwahudumia wafanyabiashara wadogo na wa kati wanaotekeleza shughuli za kiuchumi katika sekta mbalimbali.

 

Read More

Thursday, May 15, 2025

WAELIMISHA RIKA WATAKIWA KUTUMIA MBINU ZA KISASA KATIKA KUELIMISHA MASUALA YA AFYA KAZINI

 


Waelimisha rika Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) watakiwa kutumia mbinu mbadala na zinazokwenda na mazingira ya sasa katika kufikisha elimu ya afya kwa watumishi wenzao kazini huku wakijitolea kwa uzalendo na weledi ili kuendelea kuwa na mazingira mazuri ya utendaji wa kazi kwa kuzingatia afya zao.

Hayo yamebainishwa Kaimu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Bw. Eleuter Kihwele kwa niaba ya Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Dkt. Jim James Yonazi hii leo, wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya siku mbili kwa waelimisha rika mahala pa kazi, yanayofanyika mjini Morogoro.

Kihwele amesema kuwa mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo waelimisha rika katika utoaji wa elimu, hasa katika kipindi hiki ambapo jamii inakumbwa na ongezeko la magonjwa yasiyoambukizwa pamoja na changamoto nyingine za kiafya.

“Mafunzo haya yatakuwa na mada muhimu. Zingatieni ili kuwawezesha watumishi wenzenu kupata uelewa wa kina kuhusu masuala ya VVU na UKIMWI pamoja na magonjwa yasiyoambukizwa,” alisema Bw. Kihwele.

Aidha, amepongeza maandalizi ya mafunzo hayo, akisisitiza kuwa yatatoa mwanga na mwelekeo mpya wa kuhakikisha Ofisi ya Waziri Mkuu inakuwa mfano wa kuigwa katika kueneza elimu ya afya kwa watumishi wake.

Kwa mujibu wa Kihwele, mafunzo kwa waelimisha rika hufanyika kila mwaka ili kutathmini utekelezaji wa mwongozo uliopo, kubaini changamoto na kuja na mikakati bora ya kudhibiti magonjwa katika Idara na Vitengo husika.

Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Menejimenti ya Anuai za Jamii, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora;Bi. Mwanaamani Mtoo, ameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuendeleza utekelezaji wa mwongozo wa waelimisha rika kwa mafanikio makubwa.

“Sisi kama wasimamizi wa rasilimali watu, tunawapongeza kwa hatua mliyoifikia. Kuendeleza juhudi hizi ni hatua muhimu ya kudhibiti maambukizi ya VVU na UKIMWI pamoja na magonjwa yasiyoambukizwa kazini,” alisema Bi. Mtoo.

Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu imeendelea kuweka kipaumbele katika afya na ustawi wa watumishi wake, ikiwemo kutoa mafunzo ya stadi za afya kwa waelimisha rika na kuwawezesha kuwa mabalozi wa mabadiliko ya kiafya katika maeneo yao ya kazi.

 

Read More

Thursday, March 20, 2025

WANANCHI WAKUMBUSHWA KUHUSU MATUMIZI SAHIHI YA ALAMA ZA TAIFA.


Wito umetolewa kwa Wananchi kuzingatia matumizi sahihi ya Alama za Taifa ikiwemo Ngao ama Nembo ya Taifa, Bendera ya Taifa na Wimbo wa Taifa na kuendelea kujifunza matumizi sahihi ya alama hizo pamoja na matumizi  ya Gazeti la Serikali

Hayo yamesemwa na Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali Bw. George Lugome kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu, alipokuwa akizungumza na chombo kimoja cha Habari Jijini Dar es Salaam.

Bw. Lugome amesema kuwa hivi karibuni kumekuwa na upotoshwaji wa Alama za Taifa na kukumbusha kuwa Alama hizi zipo kwa mujibu wa sheria “Na yeyote atakayechezea alama hizi atapata adhabu kwa mujibu wa sheria na adhabu yake kwa yeyote anayekiuka atatumikia kifungo cha miaka miwili Jela ama faini,ama vyote viwili kwa pamoja, ambapo sheria hii ya mwaka 1964 ipo kwenye mchakato wa kubadilishwa.” Alisisitiza.

Akizungumza kuhusu Nembo ya Taifa, Bw. Lugome alisema kuwa Nembo hiyo, ipo kwa Matumizi ya shughuli za Serikali pekee na sheria imesema Wazi, na aliongeza kwa kusema kuwa matumizi ya alama za Taifa ambayo siyo sahihi yanaharibu Haiba ya Taifa na Idara ya Mpiga Chapa ndo yenye jukumu kubwa la kuhakikisha kuwa matumizi ya Alama hizi yanatumika kwa usahihi.

Aidha, Bwana Lugome Alifafanua kuwa uchapishaji holela wa alama hizi na  uchoraji wa nembo hizi kuonesha ubunifu wao, unachangia upotoshwaji na kuharibu uhalisia wake.

Kwa Upande wa Bendera ya Taifa, Bw. Lugome Alizungumza na kutolea ufafanuzi kuhusu rangi nne za Bendera ya Taifa zinazotumika

Akizungumzia Wimbo wa Taifa, Bw. Lugome alisema Wimbo wa Taifa Unavyoimbwa lazima uimbwe kwa beti zote mbili na kufuata Ala zilizowekwa na kusimama kikakamavu ambapo ni hali ya kuonesha utamaduni na Uzalendo kwa Taifa hili.

Kwa upande wa Gazeti la Serikali alisema kuwa, ni jarida Linaloratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu na Kuhaririwa na Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora, ambapo linachapishwa mara moja kwa wiki na kujikita katika kutoa taarifa Muhimu za Serikali hususan Utendaji wa Serikali na Taarifa Binafsi, na Jarida hili lipo kwa Mujibu wa Sheria ya Utumishi wa Umma, na kanuni za kudumu za Utumishi wa umma kanuni C27-30

 

Read More

Monday, March 17, 2025


 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) Mhe. William Lukuvi amesema Tanzania imebahatika kuongozwa na viongozi wanaojali utu na kutanguliza maslahi ya taifa mbele hivyo tunamshukuru Mungu kwa kuwafanya sehemu ya historia kwa sababu taifa linaendelea kushuhudia mazuri waliyofanya kwa ajili ya nchi.

 Waziri Lukuvi  ametoa kauli hiyo  wakati alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Ibada ya Misa Takatifu ya kumuombea aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano Hayati Dkt. John Pombe Magufuli iliyofanyika Kanisa Katoliki la Mt. Yohaba Maria Muzevi Chato.

 “Leo tunadhimisha miaka Minne tangu tondokewe na mpendwa wetu Hayati Rais wa Awamu ya Tano Dkt. John Pombe Magufuli, kwa hali ya kibinadamu si rahisi kusahau kumbukumbu ya kuondokewa na mpendwa wetu kwa jamii inayomfahamu na kujumuika naye katika maswala mbalimbali ya kitaifa”.

 Aidha, amebainisha kuwa, Hayati Ally Hassani Mwinyi, Rais wa Awamu ya Pili wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa uhai wake aliwahi kusema, “maisha ya mwanadamu ni hadithi tuu, basi ewe ndugu yangu kuwa hadithi nzuri kwa wale watakaosimuliwa”, hii inamaanisha viongozi waliopita wameishi vyema na ndio maana tuna ujasiri wa kusimulia yaliyomema katika kumbukizi zao na kuendelea kusimulia yaliyofanywa na Hayati Dkt, John Pombe Magufuli.

 “Hayati Dkt, John Pombe Magufuli alikuwa kiongozi aliyejali watu na rasilimali za nchi yake na mchamungu hivyo tutaendelea kushirikiana na familia katika kumuenzi, kumuombea na kutangaza mema aliyoyafanya katika jamii na kama baba wa familia na kiongozi wa taifa letu,” alieleza.

 Aidha, Waziri Lukuvi amesema, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amekuwa karibu na familia tangu wakati wa uhai wa mtangulizi wake Hayati Dkt. John Pombe Magufuli mpaka sasa.

 “Upendo na ukaribu wake kwa familia umedhihirishwa kwa mambo mengi, mambo mengine tunayaona na yapo mengine familia wanayajua na sisi wengine hatuwezi kuyaona ndio maana katika matukio muhimu kama haya familia imekuwa ikimualika moja kwa moja, na Rais Dkt Samia Suluhu Hassani amekuwa akiitikia mialiko hiyo kwa kushiriki yeye mwenyewe au kutuma miongoni mwa wasaidizi wake kuja kumuwakilisha pale anapokuwa na majukumu mengine ya kitaifa” alisema Waziri Lukuvi.

 Katika hatua nyingine Waziri Lukuvi amesema Mhe. Dkt, Samia Suluhu Hassani Rais wa Jamhuri ya Mungano wa Tanzania aliyeshika kijiti ameendeleza yale yote yaliyoanzishwa na Dkt. Magufuli na tumeshuhudia miradi mingi ikikamilika, mingine ikiwa katika hatua ya kuelekea ukamilifu na miradi mingi imeanzishwa kwa mwenendo ule ule na fikra zilezile kwa slogani yake kazi iendelee.

 “Ni adhima ya Mhe. Rais Dkt, Samia Suluhu kuwaenzi viongozi wakuu wa kitaifa waliomtangulia na hatuna budi kuwaenzi viongozi hao kwa vitendo katika utendaji washughuli zetu, hivyo ni wasihi tuendele kumuombea ndugu yetu Hayati, John Pombe Magufuli na familia yake ikiongozwa na mama Janeth Magufuli”

“Tuendelee pia kumuombea Rais wetu wa Awamu ya Sita Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ili aendelee kuliongoza taifa kwa utulivu na amani kama tunavyoshuhudia sasa Tanzania imetulia kwa sababu Mkuu wa Nchi anafanya kazi kwa niaba ya Watanzania wote,” alibainisha.

 Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe. Martin Shigela amemshukuru mama Janeth Magufuli kwa jinsi alivyoweka utaratibu wa kumkumbuka Hayati John Pombe Magufuli lakini pia amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendeleza misingi ya amani na utulivu.

 “Tuendelee kumuombea Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aendele kuliongoza taifa kwa utulivu, amani na maendeleo kama tunavyoshuhudia sasa Tanzania ikiwa imetulia,” alihimiza

Nae, Askofu wa Jimbo katoliki Rulenge Ngara Mhashamu Severine Niwemugizi amesema Kanisa Katoliki lina utamaduni wa kuwakumbuka marehemu wote, ambao pia ni desturi ya kujifunza kutokana na maisha yao.

 “Tunajua Hayati Dkt, Magufuli alipenda nidhamu katika utumishi wa umma na kuwajibika ikiwa ni pamoja na kukata mambo mabaya rushwa, unyanyasaji na uonevu hivyo tuandike kitabu chetu tukiwa tunaishi, ili tukimaliza kuandika kiwe na kurasa zenye mambo mazuri tuweze kujifunza na yale mambo mabaya tuachane nayo,” alieleza.

 Akizungumza kwa niaba familia Bi, Jesca Magufuli, amemshukuru kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassani kwa kuunga mkono na kudumisha maono ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli.

 “Miaka minne iliyopita alipotembelea hapa Chato alituahidi kama familia kwamba hata tuacha na leo tunashuhudia uaminifu wake katika kutekeleza ahadi zake,” alisema Bi. Jesca.



Read More

Friday, March 14, 2025

“WATENDAJI OFISI YA WAZIRI MKUU ENDELEENI KURATIBU VYEMA TAARIFA ZA UTEKELEZAJI WA SERIKALI KWA MANUFAA YA TAIFA” WAZIRI LUKUVI


Watendaji wa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu wamehimizwa kuratibu vyema taarifa za utekelezaji wa Serikali ya Awamu ya Sita na kuzisemea kazi hizo kwa wananchi ilia wapate uelewa wa uhakika wa miradi ya maendeleo iliyofanywa na Serikali katika maeneo yao.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uaratibu) Mheshimiwa William Lukuvi wakati akifungua kikao cha baraza la wafanyakazi la Ofisi ya Waziri Mkuu, katika Ukumbi wa Ngome Jijini Dodoma.

Ameongeza kusema Watendaji wa Ofisi ya Waziri Mkuu wana majukumu makubwa hivyo wanapaswa kuwa kioo katika utekelezaji wa kazi vizuri na usimamizi wa shughuli za Serikali ili waweze kuratibu taarifa za mafanikio kwa wananchi.

“Tunalo jukumu la kuwaambia wananchi kazi zilizofanywa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kipindi chake cha uongozi na kwa kuzipambanua vizuri ikiwa ni sehemu ya uratibu ili wananchi wazijue kwa uhakika huko waliko,” alieleza Waziri.

Ili tuweze kuratibu lazima majukumu yaliyo ndani ya Ofisi yetu yaweze kusimamiwa vizuri sana kwa kuwa mfano katika idara zetu ili tuweze kusimamia idara na taasisi zilizo nje vizuri.

Amefafanua, Waziri Mkuu anaamini kwamba watendaji wa Ofisi yake wapo na wanamsaidia katika jukumu kubwa la kuratibu shughuli zote za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Nikupongeze tena Katibu Mkuu Dkt. Yonazi kwa usimamizi mzuri na timu ya menejimenti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, tuendele kushirikiana katika kufanya kazi lakini niwapongeze Wakuu wa Idara na Vitengo nimewatembelea mnafanya vizuri sana,” alisema Waziri.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi ameshukuru Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na Naibu Waziri wa Ofisi hiyo kwa miongozo mizuri wanayotoa ili kuweza kutimiza majukumu ya kila siku.

“Viongozi wetu Wakuu wanafahamu kazi ambazo tumekuwa kukizifanya na kwa kupitia nyie tunaomba mtufikishie salamu za shukrani kwao,” alieleza

Naye Msaidizi wa Katibu wa (TUGHE) Mkoa wa Dodoma Bi, Maisha Mbilla amesema wanafahamu kwamba watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) wanafanya kazi kwenye mazingira mazuri na wanapata stahiki zao vizuri, na kuupongeza uongozi wa Ofisi hiyo.

“Hii inatutia faraja na moyo na tuna wajibu kama Chama Cha Wafanyakazi wakuongea na watumishi ili waendelee kufanya kazi kwa kufuata sheria kanuni na taratibu pamoja na miongozo ya Utumishi wa Umma,” alihimiza



Read More

Thursday, March 13, 2025

MIFUMO RAFIKI YA UPATIKANAJI WA NYARAKA IWEKWE KUWAFIKIA WANANCHI KWA WAKATI

 


Idara ya Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali yatakiwa kuweka mifumo mizuri ya usambazaji wa nyaraka za wazi kwa wananchi kupitia mifumo ya kidigitali na hata kwa mifumo ya nyaraka ngumu ili wananchi wanufaike na taarifa hizo.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) Mhe William Lukuvi alipofanya ziara katika Idara ya Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali Jijini Dodoma t ambapo amejionea maendeleo ya ujenzi na ufungaji wa mitambo mipya ya uchapishaji wa nyaraka za serikali.

Amesema, nyaraka nyingi na muhimu huchapwa kwenye Gazeti la Serikali hivyo mkiongeza uelewa kwa wananchi juu ya namna ya kulipata Gazeti la Serikali inarahisha taarifa hizo muhimu kufikia walengwa.

“Tunaweza kufanya jitihada hizi za kusambaza taarifa la Gazeti la Serikali kupatikana katika shule kwa njia za kidigitali kupita mifumo ya computa ambazo zimeanza kutumika katika utoaji wa elimu ili wanafunzi waweze kuzipata,” alifafanua

Nitoe rai kwa Idara ya Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali hasa kwenye nyaraka ambazo ni za wazi fanyeni uelimishaji ili taarifa Magazeti ya Serikali ziweze kuwafikia wananchi.

“Tunaamini Serikali kwa kununua mitambo hii ya kisasa itasaidia Watendaji wa Idara ya Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali kujiweka sawa kimafunzo na maadili ili utunzaji wa nyaraka na siri uzidi kuimarika,” alisisitiza

Hivyo basi Idara ya Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali inaendelea kuwa  mhimili Mkuu wa Serikali kwa miaka yote katika uchapishaji wa nyaraka za Serikali hasa zinapokuwa nyaraka nyingi na nyeti na zinahitajika kwa uharaka.

Kwa upande wake Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali Bw. George Lugome amesema wanatengeneza mfumo wa mtandao ambao utamsaidia mteja kujaza taarifa zake na kufanya malipo kwa njia ya mtandao na tangazo kutoka katika gazeti la serikali.

Ameongeza kusema “mfumo wa mtandao hauhusiki taarifa za mirathi ambazo uwasilishaji wake unahitaji Mhusika kuleta vielelezo vyake vya uthibitisho kwa mujibu sheria.”

Mpiga Mchapa amesema, kwa uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali katika ununuaji wa mashine za kisasa utasaidia katika kuongeza uzalishaji na kuongeza maduhuli ya Serikali.



 

Read More

Wednesday, March 12, 2025

NAIBU WAZIRI UMMY AZINDUA MTANDAO WA UWEZESHAJI WA WATU WENYE ULEMAVU MAHALI PA KAZI

 


Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masual aya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Ummy Nderiananga amezindua rasmi Mtandao wa Uwezeshaji wa Watu Wenye Ulemavu Mahali pa Kazi nchini (National Business Disability Network – NBDN).

 Mhe. Nderiananga amefanya uzinduzi huo kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Ridhiwani Kikwete ambapo alikipongeza Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) kwa kushirikiana na Shirika Lisilo la Kiserikali la Sightsavers International kwa kuona umuhimu wa kuwa na mtandao huo.

Alisema kuanzishwa kwa mtandao huo utahakikisha kuwa watu wenye ulemavu wanapata fursa sawa na kushiriki kikamilifu katika soko la ajira akisema ni jambo la msingi kwa ustawi wa jamii na kwa maendeleo ya taifa kwa ujumla.

“Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imekuwa mstari wa mbele kuhakikisha kuwa haki za watu wenye ulemavu zinaheshimiwa na kuthaminiwa,” Alisema Naibu Waziri huyo.

 Aliongeza kwamba Serikali imeendelea kutekeleza Sera na Sheria mbalimbali zinazolinda haki za watu wenye ulemavu, zikiwemo Sera ya Taifa ya Uwezeshaji Watu Wenye Ulemavu na Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na. 9 ya mwaka 2010.

 Vile vile alibainisha kuwa watu wenye ulemavu wamekuwa wakikabiliwa na changamoto mahali pa kazi, ikiwa ni pamoja na unyanyapaa, ukosefu wa miundombinu rafiki, na uelewa mdogo wa waajiri kuhusu uwezo wa watu wenye ulemavu katika kuchangia maendeleo ya taasisi na taifa.

“Napenda kuwasihi waajiri wote wa sekta binafsi nchini kuhakikisha kuwa wanazingatia masuala ya ujumuishaji kwa kutoa nafasi kwa watu wenye ulemavu, si kwa misingi ya hisani, bali kwa kutambua mchango wao katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Tunapaswa kuondoa vikwazo vyote vinavyowazuia watu wenye ulemavu kushiriki kikamilifu katika soko la ajira,”Alisisitiza.

 Aidha Naibu Waziri huyo alifafanua kwamba Serikali itaendelea kushirikiana na sekta binafsi, asasi za kiraia na wadau wote ili kuhakikisha kuwa ajenda ya ujumuishaji wa watu wenye ulemavu inatekelezwa kwa ufanisi.

 “Kwa pamoja, tunaweza kuleta mabadiliko chanya na kujenga jamii jumuishi inayotoa fursa sawa kwa wote. Hata hivyo, kupitia mtandao wa NBDN, nina imani kuwa changamoto hizi zitapungua kwa kiasi kikubwa kwa kuwa utatoa mwongozo na kusaidia waajiri kutekeleza sera za ujumuishaji kwa vitendo,”Alihimiza Mhe. Nderiananga.



 

Read More

Sunday, March 2, 2025

MHE. NDERIANANGA AGAWA FUTARI KWA WATU WENYE ULEMAVU ZANZIBAR

 


Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Ummy Nderiananga amegawa futari kwa watu wenye ulemavu 500 kutoka Wilaya Saba za Mkoa wa Kusini Unguja.

Akizungumza katika ukumbi wa Dkt. Ali Mohamed Shein, Tunguu, Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar Mhe. Nderiananga aliwaomba  waumini wa dini ya kiislamu na watanzania wote kuutumia mwezi  Mtukufu wa Ramadhan kwa  kufanya ukarimu kwa wanyonge, wasiyojiweza na watu wenye ulemavu.

Mhe. Nderiananga amegawa futari hiyo kwa kushirikiana na Shirika lisilo la kiserikali linaloshughulikia watu wenye ulemavu la Tanzania Foundation for Excellence in Disabilities (TFED) iliyoambatana na dua maalum  ya kumuombea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  katika utekelezaji wa majukumu yao  ili Taifa liwe na amani, umoja na mshikamano.

“Nimshukuru sana Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwani  viongozi wetu hawa wamekuwa watu wema wametujali na kututhamini wakati wote. Sisi watu wenye ulemavu Watoto wa Dkt. Samia na Dkt. Mwinyi tumeona ushirikishwaji mkubwa katika serikali na sekta binafsi,” Mhe. Nderiananga.

Pia alimpongeza Dkt. Samia kwa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati kwani ni nia yake njema kwa watanzania wote kuwa na maendeleo huanzia ngazi ya familia hadi Taifa kwa ujumla.

Vilevile alitumia nafasi hiyo kumpongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa kazi kubwa aliyoifanya katika utekelezaji wa miradi ya kimaendeleo kama ujenzi wa Barabara kwa kiwango cha lami.

“Mheshimiwa Rais wa Zanzibar Dkt. Hussein Ali Mwinyi amefanya kazi kubwa sana hapa Zanzibar barabara  zimejengwa kila mahali watu wanaendelea  na shughuli  zao. Sekta ya afya Dkt. Mwinyi amewashangaza wengi kwa ujenzi wa hospitali za Wilaya zenye vifaa tiba vya kisasa, sekta ya maji na elimu ambapo tunashuhudia ujenzi wa shule katika maeneo yetu,”Alipongeza.

Aidha aliwasisitiza wazazi na walezi kutowaficha  watoto wenye ulemavu ndani na badala yake wawapeleke shule kwani Serikali iko tayari kwa ajili ya kuwahudumia kuhakikisha wanatimiza ndoto zao na kuwa nguvu kazi ya Taifa.

Kuelekea maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani inayotarajiwa kuadhimishwa Machi 08 mwaka huu ameiomba jamii kuendelea kuiamini nafasi ya mwanamke katika uongozi akisema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ni mfano wa kuigwa hivyo wanawake hawana budi kujitokeza kugombea katika nafasi mbalimbali pindi wakati utakapowadia wa uchaguzi unatakaofanyika mwezi Oktoba 2025.

 

Read More

Thursday, February 27, 2025

WAZIRI LUKUVI AMEKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA UJUMBE KUTOKA SHIRIKA LA FAO

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala Sera, Bunge na Uratibu Mheshimiwa William Lukuvi amekutana na kufanya mazungumzo na ujumbe kutoka Shirika la Kilimo na Chakula Duniani (FAO) katika ukumbi wa Ofisi ya Waziri Mkuu uliyopo katika Mtaa wa posta Jijini Dodoma.

Ujumbe huo kutoka FAO umefanya ziara ya wadau wa ufadhili wa Mfuko Nyumbulifu wa Uchangiaji kwa Hiari (Flexible Voluntary Contribution - FVC) iliyohusisha  Waheshimiwa Mabalozi wa Ubelgiji na Uswisi, Wawakilishi wa Kudumu FAO katika Umoja wa Mataifa, Rome, Washauri Waandamizi wa Shirika la Maendeleo la Kimataifa (IDC) na Viongozi Waandaamizi wa FAO Makao Makuu.

Ziara hiyo ilikuwa na lengo la kuwezesha washirika (partners) kupata uelewa wa utekelezaji wa programu na miradi inayofadhiliwa kupitia Flexible Voluntary Contribution (FVC) nchini Tanzania, kuongeza uelewa, muonekano na fursa zinazopatikana kwenye FVC kama mfuko nyumbulifu wa utoaji misaada ili kuweza kufikia malengo ya kimkakati Kitaifa na Kimataifa kupitia FAO.



Read More

Wednesday, February 26, 2025

TAARIFA ZA AWALI ZA TAADHARI ZA MAAFA ZITOKE KWA WAKATI

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) Mhe. William Lukuvi ameelekeza Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura kujiratibu vizuri katika kufikisha taarifa zote za taadhari ya maafa kwa wakati ili utekelezaji wake ufanyike mapema kabla ya madhara kutokea.

Kauli hiyo ametoa leo alipotembelea Kituo cha Ufuatiliaji wa Majanga Katika Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Kilichopo Ofisi ya Waziri Mkuu, Mji wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma.

" kwa nafasi mliyonayo na teknolojia mnazotumia mnaweza kujua na kutoa taarifa zote za tahadhari bila urasimu, ili kuepuka athari kubwa za maafa zinazoweza kutokea baadae."alisisitiza Waziri Lukuvi.

Aidha muangalie na uwezekano wa kurahisisha mawasialiano ya taarifa zote za tahadhari ziweze kupatikana kila siku kwa njia ya simu ili kila mtu anayeenda kwenye shughuli ajue na achukue tahadhari.

“huduma hii iwe bure na ipatikane muda wote ili wananchi waingie wasome na wachukue tahadhari, na tutakuwa tumefanya kazi yetu vyema,” alisema

Naye Mkurugenzi Msaizidizi anaye simamia  Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Bi: Jane Kikunya amelezea kuhusu ufanyaji kazi wa kituo hicho kwamba kinajukumu kubwa la kufuatilia majanga ikiwa ni pamoja kushirikiana na taasisi mbalimbali katika ngazi ya kitaifa katika kutoa taarifa za awali za tahadhari kwa ngazi mbalimbali.

Amefafanua kwamba katika Ngazi ya Mikoa kuna vituo vya maafa vinapaswa kuanzishwa na jukumu hilo limeainishwa katika sheria ya maafa ya mwaka 2022 ambayo imeeleza kila Mkoa, kuwa na kituo cha usimamizi wa maafa ili kufanya ufuatiliaji wa majanga yanayoweza kutokea katika eneo la Mkoa husika.

Hivyo Ofisi ya Waziri Mkuu inafanya ufuatiliaji wa uanzishwaji wa vituo hivyo ambapo wameweza kukutana na Makatibu Tawala Wasaidizi wa Mikoa ambao kisheria wamepewa jukumu la usimamizi wa vituo hivyo ili kujengeana uelewa wa miongozo na namna ya uanzishaji na usimamizi wa vituo hivyo.

“Vituo hivyo vya Mikoa vitaunganishwa na mifumo ya Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu ili waweze kufanya ufuatiliaji kwa karibu,” alibainisha Bi. Jane.



Read More