Kwa upande wake, Bi. Mwakatobe ameahidi AICC kuipa Dodoma kipaumbele katika uwekezaji, na kueleza kuwa taasisi hiyo iko tayari kushirikiana na Serikali kuhakikisha miradi hiyo inatekelezwa kwa viwango vya kimataifa.
Wednesday, October 15, 2025
SERIKALI YATANGAZA FURSA ZA UWEKEZAJI WA UTALII WA MIKUTANO KATIKA MJI WA SERIKALI MTUMBA
Monday, September 29, 2025
DKT. YONAZI: TUIMARISHE LISHE, TUPUNGUZE MAGONJWA SUGU
KATIBU Mkuu, Ofisi ya Waziri
Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi amewataka wadau kushirikiana na
Serikali katika kuimarisha hali ya lishe nchini ili kupunguza kasi ya kuenea
kwa magonjwa yasiyo ya kuambukiza.
Amesema ulaji usio faa na
mitindo mibaya ya maisha vimechangia kuongezeka kwa magonjwa sugu yasiyo ya
kuambukiza jambo linalohatarisha maendeleo ya Taifa.
Dkt. Yonazi ameyasema hayo
jijini Dar es salaam leo katika Mkutano Mkuu wa 11 wa Wadau wa Lishe
unaoendelea katika kituo cha mikutano cha APC Bunju.
Dkt. Yonazi amesema tafiti zinaonesha kuwa
uzito uliozidi na uliokithiri ni chanzo kikuu cha magonjwa sugu yasiyo ya
kuambukiza yakiwemo kisukari, moyo, figo
na baadhi ya saratani.
“Napenda kukumbusha wadau,
taasisi na wataalam kushirikiana na serikali kufanya tafiti zitakazosaidia
kuleta majibu ya changamoto za lishe, pamoja na kusaidia watu kubadili tabia za
ulaji na mtindo wa maisha ili kuzuia magonjwa sugu yasiyo ya kuambukiza
yanayohusiana na ulaji usiofaa na ambayo ni tishio kwa Taifa letu,”alisema Dkt.
Yonazi
Dkt.Yonazi ameongeza kuwa Takwimu zinaonesha licha ya hali ya lishe nchini kuendelea
kuimarika bado kuna changamoto hususani kwenye uzito uliozidi na kiriba tumbo
hii kutokana maendeleo tunayoyapata na mabadiliko ya mtindo wa maisha
hususani ulaji usiofaa hivyo jitihada za
pamoja kati ya wadau na serikali zinahitajika ili kukabiliana na tatizo hili.
Akizungumza kuhusu mkutano huo
Dkt. Yonazi amesema lengo ni kupokea na kujadili hatua iliyofikiwa katika utekelezaji
wa afua za lishe kwa kipindi cha Mwaka wa Tatu 2024/2025 katika maeneo mahsusi
yaliyoanishwa kwenye Mpango Jumuishi wa Kitaifa wa Lishe (2021/22-2025/26).
Vilevile amesema mkutano huo
unatoa fursa kwa wadau wote wa lishe kujadili namna utekelezaji ulivyofanyika,
changamoto na mikakati ya kufanikisha utekelezaji katika kipindi kilichobaki
cha utekelezaji wa mpango huo hususan mwaka 2025/26.
Kwa mujibu wa Dkt. Yonazi
mkutano huo unatazamiwa kuongeza msukumo mpya wa utekelezaji wa afua za lishe
miongoni mwa wadau kama moja ya nguzo muhimu kwa maendeleo ya Taifa.
“Uwepo wenu hapa, ni
uthibitisho tosha wa ushirikiano mlionao na utayari wenu katika kuhamasisha
uboreshaji wa hali ya lishe kwa Watanzania, hususani makundi yanayoathirika
zaidi ambayo ni watoto wadogo na wachanga, watu wenye mahitaji maalum, wanawake
wajawazito na wale walio katika umri wa uzazi,”amesema Dkt. Yonazi.
Dkt. Yonazi amewashukuru wadau wote walitoa mchango wa fedha na
ushauri wa kitaalamu katika kufanikisha maandalizi ya mkutano huo na
amewahakikishia kuwa serikali itaendelea kuunga mkono juhudi za wadau ili
kuhakikisha Taifa linapata mafanikio dhidi ya mapambano ya tatizo la utapiamlo.
Thursday, September 25, 2025
DKT. YONAZI ATOA WITO WATUMISHI KUBEBA MAONO YA DIRA YA TAIFA 2050
Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri
Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Dkt. Jim Yonazi, ametoa wito kwa Viongozi,
Menejimenti na Watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zake kubeba malengo
ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 kama sehemu ya wajibu wao wa kitaifa ili
kuweza kufikia maono yaliyopo kufikia mwaka 2050.
Dkt. Yonazi ametoa wito huo wakati ufunguzi wa
Kikao cha Mazingativu ya Menejimenti, Wakuu wa taasisi na Watumishi wa Ofisi ya
Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu na taasisi zake kinachofanyika leo Jijini
Arusha.
“Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 tayari
imeshazinduliwa, Dira hii ni ramani ya mustakabali wa nchi yetu, ikitupa
taswira ya nchi ambayo tunaihitaji kuwa nayo katika ndani ya miaka 25 ijayo,
ili kufanikisha maono haya kila mmoja wetu anawajibu na anajambo la kulifanya,
ni wajibu wetu kujiuliza kwamba nitachangia nini kuhakikisha nchi yangu
inafikia maono haya kufikia mwaka 2050” ameeleza Dkt. Yonazi.
Aidha, amebainisha kuwa, kila mmoja mahali
pake pa kazi anawajibu kwa kuhakikisha nchi ya Tanzania inakuwa nchi bora na
mahali bora pa kuishi kwa kuweka misingi bora ifikapo mwaka 2050.
Akizungumza kuhusu kikao hicho, Dkt. Yonazi
amebainisha kuwa, kikao hicho ni sehemu ya utamaduni wa Ofisi ya Waziri Mkuu
kutenga muda kila mwaka kwa ajili ya kujitafakari, kujifunza na kujipanga upya
kwa lengo la kuboresha utendaji katika kutekeleza majukumu ya Ofisi hiyo.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Arusha,
Joseph Mkude akimuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Arusha CPA. Amos Makalla ametoa
wito kwa Watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu kuwa wabunifu katika kufikiri na
kutekeleza majukumu yao, ili kuweza kutoa huduma zinazokidhi mahitaji na
matarajio ya wananchi kwa ufanisi zaidi.
“Dunia ya sasa inabadilika kwa
kasi kubwa na changamoto zake zinahitaji mbinu mpya za kuzikabili, ni wajibu
wetu kuwa wabunifu katika kufikiri na kutekeleza majukumu yetu, ili tuweze
kutoa huduma zinazokidhi mahitaji na matarajio ya wananchi kwa ufanisi zaidi.
Hivyo, kubadilika kulingana na wakati ni muhimu ili kuendana na mabadiliko ya
kidunia, kitaifa na kijamii, tukizingatia misingi hii, tutakuwa na Ofisi yenye
weledi, inayothamini maendeleo endelevu na inayokabiliana na changamoto kwa
mafanikio” alisema.
Aidha, Mkuu wa Wilaya huyo amebainisha kuwa
“Kwa kuwa jukumu la uratibu, ufuatiliaji na tathmini ya shughuli zote za
Serikali lipo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, nitumie fursa hii kutoa rai kuwa
tuendelee kulitekeleza jukumu hili kwa ufanisi wa hali ya juu. Kila taasisi
inapaswa kuonesha matokeo halisi katika maeneo yake ya utekelezaji, tuweke
mkazo zaidi katika kuhakikisha kwamba kazi zetu zinajikita kwenye matokeo
yanayogusa maisha ya wananchi, badala ya kuishia kwenye michakato au
utekelezaji usioonesha matokeo”.
Mbali na hayo Mhe. Mkude
ametoa wito wa kushiriki uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani kwani
Uchaguzi huo ni fursa ya kipekee kushiriki katika kuimarisha misingi ya
demokrasia na utawala bora.
“Kila Mtanzania anatakiwa kutimiza haki na
wajibu wake wa kikatiba kwa kupiga kura, ili kuchagua viongozi watakaoliongoza
Taifa letu katika ngazi zote, aidha, ni wajibu wa kila mmoja wetu kuhakikisha
tunadumisha amani, mshikamano na utulivu katika kipindi chote cha uchaguzi, ili
Tanzania iendelee kubaki kuwa mfano bora wa utulivu, mshikamano na demokrasia
barani Afrika” ameongeza.
Kikao hicho kinaendelea Jijini Arusha, na mada
mbalimbali zitawasilishwa ikiwemo ikiwemo Matumizi ya Akili Unde (AI) mahala pa
kazi na mustakabali wa ajira kutokana na maendeleo ya kasi ya sayansi na
teknolojia, masuala ya afya ya akili, fursa za uwekezaji kwa watumishi na
maandalizi ya maisha baada ya kustaafu, masuala ya itifaki na ustaarabu na Dira
ya Maendeleo ya Taifa 2050, ili kuweza kujiimarisha katika nyanja mbalimbali
kitaaluma, kimaisha na kiutumishi.
Sunday, September 21, 2025
UBUNIFU UENDELEZAJI MAKAO MAKUU, MJI WA SERIKALI WAHITAJIKA- DKT. YONAZI
Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri
Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi amesisitiza ubunifu katika
uendelezaji wa Makao Makuu na Mji
Serikali ili kuweza kuvutia watalii wa ndani na nje.
Dkt. Yonazi ametoa msisitizo
huo wakati wa ziara yake nchini Malaysia alipotembelea Mji Mkuu wa Utawala wa
Malaysia uitwao Putrajaya.
"Ni muhimu wataalam
kuzingatia masuala yanayofanya mji wa Serikali kuwa kivutio kwa wananchi na
watalii kutoka nje. Masuala hayo ni ubunifu katika majengo, utunzaji wa
mazingira na miundombinu na huduma muhimu hasa nyumba za ibada, huduma za fedha
na maeneo ya kupumzika" amesema Dkt. Yonazi.
Aidha, Dkt. Yonazi ameahidi kuendelea kuimarisha
ushirikiano na taasisi za Kimataifa ili kubadilishana uzoefu na kujifuza masuala
ambayo yataongeza tija na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya Ofisi ya
Waziri Mkuu na Serikali kwa ujumla.
Katika ziara hiyo Dkt. Yonazi
ameambata na Balozi wa Tanzania nchini Malaysia Mhe. Dkt. Mahadhi Maalim,
Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Uratibu wa Shughuli za Serikali Bw. Paul
Sangawe, Wataalam kutoka Ubalozi wa Tanzania Nchini Malaysia na kutoka Ofisi ya
Waziri Mkuu.
Tuesday, September 16, 2025
DKT. YONAZI ATANGAZA FURSA ZILIZOPO MAKAO MAKUU YA MJI WA SERIKALI DODOMA NCHINI KOREA.
Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi leo tarehe 16 Septemba, 2025 ameshiriki Mkutano wa Kimataifa wa Uendelezaji Miundombinu unaofanyika Jijini Seoul nchini Korea.
Katika Mkutano huo Dkt. Yonazi
amepata fursa ya kuwasilisha mada kuhusu hatua iliyofikiwa katika zoezi
lakuhamisha Makao Makuu na fursa za uendelezaji wa Jiji la Dodoma pamoja na Mji
wa Serikali.
Aidha, Dkt. Yonazi amekutana
na Mwenyekiti wa KFINCO na taasisi inayoratibu uendelezaji wa Mji wa Serikali
Korea (National Agency For Administrative City Construction of KOREA-NA ACC)
kwa lengo la kuimarisha ushirikiano katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo
pamoja na utekelezaji wa makubaliano ya ushirikiano baina Ofisi ya Waziri Mkuu
(Sera, Bunge na Uratibu) na Taasisi ya NAACC.
Katika mkutano huo, Dkt. Jim
Yonazi ameongozana na Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Uratibu wa Shughuli za
Serikali Bw. Paul Sangawe na wajumbe wengine kutoka Tanzania.
Saturday, September 6, 2025
AFDP YADHAMIRIA KUONGEZA UPATIKANAJI WA MBEGU BORA NCHINI
Ujumbe wa Programu ya
Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kwa kushirikiana na Mfuko wa Kimataifa wa
Maendeleo ya Kilimo (IFAD), umesema utaendelea kuwekeza katika uzalishaji na
upatikanaji wa mbegu bora ili kuongeza tija kwa wakulima nchini.
Kauli hiyo imetolewa na
kiongozi wa ujumbe huo, Bi. Nester Mashingaidze, alipozungumza na wakulima wa
Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro, alipokuwa akikagua utekelezaji wa programu
hiyo inayolenga kuongeza uzalishaji wa mahindi, alizeti, maharage na mimea
jamii ya mikunde.
“Tunalenga kuongeza
upatikanaji wa mbegu bora kwa kushirikiana na taasisi kama TARI, ASA, na TOSCI
ili kuwafikia wakulima wengi zaidi kwa wakati,” alisema Bi. Mashingaidze.
Kwa upande wake, Bw. Salum
Mwinjaka – Mratibu wa Programu hiyo kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, alisema AFDP
inatekelezwa katika mikoa 11 ya Tanzania Bara pamoja na visiwa vya Unguja na
Pemba. Alibainisha kuwa programu inajikita katika kilimo kinachohimili
mabadiliko ya tabianchi, lishe na usawa wa kijinsia.
Naye, Mhandisi Enock Nyanda
kutoka TAMISEMI, alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na wizara za
kisekta kufikisha huduma kwa wananchi kwa ushirikiano na wadau wa maendeleo.
Wakulima waliopokea mafunzo
kutoka kwenye programu hiyo wamesema imewasaidia kuachana na kilimo cha mazoea
na kuhamia kwenye kilimo chenye tija kwa kutumia mbegu bora na za kisasa.
Tuesday, September 2, 2025
WAZALISHAJI WA MBEGU MKALAMA WAOMBA SERIKALI KUIMARISHA UFUNGASHAJI
Wazalishaji wa mbegu za alizeti katika Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama, mkoani Singida, wameiomba Serikali kuongeza juhudi katika kuwawezesha kuandaa vifungashio bora vya mbegu ili kuongeza thamani ya mazao yao sokoni.
Bw. Athumani Ramadhani, mzalishaji wa mbegu aina ya Record, alisema: “Tunaomba Serikali itupe msaada wa kitaalamu kuandaa vifungashio bora vitakavyotangaza mbegu zetu na kuongeza thamani sokoni.”
Naye Bi. Aziza Ramadhani aliongeza kuwa uzalishaji huo umeimarisha ushirikiano wao na taasisi za Serikali kama ASA na TOSCI, zinazopima ubora kabla ya mbegu kuingia sokoni.
Monday, September 1, 2025
DKT. KILABUKO: OFISI YA WAZIRI MKUU ITAENDELEA KUSHIRIKIANA NA IFAD
Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya
Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Dkt. James Kilabuko, amesema Serikali
itaendelea kushirikiana kwa karibu na Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo
(IFAD) katika utekelezaji wa miradi ya kilimo na uvuvi nchini.
Ametoa kauli hiyo Jijini
Dodoma wakati wa kikao na ujumbe wa IFAD waliopo nchini kufuatilia utekelezaji
wa mradi wa programu ya kuendeleza sekta ya Kilimo na uvuvi (AFDP).
“Nawahakikishia kuwa Ofisi ya
Waziri Mkuu ipo tayari kutoa ushirikiano wote unaohitajika ili kuhakikisha
miradi mnayoitekeleza inaleta matokeo chanya,” amesema Dkt. Kilabuko.
Saturday, August 23, 2025
SERIKALI KUGHARAMIA MAZISHI YA WALIOFARIKI KATIKA AJALI YA MGODI NYANDOLWA.
Waziri wa
Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge na Uratibu Mhe. William
Lukuvi, amemfikishia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia
Suluhu Hassan, salamu za pole kufuatia ajali ya kufukiwa kwa mafundi katika
Mgodi wa Dhahabu wa Nyandolwa, iliyotokea tarehe 11 Agosti 2025 katika Mkoa wa
Shinyanga.
Waziri
Lukuvi ameeleza kuwa Serikali imepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za ajali
hiyo, na kwa niaba ya Rais Samia, ametoa pole kwa familia zilizopoteza wapendwa
wao katika tukio hilo la kusikitisha. Aidha, ameeleza kuwa Serikali itagharamia
kikamilifu gharama za mazishi kwa waathirika wa ajali hiyo pamoja na matibabu
kwa waliofikwa na tukio hilo.
Akizungumza
na wanandugu wa marehemu na wale waliokwama mgodini, Mhe. Lukuvi amewatia moyo
na kuwahakikishia kuwa Serikali ipo pamoja nao katika kipindi hiki kigumu.
Ametoa wito kwa timu za uokoaji kuongeza juhudi na kasi ya uokoaji ili kuwaokoa
mafundi waliokwama kwa haraka na usalama zaidi.
“Tunaamini
kuwa kazi kubwa imefanyika lakini bado tunahitaji jitihada zaidi. Serikali
inatambua uzito wa tukio hili na itaendelea kutoa ushirikiano wa karibu kwa
kuhakikisha kila jitihada zinafanyika kwa ufanisi,” amesema Lukuvi.
Kwa upande
wake, Msimamizi wa Mgodi huo, Fikiri, ameiambia Serikali kuwa ndani ya kipindi
cha siku tatu hadi nne zijazo, zoezi la kuwaokoa wahanga waliokwama litakuwa
limekamilika. Ameeleza kuwa vifaa vya kutosha vimeletwa eneo la tukio na
wataalamu wanaendelea na kazi kwa umakini mkubwa kuhakikisha mafanikio ya
haraka.
Kabla ya
kuwasili katika eneo la mgodi, Mhe. Lukuvi alifanya ziara katika Ofisi ya Mkuu
wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita, ambapo alipokea taarifa ya kina kuhusu
maendeleo ya sekta ya madini katika mkoa huo pamoja na hali ya sasa ya shughuli
za uokoaji zinazoendelea katika mgodi wa Nyandolwa.
Akizungumza
kwa niaba ya ndugu wa wanasubiri waliofukiwa na kifusi Bw.Furaha Enock
aliishukuru Serikali kwa namna ilivyoratibu zoezi na inavyowahudumia katika
kipindi chote toka tukio kutokea na kueleza kuwa imefanya jambo la kipekee, la
heshima na la uungwana kuwashika mkono na kuhudumia kwa hali na mali na
kuwasihi wanandugu kuendelea kuwa na utulivu.
"Kipekee
ninaipongeza Serikali Yetu imetufanyia wema na imetupa faraja kwa namna
wanavyoratibu tukio zima, tunakosa neno zaidi ya Asante sana kwa Rais Dkt.
Samia pamoja na uongozo wake wote," alisema Enock
AWALI
Ziara ya
Waziri Lukuvi ni sehemu ya juhudi za Serikali za Uratibu na kutoa maelekezo kwa
karibu katika kipindi hiki cha majonzi, huku ikilenga kuimarisha utendaji wa
shughuli za uokoaji na kuhakikisha haki na heshima kwa waathirika wote wa ajali
hiyo.
Thursday, August 21, 2025
SERIKALI YAENDELEA NA JITIHADA ZA UOKOAJI MGODI WA NYANDOLWA
Imeelezwa kuwa, jitihada za
kuendelea kuokoa maisha baada ya ajali ya mgodi kutokea eneo la Nyandolwa Mkoani
Shinyanga zinaendelea usiku na mchana ambapo hadi kufikia Leo Agosti 21,2025
mafundi 10 kati ya 25 waliokuwa wamekwama chini ya ardhi wameokolewa, huku
wanne wakiwa hai, mmoja kati yao akifariki dunia muda mfupi baada ya kufikishwa
hospitalini, na saba wakikutwa wamefariki dunia.
Hayo yamebainishwa na Mkuu wa
Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita wakati akizungumza na waandishi wa habari Ofisini
kwake Mkoani humo ambapo amethibitisha taarifa hizo na kusema kuwa tukio hilo
lilitokea takribani siku 10 zilizopita, likisababisha shughuli za uokoaji
kuendelea kwa muda mrefu katika mazingira magumu.
Amesema ajali hiyo ilitokea
baada ya ardhi kutitia ghafla na kusababisha kifusi kuporomoka katika mashimo
(maduara) matatu tofauti yaliyokuwa yakikarabatiwa na mafundi ndani ya mgodi
huo, unaomilikiwa na kikundi cha Wachapakazi chini ya leseni ya uchimbaji
mdogo.
"Tunaendelea kushirikiana
na taasisi mbalimbali kuhakikisha mafundi waliobaki wanatolewa salama. Hili ni
tukio la huzuni kubwa kwa mkoa wetu na Taifa kwa ujumla," amesema Mhe.
Mhita.
Kwa upande wake, Naibu Katibu
Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Dkt. James Kilabuko, ametoa
wito kwa timu ya uokoaji kuongeza kasi na juhudi katika shughuli za uokoaji,
akisisitiza kuwa kila sekunde ina maana katika kuokoa maisha ya waliobaki chini
ya kifusi.
“Natoa pongezi kwa kikosi
kizima cha uokoaji kwa moyo wao wa kujitolea, lakini ni muhimu sasa kuongeza
kasi bila kuhatarisha usalama wa waokoaji wenyewe,” amesema Dkt. Kilabuko.
Naye, Mwenyekiti wa Tume ya
Madini, Dkt. Janet Lekashingo, amefika eneo la tukio na kutoa salamu za pole
kwa familia za marehemu na wote walioathirika na ajali hiyo. Ametoa rai kwa
waokoaji kuendelea kuwa na umakini mkubwa na kutanguliza usalama katika
operesheni ya uokoaji.
“Hii ni ajali ya kusikitisha
mno. Tume ya Madini inatoa pole kwa familia za wahanga, na tutaendelea
kufuatilia kwa karibu kuhakikisha taratibu zote za usalama katika migodi
zinasimamiwa ipasavyo ili kuepusha ajali kama hizi siku za usoni,” amesema Dkt.
Lekashingo.
Aliongezea kuwa, Timu za
uokoaji zinajumuisha maafisa kutoka Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Polisi, Tume
ya Madini, Wizara ya Madini, wachimbaji wenzao, Mgodi wa Barrick Bulyanhulu,
Serikali ya Mkoa na Wilaya ya Shinyanga, ambao wote wanaendelea kushirikiana
kuhakikisha mafundi waliobaki wanatolewa salama.
Hadi sasa, juhudi za uokoaji
bado zinaendelea katika eneo hilo la mgodi, huku matumaini yakiwa bado
hayajapotea kwa familia na ndugu wa mafundi waliobaki chini ya kifusi. Serikali
imeahidi kutoa usaidizi wa karibu kwa waathirika na kuhakikisha uchunguzi wa
kina unafanyika kubaini chanzo cha ajali hiyo.
SERIKALI YA ZAMBIA YAPATA MAFUNZO KUTOKA TANZANIA: YAPONGEZA UJENZI WA MJI WA SERIKALI DODOMA
Maofisa waandamizi kutoka
Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ya Zambia wametembelea Mji wa
Serikali Mtumba, jijini Dodoma, kwa lengo la kujifunza namna Tanzania
ilivyofanikiwa kutekeleza mradi mkubwa wa kitaifa wa kuhamishia shughuli za
serikali katika mji huo.
Wakiwa katika ziara hiyo,
maofisa hao walipokelewa na Mratibu wa Ujenzi wa Mji wa Serikali, Bw. Noel
Mlindwa, ambaye alieleza kuwa Tanzania imeweka historia kwa kuanzisha na
kutekeleza kwa mafanikio makubwa ujenzi wa mji wa serikali, chini ya uongozi wa
Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.
Bw. Mlindwa alifafanua kuwa
mji huo umejengwa kwa kuzingatia mipango bora ya kisasa, usimamizi makini wa
rasilimali na matumizi ya teknolojia, hali iliyowavutia wageni hao kutoka
Zambia.
Kwa upande wao, maofisa wa
Zambia waliipongeza Serikali ya Tanzania kwa hatua kubwa ilizopiga na
walisisitiza kuwa Mji wa Serikali Dodoma si tu ni kielelezo cha maendeleo, bali
pia ni kivutio cha kiutalii na mfano wa kuigwa kwa mataifa mengine barani
Afrika.
Saturday, August 16, 2025
UZINDUZI WA MFUMO WA ANUANI ZA MAKAZI ZANZIBAR WAFANA
Naibu Waziri wa Ofisi ya
Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Mhe. Ummy Nderiananga, ameshiriki katika
hafla ya uzinduzi wa mfumo wa anuani za makazi, unaolenga kutoa huduma ya barua
ya utambulisho wa mkazi kwa njia ya kidijitali.
Uzinduzi huo umefanyika leo
katika Mkoa wa Mjini Magharibi, Zanzibar, ukiongozwa na Mgeni Rasmi, Makamu wa
Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla.
Akizungumza katika hafla hiyo,
Mhe. Ummy amepongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia
Suluhu Hassan, pamoja na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,
Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, kwa jitihada zao za kuimarisha huduma za kijamii
kupitia mifumo ya kidijitali.
"Niwapongeze kwa
kuendelea kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi kwa urahisi zaidi kupitia
teknolojia. Mfumo huu utarahisisha utambuzi wa makazi na uboreshaji wa utoaji
wa huduma mbalimbali serikalini," alisema Mhe. Ummy.
Aidha, amezipongeza wizara
zote za kisekta kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa ushirikiano wao uliowezesha utekelezaji wa mfumo
huo muhimu kwa maendeleo ya Taifa.
Thursday, August 14, 2025
MAKATIBU WAKUU WATETA MIKAKATI YA KUENDELEZA SAFARI CHANNEL YA TBC
Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya
Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Dkt. James Kilabuko, ameongoza kikao cha
Makatibu Wakuu wa Wizara mbalimbali kilichofanyika leo jijini Dodoma kwa lengo
la kujadili namna bora ya kuimarisha uendeshaji wa Tanzania Safari Channel
chini ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC).
Akizungumza katika kikao
hicho, Dkt. Kilabuko amesema chaneli hiyo imekuwa nyenzo muhimu ya kuitangaza
Tanzania kimataifa kupitia vivutio vya utalii vilivyopo nchini, hivyo ni muhimu
kwa taasisi zote za serikali kushirikiana katika kuiendeleza.
Kwa upande wake, Mkurugenzi
Mkuu wa TBC, Dkt. Ayub Rioba Chacha, akiwasilisha taarifa kuhusu chaneli hiyo,
ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu
Hassan kwa kusaini sheria mpya ya TBC, ambayo imefungua milango ya maboresho ya
kiutendaji na kuimarisha utoaji wa huduma kwa umma.
Chaneli ya Tanzania Safari
Channel imekuwa chombo mahsusi cha kuitangaza Tanzania kama nchi yenye vivutio
vya kipekee duniani, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kimkakati kukuza sekta ya
utalii.
Tuesday, August 12, 2025
ZANZIBAR YACHOTA UZOEFU DODOMA: YAJIANDAA KUJENGA MJI WA SERIKALI KISAKASAKA
Kamati ya wataalamu kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Ikiingozwa na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar Dkt. Islam Seif Salum imetembelea miradi mikubwa jijini Dodoma ikiwemo Mji wa Serikali Mtumba na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Msalato, kujifunza utekelezaji wa Ujenzi wa Mji wa Serikali.
Ziara hiyo inalenga kuandaa
mazingira ya ujenzi wa ofisi za Serikali na Baraza la Wawakilishi eneo la
Kisakasaka, Zanzibar.
Viongozi hao wamempongeza Rais
Dkt. Samia kwa kuimarisha maendeleo ya Makao Makuu ya Nchi kupitia miradi ya
kimkakati.
Monday, August 4, 2025
HELEN KELLER INTERNATIONAL KUSHIRIKIANA NA OFISI YA WAZIRI MKUU KUIMARISHA URATIBU WA LISHE NCHINI
Kaimu Katibu Mkuu wa Ofisi ya
Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Bi. Stella Mwaisaga, amekutana na kufanya
mazungumzo na Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Kimataifa la Helen Keller
International, Bw. William “Bill” Toppeta.
Mazungumzo hayo yalilenga
kuimarisha ushirikiano baina ya Serikali ya Tanzania na shirika hilo katika
utekelezaji wa masuala ya lishe, ambapo Bw. Toppeta aliipongeza Serikali kwa
juhudi kubwa katika kusimamia na kuratibu lishe, huku akisisitiza dhamira ya
Helen Keller International kuendelea kushirikiana na Serikali katika
kuhakikisha jamii inapata huduma bora za lishe.
“Tunaishukuru Serikali ya
Tanzania kwa usimamizi wake imara katika masuala ya lishe. Tutaendelea kuwa
wadau wa karibu katika kusaidia juhudi hizi muhimu kwa afya ya wananchi,”
alisema Bw. Toppeta.
Ujumbe huo wa Helen Keller International upo nchini kwa
ziara ya kukagua na kutathmini utekelezaji wa miradi ya shirika hilo, hususan
katika sekta ya lishe, ambapo Ofisi ya Waziri Mkuu ni mratibu mkuu wa kitaifa
wa masuala hayo.
Wednesday, July 30, 2025
SERIKALI KUWEKEZA KATIKA UVUVI WA BAHARI KUU
Mkurugenzi wa Uratibu wa
Shughuli za Serikali kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Paul Sangawe ameongoza
Kikao cha Kamati ya Wataalamu kuhusu matokeo ya tathmini ya kazi ya tafiti juu
ya kampuni zenye uwezo wa kujenga Meli kwa ajili ya Uvuvi katika Bahari Kuu.
Katika Kikao hicho, Bw.
Sangawe alilisitiza juu ya utekelezaji wa maelekezo ya Kikao cha Kamati ya
Usimamizi wa Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi kilichofanyika kabla ya
kikao cha wataalam. Masuala yaliyosisitizwa ni pamoja na upatikanaji kampuni
yenye uwezo wa kujenga Meli ya Uvuvi wa Bahari Kuu kwa viwango vinavyohitajika,
na kupata meli hizo kwa wakati ili kuchochea uvuvi wa kisasa nchini.
Vikao hivyo vya Programu ya
Kuendeleza Kilimo na Uvuvi ( AFDP) vimefanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa
Wizara ya Uvuvi na Uchumi wa Bluu, Zanziba
Monday, July 28, 2025
JITIHADA ZA PAMOJA ZINAHITAJIKA KUPAMBANA NA UDUMAVU – DKT. YONAZI
Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu),
Dkt. Jim Yonazi, ametoa wito kwa Serikali na wadau kushirikiana kwa karibu
katika mapambano dhidi ya tatizo la udumavu nchini.
Akizungumza katika kikao cha maandalizi ya Mkutano Mkuu wa 11
wa Wadau wa Lishe nchini, kinachotarajiwa kufanyika Septemba 4–5, 2025 jijini
Dar es Salaam, Dkt. Yonazi amesema juhudi za pamoja, tafiti, elimu na majukwaa
ya kitaifa ni muhimu katika kutokomeza udumavu.
“Tunahitaji nguvu ya pamoja kati ya Serikali na wadau kuhakikisha
tunapunguza kwa kiasi kikubwa viwango vya udumavu kupitia sera, elimu na
programu zenye tija,” amesema Dkt. Yonazi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Chakula na
Lishe Tanzania (TFNC), Dkt. Germana Leyna, amesema mkutano wa mwaka huu
utaambatana na Lishe Marathon, yenye lengo la kuhamasisha afya bora kwa jamii
na kuongeza uelewa wa masuala ya lishe.
Mkutano huo wa kitaifa unatarajiwa kufunguliwa rasmi na
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa.
Wednesday, July 23, 2025
KAMATI YA MAKATIBU WAKUU YARIDHISHWA NA UJENZI WA UWANJA MPYA WA MPIRA JIJINI ARUSHA
Kamati ya Makatibu Wakuu
inayoongozwa na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu),
Dkt. Jim Yonazi, imekagua na kuridhishwa na maendeleo ya ujenzi wa uwanja mpya
wa kisasa wa mpira wa miguu katika eneo la Olmoti, jijini Arusha. Uwanja huo
unatarajiwa kuwa miongoni mwa viwanja vitakavyotumika kwenye mashindano ya
AFCON 2027.
Dkt. Yonazi amesema maendeleo
ya mradi huo ni ya kuridhisha na uwanja huo utakuwa si tu kituo cha michezo,
bali pia kivutio cha utalii na maendeleo ya uchumi kwa wakazi wa Arusha.
“Tunaamini uwanja huu utakuwa
fursa kwa wananchi kuwekeza kibiashara. Ujenzi huu unapaswa kutazamwa kama
chachu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi,” amesema Dkt. Yonazi.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu
wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa, ametoa
shukrani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu
Hassan, kwa uwekezaji mkubwa katika miundombinu ya michezo.
Naye Rais wa TFF, Wallace
Karia, amesema uwanja huo utaongeza idadi ya matukio ya kimataifa nchini,
Kutakuza vipaji vya ndani, na kuitangaza Tanzania kimataifa kupitia michezo.
Ujenzi wa uwanja huo ni sehemu
ya maandalizi ya Tanzania kuandaa mashindano ya AFCON 2027, kwa ushirikiano na
Kenya na Uganda
WAZIRI LUKUVI AWAPONGEZA MALIASILI KWA KUTEKELEZA MAONO YA MHE. RAIS SAMIA
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri
Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Mhe. William Lukuvi ameipongeza Wizara ya Maliasili
na Utalii kwa kutekeleza kikamilifu maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuwa Wizara ya kwanza kukamilisha
ujenzi wa jengo la Ofisi na kuwezesha Idara na Vitengo vyake kuhamia Mji wa
Serikali Mtumba, Dodoma.
Waziri Likuvi ametoa pongezi
hizo leo alipotembelea Wizara hiyo kwa lengo la kukagua ujenzi wa Majengo ya
Serikali ambao ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu ya Serikali kuhamia Dodoma.
Mhe. Lukuvi amesema kuwa
Wizara ya Maliasili na Utalii licha ya kukamilisha mapema ujenzi wa jengo hilo,
inastahili pia kupongezwa kuwa wa kwanza kuhamia na kuwa mfano katika Matumizi
ya samani za Ofisini zilizozalishwa hapa nchini kupitia mazao ya Misitu.
"Ninyi ni mabalozi wazuri
wa Matumizi ya bidhaa zetu za hapa nchini zinazotokana na Misitu yetu, niimani
yangu kuwa Wizara zote zitaiga mfano huu". Aliongeza Mhe. Lukuvi
Aidha Mhe. Lukuvi ametoa rai
kwa watumishi wa Wizara hiyo kuhakikisha wanatunza vyema miundombinu na vifaa
vilivyopo ili viweze kudumu kama ilivyo kusudiwa.
Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya
Maliasili na Utalii Dkt. Hassan Abbasi amemshukuru Waziri Lukuvi kwa ziara
yake, na kuahidi kuwa Wizara itatekeleza vyema maelekezo aliyoyatoa hususani ya
usimamizi mzuri wa Matumizi ya jengo na vifaa vilivyopo.
Tuesday, July 22, 2025
MIUNDOMBINU YA MICHEZO ZANZIBAR YAVUKA KIWANGO CHA KIMATAIFA KUELEKEA CHAN
Serikali imeridhishwa na
maandalizi ya miundombinu ya michezo Zanzibar kuelekea Mashindano ya Mataifa ya
Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN), huku Uwanja wa Amaan Complex ukitajwa
kuwa katika viwango vya kimataifa.
Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu
wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Dkt. Jim Yonazi, mara baada
ya kuongoza Kamati ya Makatibu Wakuu kukagua maandalizi ya CHAN katika visiwa
vya Zanzibar.
“Tumejionea hali halisi ya miundombinu, hasa
Uwanja wa Amaan. Uko katika viwango vya kimataifa, na tunaamini Zanzibar ipo
tayari kuwa sehemu ya mashindano haya muhimu kwa bara letu la Afrika,” amesema
Dkt. Yonazi.
Aidha, Dkt. Yonazi alieleza
kuwa hatua hiyo inaonesha utayari wa Taifa kuandaa mashindano ya kimataifa,
huku akisisitiza kuwa mashindano ya CHAN ni fursa kubwa ya kuimarisha michezo
na kukuza uchumi wa ndani.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu
Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo (SMZ), Mhe. Fatma Hamad Rajab,
alieleza kuwa Uwanja wa Aman Complex tayari umekidhi vigezo vyote vinavyohitajika
na Zanzibar iko tayari kuwapokea wachezaji, mashabiki na wageni kutoka mataifa
mbalimbali.
Kamati hiyo ya Makatibu Wakuu
inafanya ziara katika mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara na Visiwani ili kukagua
maandalizi ya CHAN na AFCON 2027.
Mashindano ya CHAN
yanatarajiwa kuanza rasmi tarehe 2 Agosti 2025 yakihusisha wachezaji wanaocheza
ligi za ndani kutoka mataifa mbalimbali barani Afrika.
Monday, July 21, 2025
TANZANIA YATANGAZA UTAYARI WA KUANDAA MASHINDANO YA CHAN
Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Dkt. Jim Yonazi, amesema kuwa Tanzania ipo tayari kwa ajili ya kuandaa Mashindano ya Mataifa ya Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN), yatakayoanza rasmi Agosti 2, 2025.
Akizungumza mara baada ya
ziara ya ukaguzi wa miundombinu ya michezo jijini Dar es Salaam, Dkt. Yonazi
alisema maandalizi yamefikia hatua nzuri na viwanja viko tayari kwa mashindano
hayo makubwa.
Akiwa Mwenyekiti wa Kamati ya
Makatibu Wakuu ya CHAN na AFCON, Dkt. Yonazi alitembelea viwanja vya Benjamin
Mkapa, Isamuhyo, Shule ya Sheria na Gymkhana, akisisitiza kuwa Serikali
imejipanga kuhakikisha miundombinu yote inakidhi viwango vya kimataifa.
Katibu Mkuu wa Wizara ya
Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Bw. Gerson Msigwa, ametoa wito kwa
Watanzania kuonesha uzalendo kwa kujitokeza kwa wingi viwanjani kuishangilia
Taifa Stars.
#CHAN2025 #TaifaStars #TanzaniaYapoTayari
Friday, July 18, 2025
DKT. YONAZI AIPONGEZA OFISI YA WAZIRI MKUU MAONESHO SABASABA
Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri
Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi amewapongeza
watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu kwa jitihada kubwa wanazozifanya katika
utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku kwa maendeleo ya Taifa.
Dkt. Yonazi ameyasema hayo leo
Ofisini kwake jijini Dodoma akikabidhiwa tuzo na Mkurugenzi wa Idara ya
Uwezeshaji Kiuchumi na Maendeleo ya Sekta Binafsi Bw. Conrad Milinga
iliyotolewa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt.
Hussein Ali Mwinyi wakati akifungua Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya
Dar es Salaam Sabasaba 2025.
Alisema Ofisi ya Waziri Mkuu
kupokea tuzo kumeongeza motisha katika ushiriki wa maonesho yajayo makubwa ya
Kimataifa ya Sabasaba na kutambua mchango wa Ofisi hiyo iliyoutoa kwa wananchi
katika kipindi chote cha maonesho hayo na kutambua huduma ianayotolewa kwa
wananchi.
“Ofisi ya Waziri Mkuu
imefurahi sana kupokea tuzo hii kama ishara ya kutambua ushiriki wetu na
mchango ambao Ofisi yetu inatoa kwa wananchi hivyo tunaamini ushiriki wetu
unaofuata utakuwa wa viwango vya juu sana,” Alisema Dkt. Yonazi.
Pia aliishukuru Serikali kwa
juhudi kubwa inazofanya chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.
Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania
(TanTrade) ambayo ndio mratibu wa Maonesho kwa
kuhakikisha maonesho hayo yanaleta tija na mageuzi makubwa katika sekta
ya kiuchumi kwa wananchi na Kimataifa.
“Tunazishukuru sana Taasisi
mbalimbali ambazo tumeshirikiana nazo na viongozi ambao wameendelea kutupa
maelekezo yaliyowezesha kufanya vizuri katika maonesho hayo na tunaamini kwamba
tutaendelea kuwa washindi au hata washindi wa jumla,”Alishukuru.
Ikumbukwe Maonesho ya 49 ya
Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam Sabasaba 2025 yalifunguliwa na Rais wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi
tarehe 07 Julai, 2025 na kufungwa na Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa katika viwanja vya maonesho
Sabasaba jijini Dar es Salaam Julai 13, 2025.
"KILA SEKTA IJIANDAE KUPOKEA WAGENI KUELEKEA CHAN", DKT. YONAZI
Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri
Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi
amezitaka sekta zote kujianda kupokea wageni mbalimbali kuelekea Mashindano ya
Mataifa ya Afrika (CHAN) yanatayorajiwa kuanza Mwanzoni mwa mwezi wa Agosti 2025.
Dkt. Yonazi ametoa rai hiyo
wakati akiongoza Kikao cha Makatibu Wakuu cha Tathmini ya Maandalizi ya CHAN na
AFCON kilichofanyika leo katika Ukumbi
wa Ofisi ya Waziri Mkuu Jijini Dodoma.
Aidha, ameeleza kuwa jukumu la
Serikali ni kuleta fursa na kuweka miundombinu ili kila sekta inufaike na ugeni
huu mkubwa na kusisitiza hii ni fursa ya kutuamsha katika kuandaa matukio
makubwa.
Pia, Dkt. Yonazi amesisitiza
umuhimu wa kutoa hamasa kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
ili kila mtanzania aamasike na kushiriki katika mashindano haya ya CHAN.
Ikumbukwe Mashindano ya CHAN
yanatarajiwa kutimua vumbi kuanzia Agosti 2, 2025 ambapo timu ya Taifa ya
Tanzania (Taifa Stars) itachuana na Timu ya Taifa ya Burkina Faso katika Uwanja
wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.
MITANDAO YA KIJAMII
Popular Posts
-
Na. OWM, Dodoma. Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu, imefanya ukaguzi wa utekelezaji wa sheria Na.5 y...
-
Wataalamu wa Afya moja wakiwa katikapicha ya pamoja wakati wa mkutano wa wataalamu wa Afya moja uliojikita katika ulinzi na usalama...
-
Na. OWM, ARUSHA Wataalam wa sheria kutoka katika sekta ya Afya ya binadamu, Afya ya wanyamapori na mifugo pamoja na mazingira wameshauri...
-
Washiriki wa Mkutano wa mwaka wa Wataalamu wa Maabara wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa mkutano wa mwaka kwa wataalam wa maabara w...
-
TAMOBA wafanya wasilisho la mfumo maalum wa kielektroniki wa ulinzi na usalama wa Bodaboda na BajajiKampuni ya Tanzania Motorcycle and Bajaj Association (TAMOBA) imefanya wasilisho maaluum kwa Ofisi ya Waziri Mkuu kuhusu mfumo maalum wa ...