Thursday, December 6, 2018

WAZIRI MKUU AFUNGUA KIWANJA CHA TAIFA CHA MCHEZO WA BASEBALL


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amefungua kiwanja kipya cha Taifa cha mchezo wa Baseball na kuzindua mashindano ya Taifa ya Baseball nchini.
Amewaagiza viongozi wa Wizara ya Habari, Sanaa, Michezo na Utamaduni na Ofisi ya Rais-TAMISEMI waone umuhimu wa kuuendeleza mchezo huo.
Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Alhamisi, Desemba 6, 2018) alipofungua kiwanja cha Baseball katika shule ya Sekondari ya Azania, jijini Dar es Salaam.
Amesema iwapo mchezo huo utaratibiwa vizuri na kuingizwa katika michezo  UMISETA na UMITASHUMTA utaleta tija kwa wanafunzi wanaoucheza nchini.
Waziri Mkuu amesema thamani ya uwanja huo ni takribani Dola za Kimarekani 80.234 ambazo zimetolewa kwa msaada kutoka Serikali ya Japani.
Amesema anaishukuru Serikali ya Japan na amefarijika kwa dhamira yao ya kuunga mkono utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi CCM 2015-2020 hususan ibara ya 161.
Waziri Mkuu amesema ilani inaielekeza Serikali kujenga na kuimarisha miundombinu ya michezo nchini na kuifanya sekta ya michezo kutoa ajira hususan kwa vijana.
“Pia naishukuru Osaka Rotary Club ya nchini Japan kwa msaada wao wa dola za Kimarekani 12,856 kwa kufadhili mashindano hayo ya sita ya mchezo wa Baseball.”
Amesema jitihada hizo zitaufanya mchezo wa baseball kuwa ni mmoja wa mchezo huo kukua kwa kasi na unachezwa kuanzia ngazi za shule ya msingi na sekondari.
“Nina hakika baada ya hapo Tanzania itaweza kushiriki kwenye mashindano ya kitaifa na kimaifaifa na hasa yale ya Olimpiki ya Tokyo Japan 2020.
Kadhalika, Waziri Mkuu ameagiza uwanja huo ulindwe na utunzwe ipasavyo ili utumike katika mashindano ya ndani na nje ili uwe sehemu ya kuitangaza nchi.
Awali, Balozi wa Japan nchini, Balozi Shinichi Goto alisema nchini Japan mchezo huo pia unasaidia katika kuwajenga vijana kukua kinidhamu na kujiamini.
Alisema anatarajia kwamba mashindano ya mchezo huo yatakuwa endelevu nchini na wachezaji watacheza vizuri kutokana na uwepo wa uwanja mzuri.
Balozi huyo alisema mchezo huo unafundishwa na walimu wa Kijapani katika mikoa mbalimbali Tanzania Bara na Zanzibar.


 (mwisho)


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.