Sunday, May 9, 2021

Waziri Mhgama aridhishwa na utendaji wa NSSF

 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Utatibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama amepongeza kazi inayofanywa na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii wa NSSF kwa kuhakikisha wanahudumia wateja kwa weledi na ufanisi katika kufikia malengo yaliyopo.

 

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa NSSF mapema hii leo Mei 9, 2021 mkoani Morogoro waziri alionesha kufurahishwa na mwenendo wa mfuko ikiwa ni pamoja na matumizi mazuri ya fedha na kupata hati safi ya ukaguzi.

 

Waziri alieleza uwepo wa mafaniko hayo yanaenda sambamba na uwepo wa mabaraza ya wafanyakazi sehemu za kazi hivyo yaendelee kutumika kwa uhumimu wake ili kuimarisha umoja na mshikamano katika utendaji kazi wa kila siku.

 

“Mabaraza ya Wafanyakazi ni vyombo vya ushauri na usimamizi yana wajibu wa kuhakikisha kuwa Waajiri na Watumishi wanatambua wajibu na haki zao, wanazingatia maadili ya utumishi wao ili kuleta matokeo ya utendaji kazi yenye tija, staha na upendo, hivyo tuyatumie kwa tija”. Alisema Waziri Mhagama.

 

Waziri alitumia fursa hiyo kuwakumbusha watumishi wote wa mfuko huo kuendelea kuchapa kazi kwa juhudi na kutimiza wajibu kwa kila mmoja katika eneo lake la kazi.

 

“Ni muhimu wa kila Mtumishi kuonesha juhudi za utendaji kazi kwa kufuata kanuni za maadili ya utendaji kazi katika Utumishi wa Umma za Mwaka 2005. Kanuni hizi zikifuatwa kwa ukamilifu Watumishi watatoa huduma bora na stahiki kwa Wanachama ambao ndiyo waajiri wetu”.Alisisitiza

 

Aidha aliendelea kuwaasa Mameneja wa Mikoa, Wakuu wa Idara na Vitengo wasimamie kwa dhati suala la maadili katika sehemu zao za kazi na kuendelea   kutumia muda wa kazi kuhudumia wanachama kwa kujibu hoja zao na kutatua kero zao kwa haraka na kwa ufanisi.

 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Masha Mshomba alishukuru na kumhaidi Waziri kuyatendea kazi maelekezo yake na kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi na kuhakiksha malengo yanafikiwa.

 

“Nitafanya kazi kwa jududi na maarifa kwa kushirikiana na watumishi wote ili kukidhi mahitaji ya wanachama na nchi kwa ujumla”Alisema Mshomba.

Aliahidi kuendelea kuboresha huduma kwa kuhakikisha mifumo inakaa vizuri na kuhakikisha kazi zinakwenda vizuri na kukomboa wakati huku wakifanya kazi kwa umoja.

 

AWALI

Mkutano wa 47 wa Baraza la Wafanyakazi wa NSSF ulilenga kupitia Taarifa ya utekelezaji wa bajeti ya Mfuko kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020; kujadili na kupitisha Mpango wa Mfuko wa Mwaka 2021/2022; na kujadili na kupitisha Bajeti ya Mfuko kwa mwaka 2021/2022.Aidha ulitoa fursa kujadili masuala mbalimbali yanayohusu Taasisi hiyo ili kuendelea kuwa na tija nchini.

 

=MWISHO=

 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu, Kazi, Vijana,Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama pamoja na meza kuu wakiimba wimbo wa umoja na mshikamano wakati wa mkutano huo.
 Baadhi ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la NSSF wakiimba wimbo wa umoja na         mshikamano kabla ya ufunguzi wa baraza hilo.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu, Kazi, Vijana,Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama akihutubia wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa 47 wa Baraza la Wafanyakazi la NSSF lililofanyika Mkoani Morogoro Mei 9, 2021.

Mkurugenzi Mkuu NSSF Bw.Masha Mshomba  ahutubia na kueleza utekelezaji wa ofisi yake kabla ya ufunguzi wa mkutano wa Baraza la Wafanyakazi la NSSF lililofanyika Mkoani Morogoro.

Baadhi ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la NSSF wakifuatili kikao hicho.

Meneja Uhusiano na Elimu kwa Umma NSSF Bi. Lulu Mengele akiongoza mkutano wa baraza la wafanyakazi wa ofisi hiyo uliofanyika hii leo Mei 9, 2021 Mkoani Morogoro.
Baadhi ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la NSSF wakifuatili kikao hicho.



EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.