Friday, September 22, 2023

NAIBU WAZIRI NDERIANANGA: ENDELEENI KUZINGATIA UBORA KATIKA UZALISHAJI WA MBEGU

 


Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Ummy Nderiananga ameupongeza uongozi wa Wakala wa Taifa wa Uzalishaji na Uendelezaji wa mbegu za kilimo (ASA) kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuzalisha na uendelezaji wa mbegu nchini huku akiwasihi kuendelea kuzingatia ubora na weledi katika majukumu ya kuzalisha mbegu bora hizo ili kuendelea kuwa na uhakika wa chakula cha kutosha nchini. 

Ametoa pongezi hizo wakati wa ziara yake ya kikazi kufuatili shughuli za utekelezaji wa Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo na Uvuvi ya AFDP ambayo inaratibiwa na ofisi yake na kutekeleza katika mikoa mbalimbali nchini ikiwemo Morogoro.

Akiwa katika ziara hiyo alitembelea Kituo cha Kuendeleza Ukuzaji Viumbe Maji Kingolwira, Wakala wa Taifa wa Uzalishaji na Uendelezaji wa mbegu za kilimo (ASA) Pamoja na Taasisi ya Kuthibiti Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI) zilizopo Mkoani Morogoro.

Mhe.Ummy amesema upo umuhimu wa kuendelea kuunga mkono Programu ya kuendeleza sekta ya Kilimo na Uvuvi nchini kwa kuzingatia inaongeza tija hasa katika kuhakikisha kunakuwa na mbegu bora nchini. 

“Ofisi ya Waziri Mkuu tunaendelea kufanya uratibu na kutathmini ya programu hii ambayo ni ya miaka sita hivyo endeleeni kufanya kazi vizuri, kwa weledi huku mkiunga jitihada za Mhe Rais za kuona Tanzania inakuwa ghala kubwa la chakula, Serikali haita waacha nyumba, inaendelea kuunga mkono jitihada hizi.” alisema Mhe. Nderiananga

Aidha aliwataka kuendelea kuzingatia ubora na viwango katika utekelezaji wa majukumu ya uzalishaji wa mbegu bora na zinazoendana na mahitaji halisi.

 “Eneo la mbegu ni muhimu sana, bila kuwa na mbegu nzuri hatuwezi kuwa na matokeo ya chakula kizuri, hivyo ninawapongeza mnafanya kazi nzuri endeleeni maana tunategemea sana sekta yetu ya kilimo ili kuendelea kuwa na uhakika wa chakula nchini,”alisisitiza.

Kwa upande wake Mchumi Mwandamizi kutoka wa Wakala wa Taifa wa Uzalishaji na Uendelezaji wa Mbegu za Kilimo (ASA) Bw. Edmund Kayombo akizungumza kuhusu wakala hiyo amesema umeendelea kutoka huduma za kuongeza uzalishjaji na usambazanji mbegu bora, kuhamasisha sekta binafsi kushiriki katika uzalishaji na usambazaji wa mbegu bora, kuhamasisha wakulima kutumia mbegu bora na kushirikiana na kituo cha utafiti ili kuhakikisha mbegu mpya zinazaliwashwa na kusambazwa kwa wakulima.

“Wakala wa Mbegu za kilimo una jumla ya mashamba 14 ikiwemo mashamba ya kilimi yaliyopo Nzenga, Msungula (Kasulu), Chalinze, Nane nane - Morogoro, Tanganyika, Dabaga kilosa, Arusha (Tengelu), Namtumbo (Songera), Njombe, ambayo yanajumla ya ukubwa wa hekta 16,909,” alisema Kayombo.


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.