Friday, October 6, 2023

IDARA YA MENEJIMENTI YA MAAFA NCHINI YASHIRIKISHA UJUZI KWA WANAFUNZI NA WAKUFUNZI KUTOKA MALAWI


 

Idara ya Menejimenti ya Maafa Nchini yashirikisha ujuzi wa masuala ya usimamizi wa maafa kwa wanafunzi na wakufunzi kutoka Chuo cha Ukamanda na Unadhimu Jeshi la Ulinzi la Malawi walifanya ziara yao ya mafunzo nchini Tanzania.

 Akizungumza wakati wa kikao kilifanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Waziri Mkuu Jijini Dar es salaam kilicholenga kubadilishana uzoefu katika usimamizi wa maafa kati ya wataalam wa Ofisi ya Waziri Mkuu na ujumbe wa wanafunzi na wakufunzi kutoka chuo hicho, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Luteni Kanali Selestine Masalamado amesema mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo na kubadilishana uzoefu katika masuala ya usimamizi wa maafa na kueleza kuwa ujio wao ni moja ya ishara kuwa nchi hizo mbili zimeendelea kuwa na mahusiano mazuri na kupongeza hatua hiyo.

 “Hatua hii ya kukutana pamoja na kupeana uzoefu imetufariji na inaimarisha umoja baina yetu, hivyo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaendelea kuimarisha mahusiano yaliyopo na Serikali ya Jamhuri ya Malawi katika masuala ya menejimenti ya maafa kwa kuhakikisha tunatumia fursa zilizopo katika kuyafikia malengo hayo,”alisema Kanali Masalamado.

Aidha alitumia fursa hiyo kuwaeleza kuwa, Tanzania imeendelea kuimarisha mifumo ya kiutendaji katika kukabiliana na maafa huku akisema uwepo wa Teknolojia ya TEHAMA umeendelea kurahisisha masuala ya usimamizi wa maafa nchini hasa upande wa mawasilisno wakati wa dharura kwa kuanzishwa kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharula katika Ofisi ya Waziri Mkuu ambacho kimerahisisha mawasiliano kwa ajili ya upatikanaji wa taarifa za maafa nchini.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo cha Ukamanda na Unadhimu Jeshi la Ulinzi la Malawi na kiongozi wa msafara huo kutoka chuo hicho, Brigedia Jen. Luke Mwetseni amepongeza namna nchi ya Tanzania inavyoendelea na masuala ya menejimenti ya maafa huku akishukuru namna Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilivyowasaidia wakati wa maafa ya Kimbunga Freddy kilichotokea Machi, 2023 ambapo Tanzania ilitoa misaada mbalimbali ikiwemo ya kibinadamu na fedha kwa Taifa hilo.

“Serikali ya Tanzania ilitushika mkono wakati wa maafa ya Kimbunga Freddy kwa kutupatia Mablanketi, madawa ya binadamu, fedha pamoja na ndege kutoka jeshi la Wananchi wa Tanzania zilizosafiri kuja Malawi kwa lengo la wokozi, tunashukuru sana kwa namna mlivyojali, hii inaonesha namna mlivyojipanga katika masuala ya menejimenti ya maafa hongereni sana,” alisema Brig Jen. Mwetseni

Aidha alimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake makini katika masuala ya Menejimenti ya maafa na kusema kuwa wanaitumia Tanzania kama nchi ya mfano kuja kujifunza kwa vitendo namna inavyoratibu masuala ya maafa ili kuendelea kuwa na jamii stahimilivu katika maafa.

“Kwa kutambua mchango wenu tumekuja na tuzo hii maalum kwa ajili ya kuonesha kuwa tulitambua na kujali Serikali yenu ilivyotutendea sisi watu wa Malawi wakati wa maafa, tunaahidi kuendelea kushirikiana katika kuimarisha umoja huo,” alisisitiza Brigedia Jen. Mwetseni.

Awali alisema kuwa, ujio wao nchini unatija kubwa na utasaidia wanafunzi hao kuongeza ujezi utakao wasaidia wanapoelekea kumaliza mafunzo katika chuo hicho pamoja na kuwaongezea maarifa katika utendaji kazi wao.

 


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.