Wednesday, October 11, 2023

WAZIRI MHAGAMA, AZINDUA MUONGOZO WA UWEKEZAJI MKOA WA MANYARA.


 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama ametoa wito kwa watendaji wa Serikali; kujipanga na kuhakikisha Muongozo wa uwekezaji kwa Mkoa Manyara unawafikia wananchi wote ili kufanya kazi kwa tija.

Kauli hiyo ameitoa Mkoani Manyara wakati wa Ufunguzi wa wiki ya Kitaifa ya Vijana tukio alilolifanya kwa niaba ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa.

“Tunataka Muongozo huu uweze kutoa fursa nyingi kwa vijana ili uweze kujenga kizazi ambacho kitatatumia Muongozo huu kwa muda mrefu” alieleza.

Aliendelea kusema kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu italeta timu ya baraza la uwezeshaji kiuchumi, timu ambayo itasaidia kujenga uwezo kwenye dhana kutengeneza vitu asilia (Local content) ili kuongeza tija na kuweka mazingira wezeshi yatakayochochea wanawekezaji.

“Makapuni yaliyowekeza katika Mkoa wa Manyara yaone namna ya kutumia fedha zile zinazorudi kwa jamii, kwa kuwekeza katika vikundi vya vijana wabunifu ili kupitia muongozo wa uwekezaji usaidie kuleta tija kwa vijana na maendeleo ya Mkoa,” alihimiza

Akizungumza kuhusu madhimisho ya wiki ya vijana, Mhe. Waziri Mhagama amesema ubunifu aliyouona wakati alipotembelea Mabanda, hasa uliofanywa na kijana Said Mussa wa kubuni namna ya kutengeneza taa za magari zilozoharibika na kurudisha katika muonekano mpya ni ubunifu mzuri.

“Kijana Huyu wa Kitanzania akifanikiwa kuhuisha teknolojia hiyo basi tutakuwa uwezo huko mbele kujenga viwanda vidogo vidogo vingi vya kuzalisha taa za magari nakusaidia kuongeza pato la kigeni na Kubrand Tanzania ya Mhe. Samia Kupitia Ubunifu wa Vijana,” alisema.

Namshukuru sana Mhe. Mhe. Prof. Joyce L. Ndalichako na Katibu Mkuu Mhandisi Cyprian John Luhemeja kwa kuridhia kumpatia Mkopo kijana huyu ili kuhakikisha anafanya vizuri katika ugunduzi alioufanya.

Naye Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi vijana ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Joyce Ndalichako amesema wiki ya vijana inalenga kutambua Mchango wa Waasisi wa Taifa Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere na Hayati Shekh Abeid Amani Karume.

 

Ameongeza kusema Maadhimisho ya wiki ya vijana Kitaifa ya Mwaka 2023 yanayofanyika Mkoani Manyara, kauli mbiu yake ni,” Vijana na Ujuzi Rafiki kwa Mazingira na Maendeleo Endelevu”. Maadhimisho ya vijana yanakutanisha vijana na wananchi wa Mikoa yote ya Tanzania Bara na Visiwani ambapo vijana wanapata fursa ya kubadilishana uzoefu. Ni fursa kwa Serikali na Wadau kutambua mchango mzuri wa vijana kwa maendeleo ya nchi yetu.

 “Natoa shukrani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuwajali na kuthamini vijana wa Tanzania kwa matendo kwa kuhakikisha vijana wanapatiwa mitaji ya kuendeleza biashara zao au kwa kuanzisha shughuli za maendeleo,” alibainisha

Awali Mkuu wa Mkoa wa Manyara Bi, Queen Sendiga alimshukuru Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt, Samia Suluhu Hassan kwa kuchagua Manyara kuwa Mwenyeji wa Kilele cha Madhimisho ya Siku ya vijana kitaifa, Mwenyeji wa Misa Maalumu ya Kumbukizi ya Baba wa Taifa, na Mwenyeji wa Killele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru.

“Moja ya mambo makubwa yatakayoachwa katika Mkoa wa Manyara, kutokana na kuwa Mwenyeji wa kilele cha Mbio za Mwenge wa uhuru ni pamoja na Ujenzi wa uwanja Mkubwa wa kisasa wa Mpira wa Miguu ambao Umejengwa kwa hadhi,” alisema


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.