Thursday, June 22, 2017

MWINYIMVUA: VIJANA WASHIRIKISHWE KULETA MABADILIKO BARANI AFRIKA



Watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu wameaswa kufanya kazi kwa uadilifu kwa kuzingatia maadili na utendaji katika Utumishi wa Umma wakati wa Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma.

Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera na Uratibu Dkt. Hamisi Mwinyimvua alipokutana na wafanyakazi wa ofisi yake Dodoma kwa lengo la kuiadhimisha Wiki hiyo inayofanyika kila mwaka kuanzia Juni 16-23 Barani Afrika ambapo kauli mbiu ya mwaka huu ni 

“Kuimarisha Ushirikishwaji wa Jamii katika Utoaji Huduma: Vijana washirikishwe kuleta Mabadiliko Barani Afrika”.

“Kila mtumishi wa umma anapaswa kuwa mwadilifu na mchapakazi hivyo niwaombe watumishi wote muwe mfano kwa kuwa waadilifu katika utendaji wenu kwa kuzingatia sheria zote za utumishi wa umma ili kuisaidia Serikali na kuwafikia wananchi kiujumla.”alieleza Dkt.Mwinyimvua

Katika kuiadhimisha wiki hii ya utumishi wa Umma ni wakati pekee wa kujitathimini eneo la kiutendaji na kuona maeneo yenye mapungufu ili yafanyiwe maboresho kwa haraka lengo likiwa kuondokana na mazoea yaliyokuwepo na kuendana na kasi ya Serikali ya Awamu ya Tano.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu, Issa Nchansi amewataka watumishi  kuzingatia mambo nane muhimu yaliyoainishwa katika Kanuni za Maadili ya Utendaji katika Utumishi wa Umma ikiwemo; Utoaji wa huduma bora, Utii kwa Serikali, bidii ya kazi, kutoa huduma bila upendeleo, uwajibikaji kwa umma,kuheshimu sheria, matumizi sahihi ya taarifa na uadilifu sehemu ya kazi.

Naye, Katibu Mkuu (Waziri Mkuu na Bunge) Bi. Maimuna Tarishi aliwaomba watumishi wote kuzingatia kauli mbiu ya mwaka huu kwa kuwawezesha vijana kielimu, kiuchumi na kijamii ili waweze kuzalisha na kuwa tegemeo la taifa.

“Niwaombe watumishi wote kuiangalia hili kundi la vijana wanaoajiriwa na Serikali kwa kuwatia moyo na kuwaunga mkono katika utekelezaji wa kazi zao” alisisitiza Tarishi

Sambamba na hili, Katibu Mkuu, Tarishi alisema  kuwa ili kuwe na utendaji wenye matokeo lazima kuitumia wiki hii kukumbushana majukumu na nafasi zetu katika kuitumikia serikali.

“Tuwe na utendaji wenye matokeo na si kuhesabu siku, miezi hadi mwaka bali tuwajibike kwa uadilifu kila muda tuwapo Serikalini.”


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.