Monday, August 21, 2023

WAZIRI MHAGAMA AHIMIZA MASHIRIKIANO

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu ) Mhe. Jenista Mhagama ameitaka Idara ya Ufutiliaji na Tathimini ya Utendaji wa Shughuli za Serikali kushirikiana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Nchini, (TAKUKURU) katika kutumia Mfumo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathimini ya Utendaji wa Shughuli za Serikali, ili kuweza kuondoa upendeleo, Rushwa na kutoa huduma bora kwa wananchi katika utendaji Serikalini.

Kauli hiyo ameitoa leo Jijini Dodoma alipokuwa katika kikao kazi cha Mapitio kilichohusisha Wakurugenzi, wa Idara na Wakuu wa vitengo wa Ofisi hiyo ambapo, Mamlaka ya Serikali Mtandao imefanya wasilisho la Mfumo wa Taifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji wa shughuli za Serikali.

Waziri Mhagama Alisema kuwa, eneo la Ufuatiliaji na Tathmini ni eneo ambalo haliwezi kukwepeka “Leo Tumekutana hapa tumefanya kazi nzuri ya kufanya mapitio na kuangalia ramani hii ambayo inaanza na kuwa na mfumo wa Ufuatilia na Tathmini Nchini, kama nyenzo muhimu sana ya Utendaji kazi ndani ya Serikali.” Alisisitiza

Aliendelea kusema kuwa, Mfumo huu utasaidia kushauri namna ya kujipanga na namna ya kufanya kazi ndani ya Serikali ,“Mfumo huu utusaidie kuchakata  kila kitu na kutusaidia kupata matokeo sahihi kwa jambo sahihi na shughuli sahihi, katika kupima utendaji kazi na matokeo yake.” Alifafanua.

Aidha, Alisema pia kwa Mujibu wa Sheria kuna Taasisi ambazo zimekasimiwa majukumu ya kufanya, zinazofanana na Idara hii akitolea mfano Tume ya Taifa ya Mipango, na kusema ni lazima kukutana na Tume hii ya Mipango ili kila mtu afanye kazi kwa kufuata Sheria na Kuzingatia Mifumo iliyopo. “Ni lazima kufanya Tathmini na Ufuatiliaji wa matumizi sahihi ya fedha katika Utekelezaji wa Miradi na utendaji wa shughuli za Serikali, eneo hili kwenye mfumo liwekwe vizuri na liweze kutusaidia,” Alisema.

Kwa Upande wake Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Ummy Nderiananga, Alisema Mamlaka ya Serikali Mtandao (Ega) imefanya wasilisho zuri lenye kutoa muelekeo wa Utendaji wa Shughuli za Serikali Utakaosaidia Ofisi ya Waziri Mukuu kuratibu vizuri shughuli za utendaji Serikalini katika kuripoti na kufanya Tathmini.

Akiongea baada ya wasilisho hilo, Mkurugenzi wa Idara ya Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji wa Shughuli za Serikali, kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Bi. Sakina Mwinyimkuu alisema, Idara yake Itajitahidi kufuatilia kwa Ukaribu ukamilishwaji wa mfumo huo kwa wakati, ili Taasisi za Umma ziweze kushirikishwa na mfumo uweze kufanya kazi kwa wakati kwenye upimaji wa Utendaji wa Shughuli za Serikali.

Awali, Akiongea katika kikao kazi hicho, Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA cha Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge na Uratibu) Bw. Innocent Mboya alisema, Amepokea maelekezo ya kukamilisha mfumo huo ndani ya mwaka huu wa fedha 2023/2024.

 “Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Kushirikiana na Mamlaka ya Serikali Mtandao, tunaahidi kwamba ndani ya hizi wiki mbili, tutakuwa tumeandaa mpango kazi ambao utatupeleka kwenye ramani na utelekelezaji wa mfumo huu, na ndani ya miezi mitatu tutakuwa tumekamilisha mfumo huu kwa kufuata matakwa na maelekezo ya Serikali.”  Alisisitiza

Walisisho hili ni Sehemu ya Utekelezaji wa Maelekezo ya Mhe. Waziri Mhagama aliyoyatoa katika kikao cha mazingativu kilichofanyika Mkoani Arusha Mapema Mwezi huu.


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.