Monday, December 9, 2019

RAIS MAGUFULI AHIMIZA AMANI, MSHIKAMANO NA KUJITEGEMEA SHEREHE ZA UHURU






Na. OWM, MWANZA

Amani, mshikamano, kufanya kazi kwa bidii na kujitegemea ni kati ya mambo yaliyosisitizwa na Rais wa Tanzania, Mhe.Dkt John Pombe Magufuli katika hotuba yake ya maadhimisho ya miaka 58 ya Uhuru wa Tanganyika.

Kauli Mbiu ya mwaka huu ni “Miaka 58 ya Uhuru na Miaka 57 ya Jamhuri: Uzalendo, Uwajibikaji ni Msingi wa Ujenzi wa Uchumi wa Taifa letu”

Sherehe hizo zilizofanyika kitaifa kwa mara ya kwanza katika Kanda ya Ziwa mkoa wa Mwanza , zimehudhuriwa na viongozi wakuu wa kitaifa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa na Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Wawakilishi Mhe. Dr. Ali Mohamed Shein.

Aidha, Viongozi Wakuu Wastaafu wakiwemo Marais, Makamu wa Rais na Mawaziri Wakuu ni miongoni mwa walio hudhuria sherehe hizo. Pia,  Mawaziri, Makatibu Wakuu, Wakuu wa Taasisi mbali mbali za Serikali na Mabalozi wanaowakilisha nchi zao nchini ni miongoni mwa waalikwa  walioshriki sherehe hizo.

Akizungumza katika maadhimisho hayo yaliyofanyika mjini Mwanza katika uwanja wa CCM Kirumba leo Jumatatu Desemba 9, 2019, Mhe. Rais, Dkt. Magufuli amesema Serikali imejipanga na itafanya kila lililo ndani ya uwezo wake kulinda amani na utulivu.

“Mshikamano na umoja wa Kitaifa ni nyenzo ya kufanikiwa zaidi. Serikali inawahakikishia wananchi kuendelea kulinda na kudumisha amani hiyo. Kazi ya kuendeleza Taifa sio lelemama. Viongozi na waasisi wa Taifa hili wamefanya mengi kwa mafanikio makubwa licha ya changamoto nyingi,” amesema Mhe. Rais Magufuli.

Mhe. Rais, katika hatua nyingine amepongeza juhudi ambazo serikali za awamu zote zilizotangulia kuiongoza nchi hii zilizozifanya kwa mafanikio makubwa  katika  kuboresha  nyanja za Kiuchumi na Kijamii ili kuhakikisha nchi yetu inajitegemea,  ameongeza kuwa  serikali ya awam ya tano inaendelea kuboresha na kuimarisha miundombinu ya usafirishaji, na nishati ya umeme kwa kuwa ni muhimili wa ujenzi wa viwanda kwa ustawi wa uchumi wa nchi.

“Katika kipindi cha miaka 58 ya Uhuru, Tanzania imeweza kupiga hatua kubwa katika Nyanja za kiuchumi na kijamii, wakati tunapata uhuru tulikuwa na shule za msingi 310 kwa sasa zipo shule 17,379, shule za sekondari zilikuwa 41 na sasa hivi zipo 4,817, tulikuwa na chuo kikuu 1  kwa sasa vipo vyuo vikuu 48”

“Tulikuwa na madaktari wazalendo 12, Kwa sasa tunao madaktari 9,400, wahandisi wazalendo walikuwa 2 kwa sasa wapo   wahandisi 19,164 walio sajiliwa,  vituo vya kutolea huduma za Afya vilikuwa 195 leo  hii vipo vituo vya kutolea huduma za Afya 7,293, Barabara za  kiwango cha lami  za kuunganisha mkoa na mkoa pia wilaya na wilaya zilikuwa kilometa  360 tu,  leo hii tunazo kilometa 12,679.55”  Amesisitiza Mhe.Rais Magufuli.

Mhe. Rais amebainisha kuwa katika kuhakiksha nchi inakuwa na  uchumi imara serikali ya awamu ya tano imeendelea kujenga viwanda ambapo kwa sasa tayari vimejengwa viwanda 4,000, Pia ameitaja miradi ya maendeleo ambayo serikali ya awamu ya tano inaendelea kuitekeleza kwa lengo la kuimarisha ustawi wa uchumi kuwa ni pamoja na kujenga reli ya kisasa, kujenga bwawa la Nyerere litakalozalisha megawati 2,115 za Umeme, Kujenga viwanja vya ndege 11, kununua ndege  11 na kusambaza umeme katika vijiji vyote vya Tanzania.

Aidha, katika kusherehekea Maadhinisho ya siku ya Uhuru, Mhe.Rais wa Dkt, Magufuli, ametangaza kuwaachia huru wafungwa 5,533 ambao walikuwa wamefungwa katika Magereza mbalimbali nchini.

"Nilitembelea Magereza nikashuhudia kuna mlundikano wa wafungwa, mpaka leo kuna Wafungwa 17,547 na Mahabusu 18,256, hii ni idadi kubwa, kwa hao wafungwa kuna baadhi wamefungwa kwa makosa madogo, " amesema Mhe. Rais Magufuli

"Hali ya pale Butimba ilinihuzunisha sana, kwa kutambua Dini zote zinatufundisha tusamehe na kuamini wafungwa wengi wanajutia makosa yao, kwa mujibu wa Mamlaka niliyonayo ya Kikatiba, nimewasamehe wafungwa 5,533" ameongeza Mhe. Rais Magufuli


Mhe.Rais, Magufuli akimalizia hotuba yake hakusita kuipongeza Kamati ya Maandalizi kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, kwa kuratibu Sherehe hizo, Kupitia Idara ya Maadhimisho na Sherehe za Kitaifa, ambapo amempongeza Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama, kwa kumsaidia vyema Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa wa sherehe hizo. Pia Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Uwekezaji), Bi.Dorothy Mwaluko ambaye amekuwa akifuatilia maandalizi ya kila siku ya sherehe hizo kupitia Idara ya Maadhimisho na sherehe za Kitaifa.

Awali Sherehe hizo zilipambwa na  Gwaride la askari wa majeshi ya Ulinzi na Usalama nchini pamoja na  onesho maalum la pamoja lilojumuisha  Sungusungu wapatao 1200,  sambamba na makundi manne ya manju na ngoma ya mang’ombe ga Kijiji.

Aidha Vikundi vya burudani vya  Wasanii pamoja na wanamziki  wa Kizazi kipya  na ngoma za asili kutoka mikoa ya Mwanza, Kagera na Mara wametumbuiza na kuburudisha wananchi waliohudhuria.

Katika sherehe hizo, kabla ya kuhitimisha hotuba yake Mhe. Rais, alimkaribisha Rais wa Zanzibar, Marais Wastaafu, Mawaziri Wakuu wa staafu na Viongozi wa vyama vya siasa nchini. Katika salamu zao viongozi hao kwa pamoja wamesisitiza,  Amani, mshikamano, kufanya kazi kwa bidii ili nchi iendelee kuwa na uchumi imara kama ambavyo Mhe. Rais ameweza kuimarisha uchumi huo kwa kipindi hiki cha utawala wake.
MWISHO






EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.