Friday, February 21, 2020

DKT. SHEIN ATAKA MIKAKATI YA PAMOJA YA KUKABILIANA NA MAAFA KWA NCHI ZA SADC

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema “Kufanyika kwa Mkutano wa SADC ni hatua muhimu katika kujenga matumaini mapya ya wananchi kuhusiana na maafa, tukizingatia kwamba katika miaka ya hivi karibuni  kumekuwa na ongezeko kubwa la  maafa pamoja na viashiria  vyake  katika nchi wanachama wa SADC.”Ameyasema hayo wakati akifungua  Mkutano wa Mawaziri wenye Dhamana ya Menejimenti ya Maafa kwa Nchi za SADC, leo tarehe 21, Februari, 2020, Zanzibar. 
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na wenye Ulemavu  Mhe. Jenista Mhagama amesisitiza “Ushiriki wa kisekta katika kukabiliana na maafa ni njia pekee ya kupunguza madhara ya  maafa kwa Nchi wanachama wa SADC”, leo tarehe 21, Februari, 2020, Zanzibar, wakati wa Mkutano wa Mawaziri wenye Dhamana ya Menejimenti ya Maafa kwa Nchi za SADC.
Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) Dkt. Stergomena Tax akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa kwanza wa Mawaziri wenye dhamana ya kusimamia maafa na kusisitiza kuwa  “Majanga hayana urasimu kitu muhimu kushirikiana kwa pamoja katika kukabiliana nayo pindi yanapotokea nchini”, leo tarehe 21, Februari, 2020, Zanzibar.  
Baadhi ya waalikwa kwenye mkutano wa Mawaziri wenye dhamana ya Menejimenti ya  Maafa kwa Nchi  wanachama wa SADC wakiwemo Mawaziri, Washauri wa Rais na Makamanda wa Vikosi vya ulinzi na Usalama wakisikiliza hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kukabiliana na Maafa Zanzibar, leo tarehe 21, Februari, 2020, Zanzibar.
Baadhi ya waalikwa kwenye mkutano wa Mawaziri wenye dhamana ya Menejimenti ya  Maafa kwa Nchi  wanachama wa SADC, wakifuatilia  mkutano huo leo tarehe 21, Februari, 2020, Zanzibar. 
Baadhi ya waalikwa kwenye mkutano wa Mawaziri wenye dhamana ya Menejimenti ya  Maafa kwa Nchi  wanachama wa SADC, wakifuatilia  mkutano huo leo tarehe 21, Februari, 2020, Zanzibar. 
Baadhi ya waalikwa kwenye mkutano wa Mawaziri wenye dhamana ya Menejimenti ya  Maafa kwa Nchi  wanachama wa SADC, wakifuatilia  mkutano huo leo tarehe 21, Februari, 2020, Zanzibar. 
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein akiwa katika picha ya pamoja na Mawaziri wenye dhamana ya Menejementi ya maafa kwa Nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo kusini mwa Afrika SADC baada ya kufungua Mkutano huo leo tarehe 21, Februari, 2020, Zanzibar.


Na. OWM, ZANZIBAR

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein amesema maeneo ya visiwa yapo katika hatari  kubwa  zaidi ya kukumbwa na maafa ukilinginisha na maeneo mengine duniani, hivyo alitoa wito kwa nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kuja na mikakati imara itakayoainisha mbinu za kutambua na kuwahi viashiria vya maafa kabla madhara hayajatokea.

“Tuna jukumu la kuendelea kushirikiana kati ya Serikali zetu, Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Kimataifa, Taasisi za Utafiti, Sekta Binafsi, Taasisi za Kidini, Taasisi za Fedha na  Mashirika yasiyo ya Serikali, Asasi za Kiraia na Vyombo vya Habari katika suala hili. Tukifanya hivyo, itakuwa tumeitekeleza kwa vitendo kaulimbiu ya mkutano huu isemayo:  “Ushiriki wa kisekta kwenye kupunguza madhara ya maafa ni njia bora ya kujenga uhimili katika ukanda wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika.” 

Rais Shein amesema hayo leo tarehe 21, Februari, 2020 Zanzibar alipokuwa anafungua kikao cha Mawaziri wa nchi za SADC wenye Dhamana ya Menejimenti ya Maafa.

Rais Shein ameeleza kuwa maafa yana madhara makubwa katika nchi, endapo hakutakuwa na mipango thabiti ya kukabiliana nayo na kutolea mfano namna vimbunga vya Idai, Kenneth na vinginevyo vilivyosababisha vifo, uharibifu wa mali na miundombinu katika nchi za Malawi, Zambia, Zimbawe, Msumbiji na Comoro.

Rais Shein amefafanua kuwa maafa yanabadilisha agenda za maendeleo ya nchi mbali mbali duniani kwa sababu fedha zilizotengwa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo zinabadilishwa matumizi kukidhi dharura za maafa kwa gharama kubwa zaidi.

Akitoa mfano wa mpango wa Sendai wa kukabiliana na maafa ambao unaonesha kati ya mwaka 2015 hadi 2018 nchi za Afrika zimekubwa na matukio 160 ya maafa ambayo yamesababisha uharibifu mkubwa wa mali na miundombinu. Ameeleza kuwa mpango huo unaonesha kuwa zinahitajika Dola za Marekani bilioni 3700 ili nchi zilizoathirika ziweze kurejesha hali yake ya kawaida. “Kiasi kikubwa hiki cha fedha kinatumika kujenga upya miundombinu iliyoharibika badala ya kujenga miundombinu mipya”, Rais Shein alisema.

Rais wa Zanzibar amewambia wajumbe wa mkutano huo hatua zilizo fanywa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar katika kuimarisha uhimili wa kukabiliana na maafa, kwa kuzingatia kuwa Zanzibar ni miongoni mwa visiwa ambavyo hupata madhara ya maafa.

Hatua hizo ni pamoja na kuandaa Sera ya kukabiliana na maafa ya mwaka 2011 na sheria yake ya mwaka 2015, kuanzisha Kamisheni inayoshughulikia masuala ya maafa na mpango wa mawasiliano wakati wa maafa. 

Aidha, amebainisha hatua nyingine kuwa ni pamoja na mpango wa elimu ya kujikinga na maafa kwa wanianchi, kuimarisha vyombo vya usafiri wa baharini ikiwemo ununuzi wa meli mbili kubwa za MV. Mapinduzi II ya abiria na MV. Ukombozi II kwa ajili ya kubeba mafuta, ujenzi wa vituo vitatu vya uokozi, ununuzi wa vifaa vya kisasa vya kufuatilia usafiri wa majini ikwemo ndege zisizokuwa na rubani na boat za uokoaji na kuzimia moto.

Dkt. Shein amesema ili kukabiliana na maafa ya mafuriko ambayo huwa yanakikumba kisiwa hicho kutokana na mvua za mwezi Oktoba hadi Desemba na mwezi Machi hadi Juni, nchi hiyo kwa msaada wa Serikali ya Falme za Kiarabu (UAE) imejenga kituo cha kuhifadhi watu wanaoathirika na mafuriko ambacho kina nyumba 30 zenye miundombinu yote kwa ajili ya maisha ya mwanadamu.

Aidha, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imechukua mkopo wa Dola za Marekani milioni 93 kwa ajili ya ujenzi wa mitaro inayopeleka maji baharini wakati wa mafuriko. Ujenzi huo ambao upo katika hatua za mwisho utakapokamilika, Dkt. Shein aliwahakikishia wajumbe wa mkutano huo kuwa, Zanzibar itaweza kuepuka mafuriko au Kupunguza kwa kiasi kikubwa.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Mhe. Jenista Muhagama (Mb)ameeleza kuwa malengo ya kuanzishwa kwa Kamati ya Mawaziri wenye Dhamana ya Maafa likiwemo lengo la kulishauri Baraza la Mawaziri wa nchi za SADC namna ya kupunguza madhara ya maafa. Alisema maafa yaliyosababishwa na majanga ya vimbunga vya Idai na Kenneth katika nchi za SADC, ukame na mafuriko ambayo hayana mipaka yamedhihirisha umuhimu wa nchi hizo kuwa na mpango wa ushirikiano wa kukabiliana na maafa.

Alieleza ili kwenda sambamba na juhudi za kikanda na kimataifa, Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mhe. Rais Dk. John Pombe Joseph Magufuli itaendelea kuimarisha uwezo wake wa usimamizi wa maafa katika Nyanja zote. 

Amebainisha hatua zilizochukuliwa na zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ni pamoja na kuandaa Mkakati wa Taifa wa Kupunguza Madhara ya Maafa; kuandaa Wasifu wa Janga la Mafuriko na Ukame; kuandaa Mpango wa Dhamira ya Taifa wa Utekelezaji wa Makubaliano ya Paris kuhusu mabadiliko ya tabianchi; kuandaa Mfumo wa Taifa wa Ufuatiliaji wa Taarifa za Gesi Joto;  Kuandaa Mipango ya Kukabiliana na Dharura za Afya ya Binadamu, Mifugo na Wanyama; kuandaa Mkakati wa Taifa wa Usimamizi wa Mazao baada ya Kuvuna.

Naye Katibu Mtendaji wa SADC, Dkt. Stergomena Tax aliwambia wajumbe wa mkutano huo kuwa majanga hayataki urasimu yanapotokea, yanahitaji hatua za haraka na zinazoeleweka ili kuyakabili ipasavyo kabla hayajasababisha madhara makubwa.

Dkt. Tax alifafanua kuwa mkutano huo kufanyika Zanzibar ni fursa nzuri kwa nchi za SADC kujua vizuri muungano wa Tanzania na Zanzibar ambao umedumu kwa miaka mingi sasa. Aidha, alisema itakuwa fursa nzuri kwa nchi hizo kujionea vivutio vya kipekee vya kisiwa cha Zanzibar ambacho kina umaarufu mkubwa duniani kote.

Serikali ya Tanzania imekuwa mwenyeji wa Mkutano wa Kwanza wa Kamati ya Mawaziri wanaohusika na Menejimenti ya Maafa kwa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika baada ya Tanzania kuchukua rasmi nafasi ya Mwenyekiti wa jumuiya kuanzia mwezi Agosti, 2019 kwa kipindi cha mwaka mmoja hadi mwezi Agosti, mwaka huu (2020).  Hatua hii inatokana na utaratibu wa kawaida wa mzunguko wa kushika nafasi hiyo kulingana na mkataba wa kuanzishwa kwa jumuiya hiyo.
MWISHO.



EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.