Wednesday, February 26, 2020

ZAIDI YA WAFANYABIASHARA NA WAWEKEZAJI 560 WASIKILIZWA KERO ZAO SHINYANGA

NA. MWANDISHI WETU
Zaidi ya wafanyabiashara na wawekezaji 560 mkoani Shinyanga wamekutana katika mkutano wa mashauriano baina ya Serikali na Sekta binafsi ili kusikilizwa na kupata ufumbuzi wa changamoto katika maeneo yao ya uwekezaji na biashara ili kuendelea kuwa na tija katika maendeleo yao na nchi kwa ujumla.
Mkutano huo ulililofanyika tarehe 26 Februari, 2020 ulioandaliwa na  Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji) kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkoa wa Shinyanga na  kufanyika  katika Ukumbi wa mikutano wa NSSF mkoani humo.
Mkutano ulijumuisha makundi yote ikiwemo, wakulima, wafugaji, wafanyabiashara wakubwa na wadogo, wachimba madini, wavuvi pamoja na wenye viwanda na  wawekezaji katika sekta mbalimbali.
Mkutano ulihudhuriwa na Mawaziri na Manaibu mawaziri kutoka Wizara nane ikiwemo Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji), Wizara ya Fedha na Mipango, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Mambo ya Ndani, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano,Wizara ya Maliasili na Utalii na Wizara ya Madini.
Akizungumza wakati wa kufunga mkutano huo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Uwekezaji nchini Mhe.Angellah Kairuki alieleza namna Serikali ilivyoendelea na jitihada za kuhakikisha uboreshwaji wa mazingira ya uwekezaji nchini ikiwa ni pamoja na kutungwa kwa sheria mpya ya uwezeshaji biashara (Business Facilitation Acts)
Aidha sheria itasaidia kufanya mapitia ya sera na sheria stahiki kwa lengo la kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara nchini.
Aliongezea kuwa, uwepo wa mikutano hiyo inaongeza hamasa kwa wafanyabiashara na wawekezaji kueleza kero wanazokabiliana nazo pamoja na kupatiwa majibu ya papo kwa hapo na Mawaziri wa Sekta husika.

“Mikutano imeibua hoja muhimu zilizopatiwa ufumbuzi na mawaziri wa sekta mbalimbali  niwatoe shaka Serikali itaendelea kuwaunga mkono na ni vyema mkaendelea kufuata sheria na kanuni zilizopo katika kuwekeza kwenu,”.alisisitiza Waziri Kairuki.

Naye Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega amewahakikishia wafugaji wa samaki kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira bora ya kuwawezesha wafugaji kufuga samaki na kueleza kuwa, mabwawa ya samaki yameongezaka kutokana na jitihada zilizopo na kueleza namna Serikali inavyoendelea kudhiti uvuvi haramu baharini na maziwa.
Sambamba na hili Naibu Waziri alieleza kuwa  jitihada za ujenzi wa viwanda vikubwa vya kuchakata mazao yatokanayo na mifugo nchini zinaendelea hivyo wananchi hawana budi kuwa na matumaini makubwa na Serikali yao.
Aidha Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Ashantu Kijaji aliwahaikishia wajumbe wa mkutano huo namna wizara yake ilivyojipanga kuondoa changamoto za gharama kubwa za mikopo katika benki pamoja na suala la utitiri wa kodi baada ya kulalamikiwa na wafanyabiashala hao.
“Nimewafurahia wana Shinyanga kwa uwazi wenu wa kujieleza vizuri, niwahakikishie kuwa,mwisho wa malalaiko yenu haupo mbali tutahakikisha sekta ya fedha inatatua kero zenu na kushughulikia upatikanaji wa mikopo na kwa gharama zinazoeleweka,”alieleza Dkt. Kijaji
Serikali imefanya jitihada kubwa kuhakikisha Taasisi zetu za mikopo zinashusha gharama za mikopo (riba) kwa ajili ya shughuli za kijamii zinazowahusu.


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.