Friday, February 7, 2020

SERIKALI YATUMIA SH. BILIONI 128 KUBORESHA ELIMUMSINGI BILA ADA

*Maboresho yagusa vyuo vya ualimu, VETA na ujenzi wa mabweni
*Wanafunzi 130,072 wa elimu ya juu waata mikopo ya sh. bilioni 266.4

SERIKALI imetoa jumla ya shilingi bilioni 128.1 kwa ajili ya kugharamia elimumsingi bila ada katika kipindi cha kuanzia Julai hadi Desemba 2019.

Hayo yameelezwa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa leo (Ijumaa, Februari 7, 2020) wakati akitoa hotuba ya kuahirisha Mkutano wa 18 wa Bunge jijini Dodoma. Bunge limeahirishwa hadi Machi 31, mwaka huu.

“Serikali imeboresha elimu ya msingi kwa kuendelea kutekeleza programu ya elimumsingi bila ada ambapo Serikali inagharamia chakula kwa wanafunzi 189,226 wa kutwa na bweni, posho ya madaraka kwa walimu wakuu 23,843, fidia ya ada kwa wanafunzi 1,874,331 na ruzuku ya uendeshaji wa shule,” amesema.

Akielezea kuhusu matokeo ya mitihani ya kitaifa, Waziri Mkuu amesema matokeo chanya ya maboresho hayo ni kuongezeka kwa kiwango cha ufaulu katika upimaji wa kitaifa kwa darasa la nne, kidato cha pili na mitihani ya kitaifa kidato cha nne kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2015 hadi 2019. “Shule za Kata nazo zimeendelea kufanya vizuri na kuongeza matumaini kwa Watanzania walio wengi,” ameongeza.

“Matokeo ya upimaji wa kitaifa wa darasa la nne kwa mwaka 2019, yamebainisha kuwa jumla ya wanafunzi 1,531,120 walifaulu ikilinganishwa na wanafunzi 1,213,132 waliofaulu mwaka 2018. Ufaulu huo ni sawa na ongezeko la asilimia 26.21. Kwa upande wa kidato cha pili, wanafunzi 514,251 walifaulu upimaji wa kitaifa kwa mwaka 2019 ikilinganishwa na wanafunzi 452,273 waliofaulu upimaji huo mwaka 2018 sawa na ongezeko la asilimia 13.7,” amesema.

“Kwa upande wa kidato cha nne, mwaka 2019 wanafunzi 340,914 kati ya wanafunzi 422,722 walifaulu mtihani wa taifa wa kidato cha nne. Ubora wa ufaulu wa wanafunzi nao umeongezeka kwa mwaka 2019. Kwa mfano, wanafunzi 135,301 sawa na asilimia 32.01 walipata ufaulu mzuri wa daraja la kwanza hadi la tatu,” ameongeza.

Akielezea kuhusu maboresho ya miundombinu ya eimu, Waziri Mkuu amesema maboresho na uwekezaji wa Serikali katika sekta ya elimu yamekuwa chachu ya kuongezeka kwa kiwango cha ufaulu na wakati mwingine kuleta changamoto kwenye miundombinu ya elimu.

“Hata hivyo, Serikali imeendelea kukamilisha usajili wa shule mpya, kuongeza vyumba vya madarasa 1,218 na mabweni 14 ili wanafunzi wote waliofaulu kuingia kidato cha kwanza mwaka 2020, waweze kuanza masomo kwa wakati,” amesisitiza.

Akitoa ufafanuzi kuhusu maboresho kwenye elimu ya juu, Waziri Mkuu amesema  Serikali imeimarisha elimu ya juu, ufundi na ustawi wa jamii kwa kuendelea kutoa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu ambapo hadi Desemba mwaka jana, sh. bilioni 266.4 zimetolewa kwa wanafunzi 130,072. “Kati yao, wanafunzi 49,493 ni wa mwaka wa kwanza na 80,579 wanaoendelea,” amesema.

Amesema Serikali imeendelea kujenga mabweni ya wanafunzi wa kike; kukarabati majengo ya vyuo vikuu na vyuo vya ualimu; kuboresha vyuo vya VETA kwa kujenga na kuboresha vyuo na kununua vifaa vya kufundishia na kujifunzia.

“Vilevile, Serikali imeimarisha vyuo vya maendeleo ya jamii na ustawi wa jamii kwa kuanzisha vituo vya ubunifu vitano sambamba na kutekeleza programu ya uanagenzi ili wapate ujuzi wa kujiajiri unaoendana na ushindani wa soko la ajira,” amesema.


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.