Monday, December 4, 2017

MPANGO WA SHILINGI BILIONI 1 WA KUSAIDIA WATU WENYE ULEMAVU NCHINI WAZINDULIWA

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Ajira, Kazi, Vijana na Watu wenye Ulemavu), Jenista Mhagama akifafanua umuhimu wa mafunzo ya ufundi kwa watu wenye Ulemavu kwa Balozi wa Kuwait nchini Tanzania Jassem Al-Najem, wakati ubalozi huo ulipozindua mpango wa kuwasaidia watu wenye ulemavu nchini katika Chuo cha Ufundi kwa watu wenye Ulemavu, Yombo jijini Dar es Salaam, tarehe 30 Novemba, 2017.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Ajira, Kazi, Vijana na Watu wenye Ulemavu), Jenista Mhagama pamoja na wanafunzi wa Chuo cha Ufundi kwa watu wenye Ulemavu, Yombo jijini Dar es Salaam wakipokea sehemu ya vifaa vya kuwasaidia watu wenye ulemavu kutoka  kwa Balozi wa Kuwait nchini Tanzania Jassem Al-Najem, wakati ubalozi huo ulipozindua mpango wa kuwasaidia watu wenye ulemavu nchini, tarehe 30 Novemba, 2017.

Kama inavyoeleweka kila tarehe 3 Desemba ya kila mwaka jamii ya kimataifa ikiwemo Tanzania huadhimisha siku ya watu wenye ulemavu Duniani. Kwa kutambua hilo serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na nchi ya Kuwait wamezindua Mpango wa kuwasaidia watu wenye ulemavu nchini.

Mpango huo utakaogharimu kiasi cha shilingi bilioni moja utafadhiliwa na serikali ya Kuwait na utatekelezwa Tanzania Bara na Tanzania visiwani kwa kuyashirikisha mashirika yasiyokuwa ya serikali na asasi za kijamii.

Akiongea wakati wa kuzindua mpango huo leo tarehe 30, Novemba 2017, katika Chuo cha Ufundi Yombo kwa Watu wenye Ulemavu, jijini Dar es Salaam, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Ajira, Kazi, Vijana na Watu wenye Ulemavu), Jenista Mhagama alifafanua kuwa serikali ya awamu ya Tano imedhamiria kuboresha ustawi wa watu wenye ulemavu nchini kwa kushirikiana na wadau wote.

“Ninatoa wito kwa Taasisi za serikali na zisizo za serikali kila ziendelee kushirikiana na wizara yangu pale wanapo ona wana nafasi kidogo katika kuwasaidia watu wenye Ulemavu nchini ili waweze kuishi na kuhudumiwa katika shughuli zote ambazo ni haki zao kwa mujibu wa katiba ya nchi yetu” alisema Mhagama

Mhagama aliishukuru nchi ya Kuwait kwa dhamira yake ya kuwasaidia watu wenye ulemavu nchini ambapo wamezindua mpango huo kwa kutoa vifaa vya kuwasaidia watu wenye ulemavu katika Chuo cha Ufundi Yombo kwa Watu wenye Ulemavu.

Kwa upande wake Balozi wa Kuwait nchini Tanzania Jassem Al-Najem alifafanua kuwa nchi yake inatambua juhudi za serikali ya awam ya tano katika kushughulikia masuala ya watu wenye ulemavu na kwa kulitambua hilo wameamua kuwa na mapango huo ili kutambua mchango wa watu wenye ulemavu.

“Leo nazindua mpango kwa kutoa msaada wa kwanza kwa wanafunzi wenye ulemavu katika kituo hiki kwa kusaidia viti vya maringi, magongo vifaa vya kusaidia watu wenye udhaifu wa kusikia  na miwani na fimbo kwa wasiiona, ni matumaini yangu kuwa mpango huu utakuwa na manufaa kwa wote” alisema Al-Najem.

Awali akiongea katika makabidhiano ya vifaa hivyo Kaimu Mkuu wa Chuo cha Ufundi Yombo kwa Watu wenye Ulemavu, Mariam Chelangwa alieleza kuwa anashukuru kwa kuwa watu wa kwanza wa kunufaika na mpango huo kwa kupata msaada wa vifaa vya kuwasaidia wanafunzi ambavyo vitawasaidia kupata mafunzo bora.


Serikali imeendelea na juhudi za kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata haki stahiki nchini ambapo tangu mwaka 2004 serikali iliandaa Sera ya Taifa ya Maendeleo na Huduma kwa watu wenye Ulemavu, pamoja na sheria na. 9 ya mwaka 2010 inaweka msisitizo wa haki za watu wenye ulemavu katika ajira, afya na shughuli za kiuchumi. 


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.