Tuesday, January 30, 2018

SERIKALI YAAZIMIA KUBORESHA MAZINGIRA YA BIASHARA NA UWEKEZAJI NCHINI

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Uratibu) Prof. Faustin Kamuzora akichangia hoja katika mkutano wamashauriano baina ya sekta ya umma na sekta binafsi, katika ukumbi wa (JNICC)   Wengine jukwaani kushotoni Eng. Raymond Mbilinyi katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Biashara (TNBC), Bw. Godfrey Simbeye Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF).
Serikali imeazimia kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini kwa kuweka mifumo ya kielektroniki katika utoaji wa huduma ili kuongeza ufanisi katika utendaji wa kazi na kuondoa urasimu usio wa lazima .
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa mapangokazi baina ya Sekta ya Umma na Sekta binafsi Prof. Faustin Kamuzora alisema leo tarehe 30 Januari, 2018 katika Ukumbi wa Mikutano wa JNICC Dar es Salaam, mkutano huu ni ushahidi kwamba Serikali na Sekta Binafsi ni wadau muhimu katika kuleta maendeleo ya kiuchumi na kijamii na kwamba mazingira wezeshi ya biashara ni kichocheo muhimu katika jitihada za Serikali kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi.
“Serikali ya Awamu ya Tano imeweka kipaumbele katika utekelezaji wa Mpangokazi wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (Roadmap for Improvement of Business Environment and Investment Climate in Tanzania), utekelezaji wa Mpangokazi huu utaiwezesha nchi yetu kufikia malengo yake ya kujenga uchumi wa viwanda,  na kuongeza fursa za ajira na kuiwezesha Sekta Binafsi kuchangia katika ukuaji wa uchumi na kuwa nchi ya kipato cha kati ifikapo mwaka 2025”, Alisema Prof. Kamuzora.
Prof. Kamuzora alieleza kuwa, miongoni mwa maboresho yaliyofanyiwa kazi na Serikali ni pamoja na kuboresha mfumo wa usajili wa biashara na kampuni kwa kuanzisha mfumo wa usajili kwa njia ya mtandao (On-line Registration System) utakao anza kutumika hivi karibuni, pamoja na kuimarisha mfumo wa usimamizi wa ardhi kwa kuanzisha mfumo unganishi wa kielektroniki wa utunzaji wa kumbukumbu  kwenye masjala ya ardhi (Integrated Land Management Information System) na kuongeza ufanisi katika utendaji bandarini kwa kuimarisha mifumo ya kielektroniki ya malipo na utoaji wa huduma kwa wasafirishaji wa shehena.
 “Napenda kutoa rai kwa waratibu wa mazingira ya biashara kutoka Wizara na Taasisi za Serikali kutumia fursa ya mkutano huu kujifunza  kutoka kwa wadau wa sekta binafsi kwa lengo la kuboresha utoaji huduma kwa kuzingatia kazi na ufanisi wa biashara”, alisema Kamuzora.
Tumeunda kikosi kazi cha taifa cha uanzishwaji wa mfumo “Building codes” za nchi nzima, ili kuweza kufanikisha mashirikiano haya baina ya sekta umma na sekta binafsi kwa haraka na itasaidia kuleta ubunifu kulingana na mabadiliko kwenye ulimwengu wa kibiashara na mahitaji ya nyakati, alisisitiza Kamuzora.  
Uchambuzi wa awali wa taarifa ya wepesi wa kufanya biashara ya mwaka 2018 umeonesha kwamba Wizara na Taasisi za Serikali zina jukumu kubwa la kuhakikisha kwamba Tanzania inakuwa na mazingira rafiki na yanayotabirika ya kufanya biashara ili kuvutia uwekezaji wa ndani na nje na kuiwezesh seta binafsi kuongeza fursa za ajira.

Mkutano huo wa siku moja umelenga kuleta mikakati bora itakayoiwezesha Tanzania kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara baina ya Sekta a Umma na Sekta Binafsi , hiini pamoja na kuboresha mazingira ya kutoa huduma kwa sekta binafsi tutakuwa tumeshiriki kikamilifu katika kulifikia azma ya Serikali ya kujenga uchumi wa viwanda kama inavyoelekezwa kwenye Mpango wa pili wa Maendeleo wa miaka mitano 2016/2017-2020/21. 
Baadhi ya wageni waalikwa na wawakilishi mbalimbali kutoka sekta binafsi na Sekta ya Umma walioshiriki mkutano huo uliofanyika Januari 30 2018 Jijni Dar es Salaam.
Katibu mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Uratibu) Prof. Faustin Kamuzora akijibu maswali kutoka kwa waandishi wa habari baada ya majadiliano kuhusu mpangokazi wa kuboresha mazigira ya biashara na uwekezaji nchini. 



EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.