Friday, January 5, 2018

WAZIRI MKUU ATATUA MGOGORO WA MIAKA MIWILI


*Ni wa ujenzi wa Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga
*Asema hataki kusikia wakijenga karibu na chanzo cha maji

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemaliza mgogoro wa ujenzi wa makao makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga ambao umedumu kwa miaka miwili.

Ametoa uamuzi huo jana jioni (Ijumaa, Januari 5, 2018) wakati akizungumza na watumishi na madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga pamoja na Halmashauri ya Mji wa Mbinga, kwenye ukumbi wa Jumba la Maendeleo, mjini Mbinga.

“Ninazo taarifa kuwa kuwa mnagombea mahali pa kujenga makao makuu ya Halmashauri hadi mnataka kujenga kwenye chanzo cha maji. Hiyo haikubaliki. Kwenye vyanzo vya maji hakujengwi miji, tena Afisa Maliasili nenda ukapande miti zaidi ili tutunze chanzo chetu,” alisema na kuamsha shange ukumbini.

Wataalamu wa Halmashauri hiyo walikuwa wakivutana na Madiwani juu ya makao makuu hayo kujengwa Ndengu (ambako ni karibu na chanzo cha maji) huku wengine wakitaka yajengwe Kigonsera kwa madai kuwa kote ni karibu na wananchi.

Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga iligawanywa Julai 2015 kwa kupata Halmashauri ya Mji wa Mbinga na Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga na ilianza kazi Julai 2016.

Waziri Mkuu alisema Halmashauri hiyo si ya kwanza kuwa na migogoro, kwa hiyo nimeamua mjenge hapa hapa mjini Mbinga. Mkijenga huko wanakotaka hawa mtagombana na mkijenga kule nako pia mtagombana, lakini ugomvi wenu ni kwa faida ya nani? Kama si kuwaumiza wananchi mnaowaongoza ni nini?,” alihoji Waziri Mkuu.

“Miaka yote mmekuwa mkipata huduma kutokea hapa hapa kabla Halmashauri hizi hazijatenganishwa. Tumeleta fedha mara mbili, mara ya kwanza sh. milioni 500 na ya pili sh. milioni 400 lakini hazijatumika kwa sababu ya migogoro yenu isiyo na tija. Kwa hiyo, makau makuu yatajengwa hapa hapa mjini,” alisisitiza Waziri Mkuu.

Waziri Mkuu alisema kesi kama hizo zilishatokea Musoma Mjini na Vijijini, Lindi Mjini na Vijijini, Kigoma Mjini na Vijijini, na Singida Mjini na Vijijini ambako kote huko Halmashauri za Wilaya za Vijijini zimejengwa mjini na wananchi wanaendelea kupatiwa huduma kama kawaida.

Wakati huohuo, Waziri Mkuu amemuagiza Naibu Waziri (OR-TAMISEMI), Bw. Joseph Kakunda afuatilie suala la sh. milioni 700 ambazo zimetolewa na Serikali kwa ajili ya mradi wa maji lakini Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga imezitoa kwa kampuni ambayo haina hadhi ya kupokea kiasi hicho cha fedha.

“Tumeleta kwa ajili ya mradi wa maji lakini ninyi mkaipa kazi kampuni ambayo haina hata uwezo wa kupokea sh. milioni 500. Ninazo taarifa kuwa Halmashauri hii mmeshalipa asilimia 80 ya fedha kwa mkandarasi huyo na wala maji hayajatoka hadi leo. Naibu Waziri fuatilia na nipate taarifa,”alisema.

Waziri Mkuu anaendelea na ziara yake ya kikazi mkoani Ruvuma kwa kutembelea wilaya ya Nyasa ambako atazungumza na watumishi na madiwani, ataweka jiwe la msingi la ujenzi wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, atakuwa mgeni rasmi kwenye tamasha la utalii na pia kuhutubia mkutano wa hadhara.


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.