Thursday, January 16, 2020

WAZIRIKAIRUKI ATEMBELEA KIWANDA CHA MIFUKO CHA SAMAKI INVESTMENT BAGAMOYO.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Uwekezaji nchini Mhe. Angellah Kairuki ametembelea kiwanda cha kuchakata mifuko chakavu na kuzalisha mipya cha SAMAKI investment ili kukagua mazingira ya wawekezaji nchini pamoja na kusikiliza changamoto zao na kuzitafutia ufumbuzi ili kuendelea kuwa na  mazingira rafiki kwa wawekezaji nchini.
Waziri huyo ametembelea kiwanda hicho kilichopo katika Kata ya Zinga Wilaya ya Bagamoyo mkoa wa Pwani Januari 16, 2020 ili kujionea mazingira yao pamoja na kupokea changamoto wanazokabiliana nazo ili kuona namna ya kushirikiana nao katika kuzitatua ili kufikia malengo.

Katika ziara hiyo aliambatana na viongozi wa Wilaya ya Bagamoyo, Mbunge wa Chalinze Mhe. Ridhiwani Kikwete pamoja na watendaji wa Ofisi yake ambapo alifurahishwa na utendaji kazi wa kiwanda hicho kwa kuchakata mifuko chakavu na kuzalisha mipya pamoja na mifuko ya kisasa na kusema kuwa ni ya kuridhisha.

“Niwapongeze sana kwa kuendelea kuzalisha mifuko katika ukubwa tofauti, ikiwemo ile ya Kilo 25, 50 na 100 na hii itasaidia kuwafikia wateja wenye mahitaji tofauti tofauti kwa kuzingatia ubora unaotakiwa,” alisema Waziri Kairuki

Alisema licha ya kazi nzuri inayoendelea katika kiwanda hicho bado kuna kazi kubwa ya kuwajengea uwezo vijana wa Kitanzania kwa kuhakikisha wanapewa mafunzo na ujuzi wa kutosha ili waweze kuleta tija katika nchi yao.

Aidha waziri aliwataka waendelee kuzalisha kwa kuzingatia sheria na taratibu zilizopo nchini ili kuendelea kuwekeza kwa uhuru bila uvunjifu wa sheria za uwekezaji zilizopo.

Aidha akijibu changamoto zilizoainishwa ikiwemo ya kukosekana kwa huduma za umeme wa uhakika, ucheleweshwaji wa vibali vya wafanyakazi, kukosa kibali cha kuingiza malighafi kutoka nchi za nje na ufinyu wa eneo la kiwanda, Waziri alieleza Serikali itahakikisha inaboresha mazingira kwa kuhakikisha changamoto za umeme zinatatuliwa na kumwagiza Mhandisi Mkuu wa Mkoa TANESCO, Kenneth Boymanda kuhakikisha changamoto hiyo inatatuliwa ifikapo Machi, 2020.

“Nimetembelea viwanda vingi mkoa wa Pwani na vingi vimeongelea changamoto hii ya ukosefu wa umeme wa uhakika, hivyo Mhandishi mkuu wa mkoa, hakikisheni mnamaliza changamoto hii mapema ili kutowakwamisha wawekezaji wetu kwa kukosa umeme wa uhakika,”alisema Waziri Kairuki.

Naye Mmiliki wa kiwanda hicho Bw. Xiawei Yu alimshukuru waziri kwa kutembelea kiwandani hapo na kuahidi kuendelea kuzalisha kwa kuzingatia sheria kama zinavyoelekeza kwa kuzingatia mradi huo ni mkubwa na una tija kwa jamii yote kwa kuzingatia umuhimu wa mifuko ya kisasa.
“Tutaendelea kuzingatia taratibu zilizopo na kampuni yetu imedhamiria kuzalisha mifuko bora ya kubebea nafaka mbalimbali na kuhakikisha wateja wanapata bidhaa bora zenye uhakika,”alieleza Bw. Yu.

Aliongezea kuwa, uwepo wa kiwanda hicho umechangia upatikanaji wa ajira kwa vijana wapatao 126 kati yao 71 ni wenye ajira rasmi na 55 ni vibarua kwa kazi ndogondogo za msimu zinazojitokeza kiwandani hapa.

Kiwanda cha SAMAKI Investment kilisajiliwa tarehe 28 Septemba 2012 na kuanza kufanya kazi rasmi mwezi Juni, 2013   katika eneo la Mabibo Sokoni eneo la Urafiki Jijini Dar es Salaam, mnamo mwaka 2017 kutokana na ufinyu wa eneo, kiwanda kilihamia katika Kata ya Zinga Wilaya ya Bagamoyo mkoa wa Pwani. Mradi umegharimu wastani wa Tshs bilioni 4. 950 kwa ajili ya ujenzi na ununuzi wa mitambo ya kisasa kwa ajili ya uzalishaji.


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.