Saturday, April 6, 2019

SERIKALI YAONGEZA NGUVU UZALISHAJI WA MAFUTA-MAJALIWA

UZALISHAJI mdogo wa zao la Michikichi ni miongoni mwa sababu za kushindwa kujitosheleza kwa mahitaji ya mafuta ya kula nchini na Serikali imekuwa ikilazimika kutumia fedha nyingi za kigeni kwa ajili ya kununua mafuta  hayo kutoka nje ya nchi.

Kutokana na changamoto hiyo, Serikali imeamua kuweka nguvu kubwa kwenye uzalishaji wa mazao ya mbegu za mafuta ili kuondokana na utegemezi na kuokoa matumizi ya fedha za kigeni.

Hayo yamesemwa leo (Alhamisi, Aprili 4, 2019) na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa wakati akiwasilisha hotuba ya Mapitio na Mwelekeo wa Kazi za Serikali na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa mwaka 2019/2020.

Waziri Mkuu amesema katika kutekeleza azma hiyo, Serikali imeanza kuimarisha kilimo cha zao la michikichi hususan katika mkoa wa Kigoma ili kusaidia upatikanaji wa mbegu bora za chikichi.

Amesema lengo ni kuzalisha na kusambaza kwa wakulima miche ipatayo milioni 20 katika kipindi cha miaka minne (2018/2019 hadi 2021/2022), pia Serikali imeamua kukifanya Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Kihinga, mkoani Kigoma kuwa Kituo cha Utafiti wa Mbegu Bora za michikichi.

“Maamuzi haya ya Serikali yameanza kuzaa matunda, hadi kufikia Februari 2019, Kituo cha Kihinga kimezalisha mbegu 4,747 ambazo zimefanyiwa uoteshwaji wa awali. Katika mwaka 2019/2020, Serikali imepanga kuzalisha miche ya michikichi milioni tano.”

Waziri Mkuu amesema matarajio ya Serikali ni kuhakikisha kwamba usimamizi mzuri wa mkakati huo wa miaka minne utalisaidia Taifa kuondokana na uagizaji wa mafuta ya kula kutoka nje, kutengeneza fursa mbalimbali za ajira na kuwaongezea kipato wakulima wa michikichi.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema hali ya uzalishaji wa mazao ya chakula kwa msimu wa 2017/2018 na upatikanaji wa chakula kwa mwaka 2018/2019, imeendelea kuimarika.

Waziri Mkuu amesema hatua hiyo imetokana na hali nzuri ya mvua katika maeneo mengi ya nchi, kuongezeka kwa tija na uzalishaji. “Uzalishaji wa mazao ya chakula umefikia tani milioni 16.89 ikilinganishwa na mahitaji ya chakula ya tani milioni 13.57 na kufanya nchi kuwa na ziada ya chakula ya tani milioni 3.32.”

Amesema uzalishaji wa mazao makuu ya kimkakati yakiwemo chai, kahawa, korosho, pamba na tumbaku umeimarika kutokana na juhudi zinazofanywa na Serikali ikiwemo kuimarisha ushirika.

“Kwa mfano, uzalishaji wa zao la pamba uliongezeka kutoka tani 132,934 mwaka 2017/2018 hadi kufikia tani 222,039 mwaka 2018/2019 wakati uzalishaji wa zao la Kahawa uliongezeka kutoka tani 45,245 hadi kufikia tani 65,000.”

Waziri Mkuu amesema Serikali imeendelea kutoa kipaumbele kwa mazao hayo na mengine kwa kuwa ndiyo mhimili wa kutoa malighafi za kuendesha viwanda na yana mnyororo mpana wenye fursa ya kutoa ajira nyingi na kuliingizia Taifa fedha za kigeni.

(mwisho)
                       BONYEZA HAPA KUSOMA HOTUBA YA BAJETI


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.