Wednesday, August 9, 2017

VIJANA WATAKIWA KUWA CHACHU YA MABADILIKO CHANYA NCHINI

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu,(Sera, Bunge, Ajira na Watu wenye ulemavu), Jenista Mhagama amewataka vijana nchini kuwa chachu ya mabadiliko chanya nchini kwa kushiriki kikamilifu katika kuleta maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Akiongea na waandishi wa Habari mjini Dodoma, tarehe 9 Agosti, 2017, kuhusu siku ya Kimataifa ya Vijana Duniani, Mhagama alifafanua kuwa Vijana ndio wenye nguvu zaidi za kufanya kazi, Vijana ni wabunifu, Vijana ndio chachu ya mabadiliko chanya katika jamii na Vijana ndio warithi wa Taifa.

“Kila mwaka Umoja wa Mataifa huandaa kauli mbiu ambayo hutumika kama mwongozo wa masuala ya Vijana yanayotakiwa kutiliwa mkazo kwa mwaka husika.  Kauli mbiu ya mwaka huu wa 2017 ni“USHIRIKI NA USHIRIKISHWAJI WA VIJANA KATIKA KUDUMISHA AMANI” alisisitiza Mhagama.
Mhagama aliongeza kuwa Lengo la Kauli mbiu hii ni kuenzi mchango wa vijana katika kulinda na kutunza amani za Nchi zao na Dunia kwa ujumla, pia kuendelea kuzihimiza Nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa kuwashirikisha kikamilifu vijana katika mikakati mbalimbali ya kudumisha amani.

Aliongeza kuwa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani mwaka huu 2017, yatafanyika kitaifa, Agosti 12 Mkoani Dodoma. Sababu ya Kufanyika Maadhimisho Mkoani mkoani Dodoma ni pamoja na Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi, na Uwepo wa Viongozi wote wa Serikali Mkoani humo.


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.