Wednesday, April 4, 2018

KAMATI ZA WATU WENYE ULEMAVU ZA MKOA KUTAMBULIKA KISHERIA

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimiana na Afisa Mtetezi CCBRT Bw. Fredrick Msigala kwenye viwanja vya Bunge baada ya kuwasilisha hotuba  kuhusu mapitio na mwelekeo wa kazi za serikali na makadirio ya mapato na matumizi ya  fedha  za Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa mwaka 2018/2019, bungeni mjini Dodoma Aprili 4, 2018.

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali itaendelea kuboresha huduma kwa watu wenye ulemavu kwa kuzingatia sheria zilizopo ikiwa ni pamoja na kusimamia uundwaji wa kamati zinazoshughulikia masuala yao hapa nchini.

Ameyasema hayo leo (Jumatano, Aprili 4, 2018) wakati akiwasilisha hotuba ya mapitio na mwelekeo wa kazi za Serikali na makadirio ya mapato na matumizi ya fedha za ofisi yake kwa mwaka wa fedha 2018/2019 Bungeni dodoma.

Amesema Serikali itaboresha mazingira ya watu wenye ulemavu kwa kuhakikisha uundwaji wa kamati zao zinazotambulika kisheria ili kusaidia kutatua changamoto zinazowakabili na kuhakikisha kila mkoa unaunda kamati hizo ambapo hadi sasa mikoa 12 imekamilisha zoezi la uundwaji wa kamati hizo.

“Tayari Serikali imeunda kamati za watu wenye ulemavu katika mikoa 12 ya Geita, Kagera, Kilimanjaro, Mbeya, Mwanza, Njombe, Pwani, Singida, Rukwa, Shinyanga, Simiyu na Tabora. Ufuatiliaji unaendelea kufanyika ili kuhakikisha kuwa mikoa mingine nayo inaunda kamati hizo,” alisema Waziri Mkuu.

Waziri Mkuu amesema katika kuhakikisha uboreshaji wa huduma kwa watu wenye ulemavu, Serikali imeendelea kutoa vifaa zaidi ili waweze kushiriki katika shughuli za kimaendeleo ikiwa ni pamoja na kuhakikisha wanajikwamua kiuchumi.

“Serikali kwa kushirikiana na wadau imeendelea kutoa vifaa saidizi kwa jamii ya watu wenye ulemavu ili kuwawezesha kufanya shughuli zao bila utegemezi kwa kuwapatia baadhi ya vifaa ikiwemo viti mwendo 240, bajaji 6, magongo ya kutembelea 350, kofia pana 128, fimbo nyeupe 175, miwani maalum kwa wenye uoni hafifu 70, shime sikio 20, vyerehani 8, vifaa vya kukuzia maandishi 65, mafuta maalum ya kukinga ngozi dhidi ya mionzi ya jua 35, viti maalum vya kuogea 50 na nyenzo nyingine za kujimudu,” alisema.

Alisema Serikali imeendelea kuviboresha vyuo vya watu wenye ulemavu vya Yombo, Dar es Salaam na Sabasaba, Singida ili kuhakikisha wanashiriki katika fursa zote ikiwemo za elimu ili wawe na ujuzi utakaowawezesha kushiriki katika fursa za ajira nchini ikiwa ni utekelezaji wa Sheria Na. 9 ya Watu Wenye Ulemavu ya mwaka 2010.

Alisema Serikali itaendelea kutoa huduma kwa watu wenye ulemavu ikiwa ni pamoja na kukamilisha uanzishwaji wa Mfuko wa Taifa wa Maendeleo wa Watu wenye Ulemavu, kuanzisha madawati ya watu wenye ulemavu, kuhamasisha sekta binafsi na umma kuweka miundombinu rafiki kwa watu wenye ulemavu na kuwataka waajiri wote wawaajiri watu wenye ulemavu wenye sifa kwenye nafasi mbalimbali.


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.