Saturday, April 28, 2018

SERIKALI KUENDELEA KUKOMESHA AJIRA HATARISHI ZA WATOTO

Na.MWANDISHI WETU
Serikali imedhamiria kuendelea kukomesha ajira hatarishi za watoto ili kuhakikisha kuwa watoto wanalindwa na kuwapa nafasi stahiki kulingana na sheria na kanuni zilizopo nchini.
Hayo yameelezwa na Waziri wa Nchi Ofisi (Sera, Bunge, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama alipohudhuria katika kilele cha Siku ya Afya na Usalama Mahali Pa Kazi Duniani inayoadhimishwa kila mwaka  tarehe 28 Aprili ambapo Kitaifa ilifanyika Mkoani Iringa.
Waziri alieleza kuwa, katika mapambano haya ya ajira hatarishi kwa watoto ni moja ya utekelezaji wa kampeni zinazolenga kuharakisha utekeleezaji wa vipaumbele vilivyomo kwenye lengo namba (8) la Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa ambalo ni kuboresha mazingira ya wafanyakazi na kukomesha ajira mbaya kwa watoto.
“Tuendelee kupiga vita ajira mbaya kwa watoto kwa kuzingatia kampeni zilizopo hasa ile ya kuboresha mazingira ya wafanyakazi ifikapo mwaka 2030 pamoja na kukomesha ajira mbaya za watoto ifikapo mwaka 2025,” alisema Waziri
Waziri aliongezea kuwa katika kuhakikisha watoto wanakuwa na mazingira salama , Lazima kuwe na mikakati  ya pamoja baina ya utatu katika masuala ya kazi na ajira ikiwemo na kujenga utamaduni wa kujikinga na vihatarishi sehemu za kazi vinavyoweza kusababisha kuhatarisha afya na usalama wa wafanyakazi.
Aidha kama Taifa lazima tuoneshe umuhimu wa kuhakikisha kampeni hii inakuwa na matokeo chanya na kuendelea kuwa na Taifa lenye maendeleo.
Waziri aliongezea kuwa kulingana na Matokeo ya Utafiti wa Mtakwimu Mkuu wa Serikali uliofanyika mwaka 2014 na matokeo yake kuchapishwa mwaka 2016 ulibainisha kuwa, hali ya ajira  hatarishi za watoto kuzidi kuwa mbaya zaidi katika sehemu za mashambani, sekta ya madini, misitu na uvuvi.
“Kwa mujibu wa taarifa za Mtakwimu Mkuu wa Serikali za mwaka 2014 zilibaini kuwa watoto wenye umri kati ya  miaka  5-17 walioko kwenye ajira ni takribani milioni 4.2 ambayo ni asilimia 28.8 ya wafanyakazi wote na kati ya hao asilimia 21.5 wako kwenye ajira hatarishi hususan sehemu za mashambani ambako asilimia 35.6 ya wafanyakazi wote ni watoto”,alisisitiza Mhe.Waziri
Kwa upande wake Kaimu Mtendaji Mkuu wa OSHA, Khadija Mwenda alieleza kuwa wataendelea kutekeleza majukumu yao kwa kuhakikisha sheria zilizopo zinafuatwa bila kukiukwa hususan kwa makundi maalum iliwemo yale ya vijana na makundi ya watu wenye ulemavu.
“kwa kuwa Vijana wadogo ndiyo nguvu kazi ya taifa hivyo wanastahiri kulindwa na kuangaliwa kwa jicho la pekee ili kuwa na kizazi endelevu,”alisema Mwenda
AWALI

Aprili 28 ya kila mwaka ni siku ya Kimataifa ya kuadhimisha masuala ya Afya na Usalama Mahali Pa Kazi, ambapo huwa na Kauli Mbiu inayotumika duniani kote ambayo inatolewa na Shirika la Kazi la Duniani.Kauli mbiu ya mwaka huu ni “Kizazi Salama chenye Afya –Generation Safe and Health”.Kaulimbiu hiyo ili kuendana na mazingira ya nchi yetu iliboreshwa na kuwa “Kizazi Salama Chenye Afya kwa Uchumi wa Viwanda Generation Safe and Health for Industrial Economy”.


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.