Friday, November 15, 2019

JAMII YAASWA KUWATUNZA WAZEE


WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amesema jamii inatakiwa kuwajali na kuwatunza wazee na watu wenye mahitaji maalumu kwani hilo ni jukumu la watu wote na si kuiachia Serikali pekee.

Ameyasema hayo leo (Ijumaa, Novemba 15, 2019) wakati wa kikundi cha wake wa viongozi nchini cha New Millenium Group kilipotembelea makazi ya wazee ya Nunge katika kata ya Vijibweni Wilaya ya Kigamboni jijini, Dar es Salaam na kutoa misaada wa vitu mbalimbali.

Waziri Ndalichako amesema kuwa ‘’jukumu la kutunza wazee ni letu sote, nawashukuru wake wa viongozi kwa umoja wenu, nawaomba muendelee na moyo huu wa kuwasaidia watu wenye mahitaji maalumu.”

Amesema Serikali imefanya ukarabati wa nyumba 10 kati ya 50 zilizopo katika makazi hayo ya wazee na itaendelea kuzikarabati nyumba  zote zilizobaki na kujenga uzio ili makazi hayo yasiingiliwe na watu wanaozunguka eneo hilo.

Naye,Mwenyekiti wa New Millenium Group, Mke wa Waziri Mkuu Msaafu, Mama Tunu Pinda  amesema akinamama hao wamekesha usiku na mchana kuhakikisha wazee hao wanapata mahitaji na wametoa walichobarikiwa na Mwenyezi Mungu.

‘’Kikundi chetu katika kutimiza miaka 10 tangu kianzishwe tumeamua kurudisha fadhila kwa jamii kwa kutoa tulichobarikiwa. Ikumbukwe kuwa nasi ni wazee watarajiwa ni asilimia nne tu ya wazee wanapata mafao wengine hawana msaada wowote. Wazee kuanzia miaka 60 hunyemelewa na magonjwa mbalimbali hivyo jamii isiwasahau.”

Kwa upande wake, Mlezi wa kikundi hicho, Mke wa Waziri Mkuu Mama Mary Majaliwa amewashukuru akinamama wenzake wanaounda umoja huo na kuiomba jamii iwaunge mkono.

“Akina Mama wa Millennium mmekuwa mfano bora kwa wenzetu nawaomba tudumishe umoja wetu na tunamshukuru Mama yetu Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli kwa kuungana nasi katika kuwapa tabasamu wazee wetu wa Nunge.” 

Awali, Afisa Mfawidhi wa kituo hicho Jacklina Kanyamweri amewashukuru akinamama kikundi cha New Mellinium Group kwa kuwakumbuka wazee na watu wenye uhitaji ambapo amewaomba  wasichoke kwani wazee wana mahitaji mengi  ikiwemo ujenzi wa uzio katika makazi hayo na ukarabati wa barabara. 

Akina Mama wanaounda umoja huo wametoa misaada wa vitu mbalimbali ikiwemo sabuni, nguo, gypsum, baiskeli za watoto, mafuta. Wametembelea kituo hicho wakiwa katika maadhimisho ya miaka 10 tangu kuanzishwa kwa umoja huo.

Kadhalika, akinamama hao wameahidi kukarabati bwalo la wazee hao na kujenga mnara wa tenki la kuhifadhia maji pamoja na kutengeneza mfumo wa maji unaopeleka katika nyumba za wazee hao kadri Mwenyezi Mungu atakavyowajaalia. 

Kwa upande wao, wazee wanaotunzwa katika makazi hayo wameiomba Serikali kutowatupa na wamewashukuru akinamama wa New Millennium Group kwa moyo wao wa pekee kwa walivyojitoa. 

(mwisho)


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.