Tuesday, March 3, 2020

TUTAENDELEA KUSHIRIKIANA NA WAWEKEZAJI-MAJALIWA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali itaendelea kufanya kazi kwa kushirikiana na wawekezaji katika sekta mbalimbali nchini wakiwemo wenye viwanda vya kuzalisha saruji.
Amesema katika kuhakikisha inalinda viwanda vya ndani vya kuzalisha saruji Serikali imeamua kuzuia uingizwaji wa saruji kutoka nje ya nchi.
Waziri Mkuu aliyasema hayo leo(Jumanne, Machi 3, 2020) wakati akizungumza na watumishi wa kiwanda cha saruji cha Simba alipotembelea kiwanda hicho akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Tanga.
Amesema licha ya Serikali kupata kodi kutokana na uwepo wa kiwanda hicho, pia kimesaidia katika kutatua changamoto ya ajira hususani kwa vijana.
Naye, Waziri wa Madini, Doto Biteko amesema ameupongeza uongozi wa kiwanda hicho kwa kuwa wanazingatia sheria zote za madini ukilinganisha na viwanda vingine.
Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa kiwanda hicho, Reinhardt Swart alisema kiwanda hicho kinauwezo wa kuzalisha tani milioni 1.25 kwa mwaka lakini kutokana na mahitaji ya soko kinazalisha tani milioni 1.075 kwa mwaka.
Mkurugenzi huyo aliongeza kuwa kiwanda hicho kimeajiri jumla ya wafanyakazi 319 kati yao wazawa ni 316 na watumishi watatu ni raia ya kigeni.
Pia, Mkurugenzi huyo alitumia fursa hiyo kuishukuru Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli kwa kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini.


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.