Friday, January 18, 2019

KILOSA WATAKA MABWAWA KUPUNGUZA ATHARI ZA MAFURIKO


Wilaya ya Kilosa imekuwa ikiathiriwa na mafuriko ya mara kwa mara kutokana na  mvua nyingi zinazonyesha nchini na kusababisha kujaa kwa maji katika mito mikubwa inayopita katika wilaya hiyo ambayo ni mto Mkondoa na Mkundi. Kutokana na hali hiyo Kamati ya Wilaya ya Usimamizi ya Maafa Kilosa imeliomba Baraza la Taifa la Usimamizi wa Maafa kuzielekeza wizara za kisekta kukamilisha mpango wa kufufua na kujenga mabwawa wilayani humo, ili kupunguza kasi ya maji yanayo jaa katika mito hiyo.
Akiongea wilayani Kilosa wakati wa kufuatilia hatua za urejeshaji hali kutokana na athari za maafa ya mafuriko yaliyotokana na mvua zilizonyesha, Mkurugenzi Idara ya Uratibu wa Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali, Jimmy Matamwe ameeleza kuwa wamelipokea ombi hilo ambalo ni muhimu kutekelezwa kwa ajili ya kupunguza athari za maafa wilayani humo.
“Mvua zinaponyesha na tukawa na utaratibu mzuri wa kuyavuna maji hayo, matokeo ya mvua hizo huwa zinachochea shughuli za maendeleo hasa kilimo, lakini bila kuyavuna maji yanaweza kusababisha maafa kama  mafuriko. Kwa kulitambua hili, tutaratibu wizara husika kuhakikisha mabwawa yanafufuliwa ili kuhifadhi maji na kupunguza maji mengi yanayoingia mto Mkondoa” Alisisitiza Kanali, Matamwe.
Kanali Matamwe amewataka wananchi wa kilosa kutoendeleza shughuli za kibinadamu kando ya mto huo kutokana na kuwa serikali imetumia gharama kubwa za kujenga tuta la mto Mkondoa kwa lengo la kupunguza athari za maafa yaliyokuwa yanatokea baada ya mto huo kujaa.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa, ambaye pia ni mwenyekiti wa Kamati ya Wilaya ya Maafa Bw. Asajile Mwambambale, amefafanua kuwa ipo haja ya kuharakisha ujenzi wa bwawa  la Kidete ili kuweza kupunguza kasi ya maji ma wingi wa maji yanayo ingia mto Mkondoa, ambapo athari zake za mafuriko  huathiri watu, mali na miundombinu ya Kilosa.
“Pamoja na kuwa tungependa utafiti wa kina ufanyike kuanzia kwenye chanzo cha mto Mkondoa  ili kuweza kuelewa tabia  ya mto huu, niliombe Baraza la Taifa la Usimamizi wa maafa, litusaidie kuzielekeza hizi wizara za kisekta, ikiwemo wizara ya maji, zikamilishe mipango ya kufufua  na kujenga mabwawa ambayo yatasaidia kuhifadhi maji na kupunguza wingi wa maji yanaoyoingia katika mto Mkondoa” alisema Mwambambale.
Mwambambale amefafanua kuwa wilaya ya kilosa imeendelea kutekeleza mpango wa Kujiandaa na Kukabiliana na mafuriko kwa kutoa mchanga kwenye mto Mkondoana Mkundi, ili kuongeza kina cha mito hiyo. Pia zoezi la Upandaji wa miti na matete kando ya  mto Mkondoa limefanyika. Aidha Kamati za maafa za kata na vijiji pamoja na timu za uokoaji na kutoa misaada kwa waathirika wakati wa maafa zimejengewa uwezo.
Wilaya ya Kilosa ni miongoni mwa wilaya 7 za mkoa wa Morogoro ambayo imekuwa ikiathiriwa na mafuriko ya mara kwa mara kutokana na mvua zinazonyesha mikoa ya jirani ya Dodoma na Manyara hususani Wilaya za Mpwapwa, Kongwa na Kiteto, maji ya mvua hizo hupita wilayani Kilosa kupitia mto Mkondoa na Mkundi.


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.