Friday, January 4, 2019

RAIS AMEDHAMIRIA KUFUNGUA MILANGO LA MAENDELEO NCHINI

*Ni ile iliyokuwa imejifunga kwa muda mrefu kwenye mikoa mbalimbali

RAIS Dkt. John Magufuli amedhamiria kufungua milango na fursa za maendeleo iliyokuwa imejifunga kwa muda mrefu kwenye mikoa mbalimbali nchini ukiwemo mkoa wa Ruvuma.

Hayo yamesemwa leo (Ijumaa, Januari 4, 2019) na Waziri MKuuKassim Majaliwa apozungumza na wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika kijiji Nyoni, Mbinga.

Waziri Mkuu ambaye yuko mkoani Ruvuma kwa ziara ya kikazi ya siku nne amesema Serikali itahakikisha milango ya maendeleo katika maeneo yote nchini inafunguka.

Amesema miongoni mwa miradi inayotekelezwa na Serikali ambayo inalenga kufungua milango na fursa ya maendeleo ni pamoja na ujenzi wa miundombinu ya barabara.

Waziri Mkuu ametolea mfano wa barabara inayojengwa kutoka Mbinga hadi Mbamba bey kwamba itafungua fursa za kiuchumi kwa wananchi pamoja na Taifa kwa ujumla.

Kadhalika, Waziri Mkuu amezungumzia suala ya utendaji kwa watumishi wa umma, ambapo amewataka watekeleze majukumu yao ipasavyo na hayo ndio matakwa ya Serikali.

“Lazima watumishi wa umma wawajibike kwa kuwatumikia wananchi ipasavyo na wazingatie wajibu wao. Serikali haitawavumilia watumishi wazembe, wala rushwa.” 

Pia Waziri Mkuu amewasisitiza watumishi wa umma kwenda kwa wananchi kusikiliza kero na changamoto mbalimbali zinazowakabili ili kushirikiana nao katika kuzipatia ufumbuzi.

Amesema kitendo cha wananchi kuwasilisha malalamiko yao kupitia mabango kwenye mikutano ya viongozi kinaonesha kwamba watumishi hawaendi kwa wananchi.

“Watumishi wa Mbinga acheni kukaa ofisini na badala yake tengeni siku tatu kwa wiki na kwenda vijijini kwa ajili ya kuwasikiliza wananchi na kutatua kero zinazowakabili.”

Mkutano huo ulihudhuriwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Ajira na Wenye Ulemavu, Jenister Mhagama na Waziri wa Kilimo Japhet Hasunga, Naibu Waziri wa Maji, Jumaa Aweso.

Wengine ni Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Damas Ndumbaro, Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mhandisi Stella Manyanya, Naibu Waziri OR-TAMISEMI Joseph KandegeMkuu wa Mkoa wa Ruvuma Christina Mndeme na maafisa wengine wa Serikali.


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.