Saturday, November 18, 2017

WAZIRI MKUU AONGOZA MAOMBOLEZO YA KIFO CHA KATIBU MKUU WA CWT


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameungana na wanafamilia, Viongozi wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) katika kuomboleza kifo cha aliyekuwa Katibu Mkuu wa CWT, Bw. Yahya Msulwa nyumbani kwa marehemu, Tuangoma Jijini Dar es Salaam. 
Bw. Msulwa  amefariki dunia juzi (Alhamisi, Novemba 16, 2017) katika Hospitali ya Aga Khan jijini Dar es Salaam alikokuwa akipatiwa matibabu. Katika maombolezo hayo Waziri Mkuu ameambatana na Mkewe Mama Mary Majaliwa.

Akizungumza kwa niaba ya Serikali, Waziri Mkuu amesema kifo hicho ni pigo kwa Serikali kwa sababu marehemu alishirikiana nayo vizuri akiwa kiongozi wa walimu ambao ni zaidi ya asilimia 65 ya watumishi wa umma.

Waziri Mkuu amesema kuwa marehemu alikuwa mchapakazi na mwenye ushirikiano mzuri na wenzake, ambapo Novemba 12, 2017 alipokea barua kutoka CWT iliyosainiwa na marehemu akimualika kushiriki kwenye shughuli za chama.

“Wote tumeguswa na msiba huu, marehemu alikuwa mtumishi wa muda mrefu wa Chama cha Walimu Tanzania tangu mwaka 1996 na alikuwa rafiki na ndugu wa kila mmoja. Alikuwa na tabia njema, hivyo tunatakiwa kuyaenzi mambo mema aliyotuachia”
Waziri Mkuu ameongeza kuwa “Wajibu wetu sote ni kumuombea kwa Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahali pema. Nawaomba wanafamilia, mke wa marehemu na watoto kuwa na moyo wa subira katika kipindi hiki kigumu cha kuondokewa na mpendwa wetu.”
Marehemu anatarajiwa kuzikwa leo katika makaburi ya Kisutu Jijini Dar es Salaam


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.