Friday, March 8, 2019

NAIBU WAZIRI MAVUNDE AWAASA WANAWAKE KUDUMISHA UPENDO NA UMOJA

NA.MWANDISHI WETU
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana na Ajira Mhe.Anthony Mavunde amewaasa wanawake kudumisha upendo na umoja katika kushiriki shughuli za maendeleo nchini kwa kushikamana pamoja bila kujitenga.
Kauli hiyo ameitoa wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Machi 08, 2019 katika Viwanja vya Mashujaa Jijini Dodoma kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Uratibu, Kazi, Vijana na Wenye Ulemavu Mhe.Jenista Mhagama.
Maadhimisho ya mwaka huu yana kauli mbiu inayosema “Badili Fikra Kufikia Usawa wa Kijinsia kwa Maendeleo Endelevu”
Naibu Waziri alibainisha miongoni mwa changamoto zinazokwamisha maendeleo ya wanawake ni pamoja na kukosekana kwa umoja, upendo na ushirikiano ambao unawaga katika makundi na kusababisha wanawake kutokuwa na maendeleo ya pamoja.
“Niseme ukweli japokuwa hamtaupenda kwa leo, miongoni mwa sababu zinazowakwamisha katika kuendelea ni tabia ya chuki miongoni mwenu, umbeya na makundi yasiyoleta tija za kimaendeleo,”alieeza Mavunde
Aliongezea kuwa, wanawake wanapaswa kubalidi mitazamo na tabia ambazo zinawaga na kuondoa upendo kati yao na kujikuta wanajitenga hivyo, kupunguza nguvu kazi ya pamoja katika uzalishaji na kuchangia kusuasua kwa maendeleo yao.
Aidha Mavunde alieleza kuwa, kwa kuzingatia mchango wa wanawake katika kuleta maendeleo nchini ni vyema wakaishi kwa upendo na umoja ili kufikia malengo ya kuwa na Tanzania ya Viwanda.
“Kimsingi wanawake ni nguzo imara inayotegemewa na Taifa kwa kuzingatia uthubutu na namna Mungu alivyowapa roho ya kuvumilia na kuwaamini katika utendaji wenye uadilifu,”alisisitiza Mavunde
Aidha alieleza kuwa kwa kuzingatia kauli mbiu ya mwaka huu jamii haina budi kutathmini hatua tulizofikia kama Taifa katika masuala ya usawa wa kijinsia na uwezeshaji wanawake na wasichana na kutumia maadhimishi hayo kama fursa ya namna bora ya kukabili changamoto zinazowakabili wanawake katika kujiletea maendeleo. 
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Wanawake TUCTA Bi.Rehema Ludanga alieleza furaha yake kwa mwitikio mkubwa wa Wanawake Mkoani Dodoma kwa ushiriki wao pamoja na kuipongeza Serikali kwa jitihada zake za kuendelea kupinga unyanyasaji wa kijinsia kwa kuanzisha madawati ya jinsia ambayo yanatoa fursa za kutetea haki za wanawake nchini.
“Kipekee nawapongeza wanawake wote waliojitokeza kuiadhimisha siku hii muhimu pamoja na Serikali yetu sikivu kwa jitihada zake za kuendelea kuwaangalia wanawake na haki zao kwa kuanzisha madawati ya jinsi 422 nchini yanayotoa fursa za kusikiliza masuala yanayowakabili wanawake nchini,”alisisitiza Rehema

=MWISHO=


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.