Tuesday, June 25, 2019

SERIKALI YA KENYA YAMKANA JAGUAR

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali ya Kenya imesema kauli iliyotolewa na Mbunge wa jimbo la Starehe nchini humo, Charles Njagua Kanyi maarufu Jaguar si kauli ya Serikali, hivyo amewataka Watanzania wawe watulivu.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Jumanne, Juni 25, 2019) wakati akitoa kauli ya Serikali kuhusu kauli iliyotolewa na mbunge huyo ya kuwataka wafanyabiashara kutoka nchi mbalimbali ikiwemo Tanzania waondoke nchini Kenya ndani ya saa 24.

Amesema baada ya mbunge huyo kutoa kauli hiyo, Serikali ilianza kulifanyiakazi jambo hilo ambapo ilimuita Balozi wa Kenya nchini Tanzania ili kujua kama huo ni msimamo wa Serikali yao ama la, ambapo balozi huyo alimesema ile si kauli ya Serikali ya Kenya wala wananchi.

Hata hivyo, Waziri Mkuu amesema mbali na kuwasiliana na Balozi huyo, pia Serikali imewasiliana na Balozi wa Tanzania nchini Kenya ili afuatilie kuhusu kauli ya Mbunge huyo, hivyo amewataka Watanzania waendelee kushirikiana na Wakenya.

“Si kauli nzuri na kauli hii iliyotolewa na mtu mmoja linajenga chuki baina ya mtu na mtu, nchi na nchi na tayari Serikali ya Kenya inalifanyia kazi suala hili na imetuomba Watanzania tuendelee kuwa wavumilivu.”

Waziri Mkuu amesema tamko lile linaweza kuibua chuki na vurugu miongoni mwa nchi mbalimbali zikiwemo za Afrika Mashariki na tayari Wabunge wa Bunge Afrika Mashariki wanaoendelea na kikao cha Bunge hilo jijini Arusha wamepinga na kulaani kauli hiyo.
Wamesema hawatoa nafasi kwa mtu yeyote kuvuruga nchi hizo.

Hivyo, Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwasihi Watanzania popote walipo waendelee kuishi vizuri na Wakenya kwa kuwa wao hawana chuki na Watanzania bali ni mtu binafsi. Pia amewatahadharisha wananchi wa Afrika Mashariki wawe makini na kauli zao ili kuepusha vurugu.

 (mwisho)


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.