Saturday, June 1, 2019

WAZIRI MKUU AWATANGAZIA NEEMA WAKULIMA WA KOROSHO

*Asisitiza kwamba madai yote kumalizwa ndani ya mwaka huu wa fedha

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewahakikishia wakulima wa korosho ambao bado hawajalipwa kuwa Serikali italipa fedha hizo ambazo ni zaidi ya bilioni 20 mwaka huu.

Amesema wakulima ambao bado hawajalipwa au kumaliziwa malipo yao baada ya Serikali kumaliza uhakiki majina yao yatapelekwa TADB kwa ajili ya malipo.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Jumamosi, Juni 1, 2019) katika kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM mkoa wa Lindi, kilichofanyika kwenye ukumbi wa CCM mkoa.

“Wakulima wote wanaodai malipo yao ya korosho watalipwa katika mwaka huu wa fedha kwa kuwa ni haki yao na kwamba Serikali haitodhulumu haki ya mkulima yeyote.”

Kadhalika, Waziri Mkuu amesisitiza suala la uboreshwaji wa miundombinu mbalimbali ya kutolea huduma zikiwemo barabara ili ziweze kupitika kwa urahisi wakati wote.

Amesema uboreshwaji wa mbiundombinu pamoja na huduma nyingine za jamii ni jukumu la watendaji, hivyo wahakikishe wananchi wote wanahudumiwa bila ya kubaguliwa.

“Kila aliyepewa jukumu ahakikishe analitekeleza ipasavyo. Watendaji hakikisheni mnawatumikia Watanzania wote vizuri, kusiwe na ubaguzi wa kisiasa, kidini na kikabila.”

Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ilani katika kikao hicho, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Godfrey Zambi amesema zoezi la malipo ya fedha za korosho zilizohakikiwa linaendele.

Amesema hadi Mei 31 mwaka huu kilo 51,990,999.97 zenye thamani ya sh. bilioni 171,570,299,912 ambazo ni sawa na asilimia 87.6 zimeshalipwa kwa wakulima husika.

Mkuu huyo wa mkoa amesema kiasi cha bilioni 23,404,086,508 bado hazijalipwa kwa wakulima wa korosho wa mkoa wa Lindi. Korosho hizo zilihakikiwa kituo cha Mtwara.

Kikao hicho kimehudhuriwa na wabunge wa mkoa wa Lindi, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri na Manispaa pamoja na Wakuu wa Idara.

 (mwisho)


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.