Friday, June 28, 2019

WAZIRI KAIRUKI AUTAKA UONGOZI WA KNAUF KUENDELEA KUSHIRIKIANA NA JAMII INAYOWAZUNGUKA.

NA.MWANDISHI WETU – OWM
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Uwekezaji Mhe. Angellah Kairuka ameutaka uongozi wa kiwanda kinachotengeneza bidhaa za cha za jasi (Gypsumboard) cha KNAUF kuendelea kushirikiana na jamii inayowazunguka katika kujiletee maendeleo.
Ametoa kauli hiyo mapema mwishoni mwa wiki hii alipotembelea kiwanda hicho kilichopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga mkoa wa Pwani ili kukagua shughuli za uzalishaji zinazoendela pamoja na kusikiliza changamoto za wawekezaji hao na kuweza kujadili masuala ya kuendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini.
Waziri Kairuki aliwataka kuona umuhimu wa kuchangia katika shughuli za kimaendeleo katika maeneo yanayozunguka kiwanda hicho hususan katika uboreshaji wa miundombinu na utoaji wa misaada itakayofikia jamii kwa sehemu kubwa na si mtu mmoja mmoja ili kuleta maendeleo katika eneo kubwa na kuondoa tofauti kubwa za kimaendeleo zisizoendana na maendeleo ya maeneo kiwanda hicho.
“Ni muhimu sana, na ni busara kuona ni kwa  namna gani mnashirikiana na wananchi wanaozunguka eneo hili katika kuleta maendeleo ili kuhakikisha mnakubalika , na kuleta maendeleo ya eneo husika na kuondoa tofauti za kimaendeleo kati ya ustawi wa kiwanda na jamii inayowazunguka”alieleza Waziri Kairuki
Waziri aliutaka uongozi huo kushiriki kimalilifu katika shughuli za maendeleo ikiwemo kuchangia kuboresha miundombinu inayozunguka mazingira ya kiwanda ili kuendelea kushiriki kwa vitendo na kuunga mkono jitihada za kuendelea eneo hilo.
Sambamba na hilo Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga, Jumaa Abeld aliomba uongozi wa kiwanda kuona namna ya kuchangia katika maendeleo ya eneo lao kwa kuchangia ujenzi wa vyumba vya madarasa sita katika shule ya msingi ya Kitangwi pamoja na madarasa manne  katika shule ya msingi ya Kisemvule zilizopo Wialya ya Mkuranga katika mkoa huo.
“Ombi letu ni kuona namna kiwanda hiki kinavyoweza kuchangia katika maendeleo kwa kutujengea vyumba sita vya madarasa katika shule zinazotuzunguka ili kusaidia uhaba uliopo na kusaidi watoto wetu kujifunza katika mazingira mazuri,”alisema Jumaa.
Aidha Meneja Masoko wa Kiwanda hicho Bi. Zainab Mwasara aliahidi ifikapo Julai 05 mwaka huu uongozi wa kiwanda utatoa taarifa za utekelezaji wa maombi hayo ya ujenzi wa vyumba vya madarasa 6.
“Tunaahidi kukutana kama uongozi wa kiwanda ili kujadili na kutekeleza masuala ya msingi ikiwemo hili la ujenzi wa vyumba vya madarasa ili kuendelea kuleta tija kwa uwepo wa kiwanda katika eneo hili,”alisema Mwasara.
Naye, Meneja Fedha wa kiwanda hicho Bi. Wema Mboga alishukuru Serikali kwa kuendelea kuboresha mazingira ya wawekezaji nchini na kumpongeza ziara ya Waziri katika kutatua na kuahidi kufanyia kazi masuala yaliyoelezwa kuwa ni changamoto kiwandani hapo ikiwemo uhaba wa upatikanaji wa nishati ya umeme ya uhakika, kutokamili kwa leseni za uchimbaji kwa wakati, tozo kubwa za malighafi na kuongezeka kwa gharama za uzalishaji kiwandani hapo.
AWALI
Kiwanda cha KNAUF kilianzishwa mwezi Novemba mwaka 2015 kwa lengo la kuzalisha bidhaa za jasi (Gypsum board), gundi za jasi, pamoja na chuma za jasi (metal profile) kufanya kazi na usambazaj.Kiwanda kinafanya kazi katika nchi zaidi ya 80 ambapo katika nchi za kusini mwa Janga la Sahara, Tanzania ni nchi pekee ambayo ina uwekezaji huo kutokana na sababu za mazingira mazuri ya kibiashara na uwekezaji pamoja na sababu za kijiografia.Kampuni imeajiri wazawa 150 katika Nyanja zote kwa kulenga ifikapo 2020 kiwanda kiweze kuendeshwa na wazawa pasipo kutegemea wataalam kutoka nje.
=MWISHO=


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.