Saturday, July 20, 2019

WAZIRI MKUU AZINDUA SAFARI ZA RELI YA TANGA -MOSHI

*Apokea treni ya kwanza yenye tani 800 za saruji

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amepokea treni ya kwanza ya mizigo kutoka Tanga ikiwa ni ishara ya uzinduzi wa reli ya kutoka Tanga hadi Moshi.

Waziri Mkuu amepokea treni hiyo leo (Jumamosi, Julai 20, 2019) ambayo iliwasili saa 4:30 asubuhi kwenye stesheni ya Moshi na kukata utepe wa uzinduzi saa 4:32, kisha akapanda kwenye treni hiyo saa 4:33.

Akizungumza na mamia ya wakazi wa mji wa Moshi na wengine kutoka mkoa jirani wa Tanga, Waziri Mkuu amesema amefurahi kupokea treni hiyo yenye mabehewa 20 yaliyokuwa na mzigo wa tani 800 za saruji kutoka kampuni ya Saruji ya Tanga. 

Amesema kukamilika kwa kipande cha reli ya Tanga - Moshi na kuanza kutoa huduma leo hii, ni mwendelezo wa utekelezaji wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano kuhakikisha miundombinu ya usafiri na usafirishaji inafaidika na fursa ya kijiografia iliyopo nchini kwa kutoa huduma za usafiri na uchukuzi wa reli kwa uhakika, usalama na kwa gharama nafuu.

“Wataalamu wa masuala ya usafirishaji duniani wanaeleza kuwa matumizi ya reli kwa ajili ya usafirishaji wa shehena, hupunguza gharama za bidhaa kwa asilimia kati ya 30 na 40. Vilevile, matumizi ya reli huwa ni kichocheo kikubwa cha ukuaji wa uchumi kutokana na ukweli kwamba, kupitia usafiri wa reli unaweza kusafirisha mizigo mingi kwa haraka na kwa wakati mmoja kwenda kwa mlaji,” amesema.

Amesema kama ilivyo kwa mradi wa SGR, njia ya reli ya Tanga - Moshi yenye urefu wa km. 353, ukarabati wake unagharamiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na umetekelezwa na wataalamu wazawa.

“Kwa msingi huo, naagiza viongozi na watendaji wa mikoa na maeneo ambayo yanapitiwa na reli hii, kwa kushirikiana na Shirika la Reli Tanzania, waanze mara moja kampeni ya kutoa elimu kwa umma kuhusu usalama lakini pia kuwakumbusha wananchi kuwa walinzi wa miundombinu hii muhimu ya reli,” amesema.

Akitoa salamu kwa niaba ya makatibu wakuu wa vyama 19 vya siasa nchini, Katibu Mkuu wa ADC, Bw. Hassan Doyo alisema kufufuliwa kwa treni hiyo ya mizigo kutawasaidia wachimbaji wa madini walioko Makanya, Same ambao walikuwa wakipata taabu ya kukodisha malori na kusafirisha bidhaa zao hadi kiwanda cha saruji cha Tanga.

Alisema reli hiyo itawanufaisha pia wachimbaji wa Kabuku, wilayani Handeni. "Wachimbaji wa madini ya chuma walioko Kabuku, walikuwa wanapata shida ya kusafirisha mizigo yao kwa barabara hadi Mtwara, gharama ziko juu mno. Lakini sasa watapata ufumbuzi baada ya reli hii kufufuliwa," alisema.

Mapema, akitoa taarifa kuhusu mradi huo, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Bw. Masanja Kadogosa alisema makadirio ya gharama za kufufua reli hiyo kutoka Korogwe hadi Arusha yalikuwa sh. bilioni 14 lakini mpaka sasa wametumia sh. bilioni 5.7.

Alisema ujenzi huo ulifanywa na wafanyakazi wazawa 525 kutoka TRC wakiwemo vibarua 466, wahandisi 12 na mafundi wa reli na nyanja nyingine 47. "Hawa watapata ajira ya kudumu na ndiyo wataisimamia hii reli," alisema. 

Alisema reli ya mizigo ilikuwa haifanyi kazi kwa miaka 12 iliyopita na huduma ya kusafirisha abiria ilisitishwa tangu mwaka 1994.

Hafla huyo ilihudhuriwa na Naibu Mawaziri wa Uchukuzi, TAMISEMI, Wabunge, watendaji wa Serikali, wawakilishi wa vyama vya siasa na wananchi mbalimbali. 



(mwisho)


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.