Friday, February 22, 2019

BENKI PUNGUZENI RIBA ZA MIKOPO MNAYOITOA-MAJALIWA


WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amezitaka benki nchini zipunguze viwango vya riba zinazotozwa kupitia mikopo mbalimbali wanayoitoa kwa wananchi.

Aliyasema hayo jana jioni (Ijumaa, Februari 22, 2019) alipozungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Bomang’ombe wilayani Hai.

Waziri Mkuu ambaye yuko mkoani Kilimanjaro kwa ziara ya kikazi alisema kitendo cha benki kutoza riba kubwa kinawaumiza wajasiriamali nchini.

Pia, Waziri Mkuu aliwataka wananchi hususani, vijana, wanawake na wenye ulemavu kuchangamkia fursa ya mikopo inayotolewa katika Halmashauri.

Alisema kila halmashauri inatakiwa itenge asilimia 10 ya mapato yake kwa ajili ya kuwawezesha vijana, wanawake na wenye ulemavu kupata mitaji.

Katika hatua nyingine,Waziri Mkuu amewataka wakulima wa kahawa wabadilike na kuondoa miti ya zamani na kupanda mipya ili waongeze tija.

Waziri Mkuu alisema wakulima hao wanaweza kuweka utaratibu wa kuondoa miche ya zamani kwa awamu na kupanda mipya, hivyo kupata mavuno mengi.


(mwisho)


EmoticonEmoticon

Note: Only a member of this blog may post a comment.